-
KutesekaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
juu ya yaliyo mabaya; wanazungumza juu ya upunjaji kwa majivuno. Tazama! Hao ndio waovu waliostarehe mpaka wakati usio na kipimo. Wameongeza mali yao.”—Zab. 73:3, 5, 8, 12.
Siku ya Mungu ya kutoza hesabu itafika. Wakati huo atawaadhibu waovu, na kuwaharibu milele. Andiko la Methali 2:21, 22 linasema hivi: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” Hapo ndipo wanyoofu, ambao wengi wao wameteseka, watakapopata afya kamilifu na kufurahia mazao mengi ya dunia.
Mtu Akisema—
‘Kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Hilo ni jambo linalotuhangaisha sana sisi sote. Hebu nikuulize, Kwa nini umeuliza swali hilo leo?’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘(Tumia habari katika ukurasa wa 124-128.)’ (2) ‘(Tumia maandiko mengine yanayoonyesha kwamba hali fulani hususa ambayo imemfanya mtu huyo binafsi ateseke itaondolewa.)’
Au unaweza kusema: (ikiwa wanahangaishwa na ukosefu wa haki ulimwenguni): ‘Biblia inaonyesha kwa nini hali hizi zipo leo. (Mhu. 4:1; 8:9) Je, unajua kwamba inaonyesha pia mambo ambayo Mungu atafanya ili atuletee kitulizo? (Zab. 72:12, 14; Dan. 2:44)’
Pia unaweza kusema: ‘Inaonekana wewe unamwamini Mungu. Je, unaamini kwamba Mungu ni upendo? . . . Je, unaamini kwamba yeye ni mwenye hekima na kwamba yeye ni mweza-yote? . . . Basi ni lazima awe ana sababu fulani nzuri za kuruhusu kuteseka. Biblia inaonyesha sababu hizo. (Ona ukurasa wa 124-128.)’
-
-
Kutoa MimbaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kutoa Mimba
Maana: Kutoa mimba ni kuondoa tumboni kiini-tete au kitoto ambacho kwa kawaida hakiwezi kuishi nje ya tumbo la uzazi. Huenda mimba ikatoka yenyewe kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu au kwa sababu ya msiba. Kutoa mimba kimakusudi ili kuepuka tu kuzaa mtoto asiyetakiwa ni sawa na kumwua binadamu kimakusudi.
Kumfikiria yule aliye Chanzo cha uhai wa kibinadamu kunapaswa kutufanya tuwe na maoni gani juu ya jambo hili?
Mdo. 17:28: “Kupitia kwake [Mungu] tuna uhai na tunaenda na kuwako.”
Zab. 36:9: “Kwako wewe [Yehova Mungu] iko chemchemi ya uzima.”
Rom. 14:12: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”
Je, Yehova anauona uhai wa mtoto kuwa wenye thamani hata wakati wa hatua za kwanza za ukuzi baada ya mimba kutungwa?
Zab. 139:13-16: “Wewe [Yehova] uliniweka nikiwa nimekingwa katika tumbo la mama yangu. . . . Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.”
Je, Mungu amewahi kusema kwamba mtu atatozwa hesabu kwa kumdhuru mtoto ambaye hajazaliwa bado?
Kut. 21:22, 23: “Ikiwa watu watapambana nao kwa kweli wamuumize sana mwanamke mwenye mimba nao watoto wake watoke lakini kifo kisitokee, atadaiwa alipie hasara kulingana na kile ambacho mume wa mwanamke huyo atamdai; naye atakitoa kupitia kwa waamuzi. Lakini kifo kikitokea, basi utatoa nafsi kwa nafsi.” (Tafsiri fulani zinafanya ionekane kana kwamba katika sheria hii kwa Israeli jambo la maana hapa lilikuwa kile kilichompata mama, wala si kitoto. Hata hivyo, maandishi ya kwanza ya Kiebrania yanarejezea msiba ambao ungeweza kusababisha kifo cha mama au mtoto.)
Kumwua binadamu kimakusudi bila ruhusa ya Mungu ni jambo zito kadiri gani?
Mwa. 9:6: “Yeyote anayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake nayo itamwagwa na mwanadamu, kwa maana kwa mfano wa Mungu alimfanya mwanadamu.”
1 Yoh. 3:15: “Hakuna muuaji aliye na uzima wa milele ukikaa ndani yake.”
Kut. 20:13: “Usiue.”
Je, maoni ya daktari ya kwamba kuruhusu mimba ikue kutadhuru afya ya mama ni sababu inayofaa ya kutoa mimba?
Wakati mwingine madaktari hukosea. Je, ingefaa mtu auawe kwa sababu huenda mtu huyo akamdhuru mwenzake? Ikiwa wakati wa kuzaa kuna uhitaji wa kuchagua kati ya uhai wa mama na ule wa mtoto, ni juu ya watu wanaohusika kufanya uamuzi huo. Hata hivyo, maendeleo ya kitiba katika nchi nyingi yamepunguza sana uwezekano wa hali hizo kutokea.
Mtu Akisema—
‘Lakini nina haki ya kuamua mambo yanayohusu mwili wangu mwenyewe.’
Unaweza kujibu hivi: ‘Ninaelewa maoni yako. Siku hizi, watu wengine huvunja haki zetu mara nyingi; wengi hata hawajali yanayowapata watu wengine. Lakini Biblia inatoa miongozo inayoweza kutulinda. Hata hivyo, ili tufaidike, ni lazima pia tukubali wajibu.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Akina mama wengi wameachwa na baba za watoto wao. Lakini katika nyumba ambamo mume na mke wanafuata viwango vya Biblia, mume atampenda sana mke na watoto wake na kukaa nao kwa ushikamanifu na kuwaandalia mahitaji yao. (1 Tim. 5:8; Efe. 5:28-31)’ (2) ‘Ili sisi binafsi tupokee aina hiyo ya upendo na heshima, tunapaswa pia kutumia viwango vya Biblia kuhusu maoni yetu kuwaelekea washiriki wa familia yetu. Biblia inasema tunapaswa kuwa na maoni gani kuwahusu watoto tunaowazaa? (Zab. 127:3; linganisha na Isaya 49:15.)’
-
-
Kutounga Mkono Upande WowoteKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kutounga Mkono Upande Wowote
Maana: Msimamo wa wale wasiounga mkono upande wowote wala kusaidia upande wowote kati ya pande mbili au zaidi zinazoshindana. Ni wazi kwamba tangu zamani na hata leo, katika kila taifa na katika hali mbalimbali, Wakristo wa kweli wamejitahidi kutounga mkono hata kidogo mapigano kati ya vikundi vya ulimwengu. Hawawazuii watu wengine wasifanye yale wanayotaka kuhusu kushiriki katika sherehe za kizalendo, kujiunga na jeshi, kujiunga na chama cha kisiasa, kugombea cheo cha kisiasa, au kupiga kura. Lakini wao wenyewe wanamwabudu Yehova peke yake, Mungu wa Biblia; wameweka maisha yao wakfu kabisa kwake nao wanaunga mkono kikamili Ufalme wake.
Ni maandiko gani yanayounga mkono maoni ya Wakristo kuhusu mamlaka ya serikali za kilimwengu?
Rom. 13:1, 5-7: “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa [watawala wa serikali], kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu . . . Kwa hiyo kuna sababu ya lazima kwenu muwe mkijitiisha, si kwa sababu ya ghadhabu hiyo tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu. . . . Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi; yeye anayetaka ushuru, ushuru; yeye anayetaka woga, woga huo; yeye anayetaka heshima, heshima hiyo.” (Hakuna serikali ambayo inaweza kuwapo bila ruhusa ya Mungu. Bila kujali tabia ya afisa mmoja-mmoja, Wakristo wa kweli wamewaheshimu kwa sababu ya cheo chao. Kwa mfano, bila kujali jinsi ambavyo serikali zimetumia pesa za kodi, waabudu wa Yehova wamelipa kodi zao kwa unyoofu kwa sababu ya ule utumishi ambao unaweza kumfaidi kila mtu.)
Marko 12:17: “Ndipo Yesu akasema: ‘Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.’” (Kwa hiyo, nyakati zote Wakristo wametambua kwamba ni lazima ‘walipe’ kodi kwa serikali na kutimiza wajibu mkuu zaidi walio nao kwa Mungu.)
Mdo. 5:28, 29: Msemaji wa mahakama kuu ya Wayahudi alisema: “‘Hakika tuliwaagiza [mitume] msiendelee kufundisha juu ya msingi wa jina hili [la Yesu Kristo], na bado, tazameni! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu, nanyi mnaazimia kuileta damu ya mtu huyu juu yetu.’ Petro na wale mitume wengine wakajibu wakasema: ‘Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’” (Wakati ambapo amri za watawala wa kibinadamu zimepinga moja kwa moja matakwa ya Mungu, Wakristo wa kweli wamewaiga mitume kwa kumtii Mungu kwanza.)
Ni maandiko gani ambayo nyakati zote huunga mkono maoni ya Wakristo wa kweli kuhusu kushiriki katika vita halisi?
Mt. 26:52: “Yesu akamwambia: ‘Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.’” (Je, kunaweza kuwa na sababu nyingine iliyo bora zaidi ya kupigana kuliko kumlinda Mwana wa Mungu? Hata hivyo, hapa Yesu alionyesha kwamba wanafunzi hao hawakupaswa kutumia silaha halisi za vita.)
Isa. 2:2-4: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima . . . Naye hakika atafanya hukumu kati ya mataifa na kunyoosha mambo kuhusu vikundi vingi vya watu. Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” (Lazima watu kutoka mataifa yote waamue kibinafsi jinsi watakavyotenda. Wale ambao wametii hukumu ya Yehova wanathibitisha kwamba yeye ni Mungu wao.)
2 Kor. 10:3, 4: “Ingawa tunatembea katika mwili, hatupigi vita kulingana na tulivyo katika mwili. Kwa maana silaha za vita vyetu si za kimwili, bali ni zenye nguvu kwa Mungu kwa ajili ya kupindua ngome zenye nguvu.” (Hapa Paulo anaeleza kwamba hakutumia kamwe silaha za kimwili, kama vile ujanja, lugha ya majivuno, au silaha halisi, ili kulilinda kutaniko lisiharibiwe na mafundisho ya uwongo.)
Luka 6:27, 28: “Mimi [Yesu Kristo] ninawaambia ninyi mnaosikiliza, Endeleeni kuwapenda adui zenu, kuwafanyia mema wale wanaowachukia, kuwabariki wale wanaowalaani, kusali kwa ajili ya wale wanaowatusi.”
Kwa nini Yehova aliwaruhusu Waisraeli wa kale wapigane vita?
Yehova aliwaagiza Waisraeli wa kale wapigane vita ili kuimiliki nchi ambayo yeye mwenyewe alikuwa ameichagua iwe urithi wao na kuwaangamiza watu ambao matendo yao mapotovu na ukaidi wao kwa Mungu wa kweli ulimfanya Yehova awaone kuwa hawastahili tena kuishi. (Kum. 7:1, 2, 5; 9:5; Law. 18:24, 25) Hata hivyo, Rahabu na Wagibeoni walionyeshwa rehema kwa sababu walimwamini Yehova. (Yos. 2:9-13; 9:24-27) Katika agano la Sheria, Mungu aliweka kanuni za vita ambavyo alivikubali, naye akaweka masharti ya kuachilia huru na jinsi ya kuendesha vita hivyo. Vita hivyo kwa kweli vilikuwa vitakatifu kwa Yehova. Sivyo ilivyo na vita vya taifa lolote leo.
Hali mpya ilitokea wakati kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa. Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. Wafuasi wa Kristo walipaswa kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote; kwa hiyo, baada ya muda, waabudu wa Mungu wa kweli wangepatikana katika mataifa yote hayo. Hata hivyo, mataifa hayo yana kusudi gani yanapoenda kupigana vita? Je, ni kutimiza mapenzi ya Muumba wa dunia yote au ni kuendeleza faida fulani za kitaifa? Kama Wakristo wa kweli katika taifa moja wangeenda kupigana vita na taifa lingine, wangekuwa wakipigana na waamini wenzao, wakipigana na watu ambao wanamwomba msaada Mungu yuleyule. Kwa kufaa, Kristo aliwaagiza wafuasi wake waweke upanga chini. (Mt. 26:52) Yeye mwenyewe, akiwa ametukuzwa mbinguni, ataendesha kazi ya kuwaangamiza wale wanaomkaidi Mungu wa kweli na mapenzi Yake.—2 The. 1:6-8; Ufu. 19:11-21.
Historia ya ulimwengu inaonyesha Wakristo wa kwanza walikuwa na maoni gani kuhusu kujiunga na jeshi?
“Kuchunguza kwa uangalifu habari zote zinazopatikana kunaonyesha kwamba, kufikia wakati wa Markas Aurelio [maliki Mroma kuanzia mwaka wa 161 W.K., mpaka mwaka wa 180 W.K.], hakuna Mkristo aliyepata kuwa askari-jeshi; na hakuna askari-jeshi, baada ya kuwa Mkristo, aliyebaki katika utumishi wa kijeshi.”—The Rise of Christianity (London, 1947), E. W. Barnes, uku. 333.
“Sisi ambao tulipenda vita, na kuuana, na kila namna ya uovu, kila mmoja wetu duniani kote tumebadili silaha zetu za kivita,—tumebadili panga zetu zikawa majembe, na mikuki yetu ikawa vyombo vya kulimia,—nasi tunasitawisha uchaji-Mungu, uadilifu, ufadhili, imani, na tumaini, ambazo tumepata kutoka kwa Baba Mwenyewe kupitia Yule aliyetundikwa.”—Justin Martyr katika “Mazungumzo Pamoja na Trifo, Myahudi” (karne ya 2 W.K.), The Ante-Nicene Fathers (Grand Rapids, Mich.; chapisho la mwaka wa 1885 chapa ya Edinburgh), kilichohaririwa na A. Roberts na J. Donaldson, Buku la 1, uku. 254.
“Walikataa kushiriki kwa njia yoyote katika utawala wa raia au katika ulinzi wa kijeshi wa milki. . . . haingewezekana kwa Wakristo kuwa askari-jeshi, mahakimu, au wafalme, bila kuikana kazi iliyo takatifu zaidi.”—History of Christianity (New York, 1891), Edward Gibbon, uku. 162, 163.
Ni maandiko gani ambayo nyakati zote huunga mkono maoni ya Wakristo wa kweli kuhusu kujiingiza katika mambo na harakati za kisiasa?
Yoh. 17:16: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi [Yesu] si sehemu ya ulimwengu.”
Yoh. 6:15: “Yesu, akijua [Wayahudi] walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme, akaondoka tena kwenda mlimani akiwa peke yake.” Baadaye, alimwambia gavana Mroma hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.”—Yoh. 18:36.
Yak. 4:4: “Enyi wazinzi, je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Kwa nini jambo hilo ni zito sana? Kwa sababu, kama andiko la 1 Yoh. 5:19 linavyosema, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Katika Yohana 14:30, Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” Kwa hiyo, hata mtu akiunga mkono kikundi gani cha kilimwengu, atakuwa chini ya utawala wa nani?)
Kuhusu kujiingiza katika siasa, wanahistoria wa kilimwengu wanasema nini juu ya maoni ya wale wanaoitwa Wakristo wa kwanza?
“Watu wengi hawakuuelewa Ukristo wa kwanza, nao watawala wa ulimwengu wa kipagani hawakuupenda. . . . Wakristo walikataa kushiriki katika kazi fulani zilizofanywa na raia Waroma. . . . Hawakukubali cheo cha kisiasa.”—On the Road to Civilization, A World History (Philadelphia, 1937), A. Heckel na J. Sigman, uku. 237, 238.
“Wakristo walijitenga na kuwa tofauti na serikali, wakiwa jamii ya kikuhani na ya kiroho, na Ukristo ulionekana kuwa unaweza kugeuza maisha ya raia kwa jinsi ile tu ambayo, ni lazima tukiri, ndiyo iliyo safi zaidi, kwa kujitahidi zaidi na zaidi kutia hisia takatifu katika raia za serikali.”—The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries (New York, 1848), Augustus Neander, kilichotafsiriwa kutoka katika Kijerumani na H. J. Rose, uku. 168.
Ni maandiko gani ambayo nyakati zote huunga mkono maoni ya Wakristo wa kweli kuhusu sherehe zinazotia ndani bendera na nyimbo za taifa?
1 Kor. 10:14; “Ikimbieni ibada ya sanamu.” (Ona pia Kutoka 20:4, 5.)
1 Yoh. 5:21: “Watoto wadogo, jilindeni na sanamu.”
Luka 4:8: “Yesu akajibu akamwambia: ‘Imeandikwa, “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”’”
Ona pia Danieli 3:1-28.
Je, mifano na sherehe hizo kweli zina maana ya kidini?
“[Mwanahistoria] Carlton Hayes alisema zamani kwamba desturi ya kuabudu bendera na kuapa katika shule za Marekani ni mwadhimisho wa kidini. . . . Na mwishowe Mahakama Kuu Zaidi imethibitisha katika mfululizo wa kesi kwamba desturi hizo za kila siku ni za kidini.”—The American Character (New York, 1956), D. W. Brogan, uku. 163, 164.
“Karibu bendera zote za zamani zilikuwa za aina ya kidini. . . . Kwa karne nyingi bendera ya kitaifa ya Uingereza—msalaba mwekundu wa Mtakatifu George—ilikuwa ya kidini; inaonekana kwamba sikuzote walitafuta msaada wa kidini ili kuzitakasa bendera za kitaifa, na nyingi za bendera hizo zilitokana na dini.”—Encyclopædia Britannica (1946), Buku la 9, uku. 343.
“Katika sherehe ya watu wote iliyosimamiwa na makamu wa rais wa Mahakama [Kuu Zaidi ya Kijeshi] iliyofanywa Novemba 19, bendera ya Brazili iliheshimiwa. . . . Baada ya bendera kupandishwa, Waziri Jenerali wa Jeshi Tristao de Alencar Araripe alisema hivi kuhusu ukumbusho huo: ‘. . . bendera zimekuwa mungu wa dini ya kizalendo ambaye watu hutakiwa wamwabudu . . . Bendera inasujudiwa na kuabudiwa . . . Bendera inaabudiwa, kama vile Nchi ya Kuzaliwa inavyoabudiwa.’”—Diario da Justiça (Federal Capital, Brazil), Februari 16, 1956, uku. 1906.
-