Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kl sura 10 kur. 90-97
  • Ufalme wa Mungu Watawala

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufalme wa Mungu Watawala
  • Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UFALME WENYE KUSUDI
  • UHALISI WA UFALME WA MUNGU
  • UTAWALA WA UFALME—LINI?
  • Ufalme wa Mungu Ni Bora Katika Njia Zote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Serikali ya Mungu Inaanza Kutawala
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Biblia Inatufundisha Nini?
Pata Habari Zaidi
Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
kl sura 10 kur. 90-97

Sura 10

Ufalme wa Mungu Watawala

1, 2. Serikali za kibinadamu zimethibitikaje kutofaa?

LABDA umepata kununua kifaa fulani, ila tu kugundua kwamba hakifanyi kazi. Acheni tuseme kwamba ulimwita fundi fulani wa kutengeneza. Hata hivyo, mara baada ya ‘kukitengeneza’ hicho kifaa, kikaharibika. Hilo lilikatisha tamaa kama nini!

2 Ndivyo ilivyo na serikali za kibinadamu. Sikuzote wanadamu wametamani serikali ambayo ingeleta amani na furaha. Hata hivyo, kwa kweli jitihada nyingi za kutengeneza sehemu zilizoharibika katika jamii hazijawa zenye mafanikio kwelikweli. Mapatano mengi sana ya amani yamefanywa—kisha yamevunjwa. Zaidi ya hayo, ni serikali gani imeweza kuangamiza umaskini, ubaguzi, uhalifu, maradhi, na uharibifu wa mazingira? Utawala wa mwanadamu hautengenezeki. Hata Mfalme Sulemani wa Israeli mwenye hekima aliuliza hivi: “Awezaje mtu kuelewa na njia yake?”—Mithali 20:24.

3. (a) Kichwa cha mahubiri ya Yesu kilikuwa nini? (b) Watu fulani hufafanuaje Ufalme wa Mungu?

3 Usikate tamaa! Serikali ya ulimwengu iliyo thabiti si ndoto tu. Hiyo ilikuwa ndiyo kichwa cha mahubiri ya Yesu. Yeye aliuita “ufalme wa Mungu,” naye akafundisha wafuasi wake wasali uje. (Luka 11:2; 21:31) Bila shaka, nyakati nyingine Ufalme wa Mungu hutajwa miongoni mwa wanadini. Kwa kweli, kila siku mamilioni husali uje wanapoirudia ile Sala ya Bwana (ambayo huitwa pia Baba Yetu au sala ya kielelezo). Lakini watu hujibu kwa njia mbalimbali wanapoulizwa, “Ufalme wa Mungu ni nini?” Baadhi yao husema, “Umo moyoni mwako.” Wengine huuita mbingu. Biblia hutoa jibu la wazi, kama vile tutakavyoona.

UFALME WENYE KUSUDI

4, 5. Sababu gani Yehova aliamua kutokeza wonyesho mpya wa enzi kuu yake, nao utatimiza nini?

4 Sikuzote Yehova Mungu amekuwa Mfalme, au Mtawala Mwenye Enzi Kuu, wa ulimwengu wote mzima. Jambo la kwamba aliumba vitu vyote linamwinua kwenye cheo hicho chenye utukufu. (1 Mambo ya Nyakati 29:11; Zaburi 103:19; Matendo 4:24) Lakini Ufalme ambao Yesu alihubiri juu yao ni wa kusaidia, au wa pili, kwa enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote mzima. Ufalme huo wa Kimesiya una kusudi hususa, lakini hilo ni nini?

5 Kama vile ilivyoelezwa katika Sura ya 6, watu wawili wa kwanza waliasi dhidi ya mamlaka ya Mungu. Kwa sababu ya masuala yaliyotokezwa, Yehova aliamua kutokeza wonyesho mpya wa enzi kuu yake. Mungu alitangaza kusudi lake la kutokeza “mbegu” ambayo ingemponda yule Nyoka, Shetani, na kuondoa matokeo ya dhambi ya wanadamu iliyorithiwa. Hiyo “mbegu” ya msingi ni Yesu Kristo, na “ufalme wa Mungu” ndicho chombo kitakachomshinda Shetani kabisa-kabisa. Kupitia Ufalme huo, Yesu Kristo atarudisha utawala juu ya dunia kwa jina la Yehova naye atatetea enzi kuu ya Mungu yenye haki kwa wakati wote.—Mwanzo 3:15, NW; Zaburi 2:2-9.

6, 7. (a) Huo Ufalme uko wapi, na nani aliye Mfalme na watawala-washiriki wake? (b) Ni nani walio raia wa huo Ufalme?

6 Kulingana na tafsiri ya Kiswahili ya Union Version ya maneno ya Yesu kwa Mafarisayo waovu, yeye alisema: “Ufalme wa Mungu umo ndani yenu.” (Luka 17:21) Je, Yesu alimaanisha kwamba Ufalme ulikuwa ndani ya mioyo miovu ya wale watu wafisadi? La. Tafsiri ya Kigiriki cha awali iliyo sahihi zaidi inasomwa hivi: “Ufalme wa Mungu uko katikati yenu.” (NW) Yesu, aliyekuwa katikati yao, alijirejezea kuwa ndiye Mfalme wa wakati ujao. Mbali na kuwa kitu ambacho mtu anakuwa nacho moyoni mwake, Ufalme wa Mungu ni serikali halisi, inayotenda iliyo na mtawala na raia. Ni serikali ya kimbingu, kwani huitwa “ufalme wa mbinguni” na pia “ufalme wa Mungu.” (Mathayo 13:11; Luka 8:10) Katika ono, nabii Danieli alitazama Mtawala wa huo akiwa “mtu kama mwana wa binadamu” (NW) akiletwa mbele ya Mungu Mweza Yote na kupewa “mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.” (Danieli 7:13, 14) Mfalme huyu ni nani? Biblia humwita Yesu Kristo “Mwana wa binadamu.” (Mathayo 12:40, NW; Luka 17:26, NW) Ndiyo, Yehova alimteua Mwana wake, Yesu Kristo, kuwa Mfalme.

7 Yesu hatawali akiwa peke yake. Kuna 144,000 pamoja naye ambao ‘wamenunuliwa kutoka duniani’ kuwa wafalme na makuhani washiriki wake. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3; Luka 22:28-30) Raia wa Ufalme wa Mungu watakuwa familia ya duniani pote ya wanadamu wanaojinyenyekeza kwa uongozi wa Kristo. (Zaburi 72:7, 8) Lakini, tunaweza kuwaje na hakika kwamba Ufalme kwa kweli utatetea enzi kuu ya Mungu na kurudisha hali za kiparadiso kwenye dunia yetu?

UHALISI WA UFALME WA MUNGU

8, 9. (a) Twaweza kutoaje kielezi cha kutegemeka kwa ahadi za Ufalme wa Mungu? (b) Sababu gani twaweza kuwa na hakika juu ya uhalisi wa huo Ufalme?

8 Ebu wazia kwamba moto umeharibu nyumba yako. Sasa rafiki fulani aliye na uwezo anaahidi kukusaidia ujenge upya nyumba yako na kuandalia familia yako chakula. Ikiwa sikuzote rafiki huyo amekuambia kweli, je, usingemwamini? Tuseme ulirudi nyumbani kutoka kazini siku iliyofuata ukapata kwamba wafanyakazi walikuwa tayari wakianza kuondoa mabaki ya baada ya moto na kwamba familia yako ilikuwa imeletewa chakula. Bila shaka ungekuwa na uhakika kamili kwamba baada ya muda fulani, hali haingerudishwa tu bali pia ingekuwa bora hata zaidi kuliko hapo mbele.

9 Vivyo hivyo, Yehova hutupa sisi uhakikishio wa uhalisi wa Ufalme. Kama vile ionyeshwavyo kwenye Kitabu cha Biblia cha Waebrania, sehemu nyingi za Sheria zilitangulia kuonyesha mpango wa Ufalme. (Waebrania 10:1) Mimweko ya kimbele ya Ufalme wa Mungu ilikuwa wazi pia katika ufalme wa kidunia wa Israeli. Hiyo haikuwa serikali ya kawaida, kwani watawala waliketi juu ya “kiti cha enzi cha BWANA [“Yehova,” NW].” (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Zaidi ya hayo, ilikuwa imetabiriwa hivi: “Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, wala mfanya sheria kati ya miguu yake hata atakapokuja Yeye [“Shilo,” NW], mwenye milki, ambaye mataifa watamtii.” (Mwanzo 49:10)a Ndiyo, Yesu, aliye Mfalme wa kudumu wa serikali ya Mungu, angezaliwa katika nasaba hiyo ya wafalme wa Kiyudea.—Luka 1:32, 33.

10. (a) Msingi wa Ufalme wa Mungu wa Kimesiya uliwekwa lini? (b) Wale watawala-washirika-watazamiwa wa Yesu wangeongoza kazi gani ya maana duniani?

10 Msingi wa Ufalme wa Mungu wa Kimesiya uliwekwa wakati wa uteuzi wa wale mitume wa Yesu. (Waefeso 2:19, 20; Ufunuo 21:14) Hao walikuwa wa kwanza kati ya wale 144,000 ambao wangetawala mbinguni wakiwa wafalme-washiriki pamoja na Yesu Kristo. Wakiwa duniani, watawala-washirika-watazamiwa hawa wangeongoza kampeni ya kutoa ushahidi, kwa kutii amri ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.”—Mathayo 28:19, NW.

11. Kazi ya kuhubiri Ufalme inatimizwaje leo, nayo inatimiza nini?

11 Amri ya kufanya wanafunzi inatiiwa sasa kwa kadiri isiyo na kifani. Mashahidi wa Yehova wanapiga mbiu ya habari njema ya Ufalme kotekote duniani, kwa kupatana na maneno ya Yesu ya kiunabii: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Programu kubwa ya elimu inatimizwa, ikiwa sehemu moja ya kazi ya kuhubiri Ufalme. Wale wanaotii sheria na kanuni za Ufalme wa Mungu wanaona tayari amani na muungamano ambao serikali za kibinadamu haziwezi kutimiza. Yote haya yatoa uthibitisho wa wazi kwamba Ufalme wa Mungu ni uhalisi!

12. (a) Sababu gani yafaa kuwaita wapiga-mbiu wa Ufalme Mashahidi wa Yehova? (b) Ufalme wa Mungu unatofautianaje na serikali za kibinadamu?

12 Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . na mtumishi niliyemchagua.” (Isaya 43:10-12) Yesu, “shahidi aliye mwaminifu,” alitangaza kwa bidii habari njema ya Ufalme. (Ufunuo 1:5; Mathayo 4:17) Basi yafaa kwamba wapiga-mbiu wa Ufalme wa siku hii walichukue jina Mashahidi wa Yehova lililoteuliwa rasmi kimungu. Lakini sababu gani Mashahidi hutumia wakati na jitihada nyingi sana ili kuongea na wengine juu ya Ufalme wa Mungu? Wao hufanya hivyo kwa sababu Ufalme ni tumaini pekee la wanadamu. Hatimaye serikali za kibinadamu hukoma, lakini Ufalme wa Mungu hautakoma kamwe. Isaya 9:6, 7 linamwita Yesu, aliye Mtawala wa ufalme huo, “Mwana-Mfalme wa Amani” (NW) na linaongeza hivi: “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.” Ufalme wa Mungu si kama serikali za mwanadamu—ambazo zipo leo na kesho zapinduliwa. Kwa kweli, Danieli 2:44 husema hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake. . . . Nao utasimama milele na milele.”

13. (a) Ni nini baadhi ya matatizo ambayo Ufalme wa Mungu utashughulikia kwa mafanikio? (b) Sababu gani twaweza kuwa na hakika kwamba ahadi za Mungu zitatimizwa?

13 Ni mfalme yupi wa kibinadamu ambaye angeweza kumaliza vita, uhalifu, magonjwa, njaa kali, na ukosefu wa nyumba? Zaidi ya hayo, ni mtawala yupi wa kidunia ambaye angeweza kufufua wale ambao wamekufa? Ufalme wa Mungu pamoja na Mfalme wao atashughulikia mambo hayo. Ufalme hautakuwa na hitilafu, kama vile kifaa kisichofanya kazi ambacho huhitaji kutengenezwa sikuzote. Badala ya hivyo, Ufalme wa Mungu utafanikiwa, kwani Yehova aahidi hivi: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:11) Kusudi la Mungu halitashindwa, lakini utawala wa Ufalme ulitazamiwa kuanza lini?

UTAWALA WA UFALME—LINI?

14. Wanafunzi wa Yesu walielewa vibaya nini kuhusu Ufalme, lakini Yesu alijua nini juu ya utawala wake?

14 “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” Swali hilo lililoulizwa na wanafunzi wa Yesu lilifunua kwamba kufikia wakati huo wao hawakujua kusudi la Ufalme wa Mungu na wakati uliowekwa rasmi wa utawala wa huo kuanza. Akiwaonya wasikisie-kisie juu ya hilo jambo, Yesu alisema hivi: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.” Yesu alijua kwamba utawala wake juu ya dunia uliwekwa kwa ajili ya wakati ujao, muda mrefu baada ya ufufuo na kupaa kwake mbinguni. (Matendo 1:6-11; Luka 19:11, 12, 15) Maandiko yalikuwa yametabiri hili. Jinsi gani?

15. Zaburi 110:1 husaidiaje kuelewa wakati wa utawala wa Yesu?

15 Akimrejezea Yesu kiunabii kuwa “Bwana,” Mfalme Daudi alisema hivi: “Tamko la Yehova kwa Bwana yangu ni: ‘Keti kwenye mkono wa kulia wangu mpaka mimi niweke maadui wako kuwa kibago cha nyayo zako.’” (Zaburi 110:1, NW; linganisha Matendo 2:34-36.) Unabii huu waonyesha kwamba utawala wa Yesu haungeanza mara iyo hiyo baada ya kupaa kwake mbinguni. Badala ya hivyo, yeye angengoja kwenye mkono wa kuume wa Mungu. (Waebrania 10:12, 13) Kungoja huku kungeendelea kwa muda gani? Utawala wake ungeanza lini? Biblia hutusaidia tupate majibu.

16. Ni nini kilichotendeka katika 607 K.W.K., na hili lilihusianaje na Ufalme wa Mungu?

16 Jiji pekee duniani pote ambalo Yehova aliweka jina lake juu yalo lilikuwa Yerusalemu. (1 Wafalme 11:36) Lilikuwa pia jiji kuu la ufalme wa kidunia uliokubaliwa na Mungu ambao ulikuwa mfano wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu. Kwa hiyo, kuharibiwa kwa Yerusalemu kwa mkono wa Wababiloni katika 607 K.W.K kulikuwa jambo lenye maana sana. Tukio hilo lilionyesha mwanzo wa kukatizwa kwa muda mrefu kwa utawala wa Mungu wa moja kwa moja juu ya watu wake duniani. Karne sita hivi baadaye, Yesu alionyesha kwamba kipindi hicho cha kukatizwa kwa utawala kilikuwa bado kinaendelea, kwani yeye alisema hivi: “Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa [“nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa,” NW] yatakapotimia.”—Luka 21:24.

17. (a) “Nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” ni nini, nazo zilipaswa zidumu kwa muda gani? (b) “Nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zilianza na kuisha lini?

17 Katika “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa,” serikali za kilimwengu zingeruhusiwa kukatiza utawala uliokubaliwa na Mungu. Kipindi hicho kilianza na uharibifu wa Yerusalemu katika 607 K.W.K., na Danieli alionyesha kwamba kingeendelea kwa muda wa “nyakati saba.” (Danieli 4:23-25) Huo ni muda mrefu kadiri gani? Biblia huonyesha kwamba “nyakati” tatu na nusu ni sawa na siku 1,260. (Ufunuo 12:6, 14) Kipindi hicho mara mbili, au nyakati saba, kingekuwa siku 2,520. Lakini hakuna jambo lolote lenye kutokeza lililotendeka mwishoni mwa kipindi hicho kifupi cha wakati. Hata hivyo, kwa kutumia “kila siku kuhesabiwa mwaka” kuhusu unabii wa Danieli na kuhesabu miaka 2,520 kuanzia 607 K.W.K., tunafika kwenye mwaka 1914 W.K.—Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6.

18. Yesu alifanya nini upesi baada ya kupokea nguvu za Ufalme, na hili liliathirije dunia?

18 Je, Yesu alianza kutawala mbinguni wakati huo? Sababu za Kimaandiko za kusema kwamba alianza kutawala zitazungumziwa katika sura ifuatayo. Bila shaka, mwanzo wa utawala wa Yesu haungeonyeshwa na amani ya mara iyo hiyo hapa duniani. Ufunuo 12:7-12 huonyesha kwamba baada tu ya kupokea Ufalme, Yesu angeondoa Shetani na malaika wake walio roho waovu kutoka mbinguni. Hilo lingemaanisha ole kwa dunia, lakini inatia moyo kusoma kwamba Ibilisi ana “wakati mchache tu” uliobaki. Karibuni, tutaweza kushangilia si kwa sababu tu Ufalme wa Mungu watawala bali pia kwa sababu utaleta baraka kwenye dunia na kwa wanadamu watiifu. (Zaburi 72:7, 8) Tunajuaje kwamba hili litatukia karibuni?

[Maelezo ya Chini]

a Jina Shilo lamaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake; Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Baada ya muda fulani, ikawa wazi kwamba “Shilo” alikuwa ni Yesu Kristo, “Simba aliye wa kabila ya Yuda.” (Ufunuo 5:5) Baadhi ya Targum za Kiyahudi ziliweka tu “Mesiya” au “Mesiya mfalme” mahali pa neno “Shilo.”

TAHINI UJUZI WAKO

Ufalme wa Mungu ni nini, nao watawala kutoka wapi?

Ni nani anayetawala katika Ufalme, na nani raia wa huo?

Yehova ametuhakikishiaje kwamba Ufalme wake ni uhalisi?

“Nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zilianza na kuisha lini?

[Sanduku katika ukurasa wa 94]

BAADHI YA MATUKIO YENYE MAANA YANAYOHUSIANA NA UFALME WA MUNGU

• Yehova atangaza kusudi lake la kutokeza “mbegu” itakayoponda kichwa cha yule Nyoka, Shetani Ibilisi.—Mwanzo 3:15.

• Katika 1943 K.W.K., Yehova aonyesha kwamba “mbegu” hiyo ingekuwa mzao wa kibinadamu wa Abrahamu.—Mwanzo 12:1-3, 7; 22:18.

• Agano la Sheria lililopewa Israeli katika 1513 K.W.K. huandaa “kivuli cha mema yatakayokuwa.”—Kutoka 24:6-8; Waebrania 10:1.

• Ufalme wa kidunia wa Israeli waanza katika 1117 K.W.K., na waendelea baadaye katika nasaba ya Daudi.—1 Samweli 11:15; 2 Samweli 7:8, 16.

• Yerusalemu laharibiwa katika 607 K.W.K., na “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zaanza.—2 Wafalme 25:8-10, 25, 26; Luka 21:24.

• Katika 29 W.K., Yesu atiwa mafuta kuwa Mfalme-Mteule na aanza huduma yake ya kidunia.—Mathayo 3:16, 17; 4:17; 21:9-11.

• Katika 33 W.K., Yesu apaa mbinguni, kungoja huko kwenye mkono wa kuume wa Mungu mpaka utawala wake unapoanza.—Matendo 5:30, 31; Waebrania 10:12, 13.

• Yesu atawazwa katika Ufalme wa kimbingu katika 1914 W.K. “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zinapoisha.—Ufunuo 11:15.

• Shetani na roho waovu wake watupwa hadi ujirani wa dunia na kuwaletea wanadamu ole wenye kuongezeka.—Ufunuo 12:9-12.

• Yesu asimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki