-
Yesu Alizaliwa Wakati Gani?Mnara wa Mlinzi—1980 | Oktoba 15
-
-
kuonyesha kwamba Yesu alizaliwa katika mwezi wa Ethanimu mapema katika vuli (Septemba-Oktoba).
KUSHEREHEKEA KUNAKOTAKIWA
Hivyo, ni wazi kwamba Yesu hakuzaliwa katika Desemba 25. Mahali pake, ushuhuda uliopo unaonyesha yapata Oktoba 1 wa mwaka 2 K.W.K. Kwa hiyo, kusherehekea siku yake ya kuzaliwa kwa kuadhimisha Krismas siku ya Desemba 25 hakufai kabisa kwa wale wanaoongozwa na Maandiko Matakatifu.
Hata hivyo kukosa kutajwa kwa siku yenyewe hasa ya kuzaliwa kwa Yesu hakutuhangaishi. Kwani sherehe za siku ya kuzaliwa zilizoandikwa katika Biblia ni zile za watawala wa kilimwengu.—Mwa. 40:20; Mt. 14:6; Marko 6:21-28; Yohana 18:36.
Hata hivyo, Yesu anapaswa kukumbukwa. Kwa sababu hiyo, alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, jambo ambalo wakati mwingi linaitwa Chakula cha Bwana cha Jioni. Kristo alifanya hivyo wakati wa usiku wa mwisho wa maisha yake ya kidunia, muda mfupi kabla hajatoa “nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28) Kwa kutumia mifano ya mwili na damu ambayo angetoa karibuni, Yesu aliwaamuru wafuasi wake waaminifu wale, na akawahimiza hivi: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” (Luka 22:19, 20; 1 Kor. 11:23-26) Kwa hiyo, ingawa Wakristo wa kweli wanapendezwa kadiri fulani na kujua wakati Yesu alipozaliwa, ni kifo cha Yesu Kristo wanachopaswa kukumbuka kila mwaka, wala si kuzaliwa kwake.
-
-
Kuendeleza Imani Pamoja na Mume WanguMnara wa Mlinzi—1980 | Oktoba 15
-
-
Kuendeleza Imani Pamoja na Mume Wangu
Kama ilivyosimuliwa na Elsa Abt
ALIPOKUWA katika Sachsenhausen, Harald alikuwa akiruhusiwa mara kwa mara kuandika barua yenye mistari mitano tu. Juu ya barua maneno yalipigwa muhuri hivi: ‘Kwa sababu anaendelea kuwa Mwanafunzi wa Biblia mwenye kichwa kikubwa, amenyimwa pendeleo la kuandika barua kama ilivyo kawaida.’ Muhuri wenye maneno hayo ulikuwa ukinitia moyo nyakati zote, maana maneno hayo yalionyesha kwamba mume wangu alikuwa akiendelea kuwa imara katika imani.
Siku moja katika Mei 1942, nilirudi kutoka kazini nikakuta Gestapo wakiningojea. Waliipeleleza nyumba yote, kisha wakaniamuru nichukue koti langu niwafuate. Jutta, binti yetu mdogo akainuka na kumwendea mmojawapo magestapo, mwanamume mrefu ajabu. Akivuta mguu wake wa suruale, akasema: “Tafadhali mwache mama yangu hapa! ” Kwa vile mwanamume huyo hakuitikia, Jutta akazunguka upande mwingine wa miguu yake na kusihi hivi: “Tafadhali mwache mama yangu hapa! ” Jambo hilo lilimtia mwanamume huyo wasiwasi mwingi, basi akasema kwa ukali hivi: “Mwondoe mtoto huyu mbali! Chukua kitanda chake, pia, na mavazi yake! ” Alipelekwa kwa jamaa nyingine katika jengo hilo, mlango ukafungwa kabisa, nami nikapelekwa kwenye makao makuu ya Gestapo.
Nikawaona huko Mashahidi wengine wengi waliokuwa wamekamatwa siku hiyo. Tulikuwa tumesalitiwa na mtu aliyekuwa amejifanya kuwa Shahidi hata tukawa na hakika naye. Gestapo walipotuhoji juu ya mahali ilikokuwa mashine ya kunakilia na kiongozi wa kazi ya kuhubiri kisiri alikuwa nani, mimi nikajifanya sijui lo lote. Kisha tulitupwa gerezani.
Imani yetu isiyotikisika ilipingamiza magestapo. Wakati mmoja, tulipokuwa tukihojiwa, afisa mmoja alikuja kwangu kwa makonde (ngumi). “Tutawafanyia nini nyie watu? ” akapaza sauti. “Tukiwakamata, hamjali. Tukiwapeleka gerezani, hamjali hata kidogo. Tukiwapeleka kwenye kambi ya mateso, haiwahangaishi. Tukiwahukumia kufa, wala hamna wasiwasi. Tutawafanyia nini nyie? ”
Baada ya kukaa miezi sita gerezani, mimi, pamoja na akina dada wengine Wakristo 11, tulipelekwa Auschwitz, kambi mbaya sana ya kuangamiza watu.
TUKIWA TOFAUTI NA KUHESHIMIWA
Kwanza, tulipelekwa Birkenau, mojawapo ya kambi ndogo za Auschwitz. Afisa mmoja SS alipopata kujua kwamba tulikuwa huko kwa sababu tulikuwa Wanafunzi wa Biblia, alisema hivi: “Kama ni mimi, ningeitilia sahihi karatasi niende zangu.”
“Kama ningalitaka kutia sahihi, ningaliweza kufanya hivyo kitambo,” nikajibu.
“Lakini utafia huku wewe,” akaonya. Nami nikamwambia hivi: “Niko tayari kufa.”
Baadaye tukatakiwa kupigwa picha, na kujaza fomu na karatasi nyingine za maulizo. Nilipokuwa nikingojea katika mstari uliopita katika kituo cha dawa, madaktari wawili, wao vilevile wakiwa wafungwa, walikuwa wakitazama wafungwa wanaowasili (wanaofika). Daktari mmoja alikuwa kambini muda mrefu zaidi ya yule mwenzake. Nikamsikia yule wa zamani akimwambia mdogo wake hivi: “Unaweza nyakati zote kuwatambua Wanafunzi wa Biblia.”
“Kweli? ” daktari mdogo akajibu, akiwa na mashaka kidogo. “Vema, basi, ebu nionyeshe, nani aliye Mwanafunzi wa Biblia katika kikundi hiki.” Nilikuwa ndipo ninawapita katika mstari, nao hawakuweza kuiona alama yangu ya pembetatu, rangi ya urujuani. Hata hivyo, yule daktari mkubwa akaonyesha kidole kwangu, akasema: “Huyu ni Mwanafunzi wa Biblia.” Yule mdogo akazunguka, akatazama alama yangu, akapaza sauti na kusema: “Umesema kweli! Ulijuaje? ”
“Watu hawa wanaonekana tofauti,” akasema. “Unaweza kuwatofautisha na watu wengine.”
Ikawa ndivyo. Tulionekana tofauti. Tulitembea tukiwa tumenyoka, hatukuonekana wenye huzuni. Nyakati zote tulitazama mbele; tuliwatazama watu wengine wazi-wazi na kwa uhuru. Tulikuwa huko kama mashahidi wa jina la Yehova. Ndiyo sababu tulikuwa na mwenendo tofauti, na wengine waliutambua.
Sisi akina dada 12 tulikuwa katika Birkenau siku chache tu. Kisha tukapelekwa Auschwitz tukafanye kazi katika nyumba za maafisa wa SS. Walitaka Mashahidi wa Yehova peke yao kwa kazi hiyo; waliogopa kukubali wengine wafanye kazi katika nyumba zao. Walijua kwamba sisi hatungejaribu kuwapa sumu; tulikuwa wanyofu na hatungeiba wala kujaribu kutoroka.
UZIMA NA MAUTI KATIKA AUSCHWITZ
Kwa muda fulani sote tuliishi katika kambi ya mateso, pamoja na wafungwa wengine, katika orofa ya chini ya nyumba kubwa ya matofali. Ukafika wakati wa kupewa migawo yetu ya kazi. “Ni nani anayetaka kufanya kazi mahali fulani? ” tukaulizwa. Lakini tukanyamaza. Kumbe, mna kiburi sana,” msimamizi wa kike akasema.
Sivyo, hatuna kiburi,” msichana rafiki yangu akajibu, “lakini ukituweka po pote, hapo ndipo tutakapofanya kazi.” Na hayo ndiyo yaliyokuwa maongozi yetu. Hatukutaka kuchagua mahali pa kufanya kazi, maana tulikuwa tukimwomba Yehova atupe uongozi wake. Iwapo tungewekwa mahali pagumu, tungeweza kuomba hivi: “Yehova, tafadhali tusaidie sasa.”
Mgawo wangu ulikuwa kufanya kazi kwa afisa wa SS aliyeishi nje ya kambi. Kazi yangu ilikuwa kusafisha nyumba yake, kusaidia mke wake kupika, kutunza mtoto wao na kununua vitu mjini—Mashahidi wa Yehova peke yao ndio waliotumainiwa kuwa wanaweza kutoka kambini pasipo kulindwa na askari. Bila shaka, sikuzote tulikuwa tukivaa mavazi ya gerezani yenye mistari-mistari. Baada ya kitambo kidogo tukaruhusiwa kuishi mahali tulikofanya kazi, badala ya kurudi kambini usiku. Mimi nilikuwa nikilala katika orofa ya chini ya nyumba ya afisa wa SS.
Lakini hatukuonwa kama watu kweli kweli. Kwa mfano, wakati afisa wa SS aliponiita kwenda afisini kwake, nilitakiwa kusimama mlangoni na kusema: “Mfungwa Namba 24,402 aomba ruhusa ya kuingia.” Na nikiisha kupokea maagizo yake, nilitakiwa niseme hivi: “Mfungwa Namba 24,402 aomba ruhusa ya kuondoka.” Majina yetu hayakutumiwa hata kidogo.
Kama katika kambi nyingine, chakula cha kiroho kwa namna ya Mnara wa Mlinzi na vitabu vingine kilikuwa kikiingizwa kwa kawaida katika Auschwitz. Hata nilipokea barua kutoka kwa Harald. Hivi ndivyo mawasiliano ya kawaida yalivyoanzishwa na Mashahidi wa kutoka nje:
Wengine wa kikundi chetu, kutia na rafiki yangu Gertrud Ott, walipewa mgawo wa kufanya kazi katika hoteli ambako jamaa za maafisa wa SS ziliishi. Siku moja Gertrud alikuwa akisafisha madirisha wakati wanawake wawili walipopita karibu naye, na, bila kutazama juu, mmoja akasema, “Sisi ni Mashahidi wa Yehova vilevile.” Baadaye, waliporudi, Gertrud akawaambia hivi: “Nendeni kwenye maliwato.” Wakakutana huko na kuongea, na tangu wakati huo wakafanya mpango wa kukutana kwingine ili waingize kwa siri vitabu bora vya kujifunza Biblia na kuleta habari nyingine.
Tulimshukuru Yehova kwa kutuongoza na kutulinda wakati wa miaka hiyo ya kuwa katika Auschwitz, sana sana kwa vile tulivyojua kwamba kulikuwako na vituko vibaya sana vilivyokuwa vikitendeka huko. Magari yenye kujaa Wayahudi yalikuwa yakiwasili na kupelekwa moja kwa moja kwenye vyumba vyenye sumu! Wakati mmoja nilimtunza msimamizi mmoja wa kike kambini aliyekuwa amefanya kazi katika vyumba vyenye sumu, naye akaniambia mambo yaliyokuwa yakitendeka huko.
“Watu wanaingizwa kama wanyama chumbani,” akaeleza, “na katika mlango wa kwenda kwenye chumba kingine kuna ishara inayosema, ‘Kwenye Maliwato.’ Wanaambiwa wavue mavazi yao. Wakiwa uchi kabisa, wanaingia katika ‘maliwato.’ Kisha mlango unafungwa nyuma yao. Lakini sumu, badala ya maji, ndiyo inayotoka katika mabomba ya kunyunyizwa.” Aliyokuwa ameona huko yalikuwa yamemchukiza sana, kiasi cha kwamba akawa mgonjwa kimwili.
KWENYE KAMBI NYINGINE NA UKOMBOZI
Kuanzia na Januari 1945, Wajeremani waliendelea kushindwa katika mpaka wa mashariki. Katika jitihada ya kuondoka katika kambi za mateso, wengi wetu walihama kutoka kambi hii kwenda kwenye kambi nyingine. Baada ya kusafiri siku nne mchana na usiku kuelekea kambi ya Gross-Rosen, akina dada fulani wakawa hoi wasiweze kuendelea na safari. Kilikuwa kitulizo kama nini usiku wa tatu tuliporuhusiwa mwishowe tulale katika ghala ya nafaka iliyosongamana watu! Chakula peke yake tulichokuwa nacho katika safari yote hiyo ni mkate mdogo tuliokuwa tumechukua. Hakuna ye yote kati yetu aliyedhani kuwa tungeweza kupona siku nyingine ya kusafiri. Lakini ndipo likatokea jambo la ajabu ambalo sitasahau kamwe.
Tulipoanza kusafiri siku ya pili yake, daktari SS niliyekuwa nimefanya kazi kwake wakati mmoja akatuona, naye akaanza kupaza sauti akisema: “Wanafunzi wa Biblia tokeni! Wanafunzi wa Biblia tokeni! ” Kisha akaniambia: “Uhakikishe kwamba tumewapata ninyi nyote.” Basi sote akina dada 40 tukapelekwa kituoni na mipango ikafanywa ya kutusafirisha kwa garimoshi. Ilionekana kwetu kama mwujiza.
Magari ya moshi yalisongamana watu, na watatu kati yetu tukapotea mahali pa kushukia, tukaenda moja kwa moja mpaka Breslau (Kipoland, Wroclaw). Tukashukia hapo nasi tukaelekezwa kwenye kambi. Tulipofika penye lango, askari walinzi wakacheka, wakacheka wee, mwishowe wakasema hivi: “Ni Mashahidi wa Yehova tu ambao wangekuja huku kwa hiari yao.” Lakini tulijua kwamba dada zetu wangepata taabu sana kama hatungerudi kwenye kambi.
Tukawa katika Gross-Rosen muda wa juma mbili tu, kisha tukasafirishwa kwenye kambi ya Mauthausen karibu ya Linz katika Austria. Hali za huko zilikuwa zenye kuogopesha sana. Watu wengi mno walikusanywa-kusanywa pamoja. Chakula kilikuwa haba, wala hata hatukuwa na majani makavu ya kulalia, isipokuwa mbao tu. Baada ya kukaa kidogo tukaanza kusafiri tena, kuelekea kambi ya Bergen-Belsen, karibu ya Hannover, Ujeremani. Dada mmoja wetu akafia njiani. Kwa sababu ya hali mbaya sana iliyokuwa katika kambi hii, akina dada zetu wengi waliokuwa wamepona kusafirishwa mpaka kufikia hapa, sasa wakafa.
Watu karibu 25 kutoka katika kikundi chetu walipelekwa bado kwenye kambi nyingine, ya siri, inayoitwa Dora-Nordhausen. Hapo mwanzoni kambi hiyo ilikuwa ya wanaume tu, lakini majuzi makahaba fulani walikuwa wamepelekwa huko. Walakini, mkuu wa kambi hiyo alimweleza wazi msimamizi wa kike kwamba sisi tulikuwa watu tofauti. Tukapata nafuu katika Dora-Nordhausen. Ndugu mmoja alikuwa akifanya kazi katika chumba cha kupikia wafungwa, naye alihakikisha kwamba tumepewa chakula kizuri.
Wakati huo kumalizika kwa vita kukawa kumekaribia. Mipango ilifanywa ili kutusafirisha kwenye mahali ambapo ni karibu na Hamburg. Mimi nilipewa mkebe wa nyama na mkate kuwa chakula cha safarini, lakini wanaume hawakupokea kitu. Ndugu mmoja wa Poland akawa mgonjwa sana; basi nikampa chakula nilichokuwa nacho. Baadaye, akaniambia kwamba chakula hicho kiliokoa uhai wake. Njiani, tukakutana na askari wa Kiamerika, nasi tukakombolewa. Wale askari SS wakavalia mavazi ya kiraia waliyokuwa wamechukua safarini, wakaficha silaha zao wakakimbia. Vita ikawa inamalizika!
Harald na mimi tulipoonana baada ya mwezi mmoja, ilikuwa ajabu. Tukakumbatiana kwa muda mrefu zaidi sana—ilikuwa imepita miaka mitano tangu tulipotenganishwa.
MAJARIBU NA BARAKA ZAIDI
Tuliporudi nyumbani tukakuta ujumbe huu mlangoni: “Jutta Abt huishi humu. Wazazi wake wako katika kambi ya mateso.” Tulifurahi kama nini kurudi nyumbani—tukiwa salama! Sana sana jambo la kufurahisha ni kujua kwamba tulikuwa tumekuwa waaminifu kwa Yehova.
Miaka yangu ya kukaa katika kambi za mateso Ujeremani ilinifundisha somo kubwa. Ni hili, jinsi roho ya Yehova inavyoweza kukutia nguvu sana unapojaribiwa sana! Kabla sijakamatwa, nilikuwa nimesoma barua ya dada mmoja iliyosema kwamba wakati wa jaribu kali, roho ya Yehova inafanyiza utulivu ukujie. Nikadhani anatia maneno chumvi tu. Lakini nilipopatwa na majaribu mimi mwenyewe, nikajua kwamba yale aliyokuwa amesema yalikuwa kweli. Inakuwa namna hiyo kweli kweli. Huwezi kuwaza itakuwa hivyo, ikiwa hujapata kujaribiwa. Hata hivyo ndivyo ilivyotukia kwangu kweli kweli. Yehova anasaidia.
Kilichonisadia mimi katika kutenganishwa kwangu na binti yangu ni lile agizo ambalo Yehova alimpa Ibrahimu amtoe mwanawe awe dhabihu. (Mwa. 22:1-19) Yehova hakumtaka kweli kweli amwue Isaka, bali alitaka tu aone utii wa Ibrahimu. Kwa habari yangu, nikafikiri kwamba Yehova hanitaki nimtoe mtoto wangu awe dhabihu, ila ataka tu nimwache. Hilo si kitu likilinganishwa na lile ambalo Ibrahimu aliombwa kufanya. Jutta ameendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova miaka mingi yote hiyo, na kwa hiyo tunafurahi sana.
Uaminifu wa mume wangu umekuwa kwangu furaha na nguvu nyakati zote. Sina budi (lazima) nimpende na kumheshimu kwa uaminifu wake huo ambao amemwonyesha Yehova. Na kama matokeo ya huo, tumethawabishwa sana.
-
-
Ubatizo—Wonyesho wa ImaniMnara wa Mlinzi—1980 | Oktoba 15
-
-
Ubatizo—Wonyesho wa Imani
“Kwa moyo mtu huamini apate haki, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la waziwazi la wokovu.”—Kum. 10:10, NW.
1. Kulingana na Mathayo 28:19 NW, Mtu anaonyeshaje kwamba amekuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo?
BWANA Yesu Kristo ndiye aliyetuwekea kielelezo cha kubatizwa. Wote wanaotaka kuwa wanafunzi wake wanapaswa kuzamishwa hivyo. Jambo hilo laonekana wazi katika amri aliyotoa Mwana wa Mungu akiwapa wafuasi wake baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu. Twasoma hivi: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.”— Mt. 28:19, NW.
2. (a) Maana ya ubatizo wa maji ni nini? (b) Ili ubatizo uwe na maana ya kweli, ni jambo gani linalohitajiwa kwa mtu?
2 Ubatizo wa maji unafananisha nini? Unamaanisha kwamba inajulikana mbele
-