-
Je, Unaweza Kuamini Miujiza Inayotajwa Katika Biblia?Mnara wa Mlinzi—2012 | Agosti 1
-
-
Je, Unaweza Kuamini Miujiza Inayotajwa Katika Biblia?
IKIWA ungesikia hadithi yenye kushangaza, ni wazi kwamba ungeamini tu ikiwa mtu anayekusimulia anategemeka. Kutegemeka kwa mtu huyo kunatia ndani jinsi anavyoeleza hadithi hiyo na kama amekuwa akisema ukweli. Ikiwa kwa miaka mingi amekuwa akisema ukweli na hajawahi kukudanganya kimakusudi, basi utakuwa na sababu nzuri ya kuamini mambo anayokuambia sasa.
Hivyo ndivyo ilivyo na miujiza inayotajwa katika Biblia. Sote hatukuwepo miujiza hiyo ilipotukia. Lakini tunaweza kuamini hadithi za Biblia ikiwa tu imekuwa ikisema ukweli. Kwa njia gani? Mambo yafuatayo yanafanya miujiza inayotajwa katika Biblia iwe yenye kuaminika.
Miujiza mingi ilifanywa hadharani. Wakati fulani miujiza hiyo ilishuhudiwa na maelfu au hata mamilioni ya watu. (Kutoka 14:21-31; 19:16-19) Haikufanywa kwa siri, mahali ambapo watu hawangeweza kuiona.
Miujiza hiyo haikuwa maonyesho yenye mambo mengi. Hakukuwa na vifaa vya kipekee au maonyesho yenye madoido mengi, wala taa za kupumbaza watu. Miujiza mingi inayotajwa katika Biblia, ilitukia bila kupangiwa na pia ilitukia baada ya watu kuomba msaada. (Marko 5:25-29; Luka 7:11-16) Katika hali kama hizo, mtu hangeweza kupanga mapema miujiza atakayofanya.
Kusudi kuu la watu waliofanya miujiza halikuwa kujiletea sifa, utukufu, au utajiri. Badala yake, kusudi kuu la miujiza lilikuwa kumletea Mungu utukufu. (Yohana 11:1-4, 15, 40) Mtu yeyote aliyejaribu kujipatia mali akitumia nguvu za kufanya miujiza alishutumiwa vikali.—2 Wafalme 5:15, 16, 20, 25-27; Matendo 8:18-23.
Miujiza mbalimbali iliyo katika Biblia inaonyesha kwamba haikuwa tu kazi ya wanadamu. Kwa mfano, kutulizwa kwa upepo na bahari, kubadilishwa kwa maji na kuwa divai, kusimamishwa na kuanzishwa tena kwa mvua, wagonjwa kuponywa, na vipofu kuwezeshwa kuona tena. Miujiza hiyo yote na mingine mingi inaonyesha kwamba nguvu zinazozidi za wanadamu ambazo zinaweza kushinda kila kitu ziliwawezesha kufanya miujiza hiyo.—1 Wafalme 17:1-7; 18:41-45; Mathayo 8:24-27; Luka 17:11-19; Yohana 2:1-11; 9:1-7.
Wapinzani walioshuhudia miujiza hiyo hawakupinga kwamba ilitukia. Yesu alipomfufua Lazaro, rafiki yake, wapinzani wa kidini wa Yesu hawakupinga kwamba Lazaro alikuwa amekufa. Hawangeweza kupinga kwa sababu siku nne zilikuwa zimepita tangu Lazaro alipokufa. (Yohana 11:45-48; 12:9-11) Karne kadhaa baada ya kifo cha Yesu, waandikaji wa Talmud ya Kiyahudi waliendelea kukubali kwamba Yesu alikuwa na nguvu za kimuujiza. Walitilia shaka tu chanzo cha nguvu hizo. Vivyo hivyo, wanafunzi wa Yesu walipoletwa mbele ya mahakama ya Kiyahudi, hawakuulizwa hivi: “Mlifanya miujiza?” Badala yake waliulizwa: “Mlifanya jambo hilo kwa nguvu gani au katika jina la nani?”—Matendo 4:1-13.
Hivyo basi, unaweza kuamini mambo ambayo Biblia inatuambia kuhusu miujiza? Kutokana na mambo ambayo tumechunguza, ni wazi kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu miujiza ni yenye kutegemeka. Kuna sababu nyingine zinazoweza kufanya tuamini masimulizi hayo ya Biblia. Kwa mfano, Biblia inapoeleza kuhusu tukio fulani, mara nyingi inataja wakati, mahali, na majina ya wahusika. Hata watu wanaokosoa Biblia wameshangazwa sana na usahihi wa habari za kihistoria zilizo katika Biblia. Unabii mwingi wa Biblia umetimia kikamili, kutia ndani hata habari ndogondogo. Zaidi ya hayo, Biblia ina mashauri ya jinsi ya kufanya uhusiano kati ya wanadamu uwe na furaha—mashauri ambayo yamewasaidia watu wa umri mbalimbali na wenye hali tofauti-tofauti. Ushauri wa Biblia unaohusu uhusiano kati ya wanadamu, umethibitika kuwa bora kabisa.
Ikiwa unatilia shaka masimulizi ya Biblia, kwa nini usitenge wakati wa kuichunguza kwa makini? Kadiri unavyoendelea kuijua, ndivyo utakavyozidi kuiamini. (Yohana 17:17) Utatambua kwamba unaweza kuamini mambo ambayo inakuambia kuhusu miujiza iliyotukia zamani. Ukiamini masimulizi hayo, utakuwa na msingi mzuri wa kuamini mambo ambayo Biblia inasema yatatukia hivi karibuni.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wapinzani wa Yesu hawakupinga kwamba Lazaro alikuwa amekufa
-
-
Miujiza Ambayo Itatukia Hivi KaribuniMnara wa Mlinzi—2012 | Agosti 1
-
-
Miujiza Ambayo Itatukia Hivi Karibuni
UNGEHISIJE ikiwa ungetambua kwamba daktari ambaye alikuwa amepangiwa kukufanyia upasuaji mkubwa hajawahi kufanya upasuaji kama huo? Ni wazi kwamba ungekuwa na wasiwasi mwingi. Lakini kwa upande mwingine, ungehisije ikiwa ungetambua kwamba daktari huyo alikuwa stadi katika kazi yake na alikuwa amewahi kufanya mamia ya upasuaji kama huo na akafaulu? Bila shaka, ungekuwa na uhakika kwelikweli kwamba anaweza kukusaidia.
Ulimwengu huu mwovu unahitaji kufanyiwa “upasuaji” mkubwa sana. Kupitia Neno lake Biblia, Yehova Mungu ameahidi kwamba atarudisha dunia hii kuwa Paradiso. (2 Petro 3:13) Lakini ili iwe hivyo, kwanza lazima uovu uondolewe, ukatiliwe mbali kabisa. (Zaburi 37:9-11; Methali 2:21, 22) Mambo yote yenye kuhuzunisha tunayoona leo, lazima yaondolewe kabla ya paradiso kurudishwa duniani. Muujiza utahitajika ili jambo hilo litukie!—Ufunuo 21:4, 5.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba mabadiliko hayo makubwa yatatukia hivi karibuni. Kwa nini? Kwa sababu miujiza ambayo tayari Yehova Mungu amefanya inathibitisha kwamba ana nguvu za kutimiza ahadi zake. Linganisha miujiza sita tu kati ya mingi inayotajwa katika Biblia na ahadi za wakati ujao ambazo inatoa.
Endelea kujifunza kuhusu ahadi za wakati wetu ujao zinazotajwa katika Biblia. Kadiri imani yako inavyoimarika ndivyo tumaini lako litakavyoongezeka—tumaini la kuishi wakati ambao wewe mwenyewe utafaidika kutokana na miujiza ambayo Yehova anafanya.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9, 10]
MUUJIZA:
YESU ALILISHA MAELFU YA WATU KWA MIKATE NA SAMAKI WACHACHE.—MATHAYO 14:13-21; MARKO 8:1-9; YOHANA 6:1-14.
AHADI:
“Hakika dunia itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.”—ZABURI 67:6.
INAMAANISHA NINI?
HAKUNA MTU ATAKAYETESEKA TENA KWA SABABU YA NJAA.
MUUJIZA:
YESU ALIWAPONYA VIPOFU.—MATHAYO 9:27-31; MARKO 8:22-26.
AHADI:
“Macho ya vipofu yatafunguliwa.”—ISAYA 35:5.
INAMAANISHA NINI?
VIPOFU WOTE WATAKUWA NA UWEZO WA KUONA.
MUUJIZA:
YESU ALIPONYA VILEMA.—MATHAYO 11:5, 6; YOHANA 5:3-9.
AHADI:
“Kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya.”—ISAYA 35:6.
INAMAANISHA NINI?
VILEMA WOTE WATAPONYWA.
MUUJIZA
YESU ALIPONYA MAGONJWA MBALIMBALI.—MARKO 1:32-34; LUKA 4:40.
AHADI:
“Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—ISAYA 33:24.
INAMAANISHA NINI?
MAGONJWA YOTE YENYE KUDHOOFISHA YATAONDOLEWA. TUTAFURAHIA AFYA KAMILI.
MUUJIZA:
YESU ALIDHIBITI NGUVU ZA ASILI.—MATHAYO 8:23-27; LUKA 8:22-25.
AHADI:
“Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatafanya kazi ya bure.”—ISAYA 65:21, 23.
“Utakuwa mbali sana na ukandamizaji—kwa maana hutaogopa yeyote—na jambo lolote lenye kutia hofu, kwa maana halitakuja karibu nawe.”—ISAYA 54:14.
INAMAANISHA NINI?
MISIBA YA ASILI HAITAKUWAPO TENA.
MUUJIZA:
YESU ALIFUFUA WAFU.—MATHAYO 9:18-26; LUKA 7:11-17.
AHADI:
‘Wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ —YOHANA 5:28, 29.
“Bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake.”—UFUNUO 20:13.
INAMAANISHA NINI?
WAPENDWA WETU WALIOKUFA WATAFUFULIWA.
-