Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
    • SURA YA TATU

      Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?

      • Mungu ana kusudi gani kwa wanadamu?

      • Mungu amepingwaje?

      • Maisha yatakuwaje duniani wakati ujao?

      1. Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia?

      KUSUDI la Mungu kwa dunia ni zuri ajabu. Yehova anataka dunia ijae watu wenye furaha na afya. Biblia inasema kwamba ‘Mungu alipanda bustani katika Edeni na kuchipusha kila mti wenye kutamanika kwa macho ya mtu na ulio mwema kwa chakula.’ Baada ya Mungu kumuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, aliwaweka katika makao hayo mazuri na kuwaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28; 2:8, 9, 15) Kwa hiyo Mungu alikusudia wanadamu wawe na watoto, waieneze bustani hiyo duniani pote, na kuwatunza wanyama.

      2. (a) Tunajuaje kwamba kusudi la Mungu kwa dunia litatimia? (b) Biblia inasema nini kuhusu wanadamu kuishi milele?

      2 Je, unafikiri kusudi la Yehova Mungu kwamba wanadamu waishi katika dunia iliyo paradiso litatimia? Mungu anasema hivi: “Mimi nimesema hilo; pia nitalitimiza.” (Isaya 46:9-11; 55:11) Naam, Mungu atatimiza kusudi lake! Kuhusu dunia, anasema kwamba “hakuiumba tu bila sababu,” bali “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mungu alitaka dunia ikaliwe na watu wa aina gani? Naye alitaka wakae humo kwa muda gani? Biblia inajibu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

      3. Ni hali gani zenye kuhuzunisha zilizopo duniani leo, na ni maswali gani yanayozuka?

      3 Ni wazi kwamba kusudi la Mungu halijatimia bado. Leo watu wanakuwa wagonjwa na kufa; hata wanapigana na kuuana. Mambo yaliharibika. Hata hivyo, hapana shaka kwamba Mungu hakukusudia dunia iwe kama ilivyo leo! Ni nini kilichotukia? Kwa nini kusudi la Mungu halijatimia? Hakuna kitabu chochote cha kihistoria kilichoandikwa na mwanadamu kinaweza kutuambia kwa sababu matatizo yalianzia mbinguni.

      ADUI ATOKEA

      4, 5. (a) Ni nani hasa aliyetumia nyoka kuzungumza na Hawa? (b) Mtu aliyekuwa mzuri na mnyoofu anawezaje kugeuka na kuwa mwizi?

      4 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinataja kuhusu mpinzani wa Mungu aliyetokea katika bustani ya Edeni. Anaitwa “nyoka,” ingawa hakuwa mnyama halisi. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia anaitwa “Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” Pia anaitwa “yule nyoka wa zamani.” (Mwanzo 3:1; Ufunuo 12:9) Malaika huyo mwenye nguvu, au kiumbe asiyeonekana mwenye mwili wa kiroho, alitumia nyoka kuzungumza na Hawa, kama vile mtu mwenye ustadi anavyoweza kufanya ionekane kana kwamba sauti inatoka katika mwanasesere au sanamu. Bila shaka kiumbe huyo alikuwapo Mungu alipokuwa akiitayarisha dunia kwa ajili ya wanadamu.—Ayubu 38:4, 7.

      5 Kwa kuwa uumbaji wote wa Yehova ni mkamilifu, basi, ni nani aliyemfanya “Shetani Ibilisi”? Kwa ufupi, mmoja kati ya wana wenye nguvu wa Mungu aligeuka akawa Ibilisi. Jinsi gani? Leo mtu ambaye wakati fulani alikuwa mzuri na mnyoofu anaweza kugeuka na kuwa mwizi. Hilo linawezekanaje? Huenda mtu akaruhusu tamaa mbaya iingie moyoni mwake. Akiendelea kuisitawisha, tamaa hiyo inaweza kuwa na nguvu sana. Kisha akipata nafasi, anaweza kutenda kulingana na tamaa hiyo mbaya ambayo imekuwa ikisitawi moyoni mwake.—Yakobo 1:13-15.

      6. Mmoja kati ya wana wenye nguvu wa Mungu aligeukaje na kuwa Shetani Ibilisi?

      6 Ndivyo ilivyokuwa kuhusu Shetani Ibilisi. Huenda alimsikia Mungu akiwaambia Adamu na Hawa wazae watoto na kuijaza dunia. (Mwanzo 1:27, 28) Haikosi Shetani aliwaza hivi: ‘Kwani, si wanadamu hao wote wanaweza kuniabudu mimi badala ya kumwabudu Mungu!’ Kwa hiyo, tamaa mbaya ikaanza kusitawi moyoni mwake. Mwishowe, akaamua kumdanganya Hawa kwa kumwambia uwongo kumhusu Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Basi, akawa “Ibilisi,” jina linalomaanisha “Mchongezi.” Wakati huohuo akawa “Shetani,” jina linalomaanisha “Mpinzani.”

      7. (a) Kwa nini Adamu na Hawa walikufa? (b) Kwa nini wazao wote wa Adamu huzeeka na kufa?

      7 Kwa kutumia uwongo na ujanja, Shetani Ibilisi aliwafanya Adamu na Hawa wamwasi Mungu. (Mwanzo 2:17; 3:6) Mwishowe, wakafa kwa sababu ya uasi kama Mungu alivyokuwa amesema. (Mwanzo 3:17-19) Kwa kuwa Adamu alipoteza ukamilifu alipoasi, wazao wake wote walirithi dhambi kutoka kwake. (Waroma 5:12) Hali hiyo inaweza kulinganishwa na sufuria inayotumiwa kuoka mikate. Ikiwa sufuria hiyo imejikunja, kila mkate utakaookwa katika sufuria hiyo utakuwaje? Kila mkate utakuwa na alama, au kasoro. Vivyo hivyo, kila mwanadamu amerithi “kasoro” ya kutokamilika kutoka kwa Adamu. Ndiyo sababu wanadamu wote huzeeka na kufa.—Waroma 3:23.

      8, 9. (a) Yaelekea Shetani alidai nini? (b) Kwa nini Mungu hakuwaharibu waasi hao mara moja?

      8 Shetani alipowashawishi Adamu na Hawa wafanye dhambi dhidi ya Mungu, alianzisha uasi. Alikuwa akipinga utawala wa Yehova. Ni kana kwamba Shetani alikuwa akisema: ‘Mungu ni mtawala mbaya. Yeye husema uwongo na kuwanyima raia wake vitu vizuri. Wanadamu hawahitaji kutawaliwa na Mungu. Wanaweza kujiamulia yaliyo mema na mabaya. Na watakuwa na maisha mazuri zaidi nikiwatawala.’ Mungu angeshughulikiaje upinzani huo? Watu fulani husema kwamba afadhali Mungu angewaua tu waasi hao. Lakini je, kufanya hivyo kungetatua upinzani wa Shetani? Je, kungethibitisha kwamba utawala wa Mungu ndio unaofaa?

      9 Yehova hangewaua waasi hao mara moja kwa sababu yeye ni Mungu mwenye haki kabisa. Aliamua kwamba wakati ulihitajiwa ili kutatua upinzani wa Shetani kwa njia yenye kuridhisha na kuthibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo. Kwa hiyo Mungu akaamua kwamba atawaacha wanadamu wajitawale kwa muda fulani chini ya uvutano wa Shetani. Sura ya 11 ya kitabu hiki itaeleza sababu iliyomfanya Yehova aamue hivyo na kuruhusu muda wa kutosha upite kabla ya kutatua masuala hayo. Hata hivyo, kwa sasa ni vizuri kujiuliza hivi: Je, Adamu na Hawa walikuwa na sababu ya kumwamini Shetani ambaye hakuwa amewafanyia jambo lolote zuri? Je, walikuwa na msingi wowote wa kuamini kwamba Yehova ambaye alikuwa amewapa vyote walivyokuwa navyo, ni mwongo na mkatili? Wewe ungefanyaje?

      10. Unawezaje kuunga mkono upande wa Yehova na kumpinga Shetani?

      10 Ni vizuri kufikiria maswali hayo kwa sababu kila mmoja wetu anakabili masuala hayo leo. Naam, wewe una nafasi ya kuunga mkono upande wa Yehova na kumpinga Shetani. Unaweza kumkubali Yehova kuwa Mtawala na kuonyesha kwamba Shetani ni mwongo. (Zaburi 73:28; Methali 27:11) Inasikitisha kwamba, kati ya mabilioni ya watu ulimwenguni pote, ni wachache tu wanaoamua kufanya hivyo. Hilo linatokeza swali muhimu, Je, kweli Biblia inafundisha kwamba Shetani anatawala ulimwengu huu?

      NI NANI ANAYEUTAWALA ULIMWENGU HUU?

      Mkono wa Shetani ukimwonyesha Yesu serikali na falme zote za ulimwengu

      Shetani angewezaje kumwahidi Yesu falme zote za ulimwengu ikiwa hazikuwa zake?

      11, 12. (a) Kushawishiwa kwa Yesu kunaonyeshaje kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu? (b) Ni nini kingine kinachothibitisha kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu?

      11 Yesu hakuwa na shaka yoyote kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu. Pindi moja Shetani alimwonyesha Yesu kimuujiza “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” Kisha Shetani akamwahidi Yesu: “Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” (Mathayo 4:8, 9; Luka 4:5, 6) Hebu fikiria: Je, Shetani angeweza kumshawishi Yesu kwa kutoa ahadi hiyo ikiwa hakuwa mtawala wa falme hizo? Yesu hakupinga kwamba serikali zote hizo za ulimwengu hazikuwa za Shetani. Bila shaka, Yesu angepinga ikiwa hazikuwa za Shetani.

      12 Bila shaka, Yehova ndiye Mungu Mweza-Yote, Muumba wa ulimwengu wetu wa ajabu. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova Mungu au Yesu Kristo ni watawala wa ulimwengu huu. Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Hata Biblia inamwita Shetani Ibilisi “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Kuhusu mpinzani huyo au Shetani, mtume Mkristo Yohana aliandika: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

      JINSI ULIMWENGU WA SHETANI UTAKAVYOONDOLEWA

      13. Kwa nini tunahitaji ulimwengu mpya?

      13 Ulimwengu unazidi kuwa hatari mwaka baada ya mwaka. Kuna majeshi mengi yanayopigana, wanasiasa wafisadi, viongozi wa kidini wanafiki, na wahalifu sugu. Haiwezekani kuubadili ulimwengu kwa ujumla. Biblia inasema kwamba hivi karibuni Mungu atauondolea mbali ulimwengu huu mbovu katika vita vya Har–Magedoni. Kisha ataleta ulimwengu mpya wenye uadilifu.—Ufunuo 16:14-16.

      14. Mungu amemchagua nani awe Mtawala katika Ufalme Wake, na hilo lilitabiriwaje?

      14 Yehova Mungu alimchagua Yesu Kristo awe Mtawala wa Ufalme au serikali Yake ya mbinguni. Biblia ilitabiri hivi zamani: “Kwa maana kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa; na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake. Naye ataitwa . . . Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Kuhusu serikali hiyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Kama tutakavyoona baadaye katika kitabu hiki, karibuni Ufalme wa Mungu utaondolea mbali serikali zote za ulimwengu huu nao utatawala badala ya serikali hizo. (Danieli 2:44) Kisha Ufalme wa Mungu utaleta paradiso duniani.

      ULIMWENGU MPYA U KARIBU!

      Watu wakiimba, wakicheza ala za muziki, na kufurahia maisha katika dunia mpya

      15. “Dunia mpya” ni nini?

      15 Biblia inatuhakikishia hivi: “Kulingana na ahadi yake [Mungu] tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13; Isaya 65:17) Nyakati nyingine Biblia inapotaja “dunia,” inamaanisha watu wanaoishi duniani. (Mwanzo 11:1) Kwa hiyo “dunia mpya” yenye uadilifu ni jamii ya watu watakaopata kibali cha Mungu.

      16. Ni zawadi gani yenye thamani sana ambayo Mungu atawapa wale walio na kibali chake, na tunapaswa kufanya nini ili tuipokee?

      16 Yesu aliahidi kwamba katika ulimwengu mpya unaokuja, wale wanaopata kibali cha Mungu watapokea zawadi ya “uzima wa milele.” (Marko 10:30) Tafadhali fungua Yohana 3:16 na Yohana 17:3 katika Biblia yako, na usome yale ambayo Yesu alisema tunapaswa kufanya ili tupate uzima wa milele. Sasa ona baraka zinazotajwa katika Biblia zitakazofurahiwa na wale wanaostahili kupokea zawadi hiyo ya pekee kutoka kwa Mungu katika dunia itakayokuwa Paradiso.

      17, 18. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba kutakuwa na amani na usalama duniani pote?

      17 Hakutakuwa na uovu, vita, uhalifu, na ujeuri. “Mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia.” (Zaburi 37:10, 11) Kutakuwa na amani kwa sababu ‘Mungu atakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Kisha “mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena”—yaani, milele!—Zaburi 72:7.

      18 Waabudu wa Yehova wataishi kwa usalama. Nyakati zote Waisraeli katika nyakati za Biblia walipomtii Mungu, waliishi kwa usalama. (Mambo ya Walawi 25:18, 19) Litakuwa jambo zuri ajabu kufurahia usalama kama huo katika Paradiso!—Isaya 32:18; Mika 4:4.

      19. Tunajuaje kwamba kutakuwa na chakula kingi katika ulimwengu mpya wa Mungu?

      19 Hakutakuwa na upungufu wa chakula. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Yehova Mungu atawabariki waadilifu wake, na “hakika dunia itatoa mazao yake.”—Zaburi 67:6.

      20. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba dunia nzima itakuwa paradiso?

      20 Dunia nzima itakuwa paradiso. Kutakuwa na makao na bustani zenye kupendeza katika sehemu zilizokuwa zimeharibiwa na wanadamu wenye dhambi. (Isaya 65:21-24; Ufunuo 11:18) Kadiri wakati unavyopita, sehemu za dunia zinazokaliwa zitapanuka mpaka dunia yote iwe yenye kupendeza na kuzaa sana kama bustani ya Edeni. Na Mungu hatakosa kamwe ‘kufumbua mkono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’—Zaburi 145:16.

      21. Ni nini kinachoonyesha kwamba kutakuwa na amani kati ya wanadamu na wanyama?

      21 Kutakuwa na amani kati ya wanadamu na wanyama. Wanyama mwitu na wa kufugwa watalisha pamoja. Hata mtoto mdogo hataogopa wanyama ambao ni hatari leo.—Isaya 11:6-9; 65:25.

      22. Ni hatua gani itakayochukuliwa kuhusiana na magonjwa?

      22 Magonjwa hayatakuwapo. Akiwa Mtawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu, Yesu ataponya watu kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko alivyofanya alipokuwa duniani. (Mathayo 9:35; Marko 1:40-42; Yohana 5:5-9) Hatimaye, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24; 35:5, 6.

      23. Kwa nini ufufuo utaleta shangwe mioyoni mwetu?

      23 Wapendwa waliokufa watafufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele. Wote wanaolala katika kifo walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa. “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29.

      24. Unaonaje kuhusu kuishi katika Paradiso duniani?

      24 Wale wanaoamua kujifunza kuhusu Muumba wetu Mtukufu, Yehova Mungu na kumtumikia wana tumaini zuri kama nini! Yesu alikuwa akizungumzia Paradiso ya wakati ujao hapa duniani alipomwahidi hivi yule mtenda maovu aliyetundikwa pamoja naye: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Tunapaswa kujifunza mengi zaidi kumhusu Yesu Kristo, atakayetumiwa kuleta baraka hizo zote.

      MAMBO AMBAYO BIBLIA INAFUNDISHA

      • Kusudi la Mungu la kuifanya dunia iwe paradiso litatimia.—Isaya 45:18; 55:11.

      • Shetani ndiye anayeutawala ulimwengu huu.—Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19.

      • Katika ulimwengu mpya unaokuja, Mungu atawabariki sana wanadamu.—Zaburi 37:10, 11, 29.

  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
    • SURA YA NANE

      Ufalme wa Mungu Ni Nini?

      • Biblia inatufundisha nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

      • Ufalme wa Mungu utafanya nini?

      • Ufalme huo utatimiza mapenzi ya Mungu duniani wakati gani?

      1. Tutazungumzia sala gani inayojulikana sana?

      MAMILIONI ya watu ulimwenguni wanajua sala ambayo wengi huiita Sala ya Baba Yetu, au Sala ya Bwana. Majina hayo mawili yanarejelea ile sala inayojulikana sana ambayo Yesu Kristo mwenyewe aliitoa kama kielelezo. Ni sala yenye maana sana, na kuchunguza mambo matatu ya kwanza katika sala hiyo kutakusaidia kujua mambo mengi ambayo Biblia inafundisha.

      2. Ni mambo gani matatu ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake waombe?

      2 Mwanzoni mwa sala hiyo ya kielelezo, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake hivi: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’” (Mathayo 6:9-13) Mambo hayo matatu yanayoombwa yanamaanisha nini?

      3. Tunahitaji kujua nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

      3 Tayari tumejifunza mengi kuhusu jina la Mungu, Yehova. Na kwa kadiri fulani tumezungumzia mapenzi ya Mungu, yaani, mambo ambayo amefanya na yale atakayowafanyia wanadamu. Hata hivyo, Yesu alimaanisha nini alipotuambia tusali: “Ufalme wako uje”? Ufalme wa Mungu ni nini? Ufalme huo utakapokuja, utalitakasaje jina la Mungu au kulifanya liwe takatifu? Na kuja kwa Ufalme huo kunahusianaje na kutendeka kwa mapenzi ya Mungu?

      UFALME WA MUNGU NI NINI?

      4. Ufalme wa Mungu ni nini, na Mfalme wake ni nani?

      4 Ufalme wa Mungu ni serikali iliyosimamishwa na Yehova Mungu ikiwa na Mfalme ambaye amechaguliwa na Mungu. Mfalme wa Ufalme wa Mungu ni nani? Ni Yesu Kristo. Yesu akiwa Mfalme, ni mkuu kuliko watawala wa kibinadamu na anaitwa “Mfalme wa wale wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wanaotawala wakiwa mabwana.” (1 Timotheo 6:15) Ana nguvu za kufanya mambo mengi mazuri kuliko mtawala yeyote wa kibinadamu, hata yule aliye bora zaidi.

      5. Ufalme wa Mungu unatawala kutoka wapi, nao utatawala nini?

      5 Ufalme wa Mungu utatawala kutoka wapi? Kwani, Yesu yuko wapi? Unakumbuka, tulijifunza kwamba aliuawa kwenye mti wa mateso, na baadaye akafufuliwa. Muda mfupi baadaye, alirudi mbinguni. (Matendo 2:33) Kwa hiyo, huko ndiko Ufalme wa Mungu uliko, yaani, mbinguni. Ndiyo sababu Biblia huuita ‘ufalme wa mbinguni.’ (2 Timotheo 4:18) Ingawa Ufalme wa Mungu uko mbinguni, utatawala dunia.—Ufunuo 11:15.

      6, 7. Kwa nini Yesu ni Mfalme wa pekee?

      6 Kwa nini Yesu ni Mfalme wa pekee? Sababu moja ni kwamba, hatakufa kamwe. Ikimlinganisha na wafalme wa kibinadamu, Biblia inamwita Yesu “yeye peke yake asiyeweza kufa, anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa.” (1 Timotheo 6:16) Hilo linamaanisha kwamba mambo yote mazuri ambayo Yesu atafanya yatadumu. Naye kwa kweli atafanya mambo mengi mazuri.

      7 Hebu fikiria unabii huu wa Biblia kumhusu Yesu: “Roho ya Yehova itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumwogopa Yehova; naye atakuwa na shangwe katika kumwogopa Yehova. Na hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isaya 11:2-4) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yesu atakuwa Mfalme mwadilifu na mwenye huruma atakayetawala watu wa dunia. Je, ungependa kuwa na mtawala kama huyo?

      8. Ni nani watakaotawala pamoja na Yesu?

      8 Jambo lingine kuhusu Ufalme wa Mungu ni kwamba Yesu hatatawala akiwa peke yake. Atatawala pamoja na wengine. Kwa mfano, mtume Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Tukiendelea kuvumilia, tutatawala pamoja pia tukiwa wafalme.” (2 Timotheo 2:12) Naam, Paulo, Timotheo, na waaminifu wengine ambao wamechaguliwa na Mungu watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa mbinguni. Ni wangapi watakaokuwa na pendeleo hilo?

      9. Ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Yesu, na Mungu alianza kuwachagua lini?

      9 Kama tulivyoona katika Sura ya 7 ya kitabu hiki, mtume Yohana aliona katika maono “Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya Mlima Sayuni [akiwa mfalme mbinguni], na pamoja naye 144,000 wakiwa na jina lake na jina la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao.” Hao 144,000 ni nani? Yohana mwenyewe anatuambia hivi: “Hao ndio wale wanaoendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda. Hao walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 14:1, 4) Ndiyo, ni wafuasi waaminifu wa Yesu Kristo waliochaguliwa hasa kutawala mbinguni pamoja naye. Baada ya kufufuliwa na kuenda mbinguni, “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia,” pamoja na Yesu. (Ufunuo 5:10) Tangu siku za mitume, Mungu amekuwa akiwachagua Wakristo waaminifu ili kukamilisha idadi hiyo ya 144,000.

      10. Kwa nini ni mpango wa upendo kwa Yesu na wale 144,000 waliofufuliwa kuwatawala wanadamu?

      10 Mungu alionyesha upendo kwa kufanya mpango ili Yesu na wale 144,000 wawatawale wanadamu. Kwanza, Yesu amewahi kuwa mwanadamu na kuteseka. Paulo alisema kwamba Yesu “si mtu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi.” (Waebrania 4:15; 5:8) Watawala wenzake pia wameteseka na kuvumilia wakiwa wanadamu. Isitoshe, wamepambana na kutokamilika na kukabiliana na magonjwa ya aina mbalimbali. Bila shaka, wataelewa matatizo yanayowakabili wanadamu!

      UFALME WA MUNGU UTAFANYA NINI?

      11. Kwa nini Yesu aliwaambia wanafunzi wake waombe mapenzi ya Mungu yatendeke mbinguni?

      11 Yesu alipowaambia wanafunzi wake waombe Ufalme wa Mungu uje, aliwaambia pia waombe mapenzi ya Mungu yatendeke “duniani kama ilivyo mbinguni.” Mungu yuko mbinguni, na sikuzote malaika waaminifu wamekuwa wakitenda mapenzi yake huko. Hata hivyo, katika Sura ya 3 ya kitabu hiki, tulijifunza kwamba malaika mwovu aliacha kutenda mapenzi ya Mungu na kuwafanya Adamu na Hawa watende dhambi. Katika Sura ya 10, tutajifunza mengi zaidi kuhusu yale ambayo Biblia inafundisha kumhusu malaika huyo mwovu, anayeitwa Shetani Ibilisi. Shetani na malaika walioamua kumfuata, wanaoitwa roho waovu, waliruhusiwa kuishi mbinguni kwa muda. Kwa hiyo, si wote waliokuwa mbinguni walikuwa wakitenda mapenzi ya Mungu. Mambo yangebadilika wakati Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala. Mfalme mpya aliyetawazwa, Yesu Kristo, angepigana vita na Shetani.—Ufunuo 12:7-9.

      12. Ni mambo gani mawili muhimu yanayotajwa katika Ufunuo 12:10?

      12 Maneno yafuatayo ya kinabii yanaeleza jambo ambalo lingetukia: “Nikaisikia sauti kubwa mbinguni ikisema: ‘Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake, kwa sababu [Shetani] mshtaki wa ndugu zetu ametupwa chini, anayewashtaki mchana na usiku mbele za Mungu wetu!’” (Ufunuo 12:10) Je, unaona mambo mawili muhimu yanayotajwa katika mstari huo wa Biblia? Kwanza, Ufalme wa Mungu unaanza kutawala Yesu Kristo akiwa Mfalme. Pili, Shetani anatupwa duniani kutoka mbinguni.

      13. Hali imekuwaje baada ya Shetani kutupwa kutoka mbinguni?

      13 Mambo hayo mawili yamekuwa na matokeo gani? Kuhusu mambo yaliyotokea mbinguni tunasoma hivi: “Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake!” (Ufunuo 12:12) Ndiyo, malaika waaminifu walio mbinguni wanafurahi kwa sababu baada ya Shetani na malaika zake kuondolewa, wote walio mbinguni ni waaminifu kwa Yehova Mungu. Kuna amani na upatano kamili wenye kudumu. Mapenzi ya Mungu yanatendeka mbinguni.

      Matuki ya taabu, vita, uhalifu na uchafuzi wa hali ya hewa

      Kutupwa kwa Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni kulileta ole duniani. Matatizo hayo yatakwisha karibuni

      14. Hali imekuwaje tangu Shetani alipotupwa duniani?

      14 Hata hivyo, namna gani duniani? Biblia inasema: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Shetani ana hasira kwa sababu ametupwa kutoka mbinguni na ana kipindi kifupi tu cha wakati. Kwa hasira anasababisha dhiki, au “ole” duniani. Tutajifunza mengi zaidi kuhusu “ole” hiyo katika sura inayofuata. Hata hivyo, kwa kuwa Shetani ametupwa duniani na anasababisha dhiki, tunaweza kuuliza, Ufalme huo utafanyaje mapenzi ya Mungu yatendeke duniani?

      15. Mapenzi ya Mungu kwa dunia ni nini?

      15 Kumbuka mapenzi ya Mungu kwa dunia. Ulijifunza kuyahusu katika Sura ya 3. Katika Edeni, Mungu alionyesha kwamba mapenzi yake ni kwamba dunia iwe paradiso iliyojaa jamii ya wanadamu waadilifu na wasiokufa. Shetani aliwafanya Adamu na Hawa watende dhambi, na hilo likachelewesha kutimia kwa mapenzi ya Mungu duniani, lakini kusudi lake halikubadilika. Bado Yehova anakusudia kwamba “waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Na Ufalme wa Mungu utatimiza hayo. Jinsi gani?

      16, 17. Andiko la Danieli 2:44 linasema nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

      16 Hebu fikiria unabii ulio kwenye Danieli 2:44. Tunasoma: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” Hilo linatuambia nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

      17 Kwanza, Ufalme wa Mungu ungesimamishwa “katika siku za wafalme hao,” au wakati falme nyingine zingekuwa zikitawala bado. Pili, Ufalme huo utadumu milele. Hautashindwa wala serikali nyingine haitachukua mahali pake. Tatu, tunaona kwamba kutakuwa na vita kati ya Ufalme wa Mungu na falme za ulimwengu huu. Ufalme wa Mungu utashinda. Hatimaye, Ufalme wa Mungu ndio utakaokuwa serikali pekee inayowatawala wanadamu. Kisha wanadamu watafurahia utawala bora zaidi.

      18. Vita vya mwisho kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za wanadamu vinaitwaje?

      18 Biblia inasema mengi kuhusu vita vya mwisho kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za ulimwengu huu. Kwa mfano, inafundisha kwamba mwisho unapokaribia, roho waovu wataeneza uwongo ili kuwadanganya “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa.” Kwa kusudi gani? “Ili kuwakusanya [wafalme hao] pamoja kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Wafalme wa dunia watakusanywa pamoja “mahali panapoitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.” (Ufunuo 16:14, 16) Kwa sababu ya mambo yanayotajwa katika mistari hiyo miwili, vita vya mwisho kati ya serikali za wanadamu na Ufalme wa Mungu vinaitwa vita vya Har–Magedoni.

      19, 20. Kwa nini mapenzi ya Mungu hayatendeki duniani sasa?

      19 Ufalme wa Mungu utatimiza nini kupitia Har–Magedoni? Fikiria tena mapenzi ya Mungu kwa dunia. Yehova Mungu alikusudia dunia ijae jamii ya wanadamu waadilifu na wakamilifu wakimtumikia katika Paradiso. Kwa nini hilo halitendeki sasa? Kwanza, sisi ni watenda dhambi na tunakuwa wagonjwa na kufa. Hata hivyo, tulijifunza katika Sura ya 5 kwamba Yesu alikufa kwa ajili yetu ili tuweze kuishi milele. Huenda unakumbuka maneno haya yaliyo katika Injili ya Yohana: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

      20 Tatizo lingine ni kwamba watu wengi hutenda maovu. Wanasema uwongo, wanaiba, na kujihusisha katika ukosefu wa maadili. Hawataki kutenda mapenzi ya Mungu. Watu wanaotenda maovu wataharibiwa katika vita vya Mungu vya Har–Magedoni. (Zaburi 37:10) Sababu nyingine pia inayofanya mapenzi ya Mungu yasitendeke duniani ni kwamba serikali haziwatii moyo watu wafanye hivyo. Serikali nyingi hazina uwezo, ni katili, au ni zenye ufisadi. Biblia husema hivi waziwazi: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.

      21. Ufalme utatendaje mapenzi ya Mungu duniani?

      21 Baada ya Har–Magedoni, wanadamu watakuwa chini ya serikali moja tu, Ufalme wa Mungu. Ufalme huo utatenda mapenzi ya Mungu na kuleta baraka nzuri ajabu. Kwa mfano, utamwondoa Shetani na roho wake waovu. (Ufunuo 20:1-3) Nguvu za dhabihu ya Yesu zitatumiwa ili kuwaondolea wanadamu waaminifu magonjwa na kifo. Nao wataishi milele chini ya utawala wa Ufalme. (Ufunuo 22:1-3) Dunia itafanywa kuwa paradiso. Hivyo, Ufalme huo utafanya mpenzi ya Mungu yatendeke duniani na utalitakasa jina la Mungu. Hilo linamaanisha nini? Hilo linamaanisha kwamba hatimaye chini ya Ufalme wa Mungu kila mtu aliye hai atalitukuza jina la Yehova.

      UFALME WA MUNGU UTACHUKUA HATUA WAKATI GANI?

      22. Tunajuaje kwamba Ufalme wa Mungu haukuja Yesu alipokuwa duniani au baada tu ya yeye kufufuliwa?

      22 Yesu alipowaambia wanafunzi wake wasali, “Acha Ufalme wako uje,” ilikuwa wazi kwamba Ufalme huo haukuwa umekuja. Je, ulikuja Yesu alipopaa kuenda mbinguni? Hapana, kwa kuwa Petro na Paulo walisema kwamba baada ya Yesu kufufuliwa, unabii huu katika Zaburi 110:1 ulitimizwa: “Neno la Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’” (Matendo 2:32-34; Waebrania 10:12, 13) Kulikuwa na kipindi cha kungoja.

      Chini ya utawala wa Ufalme, mapenzi ya Mungu yatatendeka duniani kama ilivyo mbinguni

      23. (a) Ufalme wa Mungu ulianza kutawala lini? (b) Sura ifuatayo itazungumzia nini?

      23 Kipindi hicho cha kungoja kingeendelea kwa muda gani? Katika karne ya 19, wanafunzi wanyoofu wa Biblia walikadiria kwamba kipindi hicho kingefikia mwisho mwaka wa 1914. (Kuhusu tarehe hiyo, ona nyongeza “1914—Mwaka Muhimu Katika Unabii wa Biblia.”) Matukio ya ulimwengu yaliyoanza mwaka wa 1914 yanathibitisha kwamba kadirio hilo la wanafunzi wanyoofu wa Biblia lilikuwa sahihi. Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba katika mwaka wa 1914, Kristo alitawazwa kuwa Mfalme, kisha Ufalme wa mbinguni wa Mungu ukaanza kutawala. Hivyo, tunaishi katika kile “kipindi kifupi cha wakati” kinachobaki cha Shetani. (Ufunuo 12:12; Zaburi 110:2) Tunaweza pia kusema kwa hakika kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utachukua hatua ili mapenzi ya Mungu yatendeke duniani. Je, hiyo ni habari njema kwako? Je, unaamini kwamba inawezekana? Sura ifuatayo itakusaidia kuona kwamba Biblia inafundisha mambo haya.

      MAMBO AMBAYO BIBLIA INAFUNDISHA

      • Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni inayotawaliwa na Yesu Kristo pamoja na wale 144,000 ambao wametoka duniani.—Ufunuo 14:1, 4.

      • Ufalme huo ulianza kutawala mwaka wa 1914, na tangu wakati huo Shetani ametupwa duniani kutoka mbinguni.—Ufunuo 12:9.

      • Karibuni Ufalme wa Mungu utaharibu serikali za wanadamu, na dunia itakuwa paradiso.—Ufunuo 16:14, 16.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki