-
Usiruhusu Kitu Chochote Kikutenganishe Na YehovaMnara wa Mlinzi—2013 | Januari 15
-
-
Usiruhusu Kitu Chochote Kikutenganishe Na Yehova
“Jichagulieni leo yule mtakayemtumikia.”—YOS. 24:15.
1-3. (a) Kwa nini Yoshua aliweka mfano mzuri katika kuchagua njia inayofaa maishani? (b) Tunapaswa kukumbuka nini tunapohitaji kufanya maamuzi?
NENO “chagua” lina maana nzito sana. Mtu anayechagua huwa na njia kadhaa za kufanya jambo na kwa kiasi fulani ana hiari ya kuamua atakavyotumia maisha yake. Kwa mfano: Hebu wazia kwamba mwanamume fulani anatembea barabarani, kisha kwa ghafla anafika penye njia panda. Atachagua kufuata njia gani? Ikiwa mwanamume huyo anajua mahali anakoelekea, basi inaelekea kwamba ni njia moja tu itakayomfikisha huko lakini akifuata nyingine atapotea.
2 Biblia ina mifano mingi ya watu waliokabili hali kama hiyo. Kwa mfano, Kaini alilazimika kuchagua ikiwa atatenda kwa hasira au atadhibiti hasira yake. (Mwa. 4:6, 7) Yoshua alipaswa kuchagua ama kumtumikia Mungu wa kweli au kuiabudu miungu ya uwongo. (Yos. 24:15) Lengo au mradi wa Yoshua ulikuwa ni kukaa karibu na Yehova; kwa hiyo, alichagua njia iliyomwelekeza kwenye mradi huo. Kaini hakuwa na mradi kama huo, na alichagua njia ambayo ilimwelekeza mbali na Yehova.
3 Nyakati nyingine, huenda tukalazimika kuchagua kati ya mambo mawili au zaidi. Ikitokea hivyo, kumbuka lengo au mradi wako hasa ni kumtukuza Yehova katika kila jambo unalofanya na kuepuka jambo lolote linaloweza kukuondoa kutoka kwake. (Soma Waebrania 3:12.) Katika makala hii na ile itakayofuata, tutachunguza sehemu saba maishani ambazo hatupaswi kuruhusu chochote kitutenganishe na Yehova.
KAZI YA KIMWILI
4. Kwa nini kazi ya kimwili ni jambo muhimu?
4 Wakristo wana wajibu wa kujitegemeza wenyewe na familia zao. Biblia inaonyesha kwamba mtu yeyote ambaye hataki kuwaandalia mahitaji watu wa nyumba yake, ni mbaya kuliko mtu asiye na imani. (2 The. 3:10; 1 Tim. 5:8) Ni wazi kwamba kazi ya kimwili ni sehemu muhimu ya maisha, lakini usipokuwa mwangalifu, inaweza kukutenganisha na Yehova. Jinsi gani?
5. Ni mambo gani muhimu ya kufikiria tunapochagua kazi?
5 Tuseme kwamba unatafuta kazi. Ikiwa si rahisi kupata kazi ya kuajiriwa katika eneo lenu, huenda ukashawishiwa kukubali kazi yoyote unayopata. Hata hivyo, namna gani ikiwa kazi hiyo haipatani na kanuni za Biblia? Namna gani ikiwa ratiba au safari za kikazi zitaathiri utendaji wako wa Kikristo au kukufanya uishi mbali na familia yako? Je, utakubali kazi hiyo, ukifikiri kwamba ni afadhali kuwa na kazi isiyofaa kuliko kutokuwa na kazi? Kumbuka kwamba kuchagua njia isiyofaa kunaweza kukutenganisha na Yehova. (Ebr. 2:1) Unawezaje kufanya maamuzi ya hekima unapotafuta kazi au unapotaka kubadili kazi?
6, 7. (a) Ni miradi gani ambayo mtu anaweza kuwa nayo kuhusu kazi ya kimwili? (b) Ni mradi gani utakaokuleta karibu zaidi na Yehova, na kwa nini?
6 Kama ilivyotajwa mwanzoni, kumbuka lengo lako. Jiulize hivi: ‘Ninataka kazi yangu inisaidie kutimiza jambo gani?’ Ikiwa unaiona kazi ya kimwili kuwa njia ya kukutegemeza wewe na familia yako ili mwendelee kumtumikia Yehova, basi, Yehova atabariki jitihada zako. (Mt. 6:33) Yehova hawezi kamwe kushindwa kukutegemeza unapopoteza kazi au unapokabili matatizo ya ghafla ya kiuchumi. (Isa. 59:1) “Anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”—2 Pet. 2:9.
7 Kwa upande mwingine, namna gani ikiwa mradi wako ni kutajirika tu? Huenda utafanikiwa. Hata kama utafaulu, kumbuka kwamba “ufanisi” wa aina hiyo huwa na madhara makubwa sana. (Soma 1 Timotheo 6:9, 10.) Kukazia fikira kupita kiasi utajiri na kazi ya kimwili kutakutenganisha tu na Yehova.
8, 9. Wazazi wanapaswa kufikiria jambo gani kuhusu mtazamo wao kuelekea kazi ya kimwili? Eleza.
8 Ikiwa wewe ni mzazi, fikiria jinsi mfano wako utakavyowasaidia au kuwaathiri watoto wako. Ni jambo gani wanaloona kuwa ni muhimu zaidi kwako? Je, ni kazi yako au urafiki wako pamoja na Yehova? Wakiona kwamba cheo, umaarufu, na utajiri ndiyo mambo unayotanguliza maishani mwako, je, hawataiga mfano wako na kufuata njia hiyo hatari? Je, inawezekana kwamba hilo litafanya waache kukuheshimu kwa njia fulani ukiwa mzazi? Kijana mmoja Mkristo anasema hivi: “Sikuzote, baba yangu amekuwa akikazia fikira kazi yake tu. Mwanzoni, ilionekana kwamba alifanya kazi kwa bidii sana kwa sababu alitaka familia yetu iwe na maisha bora. Alitaka kututunza vizuri. Lakini katika miaka ya hivi karibuni, mambo yamebadilika. Anafanya kazi daima, halafu ananunua vitu vya anasa ambavyo si vya lazima. Na hilo limefanya familia yetu ijulikane kuwa familia yenye pesa nyingi badala ya familia inayowatia wengine moyo wafuatie miradi ya kiroho. Ningethamini zaidi kama baba yangu angenitegemeza kiroho badala ya kunitegemeza kifedha.”
9 Wazazi, msijitenge mbali na Yehova kwa kukazia fikira kupita kiasi kazi zenu. Kupitia mfano wenu, waonyesheni watoto wenu kwamba mnaamini kabisa kuwa utajiri bora zaidi tunaoweza kuwa nao ni wa kiroho, bali si wa kimwili.—Mt. 5:3.
10. Kijana anaweza kufikiria mambo gani anapochagua kazi ya kimwili?
10 Ikiwa wewe ni kijana anayefikiria kazi ya kimwili, unawezaje kuchagua njia inayofaa? Kama tulivyozungumzia, unapaswa kujua maisha yako yanaelekea wapi. Je, kusomea kazi fulani uliyochagua na kufanya kazi hiyo kutakuwezesha kufuatia mambo ya Ufalme kwa ukamili zaidi au je, kazi hiyo itakutenganisha na Yehova? (2 Tim. 4:10) Je, mradi wako ni kuiga mtindo wa maisha wa watu ambao furaha yao inategemea kuwa na pesa nyingi katika benki au thamani ya hisa walizowekeza? Au je, utachagua kuwa na imani kama Daudi, aliyeandika hivi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate”? (Zab. 37:25) Kumbuka, njia moja itakutenganisha na Yehova, na ile nyingine itakuongoza kwenye maisha bora zaidi. (Soma Methali 10:22; Malaki 3:10.) Utachagua njia gani?a
TAFRIJA NA BURUDANI
11. Biblia inakiri nini kuhusu tafrija na burudani, lakini tunapaswa kukumbuka nini?
11 Biblia haiwakatazi watu kufurahia maisha, wala haisemi kwamba tafrija na burudani ni mambo yanayopoteza wakati. Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Tim. 4:8) Biblia inasema pia kwamba kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kurukaruka,” na inawatia moyo watu wapumzike vya kutosha. (Mhu. 3:4; 4:6) Hata hivyo, usipokuwa mwangalifu, tafrija na burudani zinaweza kukutenganisha na Yehova. Jinsi gani? Tunaweza kukabili hatari ikitegemea mambo mawili, yaani, aina ya tafrija au burudani unayochagua, na muda unaotumia katika mambo hayo.
Tafrija inayofaa na yenye usawaziko huburudisha
12. Unapaswa kufikiria mambo gani kuhusu aina ya tafrija na burudani unayochagua?
12 Kwanza, fikiria kuhusu aina ya tafrija au burudani. Uwe na hakika kwamba unaweza kupata aina inayofaa ya tafrija na burudani nzuri. Hata hivyo, ukweli ni kwamba tafrija na burudani nyingi leo hutukuza mambo ambayo Mungu anachukia, kutia ndani jeuri, kuwasiliana na pepo, na ngono haramu. Kwa hiyo, unahitaji kuchanganua aina ya tafrija na burudani unayofurahia. Inakuathirije? Je, inakuchochea kuwa na roho ya jeuri, mashindano makali, au utaifa? (Met. 3:31) Je, inakumalizia pesa? Je, inaweza kuwakwaza wengine? (Rom. 14:21) Ni watu wa aina gani unaoshirikiana nao katika tafrija na burudani unayochagua? (Met. 13:20) Je, inakuchochea kuwa na tamaa ya kufanya mambo mabaya?—Yak. 1:14, 15.
13, 14. Unapaswa kufikiria nini kuhusu muda unaotumia katika tafrija?
13 Fikiria pia muda unaotumia katika tafrija na burudani. Jiulize hivi: ‘Je, ninatumia muda mwingi sana katika starehe hivi kwamba ninabaki na wakati mchache sana wa kufanya mambo ya kiroho?’ Ukitumia muda mwingi kupita kiasi katika tafrija na burudani, utagundua kwamba wakati wako wa kupumzika hauburudishi. Ukweli ni kwamba wale wanaokuwa na usawaziko katika tafrija na burudani wanafurahia wakati huo zaidi. Kwa nini? Dhamiri haiwasumbui wakati wa burudani kwa sababu wanajua kwamba wametimiza kwanza “mambo yaliyo ya maana zaidi.”—Soma Wafilipi 1:10, 11.
14 Kutumia wakati mwingi katika starehe kunaweza kuonekana kuwa jambo lenye kuvutia, hata hivyo, kufuata njia hiyo ya maisha kunaweza kukutenganisha na Yehova. Kim, dada mwenye umri wa miaka 20 alijifunza jambo hilo katika maisha yake. Anasema hivi: “Nilizoea kwenda kwenye karamu zote. Kila mwisho-juma kulikuwa na karamu kubwa, kuanzia Ijumaa, Jumamosi, hadi Jumapili. Hata hivyo, sasa ninaona kwamba kuna mambo mengi muhimu sana ya kufanya. Kwa mfano, nikiwa painia, mimi huamka saa 12 asubuhi na kuanza utumishi wa shambani, kwa hiyo siwezi kubaki kwenye tafrija hadi saa saba au saa nane usiku. Ninajua kwamba tafrija zote si mbaya, lakini zinaweza kumkengeusha sana mtu. Kama tu ilivyo na mambo mengine yote, tafrija zinapaswa kufanywa kwa usawaziko.”
15. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao kuchagua tafrija inayoburudisha?
15 Wazazi wana daraka la kujiandalia na kuwaandalia watoto wao mahitaji ya kimwili, ya kiroho, na ya kihisia-moyo. Hilo linatia ndani kuandaa tafrija. Ikiwa wewe ni mzazi, usiwanyime watoto furaha kwa kufanya kila tafrija ionekane ni mbaya. Hata hivyo, uwe mwangalifu kuhusu uvutano usiofaa. (1 Kor. 5:6) Ukifikiria kimbele, utapata tafrija na burudani zinazoiburudisha kwelikweli familia yako.b Ukifanya hivyo, wewe na watoto wako mtachagua njia itakayowaleta karibu zaidi na Yehova.
MAHUSIANO YA KIFAMILIA
16, 17. Ni hali gani yenye kuhuzunisha ambayo imewakumba wazazi wengi, na tunajuaje kwamba Yehova anaelewa uchungu wao?
16 Uhusiano kati ya mzazi na mtoto ni wenye nguvu sana hivi kwamba Yehova aliutumia kuonyesha jinsi anavyowapenda watu wake. (Isa. 49:15) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kuhuzunika sana mtu wa familia unayempenda anapomwacha Yehova. Dada mmoja ambaye binti yake alitengwa na ushirika anasema hivi: “Nilishuka moyo sana. Nilijiuliza hivi: ‘Kwa nini alimwacha Yehova?’ Nilijihisi kuwa na hatia, na nilijilaumu.”
17 Yehova anaelewa uchungu wako. Yeye mwenyewe ‘aliumia moyoni’ wakati mshiriki wa kwanza wa familia yake ya wanadamu, na baadaye watu wengi walioishi kabla ya Gharika walipoasi. (Mwa. 6:5, 6) Huenda ikawa vigumu kwa watu ambao hawajapatwa kamwe na jambo kama hilo kuelewa jinsi hali hiyo inavyoumiza sana. Hata hivyo, si jambo la hekima kuruhusu mwenendo usiofaa wa mshiriki wa familia aliyetengwa na ushirika ukutenganishe na Yehova. Hivyo basi, unawezaje kukabiliana na huzuni nyingi wakati mshiriki wa familia anapomwacha Yehova?
18. Kwa nini wazazi hawapaswi kujilaumu mtoto akimwacha Yehova?
18 Usijilaumu kwa sababu ya jambo lililotokea. Yehova amewapa wanadamu uhuru wa kuchagua, na kila mtu katika familia ambaye amejiweka wakfu na kubatizwa lazima ‘aubebe mzigo wake mwenyewe’ wa daraka. (Gal. 6:5) Hatimaye, mtenda-dhambi huyo atatozwa hesabu na Yehova kwa sababu ya uamuzi wake, bali si wewe. (Eze. 18:20) Pia, usiwalaumu watu wengine. Heshimu mpango wa Yehova wa nidhamu. Chukua msimamo wa kumpinga Ibilisi, usichukue msimamo dhidi ya wachungaji wanaochukua hatua ili kulilinda kutaniko.—1 Pet. 5:8, 9.
Si vibaya kutumaini kwamba mpendwa wako atamrudia Yehova
19, 20. (a) Wazazi ambao watoto wao wametengwa na ushirika wanaweza kufanya nini ili wakabiliane na huzuni yao? (b) Wazazi kama hao wana sababu nzuri ya kutumaini nini?
19 Kwa upande mwingine, ukiamua kuwa na kinyongo moyoni kumwelekea Yehova, utajitenga naye. Kwa kweli, mshiriki huyo wa familia anahitaji kuona msimamo wako thabiti wa kumtanguliza Yehova mbele ya jambo lolote lile—kutia ndani mahusiano ya kifamilia. Kwa hiyo, ili ukabiliane na hali hiyo, hakikisha unadumisha hali nzuri ya kiroho. Usijitenge na ndugu na zako waaminifu Wakristo. (Met. 18:1) Mmiminie Yehova hisia zako katika sala. (Zab. 62:7, 8) Usitafute visingizio vya kushirikiana na mshiriki wa familia aliyetengwa na ushirika, kwa mfano, kupitia simu au barua-pepe. (1 Kor. 5:11) Jishughulishe kabisa na utendaji wa kiroho. (1 Kor. 15:58) Dada aliyenukuliwa mwanzoni anasema hivi: “Ninajua kwamba ni lazima niwe na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova na kudumisha hali nzuri ya kiroho ili binti yangu atakapomrudia Yehova, niweze kumsaidia.”
20 Biblia inasema kwamba upendo “hutumaini mambo yote.” (1 Kor. 13:4, 7) Si vibaya kutumaini kwamba mpendwa wako atamrudia Yehova. Kila mwaka, wakosaji wengi wanatubu na kurudi katika tengenezo la Yehova. Yehova hana kinyongo kuelekea wakosaji wanaotubu. Badala yake, ‘yuko tayari kusamehe.’—Zab. 86:5.
FANYA MAAMUZI YA HEKIMA
21, 22. Umeazimia kufanya nini kuhusu jinsi unavyotumia uhuru wako wa kuchagua?
21 Yehova amewapa wanadamu aliowaumba uhuru wa kuchagua. (Soma Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.) Lakini uhuru huo unaambatana na daraka zito. Kila Mkristo anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninafuata njia gani maishani? Je, nimeruhusu kazi ya kimwili, burudani na tafrija, au mahusiano ya kifamilia yanitenganishe na Yehova?’
22 Upendo wa Yehova kuelekea watu wake hauyumbiyumbi kamwe. Tunaweza tu kujitenga na Yehova tukichagua kufuata njia isiyofaa. (Rom. 8:38, 39) Na si lazima iwe hivyo kwetu! Azimia kutoruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova. Makala inayofuata itazungumzia sehemu nyingine nne ambazo unaweza kuonyesha azimio hilo.
a Kwa habari zaidi kuhusu kuchagua kazi ya kimwili, tazama sura ya 38 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.
b Unaweza kupata mapendekezo katika gazeti la Amkeni! la Novemba 2011, ukurasa wa 17-19.
-
-
Endelea Kumkaribia YehovaMnara wa Mlinzi—2013 | Januari 15
-
-
Endelea Kumkaribia Yehova
“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—YAK. 4:8.
1, 2. (a) Shetani anatumia “mbinu” zipi? (b) Ni nini kitakachotusaidia tumkaribie Mungu?
YEHOVA MUNGU aliwaumba wanadamu wakiwa na uhitaji wa kumkaribia yeye. Hata hivyo, Shetani anataka tufikiri kama yeye, kwamba hatumhitaji Yehova. Huo ni uwongo ambao Shetani ameeneza tangu alipoutumia kumdanganya Hawa katika bustani ya Edeni. (Mwa. 3:4-6) Katika historia yote, wanadamu wengi wamefanya kosa hilohilo.
2 Tunafurahi kwamba si lazima tunaswe na mtego huo wa Shetani. “Sisi hatukosi kuzijua mbinu zake.” (2 Kor. 2:11) Shetani anajaribu kututenganisha na Yehova kwa kutuchochea tufanye maamuzi yasiyofaa. Lakini kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, tunaweza kufanya maamuzi yanayofaa tunapochagua kazi ya kimwili, tafrija na burudani, na tunaposhughulikia masuala ya kifamilia. Makala hii itatuonyesha jinsi ya kuwa na usawaziko kuhusiana na teknolojia, afya, pesa, na jinsi kujivunia mambo yanayofaa kunavyoweza kutusaidia ‘kumkaribia Mungu.’—Yak. 4:8.
TEKNOLOJIA
3. Toa mifano inayoonyesha jinsi teknolojia inavyoweza kutumiwa kwa njia nzuri au mbaya.
3 Vifaa vya hali ya juu vya kielektroniki vimeenea ulimwenguni pote. Vifaa hivyo vinaweza kuwa na manufaa mengi sana vikitumiwa vizuri. Lakini tukivitumia isivyofaa, vinaweza kututenganisha na Baba yetu wa mbinguni. Fikiria kuhusu kompyuta. Gazeti unalosoma sasa liliandikwa na kuchapishwa kwa kutumia kompyuta. Kompyuta inaweza kutusaidia sana kufanya utafiti, kuwasiliana, na nyakati nyingine tunaweza kuitumia kufurahia burudani. Hata hivyo, tunaweza pia kuwa waraibu wa teknolojia ya kompyuta. Wafanyabiashara huwasadikisha watu kwa ujanja waamini kwamba ni lazima wawe na vifaa vya kisasa zaidi. Mwanamume mmoja kijana alitamani sana kuwa na kompyuta ya kisasa ya mkononi hivi kwamba aliuza figo yake moja kisiri ili ainunue. Hiyo ni dhabihu ya kipumbavu kama nini!
4. Mkristo mmoja alikabilianaje na tatizo lake la kutumia kompyuta kupita kiasi?
4 Ni jambo la kuhuzunisha hata zaidi kudhabihu urafiki wako pamoja na Yehova kwa sababu ya kuitumia teknolojia vibaya au kupita kiasi. Jon, Mkristo anayekaribia umri wa miaka 30 anasema hivi: “Ninajua Biblia inasema kwamba tunapaswa ‘kununua wakati unaofaa’ kwa ajili ya mambo ya kiroho. Lakini inapohusu kompyuta, ninashindwa kujizuia.”a Mara nyingi, Jon alijikuta akitumia Intaneti hadi usiku wa manane. Anasema hivi: “Kadiri nilivyochoka, ndivyo ilivyokuwa vigumu zaidi kuacha kuwasiliana na wengine kwenye mtandao au kutazama sinema fupifupi, na baadhi ya sinema hizo zilikuwa chafu.” Ili ashinde tabia hiyo mbaya, ilimbidi Jon atumie programu inayozima kompyuta wakati wa kulala unapofika.—Soma Waefeso 5:15, 16.
Wazazi, wasaidieni watoto wenu kutumia teknolojia kwa hekima
5, 6. (a) Wazazi wana madaraka gani kuelekea watoto wao? (b) Wazazi wanawezaje kuhakikisha kwamba watoto wao wana mashirika mazuri?
5 Wazazi, hamhitaji kudhibiti kila jambo ambalo watoto wenu wanafanya, lakini mnahitaji kuchunguza jinsi wanavyotumia kompyuta. Msiwaache waingie katika vituo vya Intaneti vilivyo na maadili mapotovu, michezo yenye jeuri, mashirika mabaya, na mazoea ya kuwasiliana na pepo eti kwa sababu hamtaki kusumbuliwa. Mkifanya hivyo, huenda wakafikiria hivi: ‘Kwa kuwa Baba na Mama hawajali, ni sawa kutazama mambo hayo.’ Mkiwa wazazi, ni kazi yenu kuwalinda watoto wenu, kutia ndani matineja, ili jambo lolote lisiwatenganishe na Yehova. Hata wanyama huwalinda watoto wao kutokana na hatari. Fikiria jinsi ambavyo dubu mwenye watoto angefanya ikiwa watoto wake wangekuwa hatarini!—Linganisha na Hosea 13:8.
6 Wasaidie watoto wako washirikiane na Wakristo wengine, wadogo kwa wakubwa, ambao ni mifano mizuri. Kumbuka kwamba watoto wako wanataka utumie wakati pamoja nao! Kwa hiyo, tenga wakati wa kucheka nao, kucheza nao, na ‘kumkaribia Mungu’ pamoja nao.b
AFYA
7. Kwa nini sote tunajitahidi kudumisha afya nzuri?
7 “U hali gani?” Salamu hiyo ya kawaida inathibitisha ukweli wenye kuhuzunisha. Kwa kuwa wazazi wetu wa kwanza walimruhusu Shetani awatenganishe na Yehova, sisi sote hupatwa na magonjwa. Shetani hutumia ugonjwa kutimiza kusudi lake, kwa kuwa ni vigumu zaidi kumtumikia Yehova tukiwa wagonjwa. Na tukifa, hatuwezi kamwe kumtumikia Yehova. (Zab. 115:17) Hivyo basi, tunajitahidi kadiri tuwezavyo kudumisha afya nzuri.c Na tunapaswa pia kuhangaikia afya na hali njema ya ndugu zetu.
8, 9. (a) Tunawezaje kuepuka kupita mipaka katika masuala ya kiafya? (b) Kuna faida gani za kusitawisha shangwe?
8 Hata hivyo, ni muhimu kuepuka kupita mipaka kuhusiana na jambo hilo. Baadhi ya watu wamewapendekezea wengine kwa bidii vyakula, madawa, au bidhaa fulani, na wamefanya hivyo kwa bidii kuliko wanavyotangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Huenda wanaamini kwa unyoofu kwamba wanawasaidia wengine. Hata hivyo, haifai kuwapendekezea wengine bidhaa za afya au za urembo na mbinu za matibabu kabla au baada ya mikutano katika Jumba la Ufalme au kwenye makusanyiko. Kwa nini?
9 Sisi hukusanyika ili tuzungumzie mambo ya kiroho na kuongeza shangwe yetu, ambayo ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22) Kutoa mawaidha ya kiafya au kupendekeza madawa katika pindi hizo, iwe umeombwa mawaidha au la, kunaweza kuwakengeusha wengine wasizingatie kusudi la kiroho lililofanya tukusanyike na kuwanyang’anya wengine shangwe yao. (Rom. 14:17) Ni lazima kila mtu ajiamulie mwenyewe jinsi anavyoshughulikia masuala ya kiafya. Isitoshe, hakuna mtu anayeweza kutibu magonjwa yote. Hata madaktari bora zaidi wanazeeka na kuwa wagonjwa, na hatimaye hufa. Na kuhangaikia kupita kiasi afya yetu hakuwezi kurefusha maisha yetu. (Luka 12:25) Badala yake, “moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”—Met. 17:22.
10. (a) Ni sifa gani ambazo zinampendeza Yehova? (b) Tunawezaje kufurahia afya kamilifu?
10 Vivyo hivyo, si vibaya kuhangaikia kuwa na sura nzuri. Lakini hatupaswi kung’ang’ana sana kuondoa dalili zote za uzee. Dalili hizo zinaweza kuonyesha ukomavu, heshima, na uzuri wa moyoni. Kwa mfano, Biblia inasema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Met. 16:31) Hivyo ndivyo Yehova anavyotuona, na tunapaswa kujitahidi kuwa na maoni kama yake. (Soma 1 Petro 3:3, 4.) Basi, je, ni jambo la hekima kuhatarisha isivyo lazima afya yetu kwa kufanyiwa upasuaji hatari au kutafuta madawa ya kubadili sura yetu ili tuvutie zaidi? “Shangwe ya Yehova” ndiyo chanzo cha uzuri wa kweli unaong’aa kutoka moyoni, na uzuri huo hautegemei umri au afya ya mtu. (Neh. 8:10) Tutapata afya kamilifu na uzuri wa ujanani katika ulimwengu mpya tu. (Ayu. 33:25; Isa. 33:24) Kabla ya wakati huo, kutumia hekima na kuwa na imani kutatusaidia kubaki karibu na Yehova huku tukiridhika na hali zetu za sasa.—1 Tim. 4:8.
PESA
11. Pesa zinawezaje kuwa mtego?
11 Pesa si mbaya, wala si vibaya kufanya biashara kwa njia ya unyoofu. (Mhu. 7:12; Luka 19:12, 13) Hata hivyo, kusitawisha ‘upendo wa pesa’ kwa hakika kutatutenganisha na Yehova. (1 Tim. 6:9, 10) “Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo,” yaani, kuhangaikia kupita kiasi mahitaji ya lazima maishani, kunaweza kusonga hali yetu ya kiroho. Ndivyo ilivyo pia na “nguvu za udanganyifu wa utajiri,” yaani, kuamini uwongo wa kwamba utajiri huleta usalama na furaha ya kudumu. (Mt. 13:22) Yesu alisema wazi kwamba “hakuna” anayeweza kumtumikia Mungu na utajiri wakati uleule.—Mt. 6:24.
12. Ni mitego gani ya kifedha iliyoenea leo, na tunawezaje kuiepuka?
12 Maoni yasiyofaa kuhusu pesa yanaweza kumfanya mtu atende kwa njia isiyofaa. (Met. 28:20) Ahadi za kupata pesa haraka na kwa njia rahisi zimewafanya watu fulani wanunue tiketi za bahati nasibu au kujiingiza katika miradi ya kibiashara ambayo faida hutegemea idadi ya watu unaowashawishi wajiunge nayo. Wakristo fulani wamewashawishi washiriki wenzao wa kutaniko wajiunge na miradi hiyo. Wengine wamedanganywa kwamba watapata faida kubwa isivyo kawaida wakiwekeza pesa katika biashara fulani. Usiruhusu pupa ikufanye ulaghaiwe. Tumia hekima. Ikiwa unaahidiwa jambo linaloonekana kuwa haliwezekani, basi inaelekea ni la uwongo.
13. Maoni ya Yehova kuhusu pesa yanatofautianaje na ya watu ulimwenguni?
13 Tukitanguliza kwanza “ufalme na uadilifu wake,” Yehova hubariki jitihada zetu zenye usawaziko za kutafuta mahitaji ya lazima. (Mt. 6:33; Efe. 4:28) Yehova hataki tusinzie mikutanoni kwa sababu ya kufanya kazi kupita kiasi wala hapendi tuketi kwenye Jumba la Ufalme huku akili zetu zikitangatanga tukihangaikia pesa. Lakini watu wengi katika ulimwengu wanaamini kwamba ili wawe salama kifedha na kuishi maisha ya starehe wakati ujao, ni lazima watafute pesa kwa kila njia. Mara nyingi, wanawachochea watoto wao kuwa na mradi huohuo wa kimwili. Yesu alionyesha kwamba kufikiria kwa njia hiyo ni kukosa akili. (Soma Luka 12:15-21.) Huenda hilo likatukumbusha kuhusu Gehazi, aliyefikiri kwamba angeweza kutosheleza ulafi wake na bado aendelee kuwa na msimamo mzuri mbele za Yehova.—2 Fal. 5:20-27.
14, 15. Kwa nini hatupaswi kutegemea pesa ili kupata usalama? Toa mfano.
14 Inaripotiwa kwamba tai fulani wamekufa maji kwa sababu hawakumwachilia kutoka kwenye makucha yao samaki aliyekuwa mzito kuliko walivyoweza kubeba. Je, Mkristo anaweza kuwa kama tai hao? Alex, mzee Mkristo anaeleza hivi: “Mimi hutumia vitu kwa uangalifu sana. Ninapokosea na kumimina mafuta mengi ya kujipaka kwenye kiganja, ninarudisha kiasi fulani katika chupa yake.” Hata hivyo, Alex alijiingiza katika biashara ya kununua na kuuza hisa akidhani kwamba baada ya muda mfupi angeacha kazi yake na kuanza utumishi wa upainia. Alitumia wakati mwingi sana kufanya utafiti kuhusu thamani ya hisa na ripoti za soko la hisa. Akitumia pesa alizoweka akibani na mikopo kutoka kwa wauzaji wa hisa, alinunua hisa ambazo wakadiriaji walikuwa wametabiri kwamba zingepanda thamani haraka sana. Kinyume chake, thamani ya hisa hizo ilishuka haraka sana. Alex anasema hivi: “Nilikuwa nimeazimia kupata tena pesa zangu. Nilifikiri kwamba nikiendelea kungoja, thamani ya hisa zangu itapanda tena.”
15 Kwa miezi kadhaa, Alex hangeweza kufikiria jambo lingine lolote. Ilikuwa vigumu kwake kukazia fikira mambo ya kiroho, na alikosa usingizi. Lakini thamani ya hisa zake haikupanda kamwe. Alex alipoteza pesa zake zote na ilimbidi auze nyumba yake. Anakiri hivi: “Niliiumiza sana familia yangu.” Lakini alijifunza jambo muhimu. Anasema hivi: “Sasa ninajua kwamba mtu yeyote anayetegemea mfumo wa Shetani atavunjika moyo kabisa.” (Met. 11:28) Bila shaka, kutumaini pesa, biashara, au uwezo wetu wa kutafuta pesa katika mfumo huu ni sawa na kumtumaini Shetani, “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Kor. 4:4; 1 Tim. 6:17) Tangu wakati huo, Alex amerahisisha maisha yake “kwa ajili ya habari njema.” Anasema kwamba kufanya hivyo kumemwezesha yeye na familia yake kupata furaha zaidi na kumkaribia Yehova zaidi.—Soma Marko 10:29, 30.
KIBURI
16. Kujivunia mambo yanayofaa kunatofautianaje na kiburi?
16 Si vibaya kujivunia mambo yanayofaa. Kwa mfano, sikuzote tunapaswa kujivunia kuwa Mashahidi wa Yehova. (Yer. 9:24) Kujiheshimu kwa njia inayofaa kunatusaidia kufanya maamuzi mazuri na kuepuka kushusha viwango vyetu vya maadili. Lakini kufikiri kwamba mapendeleo au maoni yetu ni yenye thamani sana kunaweza kututenganisha na Yehova.—Zab. 138:6; Rom. 12:3.
Badala ya kutamani pendeleo fulani kutanikoni, furahia kazi yako katika huduma!
17, 18. (a) Taja mifano ya watu fulani katika Biblia waliokuwa wanyenyekevu na wale waliokuwa na kiburi. (b) Ni kwa njia gani ndugu mmoja hakuruhusu kiburi kimtenganishe na Yehova?
17 Biblia ina mifano ya watu waliokuwa na kiburi na wale waliokuwa wanyenyekevu. Mfalme Daudi alitegemea kwa unyenyekevu mwongozo wa Yehova, na Yehova akambariki. (Zab. 131:1-3) Lakini Yehova alimnyenyekeza Mfalme Nebukadneza na Mfalme Belshaza waliokuwa na kiburi. (Dan. 4:30-37; 5:22-30) Hata katika nyakati zetu, tunakabili hali zinazojaribu unyenyekevu wetu. Ryan, mtumishi wa huduma mwenye umri wa miaka 32, alihamia kutaniko lingine. Ryan anasema hivi: “Nilitazamia kwamba ningependekezwa haraka kuwa mzee, lakini mwaka mzima ulipita bila kupendekezwa.” Je, Ryan angekasirika au kuwa na uchungu, akihisi kwamba wazee hawakumheshimu? Je, angeacha kuhudhuria mikutano, na kuruhusu kiburi kimtenganishe na Yehova na watu Wake? Wewe ungefanya nini?
18 Ryan anakumbuka hivi: “Nilisoma kila makala katika machapisho yetu kuhusu matarajio ambayo hayajatimia.” (Met. 13:12) “Nikaanza kutambua kwamba nilihitaji kujifunza subira na unyenyekevu. Nilihitaji kukubali kuzoezwa na Yehova.” Badala ya kujifikiria, Ryan alianza kufikiria jinsi anavyoweza kuwatumikia wengine kutanikoni na shambani. Baada ya muda, alikuwa akiongoza mafunzo kadhaa ya Biblia yenye maendeleo. Anasema hivi: “Bila kutarajia, niliwekwa kuwa mzee mwaka mmoja na nusu baadaye. Sikuhangaikia tena jambo hilo kwa sababu nilikuwa nikifurahia sana huduma yangu.”—Soma Zaburi 37:3, 4.
KAA KARIBU NA YEHOVA!
19, 20. (a) Tunawezaje kuhakikisha kwamba mambo tunayofuatilia kila siku hayatutenganishi na Yehova? (b) Tunaweza kuwaiga watu gani waliokaa karibu na Yehova?
19 Mambo yote yaliyozungumziwa katika makala hii na ile iliyotangulia yana mahali panapofaa katika maisha yetu. Tunajivunia kuwa watumishi wa Yehova. Familia yenye afya nzuri na yenye furaha ni miongoni mwa zawadi bora kutoka kwa Yehova. Tunaelewa kwamba kazi ya kimwili na pesa zinaweza kutusaidia kutosheleza mahitaji yetu. Tunajua kwamba tafrija inaweza kutuburudisha na teknolojia inaweza kutunufaisha. Lakini kufuatilia vitu hivyo wakati usiofaa, kupita kiasi, au kwa njia inayoathiri ibada yetu kunaweza kututenganisha na Yehova.
Usiruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova!
20 Bila shaka Shetani anataka mambo hayo yatutenganishe na Yehova. Hata hivyo, unaweza kuuzuia msiba huo usikupate na usiipate familia yako! (Met. 22:3) Mkaribie Yehova na ukae karibu naye. Tuna mifano mingi katika Biblia inayoweza kutuelimisha kuhusiana na jambo hili. Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwa. 5:22; 6:9) Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Ebr. 11:27) Yesu alitegemezwa daima na Mungu kwa sababu sikuzote alifanya yale yaliyompendeza Baba yake wa mbinguni. (Yoh. 8:29) Iga mfano wao. ‘Shangilia sikuzote. Sali bila kuacha. Kuhusiana na kila jambo toa shukrani.’ (1 The. 5:16-18) Na usiruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova!
a Majina yamebadilishwa.
b Tazama habari yenye kichwa “Kuwalea Watoto Wenye Kutegemeka” katika gazeti la Amkeni! la Oktoba 2011.
c Tazama habari yenye kichwa “Njia Tano za Kuwa na Afya Bora” katika gazeti la Amkeni! la Machi 2011.
-