Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jihadhari Na Mitego Ya Ibilisi!
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Agosti 15
    • Jihadhari Na Mitego Ya Ibilisi!

      ‘Toka katika mtego wa Ibilisi.’​—2 TIM. 2:26.

      UNGEJIBUJE?

      Unahitaji kujichunguza jinsi gani ikiwa una mwelekeo wa kuwachambua-chambua wengine isivyofaa?

      Kutokana na mifano ya Pilato na Petro, unaweza kujifunza nini kuhusu kutoshindwa na woga na misongo ya watu?

      Unawezaje kuepuka kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi?

      1, 2. Katika makala hii tutachunguza mitego ipi ya Ibilisi?

      IBILISI anawawinda watumishi wa Yehova. Lengo lake hasa si kuwaangamiza, kama mwindaji wa wanyama anavyofanya. Badala yake, lengo kuu la Ibilisi ni kunasa windo au mtu akiwa hai na kumtumia mtu huyo kama atakavyo.​—Soma 2 Timotheo 2:24-26.

      2 Ili kunasa windo likiwa hai, huenda mtegaji akatumia mtego wa aina fulani. Huenda akajaribu kumfanya mnyama atoke nje mahali ambapo anaweza kumnasa kwa kitanzi. Au mtegaji anaweza kutumia mtego uliofichwa unaofyatuka ili kumnasa mnyama kwa ghafla. Ibilisi anatumia mitego kama hiyo ili kuwanasa watumishi wa Mungu wakiwa hai. Ikiwa tunataka kuepuka kunaswa, ni lazima tuwe macho na kutii ishara zinazotuonya kwamba kuna mtego au mitego ya Shetani karibu. Makala hii itachunguza jinsi tunavyoweza kujilinda dhidi ya mitego mitatu ambayo Ibilisi ametumia na kufanikiwa kwa kiasi fulani. Mitego hiyo ni (1) usemi usiodhibitiwa, (2) woga na msongo wa watu, na (3) kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi. Makala inayofuata itachunguza mitego mingine miwili ya Shetani.

      ZIMA MOTO WA USEMI USIODHIBITIWA

      3, 4. Kushindwa kuudhibiti ulimi wetu kunaweza kuwa na matokeo gani? Toa mfano.

      3 Ili kuwatimua wanyama mahali wanapojificha, huenda mwindaji akawasha moto sehemu fulani ya pori na kuwanasa wanyama wanapojaribu kukimbia. Kwa njia ya mfano, Ibilisi angependa kuwasha moto katika kutaniko la Kikristo. Ibilisi akifaulu kufanya hivyo, anaweza kufanya ndugu na dada walikimbie kutaniko, mahali penye usalama, na kuanguka mikononi mwake. Tunawezaje kushirikiana na Shetani bila kujua na hivyo kunaswa na mtego wake?

      4 Mwanafunzi Yakobo aliufananisha ulimi na moto. (Soma Yakobo 3:6-8.) Tukishindwa kuudhibiti ulimi wetu, tunaweza kuwasha moto wa mfano unaoenea kwa kasi kutanikoni. Hali hiyo inaweza kutokeaje? Fikiria mfano ufuatao: Kwenye mkutano mmoja wa kutaniko, tangazo linatolewa kwamba dada fulani amewekwa rasmi kuwa painia wa kawaida. Baada ya mkutano huo, dada wawili wahubiri wanazungumza kuhusu tangazo hilo. Mmoja wao anashangilia na kusema kwamba anamtakia painia huyo mpya mafanikio. Yule dada mwingine anatilia shaka nia ya painia huyo na kudai kwamba painia huyo anatafuta tu umaarufu kutanikoni. Ni yupi kati ya wahubiri hao wawili ambaye ungependa awe rafiki yako? Si vigumu kutambua ni dada yupi anayeweza kuwasha moto kutanikoni kupitia usemi wake.

      5. Ili kuzima moto unaosababishwa na usemi usiodhibitiwa, ni vizuri tujichunguze jinsi gani?

      5 Tunawezaje kuzima moto unaosababishwa na usemi usiodhibitiwa? Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Hivyo, hatua ya kwanza ni kuuchunguza moyo wetu. Je, tunaepuka hisia mbaya zinazochochea usemi wenye kuharibu? Kwa mfano, tunaposikia kwamba ndugu mmoja anajitahidi kufikia pendeleo fulani la utumishi, je, tunaamini mara moja kwamba ana nia nzuri, au tunahisi kwamba anachochewa na faida za kichoyo? Ikiwa tuna mwelekeo wa kufikiri kwamba ndugu zetu wanamtumikia Mungu kwa sababu za kichoyo, ni vizuri tukumbuke kwamba Ibilisi alitilia shaka nia ya Ayubu, mtumishi mwaminifu wa Mungu. (Ayu. 1:9-11) Badala ya kumshuku ndugu yetu, ingekuwa vizuri tuchunguze kwa nini tunamchambua-chambua ndugu huyo. Je, kweli tuna sababu nzuri ya kuwa na mawazo kama hayo? Au je, moyo wetu umetiwa sumu na roho isiyo ya upendo iliyoenea katika siku hizi za mwisho?​—2 Tim. 3:1-4.

      6, 7. (a) Taja baadhi ya sababu zinazoweza kutufanya tuwachambue-chambue wengine. (b) Tunapaswa kutendaje tunapotukanwa?

      6 Ona sababu nyingine ambazo huenda zikafanya tuwachambue-chambue wengine. Sababu moja inaweza kuwa kwamba tunatamani mambo tunayofanya yajulikane zaidi. Kwa kweli, huenda tunajaribu kuonyesha kwamba sisi ni bora kwa kuwadharau wengine. Au huenda tunajaribu kutoa visingizio kwa kutofanya jambo lililo sawa. Iwe tunawachambua-chambua wengine kwa sababu tunaongozwa na kiburi, wivu, au kutojiamini, matokeo ni mabaya.

      7 Huenda tukahisi kwamba tuna sababu ya kumchambua mtu fulani. Labda mtu huyo amewahi kutuumiza kwa kusema nasi bila kujidhibiti. Ikiwa ndivyo mambo yalivyo, kulipiza kisasi hakutasuluhisha tatizo hilo. Kutenda kwa njia hiyo kunafanya tu hali iwe mbaya zaidi na kunatimiza mapenzi ya Ibilisi, bali si mapenzi ya Mungu. (2 Tim. 2:26) Ni vizuri tumwige Yesu. Alipokuwa akitukanwa, “hakujibu kwa matukano.” Badala yake, “aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” (1 Pet. 2:21-23) Yesu alikuwa na hakika kwamba Yehova angeshughulikia mambo hayo kwa njia Yake na kwa wakati Wake mwenyewe. Tunapaswa kumtegemea Mungu kwa njia hiyohiyo. Tunaposema mambo mazuri yanayoponya, tunasaidia kudumisha “kifungo chenye kuunganisha cha amani” katika kutaniko letu.​—Soma Waefeso 4:1-3.

      EPUKA MTEGO WA WOGA NA MSONGO WA WATU

      8, 9. Kwa nini Pilato alimhukumu Yesu?

      8 Mnyama anayenaswa katika mtego hana uhuru wa kwenda popote anapotaka. Vivyo hivyo, mtu anayeshindwa na woga na msongo wa watu hupoteza kwa kiasi fulani uhuru wa kudhibiti maisha yake. (Soma Methali 29:25.) Acheni tuchunguze mifano ya wanaume wawili tofauti kabisa walioshindwa na misongo na kuwaogopa wengine ili tuone yale tunayoweza kujifunza kutokana na mambo yaliyowapata maishani.

      9 Gavana Mroma Pontio Pilato alijua kwamba Yesu hakuwa na hatia na inaonekana kwamba hakutaka kumdhuru. Kwa kweli, Pilato alisema kwamba Yesu hakufanya “jambo lolote linalostahili kifo.” Hata hivyo, Pilato aliamua Yesu auawe. Kwa nini? Kwa sababu Pilato alishindwa na msongo wa umati. (Luka 23:15, 21-25) Wapinzani hao walipiga kelele hivi wakimsonga Pilato afanye walichotaka: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari.” (Yoh. 19:12) Huenda Pilato aliogopa kwamba angepoteza cheo chake au labda uhai wake ikiwa angemtetea Kristo. Kwa hiyo, alijiruhusu kushawishiwa kutenda mapenzi ya Ibilisi.

      10. Ni nini kilichomfanya Petro amkane Kristo?

      10 Mtume Petro alikuwa kati ya marafiki wa karibu zaidi wa Yesu. Alitangaza hadharani kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi. (Mt. 16:16) Petro alibaki mshikamanifu wakati wanafunzi wengine walipokosa kuelewa maana ya yale ambayo Yesu alisema na hivyo wakamwacha. (Yoh. 6:66-69) Na maadui walipokuja kumkamata Yesu, Petro aliutumia upanga kumlinda Bwana wake. (Yoh. 18:10, 11) Hata hivyo, baadaye Petro alishindwa na woga na kukana kwamba hata hamjui Yesu Kristo. Kwa kipindi fulani, mtume huyo alinaswa katika mtego wa kuogopa wanadamu na akaruhusu woga huo umzuie kuwa jasiri.​—Mt. 26:74, 75.

      11. Huenda tukalazimika kupambana na uvutano gani mbaya?

      11 Tukiwa Wakristo tunahitaji kushinda misongo ya kufanya mambo yasiyompendeza Mungu. Waajiri au watu wengine wanaweza kujaribu kutulazimisha kufanya mambo ya udanganyifu au wanaweza kutushawishi tujihusishe katika mwenendo mpotovu kingono. Huenda wanafunzi wakashawishiwa na wanafunzi wenzao kuiba mitihani, kutazama ponografia, kuvuta sigara, kutumia madawa ya kulevya, kunywa pombe, au kujihusisha katika mwenendo mpotovu kingono. Kwa hiyo, ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka mtego wa woga na wa msongo wa kufanya mambo yasiyompendeza Yehova?

      12. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na mifano ya Pilato na Petro?

      12 Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mifano ya Pilato na Petro. Pilato alijua mambo machache kumhusu Kristo. Hata hivyo, alijua kwamba Yesu hakuwa na hatia na kwamba hakuwa mtu wa kawaida. Lakini Pilato alikosa unyenyekevu na upendo kumwelekea Mungu wa kweli. Ibilisi alimnasa kwa urahisi akiwa hai. Petro alikuwa na ujuzi sahihi na pia alimpenda Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine alikosa sifa ya kiasi, akawa mwoga, na akashindwa na msongo wa watu. Kabla ya Yesu kukamatwa, Petro alijigamba hivi: “Hata ikiwa wengine wote watakwazika, hata hivyo mimi sitakwazika.” (Marko 14:29) Mtume huyo angejitayarisha vizuri zaidi kukabiliana na majaribu yaliyokuwa mbele yake ikiwa angekuwa na msimamo kama ule wa mtunga-zaburi aliyemtegemea Mungu na kuimba hivi: “Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?” (Zab. 118:6) Usiku wa mwisho wa maisha Yake duniani, Yesu alimchukua Petro na mitume wengine wawili na kuingia ndani kabisa ya bustani ya Gethsemane. Hata hivyo, badala ya kukaa macho, Petro na wenzake walilala usingizi. Yesu aliwaamsha na kusema: “Endeleeni kukesha na kusali, ili msiingie katika jaribu.” (Marko 14:38) Lakini Petro alilala tena na baadaye akashindwa na woga na pia msongo wa watu.

      13. Tunawezaje kushinda misongo ya kufanya jambo fulani baya?

      13 Mifano ya Pilato na Petro inaweza kutufundisha somo lingine muhimu: Ili kufaulu kushinda misongo tunahitaji sifa kama vile ujuzi sahihi, unyenyekevu, kiasi, kumpenda na kumwogopa Yehova Mungu, wala si wanadamu. Ikiwa imani yetu inajengwa juu ya msingi wa ujuzi sahihi, tutasema kwa ujasiri na usadikisho kuhusu imani yetu. Hilo litatusaidia kushinda msongo na woga wa wanadamu. Bila shaka, hatupaswi kamwe kujiamini kupita kiasi. Badala yake, tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba tunahitaji nguvu za Mungu ili kushinda misongo ya watu. Tunahitaji kumwomba Yehova roho yake na pia ni lazima tuache upendo kumwelekea utuchochee kutetea jina na viwango vyake. Zaidi ya hayo, tunahitaji kujitayarisha kukabiliana na misongo kabla jaribu halijatokea. Kwa mfano, kujitayarisha mapema pamoja na kusali kunaweza kuwasaidia watoto wetu kujua vizuri jambo la kufanya watoto wenzao wanapojaribu kuwashawishi wafanye jambo fulani baya.​—2 Kor. 13:7.a

      EPUKA MTEGO UNAOPONDA​—KUJIHISI KUWA NA HATIA KUPITA KIASI

      14. Ibilisi angetaka tukate kauli gani kuhusu makosa tuliyotenda wakati uliopita?

      14 Nyakati nyingine mtego wa wanyama unakuwa ni gogo au jiwe zito linaloning’inizwa juu ya njia ambayo wanyama wanapitia kwa ukawaida. Mnyama asiyekuwa mwangalifu anakanyaga waya, na hivyo kusababisha gogo hilo au jiwe kuanguka na kumponda. Kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi kunaweza kulinganishwa na mzigo mzito wenye kuponda. Tunapofikiria makosa tuliyotenda wakati uliopita, huenda tukahisi ‘tumepondwa kupita kiasi.’ (Soma Zaburi 38:3-5, 8.) Shetani angetaka tukate kauli kwamba hatustahili rehema za Yehova na hatuwezi kutimiza viwango Vyake.

      15, 16. Unawezaje kuepuka kunaswa na mtego wa kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi?

      15 Unawezaje kuepuka mtego huo unaoponda? Ikiwa umefanya dhambi nzito, chukua hatua sasa ili urudishe uhusiano wako pamoja na Yehova. Waone wazee, na uwaombe msaada. (Yak. 5:14-16) Fanya yote uwezayo ili kurekebisha kosa hilo. (2 Kor. 7:11) Ukitiwa nidhamu, usivunjike moyo. Nidhamu inaonyesha kwa hakika kwamba Yehova anakupenda. (Ebr. 12:6) Azimia kutofuata tena hatua zilizokuongoza kwenye dhambi, na utende kulingana na azimio lako. Baada ya kutubu na kugeuka, uwe na imani kwamba dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo inaweza kwa kweli kufunika makosa yako.​—1 Yoh. 4:9, 14.

      16 Baadhi ya watu wanaendelea kujihisi kuwa na hatia kuhusu dhambi ambazo kwa kweli wamesamehewa. Ikiwa unahisi hivyo, kumbuka kwamba Yehova alimsamehe Petro na mitume wengine waliomwacha Mwana Wake mpendwa Yesu wakati ambapo aliwahitaji zaidi. Yehova alimsamehe mwanamume aliyetengwa na kutaniko la Korintho kwa sababu ya upotovu mbaya sana wa maadili lakini baadaye akatubu. (1 Kor. 5:1-5; 2 Kor. 2:6-8) Neno la Mungu linasema kuhusu watu waliotenda dhambi nzito ambao walitubu na kusamehewa na Mungu.​—2 Nya. 33:2, 10-13; 1 Kor. 6:9-11.

      17. Fidia inaweza kutusaidiaje?

      17 Yehova atayasamehe na kuyasahau makosa yetu ya wakati uliopita tukitubu kikweli na kukubali rehema yake. Usihisi kamwe kwamba dhabihu ya fidia ya Yesu haiwezi kufunika dhambi zako. Tukihisi hivyo, tutakuwa tumenaswa na mojawapo ya mitego ya Shetani. Licha ya yale ambayo Ibilisi anataka uamini, ukweli ni kwamba fidia inaweza kufunika dhambi za wote ambao wametenda dhambi na kutubu. (Met. 24:16) Imani katika fidia inaweza kukuondolea mzigo unaokulemea wa kujihisi ukiwa na hatia kupita kiasi na inaweza kukupa nguvu za kumtumikia Mungu kwa moyo, akili, na nafsi yako yote.—Mt. 22:37.

      HATUKOSI KUZIJUA MBINU ZA SHETANI

      18. Tunaweza kuepukaje mitego ya Ibilisi?

      18 Shetani hajali ni mtego upi anaotumia ili kutunasa, mradi tu atunase. Kwa kuwa hatukosi kuzijua mbinu za Shetani, tunaweza kuepuka kushindwa akili na Ibilisi. (2 Kor. 2:10, 11) Hatutanaswa na mitego yake ikiwa tunasali tupewe hekima ya kuvumilia majaribu. Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yak. 1:5) Tunahitaji kutenda kulingana na sala zetu kwa kuwa na funzo la kibinafsi la kawaida na kufuata Neno la Mungu. Machapisho yanayotegemea Biblia yanayotolewa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara yanaonyesha mitego inayotumiwa na Ibilisi na yanatusaidia kuiepuka.

      19, 20. Kwa nini tunapaswa kuchukia mambo mabaya?

      19 Kusali na kujifunza Biblia kunatusaidia kupenda mambo mema. Lakini pia ni jambo muhimu kujifunza kuchukia mambo mabaya. (Zab. 97:10) Kutafakari matokeo mabaya ya kufuatia tamaa za kichoyo kunaweza kutusaidia kuepuka tamaa hizo. (Yak. 1:14, 15) Tunapojifunza kuchukia mambo mabaya na kupenda kikweli yale yaliyo mazuri, tunachukia kabisa mambo ambayo Shetani anatumia kama chambo ili kutunasa; nayo hayawezi kamwe kutuvutia.

      20 Tunashukuru kama nini kwamba Mungu anatusaidia ili Shetani asitushinde akili! Kupitia roho, Neno, na tengenezo Lake, Yehova anatukomboa “kutokana na yule mwovu.” (Mt. 6:13) Katika makala inayofuata, tutajifunza jinsi ya kuepuka mitego mingine miwili ambayo Ibilisi ametumia kwa mafanikio kuwanasa watumishi wa Mungu wakiwa hai.

  • Simama Imara Na Uepuke Mitego Ya Shetani!
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Agosti 15
    • Simama Imara Na Uepuke Mitego Ya Shetani!

      ‘Simama imara na kupinga hila za Ibilisi.’​—EFE. 6:11.

      UNGEJIBUJE?

      Mtumishi wa Yehova anawezaje kuepuka kunaswa na mtego wa kupenda vitu vya kimwili?

      Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo aliyefunga ndoa kutoanguka katika shimo la uzinzi?

      Kwa nini unaamini kwamba kuna faida za kusimama imara dhidi ya kupenda vitu vya kimwili na mwenendo mpotovu wa kingono?

      1, 2. (a) Kwa nini Shetani hana huruma kuelekea watiwa-mafuta na “kondoo wengine”? (b) Ni mitego gani ya Shetani itakayozungumziwa katika makala hii?

      SHETANI IBILISI hana huruma kuwaelekea wanadamu, hasa wale wanaomtumikia Yehova. Kwa kweli, Shetani anapigana vita na watiwa-mafuta wanaobaki duniani. (Ufu. 12:17) Leo, Wakristo hao jasiri wameongoza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na wamewaonyesha watu kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu. Pia, Ibilisi hawapendi hata kidogo “kondoo wengine” ambao wanawaunga mkono watiwa-mafuta na ambao wana tumaini la kuishi milele, tumaini ambalo Shetani hana tena. (Yoh. 10:16) Haishangazi kwamba ana hasira kali sana! Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au la kuishi duniani, bila shaka Shetani hapendezwi na hali yetu njema. Lengo lake ni kutunasa.​—1 Pet. 5:8.

      2 Ili kutimiza lengo lake, Shetani ametega mitego ya aina mbalimbali. Kwa kuwa “amezipofusha akili” za watu wasioamini, hawakubali habari njema na hawawezi kuiona mitego hiyo. Hata hivyo, Ibilisi anawatega pia baadhi ya wale ambao wamekubali ujumbe wa Ufalme. (2 Kor. 4:3, 4) Makala iliyotangulia ilionyesha jinsi tunavyoweza kuepuka mitego mitatu ya Shetani: (1) usemi usiodhibitiwa, (2) woga na msongo wa watu, na (3) kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi. Acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kusimama imara dhidi ya mitego mingine miwili ya Shetani, yaani, kupenda vitu vya kimwili na kishawishi cha kufanya uzinzi.

      KUPENDA VITU VYA KIMWILI—MTEGO UNAOSONGA

      3, 4. Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo yanawezaje kumfanya mtu apende vitu vya kimwili?

      3 Katika mojawapo ya mifano yake, Yesu alisema kuhusu mbegu iliyopandwa katikati ya miiba. Alisema kwamba mtu anaweza kusikia neno, “lakini mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri hulisonga neno, naye huwa asiyezaa matunda.” (Mt. 13:22) Naam, kupenda vitu vya kimwili ni mtego unaotumiwa na adui yetu Shetani.

      4 Kuna mambo mawili ambayo yakiwa pamoja yanaweza kulisonga lile neno. Jambo moja ni “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo.” Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ kuna mambo mengi yanayoweza kukufanya uwe na mahangaiko. (2 Tim. 3:1) Kwa sababu ya kupanda sana kwa gharama ya maisha na ukosefu mkubwa wa kazi, inaweza kuwa vigumu kupata riziki. Huenda pia ukawa na mahangaiko kuhusu wakati ujao na kujiuliza, ‘Je, nitakuwa na pesa za kutosha baada ya kustaafu?’ Kwa sababu ya mahangaiko hayo, watu wengine wamejaribu kufuatia utajiri, wakifikiri kwamba pesa zitawahakikishia usalama.

      5. ‘Nguvu za utajiri’ zinaweza kwa njia gani kuwa za udanganyifu?

      5 Yesu alizungumza kuhusu jambo lingine, yaani, “nguvu za udanganyifu wa utajiri.” Jambo hilo likiwa pamoja na mahangaiko linaweza kulisonga neno. Biblia inakiri kwamba “pesa ni ulinzi.” (Mhu. 7:12) Hata hivyo, si jambo la hekima kufuatia utajiri. Watu wengi wametambua kwamba kadiri wanavyojitahidi kupata utajiri, ndivyo wanavyotumbukia katika mtego wa kupenda vitu vya kimwili. Wengine hata wamekuwa watumwa wa utajiri.​—Mt. 6:24.

      6, 7. (a) Kupenda vitu vya kimwili kunawezaje kumhatarisha mtu kazini? (b) Mkristo anapaswa kufikiria nini anapoombwa kufanya kazi saa za ziada?

      6 Tamaa ya kupata utajiri inaweza kuanza bila mtu kutambua. Kwa mfano, fikiria hali ifuatayo. Mwajiri wako anakufikia na kukwambia hivi: “Nina habari njema! Kampuni yetu imepewa kazi kubwa ya kufanya. Kwa hiyo, itakulazimu kufanya kazi kwa saa nyingi zaidi miezi michache ijayo. Lakini ninakuhakikishia kwamba si kazi ya bure kwa sababu utalipwa pesa nyingi.” Utaitikiaje ukipata fursa kama hiyo? Bila shaka, ni daraka zito kuiandalia familia yako mahitaji ya kimwili, lakini hilo si daraka pekee ulilo nalo. (1 Tim. 5:8) Unapaswa kushughulikia madaraka mengine mengi. Utafanya kazi kwa saa ngapi za ziada? Je, kazi yako ya kimwili itavuruga utendaji wako wa kiroho, kutia ndani mikutano ya kutaniko na jioni yenu ya Ibada ya Familia?

      7 Fikiria kwa uzito uamuzi wako, ni jambo gani unaloona kuwa muhimu, je, ni kiasi cha pesa utakachopata baada ya kufanya kazi saa za ziada au ni jinsi uamuzi huo utakavyoathiri hali yako ya kiroho? Je, tamaa ya kupata pesa zaidi itakufanya uache kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwako? Je, unaweza kuona jinsi kupenda vitu vya kimwili kutakavyokuathiri ikiwa utapuuza afya yako ya kiroho na ya familia yako? Ikiwa unakabili hali hiyo sasa, unawezaje kusimama imara na kuepuka kusongwa na upendo wa vitu vya kimwili?​—Soma 1 Timotheo 6:9, 10.

      8. Ni mifano gani ya Kimaandiko inayoweza kutusaidia kuchunguza mtindo wetu wa maisha?

      8 Ili kuepuka kusongwa na tamaa ya vitu vya kimwili, ni vizuri kuchunguza pindi kwa pindi mtindo wako wa maisha. Usiwe kamwe kama Esau, ambaye alionyesha kwa matendo yake kwamba alidharau mambo ya kiroho! (Mwa. 25:34; Ebr. 12:16) Na bila shaka hupaswi kuwa kama yule mwanamume tajiri aliyeombwa auze vitu vyake, awape maskini, na kumfuata Yesu. Badala ya kufanya hivyo, mwanamume huyo ‘alienda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.’ (Mt. 19:21, 22) Akiwa amenaswa na mtego wa utajiri, mwanamume huyo alipoteza pendeleo kubwa kama nini la kumfuata yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi! Uwe makini ili usipoteze pendeleo la kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo.

      9, 10. Maandiko yanasema nini kuhusu vitu vya kimwili?

      9 Ili kushinda mahangaiko yasiyo ya lazima kuhusu vitu vya kimwili, tii himizo hili la Yesu: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.”​—Mt. 6:31, 32; Luka 21:34, 35.

      10 Badala ya kushindwa na nguvu za udanganyifu wa utajiri, jitahidi kuwa na maoni ya mwandikaji wa Biblia Aguri, aliyesema hivi: “Usiniache niwe maskini sana au tajiri sana. Nipe tu kile ninachohitaji.” (Met. 30:8, Contemporary English Version) Ni wazi kwamba Aguri alielewa kuwa pesa zina uwezo wa kulinda na alielewa pia kuhusu nguvu za udanganyifu wa utajiri. Tambua kwamba mahangaiko ya mfumo huu na nguvu za udanganyifu wa utajiri zinaweza kuharibu hali yetu ya kiroho. Mahangaiko yasiyo ya lazima kuhusu vitu vya kimwili yanaweza kupoteza wakati wako, kukuchosha, na kukufanya ukose hamu ya kufuatia masilahi ya Ufalme. Kwa hiyo, azimia kutonaswa na mtego wa Shetani wa kupenda vitu vya kimwili!​—Soma Waebrania 13:5.

      UZINZI​—SHIMO LILILOFUNIKWA KWA UJANJA

      11, 12. Mkristo anawezaje kufanya uzinzi kazini?

      11 Wawindaji wanaotaka kumnasa mnyama mwenye nguvu huenda wakachimba shimo katika njia ambayo mnyama huyo hupitia mara kwa mara. Mara nyingi shimo hilo hufunikwa na kifuniko chembamba kilichotengenezwa kwa vijiti na udongo. Kishawishi kimoja ambacho Shetani anatumia kwa mafanikio zaidi kinafanana na mtego huo. Ni dhambi ya upotovu wa maadili. (Met. 22:14; 23:27) Baadhi ya Wakristo wameanguka katika shimo hilo kwa kujiruhusu kuingia katika hali zilizowashawishi kwa urahisi kutenda dhambi. Wakristo fulani ambao wamefunga ndoa wameanguka katika uzinzi baada ya kusitawisha uhusiano usiofaa wa kimahaba.

      12 Uhusiano usiofaa wa kimahaba unaweza kusitawi kati yako na mfanyakazi mwenzako. Utafiti mmoja ulionyesha kwamba zaidi ya nusu ya wanawake waliofanya uzinzi na pia wanaume 3 kati ya 4 waliofanya uzinzi walifanya hivyo na mfanyakazi mwenzao. Je, kazi yako ya kimwili inakulazimu kushirikiana na watu wa jinsia tofauti? Ikiwa ndivyo, basi una uhusiano gani pamoja nao? Je, unaweka mipaka ili uhusiano wako pamoja nao usigeuke na kuwa wa kimahaba? Kwa mfano, baada ya mazungumzo ya kawaida tu ya mara kwa mara na mfanyakazi mwenzake mwanamume, dada Mkristo anaweza kumfanya mwanamume huyo kuwa rafiki yake wa karibu, na hata kumweleza matatizo yake ya ndoa. Kwa upande mwingine, baada ya kuwa na urafiki na mfanyakazi mwenzake mwanamke, mwanamume Mkristo huenda akafikiri hivi: “Anajali maoni yangu na kunisikiliza kwa makini ninapozungumza naye. Na hata ananithamini. Laiti ningetendewa hivi nyumbani!” Je, unaweza kuona jinsi Wakristo wanaojiingiza katika hali kama hizo walivyo katika hatari ya kufanya uzinzi?

      13. Uhusiano usiofaa wa kimahaba unaweza kuanza jinsi gani kutanikoni?

      13 Uhusiano usiofaa wa kimahaba unaweza kuanza pia kutanikoni. Fikiria kisa hiki cha kweli. Daniel na mke wake, Sarah,a walikuwa mapainia wa kawaida. Daniel anasema kwamba alikubali mgawo wowote aliopewa kutanikoni. Alikuwa tayari kukubali kila pendeleo alilopata. Danieli aliwafunza Biblia vijana watano wanaume, na watatu kati yao wakabatizwa. Ndugu hao wapya waliobatizwa walihitaji sana msaada. Daniel alipokuwa akishughulikia migawo mbalimbali ya kitheokrasi, mara nyingi Sarah aliwasaidia ndugu hao. Punde si punde, hali hii ikatokea: Ndugu hao waliokuwa wanafunzi wa Biblia wa Daniel walihitaji msaada wa kihisia, na waliupata kutoka kwa Sarah. Naye Sarah alihitaji mtu anayemjali na kumsikiliza, na wanafunzi wa Biblia wa Daniel walifanya hivyo. Mtego hatari ulikuwa umetegwa. Daniel anasema hivi: “Mke wangu alidhoofika kiroho na kuumia kihisia kwa sababu ya kuwasaidia wale wanafunzi kwa miezi mingi. Jambo hilo, pamoja na kwamba nilikuwa nikimpuuza, lilisababisha madhara makubwa sana. Mke wangu alifanya uzinzi na mmoja wa ndugu hao waliokuwa wanafunzi wangu wa Biblia. Alidhoofika kiroho bila mimi kutambua kwa sababu nilijishughulisha sana na migawo yangu ya kutaniko.” Unawezaje kuepuka msiba kama huo?

      14, 15. Ni mambo gani yanayoweza kuwasaidia Wakristo waliofunga ndoa kuepuka shimo la uzinzi?

      14 Ili kuepuka kuanguka ndani ya shimo la uzinzi, tafakari kuhusu maana ya kuwa mshikamanifu kwa mwenzi wako wa ndoa. Yesu alisema hivi: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:6) Usifikiri kamwe kwamba mapendeleo yako ya kitheokrasi ni muhimu zaidi kuliko mwenzi wako wa ndoa. Isitoshe, tambua kwamba kumwacha mara kwa mara mwenzi wako wa ndoa ili kufanya kazi zisizo za lazima huenda kukaonyesha kwamba ndoa yako ni dhaifu na kunaweza kukuongoza katika kishawishi na labda hata dhambi nzito.

      15 Ikiwa wewe ni mzee kutanikoni, unapaswa kulitunza kundi. Mtume Petro aliandika hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Pet. 5:2) Bila shaka, hupaswi kuwapuuza washiriki wa kutaniko walio chini ya uangalizi wako. Hata hivyo, hupaswi kutimiza jukumu lako ukiwa mchungaji na kupuuza jukumu lako ukiwa mume. Lingekuwa jambo lisilo na maana, na hatari, kujitahidi kabisa kulilisha kutaniko huku mwenzi wako wa ndoa “akifa njaa” kiroho nyumbani. Daniel anasema, “Hupaswi kamwe kung’ang’ana kupita kiasi kutimiza mapendeleo yako huku familia yako mwenyewe ikidhoofika kiroho.”

      16, 17. (a) Wakristo waliofunga ndoa wanaweza kuchukua hatua gani zinazofaa kazini ili kuonyesha wazi kwamba hawako tayari kuwa na uhusiano wa kimahaba? (b) Ni habari gani zilizochapishwa zinazoweza kuwasaidia Wakristo kuepuka uzinzi?

      16 Mashauri mengi mazuri yamechapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ili kuwasaidia Wakristo waliofunga ndoa waepuke kuanguka katika mtego wa uzinzi. Kwa mfano, gazeti Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2006, lilitoa shauri hili: “Unapokuwa kazini na kwingineko, jihadhari na hali zinazoweza kufanya uwe na uhusiano wa karibu pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Kwa mfano, kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na mtu wa jinsia tofauti baada ya saa za kazi kunaweza kutokeza kishawishi. Ikiwa wewe ni mwanamume au mwanamke aliyefunga ndoa, unapaswa kuonyesha waziwazi kwa maneno na matendo kwamba hutaki kuwa na uhusiano wa kimahaba isipokuwa na mwenzi wako. Kwa kuwa unafuatia ujitoaji-kimungu, bila shaka hungependa kuwavutia watu kwa kucheza-cheza nao kimapenzi au kwa kuvalia na kujipamba kwa njia isiyofaa. . . . Kuweka picha za mwenzi wako wa ndoa na za watoto wako mahali pa kazi kutakukumbusha na kuwakumbusha wengine kwamba unaipenda familia yako. Azimia kutochochea wala kuruhusu vishawishi vya uhusiano wa kimahaba.”

      17 Makala yenye kichwa “Uaminifu Katika Ndoa Unamaanisha Nini Hasa?” katika gazeti Amkeni! la Aprili 2009 ilionya dhidi ya kuwazia-wazia ukifanya ngono na mtu mwingine ambaye si mwenzi wako wa ndoa. Makala hiyo ilionyesha kwamba kuwazia-wazia ukifanya ngono na mtu ambaye si mwenzi wako wa ndoa kutafanya iwe rahisi zaidi kwako kufanya uzinzi. (Yak. 1:14, 15) Ikiwa umefunga ndoa, lingekuwa jambo la hekima kupitia habari hizo mara kwa mara pamoja na mwenzi wako. Ndoa ni mpango mtakatifu ulioanzishwa na Yehova mwenyewe. Kutenga wakati wa kuzungumza na mwenzi wako wa ndoa kuhusu ndoa yenu ni njia nzuri ya kuonyesha kwamba unathamini mambo matakatifu.​—Mwa. 2:21-24.

      18, 19. (a) Uzinzi unasababisha madhara gani? (b) Kuna faida gani za kuwa mwaminifu katika ndoa?

      18 Ikiwa unashawishiwa kuanzisha uhusiano wa kimahaba usiofaa, tafakari kuhusu madhara ya uasherati na uzinzi. (Met. 7:22, 23; Gal. 6:7) Wale wanaofanya uzinzi wanamchukiza Yehova na kujiumiza wenyewe na pia kuwaumiza wenzi wao wa ndoa. (Soma Malaki 2:13, 14.) Tofauti na hilo, tafakari kuhusu faida wanazopata wale wanaodumisha mwenendo safi. Si kwamba tu wana tumaini la kuishi milele bali pia wanafurahia maisha bora sasa, kutia ndani kuwa na dhamiri safi.​—Soma Methali 3:1, 2.

      19 Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Wale wanaoipenda sheria [ya Mungu] wana amani nyingi, na hakuna kitu cha kuwakwaza.” (Zab. 119:165) Kwa hiyo, pendeni kweli, na ‘mwendelee kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima’ katika nyakati hizi zenye uovu. (Efe. 5:15, 16) Njia tunazofuata zimejaa mitego iliyotegwa na Shetani ili kuwanasa waabudu wa kweli. Lakini tumetayarishwa vizuri ili kujilinda. Yehova ametupatia tunachohitaji ili “kusimama imara” na “kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu”!​—Efe. 6:11, 16.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki