Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kuna Shetani?
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Novemba 1
    • HABARI KUU | JE, SHETANI NI KIUMBE HALISI?

      Je, Kuna Shetani?

      Mchongo unaomwonyesha Shetani, yule malaika mwovu

      Mchongo jijini Madrid, Hispania, unaoonyesha Shetani kama malaika mwovu

      “Nilizaliwa na kulelewa nchini El Salvador. Mama yangu aliniambia hivi nilipokosea: ‘Shetani anakuja kukuchukua!’ Mimi nilimjibu, ‘Mwache aje!’ Nilimwamini Mungu, sikuamini kuna Shetani.”—ROGELIO.

      Je, unakubaliana na Rogelio? Unakubaliana na ipi kati ya hoja zifuatazo?

      • Hakuna Shetani; bali ni alama tu ya kuwakilisha uovu.

      • Shetani yupo, lakini hajihusishi na mambo ya wanadamu.

      • Shetani ni kiumbe wa roho mwenye nguvu ambaye huwashawishi wanadamu.

      Kila mojawapo ya hoja hizo inaungwa mkono na watu wengi. Lakini je, ni muhimu kujua jibu sahihi? Ikiwa hakuna Shetani, basi wale wanaosema kuna Shetani wamepotoshwa. Ikiwa Shetani yupo lakini hajihusishi na wanadamu, basi hakuna haja ya kuogopa. Hata hivyo, ikiwa Shetani anashawishi na kupotosha watu, basi yeye ni kiumbe hatari kuliko wengi wanavyodhani.

      Acheni tuchunguze jinsi Maandiko Matakatifu yanavyojibu maswali yafuatayo: Shetani ni nani au ni nini? Je, ni alama ya uovu au kiumbe wa roho? Ikiwa ni kiumbe wa roho, je, anaweza kukudhuru? Ikiwa ndivyo, unawezaje kujilinda?

  • Je, Shetani Ni Alama tu ya Uovu?
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Novemba 1
    • Shetani akimtazama Ayubu, mwanamume anayeteseka

      HABARI KUU | JE, SHETANI NI KIUMBE HALISI?

      Je, Shetani Ni Alama tu ya Uovu?

      Ni rahisi kudhani kwamba Shetani tunayesoma kumhusu katika Biblia ni alama tu ya uovu. Lakini je, hivyo ndivyo Biblia inavyofundisha? Ikiwa ndivyo, kwa nini Biblia inamtaja Shetani akizungumza na Yesu Kristo na hata Mungu Mweza-Yote mwenyewe? Tuchunguze mifano miwili ya mazungumzo hayo.

      SHETANI ALIPOZUNGUMZA NA YESU

      Yesu alipoanza huduma yake, Shetani alimshawishi kwa mambo matatu. Kwanza, Shetani alijitahidi kumshawishi Yesu atumie vibaya nguvu alizopewa na Mungu ili kukabiliana na njaa yake. Kisha Ibilisi alitaka Yesu ahatarishe uhai wake na kujitafutia sifa. Mwishowe, Shetani alimwahidi Yesu kwamba angempa mamlaka juu ya falme zote za dunia ikiwa angetenda tendo dogo la ibada. Yesu alipinga vishawishi vyote hivyo, na kila mara alinukuu Maandiko.—Mathayo 4:1-11; Luka 4:1-13.

      Yesu alikuwa akizungumza na nani? Je, alikuwa akizungumza na uovu uliokuwa ndani yake mwenyewe? Kulingana na Maandiko, Yesu “amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi.” (Waebrania 4:15) Biblia pia inasema: “Yeye hakufanya dhambi, wala udanganyifu haukupatikana kinywani mwake.” (1 Petro 2:22) Yesu aliendelea kuwa mkamilifu, na alidumisha utimilifu. Hakuruhusu uovu wowote usitawi ndani yake. Ni wazi kwamba Yesu hakuwa akizungumza na uovu wowote ulio ndani yake, badala yake alikuwa akizungumza na kiumbe halisi.

      Mazungumzo hayo yanathibitisha zaidi kwamba Shetani ni kiumbe halisi.

      • Kumbuka kwamba Shetani aliahidi kumpa Yesu falme zote za dunia ikiwa angefanya tendo la ibada. (Mathayo 4:8, 9) Ahadi hiyo haingekuwa na maana yoyote kama hakuna Shetani. Zaidi ya hayo, Yesu hakupinga mamlaka ya Shetani.

      • Baada ya Yesu kupinga vishawishi hivyo, Ibilisi “akamwacha mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Je, katika kisa hiki Shetani ni uovu tu, au ni adui mwenye nguvu?

      • Ona kwamba “malaika wakaja na kuanza kumhudumia.” (Mathayo 4:11) Je, malaika hao ni viumbe wa kiroho waliomfariji na kumsaidia Yesu? Bila shaka! Kama ndivyo, kwa nini tuseme kwamba Shetani ni uovu tu?

      SHETANI ALIPOZUNGUMZA NA MUNGU

      Kisa hiki cha pili kinamhusu Ayubu, mtu aliyemwogopa Mungu. Simulizi hilo linataja pindi mbili ambazo Ibilisi alizungumza na Mungu. Katika pindi hizo mbili, Mungu alimsifu Ayubu kwa sababu ya utimilifu wake. Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu za kichoyo, pia alisema Mungu alimpa mali Ayubu ili amtumikie. Ni kana kwamba Ibilisi alidai alimjua vizuri Ayubu kuliko Mungu alivyomjua. Yehova alimruhusu Shetani kuangamiza mali za Ayubu, kuua watoto wake, na hata kudhoofisha afya yake.a Baadaye, ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa sahihi kumsifu Ayubu, na Shetani alithibitika kuwa mwongo. Mungu alimbariki Ayubu kwa sababu ya utimilifu wake.—Ayubu 1:6-12; 2:1-7.

      Katika mazungumzo yake na Shetani, je, Yehova Mungu alikuwa akizungumza na uovu ulio ndani yake mwenyewe? Biblia inasema hivi: “Mungu wa kweli, njia yake ni kamilifu.” (2 Samweli 22:31) Pia, Neno la Mungu linasema hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova Mungu, Mweza-Yote.” (Ufunuo 4:8) Utakatifu humaanisha kuwa safi, kutakata, kutokuwa na dhambi. Yehova ni mkamilifu na hana dhambi. Kwa hiyo hawezi kamwe kuwa na uovu ndani yake.

      Baada ya kuzungumza na Mungu, Shetani alimsababishia Ayubu madhara halisi

      Hata hivyo, wengine husema kwamba hata Ayubu hakuwa mtu halisi, kwa hiyo mazungumzo hayo yalikuwa hadithi tu. Lakini hivyo ndivyo ilivyo? Mistari mingine ya Biblia huthibitisha kwamba Ayubu alikuwa mtu halisi. Kwa mfano, kwenye andiko la Yakobo 5:7-11, tunaona kwamba Ayubu anatumika kama mfano wa kuwahimiza Wakristo kuvumilia hali ngumu na kuwapa faraja kwamba Yehova huwathawabisha wanaovumilia. Kisa cha Ayubu kingekuwa na umuhimu gani ikiwa Ayubu hakuwa mtu halisi na matatizo yaliyompata hayakutukia? Zaidi ya hayo, kwenye andiko la Ezekieli 14:14, 20, Ayubu anatajwa pamoja na Noa na Danieli katika orodha ya watu watatu waadilifu. Kama Noa na Danieli, Ayubu alikuwa mtu halisi, mwenye imani yenye nguvu. Ikiwa Ayubu alikuwa halisi, kwa nini Shetani ambaye alikuwa chanzo cha mateso ya Ayubu asiwe halisi?

      Kwa kweli, Biblia inamtaja Shetani kuwa kiumbe halisi wa roho. Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli Shetani anaweza kunidhuru mimi na familia yangu katika ulimwengu huu wa leo?’

      NAMNA GANI WAKATI WETU?

      Wazia ikiwa kundi la wahalifu lingevamia mji wenu. Bila shaka usalama ungepungua na maadili ya mji wenu yangeporomoka. Sasa fikiria hali inayofanana na hiyo: Shetani na roho wake waovu—viumbe wa roho ambao kama Shetani, walimwasi Mungu—wametupwa duniani. Kumekuwa na matokeo gani? Fikiria mambo unayoona kwenye taarifa za habari nchini kwenu na duniani pote.

      • Je, unaona kuongezeka kwa ujeuri licha ya jitihada za duniani pote za kuzuia hali hiyo?

      • Je, unaona kuongezeka kwa vitumbuizo vyenye mambo ya uchawi ingawa wazazi wengi wanavichukia?

      • Je, unaona uharibifu mkubwa wa mazingira, licha ya jitihada nyingi za kuzuia hali hiyo?

      • Je, inawezekana kuna tatizo kubwa katika jamii ya wanadamu—na kwamba kuna nguvu fulani inayowaongoza wanadamu kwenye majanga?

      Tafadhali ona kile ambacho Biblia inasema kuhusu chanzo cha matatizo yetu: “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye. . . . Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:9, 12) Baada ya kuchunguza uthibitisho, watu wengi wanakubali kwamba Shetani ni kiumbe hatari, na ndiye anayeupotosha ulimwengu.

      Huenda ukajiuliza jinsi unavyoweza kupata ulinzi. Ni vizuri kufanya hivyo. Makala inayofuata itatoa msaada unaofaa.

      a Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

  • Je, Tunapaswa Kumwogopa Shetani?
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Novemba 1
    • HABARI KUU | JE, SHETANI NI KIUMBE HALISI?

      Je, Tunapaswa Kumwogopa Shetani?

      Mume na mke wakitoka nje ya nyumba yenye hewa chafu na kwenda nje kwenye hewa safi

      Kaboni monoksaidi ni hatari na haionekani kama tu Shetani

      Ni vigumu kuigundua. Haina rangi wala harufu, inaweza kukudhuru bila wewe kutambua. Zaidi ya nusu ya vifo vinavyotokana na sumu husababishwa na kaboni monoksaidi. Hata hivyo, usiwe na wasiwasi. Kuna njia za kuigundua gesi hiyo hatari na kujilinda. Kwa busara watu wengi huweka vifaa vya kuonya nao hutii ving’ora vinapolia.

      Kama ilivyo kaboni monoksaidi, Shetani haonekani, ni vigumu kwa wanadamu kumgundua, naye ni hatari sana! Hata hivyo, Mungu ametuandalia msaada. Ukitumia zawadi zifuatazo hutahitaji kumwogopa Shetani.

      Uhuru wa kuchagua. Andiko la Yakobo 4:7 linatuambia hivi: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” Ingawa Shetani ana nguvu, hawezi kukulazimisha ufanye mambo ambayo hupendi. Una hiari! Andiko la 1 Petro 5:9 linasema hivi: “Chukueni msimamo mkampinge yeye [Ibilisi], mkiwa imara katika imani.” Kumbuka, ni baada tu ya Yesu kumpinga Shetani mara tatu ndipo alipomwacha. (Mathayo 4:11) Wewe pia unaweza kuamua kumpinga Shetani.

      Urafiki na Mungu. Andiko la Yakobo 4:8 linatutia moyo ‘kumkaribia Mungu.’ Yehova anakualika uwe na urafiki wa karibu pamoja naye. Unawezaje kuwa rafiki ya Mungu? Njia bora ya kuanza ni kujifunza mengi kumhusu katika Biblia. (Yohana 17:3) Unapozidi kujifunza kumhusu Yehova utachochewa kumpenda, na upendo huo utakuchochea kufanya mapenzi yake. (1 Yohana 5:3) Kuendelea kumkaribia Mungu kutakuwa na matokeo gani? Yakobo anaendelea kusema: “Naye [Mungu] atawakaribia ninyi.”

      Kijana akijifunza Biblia, kisha anasali kwa Mungu, na baadaye anateketeza vitu vya uchawi

      Yehova hutoa maandalizi ya kiroho ili kutulinda

      Ahadi ya ulinzi. Andiko la Methali 18:10 linasema hivi: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba unapaswa kutumia jina la Mungu kama hirizi. Badala yake, inamaanisha kwamba wale wanaomwabudu Mungu wanaweza kumwomba msaada wakati wowote.

      Mfano mzuri. Andiko la Matendo 19:19 linatuambia jambo zuri kuhusu Wakristo wapya huko Efeso: “Hesabu kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi wakaleta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mtu. Nao wakapiga pamoja hesabu za bei zake na kupata vikiwa na thamani ya vipande 50,000 vya fedha.”a Wakristo hao waliteketeza vitu vyote vilivyohusiana na uchawi, bila kujali hasara ya kifedha waliyopata. Mfano wao unaweza kutufundisha mambo mengi. Leo watu wengi wanapenda ushirikina na uchawi. Hata vifaa au mazoea ya kuwasiliana na pepo ambayo hayaonekani kuwa na madhara, yanaweza kumfanya mtu avamiwe na roho waovu. Ni muhimu kuteketeza chochote kinachohusiana na roho waovu, hata kama kufanya hivyo kutasababisha hasara.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

      Kwa miaka 50, Rogelio aliyetajwa kwenye makala ya kwanza ya gazeti hili, hakuamini kwamba kuna Shetani. Lakini baadaye alibadili maoni yake. Kwa nini? Rogelio anasema hivi, “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilipata Biblia. Kujifunza Biblia kulinisaidia kutambua kwamba Shetani yupo. Ujuzi huo unanisaidia nisinaswe na mitego yake.”

      “Kujifunza Biblia kulinisaidia kutambua kwamba Shetani yupo. Ujuzi huo unanisaidia nisinaswe na mitego yake”

      Je, ungependa kuishi wakati ambao Shetani hatakuwepo tena? Inawezekana! Maandiko yanatabiri kuhusu wakati ambao Shetani, anayewapotosha wengi, atatupwa “ndani ya lile ziwa la moto na kiberiti.” (Ufunuo 20:10) Kwa kweli, moto na kiberiti haviwezi kumdhuru kiumbe wa roho asiyeonekana. Kwa hiyo, ziwa la moto linamaanisha uharibifu wa milele. Shetani hatakuwepo tena. Huo utakuwa wakati wenye shangwe sana kwa wanaompenda Mungu!

      Kwa wakati huu, endelea kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova na sheria zake.b Wazia kuishi wakati ambapo, hatimaye, tutaweza kusema, “Shetani hayupo!”

      a Ikiwa vipande vinavyozungumziwa ni dinari ya Roma, basi jumla ya thamani ya vipande vyote ingekuwa mshahara wa siku kwa wafanyakazi 50,000—pesa nyingi sana!

      b Kwa habari zaidi kuhusu Shetani na uchawi, ona sura ya 10 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mwombe Shahidi wa Yehova yeyote akupatie.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki