Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ugumu wa Utunzaji
    Amkeni!—1997 | Februari 8
    • Ugumu wa Utunzaji

      “NYAKATI nyingine mimi huhisi nitoroke hali hiyo. Lakini alinihitaji kuliko wakati mwingine wowote. Nyakati nyingine nilihisi upweke sana.”—Jeanny, aliyemtunza mume wake mwenye umri wa miaka 29 kwa miezi 18 kabla ya mume kufa kwa uvimbe wa ubongo.a

      “Kuna pindi ambazo namkasirikia mama, kisha najichukia kabisa. Nahisi kwamba nimeshindwa ninapokosa kukabiliana vema na hali.”—Rose, mwenye umri wa miaka 59, aliyemtunza mama yake dhaifu mwenye umri wa miaka 90, ambaye sasa ni mgonjwa kitandani.

      Habari za ugonjwa wa kufisha au wa kusedeka zaweza kuwa pigo kubwa kwa familia na marafiki. “Ugonjwa unapogunduliwa kila familia huhisi upweke. Huenda wasijue mtu yeyote ambaye amepata kuwa na tatizo hilo,” asema Jeanne Munn Bracken, katika kitabu Children With Cancer. Mara nyingi pia wao “hupatwa na mshtuko na kutoamini,” kama alivyokuwa Elsa alipogundua kwamba rafiki yake wa karibu Betty, mwenye umri wa miaka 36, alikuwa na kansa. Sue, ambaye baba yake alikuwa mgonjwa, akawa “mgonjwa, na kuhisi utupu” tumboni alipotambua hatimaye kwamba baba yake alikuwa akifa kwa kansa.

      Washiriki wa familia na marafiki kwa ghafula huenda wakajikuta wakilazimika kuchukua madaraka ya kuwa watunzaji—wakiandaa mahitaji ya kimwili na ya kihisia-moyo ya mgonjwa. Huenda wakahitajika kutayarisha milo yenye lishe nzuri, kusimamia utibabu wake, kupanga kumsafirisha kwa daktari, kuwakaribisha wageni wa mgonjwa, kuandika barua kwa niaba ya mgonjwa na mengi zaidi. Mara nyingi utendaji huo huongezwa katika ratiba ambayo tayari imejaa shughuli.

      Hata hivyo, hali ya mgonjwa izidipo kuwa mbaya kazi ya utunzaji huzidi kuwa ngumu. Hiyo yaweza kutia ndani nini? “Kila kitu!” asema Elsa kuhusu rafiki yake ambaye ni mgonjwa kitandani, Betty. “Kumwosha na kumlisha, kumsaidia anapotapika, na kuondoa mikojo katika mifuko yake ya mkojo.” Ijapokuwa Kathy alikuwa na kazi ya wakati wote, alilazimika kumtunza mama yake mgonjwa. Sue, aliyetajwa mapema, asema juu ya “kupima na kurekodi joto [la baba yake] kila baada ya nusu-saa, akimpangusa kwa sifongo joto lake lilipoongezeka, na kumbadilishia mavazi na matandiko kila baada ya saa chache.”

      Ubora wa utunzaji ambao mgonjwa hupokea utategemea kwa kadiri kubwa hali-njema ya wale wanaomtunza. Lakini, hisi na mahitaji ya wale ambao hutunza wagonjwa mara nyingi hupuuzwa. Ikiwa utunzaji ungetokeza tu maumivu ya mgongo na mabega, tayari huo ungekuwa kazi ngumu. Lakini, kama vile watunzaji wengi watakavyothibitisha, utunzaji huandaliwa kwa gharama kubwa ya kihisia-moyo.

      “Iliaibisha Sana”

      “Mara nyingi uchunguzi hueleza juu ya mikazo inayotokezwa na hali [ya mgonjwa] ya kutotumia akili, tabia ya kuaibisha, na mifoko ya maneno,” laripoti The Journals of Gerontology. Kwa mfano, Gillian afafanua kile kilichotendeka baada ya rafiki mmoja katika mkutano wa Kikristo kuomba kwamba angependa kukutana na mama yake aliye mzee-mzee. “Mama alitazama tu bila kuitikia,” akumbuka Gillian kwa huzuni. “Iliaibisha sana nikalia machozi.”

      “Ni mojawapo ya mambo magumu zaidi kukabiliana nayo,” asema Joan, ambaye mume wake amerukwa akili. “Humfanya asahau adabu,” yeye aeleza. “Tunapokula mikahawani na wengine, nyakati nyingine yeye huenda katika meza nyingine katika chumba cha mlo, akionja jemu, na kurudisha kijiko alichotumia kwenye kibakuli cha jemu. Tunapozuru majirani, anaweza kutema mate kwenye njia ya bustani zao. Ni vigumu sana kujiondolea wazo la kwamba labda wengine wanazungumzia tabia hizo na kumwona kuwa mtu asiye na adabu. Mimi hushtuka sana kwa wazo hilo.”

      “Niliogopa Kwamba Tukiwa Wazembe . . . ”

      Kumtunza mpendwa aliye mgonjwa sana kwaweza kuogofya kwelikweli. Mtunzaji aweza kuogopa kile kiwezacho kutokea ugonjwa huo uzidipo—labda hata akiogopa kwamba mpendwa wake atakufa. Pia anaweza kuogopa kwamba hatakuwa na nguvu au uwezo wa kutimiza mahitaji ya mgonjwa.

      Elsa afafanua hivi sababu zinazofanya awe na hofu: “Niliogopa kwamba ningemwumiza Betty kimwili, hivyo nikiongezea mateseko yake, au kwamba ningefanya kitu ambacho kingefupisha uhai wake.”

      Nyakati nyingine mtunzaji huwa na hofu za mgonjwa. “Baba yangu aliogopa sana kusakamwa kwa chakula na nyakati nyingine angekuwa mwoga sana,” akasema Sue. “Niliogopa kwamba tukiwa wazembe, anaweza kusakamwa kwa chakula na hivyo hofu yake kuu impate.”

      “Unaweza Kuhuzunika kwa Sababu ya Jinsi Walivyokuwa Zamani”

      “Ni kawaida kwa watu wenye mgonjwa wa kusedeka kuwa na huzuni,” lasema Caring for the Person With Dementia. “Ugonjwa wa mgonjwa uzidipo kuwa mbaya, unaweza kupoteza mwandamani na uhusiano ambao ni muhimu kwako. Unaweza kuhuzunika kwa sababu ya jinsi walivyokuwa zamani.”

      Jennifer afafanua jinsi familia yake ilivyoathiriwa na afya ya mama yake iliyozidi kuwa mbaya: “Tulihisi vibaya. Tulikosa yale mazungumzo yake machangamfu. Tulihuzunika sana.” Gillian aeleza: “Sikutaka mama yangu afe, na sikutaka ateseke. Nilikuwa nikilia sana.”

      “Nilihisi Nimekataliwa na Kukasirika”

      Mtunzaji aweza kujiuliza: ‘Kwa nini ni mimi niliyepatwa na jambo hili? Kwa nini wengine hawasaidii? Je, hawawezi kuona nimeshindwa na hali? Kwani huyu mgonjwa hawezi kushirikiana?’ Nyakati nyingine, mtunzaji aweza kukasirika sana kuhusu kile kinachoonekana kuwa madai anayofanyiwa yenye kupita kiasi na yasiyofaa kutoka kwa mgonjwa na vilevile kutoka kwa washiriki wengine wa familia. Rose, aliyetajwa katika utangulizi, asema: “Mara nyingi mimi hujikasirikia—ndani yangu. Lakini mama husema hali hiyo huonekana katika uso wangu.”

      Yule anayeandaa utunzaji aweza kuelekezewa mafadhaiko yote na hasira zote za mgonjwa. Katika kitabu Living With Cancer, Dakt. Ernest Rosenbaum aeleza kwamba wagonjwa wengine “nyakati nyingine waweza kupatwa na ghadhabu na mshuko-moyo ambao wataelekezea mtu aliye karibu zaidi nao . . . Hasira hiyo mara nyingi hudhihirishwa na kukasirikia mambo madogo-madogo ambayo kwa kawaida mgonjwa huyo hata hangejali.” Kwa kueleweka, hilo laweza kuongezea mkazo zaidi hisia-moyo zilizo dhaifu za wale ambao hutunza mgonjwa.

      Kwa mfano, Maria alimtunza vizuri sana rafiki yake aliyekuwa akifa. Lakini, pindi kwa pindi rafiki yake alionekana kuwa mnyetivu kupita kiasi na kufikia mikataa isiyofaa. “Alikuwa akisema maneno yenye kuchoma sana na yenye ufidhuli, akiwaaibisha wapendwa wake,” Maria aeleza. Hiyo ilimwathirije Maria? “Wakati huo, mtu huonekana ‘kumwelewa’ mgonjwa. Lakini nilipoifikiria baadaye, nilihisi nimekataliwa na kukasirika na kukosa uhakika—nikawa sina mwelekeo wa kuonyesha upendo unaohitajika.”

      Uchunguzi uliochapishwa katika The Journals of Gerontology ulikata kauli hivi: “Hasira inaweza kuongezeka sana [na] nyakati nyingine kutokeza jeuri au kufanya utafakari kutumia jeuri.” Watafiti walipata kwamba karibu mtunzaji 1 kati ya kila 5 aliogopa kwamba anaweza kuwa mjeuri. Na zaidi ya 1 kati ya kila 20 hasa alitumia ujeuri kwa mgonjwa wake.

      “Nahisi Nina Hatia”

      Watunzaji wengi husumbuliwa na hisia za hatia. Nyakati nyingine hatia hufuata hasira—yaani, wanahisi hatia kwa sababu wao huhisi hasira nyakati nyingine. Hisia-moyo kama hizo zaweza kuwadhoofisha kufikia hatua ya kwamba wao wahisi hawawezi kuendelea kumtunza mgonjwa huyo.

      Katika hali fulani, hakuna namna ila kumpeleka mgonjwa atunzwe katika makao fulani au hospitali ya utunzaji. Huo waweza kuwa uamuzi wenye kufadhaisha sana ambao waweza kusumbua sana hisia za mtunzaji. “Hatimaye nilipolazimika kumpeleka mama katika makao ya utunzaji, nilihisi namsaliti, nikimtupa,” asema Jeanne.

      Iwe mgonjwa amelazwa hospitalini au la, wapendwa wake waweza kuhisi hatia kwamba hawamtunzi ifaavyo. Elsa alisema: “Mara nyingi nilihisi vibaya kwamba sikuwa na wakati wa kutosha. Nyakati nyingine rafiki yangu hangeniruhusu nimwache.” Huenda kukawa pia na hangaiko juu ya kuacha madaraka mengine ya familia, hasa ikiwa mtunzaji anatumia wakati mwingi sana hospitalini au ikiwa ni lazima afanye kazi kwa muda mrefu zaidi ili kusaidia kulipa bili zinazoongezeka. “Nalazimika kufanya kazi ili kusaidia kulipa gharama,” akaomboleza mama mmoja, “lakini nahisi hatia kwa sababu siwezi kuwatunza watoto wangu.”

      Kwa wazi, watunzaji wanahitaji sana kutegemezwa, hasa baada ya kifo cha mwenye kutunzwa. “Daraka langu kubwa zaidi [baada ya kifo cha mgonjwa] . . . ni kuondoa hisia za hatia za mtunzaji, ambazo mara nyingi hazitajwi,” asema Dakt. Fredrick Sherman, wa Huntington, New York.

      Hisia hizo zisipotajwa, zinaweza kumdhuru mtunzaji na vilevile mgonjwa. Basi, watunzaji wanaweza kufanya nini ili kukabiliana na hisia hizo? Na wengine—washiriki wa familia na marafiki—waweza kufanya nini ili kusaidia?

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

      [Sanduku katika ukurasa wa 5]

      Usiwapuuze!

      “TWAJUA kwamba asilimia 80 ya utunzaji wa wazee-wazee nyumbani hufanywa na wanawake,” asema Myrna I. Lewis, profesa-msaidizi katika idara ya tiba ya jumuiya kwenye Shule ya Tiba ya Mount Sinai, New York.

      Uchunguzi mmoja uliofanywa juu ya watunzaji walio wanawake, uliochapishwa katika Journals of Gerontology,b ulionyesha kwamba asilimia 61 ya wanawake waliripoti kwamba hawakupokea msaada wowote kutoka kwa familia au marafiki. Na zaidi ya nusu (asilimia 57.6) walisema kwamba hawakupokea utegemezo wa kutosha wa kihisia-moyo kutoka kwa waume zao. Katika kitabu Children With Cancer, Jeanne Munn Bracken asema kwamba ingawa mama huenda akawa anabeba mzigo mzito zaidi wa utunzaji, “huenda baba hataki kujishughulisha na utunzaji na badala ya hivyo anajishughulisha mno na kazi yake.”

      Hata hivyo, kuna idadi kubwa ya utunzaji unaofanywa na wanaume, asema Dakt. Lewis. Kwa mfano, waume wenye wake walio na maradhi ya Alzheimer ni wengi. Na kwa hakika wao pia hupatwa na mikazo ya kumtunza mpendwa wao aliye mgonjwa. “Wanaume hao labda ndio walio rahisi zaidi kuathirika kuliko wengine wote,” Lewis aendelea kusema, “kwa sababu mara nyingi wao ni wenye umri mkubwa zaidi ya wake zao na huenda ikawa kwamba wao wenyewe wana afya mbaya. . . . Wengi wao hawajapata mazoezi ya utunzaji wenye kutumika.”

      Familia zahitaji kulinda dhidi ya mwelekeo wa kumlemeza mshiriki mmoja anayeonekana kukabili ugumu huo vema. “Mara nyingi ni mshiriki hususa wa familia ambaye huwa mtunzaji, nyakati nyingine akiwatunza wagonjwa wengine wafuatao,” chasema kitabu Care for the Carer. “Wengi wa hawa ni wanawake ambao tayari wanaendelea kuzeeka. . . . Pia wanawake huonwa kwa ukawaida kuwa watunzaji wafaao ‘kiasili’ . . . , lakini familia na marafiki hawapaswi kuwapuuza.”

      [Maelezo ya Chini]

      b Neno gerontology hufafanuliwa kuwa “sehemu ya ujuzi unaoshughulika na kuzeeka na matatizo ya watu walio wazee-wazee.”

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Watunzaji wahitaji kutegemezwa wanapokabiliana na hisia za hatia na hasira

  • Jinsi ya Kushughulika na Hisia
    Amkeni!—1997 | Februari 8
    • Jinsi ya Kushughulika na Hisia

      JE, WAKATI huu unamtunza mpendwa wako aliye mgonjwa sana? Ikiwa ndivyo, huenda unapatwa na hisia zenye kuvuruga na zenye kuogopesha. Unaweza kufanya nini? Fikiria hisia ambazo baadhi ya watunzaji hung’ang’ana nazo na madokezo yenye kutumika ambayo yamewasaidia kukabili hali.

      Aibu. Pindi kwa pindi, tabia ya mtu ambaye ni mgonjwa yaweza kukuaibisha mbele ya watu wengine. Lakini kwa kuwaeleza marafiki na majirani hali ya ugonjwa wa mpendwa wako kwaweza pia kuwafanya kuwa wenye “hisia-mwenzi” na subira. (1 Petro 3:8) Ikiwezekana, zungumza na familia ambazo pia ziko katika hali kama yako. Huenda aibu isiwe kubwa sana mnapoelezeana mambo mliyojionea. Sue aeleza jambo lililomsaidia: “Nilimsikitikia sana babangu—hiyo ilifanya nisione aibu yoyote. Na ucheshi wake pia ulisaidia.” Ndiyo, ucheshi—wa mgonjwa na wa wale wanaomtunza—ni chombo bora cha kuondoa mikazo ya kihisia moyo.—Linganisha Mhubiri 3:4.

      Hofu. Kutojua hali ya maradhi hayo kwaweza kuogopesha kwelikweli. Ikiwezekana, tafuta ushauri wa wataalamu juu ya kile utakachotarajia ugonjwa huo uzidipo kuwa mbaya. Jifunze jinsi ya kuandaa utunzi chini ya hali hizo. Kwa Elsa, mojawapo ya mambo muhimu zaidi katika kukabiliana na hofu yake lilikuwa kuzungumza na watunzaji wengine na wauguzi wa makao ya kutunzia walio wagonjwa kuhusu kile atakachotazamia hali ya mgonjwa izidipo kuwa mbaya. Jeanny ashauri hivi: “Kabili na kudhibiti hofu zako. Hofu ya kile kiwezacho kutukia mara nyingi ni mbaya kuliko kile kitakachotukia kihalisi.” Dakt. Ernest Rosenbaum apendekeza kwamba chochote kile kinachozisababisha, hofu zako zapaswa “kuzungumziwa zizukapo.”—Linganisha Mithali 15:22.

      Huzuni. Si rahisi kushughulika na huzuni, hasa katika hali za utunzaji. Unaweza kuhuzunikia kupoteza mwandamani, hasa ikiwa mpendwa wako aliye mgonjwa hawezi kuongea tena, kusikiliza vizuri, au hata kukutambua. Wengine hawawezi kuelewa hisia kama hizo mara moja. Kuzungumza juu ya huzuni yako na rafiki mwenye ufahamu ambaye atakusikiliza kwa subira na kwa hisia-mwenzi kwaweza kukutuliza sana.—Mithali 17:17.

      Hasira na Mfadhaiko. Hizo ni matokeo ya kawaida ya kutunza mtu aliye mgonjwa sana ambaye mwenendo wake waweza kuwa mgumu nyakati nyingine. (Linganisha Waefeso 4:26.) Tambua kwamba mara nyingi ni maradhi, wala si mgonjwa, ambayo yanasababisha tabia hiyo yenye kuleta mkazo. Lucy akumbuka: “Nilipokuwa nimekasirika kabisa, nilikuwa nikilia. Kisha ningejaribu kujikumbusha hali na ugonjwa wa huyo mgonjwa. Nilijua kwamba mgonjwa alihitaji msaada wangu. Hilo lingenisaidia kuendelea kumtunza.” Ufahamu wa kina kama huo waweza kukufanya ‘usiwe mwepesi wa hasira.’—Mithali 14:29; 19:11.

      Hatia. Hisia za hatia ni za kawaida sana miongoni mwa watunzaji. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba unafanya kazi muhimu lakini iliyo ngumu sana. Kubali ukweli wa kwamba si sikuzote utaitikia kwa ukamilifu kwa neno na kwa tendo. Biblia yatukumbusha: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2; Waroma 3:23) Usiruhusu hisia zozote za hatia zikuzuie kuchukua hatua ifaayo sasa. Unapohisi umekasirika juu ya jambo ambalo ulisema au kitu ulichofanya, yaelekea utapata kwamba kusema “pole” kutafanya wewe na mgonjwa wako kuhisi afadhali. Mtu mmoja aliyetunza mtu wa ukoo aliyekuwa mgonjwa alishauri hivi: “Fanya yote uwezayo chini ya hali hizo.”

      Mshuko-Moyo. Mshuko-moyo ni wa kawaida sana—na inaeleweka—katika familia zinazokabili magonjwa mabaya. (Linganisha 1 Wathesalonike 5:14.) Mtunzaji anayepatwa na mshuko-moyo aeleza kile kilichomsaidia: “Wengi walikuwa wakitushukuru kwa kuandaa utunzaji. Maneno machache tu ya kutia moyo yaweza kukuimarisha sana uendelee mbele unapokuwa umechoka sana au umeshuka moyo.” Biblia yataarifu hivi: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha, bali neno jema huufurahisha.” (Mithali 12:25) Wengine huenda wasitambue uhitaji wako wa kitia moyo sikuzote. Hivyo, nyakati nyingine, huenda ukalazimika kwanza kutaja “uzito” ulio moyoni mwako ili upokee “neno jema” la kitia moyo kutoka kwa wengine. Ingawa hivyo, hisia za kushuka moyo zikidumu au kuwa kali zaidi, ni afadhali umwone daktari.

      Kutoweza Kusaidia. Huenda ukahisi huwezi kusaidia unapokabili maradhi yenye kulemaza. Kubali uhalisi wa hali yako. Tambua upungufu wako—huwezi kudhibiti afya ya mgonjwa, lakini unaweza kuandaa utunzaji mwororo. Usijitazamie kuwa mkamilifu, wala usitazamie mgonjwa wako au wategemezaji wako kuwa wakamilifu. Kuwa na fikira zilizosawazika hakupunguzi tu hisia za kutoweza kusaidia bali pia hupunguza mzigo wa kazi. Kwa hekima, wengi ambao wametunza mpendwa washauri: Jifunze kukabili hali siku kwa siku.—Mathayo 6:34.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      “Kabili na kudhibiti hofu zako. Hofu ya kile kiwezacho kutukia mara nyingi ni mbaya kuliko kile kitakachotukia kihalisi”

      [Sanduku katika ukurasa wa 7]

      Maneno Yenye Kutia Moyo Kutoka kwa Watunzaji

      “USISONONESHWE na mawazo yasiyofaa kujihusu. Hayo ni ya kawaida katika hali kama hizo. Kwa wazi hupaswi kuficha hisia zako kamwe. Zungumza na mtu kuhusu jinsi unavyohisi, na ukiweza, chukua likizo—nenda kwa muda fulani—ili uweze kuhisi umeburudika.”—Lucy, ambaye kazi yake katika kliniki imehusisha kusaidia idadi fulani ya watunzaji na wagonjwa vilevile.

      “Ikiwa kuna washiriki wa familia au marafiki ambao wanapatikana nao wako tayari kusaidia, acha wasaidie. Ni muhimu kwamba ushiriki mzigo huo na wengine.”—Sue, aliyemtunza baba yake kabla ya baba kufa kwa maradhi ya Hodgkin.

      “Jifunze kuwa mcheshi.”—Maria, aliyesaidia kutunza rafiki yake mpendwa aliyekufa kwa kansa.

      “Dumisha nguvu za kiroho. Mkaribie Yehova, na usali bila kukoma. (1 Wathesalonike 5:17; Yakobo 4:8) Yeye huandaa msaada na faraja kupitia roho yake, Neno lake, watumishi wake wa kidunia, na ahadi zake. Jaribu kuwa mwenye utaratibu mzuri kwa kadiri iwezekanavyo. Kwa kielelezo, hufaa kutengeneza ratiba za dawa na orodha za wasaidizi.”—Hjalmar, aliyemtunza ndugu-mkwe wake aliyekuwa akifa.

      “Jifunze yote uwezayo kuhusu hali ya ugonjwa wa mgonjwa wako. Kufanya hivyo kutakusaidia kujua jambo la kutarajia kutoka kwa mgonjwa wako na kwako wewe mwenyewe na jinsi ya kutunza mgonjwa wako.”—Joan, ambaye mume wake ana maradhi ya Alzheimer.

      “Tambua kwamba wengine wamekabili hali hiyo kabla ya wewe na kwamba Yehova aweza kukusaidia kukabiliana na chochote kile kitakachotokea.”—Jeanny, aliyemtunza mume wake kabla ya mume kufa.

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Ili kutuliza hofu zako, jaribu kujua kwa kadiri uwezavyo kuhusu ugonjwa huo

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Kuzungumza na rafiki mwenye ufahamu kwaweza kukutuliza sana

  • Kumtunza Mtunzaji—Jinsi Wengine Wawezavyo Kusaidia
    Amkeni!—1997 | Februari 8
    • Kumtunza Mtunzaji—Jinsi Wengine Wawezavyo Kusaidia

      “LAWRIE nami tumefunga ndoa kwa miaka 55—muda mrefu—na hiyo imekuwa miaka yenye kufurahisha kama nini! Kama ningeweza kumtunza nyumbani, ningefanya hivyo. Lakini afya yangu ilianza kudhoofika. Mwishowe, nililazimika kumpeleka katika makao ya utunzaji. Maumivu ya kihisia-moyo ya kueleza jambo hilo hunilemea kabisa. Nampenda na kumstahi sana nami humtembelea mara nyingi iwezekanavyo. Kihalisi, siwezi kusaidia zaidi.”—Anna, mwanamke mwenye umri wa miaka 78 ambaye kwa zaidi ya miaka 10 amemtunza mumeye ambaye ana maradhi ya Alzheimer na ambaye pia amemtunza binti yake mwenye ugonjwa wa Down kwa miaka 40 ambayo imepita.a

      Kisa cha Anna ni cha kawaida sana. Uchunguzi mmoja uliofanywa katika Visiwa vya Uingereza ulifunua kwamba “katika marika fulani (miaka ya 40 na 50) mwanamke mmoja kati ya kila wanawake wawili ni mtunzaji.” Kama ilivyojadiliwa mapema, mvurugo wa kihisia-moyo na matatizo ambayo watunzaji hukabili yaweza kuonekana nyakati nyingine kama hayawezi kuvumilika.

      “Nafikiri angalau asilimia 50 ya watunzaji hushuka moyo katika mwaka wa kwanza wa utunzaji,” asema Dakt. Fredrick Sherman, wa Shirika la Marekani la Matatizo na Magonjwa ya Walio Wazee-Wazee. Kwa wenzi wa ndoa walio wazee-wazee kama Anna, nguvu zao na afya zao zinazodhoofika zenyewe zaweza kufanya iwe vigumu zaidi kwao kushughulikia hali.

      Ili kusaidia watunzaji wakabili madaraka yao, twahitaji kutambua mahitaji yao. Hayo ni yapi, nasi twawezaje kuyatimiza?

      Watunzaji Wahitaji Kuzungumza

      “Nilihitaji kitulizo,” akasema mwanamke mmoja aliyesaidia kumtunza rafiki yake aliyekuwa akifa. Kama ilivyoonyeshwa katika makala inayotangulia, mara nyingi ni rahisi kukabili na kushughulikia matatizo mtu akiweza kuyazungumzia na rafiki mwenye ufahamu. Watunzaji wengi ambao huhisi wamenaswa na hali zao hupata kwamba kuzungumza juu ya hali zao husaidia kuelewesha hisia zao na kuondoa mkazo waliokuwa nao.

      “Nilithamini sana wakati marafiki walipotambua kwamba sote wawili tulihitaji kutiwa moyo,” akumbuka Jeanny juu ya wakati ambapo alikuwa akimtunza mume wake. Yeye aeleza kwamba wale wanaoandaa utunzaji wahitaji kitia-moyo na nyakati nyingine, mtu wa kuwasikiliza kwa hisia-mwenzi na kuwafariji. Hjalmar, aliyesaidia kutunza ndugu-mkwe wake aliyekuwa mgonjwa, akubali: “Nilihitaji mtu ambaye angesikiliza hofu na matatizo yangu na kuelewa jinsi nilivyohisi.” Kuhusu rafiki wa karibu, Hjalmar aongezea: “Nilifurahia sana kumtembelea, hata kwa nusu saa tu. Alikuwa akinisikiliza. Alijali sana. Nilifarijika sana baada ya hapo.”

      Watunzaji waweza kupata kitia-moyo kingi kutoka kwa msikilizaji mwenye ufahamu. ‘Uwe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema,’ Biblia yashauri kwa hekima. (Yakobo 1:19) Ripoti moja katika The Journals of Gerontology ilifunua kwamba “kujua tu kwamba unategemezwa mara nyingi kwatosha kukufariji sana.”

      Lakini, mbali na usikilizi mzuri na utegemezo, watunzaji wanahitaji nini kingine?

      Kuandaa Msaada Wenye Kutumika

      “Mgonjwa na familia hunufaika na njia yoyote ile ambayo upendo na kitia-moyo zaweza kuonyeshwa,” aonelea Dakt. Ernest Rosenbaum. Kwanza, “upendo na kitia-moyo” zaweza kuonyeshwa mtu anapozuru kibinafsi, wakati wa kuongea kwa simu, au katika barua fupi (labda ikiandamana na maua au zawadi fulani).

      “Nilifarijika marafiki wetu walipotutembelea kifupi,” akumbuka Sue juu ya utegemezo ambao familia yake ilipokea wakati ambapo baba yake alikuwa akifa kwa maradhi ya Hodgkin. “Mmoja wa marafiki wangu,” aendelea kusema, “alijibu simu na kusaidia kufua nguo na kuzipiga pasi.”

      Kutegemeza watunzaji kwaweza, na kwapaswa, kutia ndani msaada hususa wenye kuonekana. Elsa akumbuka: “Niliona kuwa jambo la msaada marafiki waliponisaidia kwa njia yenye kutumika. Wao hawakusema tu: ‘Kama kuna kitu niwezacho kufanya, nijulishe.’ Badala ya hivyo, wao walisema: ‘Naenda dukani. Nikuletee nini?’ ‘Je, nitunze bustani yako?’ ‘Naweza kuketi na mgonjwa na kumsomea.’ Jambo jingine tuliloona kuwa lenye kutumika lilikuwa ni kupanga wageni waandike ujumbe katika kitabu wakati rafiki yangu mgonjwa alipokuwa amechoka au kama alikuwa amelala usingizi. Kufanya hivyo kulitufanya sisi sote tuwe na furaha.”

      Kutoa msaada hususa kwaweza kutia ndani kufanya kazi zozote zile za nyumbani. Rose aeleza: “Nilithamini misaada ya kutandika vitanda, kuandika barua za mgonjwa, kuwakaribisha wageni wa mgonjwa, kupata dawa, kuosha na kutengeneza nywele, kuosha vyombo.” Familia na marafiki waweza pia kusaidia mtunzaji kwa kuchukua zamu ya kutayarisha chakula.

      Mahali ifaapo, waweza kuwa msaada wenye kutumika kusaidia na mambo ya msingi ya utunzaji. Kwa mfano, mtunzaji aweza kuhitaji msaada wa kumlisha au kumwogesha mgonjwa.

      Washiriki wa familia wenye kujali waweza kuandaa msaada wenye kutumika katika hatua za mapema za ugonjwa, lakini vipi kama huo ni ugonjwa wa kusedeka? Tukinaswa na ratiba zetu zenye shughuli nyingi, ni rahisi kwetu kusahau mkazo unaoendelea—na labda wenye kuongezeka—ambao watunzaji wanakabili. Lingekuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini ikiwa utegemezo wenye kuhitajika sana ungeanza kwisha!

      Jambo hilo likitendeka, inaweza kufaa kwa mtunzaji kuitisha mkutano wa familia ili kujadili utunzaji wa mgonjwa. Mara nyingi inawezekana kuomba msaada wa marafiki na watu wa ukoo ambao wameonyesha kwamba wako tayari kusaidia. Hivyo ndivyo Sue na familia yake walivyofanya. “Mahitaji yalipotokea,” yeye aeleza, “tulikumbuka wale ambao walikuwa wamesema wanaweza kusaidia na kuwapigia simu. Tulihisi kwamba twaweza kuwaomba msaada.”

      Wape Wakati wa Kupumzika

      “Ni muhimu kabisa,” chasema kitabu The 36-Hour Day, “kwako wewe [mtunzaji] na kwa [mgonjwa wako]—kwamba uwe na pindi za kawaida za ‘kuacha’ utunzaji wako wa muda wa saa 24 wa mtu aliye mgonjwa wa kusedeka. . . . Kuchukua wakati wa kupumzika, wa kutomtunza [mgonjwa], ni mojawapo ya mambo yaliyo muhimu zaidi uwezayo kufanya ili uweze kuendelea kumtunza mtu.” Je, watunzaji wakubaliana na hilo?

      “Bila shaka ndiyo,” ajibu Maria, ambaye alisaidia kumtunza rafiki wa karibu aliyekuwa akifa kwa kansa. “Pindi kwa pindi, nilihitaji ‘kupata nafasi ya kupumzika’ na mtu mwingine kumtunza kwa muda fulani.” Joan, anayemtunza mume wake ambaye ana maradhi ya Alzheimer, pia anakubaliana na wazo hilo. “Mojawapo ya mahitaji yetu makubwa kabisa,” yeye asema, “ni kupata vipindi vya kupumzika mara kwa mara.”

      Lakini, wao wawezaje kupata nafasi ya kupumzika kutoka kwa mkazo wa madaraka yao? Jennifer, aliyesaidia kutunza wazazi wake walio wazee-wazee, aonyesha jinsi alivyopata kitulizo: “Rafiki wa familia nyakati nyingine alimchukua mama kwa siku nzima ili kutupa nafasi ya kupumzika.”

      Huenda ukaweza kumpa mtunzaji nafasi ya kupumzika kwa kujitolea kumchukua mgonjwa kwa muda fulani, kama inawezekana kufanya hivyo. Joan asema: “Naburudika sana mtu amchukuapo mume wangu ili niwe peke yangu kwa muda.” Kwa upande mwingine, unaweza kutumia wakati na mgonjwa nyumbani kwake. Vyovyote vile, fanya iwezekane kwa mtunzaji kupata pumziko analohitaji sana.

      Lakini, kumbuka kwamba si rahisi sikuzote kwa watunzaji kupata nafasi ya kupumzika. Wao wanaweza kuhisi hatia ya kuwaacha wapendwa wao. “Si rahisi kuacha hali hiyo na kushiriki katika tafrija au kupumzika,” akubali Hjalmar. “Nilihisi kwamba nataka kuwa hapo wakati wote.” Lakini alipata utulivu mkubwa wa akili kwa kuchukua wakati wa kupumzika wakati ambapo ndugu-mkwe wake hakuhitaji msaada sana. Wengine wamepanga ili wapendwa wao watunzwe katika kituo cha utunzaji cha watu wazima cha wakati wa mchana kwa muda wa saa chache.

      Mwisho wa Ugonjwa Wote

      Kwa hakika, kumtunza mpendwa ambaye ni mgonjwa sana ni daraka kubwa sana. Hata hivyo, kumtunza mpendwa kwaweza kuwa na hisia yenye utimizo na kwenye kuridhisha sana. Watafiti na vilevile watunzaji waonyesha faida ni uhusiano imara wa familia na marafiki. Daima, watunzaji hujifunza sifa mpya na uwezo mpya. Wengi hupata manufaa za kiroho pia.

      Jambo muhimu zaidi, Biblia yaonyesha kwamba Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo, ndio watunzaji wenye huruma zaidi. Unabii wa Biblia watuhakikishia kwamba mwisho wa magonjwa, mateseko, na vifo vyote u karibu. Karibuni, Muumba wa mwanadamu mwenye kujali atawathawabisha wakazi wa dunia wenye uadilifu kwa kuwapa uhai wa milele katika ulimwengu mpya wenye afya kamili—ambamo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24; Ufunuo 21:4.

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

      [Blabu katika ukurasa wa 11]

      Hali-njema ya mgonjwa hutegemea kwa njia ya moja kwa moja hali-njema ya mtunzaji

      [Blabu katika ukurasa wa 12]

      Utegemezo wa marafiki wazuri utasaidia sana kukuendeleza kupitia nyakati zilizo ngumu zaidi

      [Sanduku katika ukurasa wa12]

      Kutoa Utunzaji Kwaweza Kuthawabisha

      ‘KUTHAWABISHA?’ wengine huenda wakajiuliza. ‘Kunaweza kuthawabishaje?’ Tafadhali ona yale ambayo watunzaji wafuatao waliliambia Amkeni!:

      “Kuacha mifuatio yako mwenyewe na tamaa zako hakumaanishi kwamba hutakuwa na furaha sana. ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.’ (Matendo 20:35) Inaweza kuridhisha sana kumtunza mtu umpendaye.”—Joan.

      “Nilishukuru kwamba niliweza kumsaidia dada yangu na ndugu-mkwe wakati walipohitaji msaada kwelikweli—bila wao kuweza kulipia. Ilitufanya tukaribiane zaidi. Natumaini kwamba siku moja naweza kutumia ustadi niliopata kusaidia mtu mwingine aliye katika hali kama hiyo.”—Hjalmar.

      “Kama ambavyo nimemwambia rafiki yangu mgonjwa, Betty, zaidi ya mara moja, nilipata mengi zaidi kuliko yale niliyotoa. Nilijifunza kuwa na hisia mwenzi na subira. Nilijifunza pia kwamba inawezekana kudumisha mtazamo ufaao chini ya hali zilizo ngumu zaidi.”—Elsa.

      “Nilikuwa mtu mwenye nguvu zaidi kiroho. Nilipata kujua vizuri zaidi jinsi ilivyo kumtegemea Yehova Mungu kila siku na kuona akiridhisha mahitaji yangu.”—Jeanny.

      [Sanduku katika ukurasa wa 13]

      Unapozuru Mtunzaji:

      • Sikiliza kwa hisia-mwenzi

      • Toa pongezi yenye kutoka moyoni

      • Toa msaada hususa

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      Tegemeza watunzaji kwa kununua vitu kwa niaba yao na kuwapikia au kwa kuwasaidia kumtunza mgonjwa

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki