Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Familia Inapokumbwa na Ugonjwa wa Kudumu
    Amkeni!—2000 | Mei 22
    • Familia Inapokumbwa na Ugonjwa wa Kudumu

      FURAHA ya familia ya Du Toit ni yenye kuvutia. Upendo mchangamfu wanaoonyeshana hupendeza sana. Ukikutana nao huwezi kujua wamevumilia magumu mengi mno.

      Kwanza, kifungua-mimba wao, Michelle, alipokuwa na umri wa miaka miwili, Braam na Ann waligundua kwamba alikuwa na maradhi ya kudumu aliyorithi ambayo hudhoofisha misuli.

      “Kwa ghafula,” aeleza mama huyo, aitwaye Ann, “utahitaji kujifunza namna ya kukabiliana na ugonjwa wa kudumu wenye kulemaza. Unagundua kwamba maisha ya familia hayatakuwa sawa tena.”

      Lakini baada ya mwana na binti mwingine kuzaliwa, familia hiyo ilikumbwa na msiba mwingine. Siku moja watoto hao watatu walipokuwa wakicheza nje, wasichana wangu wawili walikuja nyumbani wakikimbia. “Mama! Mama!” wakalia. “Njoo upesi. Neil ana tatizo fulani!”

      Alipokimbia nje, Ann aliona kichwa cha Neil mwenye umri wa miaka mitatu kikinyong’onyea upande mmoja. Hangeweza kusimamisha kichwa chake wima.

      “Nilishtuka sana,” akumbuka Ann, “na nilitambua tatizo papo hapo. Nilishuka moyo sana kuona kwamba mvulana huyu mdogo mwenye afya angekabili ugumu wa kuishi na maradhi yanayodhoofisha misuli kama dada yake mkubwa.”

      “Punde si punde ile shangwe ya kuanzisha familia yenye afya,” asema baba yao, Braam, “ilimalizwa na magumu makubwa sana ambayo tumepata kukabili.”

      Hatimaye Michelle alikufa kwa matatizo yaliyosababishwa na ugonjwa wake, licha ya matibabu bora kabisa aliyopokea hospitalini. Alikuwa na umri wa miaka 14 tu wakati huo. Neil anaendelea kupambana na athari za ugonjwa wake.

      Hilo lazusha swali hili, Familia kama ile ya Du Toit huweza kukabilianaje na magumu ya kuwa na mshiriki mmoja wa familia aliye na ugonjwa wa kudumu? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchanganue baadhi ya njia ambazo familia huathiriwa na ugonjwa wa kudumu.

  • Ugonjwa wa Kudumu—Hangaiko la Familia
    Amkeni!—2000 | Mei 22
    • Ugonjwa wa Kudumu—Hangaiko la Familia

      UGONJWA wa kudumu ni nini? Kwa njia sahili, ni ugonjwa unaodumu kwa muda mrefu. Profesa mmoja aongezea kufafanua ugonjwa wa kudumu kuwa “kuzorota kwa afya kusikoweza kutibiwa na upasuaji sahili au na matibabu ya muda mfupi.” Kinachoufanya ugonjwa wa kudumu au athari zake ziwe mbaya sana si ugonjwa wenyewe na matibabu yake tu bali ni kulazimika kuuvumilia kwa muda mrefu sana.

      Isitoshe, athari za ugonjwa wa kudumu hazimhusu mgonjwa peke yake. “Watu wengi ni sehemu ya familia,” chasema kitabu Motor Neurone Disease—A Family Affair, “na mshtuko na hangaiko linalokupata [wewe uliye mgonjwa] litawapata washiriki wako wa karibu.” Hilo lathibitishwa na mama mmoja ambaye binti yake aliugua kansa. “Kila mshiriki wa familia ameathiriwa,” asema, “iwe anaonyesha au anatambua jambo hilo au la.”

      Bila shaka, kila mmoja ataathiriwa kwa njia tofauti. Hata hivyo, washiriki wa familia wanapoelewa jinsi ugonjwa wa kudumu unavyoathiri watu kwa ujumla, huenda wakawa tayari zaidi kukabiliana na magumu ya kipekee katika hali yao hususa. Kwa kuongezea, watu wasiokuwa washiriki wa familia—wafanyakazi wenzi, wanashule wenzi, majirani, marafiki—wanapoelewa athari za ugonjwa wa kudumu, wataweza kuandaa utegemezo unaofaa wa kihisia-mwenzi. Tukiwa na habari hizo akilini, acheni tuone baadhi ya njia ambazo familia zaweza kuathiriwa na ugonjwa wa kudumu.

      Kusafiri Katika Nchi ya Kigeni

      Hali inayoipata familia yenye ugonjwa wa kudumu yaweza kufananishwa na familia kusafiri katika nchi ya kigeni. Ingawa mambo fulani yatakuwa sawa na ya nchi ya nyumbani, mambo mengine yatakuwa mageni au hata tofauti kabisa. Mshiriki wa familia anapokumbwa na ugonjwa wa kudumu mambo mengi hayatabadilika katika maisha ya familia. Hata hivyo, mambo mengine yatabadilika kabisa.

      Mwanzoni, huenda ugonjwa wenyewe ukaathiri utaratibu wa kufanya mambo katika familia na kulazimisha kila mshiriki wa familia afanye marekebisho ili kukabiliana na hali hiyo. Hilo lathibitishwa na Helen mwenye umri wa miaka 14, ambaye mama yake anaugua mshuko-moyo wa kudumu. “Sisi hurekebisha ratiba yetu kulingana na mambo ambayo Mama anaweza kufanya au asiyoweza kufanya katika siku yoyote hususa,” asema.

      Hata tiba—inayokusudiwa kutuliza ugonjwa—yaweza kuvuruga zaidi ratiba mpya ya familia. Fikiria mfano wa Braam na Ann, waliotajwa katika makala iliyotangulia. “Tulihitaji kufanya marekebisho makubwa katika kawaida yetu ya kufanya mambo kila siku kwa sababu ya tiba ya watoto wetu,” asema Braam. Ann aeleza: “Tulikuwa tukienda hospitalini mara kadhaa kila siku. Kisha, zaidi ya hilo, daktari alipendekeza tuwape watoto chakula kidogo mara sita kwa siku ili kujazia upungufu wa lishe uliosababishwa na maradhi yao. Nililazimika kubuni njia mpya kabisa ya kupika.” Ilikuwa vigumu sana kufuata agizo la kusaidia watoto wafanye mazoezi ya kuimarisha misuli. “Hilo,” akumbuka Ann, “lilikuwa kinyume cha mapenzi yangu.”

      Mgonjwa anapojipatanisha na hali isiyofaa—nyakati nyingine maumivu—inayoletwa na matibabu na uchunguzi wa wafanyakazi wa kitiba, hutegemea sana familia imsaidie na kumtegemeza kihisia-moyo. Tokeo ni kwamba washiriki wa familia hawalazimiki tu kujifunza stadi mpya za kumtunza mgonjwa bali hushurutika pia kurekebisha mtazamo wao, hisia-moyo, mtindo wao wa maisha, na kawaida yao ya kufanya mambo.

      Inaeleweka kwamba madai hayo yote hujaribu zaidi uvumilivu wa familia. Mama mmoja ambaye binti yake alilazwa hospitalini ili atibiwe kansa athibitisha kwamba inaweza “kuchosha zaidi ya vile mtu anavyoweza kuwazia.”

      Kuendelea kwa Wasiwasi

      “Kuendelea kwa heri na shari ya ugonjwa wa kudumu hutokeza hali yenye kutisha ya ukosefu wa uhakika,” chasema kichapo Coping With Chronic Illness—Overcoming Powerlessness. Wakati tu washiriki wa familia wanapozoea hali moja, huenda wakakumbwa na hali nyingine tofauti na labda ngumu zaidi. Huenda dalili zisiwe za kawaida au hata zikawa mbaya zaidi, na tiba yaweza kushindwa kutuliza hali iliyotarajiwa. Huenda ikawa lazima kubadili matibabu pindi kwa pindi au huenda yakatokeza matatizo yasiyotazamiwa. Mgonjwa azidipo kutegemea msaada kutoka kwa familia iliyotatanika na inayojikaza mno kuutoa, huenda hisia-moyo zilizodhibitiwa hapo awali zikalemea kwa ghafula.

      Hali isiyotabirika ya magonjwa mengi na tiba nyingi huzusha maswali yasiyoepukika kama vile: Hali hii itaendelea hadi lini? Ugonjwa huu utakuwa mbaya kadiri gani? Tutaweza kuvumilia hali hii kwa kadiri gani? Mara nyingi ugonjwa usiotibika huzusha hali ya wasiwasi mwishowe—“Itachukua muda mrefu kadiri gani kabla ya kifo?”

      Ugonjwa, utaratibu wa matibabu, kuchoka kabisa, na ukosefu wa uhakika yatukiapo wakati uleule huleta matokeo yasiyotazamiwa.

      Namna Ushirikiano na Wengine Huathiriwa

      “Nilihitaji kushinda hisia za kutaka kujitenga na watu na kukaa kivyangu,” asema Kathleen, ambaye mume wake aliugua mshuko-moyo wa kudumu. “Hali ilizidi kuwa mbaya,” aendelea, “kwa sababu hatukuweza kamwe kualika wala kualikwa na watu kwa ushirika. Hatimaye, tukaacha kabisa kushirikiana na watu.” Kama Kathleen, tokeo ni kwamba wengi hulazimika kukabiliana na hatia kwa sababu ya kutokuwa wakaribishaji-wageni na kukataa mialiko. Kwa nini jambo hilo hutukia?

      Ugonjwa wenyewe au matokeo yake waweza kufanya iwe vigumu au isiwezekane kushiriki katika vikusanyiko vya kirafiki. Huenda familia na mgonjwa wakauona ugonjwa huo kuwa fedheha kwa jamii, au kuhofu kwamba utaleta aibu. Huenda mshuko-moyo ukamfanya mgonjwa ahisi kuwa hafai kuonyeshwa urafiki kama awali, au huenda familia ikashindwa kabisa kuchangamana na watu. Kwa sababu mbalimbali, ugonjwa wa kudumu waweza kwa urahisi kutokeza hali ya kujitenga na watu na upweke kwa familia nzima.

      Zaidi ya hayo, si kila mtu anayejua jambo la kusema au namna ya kujiendesha anapokuwa karibu na mtu aliyelemaa. (Ona sanduku “Jinsi Unavyoweza Kuandaa Utegemezo,” kwenye ukurasa wa 11.) “Mtoto wako anapokuwa tofauti na watoto wengine, watu wengi humkodolea macho na kusema mambo yasiyofaa,” asema Ann. “Kwa kweli, utaelekea kujilaumu kwa sababu ya ugonjwa huo, na maelezo yao yatafanya uhisi hatia zaidi.” Kile anachosema Ann chahusu jambo jingine litakalopata familia.

      Hisia-Moyo Zinazovuruga

      “Ugonjwa unapobainishwa, familia nyingi hushtuka, hukosa kuamini, na kukana hali hiyo,” asema mtafiti mmoja. “Ni vigumu sana kuvumilia hali hiyo.” Naam, ni jambo linaloweza kukuvuruga unapofahamu kwamba mtu umpendaye ana ugonjwa hatari kwa uhai au unaodhoofisha. Huenda familia ikaona kwamba matumaini yake yamevunjwa-vunjwa, bila kuwa na wakati ujao ulio hakika na kuhisi hasara na huzuni kubwa.

      Ni kweli kwamba familia nyingi ambazo zimekabili hali zenye kufadhaisha kwa muda mrefu kuhusu mshiriki mmoja wa familia bila kujua kisababishi, huenda zikatulia ugonjwa unapobainishwa. Lakini huenda familia fulani zikatenda kwa njia tofauti ugonjwa unapobainishwa. Mama mmoja kutoka Afrika Kusini akiri hivi: “Niliumia sana nilipoelezwa kasoro ya watoto wetu, hivi kwamba ingekuwa afadhali kama nisingesikia kubainishwa kwa ugonjwa huo.”

      Kitabu A Special Child in the Family—Living With Your Sick or Disabled Child chasema kwamba “ni jambo la asili kupatwa na mvurugo wa kihisia-moyo . . . unapofanya marekebisho ili kupatana na hali hiyo mpya. Nyakati fulani huenda ukawa na hisia nyingi sana mpaka ukahofu kwamba huwezi kukabiliana nazo.” Mwandishi wa kitabu hicho, Diana Kimpton, ambaye wanawe wawili walikuwa na ugonjwa wa cystic fibrosis, asema: “Niliogopeshwa na hisia zangu mwenyewe na nilihitaji kujua kama ilikuwa sawa kuhisi vibaya namna hiyo.”

      Ni jambo la kawaida kwa familia kuhofu—hofu ya mambo yatakayotukia, hofu ya ugonjwa, hofu ya matibabu, hofu ya maumivu, na hofu ya kifo. Watoto hasa waweza kuwa na hofu bila kusema—ikiwa hawaelezwi kinaganaga hasa kile kinachotukia.

      Hasira huwa jambo la kawaida pia. “Washiriki wa familia,” lasema gazeti la Afrika Kusini TLC, “huenda mara nyingi wakaonyeshwa uhasama kwa sababu ya hasira ya mgonjwa.” Nao washiriki wa familia waweza kukasirishwa—na madaktari kwa kutogundua tatizo hilo mapema zaidi, wakajikasirikia wenyewe kwa kupitisha kasoro ya kurithiwa, wakamkasirikia mgonjwa kwa kutojitunza ifaavyo, wakamkasirikia Shetani Ibilisi kwa kusababisha mateso, au hata wakamkasirikia Mungu, wakihisi kwamba apaswa kulaumiwa kwa ugonjwa huo. Itikio jingine la kawaida kwa ugonjwa wa kudumu ni kuhisi una hatia. “Karibu kila mzazi au ndugu ya mtoto aliye na kansa huhisi ana hatia,” chasema kitabu Children With Cancer—A Comprehensive Reference Guide for Parents.

      Mara nyingi mvurugo huo wa hisia huongoza—kwa kiwango kikubwa au kidogo—kwenye mshuko-moyo. “Labda hili ndilo itikio la kawaida zaidi ya yote,” aandika mtafiti mmoja. “Nina faili iliyojaa barua za kuthibitisha jambo hilo.”

      Naam, Familia Zaweza Kukabiliana na Hali

      Kwa kufaa, familia nyingi zimepata kwamba kukabiliana na hali si jambo gumu sana kama lilivyoonekana mwanzoni. “Mambo unayowazia huwa mabaya zaidi kuliko hali halisi,” atoa uhakikisho Diana Kimpton. Akitegemea mambo aliyojionea, yeye aliona kwamba “wakati ujao hauwi mbaya sana kama unavyowazia unapoelezwa ugonjwa wako.” Uwe na hakika kwamba familia nyingine zimefaulu katika safari ya nchi ya kigeni ya ugonjwa wa kudumu nawe pia waweza. Wengi wameona kuwa kufahamu tu kwamba wengine waliwahi kukabiliana na hali hiyo kumewapa kitulizo na tumaini kwa kiasi fulani.

      Ingawa hivyo, huenda familia ikajiuliza, ‘Tunaweza kukabilianaje na hali?’ Makala ifuatayo itachunguza baadhi ya njia ambazo familia zimekabiliana na ugonjwa wa kudumu.

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      Familia zahitaji kutunza mgonjwa wao na kurekebisha mitazamo yao, hisia-moyo zao, na mitindo yao ya maisha

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Mgonjwa na familia watapatwa na hisia-moyo kali

      [Blabu katika ukurasa wa 7]

      Msikate tamaa. Familia nyingine zimekabiliana na hali hiyo, nyinyi pia mwaweza

      [Sanduku katika ukurasa wa 7]

      Baadhi ya Magumu ya Ugonjwa wa Kudumu

      • Kujifunza juu ya ugonjwa na jinsi ya kukabiliana nao

      • Kurekebisha mtindo wa maisha na kawaida ya kufanya mambo ya kila siku

      • Kukabiliana na mahusiano ya jamii yaliyobadilika

      • Kudumisha hali ya kawaida na kuidhibiti

      • Kuhuzunikia hasara inayotokana na ugonjwa

      • Kukabiliana na hisia-moyo zisizofaa

      • Kudumisha mtazamo unaofaa

  • Jinsi Ambavyo Familia Hukabiliana na Ugonjwa wa Kudumu
    Amkeni!—2000 | Mei 22
    • Jinsi Ambavyo Familia Hukabiliana na Ugonjwa wa Kudumu

      KUKABILIANA kwaweza kufasiliwa kuwa “uwezo wa kushughulika kwa matokeo na mikazo uliyo nayo.” (Taber’s Cyclopedic Medical Dictionary) Kwahusisha kukabili matatizo ya ugonjwa wa kudumu katika njia ambayo unaweza kuyadhibiti kwa kiasi fulani na kufurahia amani ya akili. Kwa sababu ugonjwa wa kudumu ni suala la familia, utegemezo mwaminifu na wenye upendo kutoka kwa kila mshiriki wa familia wahitajiwa ili familia ikabiliane kwa mafanikio na hali hiyo. Acheni tuchunguze baadhi ya njia ambazo familia hukabiliana na ugonjwa wa kudumu.

      Thamani ya Ujuzi

      Huenda isiwezekane kuponya ulemavu huo, lakini kujua namna ya kukabiliana kwaweza kupunguza athari za kiakili na za kihisia-moyo ziletwazo na ugonjwa huo. Hilo lapatana na mithali ya kale inayosema: “Mtu mwenye hekima ana nguvu.” (Mithali 24:5) Familia yaweza kupataje ujuzi kuhusu namna ya kukabiliana na hali hiyo?

      Hatua ya kwanza ni kutafuta daktari aliye tayari kuwasiliana na kusaidia, ambaye yuko tayari kutumia wakati kumweleza mgonjwa na familia kila jambo kwa makini. “Daktari bora,” chasema kitabu A Special Child in the Family, “hujali familia yote nzima na vilevile huwa na stadi zote za kitiba zinazohitajika.”

      Hatua ya pili ni kuendelea kuuliza maswali hususa mpaka uelewe kabisa hali kadiri uwezavyo. Hata hivyo, kumbuka kwamba unapokuwa na daktari, ni rahisi kupatwa na wasiwasi na kutatanika na hivyo kusahau kile ulichotaka kuuliza. Dokezo moja linalosaidia ni kuandika maswali kimbele. Huenda ukataka kujua kihususa ni nini unachoweza kutazamia kutokana na ugonjwa huo na matibabu yake na kile unachoweza kufanya. —Ona sanduku “Maswali Ambayo Familia Yaweza Kuuliza Daktari.”

      Ni muhimu hasa kuandalia ndugu na dada za mtoto mwenye ugonjwa wa kudumu habari ya kutosha. “Eleza tatizo kuanzia siku za kwanza-kwanza,” apendekeza mama mmoja. “Wanaweza kuona kana kwamba wametengwa na familia ikiwa hawaelewi kile kinachotukia.”

      Familia fulani pia zimepata habari inayosaidia kwa kufanya utafiti kwenye maktaba, duka la vitabu, au katika Internet—mara nyingi zimepata habari chungu nzima ihusuyo magonjwa hususa.

      Kudumisha Maisha Bora kwa Kadiri Fulani

      Ni jambo la asili kwa washiriki wa familia kutaka kudumisha maisha bora kwa kadiri fulani kwa ajili ya mgonjwa. Fikiria mfano wa Neil du Toit, aliyetajwa katika makala ya kwanza. Angali anafadhaishwa na udhaifu unaosababishwa na maradhi yake. Hata hivyo, yeye hutumia karibu saa 70 kwa mwezi katika utendaji unaomletea shangwe zaidi—kuzungumza na watu katika jumuiya yake kuhusu tumaini lake linalotegemea Biblia. “Mimi huridhika pia moyoni,” asema, “kufundisha kutaniko maagizo ya Biblia.”

      Maisha bora pia hutia ndani kuonyesha na kuonyeshwa upendo, kufurahia utendaji unaopendeza, na kuwa na tumaini. Wagonjwa wangetaka kuendelea kufurahia maisha kadiri ugonjwa wao na matibabu yao yatakavyoruhusu. Baba mmoja ambaye familia yake imekabiliana na ugonjwa kwa zaidi ya miaka 25 asema: “Tunapenda kutalii, lakini kwa sababu ya udhaifu wa mwanangu, hatuwezi kusafiri kwa miguu. Kwa hiyo tunafanya hivyo kwa njia tofauti. Tunaenda katika sehemu ambazo hazihitaji utendaji wa kutumia nguvu.”

      Naam, bado wagonjwa huwa na uwezo mbalimbali unaowapa uradhi wa kadiri fulani maishani. Ikitegemea asili ya ugonjwa wenyewe, bado wengi wanaweza kuthamini mandhari na sauti nzuri. Kadiri wawezavyo kushughulikia utendaji mbalimbali maishani, ndivyo wapatavyo maisha bora kwa kadiri fulani.

      Kushughulika na Hisia-Moyo Zisizofaa

      Sehemu muhimu ya kukabiliana na hali yatia ndani kujifunza namna ya kudhibiti hisia-moyo zenye kudhuru. Mojawapo ni hasira. Biblia hukiri kwamba mtu aweza kukasirika kwa sababu fulani. Hata hivyo, pia hutusihi tusiwe ‘wepesi wa hasira.’ (Mithali 14:29) Kwa nini ni jambo la hekima kufanya hivyo? Kulingana na kitabu kimoja cha marejezo, hasira “yaweza kukudhuru na kukufanya uwe na uchungu au kukufanya useme mambo yenye kuumiza utakayojutia baadaye.” Hata mfoko mmoja wa hasira waweza kusababisha madhara yanayoweza kuchukua muda mrefu sana kurekebishwa.

      Biblia hupendekeza: “Msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Bila shaka, hatuwezi kufanya lolote ili kuchelewesha kutua kwa jua. Lakini tunaweza kuchukua hatua ili kushughulikia “hali [yetu] ya kuchokozeka” haraka ili tusiendelee kujidhuru wenyewe na kuwadhuru wengine. Unaweza kushughulikia hali kwa njia bora zaidi wakati ambapo umetulia.

      Kama ilivyo na familia yoyote, yako pia itakuwa na heri na shari. Wengi huona kwamba wanaweza kukabiliana vyema na hali wanapokuwa na mtu wa kumwambia siri au kuzungumza na mtu mwingine mwenye huruma na hisia-mwenzi. Bila shaka Kathleen alipatwa na jambo kama hilo. Kwanza alimtunza mamake, aliyekuwa na kansa, na baadaye mumewe, aliyeugua mshuko-moyo wa kudumu na hatimaye maradhi ya Alzheimer. Akiri hivi: “Nilipata kitulizo na faraja nilipozungumza na marafiki wanaoelewa hali.” Rosemary, aliyemtunza mamake kwa miaka miwili, akubali. “Kuzungumza na rafiki mwenye moyo mweupe,” asema, “kulinisaidia nidumishe usawaziko.”

      Hata hivyo, usishangae, ukidondokwa na machozi unapozungumza. “Kulia hupunguza mkazo na maumivu, na hukusaidia uondoe huzuni,” chasema kitabu A Special Child in the Family.a

      Dumisha Mtazamo Unaofaa

      “Nia yako ya kuishi inaweza kukutegemeza unapokuwa mgonjwa,” akaandika Mfalme Solomoni mwenye hekima. (Mithali 18:14, Today’s English Version) Watafiti wa kisasa wamesema kwamba matarajio ya wagonjwa—yawe yanafaa au hayafai—mara nyingi huathiri matokeo ya matibabu yao. Ingawa hivyo, familia yaweza kudumishaje mataraja mema inapokabili ugonjwa wa muda mrefu?

      Bila kupuuza ugonjwa, familia zaweza kukabiliana vyema zinapoelekeza fikira kwenye mambo ambayo bado zinaweza kufanya. “Hali hiyo yaweza kukufanya uwe na mtazamo usiofaa kabisa,” akiri baba mmoja, “lakini wapaswa kutambua kwamba ungali na mengi sana. Ungali hai, una washiriki wa familia, na marafiki.”

      Ingawa ugonjwa wa kudumu haupasi kuchukuliwa kivivi hivi, kuwa mcheshi huzuia mtazamo usiofaa. Jambo hilo laonyeshwa na wepesi wa ucheshi wa familia ya Du Toit. Collette, dadake Neil du Toit aliye mchanga zaidi, asema: “Kwa sababu tumejifunza kukabiliana na hali fulani, twaweza kuchekelea mambo yanayotupata ambayo huenda yakawaudhi sana wengine. Lakini kufanya hivyo kwa kweli husaidia kupunguza mkazo.” Biblia hutuhakikishia kwamba “moyo uliochangamka ni dawa nzuri.”—Mithali 17:22.

      Kanuni za Kiroho za Maana Zaidi

      Sehemu muhimu ya hali njema ya kiroho kwa Wakristo wa kweli yahusisha ‘kuacha maombi yao ya bidii yajulishwe kwa Mungu kwa sala na dua.’ Tokeo litakuwa kama ilivyoahidiwa katika Biblia: “Amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” (Wafilipi 4:6, 7) Baada ya miaka karibu 30 ya kuwatunza watoto wawili walio na ugonjwa wa kudumu, mama mmoja asema: “Tumejifunza kwamba Yehova hukusaidia kukabiliana na hali. Kwa kweli hukutegemeza.”

      Zaidi ya hayo, wengi huimarishwa na ahadi za Biblia za dunia paradiso isiyo na maumivu na kuteseka. (Ufunuo 21:3, 4) “Kwa sababu ya ugonjwa wa kudumu ambao familia yetu imekabili,” asema Braam, “twapata maana zaidi ya ahadi ya Mungu ya kwamba ‘mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.’ Kama ilivyo na wengine wengi, familia ya Du Toit yatazamia kwa hamu wakati ambapo katika Paradiso “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24; 35:6.

      Jipe moyo. Maumivu na mateso yanayopata wanadamu ni uthibitisho wa kwamba hali bora zimekaribia. (Luka 21:7, 10, 11) Hata hivyo, kwa wakati uliopo, watunzaji wengi na wagonjwa wanaweza kuthibitisha kwamba kwa kweli Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na athari za kihisia-moyo ziletwazo na ugonjwa, tafadhali ona “Utunzaji—Kukabili Huo Ugumu,” katika Amkeni!, Februari 8, 1997, ukurasa wa 3-13.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

      Maswali Ambayo Familia Yaweza Kuuliza Daktari

      • Ugonjwa utaendelea namna gani, kukiwa na tokeo gani?

      • Kutakuwa na dalili gani, nazo zitadhibitiwa jinsi gani?

      • Kuna matibabu gani mengine?

      • Kuna athari, hatari, na manufaa gani za matibabu tofauti-tofauti?

      • Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuboresha hali, na ni nini kinachopasa kuepukwa?

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

      Jinsi Unavyoweza Kuandaa Utegemezo

      Huenda watu fulani wakaepuka kuwatembelea au kuwapa msaada kwa sababu ya kutojua la kusema au namna ya kushughulikia hali hiyo. Huenda wengine wakajidukiza, na kuongeza mkazo kwa familia kwa kuishurutisha ifuate madokezo wanayofikiri yatasaidia. Basi, mtu aweza kuandaaje utegemezo kwa watu walio na mshiriki wa familia mwenye ugonjwa wa kudumu bila kuingilia hali yao ya faragha?

      Onyesha hisia-mwenzi unaposikiliza. ‘Uwe mwepesi sana juu ya kusikia,’ yasema Biblia katika Yakobo 1:19. Onyesha upendezi kwa kuwa msikilizaji mzuri na kuruhusu washiriki wa familia wasema yaliyo moyoni ikiwa wanataka. Huenda wakaelekea kufanya hivyo wanapotambua kwamba una “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Ingawa hivyo, kumbuka kwamba hakuna watu wawili au familia mbili zinazotenda kwa njia ileile zikabilipo ugonjwa wa kudumu. Kwa hiyo, “usitoe shauri isipokuwa uwe unajua kikamili habari kuhusu maradhi hayo au hali hiyo,” asema Kathleen, aliyemtunza mama yake na baadaye mume wake aliyepatwa na ugonjwa wa kudumu. (Mithali 10:19) Na kumbuka, hata ikiwa una ujuzi fulani kuhusu ugonjwa huo, huenda mgonjwa na familia wakakataa kuomba shauri lako au kulikubali.

      Toa msaada unaotumika. Jitoe kikweli wanapokuhitaji, huku ukiwa mwangalifu sana kutoingilia faragha ya familia hiyo. (1 Wakorintho 10:24) Braam, ambaye amenukuliwa katika mfululizo huu wa makala, asema: “Marafiki wetu Wakristo walitupa msaada mkubwa kwelikweli. Kwa mfano, tulipolala hospitalini kwa sababu ya hali mbaya ya Michelle, sikuzote tulikuwa na marafiki kati ya wanne hadi sita walioketi pamoja nasi usiku kucha. Tulipohitaji msaada wakati wowote, tuliupata.” Mke wa Braam, Ann, aongezea hivi: “Yalikuwa majira ya baridi kali, na kwa majuma mawili tulipewa mchuzi wa aina tofauti kila siku. Tulilishwa mchuzi moto na kuonyeshwa upendo mwingi mchangamfu.”

      Sali pamoja nao. Nyakati nyingine huenda kusiwe na jambo unaloweza kufanya. Hata hivyo, kuna mambo machache yanayotia moyo kama vile kushiriki wazo la Kimaandiko linalojenga au sala ya kutoka moyoni pamoja na wagonjwa na familia zao. (Yakobo 5:16) “Usipuuze kamwe uwezo wa kusali kwa ajili ya—na pamoja na—watu walio na ugonjwa wa kudumu na familia zao,” asema Nicolas mwenye umri wa miaka 18, ambaye mama yake anaugua mshuko-moyo wa kudumu.

      Naam, utegemezo unaofaa waweza kusaidia sana familia zikabiliane na mkazo unaoletwa na ugonjwa wa kudumu. Biblia husema hivi: “Rafiki ni mwandamani anayependa nyakati zote, na ndugu huzaliwa kushiriki taabu.”—Mithali 17:17, The New English Bible.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

      Ugonjwa Usipotibika

      Huenda familia fulani zikasitasita kuzungumzia kifo kinachokaribia cha mpendwa aliye na ugonjwa usiotibika. Hata hivyo, kitabu Caring—How to Cope chasema kwamba “unapojua jambo unalotazamia na unalopaswa kufanya, huenda ikasaidia kupunguza wasiwasi.” Ingawa hatua mahususi zitatofautiana ikitegemea sheria na desturi za mahali, yafuatayo ni madokezo kadhaa ambayo huenda familia ikayafikiria inapomtunza mpendwa aliye na ugonjwa usiotibika nyumbani.

      Mapema vya Kutosha

      1. Mwulize daktari mambo unayopaswa kutazamia siku na saa za mwisho-mwisho na kile kipasacho kufanywa ikiwa kifo kitatukia usiku.

      2. Tayarisha orodha ya wale watu wanaohitaji kujulishwa juu ya kifo.

      3. Fikiria njia tofauti-tofauti za maziko:

      • Mgonjwa angependa kufanyiwa nini?

      • Kuzikwa au kuchomwa? Linganisha gharama na huduma za watu mbalimbali wanaotia maiti dawa isioze.

      • Maziko yapasa kufanywa lini? Ruhusu wakati kwa ajili ya mipango ya kusafiri.

      • Ni nani atakayeongoza maziko au hotuba ya maziko?

      • Yatafanywa wapi?

      4. Hata ikiwa mgonjwa ametulizwa kwa dawa huenda bado akawa anajua kile kinachosemwa na kufanywa karibu naye. Uwe mwangalifu usiseme jambo lolote mbele yake ambalo hungependa asikie. Huenda ukataka kumpa uhakikishio kwa kuzungumza naye kwa utulivu na kushika mkono wake.

      Mpendwa Anapokufa

      Haya ni baadhi ya mambo ambayo wengine wanaweza kufanya ili kusaidia familia:

      1. Ruhusu familia iwe na wakati wa kutosha ikiwa peke yake pamoja na aliyekufa ili iweze kukabiliana na kifo.

      2. Sali pamoja na familia.

      3. Familia inapokuwa tayari, huenda ikathamini msaada wa kujulisha watu wafuatao:

      • Daktari ili kuthibitisha kifo na kutoa hati ya kifo.

      • Mtu anayetia maiti dawa isioze, chumba cha kuhifadhi maiti, au mahali pa kuchomea maiti, ili kuchukua mwili.

      • Jamaa na marafiki. (Huenda ukasema jambo kama hili kwa busara: “Napiga simu kuhusu [jina la mgonjwa]. Nasikitika kusema kwamba nina habari mbaya. Kama ujuavyo, amepambana na [ugonjwa] kwa muda fulani, na alikufa [lini na wapi].)

      • Ofisi ya kampuni ya kuchapisha magazeti ili kuweka tangazo la kifo wakipenda.

      4. Huenda familia ikataka kuandamana na mtu fulani ili kuwasaidia kukamilisha mipango ya maziko.

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Washiriki wa familia wapaswa kufanya yote wawezayo ili kudumisha maisha bora kwa kadiri fulani

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      Kusali pamoja na familia hiyo kwaweza kuwasaidia wakabiliane na hali

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki