Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Ujifunze Biblia?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Aprili 1
    • Mwanamume akisoma Biblia katika maktaba

      HABARI KUU | JE, UNGEPENDA KUJIFUNZA BIBLIA?

      Kwa Nini Ujifunze Biblia?

      • Ni nini kusudi la maisha?

      • Kwa nini wanadamu wanateseka na kufa?

      • Ni nini kitakachotokea wakati ujao?

      • Je, Mungu ananijali?

      Je, umewahi kujiuliza maswali kama hayo? Ikiwa ndivyo, hauko peke yako. Ulimwenguni pote watu wanajiuliza maswali muhimu kuhusu maisha. Je, unaweza kupata majibu?

      Huenda mamilioni ya watu wakajibu, “Ndiyo!” Kwa nini? Kwa sababu wamepata majibu yenye kuridhisha ya maswali yao katika Biblia. Je, ungependa kujua kile ambacho Biblia inasema? Basi, utanufaika zaidi kwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova bila malipo.a

      Ni kweli kwamba inapohusu kujifunza Biblia, baadhi ya watu husema: “Nina shughuli nyingi.” “Biblia haieleweki.” “Ninaogopa kuahidi kwamba nitapatikana ili kujifunza.” Hata hivyo, wengine wana maoni tofauti. Wanakubali kujifunza kile ambacho Biblia inafundisha. Fikiria mifano michache:

      • “Nilishirikiana na makanisa ya Kikatoliki na Kiprotestanti, hekalu la Kalasinga, makao ya watawa Wabudha, na nilisomea theolojia katika chuo kikuu. Hata hivyo, maswali yangu mengi kuhusu Mungu hayakujibiwa. Kisha, Shahidi wa Yehova alinitembelea nyumbani. Nilikubali kujifunza Biblia baada ya dada huyo kujibu maswali yangu kwa kutumia Biblia.”—Gill, Uingereza.

      • “Nilikuwa na maswali mengi kuhusu maisha, lakini majibu ya mchungaji wangu hayakuniridhisha. Hata hivyo, Shahidi wa Yehova alijibu maswali yangu kwa kutumia Biblia tu. Aliponiuliza ikiwa ningependa kujifunza mengi zaidi, nilikubali mara moja.”—Koffi, Benin.

      • “Nilitaka sana kujua kinachopata watu wanapokufa. Niliamini kwamba wafu wanaweza kudhuru walio hai, lakini nilitaka kujua kile ambacho Biblia inasema. Hivyo, rafiki yangu ambaye ni Shahidi alianza kunifundisha Biblia.”—José, Brazili.

      • “Nilijaribu kuisoma Biblia lakini sikuielewa. Kisha, Mashahidi wa Yehova walinitembelea na kunifafanulia vizuri unabii unaopatikana katika Biblia. Baada ya hapo, nilitaka kujifunza mengi zaidi.”—Dennize, Mexico.

      • “Nilifikiria sana ikiwa kwa kweli Mungu ananijali. Hivyo, nikaamua kusali kwa Mungu anayetajwa katika Biblia. Siku iliyofuata, Mashahidi walinitembelea nyumbani kwangu, nami nikakubali funzo la Biblia.”—Anju, Nepal.

      Masimulizi hayo yanatukumbusha maneno haya ya Yesu: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Naam, kiasili wanadamu wana uhitaji wa kumjua Mungu. Ni Mungu tu anayeweza kutimiza uhitaji huo, na anafanya hivyo kupitia Neno lake, Biblia.

      Hata hivyo, funzo la Biblia linahusisha nini? Litakunufaishaje? Maswali hayo yatajibiwa katika makala inayofuata.

      a Biblia inasema kwamba jina la Mungu ni Yehova.

      UKWELI KUHUSU BIBLIA

      Biblia iliyofunguliwa
      • JINA: Limetokana na neno la Kigiriki bi·bliʹa, linalomaanisha “vitabu vidogo”

      • YALIYOMO: Ina vitabu 39 vilivyoandikwa katika lugha ya Kiebrania (baadhi ya habari ziliandikwa katika lugha ya Kiaramu) na vitabu 27 katika lugha ya Kigiriki

      • UANDIKAJI: Imeandikwa na watu 40 kwa zaidi ya miaka 1,600, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi 98 W.K.b

      • LUGHA: Imetafsiriwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha zaidi ya  2,500

      • USAMBAZAJI: Inakadiriwa kwamba Biblia bilioni tano zimesambazwa na hivyo kukifanya kiwe kitabu kinachosambazwa zaidi duniani

      b Ufupisho wa K.W.K. unamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida,” na W.K. unamaanisha “Wakati wa Kawaida.”

  • Mpango wa Kujifunza Biblia kwa Ajili ya Watu Wote
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Aprili 1
    • Funzo la Biblia

      HABARI KUU | JE, UNGEPENDA KUJIFUNZA BIBLIA?

      Mpango Wa Kujifunza Biblia Kwa Ajili Ya Watu Wote

      Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri hadharani. Hata hivyo, je, unajua kwamba sisi hujifunza na watu Biblia duniani pote?

      Mwanamume akijifunza Biblia kazini

      Katika mwaka wa 2014, zaidi ya Mashahidi 8,000,000 katika nchi 240, waliongoza mafunzo ya Biblia, 9,500,000 hivi kila mwezi.a Kwa kweli, idadi ya watu wanaojifunza Biblia pamoja nasi, inazidi idadi ya watu katika nchi 140 hivi!

      Ili kufanya kazi hii ya kuelimisha watu, kila mwaka Mashahidi wa Yehova huchapisha Biblia, vitabu, magazeti na machapisho mengine ya Biblia, bilioni moja na nusu hivi katika lugha 700! Jitihada hizo kubwa za kuchapisha zinasaidia watu wajifunze Biblia katika lugha wanayopendelea.

      “Sikufurahia masomo shuleni, lakini nimefurahia sana kujifunza Biblia. Mambo niliyojifunza yalinifariji sana!”—Katlego, Afrika Kusini.

      “Mambo niliyojifunza yalijibu maswali yangu yote na zaidi.”—Bertha, Mexico.

      “Nilifundishwa Biblia nyumbani kwangu kulingana na ratiba yangu. Na hilo ndilo nililotaka zaidi!” —Eziquiel, Brazili.

      “Tulijifunza kwa muda wa dakika 15 hadi 30 hivi au zaidi ikitegemea ratiba yangu.”—Viniana, Australia.

      “Sikuhitaji kulipa chochote ili kujifunza, hilo lilinishangaza sana!”—Aimé, Benin.

      “Mwalimu wangu wa Biblia alikuwa mwenye subira na fadhili. Tukawa marafiki sana.”—Karen, Ireland Kaskazini.

      “Watu wengi hujifunza Biblia bila kuwa Mashahidi baadaye.” —Denton, Uingereza.

      MAJIBU YA MASWALI YANAYOULIZWA MARA NYINGI KUHUSU MPANGO WETU WA KUJIFUNZA BIBLIA

      Utaratibu wa kujifunza umepangwa jinsi gani?

      Sisi huchukua habari mbalimbali zinazopatikana katika Biblia na kuchunguza mistari ya Biblia inayohusiana na habari hizo. Kwa mfano, Biblia inatoa majibu ya maswali kama vile: Mungu ni nani? Ana utu wa aina gani? Je, ana jina? Anaishi wapi? Je, tunaweza kumkaribia? Watu wengi hupata changamoto ya kujua ni wapi katika Biblia wanaweza kupata majibu.

      Ili kuwasaidia watu wapate majibu ya maswali ya Biblia, sisi hutumia kitabu chenye kurasa 224, kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa?b Kitabu hicho kimetayarishwa ili kuwasaidia watu kuelewa mafundisho ya msingi ya Biblia. Mafundisho hayo yanatia ndani masomo kuhusu Mungu, Yesu Kristo, kwa nini wanadamu wanateseka, ufufuo, sala, na mengine mengi.

      Funzo linaweza kufanywa wakati na mahali gani?

      Funzo linaweza kufanywa wakati na mahali panapokufaa.

      Vipindi vya kujifunza huchukua muda gani?

      Watu wengi hutenga saa moja au zaidi kila juma ili kujifunza Biblia. Hata hivyo, urefu wa kujifunza wa kila kipindi unaweza kubadilika. Tutajifunza kulingana na ratiba yako. Wengine wamejifunza kwa dakika 10 au 15 tu kila juma.

      Funzo hilo linagharimu pesa ngapi?

      Funzo na machapisho ya kujifunzia hutolewa bila malipo. Hilo linapatana na agizo hili la Yesu alilowapa wanafunzi wake: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8.

      Funzo linachukua kipindi gani mpaka kumaliza?

      Unaweza kujifunza kwa kipindi cha wakati unachopenda. Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kina masomo 19. Unaweza kumaliza masomo hayo yote kulingana na nafasi yako.

      Je, ni lazima niwe Shahidi wa Yehova baada ya kumaliza kujifunza?

      Hapana. Tunatambua na tunaheshimu uhuru alionao kila mtu wa kuamua atakachoamini. Hata hivyo, watu waliopata ujuzi wa msingi wa Biblia wanaweza kufanya uamuzi kulingana na ujuzi huo.

      Nitapata wapi habari zaidi?

      Tovuti ya jw.org/sw inatoa habari sahihi kuhusu imani na utendaji wa Mashahidi wa Yehova.

      Ninawezaje kuomba funzo la Biblia?

      • Watu wanatuma maombi ya funzo la Biblia kupitia: Intaneti, barua, na kwa kutafuta namba ya simu katika kitabu cha orodha ya namba za simu

        Tuma ombi kupitia www.jw.org/sw.

      • Tuma ombi lako ukitumia mojawapo ya anwani zinazopatikana katika ukurasa wa pili wa gazeti hili.

      • Wasiliana na Mashahidi wa Yehova walio karibu nawe. Unaweza pia kutafuta Mashahidi wa Yehova katika kitabu cha orodha ya simu.

      a Kwa kawaida, mafunzo ya Biblia huongozwa pamoja na watu mmoja-mmoja au vikundi vya watu.

      b Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Nakala zaidi ya milioni 230 za kitabu hicho zimechapishwa katika lugha zaidi ya 260.

      MSAADA KWA FAMILIA

      Eziquiel

      “Mke wangu alipoanza kujifunza Biblia, niliona akifanya mabadiliko makubwa. Maisha ya familia yetu yaliboreka. Ili kujua ni nini alichokuwa akijifunza, nilianza pia kujifunza Biblia. Yale niliyojifunza yalinifanya nisitawishe sifa nzuri. Kujifunza Biblia kumefanya familia yetu iwe na umoja.”—Eziquiel.

      Karen

      “Nilipoanza kujifunza Biblia, niliacha zoea la kutumia madawa ya kulevya, ulevi, na nilijifunza kudhibiti hasira yangu. Sasa nyumba yangu ni safi na nadhifu. Naithamini familia yangu na ninafurahia kufanya mambo yanayochangia furaha yao. Nina furaha sana.”—Karen.

      Viniana

      “Baadhi ya watu walinidhihaki kwa sababu ya kujifunza Biblia. Lakini mume wangu aliunga mkono uamuzi wangu na kuniambia hivi: ‘Usijali maneno ya watu. Jambo muhimu kwangu ni kwamba unafanya mabadiliko mazuri sana. Endelea kujifunza Biblia.’ Maisha ya familia yetu hayajawahi kuwa mazuri kama yalivyo sasa!”—Viniana.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki