-
Ishi Kupatana na Sala ya Mfano—Sehemu ya KwanzaMnara wa Mlinzi—2015 | Juni 15
-
-
Ishi Kupatana na Sala ya Mfano Sehemu ya Kwanza
“Jina lako na litakaswe.”—MT. 6:9.
1. Tunaweza kuitumiaje sala iliyoandikwa kwenye Mathayo 6:9-13 katika huduma?
WATU wengi wameikariri Sala ya Bwana. Tunapokuwa katika huduma ya shambani, mara nyingi tunaitumia sala hiyo kumsaidia mwenye nyumba aelewe kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi itakayoleta mabadiliko mazuri duniani. Au tunaweza kutumia ombi la kwanza katika sala hiyo kuthibitisha kwamba Mungu ana jina, ambalo linapaswa kutakaswa.—Mt. 6:9.
2. Je, Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kurudia-rudia maneno ya sala ya mfano kila tunaposali? Eleza.
2 Je, Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kurudia-rudia maneno ya sala hiyo kila tunaposali, kama makanisa fulani ya Kikristo yanavyofanya? Hapana. Kabla tu ya kufundisha sala hiyo ya mfano, Yesu alisema hivi: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mt. 6:7) Baadaye, Yesu aliirudia sala hiyo kwa kutumia maneno tofauti. (Luka 11:1-4) Hivyo, Yesu alitusaidia kujua mambo tunayopaswa kuomba, na ni yapi yanapaswa kuchukua nafasi ya kwanza katika sala zetu. Ndiyo sababu inaitwa sala ya mfano.
3. Tunaweza kujiuliza maswali gani tunapozungumzia sala ya mfano?
3 Katika makala hii na inayofuata, tutazungumzia sala hiyo ya mfano. Tunapofanya hivyo, jiulize hivi, ‘Sala hii inaweza kunisaidiaje kuboresha sala zangu? Na je, ninaishi kupatana na sala hii?’
“BABA YETU ULIYE MBINGUNI”
4. Maneno “Baba yetu” yanatukumbusha nini? Ni katika maana gani Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani wanamwona Yehova kuwa “Baba”?
4 Maneno “Baba yetu,” na si “Baba yangu,” yanatukumbusha kwamba sisi ni sehemu ya “ushirika mzima wa akina ndugu” ambao wanapendana kikweli. (1 Pet. 2:17) Hiyo ni baraka iliyoje! Yehova amewachagua Wakristo watiwa-mafuta wakaishi mbinguni na amewafanya kuwa wana Wake, hivyo wanamwona Yehova kuwa “Baba” yao katika maana kamili. (Rom. 8:15-17) Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani wanaweza pia kumwona Yehova kuwa “Baba” yao. Yeye ndiye huwapa uhai na kutosheleza mahitaji ya waabudu wake wa kweli. Wale wenye tumaini la kuishi duniani watakuwa watoto wa Mungu kikamili watakapofikia ukamilifu na kuendelea kuwa waaminifu baada ya jaribu la mwisho.—Rom. 8:21; Ufu. 20:7, 8.
5, 6. Ni zawadi gani nzuri ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao, na kila mtoto ana wajibu gani? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 20.)
5 Wazazi huwapa watoto wao zawadi nzuri sana wanapowafundisha kusali na kuwasaidia wamwone Yehova kuwa Baba yao wa mbinguni anayewajali. Mwangalizi wa mzunguko kutoka Afrika Kusini anakumbuka hivi: “Tangu binti zetu walipozaliwa, nilisali nao kila usiku isipokuwa wakati nilipokuwa safarini. Mara nyingi binti zetu wanasema kwamba hawakumbuki maneno ya sala hizo. Hata hivyo, wanakumbuka hali ya utulivu na usalama pamoja na utakatifu wa kuwasiliana na Baba yetu, Yehova. Walipokua, niliwatia moyo wasali kwa sauti ili niwasikie wanavyomweleza Yehova mawazo na hisia zao. Hiyo ilikuwa nafasi nzuri sana ya kujua mambo yaliyokuwa moyoni mwao. Kisha, hatua kwa hatua niliwafundisha kutaja mambo muhimu yaliyo kwenye sala ya mfano ili wasali kwa njia inayofaa.”
6 Mabinti wa ndugu huyo walifanya maendeleo ya kiroho. Sasa kila mmoja wao ana ndoa yenye furaha, na wote wanamtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote pamoja na waume zao. Zawadi nzuri zaidi ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao ni kuwasaidia wasitawishe uhusiano wa karibu sana na Yehova. Bila shaka, kila mtu ana wajibu wa kudumisha uhusiano wake na Yehova. Kufanya hivyo kunahusisha kulipenda, na kuliheshimu sana jina la Mungu.—Zab. 5:11, 12; 91:14.
“JINA LAKO NA LITAKASWE”
7. Watu wa Mungu wamepewa heshima gani, lakini tunapaswa kufanya nini?
7 Ni heshima kubwa sana kwetu kulijua jina la Mungu na kuitwa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 15:14; Isa. 43:10) Tunasali hivi kwa Baba yetu wa mbinguni: “Jina lako na litakaswe.” Kufanya hivyo kutatuchochea tumwombe Yehova atusaidie kuepuka maneno au matendo yanayoweza kulivunjia heshima jina lake takatifu. Hatupaswi kuwa kama watu fulani katika karne ya kwanza ambao walitenda kinyume cha mambo waliyohubiri. Mtume Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Jina la Mungu linafanyiwa makufuru katikati ya mataifa kwa sababu yenu.”—Rom. 2:21-24.
8, 9. Toa mfano unaoonyesha jinsi ambavyo Yehova huwabariki wale wanaotaka kulitakasa jina lake.
8 Tunataka kulitakasa jina la Mungu. Dada mmoja nchini Norway ambaye mume wake alikufa mvulana wao alipokuwa na umri wa miaka miwili, anaeleza hivi: “Ulikuwa wakati mgumu sana maishani mwangu. Nilisali kila siku, karibu kila saa, nikimwomba Yehova anisaidie kuwa mtulivu ili nisifanye uamuzi wowote usiofaa au kuvunja uaminifu wangu, na hivyo kumpa Shetani sababu ya kumdhihaki Yehova. Nilitaka kulitakasa jina la Yehova, na nilitaka mwanangu amwone tena baba yake katika Paradiso.”—Met. 27:11.
9 Je, Yehova alijibu sala za dada huyo? Bila shaka! Waamini wenzake walimtia moyo kwa kuwa alishirikiana nao kwa ukawaida. Miaka mitano baadaye aliolewa na mzee wa kutaniko. Leo mtoto wake ambaye ana umri wa miaka 20, ni ndugu aliyebatizwa. Anasema hivi: “Nina furaha sana, kwa kuwa mume wangu alinisaidia kumlea.”
10. Yehova atafanya nini ili kulitakasa jina lake?
10 Ni nini kinahitaji kufanywa ili jina la Mungu litakaswe na kuondolewa shutuma kabisa? Ni lazima Yehova awaondoe wale wote wanaopinga kimakusudi enzi yake kuu. (Soma Ezekieli 38:22, 23.) Halafu, hatua kwa hatua wanadamu watafanywa kuwa wakamilifu. Tunatazamia kwa hamu wakati huo ambapo viumbe wote wenye akili watalitakasa jina la Yehova! Hatimaye, Baba yetu wa mbinguni atakuwa “vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Kor. 15:28.
“UFALME WAKO NA UJE”
11, 12. Yehova aliwasaidia watu wake kujua jambo gani katika mwaka wa 1876?
11 Kabla Yesu hajarudi mbinguni, mitume wake walimuuliza hivi: “Bwana, je, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” Jibu la Yesu lilionyesha kwamba haukuwa wakati wao kujua Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala lini. Aliwaambia wanafunzi wake wakazie fikira kazi muhimu ambayo walipaswa kuifanya, yaani, kutoa ushahidi. (Soma Matendo 1:6-8.) Hata hivyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake watazamie kuja kwa Ufalme wa Mungu. Hivyo tangu siku za mitume, Wakristo wamekuwa wakisali Ufalme huo uje.
12 Muda ulipokaribia, Yehova aliwasaidia watu wake kujua mwaka hususa ambao Yesu angeanza kutawala mbinguni akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Mwaka wa 1876, Charles Taze Russell alichapisha makala yenye kichwa, “Nyakati za Mataifa: Zakoma Wakati Gani?” kwenye gazeti Bible Examiner. Makala hiyo iliutaja 1914 kuwa mwaka muhimu. Ilisema kuwa “nyakati saba” zinazotajwa katika unabii wa Danieli ni sawa na zile “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilizotajwa na Yesu.a—Dan. 4:16; Luka 21:24.
13. Ni nini kilichotokea mwaka wa 1914, na tangu wakati huo matukio ya ulimwengu yanathibitisha nini?
13 Mwaka wa 1914, vita vilianza kupiganwa katika mataifa ya Ulaya, na baada ya muda mfupi vilienea duniani kote. Vita hivyo, ambavyo viliisha mwaka wa 1918, vilisababisha upungufu mkubwa sana wa chakula. Kisha kukatokea mafua makali sana ambayo yaliua watu wengi zaidi kuliko vita hivyo. Huo ukawa mwanzo wa utimizo wa ile “ishara” ambayo Yesu aliitoa ili kuonyesha kuwapo kwake akiwa Mfalme mpya wa dunia. (Mt. 24:3-8; Luka 21:10, 11) Mambo mengi yanathibitisha kwamba Bwana Yesu Kristo ‘alipewa taji’ mwaka wa 1914. Naye “akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 6:2) Yesu alisafisha mbingu kwa kumtupa Shetani na roho wake waovu kwenye ujirani wa dunia. Tangu wakati huo wanadamu wamejionea ukweli wa maneno haya: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufu. 12:7-12.
14. (a) Kwa nini bado ni muhimu tuombe Ufalme wa Mungu uje? (b) Ni kazi gani muhimu tunayopaswa kufanya?
14 Unabii ulioandikwa kwenye Ufunuo 12:7-12, unatusaidia kuelewa kwa nini wanadamu wamekuwa wakipatwa na matukio mabaya sana tangu Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala. Ingawa Yesu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, alianza kutawala mbinguni, bado Shetani anatawala dunia. Hata hivyo, hivi karibuni Yesu atakamilisha ushindi wake kwa kuondoa kabisa uovu duniani. Kabla wakati huo haujafika, tutaendelea kusali Ufalme wa Mungu na uje. Wakati huohuo, tunapaswa kuishi kupatana na sala zetu kwa kushiriki kutimiza mojawapo ya sehemu muhimu ya ile “ishara.” Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14.
“MAPENZI YAKO NA YATENDEKE DUNIANI”
15, 16. Tunawezaje kuishi kupatana na sala yetu ya kuomba mapenzi ya Mungu yatendeke duniani?
15 Karibu miaka 6,000 iliyopita, mapenzi ya Mungu yalikuwa yakifanywa kwa ukamili duniani. Ndiyo sababu Yehova alipotazama mwanzo mzuri wa mwanadamu alisema kwamba kila kitu “kilikuwa chema sana.” (Mwa. 1:31) Baada ya Shetani kuasi, wanadamu wachache sana wamekuwa wakifanya mapenzi ya Mungu duniani. Hata hivyo, leo tunafurahi sana kuwa miongoni mwa Mashahidi milioni nane hivi, ambao wanasali mapenzi ya Mungu yatendeke duniani na wanajitahidi kuishi kupatana na sala hiyo. Wanafanya hivyo kwa kuishi maisha yanayomfurahisha Yehova na kuwa wenye bidii ya kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu.
Je, unawasaidia watoto wako waombe mapenzi ya Mungu yatendeke duniani na kuishi kupatana na ombi hilo? (Tazama fungu la 16)
16 Kwa mfano, dada mmoja aliyebatizwa mwaka wa 1948, na kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika anasema hivi: “Sikuzote ninasali ili watu ambao ni kama kondoo wafikiwe na kusaidiwa kumjua Yehova kabla haijawa kuchelewa sana. Pia, kabla ya kuanza kumhubiria mtu, huwa ninamwomba Yehova anipe hekima ili niufikie moyo wa mtu huyo. Kuhusiana na wale walio kama kondoo ambao tayari wamepatikana, ninasali kwa Yehova atubariki tunapoendelea kujitahidi kuwatunza.” Haishangazi kwamba dada huyu mwenye umri wa miaka 80 amefanikiwa kuwasaidia watu wengi wawe Mashahidi wa Yehova. Bila shaka, unaweza kutafakari mifano mingine mizuri ya wale ambao wana bidii ya kufanya mapenzi ya Mungu licha ya uzee.—Soma Wafilipi 2:17.
17. Unahisije unapofikiria mambo ambayo Yehova atawafanyia wanadamu ili kutimiza mapenzi yake duniani?
17 Tutaendelea kusali mapenzi ya Mungu na yatendeke duniani, hadi maadui wote wa Ufalme wa Mungu watakapoondolewa. Kisha, tutaona mapenzi ya Mungu yakitendeka kikamili mabilioni ya wafu watakapofufuliwa katika paradiso duniani. Yesu alisema hivi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [yangu] na kutoka.” (Yoh. 5:28, 29) Hebu wazia shangwe tutakayopata tunapowakaribisha wapendwa wetu waliokufa! Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu].” (Ufu. 21:4) Watu wengi watakaofufuliwa ni wale “wasio waadilifu,” yaani, wale ambao hawakuwahi kamwe kujifunza kweli kumhusu Yehova Mungu na Mwana wake. Itakuwa shangwe iliyoje kuwafundisha mapenzi ya Mungu na kusudi lake, na hivyo kuwasaidia wastahili kupata “uzima wa milele.”—Mdo. 24:15; Yoh. 17:3.
18. Mwanadamu ana mahitaji gani muhimu zaidi?
18 Ufalme wa Mungu utalitakasa jina la Yehova na kuleta amani na umoja ulimwengu pote. Hivyo, Mungu atatosheleza mahitaji muhimu zaidi ya wanadamu atakapojibu maombi matatu ya kwanza katika sala ya mfano. Katika makala inayofuata tutazungumzia mahitaji mengine muhimu ambayo Yesu alitufundisha tuombe.
a Kwa maelezo zaidi kuhusiana na jinsi unabii huo ulivyotimizwa mwaka wa 1914 wakati Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala, tazama kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 215-218.
-
-
Ishi Kupatana na Sala ya Mfano—Sehemu ya PiliMnara wa Mlinzi—2015 | Juni 15
-
-
Ishi Kupatana na Sala ya Mfano Sehemu ya Pili
“Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji.”—MT. 6:8.
1-3. Kwa nini Lana alikuwa na uhakika kwamba Yehova anajua mahitaji yetu?
LANA hatasahau kamwe mambo yaliyotokea alipokuwa nchini Ujerumani mwaka 2012. Anahisi kwamba sala zake mbili zilijibiwa. Alitoa sala ya kwanza alipokuwa ndani ya treni akielekea uwanja wa ndege. Alimwomba Yehova amsaidie kutoa ushahidi. Alitoa sala ya pili baada ya kufika uwanja wa ndege na kujulishwa kwamba safari yake imeahirishwa hadi siku iliyofuata. Lana alimwomba Yehova amsaidie kwa kuwa hakuwa na pesa za kutosha wala mahali pa kulala.
2 Mara tu baada ya kumaliza sala yake ya pili, alimsikia kijana mmoja akimwambia, “Habari Lana, unafanya nini hapa?” Kijana huyo alikuwa mwanafunzi mwenzake wa zamani! Mama na nyanya yake walikuwa wamemsindikiza kwa kuwa alikuwa anaelekea Afrika Kusini. Lana alipowaeleza hali yake, Elke, mama ya kijana huyo alimkaribisha nyumbani kwake. Elke na mama yake walikuwa wakarimu sana, na walimuuliza Lana maswali mengi kuhusu imani yake na kazi yake ya upainia.
3 Baada ya kupata kiamsha kinywa asubuhi ya siku iliyofuata, Lana aliwajibu maswali mengine mengi kuhusu Biblia, na akawaomba anwani zao ili apange mtu fulani aendelee kujibu maswali yao. Lana alifika nyumbani salama salimini na anaendelea kufanya upainia wa kawaida. Anahisi kwamba “msikiaji wa sala” alijua mambo aliyohitaji, na alimsaidia.—Zab. 65:2.
4. Tutazungumzia mahitaji gani?
4 Inaweza kuwa rahisi kumwomba Yehova msaada tunapokabili tatizo fulani bila kutazamia, naye hufurahi kusikiliza maombi hayo ya watumishi wake waaminifu. (Zab. 34:15; Met. 15:8) Hata hivyo, tunapotafakari sala ya mfano, huenda tukaona kwamba kuna mahitaji mengine muhimu ambayo hatuyataji katika sala zetu. Katika makala hii tutazungumzia maombi manne ya mwisho. Tunapofanya hivyo, fikiria jinsi maombi matatu ya mwisho yanavyofunua mahitaji yetu ya kiroho, na pia jinsi tunavyoweza kuishi kupatana na ombi la nne linalohusu mkate wetu wa kila siku.—Soma Mathayo 6:11-13.
“UTUPE LEO MKATE WETU KWA AJILI YA SIKU HII”
5, 6. Kwa nini ni muhimu tuombe “mkate wetu” wa kila siku hata kama tuna chakula cha kutosha?
5 Ona kwamba Yesu hakutufundisha tuombe mkate “wangu” wa kila siku, bali mkate “wetu” wa kila siku. Victor, mwangalizi wa mzunguko barani Afrika, anaeleza hivi: “Mara nyingi ninamshukuru sana Yehova kwa kuwa mimi na mke wangu hatuhitaji kuhangaikia chakula au kodi ya nyumba. Kila siku ndugu zetu wanatutunza kwa upendo. Hata hivyo, ninasali kwamba wale wanaotusaidia wafanikiwe kushughulikia matatizo ya kiuchumi wanayokabili.”
6 Huenda tuna chakula cha kutosha, lakini ndugu zetu wengi ni maskini au wameathiriwa na majanga. Tunapaswa kusali kwa ajili yao na kutenda kupatana na sala hizo. Kwa mfano, ikiwa tuna vitu fulani tunaweza kuwasaidia waabudu wenzetu wenye uhitaji. Pia, tunaweza kuchangia kwa ukawaida kazi ya ulimwenguni pote, tukijua kwamba pesa hizo hutumiwa kwa hekima.—1 Yoh. 3:17.
7. Yesu alitumia mfano gani ili kukazia ushauri wake, “msihangaike kamwe juu ya kesho”?
7 Inaelekea Yesu alikuwa akizungumzia mahitaji yetu ya msingi alipokuwa akifundisha kuhusu kuomba mkate wa kila siku. Alionyesha namna ambavyo Mungu huyavisha maua ya porini, kisha akasema hivi: “Je, yeye hataona ni afadhali zaidi awavike, ninyi wenye imani kidogo? Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, . . . ‘Tutavaa nini?’” Akamalizia kwa kurudia ushauri huu muhimu: “Msihangaike kamwe juu ya kesho.” (Mt. 6:30-34) Jambo hilo linaonyesha kwamba tunapaswa kuridhika na mahitaji yetu ya kila siku badala ya kufuatilia vitu vya kimwili. Mahitaji hayo huenda yakatia ndani mahali pa kuishi, kazi itakayotusaidia kuiruzuku familia yetu, na hekima ya kufanya uamuzi mzuri kuhusiana na afya. Hata hivyo, mbali na kumwomba Yehova atutimizie mahitaji yetu ya kimwili, tunapaswa kusali pia kuhusu mahitaji yetu ya kiroho ambayo ni muhimu hata zaidi.
8. Maneno ya Yesu kuhusu mkate wetu wa kila siku yanapaswa kutukumbusha nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 25.)
8 Maneno ya Yesu kuhusu mkate wetu wa kila siku yanapaswa kutukumbusha uhitaji wetu wa chakula cha kiroho. “Mwanadamu ataishi,” akasema Bwana wetu, “si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Hivyo, sikuzote tunapaswa kumwomba Yehova aendelee kutulisha chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.
“UTUSAMEHE MADENI YETU”
9. Kwa nini dhambi zetu ni kama “madeni”?
9 Kwa nini Yesu alitumia neno “madeni,” ilhali wakati mwingine alitumia neno “dhambi”? (Mt. 6:12; Luka 11:4) Zaidi ya miaka 60 iliyopita, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilifafanua kwamba tunapotenda dhambi, ni kana kwamba tunadaiwa na Yehova. Tuna wajibu wa kumpenda na kumtii Yehova. Kwa hiyo, tunapomtendea dhambi Mungu, tunakuwa tumeshindwa kutimiza wajibu wetu. Yehova akitaka, anaweza kuondoa amani yake na kuvunja urafiki wetu pamoja naye. Gazeti hilo liliongeza hivi: “Kutenda dhambi humaanisha kwamba hatumpendi Mungu.”—1 Yoh. 5:3.
10. Yehova anatusamehe kwa msingi gani, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo?
10 Tunamshukuru sana Yehova kwa kutupatia njia ya pekee ya kusamehe dhambi zetu, yaani, dhabihu ya fidia ya Yesu. Ingawa fidia hiyo ilitolewa karibu miaka 2,000 iliyopita, tunapaswa kuithamini sana kana kwamba ni zawadi tuliyopewa leo. Hiyo ni zawadi “yenye thamani sana,” kwa kuwa hakuna mwanadamu angeweza kulipa fidia tunayohitaji ili tuwekwe huru kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. (Soma Zaburi 49:7-9; 1 Petro 1:18, 19.) Pia, maneno “dhambi zetu,” na si “dhambi zangu,” yanapaswa kutukumbusha kwamba sisi sote tunahitaji zawadi hiyo ya fidia. Ni wazi kwamba Yehova anataka tufikirie si tu hali yetu ya kiroho, bali pia hali ya kiroho ya wengine, kutia ndani wale ambao wametukosea. Kwa kawaida makosa hayo huwa madogo, na yanatupatia nafasi ya kuonyesha kwamba tunawapenda kikweli ndugu zetu, na tuko tayari kuwasamehe, kama vile ambavyo Mungu hutusamehe kwa hiari.—Kol. 3:13.
Ili Mungu akusamehe, unapaswa kuwa tayari kuwasamehe wengine (Tazama fungu la 11)
11. Kwa nini ni muhimu kuwa tayari kuwasamehe wengine?
11 Inasikitisha kwamba kwa sababu ya kutokamilika, huenda nyakati nyingine tukawawekea kinyongo wale waliotukosea. (Law. 19:18) Tukianza kuongea na wengine kuhusu jambo hilo, huenda baadhi yao wakatuunga mkono, na hivyo kusababisha mgawanyiko kutanikoni. Tukiruhusu hali hiyo iendelee, tutakuwa tunaonyesha wazi kwamba hatuthamini rehema za Mungu na zawadi ya fidia. Tusipokuwa na utayari wa kusamehe, Baba yetu hatatusamehe dhambi zetu kwa msingi wa dhabihu ya Mwana wake. (Mt. 18:35) Yesu alifafanua jambo hilo mara tu alipomaliza sala yake ya mfano. (Soma Mathayo 6:14, 15.) Mwishowe, ili tunufaike na msamaha wa Mungu, ni lazima tujitahidi kuepuka mazoea ya kufanya dhambi nzito. Tamaa yetu ya kuepuka mazoea ya kufanya dhambi ndiyo msingi wa ombi linalofuata.—1 Yoh. 3:4, 6.
“USITUINGIZE KATIKA JARIBU”
12, 13. (a) Ni nini kilichotokea muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa? (b) Kwa nini hatupaswi kuwalaumu wengine ikiwa tumekubali kushawishika? (c) Yesu alitimiza nini kwa kuwa mwaminifu mpaka kifo?
12 Kufikiria kile kilichomtokea Yesu muda mfupi baada ya kubatizwa, kunaweza kutusaidia tuelewe umuhimu wa ombi hili: “Usituingize katika jaribu.” Yesu aliongozwa na roho ya Mungu kuingia nyikani. Kwa nini? “Ili kujaribiwa na Ibilisi.” (Mt. 4:1; 6:13) Je, tushangazwe na jambo hilo? Hapana. Inafaa tuelewe sababu kuu iliyomfanya Mungu amtume Mwana wake duniani. Yesu alitumwa duniani ili kutatua suala lililozushwa wakati Adamu na Hawa walipoikataa enzi kuu ya Mungu. Maswali yaliyozushwa yalihitaji wakati ili kujibiwa. Kwa mfano, je, kulikuwa na tatizo kuhusiana na jinsi Mungu alivyomuumba mwanadamu? Je, mwanadamu mkamilifu angeweza kuunga mkono enzi kuu ya Mungu licha ya kushawishiwa na “yule mwovu”? Na je, mwanadamu ana uwezo wa kujitawala, kama Shetani alivyodai? (Mwa. 3:4, 5) Bila shaka, wakati ulihitajika ili kujibu maswali hayo. Isitoshe, kujibiwa kwa maswali hayo kungewaonyesha wazi viumbe wote wenye akili kwamba utawala wa Yehova ndio bora zaidi.
13 Yehova ni mtakatifu, hivyo hamjaribu yeyote kwa mambo maovu. Badala yake, Ibilisi ndiye “Mjaribu.” (Mt. 4:3) Ibilisi anaweza kutujaribu katika njia mbalimbali. Hata hivyo, kila mmoja wetu ana uhuru wa kuchagua kukubali au kupinga kishawishi. (Soma Yakobo 1:13-15.) Yesu alipokuwa akishawishiwa na Shetani, alipinga mara moja kila kishawishi kwa kunukuu Neno la Mungu. Hivyo, Yesu aliitetea enzi kuu ya Mungu. Lakini Shetani hakukata tamaa. Alisubiri “mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Yesu aliendelea kumpinga Shetani na kumtii Mungu akiwa Mtawala wake. Alitetea uadilifu wa enzi kuu ya Yehova na kuthibitisha kwamba mwanadamu mkamilifu anaweza kuwa mwaminifu hata anapokabili jaribu kali sana. Hata hivyo, Shetani anajaribu kuwanasa wafuasi wa Yesu, kutia ndani wewe.
14. Tunapaswa kufanya nini ili tusiingie katika kishawishi?
14 Kwa kuwa maswali yaliyozuka kuhusu enzi kuu ya Mungu bado yanahitaji kujibiwa, Yehova amemruhusu Mjaribu atumie ulimwengu wake kutushawishi. Yehova hatuingizi katika majaribu. Badala yake, ana uhakika kwamba tunaweza kuwa waaminifu na anataka kutusaidia. Hata hivyo, kwa kuwa Yehova anaheshimu uhuru wetu wa kuchagua, anaturuhusu tujiamulie wenyewe ikiwa tunataka kuwa waaminifu au la. Tunapaswa kufanya mambo mawili: kuwa macho kiroho na kudumu katika sala. Yehova anajibuje sala zetu?
Endelea kuwa mtu wa kiroho na mwenye bidii katika huduma (Tazama fungu la 15)
15, 16. (a) Tunapaswa kupinga vishawishi gani? (b) Ni nani anayepaswa kulaumiwa tukikubali kushawishika?
15 Yehova hutupatia roho yake takatifu ili kutuimarisha na kutusaidia tushinde vishawishi. Pia, Mungu anatuonya kupitia Neno lake na kutaniko kuhusu hali ambazo ni lazima tuziepuke, kama vile kutumia wakati, pesa, na nguvu nyingi katika mambo yasiyo ya lazima. Espen na Janne wanaishi katika nchi tajiri barani Ulaya. Kwa miaka mingi, walitumikia wakiwa mapainia wa kawaida katika eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme nchini mwao. Walilazimika kuacha upainia walipopata mtoto wa kwanza, na sasa wana watoto wawili. Espen anasema hivi: “Tunasali kwa Yehova mara kwa mara ili tusiingie katika kishawishi, kwa kuwa sasa hatuwezi kutumia muda mwingi katika utendaji wa kitheokrasi kama ilivyokuwa zamani. Tunamwomba Yehova atusaidie tuendelee kuwa watu wa kiroho na wenye bidii katika huduma.”
16 Kishawishi kingine ambacho kimewanasa watu wengi sana katika siku za karibuni ni kutazama ponografia. Hatupaswi kumlaumu Shetani ikiwa tumeshawishika kutazama ponografia. Kwa nini? Kwa sababu Shetani na ulimwengu wake hauwezi kutulazimisha tufanye jambo lolote lisilofaa. Baadhi ya watu hutazama ponografia kwa sababu wameruhusu akili yao itafakari mambo yasiyofaa. Hata hivyo, tunaweza kupinga kishawishi hicho, kama vile ambavyo maelfu ya ndugu na dada zetu wamefanya.—1 Kor. 10:12, 13.
“UTUKOMBOE KUTOKANA NA YULE MWOVU”
17. (a) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaishi kupatana na ombi letu: “Utukomboe kutokana na yule mwovu”? (b) Tutapata faraja gani hivi karibuni?
17 Ili tuishi kupatana na ombi letu: “Utukomboe kutokana na yule mwovu,” ni lazima tujitahidi sikuzote kutokuwa ‘sehemu ya ulimwengu wa Shetani.’ Hatupaswi ‘kuupenda ulimwengu wa Shetani au vitu vilivyo katika ulimwengu.’ (Yoh. 15:19; 1 Yoh. 2:15-17) Tutafarijika sana Yehova atakapojibu ombi letu kwa kumharibu Shetani na ulimwengu wake mwovu! Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani alipofukuzwa mbinguni, alijua kuwa muda wake ni mfupi. Kwa kuwa ana ghadhabu kubwa, anafanya yote anayoweza ili avunje uaminifu wetu. Kwa hiyo, ni lazima tuendelee kuomba tukombolewe kutokana na mwovu huyo.—Ufu. 12:12, 17.
18. Tunapaswa kufanya nini ili tuokoke ulimwengu wa Shetani utakapoharibiwa?
18 Je, unatamani kuishi katika ulimwengu mpya? Basi endelea kusali Ufalme wa Mungu uje ili kulitakasa jina la Mungu na kufanya mapenzi yake yatendeke duniani. Mtegemee Yehova ili akutunze kiroho na kimwili. Naam, azimia kuishi kupatana na sala ya mfano.
-