Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mwisho”​—Unamaanisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Mei 1
    • Mwanamke anaogopa mwisho huku watu wakikimbia moto, moshi na vifusi vilivyotokana na janga

      HABARI KUU | JE,MWISHO UMEKARIBIA?

      “Mwisho” Unamaanisha Nini?

      Unaposikia maneno, “Mwisho umekaribia!” nini huja akilini mwako? Je, wewe huwazia mhubiri shupavu aliye jukwaani akihubiri kwa ishara nyingi na sauti kubwa huku akiwa na Biblia mkononi? Au je, unafikiria kuhusu mzee mwenye ndevu nyingi aliyesimama kando ya barabara, akiwa amevaa vazi refu na amejifunga kamba kiunoni, akiwa na bango lenye ujumbe kuhusu siku ya maangamizi? Kufikiria mambo hayo huwafanya watu fulani washikwe na hofu, watilie shaka au hata kuwachekesha.

      Biblia inasema kwamba: ‘Mwisho utakuja.’ (Mathayo 24:14) Tukio hilo pia linaitwa “ile siku kuu ya Mungu” na “Har–Magedoni.” (Ufunuo 16:14, 16) Ni kweli kwamba watu wengi wamechanganywa na mafundisho ya kidini na uvumi mwingi na wenye kutisha kuhusu jambo hilo. Hata hivyo, Biblia inaeleza wazi ukweli kuhusu mwisho kwa kufafanua kikamili maana ya mwisho. Neno la Mungu linatusaidia pia kujua ikiwa mwisho umekaribia. Zaidi ya hayo, Biblia inatufundisha jinsi tunavyoweza kuokoka mwisho huo! Kwanza, acheni turekebishe baadhi ya maoni yasiyofaa kuhusu mwisho na kufafanua maana ya mwisho. Kulingana na Biblia, “mwisho” unamaanisha nini?

      MWISHO HAUMAANISHI NINI?

      1. MWISHO HAUMAANISHI DUNIA KUCHOMWA MOTO.

        Biblia inasema hivi: “[Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Andiko hilo na mengine, yanatuhakikishia kwamba Mungu hataiharibu dunia wala hataruhusu kamwe iharibiwe!—Mhubiri 1:4; Isaya 45:18.

      2. MWISHO SI TUKIO LISILO NA RATIBA.

        Biblia inasema kwamba mwisho ni tukio lililopangwa, yaani Mungu ameweka wakati hususa wa kuleta mwisho. Tunasoma hivi: “Kuhusu siku ile au saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika mbinguni wala Mwana, ila Baba. Endeleeni kutazama, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.” (Marko 13:32, 33) Ni wazi kwamba, Mungu (“Baba”) ametenga “wakati uliowekwa” atakapoleta mwisho.

      3. MWISHO HAUTALETWA NA WANADAMU AU JIWE FULANI LA ANGANI LITAKALOGONGA DUNIA.

        Mwisho utaletwa na nani? Ufunuo 19:11 inasema hivi: “Nami nikaona mbingu imefunguliwa, na, tazama! farasi mweupe. Na yeye aliyeketi juu yake anaitwa Mwaminifu na wa Kweli.” Mstari wa  19 unaendelea kusema hivi: “Nami nikamwona yule mnyama-mwitu na wafalme wa dunia na majeshi yao wamekusanyika pamoja ili kupigana vita na yule anayeketi juu ya farasi na jeshi lake.” (Ufunuo 19:11-21) Ingawa maneno hayo ni ya mfano, tunaweza kujua hili: Mungu atatuma jeshi la malaika ili kuwaangamiza adui zake.

      Waokokaji wa Har-Magedoni wakiwa na shangwe baada ya kuokoka uharibifu, na kwa mbali moshi unaonekana ukipaa

      Ujumbe wa Biblia kuhusu mwisho ni habari njema wala si habari mbaya

      MWISHO UNAMAANISHA NINI?

      1. MWISHO WA SERIKALI ZA WANADAMU.

        Biblia inaeleza hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali] ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Kama ilivyotajwa katika fungu lililotangulia, “wafalme wa dunia na majeshi yao,” ambao watakuwa “wamekusanyika pamoja ili kupigana vita na yule anayeketi juu ya farasi na jeshi lake,” wataangamizwa.—Ufunuo 19:19.

      2. MWISHO WA VITA, JEURI, NA UKOSEFU WA HAKI.

        “[Mungu] anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.” (Zaburi 46:9) “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” (Methali 2:21, 22) “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.”—Ufunuo 21:4, 5.

      3. MWISHO WA DINI AMBAZO HAZIKUMPENDEZA MUNGU WALA KUWASAIDIA WANADAMU.

        “Manabii wenyewe kwa kweli wanatoa unabii kwa uwongo; nao makuhani wanakandamiza kulingana na nguvu zao. . . . Nanyi mtafanya nini mwisho wake?” (Yeremia 5:31) “Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: ‘Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.’”—Mathayo 7:21-23.

      4. MWISHO WA WATU WANAOENDELEZA NA KUUNGA MKONO MAMBO YA ULIMWENGU.

        Yesu Kristo alisema hivi: “Basi huu ndio msingi wa hukumu, kwamba nuru imekuja ulimwenguni lakini watu wamelipenda giza kuliko nuru, kwa maana matendo yao yalikuwa maovu.” (Yohana 3:19) Biblia inaeleza kuhusu uharibifu wa ulimwengu wa kale katika kipindi alichoishi mwanamume mwaminifu, Noa. “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji. Lakini kwa neno hilohilo mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:5-7.

      Ona kwamba “siku ya hukumu na ya kuangamizwa” inayokuja inalinganishwa na “ulimwengu” wa siku za Noa. Ni ulimwengu gani ulioangamizwa? Dunia yetu haikuharibiwa; bali “watu wasiomwogopa Mungu” yaani, adui za Mungu ndio ‘walioangamia.’ Katika “siku ya hukumu” atakayoleta Mungu, adui za Mungu wataangamizwa. Lakini rafiki za Mungu wataokolewa kama ilivyokuwa kwa Noa na familia yake.—Mathayo 24:37-42.

      Hebu wazia jinsi dunia itakavyopendeza baada ya Mungu kuondoa uovu wote! Ni wazi kwamba ujumbe wa Biblia kuhusu mwisho ni habari njema wala si habari mbaya. Hata hivyo, huenda bado ukawaza hivi: ‘Je, Biblia inasema mwisho utakuja lini? Je, uko karibu? Ninawezaje kuokoka mwisho huo?’

      BAADA YA MWISHO

      Hali itakuwa namna gani baada ya mwisho? Maandiko yanaeleza kuhusu kipindi hicho kizuri. Kwa mfano: “‘[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yule aliyeketi juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” (Ufunuo 21:4, 5) Mwisho haumaanishi mwisho wa maisha yako. Mungu anataka tuokoke mwisho huo, na anatueleza jinsi ya kufanya hivyo.

  • Je, Mwisho Umekaribia?
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Mei 1
    • HABARI KUU

      Je, Mwisho Umekaribia?

      Je, Mungu ataendelea kuwaacha wanadamu wajitawale na hivyo kuhatarisha wakati wao ujao? Hapana. Kama tulivyoona mapema, atachukua hatua ili kumaliza mateso na ukandamizaji ambao umekuwako kwa karne nyingi. Muumba wa wanadamu na dunia anataka ujue kwamba wakati wake wa kufanya hivyo unakaribia. Anafunuaje habari hiyo muhimu?

      Fikiria mfano huu: Unaposafiri kwa gari, huenda ukatafuta kwanza mwongozo kwenye Intaneti, ramani, na habari iliyoandikwa. Kadiri unavyoona ishara za barabarani zilizo katika mwongozo ulio nao, ndivyo unavyozidi kuwa na uhakika wa kwamba unakaribia mwisho wa safari. Vivyo hivyo, Mungu ametupatia Neno lake, linaloeleza waziwazi kuhusu ishara zinazoonyesha hali za ulimwenguni. Tunapoona ishara hizo, tunakuwa na uhakika kwamba tunaishi katika siku za mwisho.

      Biblia inaeleza kwamba matukio ya ulimwengu yatafikia wakati muhimu sana utakaoongoza kwenye mwisho. Wakati huo kutakuwa na matukio na hali mbalimbali ulimwenguni ambazo hazijawahi kutokea katika historia ya wanadamu. Fikiria baadhi ya mambo yanayotajwa katika Neno la Mungu.

      1. MISUKOSUKO ULIMWENGUNI Unabii wa Biblia ulio katika Mathayo sura ya 24 unataja matukio katika dunia yatakayokuwa ishara ya mambo mengi yatakayoongoza kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo” na “ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mstari wa 3, 14) Matukio hayo yanatia ndani vita vikubwa, upungufu wa chakula, matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine, kuongezeka kwa uasi-sheria, kukosekana kwa upendo, na njia za ujanja zinazotumiwa na viongozi wa kidini kuwapotosha watu. (Mstari wa 6-26) Ni kweli kwamba kwa kadiri fulani, matukio hayo yamekuwako kwa karne nyingi. Hata hivyo, kadiri mwisho unavyokaribia, matukio hayo yangetokea katika kipindi kimoja cha wakati chenye msukosuko. Pia, matukio hayo yangefuatwa na ishara tatu zifuatazo zenye kuonya.

      2. MITAZAMO YA WATU Biblia inasema kwamba katika “siku za mwisho,” yaani kipindi cha wakati kabla ya mwisho kufika, watu wangekuwa na mitazamo isiyofaa. Tunasoma hivi: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Ni kweli kwamba ni kawaida kuona watu wasio na heshima, hata hivyo ni katika “siku za mwisho” tu ambapo mtazamo huo ungeonekana zaidi na kufanya kipindi hicho kufafanuliwa kuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Je, umejionea hali hiyo mbaya katika mitazamo ya watu?

      3. DUNIA INAHARIBIWA Biblia inasema kwamba Mungu atawaharibu “wale wanaoiharibu dunia.” (Ufunuo 11:18) Watu wanaiharibu dunia kwa njia gani? Mambo yalikuwa hivyo katika siku za Noa. Biblia inasema hivi: ‘Dunia ilikuwa imeharibika machoni pa Mungu wa kweli, na dunia ilijaa jeuri. Basi Mungu akaiona dunia na, tazama! ilikuwa imeharibika.’ Basi Mungu akasema hivi kuhusu watu hao waovu: ‘Mimi nitawaharibu.’ (Mwanzo 6:11-13) Je, umeona uthibitisho ulio wazi kwamba dunia inaendelea kujaa jeuri? Kwa kuongezea, wanadamu katika kipindi hiki cha wakati wana uwezo huu: Kuharibu dunia kihalisi kwa kufutilia mbali uhai wa wanadamu. Wana silaha zenye uwezo huo. Pia, dunia inaharibiwa kupitia njia nyingine. Mfumo unaotegemeza uhai duniani, yaani, hewa tunayopumua, mifumo ya ikolojia ya wanyama na mimea, bahari, inaendelea kuharibiwa kwa sababu ya kutotunzwa vizuri na wanadamu.

      Jiulize, ‘Katika karne moja iliyopita, je, wanadamu walikuwa na uwezo wa kuharibu kabisa kila kitu?’ Sasa wanadamu wametengeneza silaha za kisasa zaidi na wanaharibu mazingira. Inaonekana kwamba maendeleo ya teknolojia yanayokua kwa kasi yanazidi uwezo wa mwanadamu wa kuelewa au kudhibiti madhara yanayotokana nayo. Hata hivyo, mwanadamu hawezi kuongoza au kuamua kuhusu wakati ujao wa dunia. Hata kabla ya wanadamu kuangamiza vitu vyote duniani, Mungu atachukua hatua kwa kuwaangamiza wale wanaoiharibu dunia. Ameahidi hivyo!

      4. KAZI YA KUHUBIRI ULIMWENGUNI POTE Sehemu nyingine ya ishara ya mwisho ilitabiri kwamba kazi ya pekee ingefanyika: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Kazi hiyo ya kuhubiri ingekuwa tofauti sana na njia ya kuhubiri ambayo imetumiwa na dini nyingi kwa karne nyingi. Katika siku za mwisho, ujumbe hususa ungetangazwa kwa bidii, yaani, “hii habari njema ya ufalme.” Je, unajua kikundi chochote cha kidini kinachotangaza ujumbe huo? Hata ikiwa baadhi yao wanaonekana wakihubiri ujumbe kama huo, je, wanafanya hivyo katika eneo lenu au wamesambaza habari njema katika “dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote”?

      Mashahidi wa Yehova wakihubiri katika ufuo wa bahari; wanamsomea Biblia mwanamume

      Ufalme wa Mungu unahubiriwa ulimwenguni pote katika lugha nyingi

      Tovuti ya www.jw.org/sw inakazia pia “hii habari njema ya ufalme.” Tovuti hiyo ina machapisho yanayozungumzia ujumbe huo katika lugha zaidi ya 700. Je, kuna mpango wowote unaojua unaokazia fikira kutangaza habari njema ya Ufalme ulimwenguni pote? Kabla ya Intaneti kuanza kutumiwa, Mashahidi wa Yehova walijulikana kutokana na bidii yao ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Tangu mwaka wa 1939, jalada la kila toleo la gazeti la Mnara wa Mlinzi limekuwa na maneno “Unaotangaza Ufalme wa Yehova.” Kitabu kimoja cha mambo ya dini kilisema kwamba kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova, “haina kifani katika kiwango na upana.” Habari njema inayohubiriwa inakazia kwamba hivi karibuni ‘mwisho utakuja’ kupitia Ufalme wa Mungu.

      WAKATI MUHIMU KATIKA HISTORIA YA ULIMWENGU

      Je, umejionea maishani mwako ishara hizo nne za Biblia zenye kuonya zilizotajwa katika makala hii? Kwa zaidi ya miaka mia moja, gazeti hili limetoa habari kwa wasomaji wake kuhusu matukio ya ulimwengu na kuwasaidia wathibitishe kwamba tunakaribia mwisho. Ni kweli kwamba baadhi ya wachambuzi wanapinga jambo hilo kwa kudai kwamba mambo hayo na takwimu zilizotajwa ni za kuwaziwa na zinaweza kubadilika. Pia, wanadai kwamba kuongezeka kwa vyombo vya mawasiliano hufanya hali za ulimwengu zionekane kuwa mbaya. Hata hivyo, kuna ushahidi unaoongezeka unaonyesha kwamba tunaishi katika kipindi cha mwisho kilicho muhimu katika historia ya wanadamu.

      Wataalamu fulani wanahisi kwamba tunakaribia kuona mabadiliko makubwa katika dunia hii. Kwa mfano, mwaka wa 2014, Bodi ya Sayansi na Usalama ya gazeti la Bulletin of the Atomic Scientists, ililionya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu mambo yanayotishia uhai wa wanadamu. Wanasayansi hao walisema hivi: “Uchunguzi wenye kina tuliofanya wa vitisho hivyo unatufanya tufikie mkataa kwamba kuna tisho kubwa la kuangamizwa kwa wanadamu kwa sababu ya maendeleo ya teknolojia.” Watu wengi wanazidi kuamini kwamba tuko katika kipindi muhimu zaidi katika historia ya ulimwengu. Wachapishaji na wasomaji wengi wa gazeti hili hawana shaka hata kidogo kwamba kipindi hiki cha pekee ni siku za mwisho na kwamba mwisho unakaribia. Hata hivyo, unaweza kuwa na furaha badala ya kuogopa kile kitakachotukia wakati ujao. Kwa nini? Kwa sababu unaweza kuokoka mwisho!

      JE, WAO NI WATABIRI KUHUSU MWISHO WA DUNIA?

      Mashahidi wa Yehova si watu wanaotabiri kuhusu mwisho wa dunia. Kwa zaidi ya miaka mia moja, wamekuwa wakiwafundisha watu ujumbe wenye tumaini zuri la wakati ujao. Kwa mfano, katika kusanyiko lao la mwaka wa 1958 hotuba yenye kichwa, “Ufalme wa Mungu Unatawala—Je, Mwisho wa Dunia Uko Karibu?” ilieleza kwamba “Ufalme wa Mungu unakuja, si kuiharibu dunia hii, bali kuuangamiza ulimwengu wa Shetani. Ufalme wa Mungu unakuja, si ili kuichoma moto dunia, bali kutimiza mapenzi ya Mungu hapa duniani kama ilivyo mbinguni. Hivyo, Mungu hataiharibu dunia kwa sababu aliiumba; ataitunza kwa umilele wote.”

  • Wengi Wataokoka Mwisho​—Wewe Pia Unaweza
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Mei 1
    • Shahidi wa Yehova akimhubiria mwanamke ujumbe wa Biblia

      HABARI KUU | JE,MWISHO UMEKARIBIA?

      Wengi Wataokoka Mwisho Wewe Pia unaweza

      Biblia inatuambia kwamba mwisho utahusisha maangamizi: ‘Kutakuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa. Kwa kweli, kama siku hizo hazingefupishwa, hakuna chochote chenye mwili ambacho kingeokolewa.’ (Mathayo 24:21, 22) Hata hivyo, Mungu anatuahidi kwamba watu wengi wataokoka: “Ulimwengu unapitilia mbali . . . , lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.

      Unapaswa kufanya nini ili uokoke mwisho wa ulimwengu huu unaopitilia mbali na kisha ‘kudumu milele’? Je, unahitaji kujirundikia vitu vingi au kufanya mazoezi fulani ya mwili ili kujitayarisha? Hapana. Biblia inatuhimiza kufanya matayarisho ya aina tofauti. Tunasoma hivi: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Petro 3:10-12) Muktadha unaonyesha kwamba “vitu vyote” vitakavyoharibiwa vitatia ndani sehemu za utawala wa ulimwengu huu na wote wanaounga mkono utawala huo badala ya utawala wa Mungu. Ni wazi kwamba, kujirundikia vitu vingi hakutaweza kutuokoa kutokana na uharibifu unaokuja.

      Kwa kweli, wokovu wetu unatia ndani kumtumikia Yehova Mungu na kujifunza kuhusu aina ya mwenendo na matendo yanayompendeza. (Sefania 2:3) Badala ya kufuata maoni ya watu wengi na kupuuza ishara zinazoonyesha waziwazi kwamba tunaishi katika kipindi muhimu sana cha wakati, tunahitaji “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Mashahidi wa Yehova wanaweza kukuonyesha katika Biblia jinsi unavyoweza kuokoka siku hiyo inayokuja.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki