-
Mahangaiko Yako Kila Mahali!Mnara wa Mlinzi—2015 | Julai 1
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO
Mahangaiko Yako Kila Mahali!
“Nilienda kununua chakula lakini nikapata tu biskuti iliyouzwa mara 10,000 zaidi ya bei ya kawaida! Siku iliyofuata, maduka yote hayakuwa na chakula.” —Paul, Zimbabwe.
“Mume wangu aliniambia kwamba ananiacha. Nitakabiliana jinsi gani na usaliti huo? Nitafanya nini na watoto wangu?”—Janet, Marekani.
“Ving’ora vinapolia na mabomu kuanza kulipuka, mimi hukimbia na kujificha. Hata baada ya saa kadhaa kupita, mikono yangu bado hutetemeka.”—Alona, Israeli.
Tunaishi katika kipindi chenye mahangaiko, yaani, “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wengi wanakabili hali ngumu za kiuchumi, kuvunjika kwa familia, vita, milipuko ya magonjwa hatari, na misiba ya asili au ile inayosababishwa na wanadamu. Pia, kuna mahangaiko ya kibinafsi kama vile: ‘Je, uvimbe uliogunduliwa katika mwili wangu ni kansa?’ ‘Wajukuu wangu watalelewa katika ulimwengu wenye tabia gani?’
Si mahangaiko yote ambayo ni mabaya. Kwa kawaida, sisi hupatwa na mkazo kabla ya kufanya mtihani, kufanya jambo fulani mbele ya watu, au usahili wa kazi. Pia, woga unaofaa hutusaidia kuepuka hatari. Hata hivyo, mahangaiko yanayopita kiasi au yanayoendelea kwa muda mrefu yana madhara. Uchunguzi uliofanywa hivi karibuni uliohusisha watu zaidi ya 68,000, unaonyesha kwamba hata mahangaiko ya kiasi yanaweza kusababisha kifo cha mapema. Kwa sababu hiyo, Yesu aliuliza hivi: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” Kwa kweli, mahangaiko hayamsaidii mtu kuwa na maisha marefu. Kisha, Yesu akashauri hivi: “Acheni kuhangaika.” (Mathayo 6:25, 27) Lakini, hilo linawezekanaje?
Jibu la swali hilo linatia ndani kutumia hekima, kusitawisha imani ya kweli kuelekea Mungu, na kujenga tumaini linalotegemeka la wakati ujao. Hata ikiwa sasa hatukabili hali ngumu, huenda tukakabili hali hizo wakati ujao. Hivyo, acheni tuone jinsi kufuata hatua hizo kulivyomsaidia Paul, Janet, na Alona kushughulika na mahangaiko.
-
-
Mahangaiko Kuhusu PesaMnara wa Mlinzi—2015 | Julai 1
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO
Mahangaiko Kuhusu Pesa
“Baada ya kushuka kwa thamani ya pesa nchini kwetu, chakula kilipanda bei na kukosekana. Tulipanga foleni kwa saa kadhaa lakini mara nyingi chakula kiliisha hata kabla ya foleni kumalizika. Watu walikonda sana kwa sababu ya njaa, na wengine hata walizimia mitaani. Mahitaji ya msingi yaliuzwa kuanzia mamilioni, na kisha mabilioni. Mwishowe, sarafu ikashuka thamani. Sikuwa tena na akaunti ya benki, bima, na malipo ya uzeeni,” akasema Paul, mume na baba wa watoto wawili.
Paul
Paul alijua kwamba ili kuitunza familia yake, alihitaji kutumia “hekima inayotumika.” (Methali 3:21) Anasema hivi: “Nilikuwa fundi wa umeme, lakini nilifanya kazi yoyote ile niliyopata hata kama nililipwa kidogo. Wengine walinilipa kwa kunipatia chakula au bidhaa za nyumbani. Nilipolipwa miche minne ya sabuni, nilitumia miwili na kuuza iliyobaki. Mwishowe nilipata vifaranga 40. Walipokua, niliwauza na kununua wengine 300. Baadaye, nilibadilishana kuku 50 kwa mifuko miwili ya kilo 50 za unga wa mahindi. Hivyo, niliweza kulisha familia yangu na watu wengine kwa muda mrefu.”
Paul alijua pia kwamba jambo muhimu zaidi ambalo mtu anaweza kufanya ni kumtegemea Mungu. Tunapofanya kile ambacho Mungu anatuamuru, yeye hutusaidia. Kuhusu kutafuta mahitaji ya msingi ya maisha, Yesu alisema hivi: “Acheni kuhangaika kwa wasiwasi; kwa maana . . . Baba yenu anajua mnahitaji mambo hayo.”—Luka 12:29-31.
Inasikitisha kwamba, Shetani, ambaye ni adui mkubwa wa Mungu, amewadanganya watu wengi ulimwenguni waone kuhangaikia mahitaji ya kimwili kuwa jambo la msingi maishani mwao. Watu wana wasiwasi kupita kiasi kuhusu mahitaji yao, yawe ni halisi au ya kuwaziwa, nao hujitahidi kabisa kutafuta vitu wasivyohitaji. Wengi wamejiingiza katika madeni na mwishowe kugundua kwamba “mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.”—Methali 22:7.
Baadhi ya watu hufanya maamuzi yasiyofaa. Paul anasema hivi: “Jirani zangu wengi waliacha familia zao na marafiki na kuhamia nchi nyingine ili kutafuta ‘maisha bora.’ Baadhi yao walisafiri bila kuwa na vibali vya uhamiaji na jambo hilo lilifanya iwe vigumu kupata kazi. Mara nyingi walihitaji kuwakimbia polisi na waliishi mitaani. Hawakumruhusu Mungu awasaidie. Hata hivyo, tukiwa familia tuliazimia kukabiliana na matatizo ya kiuchumi huku tukimtegemea Mungu.”
KUFUATA USHAURI WA YESU
Paul anaendelea hivi: “Yesu alisema: ‘Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.’ Hivyo, kila siku nilisali kwamba Mungu ‘atupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii’ ili tuendelee kuwa hai. Naye alitusaidia kama tu Yesu alivyoahidi. Si mara zote tulipata chakula tulichopenda. Pindi moja, nilisimama katika foleni ya chakula bila kujua chakula kinachouzwa. Nilipomfikia muuzaji, niligundua kwamba ni maziwa-mgando. Sipendi maziwa-mgando. Hata hivyo, usiku huo tulikula maziwa-mgando. Ninamshukuru Mungu kwamba katika kipindi hicho chote, familia yangu haikuwahi kulala njaa.”a
Mungu ameahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—Waebrania 13:5
“Kwa sasa, hali yetu ya kiuchumi ni nzuri. Hata hivyo, mambo tuliyojionea yametufundisha kwamba kumtegemea Mungu ni dawa ya mahangaiko. Yehovab ataendelea kutusaidia ikiwa tu tutaendelea kufanya mapenzi yake. Tumejionea ukweli wa Zaburi 34:8: ‘Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia.’ Sasa, hatuogopi kukabili hali ngumu ya kiuchumi ikiwa itatokea tena.”
Mungu anawasaidia waaminifu kupata ‘mkate kwa ajili ya siku’”
“Sasa tunaelewa vizuri kwamba ili kuwa hai, wanadamu wanahitaji chakula, na si kazi au pesa. Tunasubiri kwa hamu wakati ambapo ahadi hii ya Mungu itatimizwa: ‘Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani.’ Kwa sasa, ‘tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.’ Tunaimarishwa na maneno haya ya Biblia: ‘Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye amesema: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” Hivi kwamba tuwe hodari na kusema: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”’”c
Imani ya kweli inahitajiwa ili ‘kutembea pamoja na Mungu’ kama Paul na familia yake wanavyofanya. (Mwanzo 6:9) Iwe sasa unakabili hali mbaya ya uchumi au huenda ukakabili hali hiyo wakati ujao, mfano mzuri wa Paul katika kuonyesha imani na kutumia hekima, unatufundisha masomo muhimu.
Hata hivyo, vipi ikiwa matatizo ya familia yanakufanya uwe na mahangaiko?
a Soma Mathayo 6:11, 34.
b Yehova ni jina la Mungu kama linavyotajwa katika Biblia.
-
-
Mahangaiko Kuhusu FamiliaMnara wa Mlinzi—2015 | Julai 1
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO
Mahangaiko Kuhusu Familia
“Muda mfupi baada ya baba yangu kufa, mume wangu aliniambia kwamba ameanzisha uhusiano na mwanamke mwingine,” akasema Janet. “Muda mfupi baadaye, alifungasha na kuondoka bila kuniaga akiniacha na watoto wetu wawili.” Janet alipata kazi, lakini mshahara wake haukutosha kulipia gharama za nyumba. Alikabili pia mambo mengine zaidi ya matatizo ya kiuchumi. Anasema hivi: “Mimi huhangaika na kulemewa sana kutokana na majukumu mapya ambayo nilihitaji kuanza kutimiza nikiwa peke yangu.” Aliendelea kusema hivi: “Nilihisi hatia kwamba sikuweza kuwatunza watoto wangu kama wazazi wengine. Hata sasa, bado mimi huwa na wasiwasi kuhusu maoni ya wengine kuelekea mimi na watoto wangu. Je, wanaona kwamba sikufanya jitihada zozote ili kudumisha ndoa yangu?”
Janet
Sala inamsaidia Janet kudhibiti hisia zake na kusitawisha urafiki na Mungu. “Pindi ngumu zaidi ni wakati wa usiku kunapokuwa kimya kabisa, mimi hukumbuka mambo yanayonihangaisha. Kusali na kusoma Biblia hunisaidia kupata usingizi. Andiko ninalolipenda sana ni Wafilipi 4:6, 7 linalosema: ‘Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.’ Nimetumia pindi nyingi za usiku kusali na nimehisi amani ya Yehova imenifariji.”
Maneno haya ya Yesu yenye uhakikisho kuhusu sala katika Mahubiri yake ya Mlimani yanaweza kutumika katika mahangaiko ya aina zote: “Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.” (Mathayo 6:8) Tunahitaji kumwomba. Sala ni njia ya msingi ya ‘kumkaribia Mungu.’ Tutapata matokeo gani tukifanya hivyo? “Naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
Bila shaka, sala hutimiza mengi zaidi ya kutufanya tujihisi vizuri, baada ya kueleza mahangaiko yetu. Yehova, “Msikiaji wa sala,” hutenda pia kwa niaba ya wale wote wanaomwitia katika imani. (Zaburi 65:2) Ndiyo sababu Yesu aliwafundisha wafuasi wake “kusali sikuzote bila kukata tamaa.” (Luka 18:1) Ni lazima tuendelee kusali kwa Mungu na kumwomba mwongozo na msaada wake, tukiwa na uhakika kwamba atatuthawabisha kutokana na imani yetu. Hatupaswi kamwe kutilia shaka tamaa na uwezo wake wa kutenda. ‘Kusali bila kuacha’ katika njia hiyo kunaonyesha kwamba tuna imani ya kweli.—1 Wathesalonike 5:17.
KILE KINACHOMAANISHWA NA KUWA NA IMANI
Imani ni nini? Imani inahusisha “kupata ujuzi” kumhusu Mungu. (Yohana 17:3) Tunafanya hivyo kwa kujua maoni ya Mungu kupitia Biblia. Tunajifunza kwamba yeye hutuona kila mmoja wetu na anataka kutusaidia. Hata hivyo, imani ya kweli inahusisha mengi zaidi ya kujua jambo fulani kuhusu Mungu. Humaanisha pia kuwa na urafiki wa karibu pamoja naye. Kama vile ilivyo kwa marafiki, urafiki na Mungu haujitokezi tu wenyewe. Imani yetu inazidi ‘kuongezeka’ tunapoendelea kujifunza mengi kumhusu, ‘tunapofanya mambo yanayompendeza,’ na tunapojionea akitenda ili kutusaidia. (2 Wakorintho 10:15; Yohana 8:29) Imani ya namna hiyo ndiyo iliyomsaidia Janet, kukabiliana na mahangaiko yake.
Janet anasema hivi: “Jambo ambalo kwa kweli limenisaidia kujenga imani yangu ni kuona mkono wa Yehova katika kila hatua ya maisha yangu. Mara nyingi tunakabili ukosefu wa haki ambao huonekana kuwa mgumu kushughulika nao. Kupitia sali nyingi, Yehova ametokeza njia ambayo nisingeweza kamwe kuijua ya kushughulikia mahangaiko. Ninapomshukuru, jambo hilo hunikumbusha mambo mengi aliyonifanyia. Mara zote yeye hutusaidia kwa wakati unaofaa, na pindi kadhaa kwa muda mwafaka. Pia amenipa marafiki wa kweli ambao ni ndugu na dada Wakristo. Sikuzote wako tayari kunisaidia nao ni mifano mizuri kwa watoto wangu.”a
“Ninajua kwa nini Yehova anasema hivi katika Malaki 2:16: ‘Ninachukia talaka.’ Kwa mwenzi asiye na hatia huo ni usaliti mbaya sana. Ni miaka mingi imepita tangu mume wangu aliponiacha, lakini nyakati fulani mimi bado ninahisi uchungu moyoni. Ninapohisi hivyo, mimi hujaribu kuwasaidia wengine, na kufanya hivyo hunisaidia.” Hivyo, Janet amepunguza mahangaiko yake kwa kufuata kanuni ya Biblia ya kutojitenga na wengine.b— Methali 18:1.
Mungu ni “baba ya wavulana wasio na baba na mwamuzi wa wajane.”—Zaburi 68:5
Janet, anasema hivi: “Faraja yangu kubwa inatokana na kujua kwamba Mungu ni ‘baba ya wavulana wasio na baba na mwamuzi wa wajane.’ Yeye hawezi kutuacha kamwe kama mume wangu alivyofanya.” (Zaburi 68:5) Janet anajua kwamba Mungu hatujaribu kwa “mambo maovu.” Badala yake, yeye huwapa hekima “wote kwa ukarimu” na pia “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili kutusaidia kukabiliana na mahangaiko yetu.—Yakobo 1:5, 13; 2 Wakorintho 4:7.
Hata hivyo, namna gani ikiwa tuna mahangaiko kwa sababu maisha yetu yako hatarini?
b Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na mahangaiko, soma habari kuu “Je, Unaongoza Maisha Yako?” katika makala ya gazeti la Amkeni! la Julai 2015 linapatikana kwenye Tovuti ya www.jw.org/sw.
-
-
Mahangaiko Kuhusu HatariMnara wa Mlinzi—2015 | Julai 1
-
-
HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO
Mahangaiko Kuhusu Hatari
Alona, anasema hivi: “Ninaposikia mlio wa king’ora na milipuko ya mabomu, moyo wangu huenda mbio nami hukimbia ili kutafuta mahali pa kujificha. Hata hivyo, mimi huwa na wasiwasi hata ninapokuwa huko. Hali huwa mbaya hata zaidi ninapokuwa nje pasipo na mahali pa kujificha. Pindi fulani, nilipokuwa nikitembea mtaani nilianza kulia na nikashindwa kupumua. Ilinichukua saa kadhaa kutulia. Kisha, king’ora kikaanza kulia tena.”
Alona
Vita ni moja kati ya vyanzo vingi vya hatari. Kwa mfano, kujua kwamba wewe au mtu fulani unayempenda anakabili ugonjwa hatari, jambo hilo linaweza kushtua sana. Kwa wengine, hofu ya kitakachotokea wakati ujao inaweza kuwafanya wawe na mahangaiko. Huenda wakawaza hivi kwa wasiwasi: ‘Je, watoto wetu au wajukuu wetu, wataishi katika ulimwengu huu wenye vita, jeuri, uchafuzi, mabadiliko ya tabia ya nchi, na magonjwa ya mlipuko?’ Tunaweza kukabiliana jinsi gani na mahangaiko hayo?
Kujua kwamba mambo mabaya hutukia humsaidia, ‘mtu mwerevu ambaye ameuona msiba ajifiche.’ (Methali 27:12) Kama vile tunavyojitahidi kulinda afya yetu, tunaweza kuchukua hatua kulinda hali yetu ya kiakili na kihisia. Burudani zenye jeuri na ripoti za habari zilizojaa picha zinazotisha hutuongezea mahangaiko sisi na watoto wetu. Kuepuka mambo hayo hakumaanishi kwamba tunapuuza uhalisia wa mambo. Mungu hakuumba akili yetu ili kuwaza uovu. Badala yake, tunapaswa kujaza akili yetu “mambo yoyote yaliyo ya kweli, . . . uadilifu, . . . safi kiadili, . . . na ya kupendeka.” Tukifanya hivyo “Mungu wa amani” atatupa amani ya moyoni na akilini.—Wafilipi 4:8, 9.
UMUHIMU WA SALA
Imani ya kweli hutusaidia kukabiliana na mahangaiko. Biblia hutuhimiza “kukesha kuhusiana na sala.” (1 Petro 4:7) Tunaweza kumwomba Mungu msaada, hekima na ujasiri ili tuweze kukabiliana vizuri na hali zetu, tukiwa na uhakika kwamba “yeye hutusikia kwa habari ya jambo lolote tunaloomba.”—1 Yohana 5:15.
Pamoja na mume wake, Avi
Biblia inaeleza kwamba si Mungu, bali Shetani ndiye “mtawala wa ulimwengu huu” na kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Hii ndiyo sababu Yesu alitufundisha tusali hivi: “Utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) “Ninaposikia mlio wa king’ora, mimi humwomba Yehova anisaidie kudhibiti hisia zangu,” anasema Alona. “Pia, mume wangu mpendwa husali pamoja nami. Sala husaidia sana.” Ni kama tu Biblia inavyosema: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli.”—Zaburi 145:18.
TUMAINI LETU LA WAKATI UJAO
Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa mahangaiko. Kupitia Yesu, “Mkuu wa Amani,” Mungu ‘atakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Isaya 9:6; Zaburi 46:9) “Naye [Mungu] hakika atafanya hukumu kati ya vikundi vingi vya watu . . . Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena. . . . Wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:3, 4) Familia zenye furaha ‘zitajenga nyumba na kukaa ndani yake, na hakika zitapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.’ (Isaya 65:21) “Na hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa’”—Isaya 33:24.
Leo, licha ya jitihada mbalimbali, si rahisi mara zote kuzuia “tukio lisilotazamiwa” au kuepuka kuwa mahali pasipofaa na wakati usiofaa. (Mhubiri 9:11) Kama ilivyo kwa karne nyingi, vita, jeuri, na magonjwa yameendelea kuua watu wema. Watu hao wanatumaini gani?
Mamilioni ya watu, walio katika kumbukumbu ya Mungu, watafufuliwa ili waishi tena. Kwa sasa, wako salama katika kumbukumbu kamilifu ya Mungu, mpaka siku ambayo ‘wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Biblia inapozungumzia kuhusu ufufuo, hutuhakikishia hivi: “Tumaini hilo tunalo kama nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Waebrania 6:19) Mungu “ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua [Yesu] kutoka kwa wafu.”—Matendo 17:31.
Kwa sasa, hata wale ambao hujitahidi kumpendeza Mungu wanakabili mahangaiko. Kwa kuchukua hatua zinazofaa, kumkaribia Mungu kupitia sala, na kujenga imani yetu kuhusu wakati ujao kupitia Biblia, Paul, Janet, na Alona wote wamekabiliana na mahangaiko yao kwa mafanikio. Kama ilivyo katika kisa chao, “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu.”—Waroma 15:13.
-