SURA YA 35
Ninaweza Kuwa Rafiki ya Mungu Jinsi Gani?
Baada ya kukumbwa na jambo fulani lenye kuhuzunisha, Jeremy alianza kuona faida ya kuwa na urafiki pamoja na Mungu. Anasema: “Nilipokuwa na umri wa miaka 12, baba yangu alituacha. Usiku mmoja nilikuwa nikisali kitandani, nikimsihi Yehova amfanye baba yangu arudi nyumbani.”
Akiwa katika hali hiyo, Jeremy alianza kusoma Biblia. Aliposoma Zaburi 10:14, aliguswa moyo sana. Mstari huo unasema hivi kumhusu Yehova: “Mtu mwenye taabu, mvulana asiye na baba, anajikabidhi kwako. Wewe mwenyewe umekuwa msaidizi wake.” Jeremy anasema: “Nilihisi kana kwamba Yehova alikuwa akizungumza nami na kunijulisha kwamba yeye ni msaidizi wangu; yeye ni Baba yangu. Singeweza kupata baba bora kuliko yeye!”
IWE uko katika hali kama ya Jeremy au sivyo, Biblia inaonyesha kwamba Yehova anataka uwe rafiki yake. Biblia inasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Hebu fikiria maneno hayo: Ijapokuwa huwezi kumwona—na kwa kweli yeye si kijana kama wewe—Yehova Mungu anakualika uwe rafiki yake!
Lakini ili uwe rafiki ya Mungu lazima uchukue hatua fulani. Kwa mfano: Ukipanda ua unajua kwamba halitakua lenyewe. Ili likue, lazima ulitilie maji kwa ukawaida na kuliweka katika mazingira yanayofaa ukuzi. Ndivyo pia na urafiki pamoja na Mungu. Unaweza kuukuza urafiki wa aina hiyo jinsi gani?
Faida ya Kujifunza
Marafiki huwasiliana—kila mmoja husikiliza na kuzungumza. Ndivyo pia na urafiki pamoja na Mungu. Tunaposoma na kujifunza Biblia, tunamsikiliza Mungu.—Zaburi 1:2, 3.
Ni kweli kwamba huenda kiasili hupendi kusoma. Vijana wengi hupenda kutazama televisheni, kucheza, au kuwa tu na marafiki. Lakini ikiwa unataka kuwa rafiki ya Mungu, hakuna njia ya mkato. Lazima umsikilize kwa kujifunza Neno lake.
Hata hivyo, usiwe na wasiwasi. Si lazima kujifunza kuwe jambo lenye kuchosha. Unaweza kujifunza kufurahia kufanya hivyo—hata ikiwa kiasili hupendi kusoma. Jambo la kwanza unalohitaji kufanya ni kutenga wakati wa kujifunza Biblia. “Mimi nina ratiba,” anasema msichana mmoja anayeitwa Lais. “Mimi husoma sura moja ya Biblia kila asubuhi ninapoamka.” Maria, mwenye umri wa miaka 15, ana ratiba tofauti. “Mimi husoma sehemu fulani ya Biblia kila siku kabla ya kwenda kulala,” anasema.
Ili kuanza programu yako mwenyewe ya kujifunza, tazama sanduku lililo katika ukurasa wa 292. Kisha, katika nafasi iliyo hapa chini, andika wakati ambapo unaweza kutumia dakika 30 hivi ukijifunza Neno la Mungu.
․․․․․
Kupanga wakati ni hatua ya kwanza tu. Ukishaanza kujifunza, huenda ukaona kwamba nyakati nyingine si rahisi kusoma Biblia. Huenda ukakubaliana na Jezreel, mwenye umri wa miaka 11, aliyesema hivi waziwazi: “Sehemu fulani za Biblia ni ngumu na si zenye kusisimua sana.” Ikiwa unahisi hivyo, usikate tamaa. Sikuzote ona wakati wa kujifunza kuwa wakati wa kumsikiliza Yehova Mungu, rafiki yako. Mwishowe, kujifunza Biblia kutakuwa jambo lenye kusisimua na lenye faida kwako ikitegemea jitihada zako!
Sala Ni Muhimu
Tunaposali, tunazungumza na Mungu. Hebu wazia jinsi sala ilivyo zawadi ya ajabu! Unaweza kuzungumza na Yehova Mungu wakati wowote, iwe ni mchana au usiku. Anapatikana sikuzote. Pia, anataka kukusikiliza. Ndiyo sababu Biblia inakuhimiza: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.”—Wafilipi 4:6.
Kama andiko hilo linavyoonyesha, kuna mambo mengi unayoweza kumwambia Yehova. Mambo hayo yanaweza kutia ndani matatizo na mahangaiko yako. Pia yanaweza kutia ndani mambo unayothamini kutoka kwake. Wewe huwashukuru rafiki zako kwa mambo mazuri wanayokufanyia, sivyo? Basi, unaweza kumshukuru Yehova pia, ambaye amefanya mengi zaidi kuliko rafiki yeyote anavyoweza kukufanyia.—Zaburi 106:1.
Hapa chini, andika mambo unayothamini kutoka kwa Yehova.
․․․․․
Bila shaka, mara kwa mara wewe huwa na wasiwasi na mahangaiko fulani. Zaburi 55:22 inasema: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”
Hapa chini, andika mambo fulani yanayokuhangaisha ambayo ungependa kusali juu yake.
․․․․․
Mambo Ambayo Umejionea Maishani
Kuna jambo lingine kuhusiana na urafiki wako na Mungu ambalo hupaswi kupuuza. Mtunga-zaburi Daudi aliandika: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” (Zaburi 34:8) Daudi alitunga Zaburi ya 34 baada ya kupitia hali yenye kuogopesha. Alikuwa akimkimbia Mfalme Sauli aliyetaka kumwua—masaibu kwelikweli. Kisha akalazimika kutafuta kimbilio kati ya Wafilisti waliokuwa maadui. Uhai wake ulipokuwa hatarini, Daudi alijifanya mwenda-wazimu na kukimbia.—1 Samweli 21:10-15.
Daudi hakuona kwamba alikuwa ameponea chupuchupu kwa sababu ya werevu wake mwenyewe. Badala yake, alisema kwamba wokovu wake ulitokana na Yehova. Mapema katika zaburi iliyotajwa, aliandika: “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha.” (Zaburi 34:4) Mambo aliyojionea mwenyewe yalimchochea Daudi kuwahimiza wengine ‘waonje na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’a
Kuna jambo lolote maishani mwako linaloonyesha kwamba Yehova anakujali? Ikiwa lipo, liandike hapa chini. Dokezo: Si lazima liwe jambo la ajabu sana. Fikiria baraka unazopata kila siku, ambazo huenda hata ni rahisi kuzipuuza.
․․․․․
Huenda wazazi wako walikufundisha Biblia. Ikiwa ndivyo, hiyo ni baraka. Hata hivyo, bado wewe binafsi unahitaji kukuza urafiki pamoja na Mungu. Ikiwa hujafanya hivyo, unaweza kutumia habari iliyo katika sura hii kuanza kufanya hivyo. Yehova atabariki jitihada zako. Biblia inasema: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata.”—Mathayo 7:7.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 38 NA 39
Unaona ni vigumu kuzungumza na wengine kumhusu Mungu? Jifunze jinsi unavyoweza kutetea imani yako.
[Maelezo ya Chini]
a Biblia nyingine hutafsiri maneno “onjeni mwone,” kuwa “jigundulie mwenyewe,” “jionee mwenyewe,” na “kupitia mambo utakayojionea utaona kwamba.”—Contemporary English Version, Today’s English Version, na The Bible in Basic English.
MAANDIKO MUHIMU
“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.
PENDEKEZO
Ukisoma kurasa nne tu za Biblia kila siku, utamaliza kuisoma yote kwa muda wa mwaka mmoja hivi.
JE, WAJUA . . .?
Kusoma kwako kitabu hiki na kufuata mashauri yaliyomo yanayotegemea Biblia ni uthibitisho wa kwamba Yehova anapendezwa na wewe binafsi.—Yohana 6:44.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili kufaidika zaidi na funzo la Biblia la kibinafsi, nita ․․․․․
Ili kuwa na mazoea ya kusali, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Unaweza kufanya nini ili funzo la Biblia liwe lenye kupendeza zaidi?
● Kwa nini Yehova anataka kusikiliza sala za wanadamu ambao si wakamilifu?
● Unaweza kufanya nini ili sala zako ziwe na maana zaidi?
[Blabu katika ukurasa wa 291]
‘‘Nilipokuwa mdogo, sala zangu zilikuwa kama wimbo. Sasa mimi hujaribu kusali kuhusu mambo mazuri na mabaya ya kila siku. Kwa kuwa hakuna siku mbili zinazofanana kabisa, hilo hunisaidia kutorudia-rudia mambo yaleyale.’’—Eve
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 292]
Ichanganue Biblia
1. Chagua simulizi fulani katika Biblia ambalo ungependa kusoma. Sali upate hekima ya kuelewa habari hiyo.
2. Soma simulizi hilo kwa uangalifu. Usiwe na haraka. Unaposoma, piga picha akilini. Jiwazie ukiwa katika hali unayosoma: Jaribu kuona kinachoendelea, kusikia sauti mbalimbali, vuta pumzi na kunusa harufu mbalimbali, onja ladha ya chakula, na kadhalika. Fanya simulizi hilo liwe halisi akilini mwako!
3. Fikiria habari ambayo umesoma. Jiulize maswali kama vile:
● Kwa nini Yehova alitia ndani simulizi hilo katika Neno lake?
● Ni nani wanaostahili kuigwa, na ni nani walio vielelezo vya kuonya?
● Ni jambo gani la maana ninaloweza kujifunza kutokana na usomaji huo?
● Simulizi hilo linanifundisha nini kuhusu Yehova na jinsi anavyofanya mambo?
4. Toa sala fupi kwa Yehova. Mwambie mambo ambayo umejifunza kutokana na funzo lako la Biblia na jinsi unavyopanga kutumia habari hiyo maishani mwako. Mshukuru Yehova sikuzote kwa zawadi ambayo amekupa—Neno lake, Biblia Takatifu!
[Picha]
“Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.”—Zaburi 119:105.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 294]
Tanguliza Mambo ya Maana
Huna wakati wa kusali? Huna wakati wa kujifunza Biblia? Mara nyingi inategemea jinsi unavyopanga mambo yako.
Jaribu zoezi hili: Chukua ndoo, na uweke mawe kadhaa makubwa ndani yake. Kisha jaza mchanga hadi pomoni. Ndoo hiyo imejaa mawe na mchanga.
Sasa mwaga chini kila kitu kutoka katika ndoo hiyo, lakini uhifadhi mawe na mchanga huo. Rudia tena zoezi hilo: Sasa jaza mchanga kwanza, kisha ujaribu kuyaweka mawe ndani ya ndoo. Eti hakuna nafasi? Ni kwa sababu umetangulia kuweka mchanga.
Zoezi hilo linakufundisha nini? Biblia inasema: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Ukitanguliza mambo madogo kama vile burudani, hutapata kamwe nafasi ya kutosha kufanya mambo yaliyo makubwa—mambo ya kiroho. Lakini ukifuata shauri la Biblia, utaona kwamba una nafasi ya kutosha kufanya yote mawili, mambo ya Ufalme na burudani kwa kiasi kinachofaa. Siri ni kujua unachopaswa kutanguliza!
[Picha katika ukurasa wa 290]
Kama ua lililopandwa, urafiki pamoja na Mungu unahitaji kutunzwa vizuri ili ukue