-
Mtu Unayempenda AnapokufaMnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 3
-
-
HABARI KUU
Mtu Unayempenda Anapokufa
“Mwanangu,. . . usilie. Kazi ya Mungu haina makosa.”
Mwanamke anayeitwa Bebe aliambiwa maneno hayo, siku ya mazishi ya baba yake aliyekufa kutokana na aksidenti ya gari.
Bebe alimpenda sana baba yake. Maneno hayo aliyoambiwa na rafiki wa familia mwenye nia nzuri, yalimuumiza sana badala ya kumfariji. Bebe aliendelea kujiambia, “baba hakupaswa kufa.” Kuonyesha kwamba bado alikuwa na huzuni, miaka mingi baadaye Bebe alisimulia tukio hilo katika kitabu chake.
Sawa na Bebe, wengi wanakubali kwamba huzuni ya kufiwa haiishi haraka, hasa ikiwa aliyekufa alikuwa mtu wa karibu sana. Biblia inasema kifo ni “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Kifo huharibu maisha yetu na hakizuiliki. Hakuna yeyote kati yenu anayeweza kuepuka madhara ya kifo. Hivyo, haishangazi kwamba tunapopatwa na msiba mara nyingi tunashindwa kukabiliana na hali hiyo.
Huenda ukajiuliza: ‘Huzuni ya kufiwa huisha baada ya muda gani? Mtu anawezaje kukabiliana na huzuni hiyo? Ninaweza kuwafariji jinsi gani wale waliofiwa? Je, kuna tumaini lolote kwa wapendwa wetu waliokufa?
-
-
Je, Ni Vibaya Kuhuzunika Unapofiwa?Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 3
-
-
HABARI KUU | MTU UNAYEMPENDA ANAPOKUFA
Je, Ni Vibaya Kuhuzunika Unapofiwa?
Je, umewahi kuugua? Huenda ulipona haraka hivi kwamba hukumbuki tena hali ilivyokuwa. Huzuni haiwi hivyo. Daktari Alan Wolfelt alisema hivi katika kitabu chake Healing a Spouse’s Grieving Heart: “Uchungu unaotokana na huzuni hauishi.” Hata hivyo, anaongezea hivi: “Baada ya muda, huenda huzuni ikapungua ikiwa mtu atapata msaada wa kukabiliana na hali hiyo.”
Kwa mfano, fikiria jinsi mzee wa ukoo Abrahamu alivyotenda baada ya mke wake kufa. Biblia inasema kwamba “Abrahamu akaanza kuomboleza na kumlilia Sara.” Maneno ya awali “akaanza” yanaonyesha kwamba kwa muda fulani Abrahamu alikabiliana na huzuni ya kufiwa na mke wake.a Mfano mwingine ni wa Yakobo alipodanganywa kwamba mwana wake Yosefu aliuawa na mnyama-mwitu. Alihuzunika kwa “siku nyingi,” na watu wa familia yake walishindwa kumfariji. Miaka kadhaa baadaye, bado alikumbuka kifo cha Yosefu.—Mwanzo 23:2; 37:34, 35; 42:36; 45:28.
Abrahamu alihuzunika sana baada ya kifo cha mke wake mpendwa Sara
Leo pia watu wengi wanahuzunika kwa muda mrefu wanapofiwa na mtu wao wa karibu. Fikiria mifano hii miwili inayofuata.
“Mume wangu, Robert, alikufa Julai 9, 2008. Asubuhi aliyopata aksidenti mambo yalikuwa kama kawaida. Kama kawaida kabla hajaenda kazini baada ya kiamsha-kinywa, alinikumbatia, akanibusu na kuniambia ‘nakupenda.’ Hata baada ya miaka sita bado nina maumivu moyoni. Sidhani kama nitazoea kuishi bila Rob.”—Gail, mwenye miaka 60.
“Ijapokuwa mke wangu mpendwa alikufa miaka 18 iliyopita, bado mimi humkumbuka na kuhuzunika sana. Kila mara ninapoona ua au kitu chochote kinachovutia, mimi humkumbuka na kufikiria jinsi ambavyo angefurahia sana kuona kile ninachoona.”—Etienne, mwenye miaka 84.
Hivyo, ni jambo la kawaida kuwa na uchungu kwa muda mrefu. Watu huhuzunika kwa njia tofauti, hivyo si jambo la hekima kumhukumu mtu kutokana na jinsi anavyokabiliana na msiba. Wakati uleule, huenda tukahitaji kuepuka kujilaumu sana ikiwa tunahisi kwamba huzuni yetu imepita kiasi. Tunaweza kukabilianaje na huzuni?
a Isaka mwana wa Abrahamu alihuzunika pia kwa muda mrefu. Kama inavyotajwa katika makala “Igeni Imani Yao” iliyo katika gazeti hili, kwa miaka mitatu tangu mama yake afe, Isaka bado alikuwa akihuzunika.—Mwanzo 24:67.
-
-
Jinsi ya Kukabiliana na Huzuni ya KufiwaMnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 3
-
-
HABARI KUU | MTU UNAYEMPENDA ANAPOKUFA
Jinsi ya Kukabiliana na Huzuni ya Kufiwa
Kuna ushauri mwingi kuhusu jinsi ya kukabiliana na huzuni. Hata hivyo, si ushauri wote unaofaa. Kwa mfano, huenda wengine wakakushauri kwamba usilie au kuonyesha hisia zako kwa njia yoyote ile. Huenda wengine wakakusihi uonyeshe hisia zako zote. Biblia inatoa maoni yenye usawaziko kuhusu jambo hilo ambayo yanaungwa mkono na utafiti uliofanywa hivi karibuni.
Katika tamaduni fulani, ni aibu kwa mwanamume kulia. Lakini, je, kuna sababu yoyote ya msingi kuona aibu kulia mbele ya watu? Wataalamu wa akili wanakubali kwamba kulia ni njia ya kawaida ya kuonyesha huzuni. Huenda baada ya muda, kuhuzunika kukakusaidia kukabiliana na kifo cha mpendwa wako. Hata hivyo, kutohuzunika kunaweza kuwa na matokeo mabaya. Biblia haiungi mkono wazo la kwamba haifai wanaume kulia wanapohuzunika. Kwa mfano, mfikirie Yesu. Lazaro rafiki ya Yesu alipokufa, Yesu alilia hadharani hata ingawa alikuwa na uwezo wa kufufua wafu!—Yohana 11:33-35.
Kukasirika ni hali nyingine inayowapata wale wanaohuzunika hasa wanapofiwa ghafla na mtu wanayempenda. Kuna sababu nyingi zinazoweza kumfanya mtu anayehuzunika awe na hasira. Kwa mfano, huenda mtu anayeheshimiwa akasema maneno fulani bila kufikiri. Mike kutoka Afrika Kusini anasema hivi: “Baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miaka 14 tu. Tulipokuwa katika mazishi, mtumishi wa kanisa la Anglikana alisema kwamba Mungu huwachukua mapema watu wazuri kwa kuwa anawahitaji.a Maneno hayo yalinikasirisha sana kwa kuwa tulimhitaji sana baba yetu. Ingawa miaka 63 imepita, bado nina uchungu.”
Vipi kuhusu hisia za kujilaumu? Ikiwa ni kifo cha ghafla, yule aliyefiwa anaweza kuwaza hivi, ‘Huenda asingekufa ikiwa ningefanya jambo hili au lile.’ Au labda mligombana na mpendwa wako kabla hajafa. Jambo hilo linaweza kuongeza hisia za kujilaumu.
Ikiwa unajilaumu na kukasirika, jitahidi kutoficha hisia zako. Zungumza na rafiki atakayekusikiliza na kukuhakikishia kwamba watu wengi waliofiwa huhisi hivyo. Biblia inatukumbusha kwamba: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.
Yehova Mungu, Muumba wetu, anaweza kuwa Rafiki bora kwa yeyote aliyefiwa na mpendwa wake. Mmiminie moyo wako kupitia sala kwa sababu ‘anakujali.’ (1 Petro 5:7) Zaidi ya hayo, anaahidi kwamba “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote” itatuliza mawazo na hisia za wote wanaosali kwake. (Wafilipi 4:6, 7) Pia, mruhusu Mungu akusaidie kupitia Neno lake linalofariji, Biblia. Andika orodha ya maandiko yanayokufariji. (Tazama sanduku katika ukurasa huu.) Unaweza kukariri baadhi ya maandiko hayo. Kutafakari maandiko hayo kunaweza kukusaidia hasa usiku unapokuwa peke yako na unashindwa kupata usingizi.—Isaya 57:15.
Hivi karibuni, mwanamume mmoja mwenye umri wa miaka 40 ambaye tutamwita Jack, alifiwa na mke wake aliyeugua kansa. Jack anasema kwamba kuna wakati ambapo anahisi upweke sana. Lakini sala imemsaidia. Anasema, “Ninaposali kwa Yehova, sihisi upweke. Mara nyingi mimi huamka usiku na nyakati nyingine ninakosa usingizi mpaka asubuhi. Baada ya kusoma na kutafakari Maandiko yenye kufariji na kisha kumimina hisia za moyo wangu kupitia sala, ninahisi utulivu na amani kwa kiasi kikubwa hivi kwamba akili na moyo wangu hutulia na kuniwezesha kulala usingizi.”
Msichana anayeitwa Vanessa alifiwa na mama yake baada ya kuugua. Vanessa ameona nguvu ya sala. Anasema hivi: “Hali inapokuwa ngumu, mimi hutaja jina la Mungu na kuanza kulia. Yehova husikiliza sala zangu na mara zote hunipa msaada ninaohitaji.”
Watu wanaokabiliana na huzuni ya kufiwa hushauriwa kuwasaidia wengine au kujitolea katika kazi yoyote itakayonufaisha jamii. Kufanya hivyo kunaweza kuwapa shangwe na kupunguza huzuni yao. (Matendo 20:35) Wakristo wengi waliofiwa na wapendwa wao wamefarijika sana baada ya kuwasaidia wengine.—2 Wakorintho 1:3, 4.
a Hilo si fundisho la Biblia. Biblia inataja mambo matatu yanayosababisha kifo.—Mhubiri 9:11; Yohana 8:44; Waroma 5:12.
-
-
Kuwafariji WanaoombolezaMnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 3
-
-
HABARI KUU | MTU UNAYEMPENDA ANAPOKUFA
Kuwafariji Wanaoomboleza
Je, umewahi kuhisi hujui la kufanya ili kumsaidia mtu anayeomboleza baada ya kufiwa na mtu anayempenda? Wakati mwingine huenda tunahisi kwamba hatujui la kusema au kufanya hivyo tunaamua kukaa kimya na kutofanya lolote. Hata hivyo, kuna mambo tunayoweza kufanya ili kumsaidia aliyefiwa.
Mara nyingi unachohitaji kufanya ni kuwa pamoja na yule anayeomboleza na kumwambia maneno kama vile “pole sana.” Katika tamaduni nyingi, kumkumbatia mtu au kumshika mkono ni njia moja ya kumwonyesha kwamba unamjali. Mtu aliyefiwa na mpendwa wake anapoongea, msikilize kwa huruma. Zaidi ya yote, wasaidie waliofiwa kwa kufanya kazi za nyumbani kama vile kupika chakula, kutunza watoto, au kufanya mipango ya mazishi. Kumbuka kwamba maneno matupu hayavunji mfupa.
Baada ya muda, unaweza kuzungumzia sifa nzuri au mambo mazuri ambayo yule aliyekufa alifanya. Mazungumzo hayo yanaweza kumfariji mfiwa. Kwa mfano, Pam aliyefiwa na mume wake, Ian, miaka sita iliyopita, anasema hivi: “Mara nyingine watu hunieleza mambo mazuri aliyofanya Ian ambayo sikuyajua, na jambo hilo hunifanya nihisi vizuri.”
Kulingana na utafiti, wafiwa wengi hupewa misaada mingi wakati wa msiba na kisha kusahauliwa baada ya hapo kwa kuwa kila mtu anaendelea na maisha yake. Hivyo, jitahidi kuwasiliana na rafiki yako aliyefiwa kwa ukawaida.a Wafiwa wengi huthamini sana jambo hilo kwa kuwa wanapata nafasi ya kuzungumzia huzuni yao ya muda mrefu.
Mfikirie Kaori, mwanamke Mjapani aliyehuzunika sana baada ya kufiwa na mama yake na kisha miezi 15 baadaye, akafiwa na dada yake. Jambo la kupendeza ni kwamba rafiki zake wa karibu waliendelea kumsaidia. Ritsuko ambaye ana umri mkubwa kuliko Kaori aliamua kuwa rafiki yake wa karibu. Kaori anasema hivi: “Kusema kweli, sikufurahia jambo hilo. Sikutaka mtu mwingine achukue nafasi ya mama yangu, na sikufikiria kwamba kuna mtu angeweza kuwa kama mama. Hata hivyo, kwa sababu ya jinsi Mama Ritsuko alivyonitendea, nilianza kumpenda. Kila juma tulihubiri na kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja. Alinialika tunywe chai pamoja, aliniletea vyakula, na mara nyingi aliniandikia barua na kadi. Mtazamo mzuri wa Mama Ritsuko ulinisaidia sana.”
Miaka kumi na mbili imepita tangu mama yake Kaori alipokufa na sasa Kaori na mume wake ni waeneza injili wa wakati wote. Kaori anasema: “Mama Ritsuko anaendelea kunihangaikia. Ninaporudi kwetu, mara zote ninamtembelea na ninafurahia kuwa pamoja naye.”
Mtu mwingine aliyenufaika kwa kuendelea kusaidiwa na watu wake wa karibu ni Poli ambaye ni Shahidi wa Yehova kutoka Cyprus. Sozos, mume wa Poli, alikuwa mwenye fadhili na aliweka mfano mzuri akiwa mchungaji Mkristo kwa kuwakaribisha mayatima na wajane nyumbani kwao ili kushirikiana na kula pamoja nao. (Yakobo 1:27) Inasikitisha kwamba Sozos alikufa akiwa na umri wa miaka 53, baada ya kuugua kansa ya ubongo. Poli anasema: “Nilifiwa na mume wangu mshikamanifu niliyekuwa nimeishi naye kwa miaka 33.”
Tafuta njia nzuri za kumsaidia mfiwa
Baada ya mazishi, Poli na mtoto wake mwenye umri wa miaka 15 anayeitwa Daniel, walihamia nchini Kanada. Wakiwa huko walianza kushirikiana na kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Poli anasema: “Rafiki zangu katika kutaniko jipya hawakujua lolote kuhusu maisha yetu ya awali na hali ngumu tulizokabili. Hata hivyo, hilo halikuwazuia kututia moyo kwa maneno yanayofariji na kutusaidia. Msaada huo ulikuwa muhimu kwa mwana wangu hasa katika kipindi hicho ambacho alihitaji kuwa karibu sana na baba yake! Wale wanaosimamia mambo katika kutaniko walimjali sana Daniel. Mmoja wao alihakikisha kwamba lazima Daniel awepo kila mara alipoalika marafiki au walipoenda kucheza mpira.” Kwa sasa Poli na Daniel wanaendelea vizuri.
Ni kweli kwamba kuna njia nyingi za kutoa msaada na kuwafariji wanaoomboleza. Biblia hutufariji kwa kutoa tumaini zuri la wakati ujao.
a Wengine wametia alama tarehe ya kifo cha mpendwa wa rafiki au mshiriki wa familia katika kalenda ili wakumbuke kutoa faraja inapohitajika zaidi, yaani, katika tarehe hiyo au karibu wakati huo.
-
-
Wafu Wataishi Tena!Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 3
-
-
HABARI KUU | MTU UNAYEMPENDA ANAPOKUFA
Wafu Wataishi Tena!
Huenda unakumbuka kwamba Gail, aliyetajwa mwanzoni mwa mfululizo huu, alikuwa na mashaka kama angeweza kukabiliana na huzuni ya kifo cha mume wake, Rob. Hata hivyo, anatarajia kumuona tena Rob katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Anasema,“andiko ninalopenda sana ni Ufunuo 21:3, 4.” Linasema hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”
Gail anasema hivi: “Ahadi hiyo inafariji sana. Ninawasikitikia sana watu waliofiwa ambao hawajui lolote kuhusu tumaini hili la kuwaona tena wapendwa wao.” Gail anatenda kulingana na imani yake kwa kujitolea kueneza injili wakati wote, akiwahubiria jirani zake kuhusu ahadi za Mungu za wakati ujao ambapo “kifo hakitakuwapo tena.”
Ayubu alikuwa na uhakika kwamba ataishi tena
Huenda ukasema ‘Haiwezekani!’ Lakini fikiria mfano wa mwanaume aliyeitwa Ayubu. Alikuwa na ugonjwa mbaya sana. (Ayubu 2:7) Ingawa Ayubu alitamani kufa, bado aliamini kwamba Mungu ana uwezo wa kumfufua ili aishi tena duniani. Alisema hivi kwa uhakika: “Laiti ungenificha katika Kaburi . . . Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:13, 15) Ayubu alikuwa na uhakika kwamba Mungu wake hangemsahau na angetamani kumfufua.
Hivi karibuni, Mungu atamfufua Ayubu pamoja na watu wengine wengi wakati dunia hii itakapogeuzwa kuwa paradiso. (Luka 23:42, 43) Biblia inatuhakikishia hivi katika andiko la Matendo 24:15, “Kutakuwa na ufufuo.” Pia, Yesu alisema hivi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Ayubu ataona ahadi hiyo ikitimizwa. Atarudia “nguvu za ujana wake” na mwili wake utakuwa “laini kuliko wakati wa ujana.” (Ayubu 33:24, 25) Wale wote watakaopata kibali cha Mungu watafurahia jambo hilo watakapofufuliwa ili waishi duniani.
Ikiwa umefiwa na mtu unayempenda, huenda mambo tuliyozungumzia yasiondoe moja kwa moja huzuni yako. Hata hivyo, ukitafakari ahadi za Mungu zinazopatikana katika Biblia, utapata tumaini la kweli na nguvu za kuvumilia.—1 Wathesalonike 4:13.
Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na huzuni? Au je, una maswali mengine, kama vile “Kwa nini Mungu ameruhusu uovu na mateso?” Tafadhali tembelea tovuti yetu ya jw.org/sw ili uone jinsi Biblia inavyotoa majibu yanayofariji.
-