Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tunahitaji Faraja
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 5
    • HABARI KUU | UNAWEZA KUPATA WAPI FARAJA?

      Tunahitaji Faraja

      Mama akimfariji mtoto wake

      Je, unakumbuka ulipoanguka ukiwa mtoto? Huenda uliumia mkono au mguu. Je, unakumbuka jinsi ambavyo mama alikufariji? Labda, alisafisha kidonda na kisha kukifunga kwa bendeji. Ingawa ulilia, ulihisi nafuu alipokukumbatia na kukufariji. Wakati huo, ilikuwa rahisi kupata mtu wa kukufariji.

      Hata hivyo, kadiri tunavyoendelea kukua tunakabili changamoto zaidi maishani. Matatizo yanakuwa mengi, na inakuwa vigumu kupata faraja. Inasikitisha kwamba matatizo ambayo watu wazima hukabili hayawezi kwisha kwa kufungwa bendeji au kukumbatiwa. Fikiria mifano kadhaa.

      • Je, umewahi kupata mkazo kwa sababu ya kupoteza kazi? Julian anasema kwamba alipata mkazo baada ya kufutwa kazi. Aliwaza hivi, ‘Nitawezaje kuitunza familia yangu? Kwa nini kampuni imeniachisha kazi ingawa nimekuwa mfanyakazi mzuri kwa miaka mingi?’

      • Huenda unakabili changamoto kwa sababu ya kuvunjika kwa ndoa yako. Raquel anasema hivi: “Nilihuzunika sana, mume wangu aliponiacha miezi 18 iliyopita. Nilivunjika moyo sana. Niliumia kimwili na kihisia pia. Hilo liliniogopesha sana.”

      • Huenda una ugonjwa wa kudumu. Labda nyakati fulani unahisi kama Ayubu ambaye alisema hivi kwa uchungu: “Nimekataa huo; sitaishi mpaka wakati usio na kipimo.” (Ayubu 7:16) Huenda ukakubaliana na maoni ya Luis, mwanamume mwenye umri wa miaka 80 hivi aliyesema, “Nyakati nyingine mimi huhisi kana kwamba ninangojea kufa tu.”

      • Au huenda unatamani kufarijiwa kwa sababu umefiwa na mtu unayempenda. Robert anasema: “Mwanzoni sikuamini nilipopata habari kwamba mwanangu amekufa katika aksidenti ya ndege. Kisha niliumia sana, maumivu ambayo Biblia huyafananisha na upanga mrefu unaochoma nafsi.”—Luka 2:35.

      Licha ya hali hizo ngumu, Robert, Luis, Raquel, na Julian wamepata faraja. Wamepata Yule anayeweza kuwafariji, yaani, Mungu Mwenye enzi kuu ambaye ni chanzo cha faraja. Mungu huandaa faraja jinsi gani? Je, anaweza kukufariji?

  • Jinsi Mungu Anavyotufariji
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 5
    • Yesu akimgusa mtu mwenye ukoma kabla ya kumponya

      HABARI KUU | UNAWEZA KUPATA WAPI FARAJA?

      Jinsi Mungu Anavyotufariji

      Mtume Paulo alisema kwamba Yehovaa ni “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Hivyo, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu anaweza kutusaidia na kwamba Baba yetu wa mbinguni atatufariji chini ya hali yoyote.

      Bila shaka, ni lazima tufanye jambo fulani ikiwa tunataka Mungu atufariji. Je, daktari anaweza kumtibu mgonjwa ikiwa hajaenda kupata matibabu? Nabii Amosi aliuliza hivi: “Je, watu wawili watatembea pamoja isipokuwa wawe wamekutana kwa mapatano?” (Amosi 3:3) Hivyo, Maandiko yanatuhimiza hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

      Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Mungu atatukaribia? Kwanza kabisa, mara kwa mara yeye hutuambia kwamba anataka kutusaidia. (Ona sanduku.) Pili, kwa sababu tuna ushahidi kutoka kwa watu walioishi nyakati za kale na leo pia ambao wamefarijiwa na Mungu.

      Leo watu wengi hutafuta msaada kutoka kwa Mungu, kama Mfalme Daudi alivyofanya alipokabili matatizo maishani. Wakati fulani, alimwomba Yehova hivi: “Uisikie sauti ya kusihi kwangu ninapokulilia unisaidie.” Je, Mungu alimjibu? Ndiyo. Daudi aliongezea hivi: “Nami nimesaidiwa, hivi kwamba moyo wangu unashangilia.”—Zaburi 28:2, 7.

      JUKUMU LA YESU LA KUWAFARIJI WOTE WANAOOMBOLEZA

      Mungu amempa Yesu jukumu muhimu la kuwafariji watu. Miongoni mwa kazi ambazo Mungu alimpa Yesu ni “kufunga majeraha ya waliovunjika moyo” na “kuwafariji wote wanaoomboleza.” (Isaya 61:1, 2) Kama ilivyotabiriwa, Yesu aliwahangaikia sana ‘wote waliotaabika na kulemewa na mizigo.’—Mathayo 11:28-30.

      Yesu aliwafariji watu kwa kuwapa ushauri wenye hekima, kuwatendea kwa fadhili, na wakati mwingine kuwaponya. Siku moja mtu mwenye ukoma alimsihi Yesu hivi: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu akamsikitikia na kumjibu: “Ninataka. Takasika.” (Marko 1:40, 41) Yule mtu mwenye ukoma akapona.

      Leo, Mwana wa Mungu hayuko duniani ili kutufariji moja kwa moja. Hata hivyo, Yehova, “Mungu wa faraja yote,” anaendelea kuwafariji wale walio na uhitaji. (2 Wakorintho 1:3) Fikiria njia nne ambazo Mungu hutumia kuwafariji watu.

      • Biblia. “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.”—Waroma 15:4.

      • Roho Takatifu ya Mungu. Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu, kutaniko lote la Kikristo liliingia katika kipindi cha amani. Kwa nini? Kwa sababu ‘lilitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu.’ (Matendo 9:31) Roho takatifu ya Mungu, yaani, nguvu yake ya utendaji, ina nguvu nyingi. Mungu anaweza kuitumia kumfariji mtu yeyote katika hali yoyote.

      • Sala. Biblia inatushauri hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote.” Kisha inaongeza, “maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

      • Wakristo Wenzetu wanaweza kuwa marafiki wa kweli na kutufariji tunapopatwa na matatizo. Mtume Paulo alieleza kwamba waandamani wake walikuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ katika ‘uhitaji na dhiki.’—Wakolosai 4:11; 1 Wathesalonike 3:7.

      Mashahidi wa Yehova wakimfariji Mkristo mwenzao

      Hata hivyo, huenda ukajiuliza ikiwa kweli mambo hayo yanaweza kukusaidia. Hebu tuchunguze watu ambao walikabili matatizo yaliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Kama wao, utatambua kwamba Mungu anaendelea kutimiza ahadi hii yenye kutia moyo: “Kama vile mtu ambaye mama yake mwenyewe anaendelea kumfariji, ndivyo mimi nitakavyoendelea kuwafariji ninyi.”—Isaya 66:13.

      a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.

      Jinsi Tunavyojua Kwamba Mungu Anapenda Kutufariji

      • “Wewe mwenyewe, Ee Yehova, umenisaidia na kunifariji.”​—Zaburi 86:17.

      • “‘Wafarijini, wafarijini watu wangu,’ asema Mungu wenu.”​—Isaya 40:1.

      • “Yehova amesema hivi: . . . ‘Kama vile mtu ambaye mama yake mwenyewe anaendelea kumfariji, ndivyo mimi nitakavyoendelea kuwafariji ninyi.’”​—Isaya 66:12, 13.

      • “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.”​—Mathayo 5:4.

      • ‘Mtupieni [Mungu] mahangaiko yenu yote, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’​—1 Petro 5:7.

  • Faraja Wakati wa Matatizo
    Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 5
    • HABARI KUU | UNAWEZA KUPATA WAPI FARAJA?

      Faraja Wakati Wa Matatizo

      Kuna aina mbalimbali za matatizo. Ni kweli kwamba hatuwezi kuzungumzia matatizo yote ambayo wanadamu hukabili, hata hivyo, tutazungumzia mifano minne iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Chunguza jinsi watu waliokabili matatizo ya aina mbalimbali walivyopata faraja ya kweli kutoka kwa Mungu.

      UNAPOKOSA AJIRA

      Jonathan akisafisha dirisha la kioo

      “Nilijifunza kukubali kazi za aina mbalimbali, na tuliepuka matumizi yasiyo ya lazima.”​—Jonathan

      Setha anakumbuka hivi: “Mimi na mke wangu tuliachishwa kazi wakati mmoja. Kwa miaka miwili tulitegemea msaada kutoka kwa familia na kufanya vibarua. Kwa sababu hiyo mke wangu, Priscilla, alishuka moyo nami nilijihisi sifai.

      “Tulikabilianaje na hali hiyo? Priscilla alikumbuka kwa kawaida maneno ya Yesu yaliyo katika Mathayo 6:34. Yesu alisema tusihangaike juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Pia, sala za kutoka moyoni zilimsaidia asonge mbele. Kwa upande wangu, andiko la Zaburi 55:22 lilinifariji. Kama mtunga zaburi, nilimtupia Yehova mahangaiko yangu, naye alinitegemeza. Ingawa nimepata kazi, tunajitahidi kuishi maisha rahisi kulingana na shauri la Yesu katika Mathayo 6:20-22. Zaidi ya yote, tumemkaribia Mungu zaidi na tumekuwa na uhusiano wa karibu.”

      Jonathan anaeleza hivi: “Biashara ya familia yetu ilipofilisika, nilihofia sana wakati ujao. Kuporomoka kwa uchumi kulisababisha biashara yetu iliyodumu kwa miaka 20 kufilisika. Tulianza kugombana na mke wangu kwa sababu ya pesa. Tuliogopa kununua vitu kwa kutumia kadi ya benki kwa kuhofia kwamba wauzaji wangeikataa.

      “Hata hivyo, Neno la Mungu na roho yake vilitusaidia kufanya maamuzi yanayofaa. Nilijifunza kukubali kazi za aina mbalimbali, na tuliepuka matumizi yasiyo ya lazima. Pia, Mashahidi wa Yehova wenzetu walitupatia msaada. Walitusaidia kuendelea kujiheshimu na hali zilipokuwa ngumu walitupatia msaada.”

      NDOA INAPOVUNJIKA

      Raquel anakumbuka: “Mume wangu aliponiacha ghafla, nilikasirika na kuumia. Nililemewa na huzuni nyingi. Hata hivyo, nilimkaribia Mungu, naye akanifariji. Kusali kila siku kulinisaidia kuwa na amani ya Mungu ambayo ililinda moyo wangu. Kwa kweli, Mungu aliuponya moyo wangu uliovunjika.

      “Pia, ninashukuru kwa sababu Neno lake Biblia, limenisaidia kudhibiti hasira na kuondoa kinyongo. Nilitafakari maneno ya mtume Paulo yaliyo katika Waroma 12:21: ‘Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.’

      Raquel akimsomea mtu andiko

      “Kuna wakati wa ‘kuacha kutafuta kilichopotea.’ . . . Sasa, nina malengo mapya maishani.”​—Raquel

      “Rafiki yangu mmoja alinieleza kuhusu umuhimu wa kuendelea na maisha. Alinisomea Mhubiri 3:6 na kwa fadhili akaniambia kwamba kuna wakati wa ‘kuacha kutafuta kilichopotea.’ Huo ulikuwa ushauri wenye kuumiza, lakini ulinifaa. Sasa nina malengo mapya maishani.”

      Elizabeth anasema: “Ndoa inapovunjika, unahitaji msaada wa kihisia. Nilikuwa na rafiki wa karibu ambaye kila siku alinisaidia kihisia. Alilia pamoja nami, alinifariji, na kunisaidia nijihisi kwamba ninapendwa na sijapuuzwa. Nina uhakika kwamba Yehova alimtumia ili kunisaidia kupona maumivu yangu ya kihisia.”

      UGONJWA NA UZEE

      Luis husali ili kuimarishwa na Mungu

      “Baada ya kusali kwa Mungu, mimi huhisi kwamba roho yake imenitia nguvu.”​—Luis

      Luis aliyetajwa katika makala ya kwanza ya gazeti hili, ana tatizo kubwa la moyo, na amenusurika kufa mara mbili. Kwa sasa, anahitaji kutumia kifaa cha kumsaidia kupumua kwa saa 16 kila siku. Luis anasema hivi: “Mimi husali kwa Yehova kwa ukawaida. Baada ya kusali kwa Mungu, mimi huhisi kwamba roho yake imenitia nguvu. Sala hunipa ujasiri wa kuendelea kuishi kwa sababu ninamwamini Mungu na ninajua kwamba ananijali.”

      Petra mwenye umri wa miaka 80 hivi anasema: “Ningependa kufanya mambo mengi, lakini hali yangu hainiruhusu. Kadiri nguvu zinavyoendelea kupungua mimi hujihisi vibaya. Ninajiona kuwa dhaifu na ninalazimika kutumia dawa kwa ukawaida. Mara nyingi mimi hukumbuka jinsi Yesu alivyomwomba Baba yake amwondolee tatizo fulani ikiwa ingewezekana. Hata hivyo, Yehova alimwimarisha Yesu, na huniimarisha mimi pia. Kusali kila siku huniimarisha sana. Baada ya kuzungumza na Yehova, mimi hujihisi vizuri sana.”—Mathayo 26:39.

      Julian ambaye ameugua ugonjwa wa mfumo wa neva kwa karibu miaka 30 anahisi hivyo pia. Anasema hivi: “Nimeacha cheo changu na sasa ninatumia kiti chenye magurudumu. Hata hivyo, maisha yangu yana kusudi kwa sababu ninawasaidia wengine. Kutoa kunaweza kupunguza mkazo, na Yehova hututia nguvu wakati wa shida kama anavyoahidi. Kama mtume Paulo, ninaweza kusema hivi kwa hakika: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.’”—Wafilipi 4:13.

      TUNAPOFIWA

      Antonio anakumbuka hivi: “Mwanzoni sikuamini nilipopata taarifa kwamba baba yangu amekufa katika aksidenti ya barabarani. Hakupaswa kufa, kwa kuwa alikuwa mpita njia tu. Hata hivyo, singeweza kufanya jambo lolote. Kabla ya kufa alilazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kwa siku tano. Nilijidhibiti ili nisilie mbele ya mama yangu, lakini nilipokuwa peke yangu nililia kwa uchungu. Mara kwa mara nilijiuliza ‘Kwa nini?’

      “Katika kipindi hicho kigumu, niliendelea kumwomba Yehova anisaidie kudhibiti hisia zangu na kuwa na amani ya akili. Pole kwa pole nilihisi utulivu. Nilikumbuka kwamba Biblia husema ‘tukio lisilotazamiwa’ linaweza kumpata yeyote. Kwa kuwa Mungu hasemi uwongo, nina uhakika kwamba nitamwona baba yangu atakapofufuliwa.”—Mhubiri 9:11; Yohana 11:25; Tito 1:2.

      Robert na mke wake wakitazama albamu ya picha

      “Ingawa aksidenti hiyo ya ndege ilisababisha kifo cha mtoto wetu, tuna kumbukumbu za mambo mengi mazuri tuliyofurahia pamoja.”​—Robert

      Robert, aliyetajwa katika makala ya kwanza ana maoni kama hayo. Anasema: “Kwa sababu ya kusali kwa Yehova, mimi na mke wangu tumepata amani ya akili inayotajwa katika Wafilipi 4:6, 7. Amani hiyo ya akili ilitusaidia kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu tumaini letu la ufufuo. Ingawa aksidenti hiyo ya ndege ilisababisha kifo cha mtoto wetu, tuna kumbukumbu za mambo mengi mazuri tuliyofurahia pamoja. Sisi huzithamini kumbukumbu hizo.

      “Mashahidi wenzetu walipotueleza kwamba walituona katika televisheni tukieleza kuhusu imani yetu kwa utulivu, tuliwaambia kwamba hilo lilitokana na sala nyingi zilizotolewa kwa niaba yetu. Ninaamini kwamba Yehova alituimarisha kupitia jumbe nyingi za faraja walizotutumia.”

      Mifano hiyo inaonyesha kwamba Mungu anaweza kuandaa faraja kwa watu wanaokabili matatizo na changamoto mbalimbali. Namna gani wewe? Hata iwe unakabili tatizo gani maishani, unaweza kupata faraja.b Mwombe Yehova akusaidie. Yeye ni “Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3.

      a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

      b Ikiwa ungependa kumkaribia Mungu na kupata faraja, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu au utume barua katika ofisi ya tawi iliyo karibu nawe.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki