-
Usikate Tamaa!Amkeni!—2014 | Aprili
-
-
HABARI KUU
Usikate Tamaa!
IKIWA ungekutana na Dianaa ungeona jinsi alivyo msichana mwenye urafiki, mwenye akili, na mchangamfu. Hata hivyo, licha ya kuonekana mwenye furaha na urafiki, mara nyingi Diana huwa amevunjika moyo. Anasema: “Kila siku mimi hutamani kufa. Ninaamini kabisa kwamba ulimwengu haunihitaji.”
“Uchunguzi fulani umeonyesha kwamba kwa kila mtu anayejiua, wengine 200 wamejaribu kujiua na wengine 400 wamefikiria kujiua.”—JARIDA LA THE GAZETTE, MONTREAL, KANADA.
Diana anasema kwamba hawezi kujiua. Hata hivyo, mara nyingine haoni sababu ya kuendelea kuishi. Anasema: “Jambo ninalotamani zaidi ni kufa katika aksidenti. Nimekuja kuona kifo kama rafiki badala ya adui.”
Watu wengi wanaweza kuelewa hisia za Diana na wengine wao wamefikiria au hata wamejaribu kujiua. Hata hivyo, wataalamu husema kwamba, lengo la wengi wanaojaribu kujiua si kukomesha maisha yao bali ni kukomesha mateso yanayowapata. Kwa ufupi, wanaamini kwamba wana sababu nzuri ya kufa, wanachohitaji ni sababu ya kuendelea kuishi.
Usikate tamaa! Chunguza sababu tatu za kuendelea kuishi.
a Jina limebadilishwa.
-
-
Kwa Sababu Mambo HubadilikaAmkeni!—2014 | Aprili
-
-
HABARI KUU | USIKATE TAMAA!
1 Kwa Sababu Mambo Hubadilika
“Tunakazwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa.”—2 WAKORINTHO 4:8.
Kujiua kumeitwa “suluhisho la kudumu la tatizo la muda mfupi.” Ingawa huenda ikawa vigumu kuamini, hali yenye kufadhaisha hata ile unayohisi imepita uwezo wako ni ya muda tu. Kwa kweli inaweza kubadilika na kuwa bora kwa njia isiyotazamiwa.—Ona sanduku “Hali Zao Zilibadilika.”
Hata hali isipobadilika, ni vizuri kushughulikia tatizo moja baada ya lingine. Yesu alisema, “Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.”—Mathayo 6:34.
Utafanya nini ikiwa hali yako haiwezi kubadilika? Kwa mfano, labda una ugonjwa wa kudumu. Au labda umekata tamaa kwa sababu ya kuvunjika kwa ndoa au umefiwa na mtu unayempenda.
Hata katika hali kama hizo, bado kuna jambo unaloweza kubadili: maoni yako kuhusu hali hiyo. Unapokubali kwamba kuna mambo usiyoweza kubadili, inakuwa rahisi zaidi kuwa na maoni yanayofaa. (Methali 15:15) Pia, itakuwa rahisi zaidi kwako kuvumilia hali ngumu badala ya kuona kifo kama suluhisho. Matokeo ni nini? Utaanza kudhibiti maoni yako kuhusu hali ambayo inaonekana kwamba imepita uwezo wako.—Ayubu 2:10.
KUMBUKA: Huwezi kupanda mlima kwa hatua moja tu, lakini unaweza kuupanda hatua kwa hatua. Ndivyo unavyoweza kukabiliana na matatizo, hata yakiwa makubwa kama mlima.
UNACHOWEZA KUFANYA SASA: Zungumza na mtu fulani, labda rafiki au mtu wa familia kuhusu hali yako. Huenda mtu huyo akakusaidia kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu hali yako.—Methali 11:14.
-
-
Kwa Sababu Kuna MsaadaAmkeni!—2014 | Aprili
-
-
HABARI KUU | USIKATE TAMAA!
2 Kwa Sababu Kuna Msaada
“[Mtupieni Mungu] mahangaiko yenu yote . . . , kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 PETRO 5:7.
Kifo kinaweza kuonekana kuwa bora kuliko kuishi unapohisi huwezi kubadili hali yako. Hata hivyo, hebu fikiria mambo yafuatayo ambayo yanaweza kukusaidia.
Sala. Kusali si njia ya kukufanya uhisi vizuri tu wala si jambo tunalofanya tunapokata tamaa. Ni mawasiliano halisi kati yako na Yehova Mungu, ambaye anakujali. Yehova anataka umweleze mambo yanayokuhangaisha. Kwa hakika, Biblia inatuhimiza hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.”—Zaburi 55:22.
Kwa nini usizungumze na Mungu katika sala leo? Tumia jina lake, Yehova, na umweleze yaliyo moyoni mwako. (Zaburi 62:8) Yehova anataka uwe rafiki yake. (Isaya 55:6; Yakobo 2:23) Sala ni njia ya mawasiliano unayoweza kutumia wakati wowote na mahali popote.
Kulingana na uchunguzi wa Shirika la Marekani la Kuzuia Kujiua, “utafiti umeonyesha kwamba idadi kubwa ya watu waliojiua, yaani, asilimia 90 au zaidi, walikuwa na ugonjwa wa kiakili walipojiua. Hata hivyo, mara nyingi ugonjwa huo haukutambuliwa, haukupimwa, au kutibiwa ifaavyo”
Watu wanaokujali. Uhai wako ni muhimu kwa wengine kutia ndani watu wa familia yako au marafiki ambao huenda tayari wameonyesha kwamba wanakujali. Watu wanaokujali wanatia ndani watu ambao hujawahi kuwaona. Kwa mfano, katika utumishi wao, mara nyingine Mashahidi wa Yehova hukutana na watu waliofadhaika, na baadhi ya watu hao wamekiri kwamba walihitaji sana msaada na walikuwa wamefikiria kujiua. Kuhubiri nyumba kwa nyumba kumewapa Mashahidi wa Yehova nafasi ya pekee ya kuwasaidia watu kama hao. Mashahidi wa Yehova wanamwiga Yesu kwa kuwajali wanadamu wenzao. Wanakujali wewe pia.
—Yohana 13:35.
Msaada wa wataalamu. Mawazo ya kujiua mara nyingi huletwa na ugonjwa wa kubadilika kwa hisia kama vile kushuka moyo. Hupaswi kuaibika iwapo una ugonjwa wa kihisia kwani ni sawa tu na ugonjwa mwingine. Kwa kweli kushuka moyo kumeitwa “homa ya akili.” Mtu yeyote anaweza kupatwa na ugonjwa huo na unaweza kutibiwa.a
KUMBUKA: Kwa kawaida, huwezi kupambana peke yako na ugonjwa wa kushuka moyo. Hata hivyo, unaweza kufaulu ikiwa utasaidiwa.
UNACHOWEZA KUFANYA SASA: Tafuta daktari anayetegemeka ambaye hutibu magonjwa ya kihisia kama vile kushuka moyo.
a Ikiwa unalemewa na mawazo ya kujiua au hayaishi, tafuta msaada labda kwa kupiga simu kwenye kituo cha kutoa msaada au kwenye idara ya hospitali inayoshughulikia hali za dharura. Utapata wataalamu wanaoweza kukusaidia.
-
-
Kwa Sababu Kuna TumainiAmkeni!—2014 | Aprili
-
-
HABARI KUU | USIKATE TAMAA!
3 Kwa Sababu Kuna Tumaini
“Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” —ZABURI 37:11.
Biblia inakiri kwamba maisha ya mwanadamu ni “mafupi na yenye kujaa msukosuko.” (Ayubu 14:1) Leo, sote hupatwa na misiba mbalimbali. Lakini watu wengine huhisi wametamaushwa kabisa na maisha, kana kwamba hakuna tumaini lolote la wakati ujao. Je, unahisi hivyo? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba Biblia inatoa tumaini la kweli kwa ajili yako na wanadamu wote. Kwa mfano:
Biblia inafundisha kwamba Yehova Mungu alitaka tuwe na maisha bora.—Mwanzo 1:28.
Yehova Mungu anaahidi kuifanya dunia yetu iwe paradiso.—Isaya 65:21-25.
Bila shaka, ahadi hiyo itatimizwa. Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linasema:
“Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”
Tumaini hilo si ndoto tu. Yehova Mungu amekusudia kulitimiza, naye ana nguvu na nia ya kufanya hivyo. Tumaini la Biblia ni lenye kutegemeka na linakufariji ili “Usikate tamaa!”
KUMBUKA: Ingawa hisia zako zinaweza kubadilika-badilika kama mashua iliyo kwenye bahari yenye msukosuko, tumaini lililo katika Biblia linaweza kuwa kama nanga inayokuimarisha.
UNACHOWEZA KUFANYA SASA: Chunguza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu tumaini la kweli la wakati ujao. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia. Unaweza kuwasiliana nao katika eneo lenu au upate habari muhimu katika Tovuti yao ya jw.org/sw.a
a Pendekezo: Tembelea jw.org/sw na utafute sehemu ya MACHAPISHO >
MAKTABA KWENYE MTANDAO. Ukiwa hapo tafuta maneno kama vile “kushuka moyo” au “kujiua” ili upate msaada zaidi.
-