-
Uchungu wa KufiwaAmkeni!—2018 | Na. 3
-
-
KUKABILIANA NA HUZUNI YA KUFIWA
Uchungu Wa Kufiwa
“Baada ya miaka zaidi ya 39 ya ndoa, mke wangu, Sophia,a aliugua kwa muda mrefu na hatimaye akafa. Rafiki zangu walinitegemeza sana, na nilijishughulisha na mambo mengi ili kuondoa mawazo. Lakini kwa mwaka mzima, nilihisi uchungu usioelezeka. Hisia zangu zilikuwa zikipanda na kushuka, na sikuweza kuzidhibiti. Na hata sasa, ingawa miaka mitatu hivi imepita tangu alipokufa, bado nyakati fulani huwa ninapata hisia kali za uchungu, na mara nyingi huwa zinakuja wakati nisiotarajia.”—Kostas.
Je, umefiwa na mtu unayempenda? Ikiwa ndivyo, basi unaelewa hali ya Kostas. Kuna mambo machache sana yanayoweza kutokeza uchungu mwingi kama ule unaotokana na kufiwa na mwenzi wa ndoa, mtu wa ukoo, au rafiki wa karibu. Makala iliyochapishwa na jarida fulani (The American Journal of Psychiatry) inasema kwamba “kifo hufanya tuhisi waziwazi kwamba tumempoteza kabisa mtu tunayempenda, wazo linaloleta uchungu mwingi sana.” Baada ya kufiwa, huenda mtu akajiuliza: ‘Nitahisi uchungu huu hadi lini? Kweli nitawahi kuwa na furaha tena? Ni nini kitanisaidia kupunguza huzuni niliyo nayo?’
Toleo hili la Amkeni! litajibu maswali hayo. Makala inayofuata itazungumzia hali unazoweza kutazamia baada ya kufiwa. Halafu tutachunguza mambo yanayoweza kukusaidia kupunguza huzuni ya kufiwa.
Tunatumaini kwamba makala hizo zitawafariji wote waliofiwa na kuwasaidia wakabiliane na uchungu walio nao.
a Baadhi ya majina katika makala za toleo hili yamebadilishwa.
-
-
Hali Unazoweza KutazamiaAmkeni!—2018 | Na. 3
-
-
KUKABILIANA NA HUZUNI YA KUFIWA
Hali Unazoweza Kutazamia
Ingawa baadhi ya wataalamu husema kwamba watu waliofiwa hupitia hali fulani hususa zinazofuatana, ukweli ni kuwa kila mtu huomboleza kwa njia yake. Je, tofauti hizo zinamaanisha kwamba wengine hawahuzunishwi sana na msiba au wanazuia hisia zao? Inategemea. Ingawa kueleza na kuonyesha hisia zetu tunapofiwa kunaweza kusaidia kupunguza uchungu, hakuna njia moja hususa ya kuomboleza. Huzuni anayoonyesha mtu itategemea utamaduni, utu, mambo ambayo amepitia maishani, na jinsi kifo kilivyotokea.
HALI ITAKUWA MBAYA KADIRI GANI?
Huenda watu waliofiwa wasijue kihususa watapitia hali gani. Hata hivyo, kuna hisia na changamoto ambazo kwa kawaida hutokea baada ya mtu kufiwa. Acheni tuchunguze baadhi ya hali hizo.
Kulemewa sana na hisia. Huenda mtu aliyefiwa akalia sana, akatamani sana kumwona tena mpendwa wake, na hisia zake zikawa zikibadilika-badilika. Hisia hizo zinaweza kuzidi anapoota au kumkumbuka mpendwa wake. Hata hivyo, mwanzoni watu wengi hushtuka na huwa hawaamini kilichotokea. Tiina anaeleza jinsi alivyohisi mume wake, Timo, alipokufa ghafla: “Mwanzoni nilishtuka kiasi kwamba sikuhisi chochote. Nilishindwa hata kulia. Nililemewa sana na hisia hivi kwamba wakati mwingine nilishindwa kupumua. Sikuamini kabisa kile kilichokuwa kimetokea.”
Ni kawaida pia kuwa na wasiwasi mwingi, hasira, na kuhisi hatia. Ivan anasema: “Baada ya kifo cha Eric, mwana wetu mwenye umri wa miaka 24, mimi na mke wangu Yolanda, tulikuwa wenye hasira sana kwa kipindi fulani! Hilo lilitushangaza, kwa sababu kabla ya hapo hatukujiona kuwa watu wenye hasira. Pia tulihisi tukiwa na hatia kwa sababu tulifikiri huenda hatukufanya yote tuliyoweza ili kumsaidia mwana wetu.” Alejandro, ambaye mke wake alikufa baada ya kuugua kwa muda mrefu, alihisi akiwa na hatia pia. Anasema: “Mwanzoni nilihisi kwamba ikiwa Mungu anaruhusu niteseke kiasi hiki, basi mimi ni mtu mbaya. Kisha nikaanza kuhisi hatia kwa sababu ni kana kwamba nilikuwa nikimlaumu Mungu kwa mambo yaliyotokea.” Na Kostas, aliyetajwa kwenye makala iliyotangulia, anasema: “Mara kadhaa nilimkasirikia Sophia kwa sababu ya kuniacha. Kisha nilihisi hatia. Kwa kweli, yeye si wa kulaumiwa.”
Fikira zinazohangaisha. Nyakati fulani huenda mtu akawa na mawazo yanayohangaisha yanayojitokeza ghafla. Kwa mfano, mtu aliyefiwa huenda akafikiri kwamba anamskia, anamhisi, au hata anamwona mpendwa wake. Au huenda akashindwa kukazia fikira kile anachofanya au akawa akisahausahau mambo. Tiina anasema: “Kuna nyakati ambazo ningeshtukia akili ikiwa mbali sana ingawa nilikuwa nikizungumza na watu! Ningejikuta nimezama kwenye mawazo nikifikiri kuhusu kifo cha Timo. Tatizo hilo la kushindwa kukazia fikira mambo lilinihangaisha pia.”
Kutamani kujitenga. Mtu aliyefiwa huenda asifurahie kuchangamana na watu. Kostas anasema: “Sikuhisi huru kukaa katika kikundi cha wenzi wa ndoa. Na wakati huohuo nikiwa na waseja nilihisi nikiwa mahali pasiponifaa.” Yolanda, mke wa Ivan, anasema: “Ilikuwa vigumu sana kwetu kukaa na watu ambao walilalamika kuhusu matatizo yaliyoonekana kuwa madogo ukilinganisha na yetu! Halafu kuna wengine ambao walikuwa wakisema mambo mazuri yanayotimizwa na watoto wao. Nilifurahi pamoja nao, lakini wakati huohuo mazungumzo hayo hayakunivutia. Mimi na mume wangu tulielewa ni lazima maisha yaendelee, lakini hatukuwa na tamaa au subira ya kukabiliana na hisia zilizosababishwa na mazungumzo hayo.”
Matatizo ya afya. Kupungua au kuongezeka kwa hamu ya chakula na uzito, na vilevile kulala sana au kukosa usingizi, ni hali za kawaida. Aaron anaeleza hali ilivyokuwa mwaka ambao baba yake alikufa: “Nilikuwa na tatizo la kulala. Nilishtuka muda uleule kila siku usiku na kuanza kufikiria kifo cha baba.”
Alejandro anasema alipata matatizo ya afya yasiyoeleweka: “Nilifanyiwa uchunguzi mara kadhaa na daktari, lakini alinihakikishia kwamba sina tatizo lolote. Nilihisi kwamba huzuni ya kufiwa ndiyo iliyokuwa ikisababisha matatizo hayo.” Baada ya muda, hali hiyo iliisha. Hata hivyo, Alejandro alifanya uamuzi wa busara kwenda kumwona daktari. Huzuni ya kufiwa inaweza kuathiri mfumo wa kinga mwilini, kufanya tatizo la afya ulilonalo liongezeke, au hata kusababisha tatizo jipya lijitokeze.
Kushindwa kutimiza majukumu ya msingi. Ivan anasema: “Eric alipokufa, tulihitaji kuwafahamisha watu wa ukoo, marafiki, na watu wengine kama vile mwajiri wake na mmiliki wa nyumba aliyokuwa amepanga. Pia tulipaswa kujaza fomu nyingi zilizohusu mambo ya kisheria. Vilevile tulihitaji kupanga vitu vya Eric. Mambo hayo yote yalitaka umakini mkubwa ilhali tulikuwa tumechoka kimwili, kiakili, na kihisia.”
Lakini kwa wengine changamoto kubwa hutokea wanapolazimika kushughulikia majukumu ambayo awali hawakuhitaji kuyafanya. Ilikuwa hivyo kwa Tiina. Anasema: “Timo alishughulikia mambo yote yaliyohusiana na benki na biashara. Sasa ilibidi nibebe jukumu hilo, jambo lililoniongezea mkazo. Kweli, ningeweza kufanya mambo hayo yote kwa njia inayotakiwa?”
Hali zilizotajwa katika makala hii, huenda zikafanya ionekane kwamba mtu hupitia kipindi kigumu sana baada ya kufiwa. Ukweli ni kwamba uchungu wa kufiwa na mtu tunayempenda unaweza kuwa mkali sana, lakini kujua jambo hilo mapema kunaweza kumsaidia mtu aliyefiwa kuhimili hali hiyo. Kumbuka pia kwamba si watu wote hupitia hali hizo zote zilizotajwa. Kwa kuongezea, kwa kiasi fulani inafariji kujua kwamba kuhisi uchungu mwingi baada ya kufiwa ni jambo la kawaida.
KWELI NITAWAHI KUWA NA FURAHA TENA?
Utarajie nini? Uchungu wa kufiwa haudumu milele, bali hupungua hatua kwa hatua. Haimaanishi kwamba “jeraha” la kufiwa litapona kabisa au yule aliyekufa atasahaulika. Lakini, pole kwa pole, maumivu hupungua. Huenda hisia hizo zikaibuka mambo fulani yanapokuja akilini au katika nyakati fulani za pekee kama vile tarehe mliyofunga ndoa inapofika. Hata hivyo, baada ya muda, wengi hufikia hatua nzuri ya kihisia hivi kwamba wanafaulu tena kushughulikia vizuri majukumu yao ya kila siku. Itakuwa rahisi kufikia hatua hiyo hasa ikiwa mtu aliyefiwa anategemezwa na watu wa familia au marafiki na anafanya kile kinachohitajika ili kukabiliana na hali yake.
Huzuni itadumu kwa muda gani? Kwa baadhi ya watu, uchungu hudumu kwa miezi michache tu. Hata hivyo, kwa walio wengi, huenda mwaka mmoja au miwili ikapita kabla ya kuanza kuhisi nafuu. Na kwa wengine hali hiyo hudumu kwa muda mrefu zaidi.a Alejandro anasema: “Uchungu wangu ulidumu kwa miaka mitatu hivi.”
Uwe na subira. Usihangaike kuhusu kesho, usijilinganishe na wengine, na ukumbuke kwamba uchungu huo hautadumu milele. Ingawa hivyo, je, kuna mambo unayoweza kufanya ili kupunguza huzuni uliyo nayo na kuizuia isidumu kwa muda mrefu kupita kiasi?
Ni kawaida kuhisi uchungu mwingi baada ya kufiwa
a Uchungu wa baadhi ya watu huwa “sugu” na hudumu kwa kipindi kirefu sana, na hivyo huenda wakahitaji kupata msaada wa wataalamu wa afya ya akili.
-
-
Huzuni ya Kufiwa—Jinsi ya Kukabiliana NayoAmkeni!—2018 | Na. 3
-
-
KUKABILIANA NA HUZUNI YA KUFIWA
Huzuni ya Kufiwa Jinsi ya Kukabiliana Nayo
Leo, kuna ushauri mwingi sana wa jinsi ya kukabiliana na huzuni ya kufiwa, na ushauri fulani unaweza kuwa na matokeo zaidi kwako kuliko mwingine. Huenda hiyo ni kwa sababu kila mtu huomboleza kwa njia tofauti, kama makala iliyopita ilivyosema. Ushauri unaomfaa mtu mmoja huenda usimfae mwingine.
Hata hivyo, kuna mapendekezo ya msingi ambayo yamewasaidia watu wengi. Wataalamu wengi huyarejelea, na yanapatana na kanuni zisizopitwa na wakati ambazo zimeandikwa katika Biblia, kitabu cha kale kilichojaa hekima.
1: KUBALI MSAADA WA FAMILIA NA MARAFIKI
Baadhi ya washauri wanasema kwamba kukubali msaada wa wengine ndiyo njia bora ya kukabiliana na huzuni ya kufiwa. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda ukataka kuwa peke yako. Huenda hata ukawakasirikia wale wanaojaribu kukusaidia. Ni kawaida kuhisi hivyo.
Usihisi kwamba unapaswa kuwa na wengine nyakati zote, lakini pia usijitenge nao kupita kiasi. Isitoshe, huenda ukahitaji msaada wao baadaye. Kwa fadhili, wajulishe mambo unayohitaji wakati huo na yale usiyohitaji.
Ikitegemea mahitaji yako, amua utatumia kiasi gani cha muda ukiwa peke yako na kiasi gani ukiwa na wengine.
KANUNI: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja . . . Kwa maana mmoja wao akianguka, mwenzake anaweza kumwinua.”—Mhubiri 4:9, 10.
2: KULA CHAKULA CHENYE LISHE NA UTENGE MUDA WA MAZOEZI
Chakula chenye lishe kitakuimarisha na kukupa nguvu unapopitia kipindi hicho cha huzuni. Jitahidi kula aina tofauti-tofauti za matunda, mboga za majani, na vyakula vyenye protini visivyo na mafuta mengi.
Kunywa maji mengi na vinywaji vingine vyenye virutubisho.
Ikiwa huna hamu ya chakula, kula kiasi kidogo kila baada ya muda mfupi. Unaweza pia kumuuliza daktari wako ikiwa inafaa utumie vidonge vinavyoongeza virutubisho mwilini.a
Mazoezi ya kutembea na ya aina nyingine yanaweza kupunguza hisia mbaya. Kufanya mazoezi kutakupatia nafasi ya kutafakari kuhusu pengo lililoachwa au kukusaidia kuondoa mawazo hayo akilini.
KANUNI: “Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.”—Waefeso 5:29.
3: LALA VYA KUTOSHA
Kwa kawaida, kulala ni muhimu. Lakini usingizi ni muhimu hata zaidi kwa wale waliofiwa kwa sababu, huzuni ya kufiwa huongeza uchovu.
Epuka kutumia kwa wingi vinywaji vyenye kafeini au kileo kwa sababu vinaweza kufanya ukose usingizi.
KANUNI: “Ni afadhali konzi moja ya pumziko kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kukimbiza upepo.”—Mhubiri 4:6.
4: UWE TAYARI KUBADILIKA
Kumbuka kwamba kila mtu hukabiliana na huzuni ya kufiwa kwa njia tofauti. Hivyo, jitahidi kujua njia inayokufaa wewe binafsi.
Baadhi ya watu huona kwamba wanapoeleza hisia zao kwa wengine wanahisi vizuri zaidi, lakini wengine hupendelea kutojieleza. Hata wataalamu wana maoni yanayotofautiana kuhusu umuhimu wa mtu kueleza hisia zake baada ya kufiwa. Ikiwa ungependa kueleza jinsi unavyohisi lakini unasita, unaweza kuanza kwa kufunua hatua kwa hatua hisia zako kwa rafiki yako wa karibu.
Baadhi ya watu wametambua kwamba kulia huwasaidia kupunguza huzuni waliyo nayo, ilhali wengine hufanikiwa kukabiliana na huzuni yao bila kulia sana.
KANUNI: “Moyo hujua uchungu wake wenyewe.”—Methali 14:10.
5: EPUKA MAZOEA YENYE MADHARA
Baadhi ya watu waliofiwa huamua kunywa pombe kupita kiasi au kutumia dawa za kulevya ili kupunguza uchungu. Njia hiyo ya “kutuliza mawazo” ni yenye madhara. Utulivu wowote unaopatikana kwa njia hiyo haudumu, badala yake, mazoea hayo huleta matatizo makubwa. Tuliza mawazo yako kwa kutumia mbinu zisizosababisha madhara.
KANUNI: “Acheni tujisafishe kila unajisi.”—2 Wakorintho 7:1.
6: JISHUGHULISHE NA MAMBO TOFAUTI
Watu wengi wametambua kwamba kujishughulisha na mambo yatakayohamisha akili zao na hivyo kufanya wasifikirie sana kuhusu kifo cha mpendwa wao, huwasaidia kupunguza huzuni waliyo nayo.
Unaweza kufanya hivyo kwa kuanzisha au kuimarisha urafiki na watu wengine, kujifunza ustadi mpya, au kufanya mambo mengine unayofurahia.
Kadiri muda unavyopita, utaona hali ikibadilika. Utagundua kwamba muda unaotumia kufikiria kifo cha mpendwa wako unazidi kupungua, ishara ya kwamba umeanza kurudia hali yako ya kawaida.
KANUNI: “Kuna wakati uliowekwa wa kila jambo, . . . wakati wa kulia na wakati wa kucheka; wakati wa kuomboleza kwa sauti na wakati wa kucheza dansi.”—Mhubiri 3:1, 4.
7: UWE NA RATIBA YA KILA SIKU
Rudia ratiba yako haraka iwezekanavyo.
Ukifuata ratiba hususa ya muda wa kulala, kufanya kazi, na mambo mengine, unaweza kuanza kurudia hali yako ya kawaida.
Kuwa na mambo mengi mazuri ya kufanya kutakusaidia kupunguza maumivu ya kihisia.
KANUNI: “Hataona kwa urahisi jinsi siku za maisha yake zinavyopita, kwa sababu Mungu wa kweli humshughulisha na shangwe ya moyo wake.”—Mhubiri 5:20.
8: SUBIRI MUDA UPITE KABLA YA KUFANYA MAAMUZI MAKUBWA
Watu wengi wanaofanya maamuzi makubwa muda mfupi baada ya kufiwa, hujutia maamuzi hayo baadaye.
Ikiwezekana, subiri muda upite kabla ya kuhama, kubadili kazi, au kutupa vitu vya mpendwa wako aliyekufa.
KANUNI: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio, lakini wote walio na haraka kwa hakika watakuwa maskini.”—Methali 21:5.
9: JIKUMBUSHE KUMHUSU MPENDWA WAKO
Watu wengi waliofiwa huhisi vizuri wanapofanya mambo yanayowasaidia kumkumbuka mpendwa wao aliyekufa.
Huenda kukusanya picha au vitu vinavyokukumbusha mambo fulani kuhusu mpendwa wako, au kuandika matukio yanayomhusu unayopenda kubaki nayo akilini, kukakupatia faraja.
Tunza vitu vinavyokukumbusha mambo mliyofurahia, na utakapohisi una nguvu, vipitie ili kujikumbusha kuhusu nyakati hizo.
KANUNI: “Kumbukeni siku za zamani.”—Kumbukumbu la Torati 32:7.
10: BADILI MAZINGIRA
Ikiwezekana, chukua likizo usafiri.
Ikiwa hali hazikuruhusu kuchukua likizo ndefu, unaweza kutumia siku moja au mbili kufanya mambo yanayokufurahisha, kama vile kutembelea maeneo yenye kuvutia au makumbusho.
Kubadili mazingira, hata kama ni kwa muda mfupi, kunaweza kukusaidia.
KANUNI: “Twendeni faraghani mahali pasipo na watu ili mpumzike kidogo.”—Marko 6:31.
11: WASAIDIE WENGINE
Kumbuka kwamba unapowasaidia wengine unahisi vizuri na hivyo kupunguza huzuni yako.
Unaweza kuanza kwa kuwasaidia watu ambao wameathiriwa na kifo cha mpendwa wako, kama vile marafiki au watu wa ukoo ambao huenda wakahitaji mtu wa kuwafariji.
Kuwasaidia na kuwafariji wengine kutakusaidia upate tena shangwe na kusudi.
KANUNI: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
12: CHANGANUA UPYA MAMBO UNAYOTANGULIZA
Kufiwa kunaweza kukusaidia kutambua mambo yaliyo muhimu zaidi maishani.
Tumia fursa hiyo kuchunguza jinsi unavyoishi.
Baada ya kujichunguza, fanya mabadiliko yanayohitajika.
KANUNI: “Ni afadhali kwenda katika nyumba yenye maombolezo kuliko kwenda katika nyumba yenye karamu, kwa sababu huo ndio mwisho wa kila mwanadamu, na walio hai wanapaswa kuweka moyoni jambo hilo.”—Mhubiri 7:2.
Kwa kweli, hakuna chochote kitakachoondoa kikamili uchungu ulio nao. Hata hivyo, watu wengi ambao wamefiwa wanakubali kwamba kutumia mapendekezo kama yaliyotajwa kwenye makala hii, kumewasaidia kupunguza huzuni yao. Bila shaka, kuna mambo mengine, zaidi ya yale yaliyotajwa, ambayo yanaweza kukusaidia. Lakini ikiwa utatumia baadhi ya mapendekezo haya, uchungu ulio nao utapungua kwa kiwango kinachoridhisha.
a Gazeti la Amkeni! halipendekezi matibabu fulani hususa.
-
-
Kitabu Kinachotoa Ushauri Bora na FarajaAmkeni!—2018 | Na. 3
-
-
KUKABILIANA NA HUZUNI YA KUFIWA
Kitabu Kinachotoa Ushauri Bora Na Faraja
KATIKA MIAKA YA HIVI KARIBUNI, UTAFITI MWINGI UMEFANYWA KUHUSU JINSI YA KUKABILIANA NA UCHUNGU WA KUFIWA NA MTU WA KARIBU. Hata hivyo, kama ilivyotajwa awali, ushauri bora unaotolewa na wataalamu mara nyingi unapatana na hekima iliyo katika Biblia, kitabu kilichoandikwa zamani. Hilo linaonyesha wazi kwamba mwongozo wa Biblia haupitwi na wakati. Lakini zaidi ya kutoa ushauri wenye kutegemeka, Biblia hutoa habari ambazo hatuwezi kupata mahali pengine popote zinazoweza kumfariji sana mtu aliyefiwa.
Inatuhakikishia kwamba wapendwa wetu hawateseki
Biblia inasema hivi katika Mhubiri 9:5: “Waliokufa hawajui jambo lolote.” ‘Mawazo yao hupotea.’ (Zaburi 146:4) Pia, Biblia inafananisha kifo na usingizi mtulivu.—Yohana 11:11.
Tunapata faraja kujua kwamba kuna Mungu anayetupenda
Katika Zaburi 34:15, Biblia inasema kwamba, “macho ya Yehovaa yanawatazama waadilifu, na masikio yake yanasikiliza kilio chao cha kuomba msaada.” Hatumwelezi Mungu hisia zetu ili tu tuhisi vizuri au tupange mawazo yetu. Badala yake, sala hutuwezesha kusitawisha uhusiano wa kibinafsi na Muumba wetu, ambaye hutumia nguvu zake kutufariji.
Inatupatia tumaini zuri la wakati ujao
Wazia wakati ambapo wale walio katika makaburi watafufuliwa na kuishi tena duniani! Tumaini hilo linatajwa mara nyingi katika Biblia. Vilevile, Biblia inaeleza jinsi hali itakavyokuwa duniani wakati huo. Inasema kwamba Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.
Wengi ambao wanamwamini Yehova, Mungu aliyeitunga Biblia, wanapata nguvu za kukabiliana na huzuni wanapofiwa, kwa sababu wanaamini kabisa watawaona tena wapendwa wao. Kwa mfano, Ann, ambaye alifiwa na mume wake aliyekuwa ameishi naye kwa miaka 65, anasema: “Biblia hunihakikishia kwamba wapendwa wetu waliokufa hawateseki na kwamba Mungu atawafufua wote walio katika kumbukumbu yake. Mimi hutafakari jambo hilo kila mara ninapomfikiria mume wangu aliyekufa, na kwa njia hiyo, ninafaulu kustahimili pigo hilo kubwa zaidi maishani mwangu!”
Tiina, aliyetajwa awali, anasema: “Tangu Timo alipokufa, nimeona Mungu akinitegemeza. Kwa kweli, nimehisi kabisa Yehova akinisaidia katika kipindi hiki kigumu. Na tumaini la ufufuo linalotajwa katika Biblia ni halisi sana kwangu. Linaniimarisha na kunipa nguvu za kuvumilia hadi nitakapomwona tena Timo.”
Maelezo hayo yanapatana na ya mamilioni ya watu wanaoiamini Biblia. Ikiwa unahisi kwamba ahadi za Biblia si za kweli au ni ndoto tu, tafadhali, angalau chunguza ili ujithibitishie mwenyewe ikiwa ushauri na ahadi zake ni zenye kutegemeka. Bila shaka, utatambua kwamba Biblia ndicho kitabu kinachotoa ushauri bora na faraja kwa wale waliofiwa.
JIFUNZE MENGI ZAIDI KUHUSU TUMAINI LA WAFU
Tazama video zinazohusiana na habari hiyo kwenye tovuti yetu, jw.org/sw
Biblia inaahidi kwamba, tutawakaribisha tena wapendwa wetu waliokufa watakapofufuliwa wakati ujao
Ni nini hutupata tunapokufa? Jibu la Biblia linafariji na kutia moyo sana
Kukiwa na habari nyingi mbaya, unaweza kupata wapi habari njema? Video hii inatoa utangulizi wa broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!
Tafuta kwenye MACHAPISHO > VIDEO (Kisha, Mikutano na Huduma Yetu)
a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.
-