SURA YA 11
Kuna Ubaya Kufanya Urafiki Kupitia Intaneti?
Ni njia gani ya mawasiliano unayopenda?
□ Uso kwa uso
□ Simu
□ Kompyuta
Ni nani ambaye unaona ni rahisi kuwasiliana naye?
□ Wanafunzi wenzako
□ Watu wa familia
□ Wakristo wenzako
Ni wapi hasa unapoona kwamba ni rahisi kuzungumza kwa uhuru?
□ Shuleni
□ Nyumbani
□ Katika mikutano ya kutaniko
UMEJIBUJE swali la kwanza? Je, umejibu kwamba unapendelea kuwasiliana kupitia kompyuta badala ya kuzungumza uso kwa uso? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayependelea kufanya hivyo. Vijana wengi hutumia Intaneti kuanzisha na kuendeleza urafiki. Msichana anayeitwa Elaine anasema: “Inasisimua kujua kwamba unaweza kukutana na watu kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu—watu ambao hungepata kuwajua kamwe.” Tammy, mwenye umri wa miaka 19, anataja jambo lingine linalowavutia watu. “Unaweza kuwafanya watu wakuone vyovyote vile unavyotaka,” anasema. “Unapozungumza na mtu uso kwa uso, asipopendezwa nawe, hakuna lolote unaloweza kufanya.”
Sasa angalia jinsi ulivyojibu swali la pili na la tatu. Usishangae ikiwa ni rahisi zaidi kwako kuzungumza na wanafunzi wenzako kuliko Wakristo wenzako katika mikutano ya Kikristo. “Shuleni, ni rahisi zaidi kupata watu walio katika hali kama yako,” anasema Jasmine mwenye umri wa miaka 18. “Hilo hufanya iwe rahisi zaidi kuzungumza nao.”
Hivyo basi, inaeleweka ni kwa nini ungependa kuwasiliana na wanafunzi wenzako kupitia Intaneti. Tammy anakiri kwamba kwa muda fulani alikuwa akifanya hivyo. Anasema: “Wanafunzi wenzangu wote walikuwa wakiwasiliana katika Intaneti, nami sikutaka kubaki nyuma.”a Natalie, mwenye umri wa miaka 20, alianzisha gombowavu (Web page) katika Intaneti ili kuwasiliana na marafiki. “Tekinolojia imepiga hatua,” anasema. “Kuna njia nyingi mpya za kuwasiliana. Hiyo ni moja kati ya njia hizo, nami naipenda.”
Usipuuze Hatari
Bila shaka, watu fulani huona kwamba ni rahisi zaidi kuanzisha na kuendeleza urafiki katika Intaneti. Kwa mfano, Natalie anasema: “Katika Intaneti unakuwa na ujasiri ambao kwa kawaida hungekuwa nao unapozungumza na mtu uso kwa uso.” Tammy pia ana maoni kama hayo. “Ikiwa wewe ni mtu mwenye haya,” anasema, “unapowasiliana kupitia Intaneti, una nafasi ya kutosha kupanga mambo hususa utakayosema.”
Hata hivyo, kuna hatari za kuwasiliana kupitia Intaneti, na kuzipuuza kungekuwa upumbavu. Kwa mfano: Je, ungefumba macho yako huku ukitembea katika mtaa hatari? Kwa nini basi uzurure-zurure katika Intaneti bila kujali hatari zilizomo?
Fikiria hatari za kujaribu kupata marafiki katika Intaneti. Elaine, ambaye wakati fulani alikuwa na mazoea ya kupiga gumzo na watu asiowajua katika Intaneti, anasema: “Ni rahisi sana kuanzisha mazungumzo na watu wapotovu. Nyakati nyingine hata haichukui muda kabla ya mtu kuanza kusema mambo machafu au kuuliza maswali kama vile: ‘Wewe ni bikira? Wewe hufanya ngono ya kinywa?’ Wengine hata huomba mzungumzie mambo machafu ili kujisisimua kingono.”
Namna gani ikiwa ni mazungumzo tu na rafiki unayemwamini? Bado unahitaji kuwa mwangalifu. “Unaweza kutumia muda mwingi sana ukizungumza na mtu wa jinsia tofauti, hata kama mtu huyo ni ‘rafiki tu,’” Joan anasema. “Kadiri unavyotumia muda mwingi zaidi ukimtumia mtu huyo ujumbe, ndivyo urafiki wenu unavyozidi kukua, nanyi mnaweza kuanza kuzungumzia mambo ya kimahaba.”
“Wale Wanaoficha Jinsi Walivyo”
Mfalme Daudi alijua vizuri faida ya kujihadhari na marafiki wasiofaa. Aliandika: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”—Zaburi 26:4.
Katika Intaneti, je, umewahi kukutana na watu kama hao wanaozungumziwa na Daudi? Katika Intaneti, watu ‘wanaficha jinsi walivyo’ nyakati gani? ․․․․․
Kwa upande mwingine, inawezekana kwamba wewe huficha jinsi ulivyo unapotumia Intaneti? “Nilikuwa nikianza mazungumzo na watu kisha nibadili utu wangu upatane na mazungumzo hayo,” anasema Abigail, ambaye alikuwa na mazoea ya kupiga gumzo kwenye vituo vya Intaneti.
Msichana anayeitwa Leanne alitumia aina nyingine ya udanganyifu. Anasema: “Nilikuwa na mazoea ya kuwasiliana katika Intaneti na mvulana fulani wa kutaniko jirani. Muda si muda tukaanza kuambiana kwamba ‘tunapendana.’ Wazazi walipokuwa wakipita, nilikuwa nikibofya na kuficha nilichokuwa nikifanya kwenye kompyuta, nao hawakujua kamwe kilichokuwa kikiendelea. Hawakufikiri kamwe kwamba binti yao mwenye umri wa miaka 13 alikuwa akimwandikia mvulana mwenye umri wa miaka 14 mashairi ya kimapenzi. Walikuwa gizani kabisa.”
Uwe Mwangalifu
Bila shaka, haimaanishi kwamba mawasiliano yote kwenye Intaneti ni mabaya. Kwa mfano, watu wengi kutia ndani watu wazima hutumia Intaneti ili kuwasiliana na marafiki. Ikiwa ndivyo unavyofanya, je, kuna mambo yoyote unayopaswa kujihadhari nayo? Fikiria mambo yanayofuata.
● Chunguza muda unaotumia katika Intaneti, na usiruhusu Intaneti ikuibie wakati wa kufanya mambo ya maana zaidi, kutia ndani kulala. Kijana fulani anayeitwa Brian anasema: “Vijana fulani shuleni walisema kwamba walitumia Intaneti mpaka usiku wa manane.”—Waefeso 5:15, 16.
● Wasiliana tu na watu unaowajua. Watu wapotovu wana kawaida ya kutumia Intaneti wakitafuta vijana wanaoweza kudanganyika kwa urahisi.—Waroma 16:18.
● Uwe mwangalifu unapofanya mambo ya kibiashara. Uwe mwangalifu sana unapotoa habari zako za kibinafsi. Kosa dogo tu linaweza kufanya upoteze kila kitu.—Mathayo 10:16.
● Unapowatumia marafiki wako picha, jiulize, ‘Je, picha hizi zinamwakilisha mtu anayedai kwamba anamtumikia Mungu?’—Tito 2:7, 8.
● Sawa na mazungumzo ya uso kwa uso, mazungumzo katika Intaneti yakianza kuingilia “mambo yasiyofaa,” yakomeshe.—Waefeso 5:3, 4.
● Unapotumia Intaneti, usiwe mnafiki hata kidogo. Ikiwa unawaficha wazazi wako jinsi ulivyo, basi kuna tatizo. “Simfichi mama yangu chochote,” anasema tineja anayeitwa Kari. “Mimi humwonyesha ninachofanya kwenye Intaneti.”—Waebrania 13:18.
“Mvumilivu Hula Mbivu!”
Ungependa kupata marafiki? Hilo ni jambo la kawaida. Wanadamu waliumbwa wafurahie ushirika wa wengine. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, ikiwa unatamani kupata marafiki, unatenda kulingana na jinsi ulivyoumbwa! Hata hivyo, uwe mwangalifu unapochagua marafiki.
Lakini uwe na hakika kwamba unaweza kupata marafiki wazuri ukitegemea viwango vya Neno la Mungu. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 15 alisema hivi: “Si rahisi kupata marafiki wanaompenda Yehova na wakati huohuo wanakupenda. Hata hivyo, mvumilivu hula mbivu!”
Ati maneno hayawezi kuumiza? Porojo zinaweza kuchoma kama upanga. Unaweza kuzikomesha jinsi gani?
[Maelezo ya Chini]
a Urafiki shuleni utazungumziwa kwa mapana na marefu katika Sura ya 17.
MAANDIKO MUHIMU
“Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”—Zaburi 26:4.
PENDEKEZO
Usipokuwa mwangalifu, unaweza kupoteza wakati mwingi sana kwenye Intaneti! Kwa hiyo, amua kiasi cha wakati utakachotumia na kuhakikisha kwamba hupitishi wakati ulioweka. Ikihitajika, tega saa ambayo italia na kukukumbusha muda wako ukiisha.
JE, WAJUA . . . ?
Mtu mwenye nia mbaya anaweza kukupata kwa urahisi akipata habari chache tu kukuhusu katika Intaneti, kama vile jina lako, shule na namba yako ya simu.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Kila juma ningependa kutumia Intaneti kwa muda wa na ili nifanye hivyo nita ․․․․․
Nikigundua kwamba ninazungumza na mtu nisiyemjua kwenye Intaneti, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kuwasiliana na mtu kwenye Intaneti badala ya uso kwa uso kunaweza kuwa na faida na hatari gani?
● Kwa nini ni rahisi kuficha utu wako unapozungumza kwenye Intaneti?
● Ni nini kinachoweza kukusaidia usipoteze wakati mwingi katika Intaneti?
● Intaneti inaweza kutumiwa kwa ajili ya mawasiliano gani yanayofaa?
[Blabu katika ukurasa wa 103]
Siwasiliani katika Intaneti na watu nisiowajua au wale ambao kwa kawaida singeshirikiana nao.’’—Joan
[Picha katika ukurasa wa 100, 101]
Je, ungefumba macho yako huku ukitembea katika mtaa hatari? Kwa nini basi uwasiliane katika Intaneti bila kujali hatari zilizomo?