-
Ni Lazima Wakristo wa Kweli Wote Wawe Wahudumu?Mnara wa Mlinzi—1985 | Januari 15
-
-
muda wa makumi machache ya miaka iliyopita—na huo ni uthibitisho usiokanushika wa huduma ya Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10-12.
20. Sisi wahudumu Wakristo tunahitaji nini leo? Ni maulizo gani yanayobaki kujibiwa?
20 Wahudumu Wakristo leo wanahitajiwa kwa haraka zaidi ya wakati mwinginewo wote. Muda ni mfupi na mavuno ni mengi. Basi, sababu inaongezeka ya sisi kuwa wahudumu wanaostahili walio hodari wa kazi, ambao wanahubiri na kufundisha kwa njia yenye mazao. Tunaweza kufanyaje hivyo? Tunaweza kuwaje wahudumu wenye matokeo zaidi? Je! mifano ya Kristo na mitume ina mafaa kwetu leo?—Waefeso 5:15, 16; Mathayo 9:37, 38.
Mambo ya Kurudia Kujikumbusha
◻ Tunajuaje kwamba ilikuwa lazima wafuasi wote wa Kristo waliopakwa mafuta wawe wahudumu?
◻ Ni sehemu gani ambayo “mkutano mkubwa” umeshiriki katika huduma ya kisasa?
◻ Mwito wa Kikristo kwenye huduma unategemea nini?
◻ Ni uthibitisho gani ambao Mashahidi wa Yehova wanao juu ya huduma yao?
-
-
Namna ya Kuwa Wahudumu Wenye MatokeoMnara wa Mlinzi—1985 | Januari 15
-
-
Namna ya Kuwa Wahudumu Wenye Matokeo
“Kwa sababu hii nimemtuma Timotheo kwenu, aliye mwanangu mpendwa, mwaminifu katika Bwana, [kwa maana atawakumbusha] njia zangu zilizo katika Kristo, kama vile nifundishavyo kila mahali katika kila kanisa.”—1 WAKORINTHO 4:17.
1, 2. Ili mtu avutwe kwenye ukweli, jambo moja linalohitajiwa sana ni nini? (Matendo 8:12)
ROHO takatifu ilipomiminwa wakati wa Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., kundi la Kikristo lilikua likaenea kwa haraka sana. (Matendo 2:40-42; 4:4; 6:7; 11:19-21) Kilichofanya lipate mafanikio ni nini? Kwa sababu gani Wayahudi wengi sana kisha Wasamaria na Mataifa walikubali Kristo na ujumbe wa Ufalme wa Mungu?—Matendo 8:4-8; 10:44-48.
2 Ili mtu akubali habari njema za Kikristo, ni lazima mambo fulani yahusike. Kwanza, ni lazima athamini fadhili zisizostahilika ambazo Mungu alionyesha kuelekea wanadamu kwa kuchukua hatua ya kwanza kutuma Mwanaye duniani awe dhabihu ya ukombozi. Ni kama vile Yohana mwandikaji wa Biblia alivyoeleza: “Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.”—1 Yohana 4:9, 10.
3. Kwa sababu gani ni lazima mtu aone uhitaji wake wa kiroho?
3 Jambo jingine la maana sana ni nia ya kila mtu kuelekea faida za kiroho. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao. Wenye furaha ni wale wanaoona njaa na wanaoona kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watajazwa.” (Mathayo 5:3, 6, NW) Kwa kawaida mwenye kinaya, mwenye kujihesabia uadilifu mwenyewe haoni uhitaji wo wote wa kiroho na hataki tena kusikiliza ukweli. Anapotolewa ujumbe wa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi mtu wa namna hiyo atajibu, ‘Mimi sipendezwi. Nina dini yangu mwenyewe.’ Vivyo hivyo, mtu anayejitia sana katika shughuli za utafutaji wa mali hatakuwa na wakati wa mambo ya kiroho.—Mathayo 6:33, 34; 7:7, 8; Luka 12:16-21.
4. Sasa ni maulizo gani yatakayofikiriwa?
4 Lakini namna gani wale “wanaoona uhitaji wao wa kiroho” ambao wako tayari kutafuta Mungu na Ufalme wake? Wanaweza kupatikana na kutambuliwa kwa njia gani? Je! kuna lo lote ambalo sisi wahudumu wa Neno la Mungu tunaweza kufanya ili ujumbe wetu ueleweke zaidi? Tunaweza kuwaje wahudumu wenye matokeo zaidi?
Tunapaswa Kutumia Njia za Nani?
5. Kulingana na Paulo, Timotheo angefundisha Wakorintho nini?
5 Wakati mtume Paulo alipoandikia Wakristo wa Korintho barua yake ya kwanza, aliwaambia angewapelekea Timotheo, ambaye ‘angewakumbusha njia zake zilizo katika Kristo.’ Badala ya kusema “njia,” tafsiri nyingine zinataja “njia za kuishi,” “njia ya maisha” au “njia ambayo mimi naishi.” Lakini, Greek-English Lexicon of the New Testament ya Profesa Thayer inatoa fasiri hii juu ya andiko hilo: “Njia za kutendea ambazo mimi niliye mhudumu na mtume wa Kristo nafuata katika kutekeleza cheo changu.” Kwa kuwa Paulo anamalizia sentensi kwa kusema, “kama vile nifundishavyo kila mahali katika kila [kundi],” ni jambo la akili kukata maneno kwamba maneno yake yanahusu pia huduma yake yenye utendaji wala si mwenendo wake wa Kikristo tu.—1 Wakorintho 4:17.
6. Kwa sababu gani huduma ya Yesu ilikuwa na matokeo?
6 Huduma ya Yesu haikufanywa shaghalabaghala (ovyoovyo). Alitumia mpango pia katika mahubiri yake. Kwa mfano, yeye aliwafundisha mitume wake kwa uangalifu, na baadaye wale waeneza-evanjeli 70, namna ya kuhubiri kwa matokeo. Matumizi yake mwenyewe ya mifano, maswali na mitajo ya Maandiko yalikuwa mfano wa kufuatwa nao. Hiyo ingali ndiyo njia bora zaidi leo.—Luka 9:1-6; 10:1-11.
7. Tunaweza kuelezaje watu wengi iwezekanavyo habari njema?
7 Kwa kuwa huduma ya Kikristo ni jambo linalohusu uzima wa milele au kifo cha milele, tunaweza kupelekaje habari njema kwa watu walio wengi kabisa? Ni kwa njia gani tunaweza kuwa ‘hatuna hatia kwa damu ya mtu awaye yote’? Ni kwa kutumia kila njia ya utumishi. Kama mtume Paulo alivyosema, hiyo inatia ndani huduma ya “nyumba kwa nyumba.” Kitabu kimoja cha Kispania chenye maelezo yanayohusu Matendo 20:20 kinasema: “Hiyo ndiyo njia ya kuhubiri ambayo Paulo alifuata katika Efeso.”—Matendo 20:20-27.
Kizuizi cha Kwanza
8, 9. (a) Mara nyingi kizuizi cha kwanza katika huduma kinakuwa nini? (b) Kwa sababu gani Yesu aliweza kusema kwa ujasiri?
8 Mara nyingi sana kizuizi cha kwanza tunachohitaji kushinda katika huduma ni sisi wenyewe. Wengine wana maelekeo ya kujifikiria, kujisikia hawastahili sana na hawana elimu ya kutosha ili kuweza kukabiliana na watu wanaowakuta. Lakini Yesu alikuwa na maoni gani? Je! alikuwa amehudhuria shule za walimu wa kidini? Je! alikuwa na elimu ya juu? Lakini alipohubiri, watu wake mwenyewe walionaje? Mathayo anatuambia: “Wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii?” Ni kweli kwamba Yesu alikuwa mkamilifu, Mwana wa Mungu. Lakini njia alizotumia zilikuwa zenye mafaa pia kwa wanafunzi wake ambao hesabu kubwa kati yao walikuwa “watu wasio na elimu” waliopaswa kufuata mfano wake. Walichochea maoni gani, hata kati ya adui zao wa kidini? “Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.”—Mathayo 13:54; Matendo 4:13.
9 Lakini, Yesu alipata wapi mambo yote hayo aliyofunza? Kwa sababu gani alipata mafanikio mengi katika huduma yake? Je! yeye alisisimuka kupita kiasi kama wahubiri wa kisasa wanaotumia televisheni ili kuvuta wasikilizaji? Hapana. Msingi wa Yesu ulikuwa kusema kwa njia ya kueleweka vyepesi—alitumia usemi wa watu wa kawaida, alijua mahitaji yao ya kiroho na, jambo la maana kuliko yote, Yesu alitegemezwa na Baba yake. Alielewesha wazi jambo hilo alipotangaza agizo alilopewa la kufanya huduma alipokuwa katika sinagogi la mji wa nyumbani kwao, Nazareti katika Galilaya. Alisoma hivi katika kitabu cha kukunja cha nabii Isaya: “Roho [ya Yehova i] juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa, na kutangaza mwaka wa [Yehova] uliokubaliwa. . . . Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu.”—Luka 4:16-21.
10, 11. (a) Inatupasa tuwe na maoni ya namna gani juu ya huduma yetu? (b) Paulo anajibuje?
10 Leo tuna tegemezo lile lile katika huduma yetu—Yehova Mungu, Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Tunahubiri ujumbe wake, hekima yake. Sisi wenyewe tunategemea Neno lake na tunalitumia sana katika mazungumzo yetu. Basi, je! tunapaswa kujiona kwamba hatufai kuwahubiri hata watu wenye elimu au utajiri mwingi kuliko sisi?
11 Paulo anajibu hivi: “Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? . . . Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”—1 Wakorintho 1:18-29.
12. Mafanikio katika huduma yetu yanatokana na nini? (Yakobo 4:8)
12 Mafanikio katika huduma hayatokani na elimu yetu wala ukoo wetu. Yanatokana na ujumbe wa Ufalme wenyewe ambao unavuta itikio katika moyo wa mtu anayeona uhitaji wa kiroho. Jambo jingine linaloleta mafanikio ni nia njema ya Yehova kuelekea mtu huyo, kwa maana kama vile Yesu alivyosema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka.”—Yohana 6:44.
13. (a) Paulo na Barnaba waliitikiaje upinzani? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kuwa na furaha sikuzote katika huduma?
13 Basi, tukitumainia tegemezo la Yehova, tunaweza kuendesha huduma yetu kwa usadiki kama Paulo na Barnaba katika karne ya kwanza. Walipohubiri katika Ikonio, huduma yao ilileta utofautiano mkubwa wa maoni ya watu na upinzani fulani. Je! walilegeza mwendo kwa sababu hiyo? Masimulizi ya Luka yanatuambia: “Wakakaa huko wakati mwingi, wakinena kwa ushujaa katika [Yehova], aliyelishuhudia neno la neema yake, akiwajalia ishara na maajabu yatendeke kwa mikono yao.” Nasi pia tukiwa na maoni yanayofaa kuelekea watu katika eneo letu, kisha tuache matokeo mikononi mwa Yehova, sikuzote huduma itakuwa jambo la furaha, si la mzigo.—Matendo 14:1-3; Yakobo 1:2, 3.
Namna Watu Wanavyoitikia
14. Watu waliitikiaje mahubiri ya Paulo?
14 Walipokuwa wakihubiri, wala Yesu wala Paulo hawakuitikiwa vizuri sikuzote. Kwa mfano, watu wengi waliitikiaje wakati Paulo alipohubiri katika Athene? Masimulizi yanatuambia: “Baadhi ya Waepikureo na Wastoiko, wenye ujuzi, wakakutana naye. Wengine wakasema, Mpuzi huyu anataka kusema nini? Wengine walisema, Anaonekana kuwa mtangaza habari za miungu migeni, kwa maana alikuwa akihubiri habari za Yesu na ufufuo. Wakamshika, wakamchukua Areopago, wakisema, Je! twaweza kujua maana ya elimu hii mpya unayoinena? Kwa maana unaleta mambo mageni masikioni mwetu.”—Matendo 17:18-20.
15. Watu wanaitikiaje huduma yako wewe? Lakini inatupasa tukumbuke nini?
15 Inatupasa tujue kwamba huenda pia ujumbe wetu ukasikika na watu wa kisasa kuwa wa kigeni kwa sababu ya vile unavyoelezwa na vyombo vya utangazaji wa habari. Kwa sababu hiyo, watu wengi wanatangulia kufanya uamuzi juu ya jambo hilo na kutukataa kabla ya sisi kuwaeleza kwa maana uvumi unakuwa umewapa maoni mabaya. Wengine, kama Waathene wale, wanakubali kupewa habari zaidi kabla ya kufanya uamuzi. Bila shaka, wakiisha kusikiliza huenda bado wakadhihaki tumaini la Ufalme kuwa lisiloaminika. Hata hivyo, kumbuka kwamba wanapofanya hivyo wanamkataa Kristo na ujumbe wake, si wewe.—Matendo 17:32-34; Mathayo 12:30.
Tunaacha Kuwa Watu Wasiojulikana na Kuwa Rafiki
16. (a) Huenda tukaitikiaje watu tusiowajua wakitutembelea nyumbani? (b) Utangulizi wetu unapasa kutimiza nini?
16 Wewe unaonaje wakati watu usiowajua wanapokuja nyumbani kwako? Ni maulizo gani ambayo huenda yakaingia akilini mwako? Labda utajiuliza, Ni akina nani hawa? Wanataka nini? Wameniletea matata? Tunapojitokeza kama wahudumu mlangoni pa mtu, inatupasa tukumbuke hivyo. Basi utangulizi wetu unapasa kustarehesha akili zao waache wasiwasi juu ya maulizo hayo. Lakini namna gani? Haya basi, Yesu alipendekeza utangulizi gani? Alisema: “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi.”—Mathayo 10:12, 13.
17. Tunaweza kufanyaje mtu aondoe wasiwasi katika utangulizi wetu?
17 “Amani yenu na iifikilie.” Hiyo maana yake nini? Ni kwamba katika huduma yetu tunatakia kila mtu na kila nyumba amani yetu. Hivyo maneno yetu ya utangulizi yanapasa kuonyesha kwamba sisi ni wahudumu wa Mungu wanaopenda amani. Hata leo hii Wayahudi (au Waswahili) na Waislamu wanatumia salamu zinazosema “Amani na iwe nanyi” au “Amani” (“Shalom aleichem” au “Shalom” katika Kiebrania, na “Assalām ‘alaikum” au “Salām,” katika Kiarabu). Bila shaka, salamu yetu itakuwa tofauti nchi hii na hii kulingana na desturi ya mahali. Lakini shabaha ni ile ile moja—kufanya mtu mume au mtu mke aache wasiwasi ili asikilize ujumbe wa Ufalme. Kutaja jina lako kwanza, na hata kusema unaishi wapi, huenda kukasaidia kutimiza lengo hilo. Kunaonyesha hakuna jambo fulani unalojaribu kuficha. Kusudi lako na unyofu wako unakuwa wazi uonwe na watu wote. Hapo unakuwa ukifanya kama Paulo alivyoshauri: “Hakikisheni kwamba tabia yenu mbele ya watu wote haiwezi kuchambuliwa. Kwa kadiri ambayo daraka lenu linafikia, ishini kwa amani pamoja na kila mtu.”—Warumi 12:17, 18, Phillips.
18. Ni kiwango gani tunachopaswa kufikia sikuzote katika huduma yetu?
18 Kama tuko katika huduma ya nyumba kwa nyumba au tuko barabarani, watu wote wanatutazama. Mazungumzo na tabia yetu yanapasa sikuzote kuwa yasiyoweza kulaumiwa na yasiyoudhi watu. Lakini, ingawa njia yetu ya kuhubiri inapasa kuwa na upole na yenye amani, haipasi kuwa ya kuomba watu msamaha bila sababu. Sisi hatuoni aibu juu ya kuwa wahudumu wa Mungu mbele ya watu wote.—Marko 8:38.
19, 20. (a) Anapokuwa barabarani, mtu anaweza kufikiaje watu wasiojali sana mambo ya wengine? (b) Kwa sababu gani Yesu alikuwa mwenye matokeo katika ile njia ya kufikia watu kiasili, bila kufuata mpango fulani?
19 Katika mataifa fulani watu wana hali ya kushughulikia zaidi mambo yao wenyewe bila kujali mambo ya wengine. Wengine wanaona haya kufikiwa barabarani na mtu anayeonyesha magazeti. Ikiwa ndivyo ilivyo, mbona usitumie njia ya akili zaidi ya kufikia watu? Unaweza kuanza kwa busara mazungumzo na mtu asiye na haraka kisha utoe vitabu vya habari za Biblia kiasili bila kuonyesha wazi unatoa kitabu.
20 Bila shaka Yesu alikuwa mwepesi wa kutumia namna hiyo ya mahubiri. Kwa kuwa kwa kawaida Wasamaria na wanawake walidhihakiwa na Wayahudi, Yesu alitumia akili katika njia yake ya kumfikia mwanamke yule Msamaria mwenye ukosefu wa adili kwenye chemchemi ya Yakobo. Mazungumzo yake ni kiolezo cha kutolea ushuhuda wa vivi hivi na wa barabarani. Pia ni mfano mzuri wa kufundisha kwa huruma na kwa njia yenye kujenga.—Yohana 4:5-30.
21. Ni jambo gani la maana sana linaloonyeshwa katika huduma ya Paulo?
21 Jambo jingine moja la maana sana lazima lifikiriwe tunapoanza utangulizi wa kujulisha habari njema za Ufalme. Paulo alikuwa fundi wa kulifanya. Ona kama unaweza kulijua kutokana na nyingi za tangulizi zake zilizo katika Matendo 13:16-20; 17:22 na 22:1-3. Angalia kwamba katika kila pindi alitafuta mambo ambayo angeweza kukubaliana na wasikilizaji wake. Alijishirikisha nao pamoja na malezi yao. Matokeo ni kwamba walisikiliza hata kama hawakukubaliana naye. Vivyo hivyo utangulizi wetu unaweza kugusa jambo linaloleta ushirikiano wa kibinadamu kati yetu na mwenye nyumba. Labda unaona kwamba kuna watoto katika nyumba, nawe pia u mzazi. Basi hapo ninyi wawili mna hali moja, msingi wa kirafiki. Unakuwa na jambo la mazungumzo linaloweza kukuelekeza utoe ujumbe wa Ufalme!—Mathayo 18:1-6.
22. Ni maulizo gani ambayo sasa yanafaa kujibiwa?
22 Lakini mapendekezo hayo ni mwanzo tu. Ni hatua gani zaidi zinazohitajiwa ili kutokeza mwanafunzi mwingine mwishowe? Ni mambo gani mengine yanayohitajiwa ili kusaidia mtu mwingine awe na uhusiano pamoja na Mungu kupitia Kristo? Ni sifa gani zitakazofanya huduma yako iwe na matokeo zaidi?
Wewe Ungejibuje?
◻ Ni mengine gani kati ya mambo yanayohusika katika kukubali kwa mtu ujumbe wa Ufalme?
◻ Woga na kujifikiria kunaweza kushindwaje katika huduma?
◻ Shabaha ya tangulizi zetu katika utumishi wa shambani inapasa kuwa nini?
◻ Mfano wa Yesu na msaada wa Paulo unaweza kutusaidiaje katika njia yetu ya kufikia watu?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Yesu alifundisha wanafunzi wake njia zenye matokeo za kutumia katika huduma
[Picha katika ukurasa wa 16]
Ni Maulizo gani yanayoingia akilini mtu usiyemjua anapokuwa mlangoni pako?
-
-
Huduma Yenye Matokeo Inayoongoza Kwenye Wanafunzi ZaidiMnara wa Mlinzi—1985 | Januari 15
-
-
Huduma Yenye Matokeo Inayoongoza Kwenye Wanafunzi Zaidi
“Hizi zilikuwa zawadi zake: wengine wawe . . . . waeneza-evanjeli, wengine wachungaji na walimu, ili kutayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya kazi katika utumishi wake.”—WAEFESO 4:11, 12, The New English Bible.
1. Kristo alijisikiaje kuelekea watu?
KRISTO YESU hakuwa mkaa-peke-yake. Huduma yake ilihusu watu kwa njia zote. Katika yale masimulizi manne ya Injili karibu nyakati zote Yesu anajishughulisha na watu. Wakati wa safari zake aliona hali halisi waliyokuwa nayo kisha akawahurumia sana. Ikiwa wewe ni mhudumu Mkristo, je! unawaonea huruma watu unaowakuta?—Mathayo 9:35, 36.
2. Mashahidi wa Yehova wanaigaje mfano wa Yesu?
2 Huduma ya Kikristo leo lazima pia ihusu watu. Kwa kujua uhakika huo, Mashahidi wa Yehova wanatumia njia zenye kubadilikana katika utumishi wanaompa Mungu. Ulimwenguni pote wanaonekana wakisema na watu—barabarani, milangoni, katika maeneo yenye watu wengi madukani, karibu na vituo vya bas na gari-moshi, katika sehemu za viwanda, afisi na biashara. Hata watu wawe wanaishi wapi, Mashahidi wanafika huko wakitumikia wakiwa waeneza-evanjeli. Kwa sababu gani ndivyo walivyo? Kwa sababu neno “evanjeli” limetokana na neno la Kigiriki euaggelion, ambalo linamaanisha “habari njema.” Kama Kristo, ni lazima kila shahidi Mkristo wa Yehova awe mhudumu wa habari njema, mweneza-evanjeli. Basi ni lazima kila shahidi ajishughulishe na watu.—2 Timotheo 4:5; Waefeso 4:11, 12.
3. Ni njia gani ya huduma ya Kikristo iliyo na matokeo kupita zote?
3 Kazi hiyo ya kueneza evanjeli inapasa kuendeshwaje kwa njia yenye matokeo? Je! njia ya kutumia redio na televisheni kama dini nyingi sana zinavyofanya ndilo jibu la kweli? Ebu jiulize mwenyewe, Je! redio na televisheni inaweza kukujibu wewe binafsi maulizo yako kwa njia ya asili? Hapana—kwa njia fulani, hivyo ni vyombo vya utangazaji wa habari visivyoweza kusema na mtu binafsi. Huduma yenye matokeo mengi zaidi ingali ni ile iliyozoewa na Yesu na wanafunzi wake, kuelekeana uso kwa uso na watafutaji wa ukweli. Lakini inachukua wakati na jitihada, na jambo hilo lilionyeshwa na Paulo kwa mfano mwepesi kufahamika: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.”—1 Wakorintho 3:5-7.
4. Ni hatua gani tatu zinazohusika katika huduma yenye matokeo?
4 Maneno hayo yanatoa wazo la kwamba kuna hatua tatu katika huduma ya Kikristo—kupanda, kupalilia na kuvuna. Namna gani hivyo? Kwanza kuna kupanda, ule upokezaji wa kwanza wa habari njema za Ufalme. Halafu kuna kupalilia, kunakotia ndani kumimina maji juu ya kilichopandwa. Jambo hilo linafanywaje? Ni kwa kufanya maongezi zaidi ili kujibu maulizo na kumaliza mashaka ya watu. Mara nyingi hilo linaongoza kwenye funzo la kawaida la Biblia linalokaza sana ukweli wa Biblia katika akili na moyo wa mtu; kwa baraka ya Mungu, ukuzi unatokea. Matokeo ya mwisho ni kuwako kwa mwanafunzi mwingine mwenye bidii wa Kristo Yesu, mhudumu mwingine. Sasa ni kwa njia gani sisi sote tulio wahudumu tunavyoweza kupata baraka hiyo inayofurahisha ya kuvuna mwanafunzi?
5. Ni nini kitakachotusaidia tuwe wahudumu wenye matokeo?
5 Kama makala yetu iliyotangulia ilivyosema, Yesu alifundisha wanafunzi wake njia yenye mafaa ya kufanyia huduma yao. Na Paulo alitaja ‘njia zilizo katika Kristo.’ (1 Wakorintho 4:17) Makundi mengi sana ambayo alisaidia kuanzisha katika sehemu zenye kuzunguka Esia Ndogo na Ugiriki ni ushuhuda unaoonyesha wazi mafanikio yake. Tumekwisha kuzungumza nyingine za njia zilizotumiwa naye (na Yesu pia), lakini kuna nyingine zinazoweza kutumiwa kwa matokeo leo?
Msingi Ni Nini? na Ujumbe Ni Nini?
6. Ni nini ambacho lazima kiwe ndicho msingi wenye kutegemeza huduma yetu?
6 Ujumbe wa Kikristo unapasa kutegemea msingi gani? Je! unapasa kutegemea hekima na falsafa ya kibinadamu? Barua ambayo Paulo alimwandikia Timotheo inatoa jibu lililo wazi: “Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua . . . ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho.” Kwa wazi, Biblia, Neno la Mungu, inapasa kuwa ndio msingi unaotegemeza huduma yetu.—2 Timotheo 3:14-17.
7, 8. Yesu na Paulo waliwekaje mfano katika matumizi ya maandiko?
7 Kristo Yesu aliweka mfano katika jambo hilo—yeye alitumia daima maneno ya Maandiko; mtume Paulo naye alifanya ivyo hivyo. Kwa mfano, je! yeye alifika Thesalonike akifundisha falsafa ya Kigiriki? Hapana, kwa maana ni kama vile masimulizi yanavyotuambia: “Kwa hiyo kulingana na desturi ya Paulo yeye akaingia kwao, na kwa sabato tatu akazungumza pamoja nao kwa kuwapa sababu kutoka Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa mitajo ya maandiko kwamba ilihitajiwa kabisa Kristo ataabike na kuinuka kutoka kwa wafu.”—Matendo 17:1-3, NW.
8 Matokeo yakawa nini? “Wengine wao wakawa waamini.” Basi, kwa kufuata njia ya Paulo, msingi wa mahubiri yetu leo lazima uwe ni Neno la Mungu. Ndiyo sababu katika huduma yetu tuna kichwa cha Biblia kilichopendekezwa kwa maongezi. Kwa njia hiyo ukweli wa Neno la Mungu unaweza kuvuta itikio fulani katika wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho.—Matendo 17:4.
9, 10. (a) Kichwa cha mahubiri yetu leo lazima kiwe nini? (b) Toa mifano kutokana na huduma ya Paulo.
9 Sasa ulizo lile jingine ni kwamba, Ni ujumbe gani tunaopaswa kuhubiri? Basi, kichwa cha huduma ya Kristo kilikuwa nini? Yesu alijua sana agizo alilopewa, kwa maana alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” Akielekeza kwenye siku za mwisho za mfumo wetu wa sasa, alisema: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Luka 4:43, UV; Mathayo 24:14, NW.
10 Mkazo uo huo unapatikana katika mahubiri ya Paulo. Kwa mfano, kwa Wayahudi katika sinagogi ‘alinena kwa ushujaa kwa muda wa miezi mitatu, akihojiana nao, na kuwavuta katika mambo ya ufalme wa Mungu.’ Kwa wale waliokuwa Roma, ‘aliwaeleza kwa taratibu na kuushuhudia ufalme wa Mungu. ‘ Basi pasipo shaka “ufalme wa Mungu” ndio unaopasa kukaziwa katika huduma yetu ya Kikristo leo.—Matendo 19:8; 28:23, 31.
Wewe Unashambulia au Unavutia Watu?
11. Mara nyingi watu wanatendaje wanapoelekewa na Shahidi, nasi tunaweza kuzuiaje jambo hilo? (Matendo 17:17, 18)
11 Katika karne ya kwanza, watu waligawanywa na dini, kabila na taifa kama walivyo leo. (Matendo 2:7-11) Ndiyo kusema watu walio wengi wanakuwa wametangulia kuwa na maoni fulani juu ya mambo ya dini. Mara nyingi wanapokutana na Shahidi wanaona kuwa wameletewa tisho kisha wanaanza kujitetea. Tunaweza kubadili maoni hayo kwa njia gani? Ni kwa kutumia fadhili, busara na hali ya kubadilikana.
12, 13. Paulo alisemaje kwa waabudu sanamu katika Athene?
12 Angalia namna Paulo alivyoshughulika na hali kama hiyo katika mji wa Athene wenye ibada ya sanamu. Alipoona sanamu nyingi sana mara ya kwanza aliudhika. Wakati aliposimama aseme katika Areopago, je! alianza moja kwa moja kushambulia ibada ya sanamu waliyofanya? Utangulizi wake ulisema: ‘Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini. Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, Kwa Mungu Asiyejulikana. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua.’—Matendo 17:16-23.
13 Je! Paulo alitenganisha uhusiano wake na wasikilizaji wake kwa maneno hayo ya utangulizi? Hata kidogo. Njia yake ya kuwafikia ilikuwa yenye busara, si ya kushikilia mambo bila kubadilika. Hakuwalaumu, ingawa kwa maoni ya Mungu ibada yao ilikuwa ya bure. Lengo lake lilikuwa kuhubiri ujumbe wa Ufalme, si kuwashambulia. Alitambua walifuata dini sana akatumia huo kama msingi wa kuingia katika kichwa cha habari yake kuhusu Mungu wa kweli na mwakilishi wake, Yesu aliyefufuliwa. Matokeo ya njia hiyo ya kuwafikia kwa busara yakawa nini? Ingawa wengine wao walidhihaki, “wengine wakasema, Tutakusikiliza tena katika habari hiyo.” Ndiyo, alikaribishwa akafanye ziara ya kurudia!—Matendo 17:22-32.
14. Tunaweza kutumiaje mfano wa Paulo katika huduma yetu?
14 Tunaweza kutumiaje njia hiyo kuhusu huduma yetu leo? Kwanza, inatupasa tuwe macho kuziona ishara zinazotuonyesha moja kwa moja hali ya kidini ya mtu—labda kitu fulani cha kidini alichovaa au kinachoonekana mlangoni au katika chumba kikubwa cha makao yake. Hivyo, sawasawa na Paulo, sisi tunaweza mara nyingi kupata wazo la kutosha juu ya maoni ya kidini ya mtu huyo. Huo unakuwa uongozi wa kutuingiza katika utangulizi wa kirafiki unaoamsha kupendezwa, lakini usioleta ubishi. Kumbuka kwamba tunatembelea mtu sababu yetu hasa ikiwa ni kusema juu ya Ufalme wa Mungu—si kuhusika moja kwa moja katika mazungumzo ya mafundisho. Tunataka ushindi wa kupata watu, si kupata ushindi wa mabishano tu.—Linganisha 2 Timotheo 2:23-26.
15. Ni masomo gani mengine mazuri tunayoweza kujifunza kutokana na huduma ya Yesu? (Luka 10:38-42)
15 Tunaweza kujifunza jambo gani jingine kutokana na mfano wa Kristo? Tunapochunguza huduma yake tutaona usadiki wake na wepesi aliotumia kueleza mambo. Yeye hakutiwa wasiwasi na hali yo yote bali alinena kwa ajili ya Ufalme wa Mungu katika hali za namna zote, ziwe zilifaa au hazikufaa. Aliweza kuhubiri katika faragha ya nyumba fulani au kusimama mbele ya kundi la watu na kutoa mahubiri—bila maandishi ya habari, bila Biblia wala kikuza-sauti! Pia alijua kushughulika na watu wa namna zote. Watu wa hali za chini walijisikia kwamba wangeweza kumfikia. Vitu alivyovitaja ni vile walivyovijua, kama mashamba na mazao, nyavu na uvuvi wa samaki. Mifano yake ilikuwa myepesi sana kueleweka ingawa maana yake ilikuwa yenye kina kirefu. Je! sisi tunaonyesha sifa izo hizo nzuri katika huduma yetu?—Mathayo 4:18-25; 13:1-33; Luka 5:1-3.
Namna ya Kufikia Moyo
16. Kwa sababu gani lazima tuwe walimu wanaostahili?
16 Kwa kawaida inachukua wakati na funzo la uangalifu ili mtu asadikishwe juu ya ujumbe wa Biblia unaohusu Ufalme wa Mungu. Ndiyo sababu tuna mpango wa mafunzo ya nyumbani ya Biblia yanayofanywa kwa ukawaida, bila ya mtu kulipa fedha wala kulazimishwa. Yanafanywa kwa mtu yeyote anayetaka kuchunguza ahadi za Mungu ambazo ametoa kupitia Kristo. Mafunzo hayo yanaendelea kwa muda mrefu na yanakuwa na mazungumzo ya habari nyingi na maulizo mengi. Bila shaka hiyo ni kusema ni lazima tuwe walimu wenye kustahili. Lakini ni mambo gani hasa yanayohusika katika kufundisha?—1 Timotheo 4:16.
17. Ni njia gani moja aliyotumia Yesu kufikia moyo?
17 Kwa mara nyingine tunamgeukia Yesu tupate jibu. Yeye alifundisha namna gani? Tafadhali chunguza tu maandiko yanayofuata uone kama unaweza kuutambua utaratibu mwepesi ambao Yesu alitumia kufundisha wengine: Luka 6:9, 32-34, 39-42. Ulikuwa utaratibu gani? Yeye aliuliza maulizo yenye ufahamu. Kwa sababu gani alifanya hivyo? Ili kusaidia wasikilizaji wake wafikiri kwa kuziona sababu na kujichunguza kwa msaada wa mafundisho yake. Kwa kutumia maulizo alifikia mioyo yao kwa busara. Iliwapasa kuonyesha kama kweli walitaka kuwa wafuasi wake au kama makusudi yao ya kusikiliza yalikuwa ya juu-juu tu.—Mathayo 13:10-17; Marko 8:34-38.
18. (a) Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanatumia maulizo mara nyingi sana katika vichapo vyao? (b) Ni mazoea gani tusiyopopaswa kutumia sana tunapofundisha wengine?
18 Karibu misaada yote ya kujifunzia Biblia inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova katika huduma yao ina maulizo kwa kila fungu lenye maelezo ya andiko. Huo ni msaada wa kufundishia unaosaidia wale wanaojifunza Biblia waeleze maoni yao kwa maneno yao wenyewe. Ndipo inapokuwa wazi kama mtu anaelewa au haelewi mambo yanayofunzwa. Lakini, ingawa Yesu aliuliza maulizo katika pindi nyingi, yeye hakuzoea kugusia watu majibu kwa kuwatamkia neno la kwanza la jibu au silabi ya kwanza. Nyakati nyingine umejikuta ukiingia katika mazoea hayo unapokuwa na wanafunzi fulani wa Biblia? Kwa sababu gani hiyo si njia nzuri ya kutumia kwa ukawaida? Ni kwa sababu maarifa ya kujua Mungu na Kristo ambayo yanaongoza kwenye wokovu yanapasa kutegemezwa juu ya sababu na akili nzuri, si juu ya kukisia mambo hivi hivi tu.—Yohana 17:3; 1 Yohana 5:20.
Wanafunzi wa Nani?
19, 20. Ni uangalifu gani unaohitajiwa hapa? Kwa sababu gani?
19 Kufikia hapa, kuna jambo linalopasa kuonwa kwa uangalifu. Tukihubiri na kufundisha kwa njia yenye matokeo katika eneo lenye mazao, mwishowe tunatokeza wanafunzi. Lakini ni wanafunzi wa nani? Je! tunapaswa kufikiri hao ni “kondoo zangu mimi”? Na je! sisi tulio wahudumu tunapaswa kujiruhusu tuwekwe katika hali ya kusifiwa kupita kiasi? Angalia namna Paulo na Barnaba walivyoona wakati watu wa Listra walipotaka kuwatendea kama miungu. Walipaza sauti wakaliambia hivi kundi la watu hao: “Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai.”—Matendo 14:14, 15.
20 Paulo na Barnaba hawakujaribu kuvuta fikira za watu ziwaelekee wao wenyewe. Ingawa Paulo alishauri Wakristo wafuate mfano wake, kama alivyofuata wa Kristo, hakuwataka wawe wafuasi wake. Huduma tunayofanya lazima sikuzote iwe kwa utukufu wa Mungu, si wanadamu.—1 Wakorintho 3:6, 7; 11:1.
21. Kwa sababu gani wanafunzi wanakuwa wahudumu pia?
21 Baada ya muda, wanafunzi wanakuwa wahudumu. Kwa sababu gani inakuwa hivyo? Basi, inakuwaje tunapokuwa na habari zilizo njema kweli kweli za kuambia wengine? Je! tunaweza kunyamaza tu tusiwaambie? Badala ya kufanya hivyo, tunajisikia tukiwa tumekazika sana tukitaka kuambia mtu habari hizo. Ni kama Yesu alivyosema: “Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, . . . kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.” Ndivyo ilivyo kuhusu habari njema za Ufalme. Mwanafunzi ambaye moyo wake umeguswa anataka kufundisha wengine na kujiunga katika huduma kwa ukawaida na kwa kujitolea. Halafu kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa kunafuata. Hivyo kunaendelea kuwa na mfululizo usiokwisha wa wahudumu, kupatana na kanuni ya shauri ambalo Paulo alimpa Timotheo: “Hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”—Luka 6:45; 2 Timotheo 2:2.
22. (a) Kwa sababu gani Yehova ametokeza tengenezo la walimu na waeneza-evanjeli? (b) Kuna kazi gani ambayo ni lazima bado ifanywe wakati ujao?
22 Leo, duniani pote, Yehova Mungu ana tengenezo lililopewa mazoezi bora zaidi lenye walimu, waeneza-evanjeli, wahudumu wa karne ya 20. Kunao 2,600,000 wanaoshiriki katika ushuhuda wa kumalizia unaotolewa kabla mwisho haujaja juu ya mfumo huu mbovu. Lakini kikosi hicho kinachoendelea kuongezeka kinatayarishwa kwa ajili ya mwito mkubwa zaidi wa ushindani—kuelimisha mabilioni ya watu watakaorudi katika ufufuo. Wewe uko tayari katika pendeleo kubwa hilo? Je! huduma yako ina mazao sasa? Na tusali kwamba nuru yetu ing’ae kwa utukufu wa Mungu, tunapotumikia tukiwa wahudumu wenye matokeo.—Mathayo 5:16; Yohana 5:28, 29.—Kutoka u?8/15/84.
Mambo Ambayo Umejifunza
◻ Ni njia gani yenye matokeo zaidi ya kuhubiri habari njema?
◻ Lazima msingi wa kufundisha kwetu uwe nini? Ujumbe tunaotoa ni nini?
◻ Ni sifa gani zinazohitajiwa kufanya watu watusikilize?
◻ Yesu alifikiaje moyo wa wasikilizaji wake?
◻ Ni uangalifu gani unaohitajiwa tunapofundisha wengine?
-