-
Maoni ya Kikristo Juu ya Kuvuta SigaretiAmkeni!—1990 | Machi 8
-
-
Maoni ya Kikristo Juu ya Kuvuta Sigareti
NI WAZI kwamba Biblia haitaji tumbako wala kuvuta sigareti, kwa kuwa vitu hivyo havikujulikana katika nchi ya kale ya Mashariki ya Kati. Sababu sahili ni kwamba mmea wa tumbako ni wa uenyeji wa Amerika Kusini, Meksiko, na West Indies nao haukuanza kukuzwa kwenye sehemu nyingine za ulimwengu mpaka katikati ya karne ya 16.
Je! hiyo yamaanisha kwamba Biblia haisemi jambo lolote kuhusu kuvuta sigareti? Sivyo hata kidogo. Hiyo hutaarifu wazi kanuni zenye kutumika ulimwenguni pote ambazo ni miongozo kwa mwenendo wetu. Ni nini baadhi ya kanuni hizi za msingi?
Kupenda Mungu na Jirani
Ni lazima kani ya msingi yenye kuchochea Mkristo iwe ile ambayo Yesu alieleza: “Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako.”—Luka 10:27.
Mtu aweza kutoleaje Mungu upendo kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zake zote ikiwa anachakaza kimakusudi nguvu zake za kufikiri kwa kujihusisha katika tabia, zoea ovu, ambalo huongoza kwenye ugonjwa na kifo cha mapema? Mtu huonyeshaje uthamini wa zawadi ya Mungu ya uhai huku akivuta ndani nikotini ambayo ni dawa ya kulevya yenye kumzoeleza uvutaji? Mungu ndiye aliwapa “wote uzima na pumzi.” (Matendo 17:24, 25) Je! yatupasa tuchafue pumzi hiyo tuliyopewa na Mungu? Kwa maoni ya Mungu, kwa kweli hilo zoea ovu, “ni zoea au tabia mbovu, yenye kushusha tabia, au ya ukosefu wa adili.”—The American Heritage Dictionary of the English Language.
Kuvuta sigareti kwaonyeshaje upendo kwa jirani, na hali pumzi mbaya ya mvutaji na moshi wake huchafua nguo na hewa inayozunguka? Namna gani majirani wa karibu zaidi wa mvutaji, mwenzi wa ndoa na watoto wake? Je! ni upendo kufuatia mwendo ambao ungeweza kuongoza kwenye kifo cha mapema cha polepole, kilicho na maumivu ambacho wao watalazimika kuona wewe ukipatwa nacho? Je! ni kuonyesha ufikirio wa Kikristo kwa watu wengine kwa kuwashurutisha wawe wavutaji wasiojivutia wenyewe, huku wakivuta ndani mipumuo yenye sumu ya mvutaji? Si ajabu kwamba mmea wa tumbako umewekwa mahali paufaapo katika sehemu ya mimea yenye sumu, katika ile bustani ya mimea iliyoko Blanes, Hispania!
Namna gani kujipenda binafsi? Ni halali kujipenda mwenyewe kufikia hatua ya kutunza afya yako ya kimwili, ya kiakili, na ya kiroho. Mtume Paulo alitaarifu kwamba “hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.” Je! kujihusisha katika tabia ambayo pole kwa pole hudhoofisha afya yako ni kujipenda binafsi?—Waefeso 5:28, 29.
Yehova Mungu ameahidi kwamba kutakuwako ‘mbingu mpya na dunia mpya ambamo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:13, NW) Huo utakuwa ulimwengu mpya ulio safi, usio na uchafuzi wa aina yoyote. Uvutaji sigareti hautaruhusiwa wala kutamaniwa wakati huo, kwa hiyo mbona kuvuta sigareti sasa? Kwa kufaa shauri la Paulo latumika hapa: “Basi, wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Nikotini hutia unajisi wa kihalisi katika mnofu. Kuvuta sigareti hufanya isiwezekane Mkristo kumtolea Mungu mwili wake ukiwa “dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu [zake] za kufikiri.” (Warumi 12:1, NW) Nguvu za akili zaonyesha kwamba kuvuta sigareti kuna madhara na ni dhidi ya kanuni za Kikristo. Basi, hicho ndicho kichocheo cha msingi cha kuacha kabisa kuvuta sigareti ikiwa mtu ataka kufurahisha Mungu.
Kwa Nini Waliacha Kabisa?
Mamilioni ya watu kuzunguka ulimwengu wameacha kabisa kuvuta sigareti. Yawezekana kuacha. Lakini jinsi gani? Ni mambo gani yenye kuhitajiwa kabisa? Ni kichocheo chenye nguvu. Kile ambacho hufanya wengi waache ni afya, hali ya kujistahi, na upendo kwa jamaa. Lakini wengine pia wana kichocheo cha kidini—tamaa ya kufurahisha Mungu.
Kwa hiyo, namna gani kuhusu Ray, Bill, Amy, na Harley, waliotajwa katika makala yetu ya pili? Kwa nini waliacha kabisa kuvuta sigareti?
Bill, ambaye hapo kwanza alikuwa msanii mwenye madevu na nywele ndefu, alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Halafu ikawaje? “Niliamua kwamba nilitaka kumfurahisha Mungu na kumtumikia nikiwa na mwili na akili safi. Nilijipiga konde la kifua nikaamua kuacha ghafula. Sikuacha pole kwa pole. Siku ya Januari 1, 1975 ilikuwa ndiyo siku yangu ya mwisho kupuliza sigareti halafu nikatupilia mbali pakiti ile ya sigareti. Tangu wakati huo afya yangu imepata maendeleo. Ningali na kiasi kidogo cha kusakamwa na hewa mapafuni. Lakini hata nilipata maendeleo katika nguvu zangu za kutambua rangi baada ya kuacha kabisa kuvuta sigareti.”
Amy, yule muuguzi wa upasuaji, aeleza jinsi alivyoacha kabisa. “Mimi nilisaidia katika upasuaji wa kufungua moyo wazi, nami nimeona mapafu ya aina nyingi weee—ya rangi nyekundu-nyeupe na yenye afya, meusi-meusi na yenye sumu. Hata ingawa niliona mapafu hayo yaliyogonjweka vibaya sana, yenye kuonekana ni kana kwamba yamekolezwa pilipili nyeusi, bado mimi sikuacha kuvuta sigareti. Mimi nilijipumbaza, nikisema, ‘Wewe ungali mchanga. Hilo halitakupata wewe.’
“Halafu katika 1982 nikahisi uhitaji wa kunyoosha maisha yangu, nami nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Hata ingawa nilikaa pamoja na Shahidi katika kao lake, nilikuwa nikijificha na kwenda nje paani ili nikavute kidogo! Kwa hiyo ilikuwa lazima nijibane mimi mwenyewe. Nilisali sana tena kwa muda mrefu. Lakini mara nilipokwisha kufanya uamuzi ule, ilikuwa rahisi. Siku mbili za kwanza zilikuwa mtihani, lakini sala ya daima ndiyo ilinifungulia njia.”
Harley, ambaye hapo kwanza alikuwa mrukaji wa Jeshi-Bahari, alitatizwa kuvunja tabia hiyo ya kutumia nikotini. “Nilijaribu kupunguza-punguza uvutaji wangu wa sigareti, lakini sikupata mafanikio. Halafu nilipoamua kutaka kubatizwa niwe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nikajipiga konde la kifua nikaamua kuacha ghafula. Nilipita katika siku mbili au tatu za maumivu makali. Nilikuwa mwenye wasiwasi, mwenye kukazika hisia, na asiyestareheka mawazo. Nikatamani sigareti weee! Ndipo Shahidi mmoja akanisaidia kwa shauri fulani zuri. ‘Utakapo kunyoosha mkono uchukue sigareti, hapo ndipo ni lazima umpelekee Yehova sala ya kuomba msaada.’ Mimi nilipata mafanikio kwa kufanya hivyo. Wazo jingine lililonivutia ni kwamba, ‘Je! ningeweza kuwazia Yesu akiwa na sigareti katika kinywa chake?’ Hilo lilikuwa jambo lisilowazika. Lakini mimi nang’amua kwamba mvutaji sigareti huhitaji kichocheo chenye nguvu ili aache kabisa. Mimi nilikuwa nikimwambia mama yangu, ‘Mama, ni mimi mwenyewe tu ninayeumia [kwa sababu ya kuvuta].’ Kwa uhakika nilikuwa nikimuumiza yeye pia, kwa njia nyingi.”
Ray pia, yule ambaye hapo kwanza alikuwa ofisa mtumikia-manahodha wa Jeshi-Bahari, hakuona ikiwa rahisi kuacha kuvuta sigareti. “Nilikuwa nimejaribu mara chache kabla sijakutana na Mashahidi wa Yehova, lakini sikupata mafanikio. Sikuzote nilikuwa nikichangamana na wavutaji wa sigareti, na ilikuwa vigumu kukataa sigareti niliyotolewa. Lakini nilipopata kujua ukweli kutokana na Biblia, nilitaka kutumikia Yehova, sawa na vile Kristo alivyokuwa amefanya. Kwa hiyo nikaacha kwa siku moja. Nilikuwa na masikitiko kwa majuma mawili. Mwili wangu ulikuwa ukiomba sana nikotini. Lakini lo, ulifanya badiliko lililoje! Kwa ghafula nikawa tena na nishati zisizo na mipaka. Nilijihisi vema kwa kufanya hivyo. Nikawa naweza tena kujidhibiti.”
Je! Inastahiki Kuacha?
Fikira za akili nzuri zaonyesha kwamba zoea lolote lenye madhara lapasa kuachwa. Lakini hatusemi kwamba uvutaji sigareti una madhara tu. Bali ni wenye hatari ya kifo, ni wenye kuua. Ni wenye sumu. Kama vile Patrick Reynolds, mrithi wa mali nyingi za tumbako, alivyotaarifu katika ushuhuda wake kwa halmashauri ndogo ya baraza kuu la United States: “Mimi naamini kwamba kutangaza sigareti ni kuendeleza bidhaa yenye sumu na kwamba ni jambo la kiadili, lenye kufaa na lililo jema kukomesha utangazaji wote wa sigareti.”
Kwa Wakristo walio na tamaa ya kufurahisha Mungu, hakika ni jambo la kiadili, lenye kufaa na lililo jema kukomesha, si utangazaji wa tumbako tu, bali pia bidhaa zote za tumbako ili zitoke katika maisha zao. Sigareti (“zilizo salama” na zisizo salama), sigara (sigari), tumbako ya kiko, na ugoro (tumbako-mnuso)—zote hizi hutoka kwenye mmea ule ule mmoja wenye sumu, ufanyizao nikotini. Nawe huhitaji mmea huo ili kuthibitisha kwamba ‘umetoka mbali, ewe kipenzi’ wala ili kuona shangwe na ladha nzuri katika maisha yako. Hata wauzaji wa ugonjwa na kifo wajaribu kukuambia nini, umamboleo wa mtu hauonyeshwi kwa kujitilia sumu yeye mwenyewe!
-
-
Njia Kumi za Kuacha Kuvuta SigaretiAmkeni!—1990 | Machi 8
-
-
Njia Kumi za Kuacha Kuvuta Sigareti
1. Uwe na kichocheo cha kweli kweli. Uwe na sababu thabiti za kutaka kuacha kabisa—kujistahi (kujiheshimu); kuhangaikia afya yako, ya sasa na ya wakati ujao; kuhangaikia wapendwa wenye kuathiriwa na tabia yako hatari; tamaa ya kuwa safi, kimwili na kiadili, mbele yako mwenyewe na mbele za Mungu.
2. Jiwekee tarehe ya kuacha kabisa, kisha uifuate. Jipige konde la kifua uamue kuacha ghafula; njia hiyo huumiza haraka-haraka, lakini huponya haraka-haraka pia.
3. Chukua hatua hakika ili uvunje tabia hiyo. Zivunje-vunje sigareti zozote zilizo ndani ya nyumba, na umwage maji juu yazo. Fua nguo zako zote zenye harufu ya tumbako. Anza mambo yako upya, uhisi ukiwa na hali ya upya!
4. Unapokuwa ukikamilisha kujiondoa kabisa kwenye nikotini, epuka mazingira yenye tumbako nyingi na uepuke marafiki wavutaji. Zuru sehemu-sehemu ambako kuvuta sigareti hukatazwa, kama majumba ya vitu vya makumbusho na maktaba.
5. Weka akiba ya pesa ambazo ungalitumia kwa tumbako na uzihesabu baada ya mwezi mmoja! Nunua kitu ambacho wakihitaji kweli kweli. Au mnunulie zawadi mpendwa ambaye pia aweza kuushangilia ushindi wako.
6. Jitie wewe mwenyewe na mikono yako katika shughuli nyingi wakati ambapo kwa kawaida ungenyoosha mkono uchukue sigareti. Tafuna gamu (si gamu yenye nikotini) au umumunye peremende ukikazwa-kazwa na tamaa ya kuvuta sigareti. Badala ya kuvuta sigareti baada ya nyakati za chakula, safisha meno yako. Tembea mwendo fulani, andika barua, shona nguo, fanya kazi ya bustani, tengeneza vitu vilivyoharibika, safisha gari, na kadhalika.
7. Ukihisi ukiwa na wasiwasi au ukiwa chini ya mkazo, pumua kwa kina kirefu na polepole. Badala ya kunyoosha mkono uchukue sigareti, kunywa maji mengi na majimaji ya matunda. Maji husafisha mwili.
8. Fanya mazoezi bila kuruka mipaka ya uwezo wako wa kimwili. Kwanza chunguza na daktari wako ujue ni kiasi gani kifaacho. Hali yako yenye maendeleo ya kimwili itakutia moyo.
9. Punguza kiasi cha kileo ambacho wewe hunywa. Mara nyingi kileo na sigareti “huenda pamoja,” kwa kuwa kileo chaweza kuamsha tamaa ya kuvuta sigareti. Punguza pindi za kujifurahisha ambapo jambo hili lingeweza kutukia. Yaone matangazo ya tumbako kwa njia yenye uchambuzi—changanua jambo la kwamba matangazo huonekana kuwa bora kijuu-juu tu tena ni ya udanganyifu. Usinaswe tena.
10. Ikiwa wewe unatafakari kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mpelekee Mungu sala za moyo wa bidii ili kuomba msaada halafu utende kupatana na sala zako. Usitarajie muujiza; jitahidi ili iwezekane kuacha.
-