Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je! Wewe Utaendelea Kutembea Katika Ukweli?
    Mnara wa Mlinzi—1990 | Septemba 1
    • Je! Wewe Utaendelea Kutembea Katika Ukweli?

      “SINA furaha iliyo kuu kuliko hii, . . . ya kwamba watoto wangu wanakwenda katika kweli.” (3 Yohana 4) Ndivyo alivyosema mtume Yohana kuelekea mwisho wa maisha yake marefu. Uvumilivu wenye kuendelea wa ‘watoto wake,’ wale aliokuwa amewajulisha kwenye ile “kweli,” ulimletea shangwe kubwa. Yehova hushangilia pia wakati waabudu wake wabakipo katika ukweli. Ni lazima awe apendezwa kama nini leo kuona tengenezo kubwa, lenye mamilioni ya watu, likifuata mwendo huo wa hekima!—Mithali 27:11.

      Hata hivyo, ingawa watu wa Mungu kwa ujumla wameshikamana na ukweli bila kuondoleka, Wakristo fulani mmoja mmoja hupunguza mwendo au hata huacha ibada safi. Hilo si jambo lisilotarajiwa, kwa kuwa hilo hilo lilitendeka katika karne ya kwanza. (2 Timotheo 4:10; Waebrania 2:1) Hata hivyo, uhakika wa kwamba watu fulani hupunguza mwendo wakazia uhitaji wa wote kuwa macho juu ya hali yao wenyewe ya kiroho. Paulo aliwatia moyo hivi Wakristo wote: “Jithibitisheni wenyewe.” (2 Wakorintho 13:5) Kila Mkristo apaswa kujiuliza swali hili: ‘Mimi naweza kuhakikishaje kwamba nitaendelea kutembea katika ukweli?’

      Watu fulani wamepunguza mwendo au hata wakakoma kutembea katika ukweli kwa sababu walivunjwa moyo—labda na matatizo ya afya au mahitilafiano ya nyutu. Wengine wamepunguza mwendo kwa sababu walikengeushwa fikira. Wao wataka kupata shangwe ya baadhi ya matunda ya mfumo huu wa mambo maadamu upo. Twaweza kuepukaje kupunguza mwendo? Ili kujibu, acheni tufikirie kielelezo ambacho Yesu alituachia.

      Fuata Kielelezo cha Yesu

      Yesu alikabiliwa na hali nyingi ngumu. Alilazimika kushughulika na mahitilafiano ya nyutu miongoni mwa wafuasi wake, na pia kuvumilia chuki na dhihaka ya adui zake. Pia alilazimika kukinza vishawishi vya ulimwengu huu. Kwa kweli, yeye alitolewa utajiri na umashuhuri kwa kadiri ambayo ni wachache wamepata kuwa nao. (Mathayo 4:8-11; Yohana 6:14, 15) Hata hivyo, Yesu alidumu kutembea katika ukweli. Ni nini kilichomsaidia kufanya hivyo?

      Mtume Paulo atuambia aandikapo hivi: “Acheni sisi tukimbie kwa uvumilivu katika shindano la mbio ambalo limewekwa mbele yetu sisi, tunapotazama kwa mkazo sana Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu. Kwa sababu ya shangwe ambayo iliwekwa mbele yake yeye alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na amekaa kwenye mkono wa kulia wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Waebrania 12:1, 2, NW) Katika kisa cha Yesu, kukumbuka “shangwe iliyowekwa mbele yake,” thawabu za hali ya juu zilizomngojea, kulimsaidia Yesu aendelee kutembea katika ukweli. Hii “shangwe iliyowekwa mbele yake” ilizidi kwa mbali vivunja-moyo au vikengeusha-fikira vya muda alivyolazimika kukabiliana navyo.

      Kuikumbuka thawabu kwaweza kutusaidia tuvumilie, kama vile kulivyomsaidia Yesu. (Ufunuo 22:12) Kutoa kielezi, fikiria msafiri anayetembea katika kijia cha mlimani chenye kumtatiza. Achoka na kuvunjika moyo. Kila hatua ni jitihada, na kijia hicho chaonekana kuwa kisicho na mwisho. Halafu yuaja kwenye kilele cha mwinuko na kuona kule mbali mji anakoelekea. Kwa ghafula mwendo waonekana kuwa rahisi kidogo. Kuona wazi mahali anakoenda kwamsaidia kusahau uchovu wake. Vivyo hivyo Mkristo ataona ikiwa rahisi zaidi kutembea katika ukweli akikumbuka waziwazi anakoelekea.

      Mwige Mtume Paulo

      Mwingine aliyevumilia mengi ambayo yangaliweza kumvunja moyo alikuwa ni mtume Paulo. Alilazimika kushughulika na migawanyiko na mahitilafiano ya utu miongoni mwa akina ndugu, na pia kuchukuliana na tatizo kali la afya, mnyanyaso, magumu ya kimwili, na matatizo na hata upinzani ndani ya makundi. (1 Wakorintho 1:10; 2 Wakorintho 10:7-12; 11:21-29; 12:7-10) Kwa nini Paulo hakuvunjika moyo kufikia hatua ya kuacha? Yeye aeleza hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Wafilipi 4:13) Hakujaribu kubeba mizigo yake peke yake. Bali, Paulo alimtegemea Yehova ili amtegemeze.—Zaburi 55:22.

      Chanzo cha kimungu cha imara ambacho Paulo alikitegemea kimsaidie kuvumilia kipo leo pia. Biblia husema: “[Yehova] huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. Haya vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao BWANA [Yehova, NW] watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.” (Isaya 40:29-31) Tukimtegemea Yehova atupe imara kupitia funzo la kibinafsi, hudhurio la mikutano, utendaji wa Kikristo wenye bidii, na—hasa—sala, tutaweza kuvumilia vishawishi na vivunja-moyo ambavyo huenda vikatokea mara kwa mara.—Zaburi 1:1-3; Warumi 10:10; 1 Wathesalonike 5:16, 17; Waebrania 10:23-25.

      Mamilioni Wajitayarisha Kuishi Katika Paradiso

      Shetani ndiye mungu wa mfumo huu wa mambo, ambamo kwa kweli Wakristo ni wageni tu, wakaaji wasio wenyeji. (2 Wakorintho 4:4) Kwa sababu hiyo, haitupasi kushangaa ikiwa nyakati fulani twakabili vivunja-moyo au vikengeusha-fikira. Paulo aliandika katika kitabu cha Waebrania: “Hapa hatuna mji udumuo, bali twautafuta ule ujao.” (Waebrania 13:14) Kukumbuka kwamba tumaini letu halimo katika ulimwengu huu wa zamani bali katika ule ujao kwaweza pia kutusaidia tusipunguze mwendo.

      Kwa njia fulani-fulani, Wakristo ni kama wahamaji ambao huondoka kwenye bara la uenyeji wao kwa kutafuta maisha bora mahali pengine. Kwa kawaida, hiyo ni hatua ngumu kuchukua. Yahusisha kufunga virago au kutupilia mbali mali zake zote na kuacha nyumba aliyozoelea, na pia marafiki na watu wa ukoo. Yahusisha pia kwenda kwenye bara la kigeni, kuishi miongoni mwa watu ambao huenda wasimkaribishe, na kujifunza lugha mpya na njia ya maisha asiyozoea. Hata hivyo, wengi hufanya mhamo huo kwa matumaini ya kuendeleza hali yao ya vitu vya kimwili tu katika ulimwengu huu.

      Wale wanaotenda kana kwamba wanahama kutoka mfumo huu wa kale wa mambo na kuwa sehemu ya watu wa Mungu hukabili matatizo hayo. Wao hufanya marekebisho ya kitamaduni ili waishi kulingana na viwango safi vya Neno la Mungu, na hujifunza “lugha iliyo safi” ya ukweli. (Sefania 3:9; 1 Wakorintho 6:9-11) Hufanya kazi kwa bidii, pia, ili kutumikia yule Mfalme mkubwa wa Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo. Zaidi ya hilo, katika visa vingi watu wa ukoo wao na waliokuwa marafiki hapo kwanza huwakatilia mbali, hivi kwamba kikweli, wao huwaambia wabaki salama.

      Lakini Wakristo wana faida nyingi zaidi za kupata kuliko wale wahamao kwa sababu za kiuchumi. Kwanza, wao huingia katika jumuiya iwapendayo na kuwajali. (Luka 18:29, 30) La maana zaidi, wao huingia katika uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, Mungu wa ulimwengu wote mzima. Wao hupata amani ya akili na uhakika juu ya wakati ujao watazamapo mbele kwenye utimizo wa ahadi nzuri sana za Mungu. (Wafilipi 4:8, 9) Wale walio na uthamini ufaao wa mambo haya ya uhakika hawataruhusu vikengeusha-fikira au vivunja-moyo viwapunguzie mwendo daima. Hawatageuziwa kando watoke kwenye ile barabara nyembamba iongozayo kwenye uhai.—Mathayo 7:13, 14; 1 Yohana 2:15-17.

      Tunza Afya Yako ya Kiroho

      Tukitunza afya yetu ya kimwili kwa ukawaida, tuna nafasi bora ya kukinza magonjwa. Na tukiwa wagonjwa, tutapona haraka zaidi. Vivyo hivyo, tukitunza afya yetu ya kiroho, kuendeleza mwono wa wazi juu ya baraka ambazo twazionea shangwe sasa na zile zitungojazo, na tukijifunza kutegemea imara ya Yehova kuliko yetu wenyewe, tutakuwa katika hali bora ya kushughulika na matatizo yatokeayo. Hatuwezi kuepuka kabisa vikengeusha-fikira au hali zenye kuvunja moyo. Lakini ikiwa tumetunza mapema afya yetu ya kiroho kwa njia ifaayo, mambo hayo hayatatulemea.

      Kumbuka, Yehova hushangilia wakati waabudu wake wavumiliapo. Kwa hiyo acheni tulete shangwe kwenye moyo wake kwa kuendelea kutembea katika ukweli.

  • Mkutano wa Kila Mwaka—Oktoba 6, 1990
    Mnara wa Mlinzi—1990 | Septemba 1
    • Mkutano wa Kila Mwaka—Oktoba 6, 1990

      MKUTANO WA KILA MWAKA wa washiriki wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania utafanywa mnamo Oktoba 6, 1990, kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, 2932 Kennedy Boulevard, Jersey City, New Jersey. Mkutano wa utangulizi wa washiriki peke yao utafanywa saa 3:30 asubuhi, ukifuatwa na ule mkutano wa ujumla wa kila mwaka saa 4 asubuhi.

      Washiriki wa Shirika hilo wapaswa kuijulisha Ofisi ya Mwandishi sasa juu ya badiliko lolote lililotokea mwaka uliopita katika anwani zao za barua ili barua zile za kawaida za ujulisho na uwakilishi ziweze kuwafikia muda mfupi baada ya Agosti 15.

      Barua za uwakilishi, watakazopelekewa washiriki pamoja na arifa ya mkutano wa kila mwaka, zinapasa kurudishwa ili ziifikie Ofisi ya Mwandishi wa Sosaiti si baada ya Septemba 1. Kila mshiriki apaswa ajaze mambo yote yaliyo katika barua ya uwakilishi na kuirudisha haraka, akitaarifu kama atakuwapo ama hatakuwapo mkutanoni yeye binafsi. Habari zenye kutajwa katika kila barua ya uwakilishi zapasa kusema jambo hilo waziwazi, kwa kuwa ndizo zitakazotegemewa katika kujua ni akina nani watakaokuwapo binafsi.

      Inatarajiwa kwamba kipindi kizima, kutia ndani mkutano ule rasmi wa kishughuli na ripoti mbalimbali, kitamalizwa ifikapo saa 7:00 alasiri au muda mfupi baada ya hapo. Hakutakuwa na kipindi cha alasiri. Kwa sababu nafasi ni ndogo, itawezekana kuingia kwa kuwa na tiketi tu. Hakutakuwa na mipango ya kuunganisha mahali pengine-pengine kwa kamba za simu ili kuusikia mkutano wa kila mwaka.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki