Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kusitawisha Adabu za Kikristo Katika Ulimwengu Usio na Adabu
    Mnara wa Mlinzi—1989 | Juni 15
    • Kusitawisha Adabu za Kikristo Katika Ulimwengu Usio na Adabu

      “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”​—ZABURI 133:1.

      1. Adabu zimepatwa na nini?

      ADABU zimeharibiwa sana miaka hii 25 iliyopita,” anasema mchangaji habari katika safu za magazeti, Ann Landers. “Si kwamba tu wanaume hawafanyii wanawake hisani ya kuwafungulia milango ya gari au kuwapa viti katika mabasi. Ni zaidi ya hilo.” Kweli kweli, kila mahali tunapotazama, tunaweza kuona ushuhuda wa kwamba tunaishi katika ulimwengu unaozidi kukosa adabu. Watu hujisukuma mbele katika mistari, wanavuta sigareti katika vipandisha-ghorofani vilivyosongamana watu, wanafungulia sauti kubwa ya muziki wakiwa katika hadhara ya watu, na kadhalika. Tunayojionea kila siku yanatuambia kwamba ijapokuwa fursa za elimu na kiwango cha maisha kimepata maendeleo, kwa kadiri kubwa kipindi hiki chetu ni muda ambamo Asante na Tafadhali yamekuwa maneno ya kigeni, na hisani na uungwana wa kawaida umesahauliwa sana.

      2. Kwa nini haishangazi kwamba leo hakuna adabu?

      2 Je! yote haya yanashangaza? Sivyo hasa. Yanatukumbusha tu yale ambayo mtume Paulo alivuviwa kusema juu ya mwenendo wa watu katika “siku za mwisho” ambapo ‘nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zingekuwapo.’ Miongoni mwa mambo mengine, Paulo alitabiri kwamba watu wangekuwa “wajipenda wenyewe, . . . wenye kimbelembele, wenye kujigamba, . . . wasio na shukrani, . . . wasio na shauku ya asili, . . . bila kujiweza.” (2 Timotheo 3:1-3, NW) Hata mtazamo wa kijuujuu tu utafunua kwamba mwenendo huo umeenea sana leo miongoni mwa watu wa kila umri, cheo, na utaifa. Kwa nini iko hivyo? Ni visababishi gani vinavyochangia ukosefu wa ujumla wa adabu?

      Visababishi vya Ukosefu wa Adabu

      3. “Hewa” ya mfumo huu inaendelezaje ukosefu wa adabu?

      3 Maneno “wajipenda wenyewe” yanaeleza vema juu ya “kizazi cha umimi,” hiyo ikimaanisha wale ambao wamelelewa kwa kukazania mambo yao wenyewe, kujijali wenyewe tu, na kutoa maoni yao wenyewe. Roho hii, ambayo inaenea sana katika “hewa” inayotuzunguka, inapingana moja kwa moja na shauri la Biblia kwamba Wakristo wasiwe ‘wakiangalia mambo yao wenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’ (Waefeso 2:2, 3, NW; Wafilipi 2:4, UV) Tokeo ni nini? Ni kwamba kizazi kilicholelewa kikiwa na wazo la ‘fanya lako mwenyewe’ hakika hakitajali sana jinsi mwenendo wao unavyoathiri wengine.

      4. Wale wanaopuuza kabisa viwango vinavyokubaliwa wanaonwaje leo, na maoni ya Mkristo yanapasa kuwa nini juu ya jambo hili?

      4 Jambo moja ambalo hapo kwanza lilihusika sana katika kudumisha kadiri fulani ya uungwana miongoni mwa watu lilikuwa kukazwa na watu wa rika moja. Kuhangaikia vile wengine huenda wakafikiri kumekuwa kani yenye uzuizi kwa muda mrefu. Leo, hata hivyo, kadiri ambavyo mwendo wa kitendo fulani unazidi kushtua watu na kunenewa sana, ndivyo utakavyoelekea kupendwa zaidi na watu wengi. Wale wanaopuuza viwango vinavyokubaliwa hawaonwi tena kuwa wakosa adabu wala washenzi bali wamamboleo au wasofisti (waerevukaji), watu wa kusifika sana. Ingawa hivyo, kumbuka kwamba ‘kuwa msofisti’ kunamaanisha ‘kuwa katika hali isiyo ya kikawaida, isiyotakata, au isiyo ya kiasili.’ Neno hilo limetoka kwenye shina moja la Kigiriki kama neno lililofasiriwa “zilizotungwa kwa werevu” kwenye 2 Petro 1:16. Kwa uhakika, itakuwa vema Wakristo wa kweli waepuke kabisa mwelekeo huo.

      5. Ni jambo gani jingine linalochangia kufa kwa adabu?

      5 “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya,” inasema Mhubiri 8:11. Humo mna jambo jingine linalochangia ukosefu mkubwa wa adabu peupe. Kwa sababu watu wanaona ni rahisi sana kuponyoka wanapofanya mabaya, wanakauka hisia mpaka wanaona si kitu kuvunja viwango vinavyokubaliwa vya mwenendo. “Raia ambao wangeshtuka sana kutambulishwa peupe kuwa wahusika katika uhalifu wamekuwa hata hivyo wakichangamka wanapovunja peupe namna zote za sheria​—sheria za barabarani, sheria zinazohusu dawa za kulevya, sheria za kutotupa takataka ovyoovyo,” inasema makala ya mhariri ya New York Times. Tokeo ni kwamba, “ghasia, kuharibu-haribu mali za watu bila sababu na kuharibu sura ya mahali kwa kuandika-andika maneno ovyo tu” kumekuwa sehemu isiyoepukika ya matukio ya kila siku. Hivyo, uungwana, pamoja na kustahi haki za watu wengine, mali zao, na ufaragha wao, unazuiliwa na vipingamizi zaidi.

      6. Adabu za watu zinaathiriwaje na maisha zao zenye shughuli nyingi, na Yesu alikuwaje tofauti katika jambo hili?

      6 Kwa kuwa adabu kwa ujumla huonwa kuwa miongoni mwa maungwana yale madogo-madogo maishani, huwa zinasahauliwa kwa urahisi watu wanapokuwa katika haraka​—na siku hizi watu walio wengi huonekana kuwa wenye haraka wakati mwingi. Tokeo ni kwamba, wao hupitana bila hata salamu wala tabasamu yoyote usoni. Wao hupiga wengine kikumbo au kuwasukuma katika mistari, au wanakatiza mbele kwa kuingia na kutoka katika mistari yao ya barabarani ili waokoe dakika au nukta chache tu. Mara nyingi, watu hujishughulisha sana na mambo yao binafsi, au ratiba zao zinakuwa zimejaa sana mambo ya kufanya, hivi kwamba tukio lolote au mgeni asiyetazamiwa anaonwa kuwa udhia au kikatiza-shughuli. Fikiria jinsi jambo hili linavyotofautiana na vile Yesu alivyowaitikia watu waliomjia hata nyakati asipokuwa na nafasi.​—Marko 7:24-30; Luka 9:10, 11; 18:15, 16; Yohana 4:5-26.

      7. Ni lazima Wakristo wa kweli walinde dhidi ya nini kwa habari ya adabu?

      7 Hata ingawa tunaishi katika ulimwengu wa mbio-mbio, na mambo yanayodai wakati na nishati zetu yanaongezeka daima, kuruhusu mikazo hiyo isababishe tutende kwa ufidhuli hakika hakutafanya mambo yawe afadhali. Kinyume cha hivyo, mwendo huo huongoza kwenye kadiri kubwa sana ya jeuri isiyo ya kiakili tunayosikia habari zayo​—mabishano, mapigano, mizozano mikali sana, hata mauaji​—yenye kutokea kwa sababu watu wanarudishiana ufidhuli kwa ufidhuli. Yote haya ni sehemu ya roho ya ulimwengu ambao ni lazima Wakristo wa kweli wawe si sehemu yao.​—Yohana 17:14; Yakobo 3:14-16.

      Violezo Bora vya Adabu

      8. Ingawa wamezungukwa na watu wasio na adabu,Wakristo wanatiwa moyo wafanye nini?

      8 Tukiwa tumezungukwa na watu wasioonyesha kujali sana wengine, ni rahisi kujiacha tushindwe na mikazo na kuacha adabu zituponyoke. Hata hivyo, kukumbuka shauri la Biblia ‘kuacha kufanyizwa kulingana na mtindo wa huu mfumo wa mambo,’ tunaweza kuvitegemea vielelezo vingi vya kutokeza vilivyo katika Biblia na kujitahidi kuunga mkono viwango vya juu vya adabu za Kikristo katika ulimwengu wa leo usio na adabu. (Warumi 12:2, 21, NW; Mathayo 5:16) Vitendo vyetu vinapasa kuonyesha kwamba tunakubaliana kwa moyo wote na mtunga zaburi aliyetangaza hivi: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”​—Zaburi 133:1.

      9. Maandiko yanafunua nini juu ya njia ya Yehova ya kushughulika na watu?

      9 Kielelezo bora zaidi katika kuonyesha adabu ni Muumba na Baba ya wote, Yehova Mungu mwenyewe. Ni jambo la kawaida wale walio katika vyeo vya juu au walio na mamlaka juu ya wengine ‘kuenda-enda kwa mabavu na kifua’ na kudai kwamba matakwa yao yaheshimiwe. Hata hivyo, Mtu aliye juu zaidi katika ulimwengu wote mzima, Yehova Mungu, huwa mwenye adabu wakati wote anaposhughulika na wale walio chini yake. Alipokuwa akimpa baraka Abrahamu rafiki yake, yeye alisema hivi: “Inua macho yako, tafadhali, na utazame kutoka mahali ulipo.” Na tena: “Tazama juu, tafadhali, kwenye mbingu na uzihesabu nyota.” (Mwanzo 13:14; 15:5, NW) Alipokuwa akimpa Musa ishara ya nguvu Zake, Mungu alisema: “Ingiza mkono wako ndani ya kunjo la juu la vazi lako, tafadhali.” (Kutoka 4:6, NW) Miaka mingi baadaye, Yehova, kupitia Mika mnabii wake, alisema hivi hata kwa watu wake waliokengeuka: “Sikieni, tafadhali, nyinyi vichwa vya Yakobo na nyinyi maamiri wa nyumba ya Israeli. . . . Sikieni, tafadhali, jambo hili, nyinyi mlio vichwa.” (Mika 3:1, 9, NW) Katika jambo hili, je! sisi ‘tumekuwa waigaji wa Mungu’ katika kusema “Tafadhali” tunaposhughulika na wengine?​—Waefeso 5:1, NW.

      10, 11. (a) Inaweza kusemwa nini juu ya njia za Yesu na adabu zake? (b) Tunaweza kuigaje Yesu katika kuwa wenye adabu kuelekea watu wote?

      10 Yesu Kristo, yule “aliye katika kifua cha Baba,” ni kielelezo kingine cha kutokeza kinachostahili kuigwa. (Yohana 1:18) Katika kushughulika na watu, kwa upande mmoja yeye alikuwa mwenye upole mwororo na huruma, na kwa upande ule mwingine alikuwa mwenye mkazo mwingi na imara; hata hivyo hakuwa mfidhuli au mkosa fadhili kwa mtu yeyote. Kikieleza juu ya “kipawa chake cha ajabu cha kustareheka pamoja na watu wa namna zote,” kitabu The Man From Nazareth kinasema: “Peupe na hali kadhalika faraghani yeye alishirikiana na wanaume na wanawake kwa usawa. Alihisi akiwa amestareheka sana alipokuwa na watoto wadogo wasio na mengi sana, na hata ni ajabu kwamba alihisi amestareheka sana akiwa pamoja na wanyonya-mali wenye kusumbuliwa na dhamiri kama Zakayo. Wanawake watunza-nyumba walio wastahiwa, kama Maria na Martha, wangeweza kuongea naye kwa kumtobolea mambo wazi, lakini malaya maarufu pia walimwendea kana kwamba wakiwa na uhakikisho wa kwamba angewaelewa na kuwaonyesha urafiki . . . Kutojali kwake mipaka iliyowatenga kando watu wa kikawaida ni moja ya sifa za utu wake.”

      11 Kutendea kila mtu kwa staha na ufikirio unaofaa ndiyo ishara ya mtu mwenye adabu kweli kweli, na ingekuwa vema sisi tuige Yesu Kristo katika jambo hili. Ndiyo, watu walio wengi huweza kuwa wenye staha kwa watu fulani, hasa wale walio katika vyeo vya juu kuliko wao. Lakini mara nyingi wao hujitenga mbali na wale wanaowafikiria kuwa wa chini au hata wa kiwango kimoja nao, wanahusiana nao kwa umbali na kuwa wafidhuli. Kwa njia fulani hiyo inaonekana kama inawapa hisia ya ukubwa zaidi na mamlaka. Lakini imesemwa vema kwamba “ufidhuli ni kisingizio cha mtu mnyonge kwamba ana nguvu.” Hivyo, Biblia inahimiza hivi: “Katika kuonyeshana heshima, iweni wa kwanza.” (Warumi 12:10, NW) Tukifanya yote tuwezayo kufuata ushauri huo, hatutakuwa mbali katika kuwa wenye adabu kuelekea watu wote, kama Yesu alivyokuwa.

      12. Ni nini hasa maana ya fundisho la Yesu kuhusu mahusiano ya kibinadamu?

      12 Sifa hii ya mwelekeo chanya, yenye kutokeza nje-nje ili kufikia watu inawekewa kielelezo pia katika mafundisho ya Yesu, hasa katika ile inayoitwa Kanuni Bora Sana: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kwa kupendeza, katika kitabu Analects, kimoja cha Four Books (Vitabu Vinne) vya Confucius​—ambavyo kwa muda mrefu vimeitwa kipeo cha mwenendo wa kiadili katika Masharikio​—bwana-mkubwa aliulizwa na mmoja wa wanafunzi wake kama kulikuwako neno moja tu ambalo lingeweza kutumika kuwa kanuni ya mwenendo maishani. “Labda neno ‘kutendeana’ (shu) litatosha,” akajibu mwalimu, halafu akaongezea hivi: “Usiwatende wengine jambo ambalo hutaki wengine wakutende wewe.” Kwa kinyume, sisi tunaweza kuona kwa urahisi ubora mkubwa zaidi wa fundisho la Yesu. Kwa maana mahusiano ya uchangamfu, yenye ufurahishi mwingi, na ya kirafiki yanaweza kutokea wakati tu mtu anapochukua hatua ya kwanza ‘kutendea wengine’ lililo jema.

      Adabu za Kikristo Zenye Kutegemea Upendo wa Kikristo

      13, 14. (a) Ni jambo gani limeonwa hivi majuzi juu ya adabu za peupe? (b) Ni nini kinachosukuma upendezi wa sasa katika adabu na kanuni za maungwana?

      13 Kwa sababu ukosefu wa adabu umeenea sana, leo hatua ya kurudisha mwenendo unaofaa inatajwa-tajwa. “Tulikuwa na maasi dhidi ya adabu katika miaka ya 60,” anasema Marjabelle Stewart, mwandikaji na mwalimu anayejulikana sana kuhusu habari hiyo, “lakini badiliko kubwa jipya linazirudisha. Watu wanakiri kwamba ni za maana na wanataka kujua ni nini viwango vya kijamii.” Huku kupendezwa upya na adabu kunaonyeshwa katika ongezeko kubwa la vitabu, majarida, safu za ushauri katika magazeti, na maonyesho ya maongezi ya televisheni kuhusu kila jambo tangu uma inayopasa kutumiwa kwenye mlo rasmi hadi jinsi ya kusema na mtu katika mahusiano ya leo ya kijamii na kijamaa ambayo yanatatanisha na kubadilika haraka sana.

      14 Ingawa hivyo, ni kwa nini watu fulani wanazidi kuona uhitaji wa kuwa na adabu? “Katika jamii ya leo yenye mashindano,” anaeleza Stewart, “adabu ni njia ya kuendeleza maisha tu.” Ndiyo kusema, adabu zinaonwa kuwa njia ya kusaidia mtu aweze kuendelea na maisha na kupata mafanikio zaidi. Kwa hiyo watu wanasoma vitabu na kuhudhuria madarasa yanayohusu kanuni za maungwana ili wajifunze jinsi ya kuvaa kwa njia itakayoleta mafanikio, jinsi ya kufanya wengine wavutiwe nao, jinsi ya kukubaliwa barazani, na kadhalika.a Tatizo la yote haya ni kwamba adabu zimekuwa jambo la kufanywa kwa faida ya kibinafsi tu, kama kibandiko cha usoni ambacho mtu anavaa wakati wa mwigizo na kukivua uishapo. Kwa hiyo, si ajabu kwamba tunasikia tena na tena juu ya uhalifu wa kushtusha sana unaotendwa kiofisaa na watu wenye ‘malezi’ na ‘cheo’ bora zaidi.

      15, 16. (a) Mtungaji mmoja wa habari zinazohusu adabu anasema nini juu ya “sheria zilizo bora zaidi za mwenendo”? (b) Ni jinsi gani 1 Wakorintho 13:4-7 inavyohusiana na adabu za kweli za Kikristo?

      15 Hiyo ni tofauti sana na jinsi adabu zinavyopasa kuwa. Amy Vanderbilt, mtungaji wa kike anayestahiwa kuhusu habari hii, anaandika hivi katika kitabu chake New Complete Book of Etiquette: “Sheria zilizo bora zaidi za mwenendo zinapatikana katika Sura ya 13 ya Wakorintho wa Kwanza, ule usimulizi mrefu wa kupendeza uliotolewa na Mtakatifu Paulo kuhusu ufadhili. Sheria hizi hazihusiani hata kidogo na unadhifu wa kuvaa wala hazihusiani na adabu za kijuu-juu. Zinahusiana na hisia na mielekeo, hali ya kuonyesha fadhili, na ufikirio kwa wengine.”

      16 Bila shaka, kile ambacho Amy Vanderbilt alimaanisha ni kifungu kilicho kwenye 1 Wakorintho 13:4-7, NW, ambapo Paulo anaeleza kirefu sehemu mbalimbali za upendo wa Kikristo. Fikiria matokeo ya mambo machache aliyotaja. Kwa kielelezo, mtu aliye ‘mstahimilivu na mfadhili’ hakika atakuwa mwenye saburi na staha katika kushughulika na wengine. “Haujiendeshi kwa kukosa ustahifu” ni njia nyingine ya kusema “hujiendesha kwa ustahifu,” na “ustahifu” unaelezwa kuwa ni “kujipatanisha na viwango vya hali inayopendeza, ufaaji, au ubora.” Hivyo, kama vile New Testament in Modern English ya J. B. Phillips inavyofasiri kifungu hiki kifupi, “Upendo una adabu.” Ni vigumu kuwazia mtu yeyote mwenye kudhihirisha upendo huo akichukuliwa kuwa mkosa adabu.

      17. Adabu zetu ni kionyeshi cha nini?

      17 Basi, ni wazi kwamba adabu za Kikristo zinahusiana na upendo wa Kikristo. Si njia ya kufikia lengo fulani tu wala si kitu cha kuvaliwa wakati tu mtu anapopata faida kwa kufanya hivyo. Bali, adabu zetu​—jinsi tunavyoshughulika na wengine, jinsi tunavyojichukua, tunavyojiendesha, na jinsi mwenendo wetu ulivyo kwa kawaida​—zinaonyesha kadiri ambayo tunawajali wengine na kina cha upendo wetu kwao. Kama sisi ni vijana au wazee, inatupasa tujitahidi kutii shauri la Biblia: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.” (1 Wakorintho 10:24) Hivyo, adabu za Kikristo, ambazo ni sehemu moja ya upendo wa Kikristo, ni alama ya kutambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.​—Yohana 13:35.

      Wenye Adabu Nyakati Zote

      18. Inatupasa tuazimie kufanya nini tujapoona mambo yanayotuzunguka?

      18 Kuhusu kizazi chetu, Yesu alitabiri kwamba “kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12, NW) Huku kupoa kwa upendo kunaonyeshwa wazi katika mwelekeo wa kutojali na kujijali binafsi kwa upande wa watu wengi sana leo. Hata hivyo, badala ya sisi kushawishika tutende kwa namna iyo hiyo ya kutojali, tunahitaji kuzingatia akilini shauri la Paulo: “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni [andaeni, NW] yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” (Warumi 12:17, 18) Linapasa kuwa azimio letu kuwa wenye adabu nyakati zote, kama jitihada zetu zinathaminiwa au hazithaminiwi.​—Mathayo 5:43-47.

      19. Adabu zetu zinaathirije sehemu zote za maisha?

      19 Ndiyo, adabu za Kikristo ndio wonyesho asilia wa kinje-nje wa upendo na hangaikio ambalo sisi tunalo kwa wengine katika moyo wetu. Kama vile uneni wetu unavyofunua jinsi tulivyo kwa ndani, ndivyo adabu zetu pia zinavyoonyesha jinsi tunavyojali wengine au kama hatujali. (Mathayo 12:34, 35) Kwa kuwa ndivyo ilivyo, adabu zinapasa kuwa na fungu la maana katika sehemu zote za maisha yetu. Zinapasa kuwa njia ya maisha. Zinapasa kutumiwaje kwa ukamili zaidi? Adabu za Kikristo zinazofaa zinaweza kusitawishwaje kwa ukamili zaidi? Tutafikiria jambo hili katika makala inayofuata.

  • “Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”
    Mnara wa Mlinzi—1989 | Juni 15
    • “Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”

      “Ila tu jiendesheni kwa namna inayozistahili habari njema juu ya Kristo.”​—WAFILIPI 1:27, NW.

      1. Tukio moja hivi majuzi katika Jiji la New York lilifanya meya atoe sifa gani? (Warumi 13:3)

      “Zaidi ya Mashahidi 1,000” walikuja kwenye Jumba la Jiji katika Manhattan siku ya Septemba 29, 1988, ikaripoti The New York Times. Walikuja kuunga mkono pendekezo la ujenzi lililokuwa likisikizwa mbele ya Baraza la Makadirio la jiji hilo. Ingawa pendekezo la kuruhusu kujengwa kwa kao jipya kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova lilikataliwa, meya “alisifu Mashahidi kuwa ‘watu wanyofu kabisa’ na akasema walikuwa ‘wa kusifika kweli kweli.’”

      2. Adabu za Mashahidi ni tofauti jinsi gani, na kwa nini?

      2 Kwa kawaida, watu zaidi ya elfu moja wanapokuja pamoja kuonyesha wanaunga mkono kusudi fulani lisilopendwa na wengi, ni jambo gani linaloweza kutazamiwa? Kwa kawaida kunakuwako kusukumana, kupiga makelele, hata kutumia nguvu na jeuri halisi. Kwa nini Mashahidi ni tofauti? Ni kwa sababu wanatambua kwamba nyakati zote mwenendo wao unaonyesha jinsi imani yao ilivyo. Wao wanalikumbuka vema shauri la Kimaandiko: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”​—1 Petro 2:12.

      Adabu Hutukuza Yehova

      3. Adabu zetu zinatimiza fungu gani katika kuheshimu Yehova?

      3 Ni wazi kwamba kutukuza Yehova Mungu kwa mwenendo mwema ni sehemu ya daraka letu la Kikristo. (Mathayo 5:16) Bila shaka, mwenendo mwema ni kutia ndani mambo mengi​—kwa kielelezo, ufuataji haki, bidii nyendelevu, na maadili mema. Hata hivyo, sifa hizi kwa kawaida huthaminiwa na wale tu wanaotujua vema au wale tunaoshughulika nao kwa ukawaida, kama rafiki zetu, watu wa ukoo, waajiri, wafanya kazi wenzetu, na walimu. Namna gani watu walio wengi zaidi tunaoonana nao hivi hivi tu? Hapa hasa ndipo adabu zetu zinapohitajiwa. Kwa maana kama vile karatasi ya kuvutia iliyofungiliwa kwenye zawadi ya thamani inavyoipa upendezi mwingi, adabu zinafanya kile tunachotolea watu kiwe na upendezi mwingi. Hata tuwe tuna sifa gani nyingine za Kikristo au tuwe tuna makusudio ya kusifika kama nini, hayatakuwa na matokeo mengi ikiwa hatuna adabu. Kwa hiyo adabu zetu zinaweza kumleteaje Yehova utukufu?

      4. Inatupasa tuangalie adabu zetu katika maeneo gani ya maisha?

      4 “Ila tu jiendesheni kwa namna inayozistahili habari njema,” anasema Paulo. (Wafilipi 1:27, NW) Bila shaka, hii inatia ndani huduma yetu ya peupe. Lakini mwenendo na adabu zetu kwenye mahali petu pa ibada, katika ujirani wetu, kazini, shuleni, ndiyo, katika kila upande wa maisha zetu, zinahusika moja kwa moja pia katika matokeo ya huduma yetu. “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe,” anaandika Paulo. (2 Wakorintho 6:3) Sisi tunaweza kuhakikishaje kwamba tunatumia shauri hilo? Tunaweza kufanya nini tusaidiane sisi kwa sisi, hasa kuwasaidia wachanga walio miongoni mwetu, waonyeshe adabu za Kikristo nyakati zote?

      Kwenye Jumba la Ufalme

      5. Inatupasa tutambue nini tunapokuwa kwenye Jumba la Ufalme?

      5 Jumba la Ufalme ni mahali petu pa ibada. Tunakuwa hapo kwa kualikwa na Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Katika maana hiyo, sisi ni wageni kwenye nyumba ya Yehova. (Zaburi 15:1; Mathayo 18:20) Je! wewe ni mgeni mwema unapokuja kwenye Jumba la Ufalme? Ili tuwe hivyo, ni lazima tuonyeshe ufikirio na staha inayofaa si kwa mkaribishaji tu bali pia kwa wageni wale wengine. Hiyo inahusisha nini ndani?

      6. (a) Kuchelewa mikutano nyakati zote kunaonyesha ukosefu wa nini? (b) Ni jambo gani linaweza kufanywa ili kushinda tatizo hili?

      6 Kwanza, kuna lile jambo la kufika katika wakati unaofaa. Inakubaliwa kwamba si rahisi sikuzote kufanya hivyo. Watu fulani huishi mbali; wengine wana jamaa na watoto wa kutayarisha. Jitihada wanayofanya kuja kwenye mikutano ya Kikristo kwa ukawaida inastahili pongezi kweli kweli. Hata hivyo, imeonwa kwamba watu fulani wameangukia tabia ya kufika mikutanoni wakiwa wamechelewa. Wanaweza kufanya nini warekebishe jambo hili? Kwanza ni lazima mtu atambue kwamba si sikuzote ambapo tabia ya kuchelewa kwenye mikutano ya Kikristo huonyesha kutothamini ubora wa mikutano. Watu fulani wanaochelewa-chelewa huonekana wakiionea​—shangwe mikutano sawasawa na mtu mwingine yeyote​—mara wakiisha kufika pale. Lakini ilivyo ni kwamba, huenda tatizo likatokana na mipango mibaya na kutofikiria Wakristo wenzao. Moja ya sababu tunazoshauriwa ‘tusiache kukusanyika pamoja’ ni ili tupate ‘kuangaliana na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri.’ (Waebrania 10:24, 25) Ni vigumu kufanya hivyo ikiwa sisi hufika tumechelewa, muda baada ya muda, na hivyo kuvuta kando fikira za wengine au kuwasumbua. Walio wastadi wanapendekeza kwamba, ili tusichelewe, inatupasa tufike mapema vya kutosha badala ya kufika pale wakati ule ule uliowekwa. Je! wewe unahitaji kujizoeza jambo hili?

      7. Eleza usikizi kwenye mikutano unahusianaje na adabu.

      7 Adabu zinataka kwamba tuelekezee watu usikizi wetu wanaponena nasi. (Mithali 4:1, 20) Hii inatumika pia kwa mikutano ya Kikristo, ambapo wahudumu wa Mungu wananena ili kutupa sisi zawadi fulani ya kiroho ili kutujenga. Ungekuwa wonyesho wa ukosefu mkubwa sana wa adabu kwa upande wetu kama tungesinzia-sinzia, tumnong’oneze-nong’oneze aliyeketi karibu nasi, tutafune-tafune gamu au vitu vya aina ya peremende, tusome mambo mengine, au tushughulikie mambo mengine wakati wa mkutano. Kijana Elihu hakuketi kwa saburi tu muda wote wa zile hotuba ndefu zilizotolewa na Ayubu na wale waandamani watatu, bali pia ‘aliendelea kutega sikio’ kwa waliyosema na ‘akaendelea kuwageuzia usikizi wake.’ (Ayubu 32:11, 12, NW) Adabu za Kikristo zitatusukuma tuonyeshe staha inayofaa kwa mnenaji na ujumbe wake wenye msingi wa Biblia kwa kumpa usikizi na kumuunga mkono kwa njia isiyogawanyika.

      8. Tunaonyeshaje kwamba sisi ni wanafunzi wenzi wa Yesu Kristo?

      8 Kabla na baada ya mikutano, adabu za Kikristo zinatia ndani kupendezwa kwa bidii na wengine waliopo penye Jumba la Ufalme. Paulo aliona kwamba washiriki wapakwa mafuta wa kundi la Kikristo ‘sasa si wageni wala wapitaji, bali ni watu [washiriki, AW] wa nyumbani mwake Mungu.’ (Waefeso 2:19) Je! wewe unatendea Mashahidi wenzako kama watu usiowajua na kama wageni, au kama washiriki wa nyumba ile ile moja? Salamu ya kirafiki, kuwatikisa mkono kwa uchangamfu, tabasamu yenye fadhili​—labda yote hayo ni mambo madogo, lakini ni sehemu ya ushuhuda wa kwamba sisi ni wanafunzi wenzi wa Yesu Kristo. Ikiwa sisi hufanya fadhili hizo tunapokuta watu tusiowajua, je! hatupaswi kufanya hivyo “hasa kuelekea wale wanaohusiana nasi katika imani”?​—Wagalatia 6:10, NW.

      9. Watoto wanaweza kufundishwaje kuonyesha upendezi katika watu wengine zaidi ya wale wa umri wao wenyewe?

      9 Je! watoto wanaweza kufundishwa kuonyesha upendezi wa aina hii katika watu wasio wa umri wao wenyewe? Huenda watu wazima fulani wakahisi kwamba watoto wanahitaji kwenda wakacheze na rafiki zao wadogo baada ya kuketi muda wa saa moja au mbili wakisikiliza kwenye mikutano. Lakini Jumba la Ufalme sipo mahali pa mchezo. (Mhubiri 3:1, 17) Wakati mvulana wa miaka minne na nusu alipoulizwa na mwalimu wake ana ndugu na dada wangapi, yeye alijibu: “Ni wengi sana hata siwezi kuhesabu wote.” Baadaye, wazazi wake walipomuuliza juu ya jambo hili, mvulana huyo alieleza hivi: “Mimi sijui nina ndugu na dada wangapi. Ninapoenda kwenye Jumba la Ufalme, ni wengi sana.” Kwake yeye, wote wanaohudhuria ni ndugu na dada zake.

      Katika Huduma Yetu ya Peupe

      10. Ni agizo gani kutoka kwa Yesu linaloweza kutusaidia ‘tujiendeshe kwa namna inayozistahili habari njema’ tunapokuwa katika huduma yetu?

      10 Bila shaka ‘kujiendesha kwa namna inayozistahili habari njema’ kunahusisha ndani huduma yetu ya peupe. Ni lazima tuzingatie akilini kwamba tuna ujumbe wa amani, na adabu zetu zinapasa kuonyesha kwamba ndivyo ulivyo. (Waefeso 6:15) Agizo kutoka kwa Yesu ni kwamba: “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie.” Kwa kuwa wachangamfu, wenye urafiki, na wenye staha, tunajulisha mwenye nyumba kwamba tunapendezwa naye kikweli moyoni. Ingawa hivyo, nyakati fulani, huenda mtu tunayekuta mlangoni akawa hana urafiki, hata mtaka ugomvi. Je! sisi tutafadhaika na kuanza kujiendesha kwa namna yake? Angalia vile Yesu alivyoendelea kusema: “La, kwamba [nyumba ile ] haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi.” (Mathayo 10:12, 13) Adabu zetu mlangoni zinapasa sikuzote kuistahili “huduma ya upatanisho.”​—2 Wakorintho 5:18, NW.

      11. Kuvalia kwetu na sura ya kibinafsi kunaathirije fungu letu la kuwa wahudumu wa Mungu?

      11 Adabu zetu zinanena juu yetu kwa njia nyinginezo pia. Kwa kielelezo, je! sura yetu ya kibinafsi inalistahili fungu letu tukiwa mhudumu wa Neno la Mungu? Namna gani vifaa tunavyotumia​—mkoba wa vitabu, Biblia, na vitabu vya Kibiblia? Mchangia habari katika gazeti moja anawapa wanakazi ushauri huu: “Valia kikazi, si kwa mtindo wa kuhudhuria karamu, kwa mtindo wa kikusanyiko cha starehe au mchezo fulani.” Kwa nini? Kwa sababu mavazi yako na sura ya kibinafsi “ni njia ya mkato ya kuwaeleza watu wanaokuzunguka wewe ni nani na wewe ni nini na ni mahali gani panapokufaa katika utaratibu wa mambo.” Kwa hiyo tunapoendesha “shughuli” yetu ya kihuduma, mavazi na sura yetu hayapasi kuvaliwa ovyoovyo tu wala kuwa machafu-machafu, wala hayapasi kuwa na uzuri unaochoma macho ya watu wala yenye madoido ya kupita kiasi, bali sikuzote yawe ‘yanazistahili habari njema.’​—Linganisha 1 Timotheo 2:9, 10.

      12. Adabu zinaweza kuonyeshwaje kuhusiana na haki na mali za mwenye nyumba?

      12 Ingawa inatupasa ‘tuwe tayari sikuzote kuzitetea’ habari njema, adabu za Kikristo zinataka kwamba tufanye hivyo “kwa tabia pole ya moyoni na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15, NW) Hiyo inatia ndani kustahi haki na mali za mwenye nyumba. Je! sisi hupanga utendaji wetu ili tuzuru wakati unaomfaa mtu tunayemzuru? Je! tuko chonjo kuangalia kama tunakatiza shughuli au kazi fulani muhimu? Je! sisi ni wakarimu katika kutumia maneno kama “Je! naweza?” “Tafadhali,” na “Asante”? Je! tunajitahidi kuhusisha mwenye nyumba katika maongezi, au sisi tunayatawala kwa kuhofu kwamba huenda tusimalize mambo tuliyojitayarisha kusema?

      13. Toa kielezi juu ya jinsi adabu katika huduma huleta matokeo mema mara nyingi.

      13 Adabu, zikiwa pamoja na hangaikio la kibinafsi lenye moyo mweupe, mara nyingi zinafungua njia ya ushuhuda mwema. Hii ndiyo sababu mara nyingi watoto wenye adabu hupata usikizi na upendezi wa wenye nyumba mahali ambapo huenda watu wazima wakashindwa kufanya hivyo. Shahidi wa miaka 13 katika Meksiko alikuta msichana mchanga aliyetaka kujifunza. Hata hivyo, msichana huyo alisema angelazimika kufanya hivyo bila kujulikana na baba yake. Lakini mhubiri yule mchanga akahisi kwamba, ikiwa ndivyo, yeye mwenyewe anapaswa kumwomba ruhusa baba huyo kwa sababu ya kumstahi. Kwa hiyo akajitolea kunena na baba huyo na kumwambia kwamba mambo ambayo wangejifunza yalikuwa ya maana sana. Kwa kuona jinsi dada huyo mchanga alivyokuwa akichukua mambo kwa uzito na kwa kuthamini kwamba alikuwa amemjia yeye moja kwa moja, baba huyo alisema: “Ikiwa mambo mtakayojifunza ni ya maana hivyo, basi jamaa yangu yote inapaswa kujifunza.” Tokeo likawa kwamba kijana huyu wa miaka 13 alianzisha funzo la Biblia pamoja na jamaa nzima, kutia na mwana mmoja aliyefunga ndoa, pamoja na mke wake na watoto wengine waliokwisha kukua.

      Adabu Huanzia Nyumbani

      14. Adabu huanzia wapi, na ni jambo gani lililo la maana?

      14 Mara nyingi adabu za Mashahidi wachanga ni ushuhuda mzuri unaoonyesha wazi mazoezi wanayopokea nyumbani. Kweli kweli, adabu zetu ni wonyesho wa njia yetu ya maisha. Kwa sababu hii, kinyume cha vile huenda watu fulani wakafikiri, adabu zinapasa kupewa umaana mkubwa nyumbani. Katika jambo hili, kama ilivyo katika pande nyingine za maisha ya jamaa, kielelezo cha wazazi ndicho cha maana zaidi. (2 Timotheo 1:5) Kuambia watoto, “Fanya kama nisemavyo, si kama nitendavyo” kwa uhakika si njia ya kuwafundisha adabu. Mtu hujifunza mambo mengi sana yanayohusiana na adabu, si kwa maagizo ya maneno tu, bali kwa kuona na kuiga. “Wazazi hawawi wamefanya yote kabisa kwa kuwa walimu tu; wao pia ni violezo, kwa maana watoto wetu wanajifunza kwa kuiga njia zetu,” anasema Beverley Feldman, mtungaji wa Kids Who Succeed. Watoto wako wanaona wewe ukiwa na adabu za aina gani?

      15. Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao wasitawishe tabia za kuwa na adabu muda wa maisha yote?

      15 “Akina baba, msiwe mkiwachokoza watoto wenu” ndilo shauri la Biblia. (Waefeso 6:4, NW) Watoto huchokozeka na kuvurugika mawazo wanapoambiwa kwamba wanapaswa kuwa wenye fadhili na ufikirio, na bado wanaona wazazi wao wakibishana, wakisengenya watu, wakitenda kwa ufidhuli, au wakiudhika kwa urahisi. Je! wao wanaweza kulaumiwa wakitenda kwa namna iyo hiyo? Kwa upande ule mwingine, andiko linaendelea kusema hivi: “Bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” Na hiyo inatia ndani mambo yale ya msingi yanayohusu adabu, kama kusema, “Habari,” “Tafadhali,” “Asante,” na “Pole,” kuonyesha staha kwa wenye umri mkubwa, na kushirikiana vitu na wengine. (Walawi 19:32; Warumi 16:3-7) Sifa hizi ambazo wanajifunza nyumbani wakati wa utoto zitakuwa zenye thamani muda wa maisha yote.​—Mithali 22:6.

      16. Ni jitihada gani zinazohitajiwa, matokeo yakiwa nini?

      16 Kwa hiyo wazazi na watoto pia wanapaswa kuzoea adabu zikiwa sehemu ya kawaida yao ya kila siku badala ya kungoja mpaka pindi fulani ya pekee. Katika kufanya hivyo, wazazi wanapaswa kuwa wenye saburi na wavumilivu kuhusu makosa ambayo pasipo shaka watoto watafanya. Wajulisheni kwamba mnathamini sana wakiwa na mwenendo mwema, na mwe wepesi kuwapongeza wakati maendeleo yanapofanywa. Bila shaka, hii inataka jitihada nyingi kwa upande wenu. Lakini je! Maandiko hayakusema kwamba kanuni za kimungu zinapasa kukazwa kikiki katika watoto wakati “uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo [uamkapo, NW]”? (Kumbukumbu 6:7) Kufanya hivyo hufanyiza hali ya kirafiki na ya starehe nzuri nyumbani, ambayo inasaidia sana kuwakuza watoto wako wakawe watu wazima wenye msaada kwa watu, wenye kujali, na wenye adabu. Halafu watakuwa chanzo cha sifa na heshima kwako na kwa Muumba wao, Yehova Mungu.

      Kikundi cha Watu Wenye Adabu

      17. Ni nini huonwa kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova?

      17 Wale “Mashahidi zaidi ya 1,000” waliokusanyika nje ya Jumba la Jiji katika Jiji la New York alasiri hiyo ya Septemba walionyesha kwa kadiri ndogo tu jinsi Mashahidi wa Yehova hujiendesha kwa ukawaida. Mahali pengine, mwanamume mmoja alikuja kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza na baadaye akasema: “Kwa siku moja nilikuta watu, ambao hatujuani kabisa, walio na upendo wa kweli kuliko wale niliopata kuwakuta wakati wowote katika kanisa ambamo nililelewa.” Tokeo likawa nini? “Ilionekana wazi kwamba nilikuwa nimeupata ukweli,” yeye akasema. Mwanamume huyu alibadili mwendo wake wa maisha, na miezi saba baadaye akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa.​—Linganisha 1 Wakorintho 14:25.

      18. Kiwango cha adabu za Mashahidi wa Yehova kimeathirije watu wa nje?

      18 Kiwango cha adabu na mwenendo bora wa Mashahidi kwenye mikusanyiko yao ya kitaifa na kimataifa kimesifiwa sana. Katika pindi moja ya jinsi hiyo hivi majuzi katika Japani, mwongozi wa safari katika basi ya utalii alisema hivi: “Nyinyi watu mlipokuwa mkishuka basi, kila mmoja wenu, kutia na walio wachanga, hamkukosa kuniambia, ‘Asante sana.’ Hiyo ilinifurahisha sana!” Kwenye mkusanyiko mwingine, mtumikia watu kwenye kituo cha gari-moshi cha hapo karibu aliambia Shahidi hivi: “Kulikuwako vurugu kubwa sana wakati kusanyiko lililotangulia la watu 12,000 lilipofanywa kwenye Osaka Castle Hall.” Lakini akaendelea kusema hivi: “Nyinyi watu mna utaratibu kweli kweli, na mzigo umetuondokea. Tafadhali tupelekeeni shukrani zetu kwa yeyote yule anayesimamia kazi.”

      19. Kila mmoja wetu anapaswa aazimie kufanya nini kuhusu adabu?

      19 Maelezo hayo yanaonyesha nini? Kwamba Mashahidi wa Yehova kwa ujumla ‘wanajiendesha kwa namna inayozistahili habari njema.’ Namna gani sisi mmoja mmoja? Kama watoto wanaotegemea baba mwenye upendo, sisi sote, wachanga kwa wazee, na tutegemee Baba yetu wa kimbingu, Yehova, ili tupate kufundishwa kuwa watu wenye adabu, hata katika ulimwengu usio na adabu.​—Kumbukumbu 8:5; Mithali 3:11, 12.

      Wewe Unakumbuka?

      ◻ Kwa nini adabu zinahitajiwa kuwa sehemu ya mwenendo mwema?

      ◻ Ni adabu gani zinazofaa mahali petu pa ibada?

      ◻ Adabu zinaweza kuonyeshwaje katika huduma ya shambani?

      ◻ Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao wasitawishe adabu?

      ◻ Ni kiwango gani cha juu tunachopaswa kujitahidi kuunga mkono kuhusu adabu?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki