-
Vipindi vya WakatiKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
ya mwezi ilirekebishwa mara kwa mara ili kulingana na urefu wa mwaka wa jua, kama inavyoonyeshwa na Waisraeli wanaposhika sherehe za kukusanya za majira katika nyakati hususa. Kwa hiyo sherehe hizo ziliendelea kutukia wakati wa majira yanayofaa.—Law. 23:39.
Kumbuka kwamba Mungu aliwaumba wanadamu waishi milele. Dhambi ya Adamu ndiyo iliyoleta kifo. (Mwa. 2:17; 3:17-19; Rom. 5:12) Wale walioishi kabla ya Gharika walikuwa karibu zaidi na ukamilifu kuliko sisi leo, kwa hiyo waliishi muda mrefu zaidi. Lakini kila mmoja wao alikufa kabla ya kufikia miaka elfu moja.
Kwa nini Mashahidi wa Yehova husema kwamba Ufalme wa Mungu ulianzishwa mwaka wa 1914?
Mambo mawili yanayothibitisha yanaelekeza kwenye mwaka huo: (1) Orodha ya wakati ya Biblia na (2) matukio ya tangu mwaka wa 1914 yanayotimiza unabii. Hapa tutachunguza orodha ya wakati. Kuhusu utimizo wa unabii, ona kichwa “Siku za Mwisho.”
Soma Danieli 4:1-17. Mstari wa 20-37 huonyesha kwamba unabii huo ulitimia kumhusu Nebukadneza. Lakini pia una utimizo mkubwa zaidi. Tunajuaje hivyo? Mstari wa 3 na 17 huonyesha kwamba ndoto ambayo Mungu alimpa Mfalme Nebukadneza hushughulika na Ufalme wa Mungu na ahadi ya Mungu ya kumpa Ufalme huo “yeyote yule amtakaye . . . [hata] mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” Biblia nzima huonyesha kwamba Yehova alikusudia Mwana wake mwenyewe, Yesu Kristo, awatawale wanadamu akiwa mwakilishi Wake. (Zab. 2:1-8; Dan. 7:13, 14; 1 Kor. 15:23-25; Ufu. 11:15; 12:10) Maelezo ya Biblia kumhusu Yesu yanaonyesha kwamba kwa kweli ndiye aliyekuwa “mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” (Flp. 2:7, 8; Mt. 11:28-30) Basi, ile ndoto ya kinabii inaelekeza kwenye wakati ambapo Yehova angempa Mwana wake mwenyewe mamlaka ya kuwatawala wanadamu.
Ni jambo gani ambalo lingetokea kabla ya wakati huo? Utawala juu ya wanadamu, kama unavyowakilishwa na mti na kisiki chake, ungekuwa na “moyo wa mnyama.” (Dan. 4:16) Katika historia ya wanadamu kungekuwa na serikali ambazo zingekuwa na tabia za wanyama-mwitu. Katika nyakati za kisasa, tai anatumiwa kuwakilisha Marekani; simba, Uingereza; joka, China. Pia Biblia inatumia wanyama-mwitu kuwakilisha serikali za ulimwengu na mfumo wa ulimwenguni pote wa utawala wa kibinadamu chini ya uvutano wa Shetani. (Dan. 7:2-8, 17, 23; 8:20-22; Ufu. 13:1, 2) Kama Yesu alivyoonyesha katika unabii wake unaoelekeza kwenye umalizio wa mfumo wa mambo, Yerusalemu “lingekanyagwa-kanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitimie.” (Luka 21:24) “Yerusalemu” liliwakilisha Ufalme wa Mungu kwa sababu ilisemekana kwamba wafalme wake walikaa kwenye “kiti cha ufalme wa Yehova.” (1 Nya. 28:4, 5; Mt. 5:34, 35) Basi, serikali za Mataifa, zinazowakilishwa na wanyama-mwitu, ‘zingeikanyaga-kanyaga’ haki ya Ufalme wa Mungu ya kuelekeza mambo ya wanadamu nazo zingetawala chini ya uongozi wa Shetani.—Linganisha na Luka 4:5, 6.
Serikali hizo zingeruhusiwa zitawale kwa muda gani kabla Yehova hajampa Yesu Kristo Ufalme huo? Andiko la Danieli 4:16 linasema “nyakati saba” (“miaka saba,” BHN, na pia kielezi-chini katika VB kwenye mstari wa 13). Biblia huonyesha kwamba katika kuhesabu wakati wa kinabii, siku moja huhesabiwa kuwa mwaka mmoja. (Eze. 4:6; Hes. 14:34) Basi, ni “siku” ngapi zinazohusika? Andiko la Ufunuo 11:2, 3 hueleza waziwazi kwamba miezi 42 (miaka 3 1/2) katika unabii huo huhesabiwa kuwa siku 1,260. Miaka 7 itakuwa mara mbili ya siku hizo, au siku 2,520. Kutumia kanuni ya “siku moja kwa mwaka mmoja” kutatokeza miaka 2,520.
“Nyakati saba” zilianza wakati gani? Baada ya Sedekia, mfalme wa mwisho katika utawala uliowakilisha Ufalme wa Mungu, kuondolewa na Wababiloni kutoka kiti cha ufalme katika Yerusalemu. (Eze. 21:25-27) Mwishowe, mapema mwezi wa Oktoba 607 K.W.K., sehemu ya mwisho ya enzi ya Kiyahudi ikatoweka. Kufikia wakati huo gavana Myahudi, Gedalia, ambaye Wababiloni walikuwa wamemwacha atawale, alikuwa ameuawa, na Wayahudi waliobaki walikuwa wamekimbilia Misri. (Yeremia, sura ya 40-43) Orodha ya wakati ya Biblia inayotegemeka inaonyesha kwamba hilo lilitukia miaka 70 kabla ya mwaka wa 537 K.W.K., mwaka ambao Wayahudi walirudi kutoka utekwani; yaani, ilitukia kufikia mapema mwezi wa Oktoba 607 K.W.K. (Yer. 29:10; Dan. 9:2; kwa habari zaidi, ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” uku. 186-189.)
KUHESABU ZILE “NYAKATI SABA”
“Nyakati saba” = 7 x 360 = miaka 2,520
“Wakati” wa Kibiblia, au mwaka = 12 x siku 30 = 360. (Ufu. 11:2, 3; 12:6, 14)
Katika utimizo wa “nyakati saba” kila siku hulingana na mwaka mmoja. (Eze. 4:6; Hes. 14:34)
Mapema Oktoba, 607 K.W.K., hadi Desemba 31, 607 K.W.K. = mwaka 1⁄4
Januari 1, 606 K.W.K., hadi Desemba 31, 1 K.W.K. = miaka 606
Januari 1, 1 W.K., hadi Desemba 31, 1913 = miaka 1,913
Januari 1, 1914, hadi mapema Oktoba, 1914 = mwaka 3/4
Jumla: miaka 2,520
Basi, wakati huo unahesabiwaje mpaka mwaka wa 1914? Kuhesabu miaka 2,520 kutoka mapema mwezi wa Oktoba 607 K.W.K., hutufikisha mapema mwezi wa Oktoba 1914 W.K., kama ilivyoonyeshwa katika chati.
Ni nini lililotukia wakati huo? Yehova alimkabidhi Mwana wake, Yesu Kristo, aliyetukuzwa mbinguni, mamlaka ya kuwatawala wanadamu.—Dan. 7:13, 14.
Basi kwa nini bado kuna uovu mwingi duniani? Baada ya Kristo kutawazwa, Shetani na roho wake waovu walitupwa kutoka mbinguni mpaka duniani. (Ufu. 12:12) Kristo akiwa Mfalme hakuchukua hatua ya kuwaangamiza mara moja wote waliokataa kuikubali enzi kuu ya Yehova na kumkubali yeye mwenyewe akiwa Masihi. Badala yake, kama alivyotabiri, kazi ya kuhubiri duniani pote ilipasa kufanywa. (Mt. 24:14) Hiyo itasababisha kugawanywa kwa watu wa mataifa yote; wale walio waadilifu watapewa tazamio la uzima wa milele, na waovu watakatiliwa mbali milele katika kifo. (Mt. 25:31-46) Kabla ya wakati huo, hali ngumu sana zilizotabiriwa kutukia “siku za mwisho” zingeenea. Kama ilivyoonyeshwa chini ya kichwa “Siku za Mwisho,” matukio hayo yamekuwa yakionekana waziwazi tangu mwaka wa 1914. Mambo yote ambayo Yesu alitabiri yatatukia, kutia ndani “dhiki kuu” ambapo ulimwengu mbovu wa sasa utakoma.—Mt. 24:21, 22.
Mwisho wa ulimwengu huu mbovu utakuja wakati gani?
Yesu alijibu hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” Hata hivyo, alisema hivi pia: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie.”—Mt. 24:36, 34.
Pia, baada ya kusimulia matukio ambayo yangefuata kuanzishwa kwa Ufalme mikononi mwa Yesu Kristo katika mwaka wa 1914, andiko la Ufunuo 12:12, huongeza hivi: “Furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”
-
-
WanawakeKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Wanawake
Maana: Wanadamu wa jinsia ya kike ambao ni watu wazima. Katika Kiebrania, neno mwanamke ni ’ish·shahʹ, ambalo kihalisi humaanisha “mwanadamu wa kike.”
Je, Biblia inawashushia wanawake heshima au inawatendea kana kwamba ni watu duni?
Mwa. 2:18: “Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’” (Katika andiko hilo, Mungu hasemi kwamba mwanamume ni mtu bora kuliko mwanamke. Badala yake, Mungu alionyesha kwamba mwanamke angekuwa na sifa ambazo zingekamilisha zile za mwanamume katika mpango wa Mungu. Kikamilisho ni kimoja cha vitu viwili vinavyokamilishana. Basi wanawake kwa ujumla hutokeza katika sifa na uwezo fulani; wanaume nao hutokeza katika sifa nyingine. Linganisha na 1 Wakorintho 11:11, 12.)
Mwa. 3:16: “[Mungu] akamwambia mwanamke: ‘ . . . tamaa yako itakuwa kwa mume wako, naye atakutawala.’” (Tangazo hilo lililotolewa baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi halikumaanisha jambo ambalo wanaume wanapaswa kufanya bali lilimaanisha jambo ambalo Yehova alijua mapema kwamba wanaume wangefanya kwa kuwa sasa ubinafsi ulikuwa umeingia katika maisha ya wanadamu. Masimulizi kadhaa ya Biblia yaliyoandikwa baada ya tukio hilo husema kuhusu hali zenye huzuni sana zilizositawi kwa sababu ya wanaume kuwatawala wanawake kwa ubinafsi. Lakini Biblia haisemi kwamba Mungu alikubali mwenendo huo wala haisemi kwamba huo ni mfano wa kufuatwa na wengine.)
Je, kuwapa wanaume ukichwa ni kuwashushia heshima wanawake?
Kuwa chini ya ukichwa kwenyewe si kushushiwa heshima. Ukichwa hufanya mambo yaendeshwe kwa utaratibu, na Yehova ‘si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.’ (1 Kor. 14:33) Yesu Kristo yuko chini ya ukichwa wa Yehova Mungu, naye huridhika sana na uhusiano huo.—Yoh. 5:19, 20; 8:29; 1 Kor. 15:27, 28.
Mwanamume pia amepewa ukichwa wa kiasi, hasa katika familia na katika kutaniko la Kikristo. Mungu hajampa mwanamume mamlaka kamili juu ya mwanamke; mwanamume lazima atoe hesabu kwa kichwa chake, Yesu Kristo, na kwa Mungu kuhusu jinsi anavyotumia ukichwa huo. (1 Kor. 11:3) Zaidi ya hayo, waume wanaamuriwa ‘wawe wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe’ na ‘kuwapa heshima’ wake zao. (Efe. 5:28; 1 Pet. 3:7) Mahitaji ya kingono ya mume hayawekwi juu ya yale ya mke wake katika mpango wa Mungu kwa watu waliooana. (1 Kor. 7:3, 4) Wajibu wa mke mwenye uwezo, kama ulivyoandikwa katika Biblia, hukazia ubora wake katika familia na jumuiya. Wajibu huo unampa nafasi tele ambapo anaweza kutumia uwezo wake huku akithamini ukichwa wa mume wake. (Met. 31:10-31) Biblia inawaamuru watoto wamheshimu baba yao na pia mama yao. (Efe. 6:1-3) Hiyo pia hutoa uangalifu wa pekee kuhusu kutunza mahitaji ya wajane. (Yak. 1:27) Kwa hiyo, kati ya Wakristo wa kweli, wanawake wanaweza kupata usalama mkubwa, wajithamini kwelikweli, na kuridhika na utendaji wao wenyewe.
Heshima ya cheo cha mwanamke katika mpango wa Mungu inaonyeshwa zaidi na uhakika wa kwamba Yehova analitaja tengenezo lake mwenyewe la viumbe wa roho washikamanifu kama mwanamke, mke wake, mama ya watoto wake. (Ufu. 12:1; Gal. 4:26) Pia, kutaniko la Yesu Kristo la watiwa-mafuta linasemwa kuwa bibi-arusi wake. (Ufu. 19:7; 21:2, 9) Na kwa maoni ya kiroho hakuna tofauti kati ya mwanamume na mwanamke kati ya wale walioitwa katika Ufalme wa mbinguni pamoja na Kristo.—Gal. 3:26-28.
-