Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je! Kweli Ni Wizi?
    Mnara wa Mlinzi—1994 | Aprili 15
    • Je! Kweli Ni Wizi?

      ABIODUN alikuwa mtumishi-mezani mkuu katika hoteli moja kubwa ya Naijeria. Alipokuwa akifunga jumba la karamu jioni moja, alipata mfuko wa fedha zinazolingana na dola 1,827, za U.S. Bila kukawia yeye alikabidhi fedha hizo, ambazo baadaye alikabidhiwa mwenyewe, aliyekuwa mgeni kwenye hoteli hiyo. Wasimamizi wa hoteli hiyo walimthawabisha Abiodun kwa kumpandisha cheo maradufu wakampa yeye tuzo la “mfanya kazi mwema kabisa mwakani.” Mwenye fedha hizo alimthawabisha pia.

      Quality, gazeti la habari la mahali hapo, lilitoa hadithi hiyo, ikimwita Abiodun “Msamaria Mwema.” Alipoulizwa na gazeti Quality ikiwa alishawishwa ajiwekee fedha hizo, Abiodun alisema hivi: ‘Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo nikipata chochote ambacho si changu, mimi humrudishia mwenyewe.’

      Wengi katika jumuiya walishangazwa na uthibitisho wa kufuatia haki wa Abiodun. Mashahidi wenzi wa Abiodun walipendezwa na yale yaliyotukia, lakini hawakushangazwa. Duniani pote Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa kanuni zao za juu. Miongoni mwao kufuatia haki ni jambo la lazima, sehemu muhimu ya Ukristo wa kweli.

      Hata hivyo, pindi kwa pindi huenda ikawa vigumu kutofautisha kati ya hali ya kufuatia haki na ile isiyo ya kufuatia haki. Ifikirie hali hii. Festus, aliyetunza michango na hesabu za fedha katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika Afrika Magharibi, alihitaji fedha sana.a Mke wake alihitaji upasuaji hatari ambao madaktari wake walisema haukupaswa kuahirishwa. Hospitali ilitaka nusu ya fedha kimbele.

      Festus hakuwa na fedha. Alipowaendea watu kadhaa ili kupata mkopo, walikataa kumpa. Kisha akafikiria zile fedha alizokuwa akitunza kisha akasababu, ‘Je! yafaa nimwache mke wangu awe na hatari ya kifo ilihali naweza kufanya jambo fulani la kukizuia? Kwa nini “nisiazime” kutoka fedha za kutaniko? Naweza kuzirudisha watu wanaponilipa zile ninazowawia.’

      Festus alitumia fedha hizo zisizokuwa zake ili kulipa hospitali. Je! alisababu kwa usahihi? Je! tendo lake lilifaa kwa sababu ya hali ya dharura aliyokabili?

      Ni Fedha za Nani?

      Katika kuchanganua maswali hayo, acheni tupitie kwa ufupi mambo machache kuhusu chanzo na kusudi la zile fedha zilizochukuliwa na Festus. Fedha hizo zatoka kwenye michango ya hiari inayotolewa na washiriki wa kutaniko wanaotaka kuendeleza ibada safi ya Yehova. (2 Wakorintho 9:7) Hazitumiwi kulipia mishahara, kwa kuwa hakuna alipwaye kwa ajili ya yale afanyayo kutanikoni. Kinyume cha hilo, fedha zinazochangwa zinatumiwa hasa kupata na kutunza mahali pa kukutania, kwa kawaida pakiwa Jumba la Ufalme. Hilo huandaa mahali pafaapo na penye ustarehe ambapo watu—vijana kwa wazee, tajiri kwa maskini—waweza kukutania ili kupata maagizo ya Biblia.

      Hizo ni fedha za nani? Ni za kutaniko kwa ujumla. Hakuna mshiriki mmoja aamuaye jinsi fedha hizo zapasa kutumiwa. Ingawa baraza la wazee huelekeza malipo ya gharama za kikutaniko za kawaida, wakati malipo yasiyo ya kawaida yanapohitajika, wazee hutokeza jambo hilo kwa kutaniko zima ili likubaliwe.

      Kuazima au Kuiba?

      Kwa sababu ya mpango wake wa kurudisha hizo fedha upesi iwezekanavyo, Festus aliona tendo lake kuwa kuazima. Hata hivyo, Webster’s New Dictionary of Synonyms hutumia maneno mengine kuhusiana na “kuchukua na kuondoa mali za mtu mwingine kwa kawaida ikiwa kwa njia ya wizi au bila ujuzi wake na sikuzote bila kibali chake.” Maneno hayo ni “wizi” na “mwizi.” Festus alichukua fedha zilizokuwa za kutaniko, bila ruhusa au idhini. Kwa hiyo, naam, alikuwa na hatia ya wizi. Alikuwa mwizi.

      Bila shaka, kuna viwango vya lawama katika jambo linalochochea wizi. Twaweza kuona hilo kutokana na kielelezo cha Yuda Iskariote, aliyekabidhiwa utunzaji wa fedha zilizowekwa na Yesu na wale mitume waaminifu. Biblia husema hivi: “[Yuda] alikuwa mwizi na alikuwa na sanduku la pesa na alikuwa na kawaida ya kuchukua pesa zilizowekwa ndani yalo.” (Yohana 12:6, NW) Kwa kuchochewa na moyo mbaya na pupa dhahiri, Yuda alizidi kuwa mbaya. Hatimaye alijishusha kiadili kufikia hatua ya kumsaliti Mwana wa Mungu—kwa vipande 30 vya fedha.—Mathayo 26:14-16.

      Hata hivyo, Festus, alichochewa na ufikirio kuelekea mke wake aliyekuwa akiugua. Je! hili lamaanisha kwamba hakuwa na lawama? Bila shaka la. Yafikirie yale ambayo Biblia husema kuhusu wizi katika hali nyingine ionekanayo kuwa ya dharura: “Watu hawamdharau mwivi, akiiba ili kujishibisha, iwapo aona njaa; lakini akipatikana, atalipa mara saba; atatoa mali yote ya nyumba yake.” (Mithali 6:30, 31) Yaani, anapokamatwa, ni lazima mwizi akabili adhabu kamili ya sheria. Kulingana na Sheria ya Kimusa, mwizi alilazimika kulipia uhalifu wake. Basi badala ya kutia moyo au kutolea udhuru wizi, Biblia huonya kwamba hata katika hali za dharura, kuiba kwaweza kusababisha hasara ya kiuchumi, fedheha, na kwa uzito zaidi, kupoteza kibali cha Mungu.

      Wakiwa Mashahidi wa Yehova, ni lazima Wakristo wote wa kweli, hasa wale waliokabidhiwa madaraka kutanikoni, wawe kielelezo chema, ‘bila hatia.’ (1 Timotheo 3:10) Festus hakupokea zile fedha alizokuwa akitazamia, hivyo hakuweza kurudisha fedha alizokuwa amechukua. Lile alilokuwa amefanya lilipata kujulikana. Ni nini kilichompata? Kama angalikuwa mwizi asiyetubu, yeye angaliondoshwa kutoka katika kutaniko safi la Kikristo. (1 Petro 4:15) Lakini alijuta sana na kutubu. Kwa hiyo, angeweza kubaki kutanikoni, ingawa alipoteza mapendeleo yake ya utumishi.

      Kumtumaini Mungu

      Mtume Paulo alionya kwamba kuiba kwa mtu anayedai kumtumikia Yehova kwaweza kuletea jina la Mungu suto na watu wa jina Lake. Paulo aliandika hivi: “Wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe? Kwa maana jina la Mungu latukanwa katika Mataifa kwa ajili yenu.”—Warumi 2:21, 24.

      Aguri, mtu mwenye hekima wa nyakati za kale, alionyesha jambo ilo hilo. Katika sala yake aliomba ‘asiwe maskini sana akaibe na kulitaja bure jina la Mungu wake.’ (Mithali 30:9) Ona kwamba yule mtu mwenye hekima alikiri kwamba umaskini waweza kusababisha hali ziwezazo kumshawishi hata mtu mwadilifu aibe. Naam, nyakati ngumu zaweza kujaribu imani ya Mkristo katika uwezo wa Yehova wa kutimiza mahitaji ya watu wake.

      Bado, Mashahidi wa Yehova waaminifu-washikamanifu, kutia na wale walio maskini, wana imani kwamba Mungu “huwapa thawabu wale wamtafutao.” (Waebrania 11:6) Wao wajua kwamba Yehova huthawabisha waaminifu wake kwa kuwasaidia watimize mahitaji yao. Yesu alielewesha wazi jambo hilo katika Mahubiri ya Mlimani yake, akisema hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? . . . kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mathayo 6:31-33.

      Mungu huwaandaliaje wenye uhitaji katika kutaniko la Kikristo? Katika njia nyingi. Moja ni kupitia waamini wenzi. Watu wa Mungu huonyeshana upendo wa kikweli. Wao huzingatia kwa uzito onyo hili la upole la Kibiblia: “Mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo? Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”—1 Yohana 3:17, 18.

      Kotekote ulimwenguni, katika yale makutaniko zaidi ya 73,000, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni nne na nusu hujitahidi sana kumtumikia Mungu kulingana na kanuni zake zenye uadilifu. Wao wajua kwamba Mungu hatawaacha kamwe waaminifu-washikamanifu wake. Wale ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi huinua sauti zao wakikubaliana na Mfalme Daudi, aliyeandika hivi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zaburi 37:25.

      Ni afadhali kama nini kutia imani katika Mungu aliyepulizia maneno hayo, badala ya mtu kujiruhusu kushawishwa aibe na labda kupoteza upendeleo wa Mungu milele!—1 Wakorintho 6:9, 10.

  • Kuondolea Shela Ule Mpaka wa Mwisho wa Alaska
    Mnara wa Mlinzi—1994 | Aprili 15
    • Kuondolea Shela Ule Mpaka wa Mwisho wa Alaska

      KWA siku mbili sasa, sisi wanne tumesongamana ndani ya chumba kidogo katika mji mdogo maarufu wa Nome, Alaska, ambako wengi huja kutafuta dhahabu. Katika 1898 watafutaji zaidi ya 40,000 walikuja hapa kutafuta kitu kimoja tu—dhahabu! Kwa upande mwingine, sisi twatafuta hazina tofauti.

      Kwa sasa, sisi twapendezwa na “vitu vinavyotamaniwa” ambavyo huenda vikawa vyaishi katika vijiji vilivyotengwa vya Gambell na Savoonga kwenye Kisiwa cha St. Lawrence, kilometa 300 kuelekea magharibi katika Mlangobahari wa Bering. (Hagai 2:7) Huko Wainuiti huvumilia yale maji ya barafu ya Arktiki na kuwinda nyangumi kilometa chache tu kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Lakini theluji yenye kuvuma na ukungu mzito sana watuzuia tusiondoke. Ndege yetu haiwezi kuruka.

      Tungojapo, nafikiria matukio ya miaka michache iliyopita na kumshukuru Yehova Mungu kwa ajili ya baraka yake juu ya ushahidi katika maeneo ya msituni. Katika Alaska—inayoitwa na wengine mpaka wa mwisho wa ulimwengu—kuna wenyeji zaidi ya 60,000 wanaoishi katika jumuiya zaidi ya 150 zilizo mbali, ambazo zimetapakaa kotekote katika jangwa lenye ukubwa la karibu kilometa za mraba 1,600,000, ambalo halijaunganishwa kwa barabara za aina yoyote. Kwa ndege ya Watch Tower Society, tayari tumefikia zaidi ya theluthi moja ya vijiji hivyo vilivyotengwa, tukileta habari njema za Ufalme wa Mungu kwavyo.—Mathayo 24:14.

      Ili kufikia makazi hayo yaliyo mbali, mara nyingi ndege huhitaji kushuka kupitia mawingu na ukungu ambao huenda ukafunika bara kwa siku kadhaa. Baada ya kushuka, kuna ukungu mwingine bado ambao ni lazima upenywe. Kama shela, ukungu huo huzifunika akili na mioyo ya watu hawa wenye fadhili na wenye amani.—Linganisha 2 Wakorintho 3:15, 16.

      Kipindi cha Badiliko Chenye Kuumiza

      Msitu wa Alaska unakaliwa na Wainuiti, Waaleuti, na Wahindi. Kila moja ya wao wana desturi na vitabia vya kipekee kulingana na mapokeo yao. Ili kuokoka kipupwe cha Arktiki,

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki