Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jinsi ya Kupanga Maktaba ya Kitheokrasi
    Mnara wa Mlinzi—1994 | Novemba 1
    • Jinsi ya Kupanga Maktaba ya Kitheokrasi

      SHEREZADE, msichana mdogo mwerevu Mhispania, alikuwa mwenye umri wa miaka minne wakati mwalimu wake aliliambia darasa kwamba wangepaka rangi picha za “Baba Krismasi.” Mara moja, Sherezade aliomba aruhusiwe kutoshiriki. Alieleza kwamba dhamiri yake haingemruhusu kufanya hilo.

      Akishangazwa na mkatao huu, mwalimu alimwambia kwamba ilikuwa kama kupaka rangi picha ya mwanasesere na kwamba hakukuwa na lolote baya katika kufanya hilo. Sherezade alijibu: “Ikiwa ni mwanasesere, ningechagua kuchora mwanasesere mwenyewe ukiniruhusu.”

      Katika pindi nyingine darasa liliambiwa lichore bendera ya taifa. Kwa mara nyingine tena Sherezade aliuliza kama angeruhusiwa kufanya jambo jingine. Kwa njia ya ufafanuzi, alimwambia mwalimu hadithi ya Shadraka, Meshaki, na Abednego.—Danieli 3:1-28.

      Si muda mrefu baadaye mwalimu alimpigia simu mama yake Sherezade kueleza mshangao wake. “Binti yako kwa pindi kadhaa amenieleza juu ya dhamiri yake,” alijibu. “Waweza kuwazia hilo? Msichana wa umri wake akinieleza sababu inayofanya dhamiri yake imsumbue! Tazama, sikubaliani na yale unayomfundisha, lakini nakuhakikishia kwamba unafaulu. Na ninataka ujue kwamba namheshimu binti yako.”

      Msichana wa umri wa miaka minne angewezaje kujipatia dhamiri iliyozoezwa kwa Biblia? Mama yake Marina, aeleza kwamba Sherezade ana maktaba yake mwenyewe ya kitheokrasi ndani ya chumba chake cha kulala. Maktaba hiyo yatia ndani nakala zake za kibinafsi za Mnara wa Mlinzi, ambazo amepiga mstari, fasihi zake za kuhubiri, na vichapo vyote vya Watchtower Society vilivyotolewa tangu alipozaliwa. Kitu kimoja anachopenda sana katika maktaba yake ni kaseti za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, ambazo anasikiliza kila usiku akifuatisha pamoja na nakala yake ya kitabu. Ni maelezo haya ya Kibiblia yaliyomwezesha kufanya maamuzi yaliyotajwa pale juu.

      Je, maktaba ya kitheokrasi iliyopangwa vizuri ingeweza kukusaidia wewe na watoto wako? Kwa nini maktaba ya nyumbani ni ya lazima?

      “Maktaba Ni ya Lazima”

      “Maktaba ni mojapo ya vitu vya lazima maishani,” alisema Henry Ward Beecher. Bila shaka, karibu sisi sote tuna hivi “vitu vya lazima maishani,” ingawa huenda tusijue. Jinsi gani? Kwa sababu hata kama hatuna chochote ila Biblia, tunayo maktaba ya aina fulani.

      Biblia kwelikweli ni maktaba ya kitheokrasi iliyo bora sana. Katika karne ya nne, Jerome alinukuu kifungu cha maneno cha Kilatini Bibliotheca Divina (Maktaba ya Kimungu) kusimulia mkusanyo kamili wa vitabu vilivyovuviwa tuviitavyo Biblia. Yehova alituandalia maktaba hii takatifu ili kutupa msaada, mafundisho, na mwongozo wenye mafaa. Ni kitu tusichopaswa kamwe kukichukua vivi hivi. Kuwa na Biblia yote nzima kwamaanisha kwamba tuna maktaba kubwa zaidi kuliko wengi wa watumishi wa Mungu zamani.

      Wakati hati-mkono zenye thamani kubwa ndizo zilizopatikana pekee, ni nyumba chache za watu binafsi ikiwa kulikuwa na zozote, zingeweza kujivunia Biblia nzima. Paulo alipotamani kujifunza Maandiko mwishoni-mwishoni mwa kifungo chake katika Roma, ilimbidi kuuliza Timotheo amletee vitabu vya kukunjwa kutoka Esia Ndogo—labda visehemu vya Maandiko ya Kiebrania. (2 Timotheo 4:13) Hata hivyo, ndani ya masinagogi mlikuwamo mkusanyo wa vitabu vya kukunjwa, na Yesu Kristo pamoja na mtume Paulo walitumia maktaba haya vizuri katika kazi yao ya kuhubiri. (Luka 4:15-17; Matendo 17:1-3) Kwa furaha, Maandiko sasa yanapatikana kwa urahisi sana kuliko yalivyopatikana katika karne ya kwanza.

      Kwa sababu ya ubuni wa matbaa za uchapaji, leo karibu watumishi wote wa Mungu—lugha yao iwe ipi—wanaweza kujipatia Biblia nzima kwa gharama nzuri. Sisi pia tuna fursa ya kipekee ya kuongezea “maktaba” hii takatifu. Kwa zaidi ya karne moja, “mtumwa mwaminifu mwenye akili” amefanya bidii kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.—Mathayo 24:45-47.

      Lakini haielekei kwamba tutapata faida kamili ya habari hii yenye thamani ikiwa hatutapanga vizuri maktaba ya kitheokrasi ya kibinafsi. Hilo laweza kufanywaje? Bila shaka, hatua ya kwanza ni kujipatia vitabu vinavyohitajika katika maktaba hiyo. Lafaa kuifanyia bidii, maana itatuwezesha kupata kwa urahisi zaidi habari tunazohitaji hasa kushughulikia matatizo na kujibu maswali ya Biblia.

      Ni Vitabu Vipi Ninavyohitaji?

      Je, umewahi kujiuliza jinsi ungeweza kusuluhisha tatizo la mawasiliano katika ndoa yako au jinsi ungesaidia watoto wako kusema la kwa dawa za kulevya? Ungeweza kusaidiaje rafiki ambaye ameshuka moyo? Je, waweza kueleza waziwazi ni ushuhuda gani tunao kwamba Mungu yupo na kwa nini anaruhusu uovu? Hayawani-mwitu rangi nyekundu-nyangavu wa Ufunuo sura ya 17 anafananisha nini?

      Haya na maswali mengine mengi yaweza kujibiwa ukiwa na maktaba nzuri ya kitheokrasi. Watchtower Society imechapa vitabu, broshua, na makala za magazeti zinazohusu habari zote za Kimaandiko. Zaidi ya hayo, fasihi hizi huzungumzia habari za familia, hujenga imani yetu katika Mungu na Biblia, hutuwezesha kuboresha ufundi wetu wa kuhubiri, na kutusaidia kufahamu unabii wa Biblia.

      Vichapo vingi vilivyochapishwa na Sosaiti miaka 20 iliyopita bado vyapatikana. Ikiwa umeingia katika kweli karibuni, ingefaa ujipatie fasihi hizo zote zipatikanazo kwa lugha yako. Huenda ikawa kwamba mabuku yaliyojalidiwa ya miaka iliyopita ya Mnara wa Mlinzi yapatikana katika lugha yako. Vitabu vyenye kutokeza sana vya marejezo kama vile Insight on the Scriptures na Comprehensive Concordance, pia vimechapishwa katika lugha mbalimbali. Hata hivyo, kujipatia vitabu hivi ni hatua ya kwanza tu.

      Panga Vizuri Maktaba Yako!

      Kujua kwamba una kitabu mahali fulani ni jambo moja, lakini jambo gumu ni kupata kile unachohitaji. Ikiwa ni lazima tupoteze wakati mwingi tukitafuta marejezo tunayotaka, huenda tutapoteza hamu ya jambo hilo. Kwa upande mwingine, ikiwa vitabu vyetu vimepangwa vizuri, vikiwa mahali panapofaa, tutakuwa na mwelekeo zaidi wa kufanya uchunguzi wa kibinafsi.

      Ikiwezekana, ni jambo la msaada kuwa na kiasi kikubwa cha vitabu vya kitheokrasi mahali pamoja. Kama hatuwezi kununua kabati ya vitabu ikiwa imetengenezwa tayari, yaweza kutengenezwa, na mara nyingi kwa gharama ndogo sana na si lazima ichukue nafasi kubwa. Kufikia maktaba kwa urahisi ni jambo la maana pia. Vitabu vilivyowekwa orofa ya juu sana havisaidii sana ila tu kupata vumbi.

      Hatua ifuatayo ni kupanga vitabu. Wakati mdogo tu unaotumiwa kupanga vitabu kwa mpangilio mzuri huleta faida.

      Vipi ikiwa wengi wa familia yako si Mashahidi wa Yehova? Ingawa huenda usiweze kupanga maktaba kama vile ungependa, ndani ya chumba chako mwenyewe waweza kuwa na kabati ya vitabu iliyo na vichapo fulani vya Kimaandiko.

      Maktaba ya Kitheokrasi Yaweza Kusaidia Kujenga Hali ya Kiroho

      Mara vitabu vyetu vimepangwa, tunahitaji utaratibu wa kutusaidia kupata habari. Kumbukumbu letu laweza kushindwa, na huenda sisi binafsi tusijue yaliyomo katika kila kitabu katika maktaba yetu ya kitheokrasi. Hata hivyo, habari zote ndani ya maktaba zaweza kupatikana kwa urahisi. Ikiwa inapatikana katika lugha yetu ile Watch Tower Publications Index yaweza kutuwezesha kupata habari hususa katika kichwa chochote kwa muda mfupi.

      Julián, ambaye ametumika miaka mingi akiwa painia wa pekee na mzee, aeleza kwamba Index ni yenye thamani sana katika kufundisha mwanaye wa mwisho kufanya funzo la kibinafsi. “Jairo, mwenye umri wa miaka saba, alirudi nyumbani kutoka shuleni siku moja na kuniuliza, ‘Baba, Sosaiti imesema nini kuhusu dinosa?’ Tulienda mara moja kwenye Index na tukachunguza neno ‘dinosa.’ Mara moja tukapata mfululizo wa makala za jalada la Amkeni! juu ya habari hiyo. [Februari 8, 1990, Kiingereza] Siku iyo hiyo, Jairo akaanza kuisoma. Tayari anajua kwamba maktaba yetu ya kitheokrasi ina habari zenye kutumika kwa karibu kila jambo. Mimi binafsi, nasadiki kwamba watoto wetu wanapojifunza kutumia vizuri maktaba ya kitheokrasi, huwasaidia wakue kiroho. Wao hujifunza kutoa sababu, na zaidi ya hayo, wao hutambua kwamba funzo la kibinafsi laweza kufurahisha.”

      Fausto, baba ya Sherezade aliyetajwa pale mwanzoni, huamini kwamba wapaswa kuanza mapema iwezekanavyo katika kuzoeza watoto kutumia maktaba ya kitheokrasi. “Tayari tunamwonyesha Sherezade, ambaye sasa ana umri wa miaka sita, jinsi ya kutumia Index,” aeleza, “Maana anapendezwa na tazamio la Paradiso ya duniani, tulianza kwa kumwonyesha neno ‘paradiso’ katika Index halafu kuchunguza makala za Mnara wa Mlinzi zilizotajwa. Kwa kawaida tungemwonyesha picha pekee. Hata hivyo, kwa njia hii alijifunza kwamba Index ndio ufunguo wa kupata habari katika maktaba yetu ya nyumbani. Tulijua kwamba ameelewa aliporudi kutoka shuleni siku moja akiwa na swali kuhusu sherehe za Ista. ‘Kwa nini tusichunguze jambo hilo ndani ya Index?’ alimwuliza mama yake.”

      Hata tuwe na umri gani, Biblia hututia moyo “jaribuni mambo yote; lishikeni lililo jema.” (1 Wathesalonike 5:21) Hili lamaanisha tuchunguze yale Maandiko husema. (Matendo 17:11) Tukiwa na maktaba iliyopangwa vizuri, uchunguzi kama huo unaweza kufurahisha. Kila wakati tufanikiwapo kutumia maktaba yetu tunapotayarisha hotuba, kupata shauri lenye kutumika katika kushughulikia tatizo, au kuchunguza habari ya kupendeza, itatusaidia tuone thamani yenye kutumika ya maktaba yetu.

      Wazazi wa Sherezade wasema: “Katika nyumba ya Kikristo, maktaba ya kitheokrasi kwa kweli ni ya lazima!”

      [Sanduku katika ukurasa wa 30]

      WEWE UNGEWEZA KUPANGAJE VITABU VYAKO?

      Hakuna sheria za lazima za jinsi ya kupanga vitabu vyako. Hata hivyo, mpangilio mzuri ufuatao waonyesha njia moja ambayo wewe ungeweza kupanga vitabu vyako kulingana na yaliyomo.

      1. Vitabu vinavyoeleza sehemu fulani za Biblia mstari kwa mstari

      (Mifano: Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, “The Nations Shall Know That I Am Jehovah”—How?, “Your Will Be Done on Earth”)

      2. Vitabu vinavyohusu maisha ya familia

      (Mifano: Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia)

      3. Biblia na vitabu vya marejezo

      (Mifano: New World Translation of the Holy Scriptures—With References, Biblia nyingine, Watch Tower Publications Indexes, Comprehensive Concordance, Insight on the Scriptures, The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures, kamusi nzuri)

      4. Vitabu vinavyotumiwa sasa kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

      5. Kaseti na vidio

      6. Mabuku yaliyojalidiwa ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni ya Kiingereza

      7. Historia ya Mashahidi wa Yehova

      (Mifano: Vitabu-Mwaka vya Mashahidi wa Yehova, Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom)

      8. Vitabu na broshua tutumiavyo kwa kawaida katika huduma yetu

      (Mifano: Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?, Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, Wenye Umoja Katika Ibada ya Mungu wa Pekee wa Kweli)

      [Picha katika ukurasa wa 31]

      Tayari Sherezade amekuwa mwanafunzi mzuri wa Biblia

      [Picha katika ukurasa wa 31]

      Ajapokuwa mchanga, mvulana huyu anatumia maktaba ya kitheokrasi

  • Nyongeza ya Baraza Linaloongoza
    Mnara wa Mlinzi—1994 | Novemba 1
    • Nyongeza ya Baraza Linaloongoza

      KWA ajili ya kuongeza washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, kuanzia Julai 1, 1994, mshiriki mwingine mmoja ameongezwa kwa wale wazee 11 wanaotumika sasa. Mshiriki huyo mpya ni Gerrit Lösch.

      Ndugu Lösch aliingia katika utumishi wa wakati wote katika Novemba 1, 1961, na kuhitimu katika darasa la 41 la Watchtower Bible School of Gilead. Alitumika katika kazi ya mzunguko na ya wilaya katika Austria kuanzia 1963 hadi 1976. Alioa katika 1967, naye pamoja na mkeye, Merete, baadaye walitumika kwa miaka 14 wakiwa washiriki wa familia ya Betheli ya Austria katika Vienna. Miaka minne iliyopita walihamishwa na kupelekwa katika makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn, New York, ambapo Ndugu Lösch ametumika katika Ofisi za Utekelezaji na akiwa msaidizi wa Halmashauri ya Utumishi. Akiwa na ujuzi mbalimbali katika eneo la Ulaya na kujua kwake Kijerumani, Kiingereza, Kirumania, na Kiitalia, atachangia sana kazi ya Baraza Linaloongoza.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki