Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Vijana Mtafanya Nini na Maisha Zenu?
    Mnara wa Mlinzi—1987 | Agosti 15
    • Kuishi maisha ya Kikristo ya kweli kunahusu kujidhabihu, ndiyo, hata kuteseka. Siyo mwendo rahisi, lakini ndio tulioitiwa tukiwa Wakristo. Kuukubali kunahusu ‘kutokuwa hai tena kwa ajili ya nafsi zetu wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yetu.’ (2 Wakorintho 5:15) Kufikiria vielelezo vizuri kutatusaidia sisi tutumie maisha yetu katika njia hii ya kujidhabihu.

      Vielelezo vya Kutazama

      14. Yesu aliandaa mfano gani?

      14 Kielelezo ambacho unahitaji kufikiria sana ni kile ambacho Yesu alitoa. Akiwa mtu mkamilifu, yeye angeweza kuwa mwanariadha, mwanamuziki, tabibu, au mwanasheria mkubwa zaidi sana ambaye ulimwengu umepata kujua. Lakini fikira zake zilikaziwa kupendeza Baba yake wa kimbingu, hata alipokuwa kijana. (Luka 2:42-49) Baadaye yeye alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” (Luka 4:43) Kiangazi kilichopita barua moja katika Ministry gazeti la kanisa ilieleza hivi: “Mwokozi wetu alipenda kujiondoa katika umati, kisha Yeye akaenda nyumba kwa nyumba —kuwinda nafsi. Furaha yake ilikuwa kusikilizwa na nafasi moja moja. Kisha Yeye angeweza kuumimina ukweli—upendo wa Mungu.”—Luka 10:1-16.

      15. (a) Kwa sababu gani kuhubiri nyumba kwa nyumba ni mwito wa ushindani? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba huduma ya nyumba kwa nyumba ya vijana ni yenye matokeo mazuri?

      15 Imekubaliwa kwamba, kuhubiri nyumba kwa nyumba si rahisi. Kunahitaji funzo la bidii ili kufahamu habari njema za Ufalme na kazi nyingi sana ili kutayarisha utoaji wenye maana. Pia, utumishi huu unahitaji ushujaa, kwa kuwa wenye nyumba walio wengi hawapendezwi, na hata wengine ni wenye uhasama. Hata hivyo, huduma ya nyumba kwa nyumba inayofanywa na ninyi vijana ina matokeo ya ajabu, kama ilivyosemwa katika gazeti la kimtaa wa kanisa la Kiitalia La Voce. Mwandikaji alisema hivi: “Mimi binafsi, nawapenda Mashahidi wa Yehova,” ambao, yeye alieleza, “wanakuja na kukutembelea wewe nyumbani.” Yeye alitoa maelezo hivi: “Wale ninaowajua wana tabia isiyolaumika, wenye kusema kwa njia nyororo; pia ni watu wazuri na sana sana vijana. Uzuri na ujana unapoonyeshwa, unakuwa wenye kushawishi sana.”

      16. (a) Vijana wanastahili kusifiwa kwa ajili ya utendaji gani? (b) Tengenezo la Mashahidi wa Yehova linalinganaje na makanisa katika kufanya kazi iliyo ya maana zaidi duniani?

      16 Hakika, ninyi vijana mnaokubali Kristo awe kielelezo chenu mnahitaji kusifiwa sana! Vijana zaidi ya 12,000 wenye umri wa 25 na chini wamo katika kazi ya painia katika United States, na bila shaka makumi ya maelfu zaidi wanapainia sehemu nyinginezo. (Zaburi 110:3) Mnahakikishiwa kwamba, hakuna kazi nyingine ambayo ninyi mngefanya ambayo ni ya muhimu zaidi! Hata mwandikaji wa gazeti la kanisa aliyetajwa juu alisema: “Mungu anasema kwamba kazi yenye maana kabisa ni kuzuru nyumba kwa nyumba—kuwinda nafsi,” hata hivyo anaendelea, “Unasema nini juu ya jambo hili? Ni ziara ngapi ambazo wewe na mimi tunafanya? Sijaona kazi ya aina hii ikitajwa sana katika “HUDUMA.” Je! hatuwezi kuwa wenye shukrani kwamba tunashirikiana pamoja na tengenezo linalokazia takwa la kuiga mfano wa Yesu wa kuhubiri?

      17. Timotheo alitimiza nini akiwa pengine bado tineja, na ni jambo gani linaloonyesha kwamba huenda ikawa yeye alikuwa mchanga kadiri hiyo wakati huo?

      17 Kwa kuwa yale utakayofanya na maisha yako yataongozwa sana na wale unaosifu mno, kuza sifa kubwa pia kwa kielelezo kinachotolewa na kijana Timotheo. Timotheo aliyezaliwa muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu, aliiacha jamaa yake akiwa kijana na akajiunga pamoja na mtume Paulo kwenye safari yake ya pili ya umisionari. Miezi michache baadaye watu wenye ghasia waliwalazimisha Paulo na Sila kutorokea Thesalonike, lakini si kabla wao hawajafanya wanafunzi fulani. (Matendo 16:1-3; 17:1-10, 13-15) Muda mfupi baadaye Paulo alimtuma Timotheo kwenye eneo hilo hatari ili awafariji wanafunzi hao katika majaribu yao. (1 Wathesalonike 3:1-3) Labda Timotheo alikuwa katika miaka yake ya kumalizia utineja wakati huo, kwa kuwa Paulo bado alizungumza juu ya “ujana” wake Timotheo miaka 12 hadi 14 baadaye. (1 Timotheo 4:12) Je! wewe husifu sana kijana kama huyo mwenye ushujaa, na mwenye kujidhabihu?

      18. Kwa sababu gani Paulo alikuwa akitayarisha kumtuma Timotheo kwa Wakorintho?

      18 Miaka mitano baada ya mgawo wa Timotheo wa kuwatia nguvu ndugu katika Thesalonike, Paulo aliwaandikia Wakorintho kutoka Efeso: “Mnifuate mimi. Kwa sababu hii nimemtuma Timotheo kwenu,. .. atakayewakumbusha njia zangu zilizo katika Kristo, kama vile nifundishavyo kila mahali.” (1 Wakorintho 4:16, 17) Tayari akiwa amefanya kazi pamoja na Paulo kwa miaka mitano, kijana Timotheo, alifahamiana vizuri sana na njia za Paulo za kufundisha. Yeye alijua jinsi Paulo alivyokuwa amewatolea Waefeso ujumbe, kutia na jinsi alivyokuwa amewafundisha “waziwazi, na nyumba kwa nyumba.” (Matendo 20:20, 21) Akiwa amezoezwa vizuri katika njia hizo za kuhubiri, Timotheo alikuwa msaada bora kama nini kwa makundi!

      19. Paulo alisema nini juu ya Timotheo zaidi ya miaka kumi baada ya wao kuanza kutumikia pamoja?

      19 Miaka mingine mitano au sita inapita, na Paulo yumo gerezani katika Roma. Timotheo ambaye amefunguliwa kutoka gerezani hivi majuzi, yu pamoja naye. (Waebrania 13:23) Ebu wazia tamasha hiyo: Labda akimtumia Timotheo kama mwandishi wake, Paulo anawaandikia Wafilipi barua. Akizungumza kwa makusudi, Paulo anaendelea hivi: “Natumani katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo afike kwenu karibu . . . maana sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli . . . mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili, kama mwana na baba yake.”—Wafilipi 1:1; 2:19-22.

      20. Ni jambo gani linalomfanya Timotheo awe kielelezo cha cheo chenye kusifika sana kwa vijana?

      20 Hakika, kijana Timotheo ni mfano wenye kusifika sana! Yeye alikuwa mwandamani wa Paulo mwenye kutegemeka, mwaminifu, akishikamana naye nyakati nzuri na mbaya, akimtegemeza katika kazi ya kuhubiri, na akiwa na nia ya kutumikia mahali po pote alipotumwa. Yeye alidhabihu yanayoitwa maisha ya kawaida ya nyumbani, hata hivyo, utumishi wa Mungu ulimletea uradhi na utosheki ulioje katika maisha yake! Hakika Timotheo hakuwa ‘hai tena kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, bali kwa ajili ya Kristo aliyekuwa amekufa kwa ajili yake.’ (2 Wakorintho 5:15) Je! wewe unasukumwa kuiga mfano wake?

      Ishi kwa Ajili ya Ulimwengu Mpya wa Mungu

      21. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Timotheo alikuwa mtu mwenye fikira za kiroho?

      21 Kweli, Timotheo alikuwa akiishi kwa ajili ya ulimwengu mpya wa Mungu. Yeye hakuwa akifikiria tu mambo ya sasa hivi, bali alikuwa akifikiria kuyatumia maisha yake kutokeza manufaa yenye kudumu. (Mathayo 6:19-21) Kwa kuwa baba yake Timotheo alikuwa Mgiriki na ni wazi kwamba hakuwa mwamini, huenda alimsihi Timotheo afuatie elimu ya juu na kazi ya maisha ya kilimwengu. Lakini kama matokeo ya maagizo ya kimungu kutoka kwa mama na nyanya yake, maisha ya Timotheo yalikuwa yamefungamana pamoja na kundi la Kikristo. Yeye alifuatia mapendezi ya kiroho, yaelekea aliendelea kuwa mseja angaa kwa wakati fulani, na alistahili kutumikia pamoja na mtume Paulo.—2 Timotheo 1:5.

      22. Broshua Shule inakaziaje mwendo wa maisha unaofanana na ule wa Timotheo kwa vijana leo?

      22 Namna gani wewe? Je! wewe utatumia ujana wako katika njia aliyoutumia Timotheo? Broshua Shule na Mashahidi wa Yehova ilikuwa ikielekeza kwenye njia hiyo ya maisha ilipoeleza hivi kuhusu vijana Mashahidi: “Mradi wao mkubwa katika maisha ni kutumikia vya kufaa wakiwa wahudumu wa Mungu, na wanathamini masomo ya shule kuwa msaada wa kutimiza mradi huo. Basi, kwa ujumla wanachagua mitaala inayofaa ili wajipatie riziki katika ulimwengu wa sasa. Hivyo, huenda wengi wakajifunza mitaala ya kikazi au wakahudhuria shule zinazotoa mafundisho ya kazi. Wanapomaliza shule wanatamani kutafuta kazi itakayowaruhusu wakaze fikira zao juu ya kazi yao kuu, yaani, huduma ya Kikristo.”

      23. Kwa sababu gani halipaswi kuwa jambo gumu kwa vijana Wakristo kujibu ulizo hili, Mimi nitafanya nini na maisha yangu?

      23 Kwenu ninyi mnaothamini sana yale ambayo Yehova Mungu na Mwana wake wamewafanyia, halipasi kuwa jambo gumu kujibu ulizo hili: “Mimi nitafanya nini na maisha yangu? Badala ya kuishi kwa ajili yako mwenyewe na raha ya kibinafsi, utayatumia maisha yako kufanya mapenzi ya Mungu. Utaishi, kama alivyoishi Timotheo, akiwa mtu wa kiroho.

  • Vijana Je! Mnaendelea Kiroho?
    Mnara wa Mlinzi—1987 | Agosti 15
    • Vijana Je! Mnaendelea Kiroho?

      “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.”​—1 TIMOTHEO 4:15.

      1, 2. Kuendelea kiroho kunamaanisha nini, na hakumaanishi nini?

      NI NINI maana ya kuendelea kiroho? Inamaanisha kuwa kama Yesu mchanga na Timotheo, ambao walitanguliza mapendezi ya kiroho maishani mwao. Ikiwa wewe unaendelea kiroho, utajua unalotaka kufanya na maisha yako. Wewe hutasema hivi: ‘Nitaanza kufikiria kwa uzito kuhusu kumtumikia Yehova nitakapokuwa mwenye umri mkubwa zaidi.’ La, wewe utamtumikia sasa!

      2 Kwa upande mwingine, kuendelea kiroho hakumaanishi kuwa mtawa, kujifanya mtu wa dini, au hata kuwa mtu apendaye sana kusoma. Wala hakumaanishi kuwa mwenye kuhuzunika, mzito, na kutoshirikiana kirafiki na wengine kamwe. (Yohana 2:1-10) Yehova ni Mungu mwenye furaha, naye anawataka watoto wake wa kidunia wafurahi. Kwa hiyo Mungu anakubali ushirika wa kiasi katika michezo na utendaji mwingine wa tafrija.​—1 Timotheo 1:11, NW; 4:8.

      Ubatizo Ni Ushuhuda

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki