-
Kujenga kwa Vitu Visivyoweza Kuchomwa na MotoMnara wa Mlinzi—1985 | Januari 1
-
-
hasa sisi tunajenga. Hapa “moto” unafananisha nini? Je! ni mateso ya kimwili yenye jeuri? Ni wazi sivyo. Kwa maana angalia kwamba “kazi ya kila mtu” itapitishwa kwenye “moto.” Si Wakristo wote wanaopata mateso yenye jeuri. Kwa hiyo “moto” unafananisha mkazo wo wote au kishawishi cho chote kinachoweza kuharibu hali ya kiroho ya mtu.
22. Ni mengine gani kati ya majaribu ya mfano wa moto ambayo yanaweza kupata watu fulani?
22 Kwa wengine huenda “moto” ukaja katika namna ya suala la kutokuwamo. Kwa mfano, huenda wengine wakakazwa washiriki katika utendaji mbalimbali wa kisiasa au sivyo wafungwe gerezani. (Yohana 15:19) Nyakati nyingine huenda “moto” ukaja kwa njia ya werevu zaidi. Labda ni kishawishi cha kutazama sinema au vipindi vya televisheni vinavyoonyesha ngono na jeuri. Kwa vijana Wakristo huenda “moto” ukaja katika namna ya kuweza kusumbuliwa-sumbuliwa ili wafanye ngono, kukaribishwa-karibishwa watumie dawa za kulevya au kukazwa washiriki katika tafrija ya ulimwengu inayoshusha tabia. Ile tamaa ya asili ya kutaka kukubaliwa na wengine inaweza kukaza sana vijana Wakristo wakubaliane na wenzao.—1 Yohana 2:16.
23. (a) Kwa habari ya kuelekeana na majaribu hayo, ni maulizo gani yanayotokezwa, na majibu yanategemea nini? (b) Ni jambo gani litakalozungumzwa katika makala inayofuata?
23 Wakristo wa kweli walio wengi wameshinda majaribu hayo ya mfano wa moto. Lakini, jambo la kusikitisha ni kwamba wengine wameshindwa. Kwa hiyo, tunahitaji kujiuliza: Wakati wapya ambao tumefundisha watakapoelekeana na “moto,” itakuwaje kwao? Je! watakuwa kama lile jumba zuri la kifalme lililopambwa kwa dhahabu, fedha na mawe ya thamani yasiyoweza kuchomwa na moto, kisha wasimame imara? Au watakuwa kama kile kijumba kilichojengwa kwa miti, majani na manyasi, kisha wachomeke? Bila shaka, mengi yanategemea mwanafunzi mwenyewe. Ingawa hivyo, wakati ule ule mengi yanatutegemea sisi walimu—namna sisi wenyewe tumejenga. Kwa hiyo ulizo hili linabaki: Wewe unajengaje sifa hizo za kudumu katika wale unaofundisha? Hilo litazungumzwa katika makala inayokuja.
Wewe Unaweza Kueleza:
◻ Namna ujenzi wenye muungano unavyohusika katika kufundisha wengine?
◻ Namna unavyoweka Kristo kuwa “msingi”?
◻ Ni mambo gani mtu anaweza kujifunza kutokana na lililotukia katika kundi la Korintho wa kale?
◻ “Moto” ni nini, na namna hilo linavyokazia umaana wa kujenga sifa za kudumu katika wengine?
-
-
Unapofundisha, Fikia MoyoMnara wa Mlinzi—1985 | Januari 1
-
-
Unapofundisha, Fikia Moyo
1, 2. (a) Ni nini linalohitajiwa ili kujenga katika wengine uthamini wenye kina kwa Yehova na viwango vyake? (b) Kwa sababu gani si maarifa ya kichwani tu yanayohitajiwa?
IJAPOKUWA unaweza kufanya kazi ya haraka ya kusimamisha kijumba cha nyasi, hakika huwezi kujenga jumba la kifalme kwa siku moja. Ndivyo ilivyo juu ya kufanya wanafunzi. Si kazi ndogo kujenga katika wengine uthamini wenye kina juu ya Yehova na viwango vyake. Inachukua wakati mwingi na ufundi kutokeza “majumba ya kifalme” ya namna hiyo.
2 Ili kutimiza hilo, mengi yanahusika zaidi ya kuwapa maarifa. Ni kama vile Mithali 3:1 inavyosema: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu.” Lazima wanafunzi wetu wafundishwe yanayosemwa na Biblia. Lakini zaidi ya hilo, lazima ukweli wa Biblia ukazwe juu ya mioyo yao. Ndiyo, ni lazima tufikie moyo ikiwa tutajenga sifa zisizoweza kuchomwa na moto ndani ya wale tunaofundisha, tukiwasaidia kukuza uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova Mungu.
3. (a) Kwa sababu gani “ustadi wa kufundisha” unahusiana na kama tunaufikia moyo? (b) Tunapofikiria mapendekezo fulani yenye mafaa, inakupasa ukumbuke nani?
3 Ni wazi kwamba kusema ni kwepesi kuliko kufanya. Ili kufikia mioyo ni lazima tutumie “ustadi wa kufundisha” pia, zaidi ya kuwa tu na vitu vinavyofaa vya kujengea. (2 Timotheo 4:2, NW) Haitoshi kuambia wanafunzi wetu ukweli. Bali, “ustadi wa kufundisha” unahusu kuwasaidia wafikiri na kuona sababu za mambo wanayojifunza. Si kwamba akili yetu wala njia zetu ndizo zinazoweza kutokeza ukuzi wa kiroho; baraka ya Mungu ndilo jambo la maana. (1 Wakorintho 3:5, 6) Hata hivyo, kuna mapendekezo machache yanayoweza kutusaidia tufikie mioyo ya wengine. Tunapofikiria mambo hayo, wakumbuke wale unaowafundisha—wanafunzi wako wa Biblia na watoto wako.
Weka Mfano Unaofaa
4. (a) Ni nini moja la mambo yaliyofanya Yesu apate matokeo mengi katika kufikia wengine? (b) Kwa sababu gani ni jambo la maana kuweka mfano unaofaa tunapofundisha wengine?
4 Tungeweza kuwa na mfano gani mzuri wa kufikia mioyo ya wengine kushinda Yesu Kristo mwenyewe? Kwa sababu gani yeye alipata matokeo sana katika kufikia watu? Kwanza, Yesu alizoea mambo aliyohubiri, akawekea wafuasi wake mfano halisi waufuate. (Yohana 13:15; 1 Petro 2:21) Basi, hili ndilo pendekezo la kwanza: weka mfano unaofaa. Je! si jambo la akili kwamba tunapaswa kutazamiwa kuwa na sifa zile zile zinazodumu za Kikristo ambazo sisi tunataka kujenga katika wengine? Ni kama Yesu alivyosema: “Kila mwanafunzi aliyepewa mazoezi mazuri atakuwa kama mwalimu wake.”—Luka 6:40, The New Berkeley Version.
5. Maandiko yanaonyeshaje uhusiano kati ya kuweka mfano unaofaa na kufikia mioyo ya wengine?
5 Biblia inaonyesha mara nyingi uhusiano uliopo kati ya kuweka mfano unaofaa na kufikia mioyo ya wengine. Kisa kimoja, andiko la Kumbukumbu la Torati 6:4-6 linaonyesha kwamba lazima upendo kwa Yehova uwe “katika moyo wako” mzazi kabla hujaweza kuukaza ndani ya mioyo ya watoto wako. (Mithali 20:7) Tofauti na hivyo, Yesu alikemea Wafarisayo wanafiki wa siku zake kwa sababu ‘walinena lakini hawakutenda.’ Ni ajabu basi kwamba moyo wa watu ulikuwa umekuwa ‘mzito’?—Mathayo 23:3; 13:13-15.
6. Kwa sababu gani ni jambo la maana uishi kulingana na mambo unayofundisha? (Warumi 2:21-23)
6 Kwa hiyo ni lazima kuwe na upatani kati ya yale unayofundisha na yale unayozoea. Kwa mfano, ikiwa unataka kujenga katika wanafunzi au watoto wako upendo kwa Yehova na tamaa ya kumpendeza yeye, basi je! hawapaswi waweze kuona kutokana na sala zako, usemi na matendo ushuhuda wa kwamba una upendo na tamaa hiyo ndani yako? Ikiwa unataka kukaza ndani yao ufuataji thabiti wa kanuni za Biblia, je! kwanza hawapaswi kuona kwamba wewe hujaribu kwa maneno na matendo yako kuziepuka kanuni hizo? Wale tunaofundisha, hasa watoto wetu, wanaangalia mara nyingi yale tunayotenda kuliko yale tunayosema. Watu wale wengine wanapoona kwamba tunaishi kupatana na tunayofundisha, tutakuwa katika hali nzuri zaidi ya kufikia mioyo yao.
Tokeza Maulizo
7, 8. (a) Mengi ya mafanikio yetu katika kufikia wengine yanategemea nini? (b) Kwa sababu gani maulizo ni yenye msaada katika kufikia moyo?
7 Pendekezo la pili, ambalo ni jambo jingine lililofanya Yesu awe mwalimu mwenye matokeo sana, ni matumizi ya maulizo. Yesu alikuwa stadi sana katika kufanya watu wafikiri na kuona sababu za mambo. (Mathayo 17:24-27) Mengi ya mafanikio yako katika kufikia mioyo ya wale unaofundisha yanategemea matumizi yako ya maulizo. Kwa sababu gani?
8 Kwanza, kwa kutokeza maulizo unaweza kujua kama mwanafunzi wako anaelewa kweli kweli yale anayojifunza. Ingawaje, asipoelewa na kuzikubali habari hizo, zinawezaje kweli kutia mizizi moyoni mwake? (Luka 8:15) Pili, ili kufikia moyo ni jambo la msaada kujua mambo yaliyo moyoni. Huenda mawazo yaliyotangulia kudhaniwa na pia mafundisho ya uongo ya kidini yakawa yamekwama sana ndani yake. Kwa kuwa hatuwezi kusoma moyo, tunahitaji kutokeza maulizo ambayo hasa yanafanya mwanafunzi aeleze maoni ya moyoni mwake kwa maneno yake mwenyewe. Fikiria mifano fulani.
9, 10. Toa mfano wa matumizi yenye matokeo ya maulizo ya kutafuta maoni.
9 Tuseme mnazungumza sura ya 10, “Roho Waovu Ni Wenye Nguvu,” katika kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Halafu mnafika fungu la 18, kwenye ukurasa wa 97, ambapo ulizo lililopigwa chapa linauliza, “Ni mfano gani wa Wakristo wa kwanza katika Efeso ambao ni mzuri kufuata ikiwa mtu anataka kuacha kupashana habari na roho waovu?” Huenda mwanafunzi wako akajibu kwa usahihi kutokana na fungu, lakini maoni yake ni nini hasa? Labda yeye alizoea kupashana habari na roho waovu kwa miaka mingi kisha akawa anaamini sana zoea hilo. Ikiwa ndivyo, je! sasa amesadikishwa kwamba anapaswa kujitenga nalo? Huenda ikakupasa kuuliza hivi: ‘Wewe una maoni gani juu ya jambo hili? Unaweza kutumiaje habari hizi maishani mwako?’ Namna atakavyojibu sasa huenda ikafunua ni kwa kadiri gani habari hizo zimegusa moyo wake.
10 Mfano mwingine, huenda ukawa unafikiria na mtoto wako sura ya 26, “Vile Vita vya Kufanya Yaliyo Mema,” katika kitabu icho hicho. Katika ukurasa wa 220, ulizo la “b” la fungu la 8 linauliza, “Ni maoni gani, kama yalivyosemwa na kijana mmoja, ingekuwa hekima kuwa nayo?” Huenda kwanza mtoto wako akajibu kutokana na fungu, bila kueleza hasa maoni yake. Huenda ukahitaji kuchunguza ndani kidogo: ‘Lakini wewe una maoni gani juu ya jambo hili? Je! wewe unaona hilo ni jambo linalowezekana?’ Au unaweza kutokeza hali: ‘Tuseme vijana fulani shuleni wanavuta sigara na kukupa moja. Tuseme hesabu fulani ya vijana hao wangekuwa wakiangalia linalotendeka kisha waanze kukufanyia mzaha kwa sababu hukukubali. Wewe ungefanya nini?’ Wakati maulizo ya namna hiyo yanapotumiwa kwa akili, yanaweza kukusaidia ujue yaliyo katika moyo wa mtoto wako.
11. (a) Kwa sababu gani uangalifu unahitajiwa wakati wa kutumia maulizo hayo? (b) Kwa sababu gani wazazi hasa wanahitaji kujiangalia wakati watoto wao wanapotoa maoni mabaya? (Wakolosai 3:21)
11 Hata hivyo, jiangalie. Nyakati nyingine maulizo ya namna hiyo huenda yakaleta majibu yanayokushangaza au kukukatisha tamaa. Sasa iweje? Ikiwa habari mnayozungumza ni ya kuudhi mtu haraka, huenda ikawa vizuri zaidi kutolazimisha unayesema naye akubaliane nawe bali useme: ‘Kwa sasa acha tuendelee. Tutaongea tena juu ya hilo wakati mwingine.’ (Yohana 16:12) Hasa uangalifu huo unahitajiwa upande wa wazazi. Maoni mabaya yanapotolewa, zuieni hasira. Hamtaki kuharibu njia ya kupashana habari. Mtoto wenu akiogopa kueleza maoni yake, mtajuaje yaliyo moyoni mwake ili mweze kumsaidia?
Kazia Hekima ya Kutii Sheria za Mungu
12, 13. (a) Kwa sababu gani kuona hekima ya kutii sheria za Mungu kutagusa moyo wa mwanafunzi? (b) Ni nini linalohusika katika kusaidia mwanafunzi aone kwamba kutii Yehova ndio mwendo wa hekima?
12 Pendekezo la tatu ni kusaidia mwanafunzi wako aone hekima ya kutii sheria za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 4:5, 6; 10:12, 13) Jambo hilo linaweza kugusa moyo wake. Namna gani hivyo? Ikiwa yeye anasadiki kwamba kushika sheria za Yehova ni kwa faida bora zaidi zake mwenyewe, huenda hilo likamwongoza kumpenda Mungu na kutaka kumpendeza.—Zaburi 112:1.
13 Unaweza kusaidiaje wale unaofundisha waone hekima ya kutii sheria za Mungu? Tunaweza kutolea hilo mfano kwa kulinganisha sheria za Yehova na ishara zinazosema “Usipite Hapa.” Ingawa ishara hiyo yenyewe inatosha kuwa onyo, je! wewe hungekubali kwamba wakati inapoonyesha sababu ya onyo inakuwa vyepesi zaidi kutii? Kwa mfano, ikiwa ishara inasema “Usipite Hapa—Unaweza Kupigwa na Umeme,” basi aliyetaka kupita hapo anaelekea zaidi kutii onyo hilo kwa kutambua uwezekano wa yeye binafsi kupatwa na hatari.
14. (a) Ni kwa njia gani ungeweza kufikiri pamoja na mwanafunzi wako ili kumsaidia aone sababu gani mwendo fulani ni wa hekima au wa kipumbavu? (b) Ni maandiko gani yanayoonyesha umaana wa kutoa sababu inayofanya mwendo fulani uwe mwema au mbaya?
14 Ndivyo ilivyo kuhusu sheria za Mungu. Usiambie mwanafunzi wako mambo ambayo Biblia inasema ni mema na yale ambayo ni mabaya kisha uachie hapo; msaidie aone sababu gani mwendo fulani ni wa hekima au wa kipumbavu. Fikiri naye kwa kumpa sababu juu ya namna kutii sheria za Mungu kutakavyomsaidia. Msaidie aone matokeo ya kupuuza matakwa hayo. Nyakati nyingine Biblia yenyewe inafanya hivyo. Tafadhali jisomee Mithali 22:24, 25; 23:4, 5; 24:15, 16, 19, 20. Angalia kwamba katika kila kisa Biblia inatoa sababu ya linalofanya mwendo fulani uwe mwema au mbaya.
15. Tumia maulizo na maandiko yaliyoonyeshwa ili kuzungumza hekima ya kutii yale ambayo Mungu anasema juu ya udanganyifu na uasherati.
15 Kwa mfano, fikiria namna maulizo na maandiko yanayofuata yanavyokazia hekima ya kutii sheria za Mungu.
Kusema uongo, Kuiba: Kwa sababu gani udanganyifu unaleta madhara? (Mithali 15:27; 20:10; Ufunuo 21:8) Kwa sababu gani ni jambo lenye faida uwe mnyofu unaposhughulika na wengine? (Mithali 3:3, 4; 12:19; Waebrania 13:18)
Uasherati: Ukosefu wa adili unaweza kutuumizaje? (Mithali 5:9; 7:21-23; 1 Wakorintho 6:18) Unaweza kuleteaje wengine madhara? (1 Wathesalonike 4:6; 1 Wakorintho 5:6; Waebrania 12:15, 16) Unafaidikaje unapotii viwango vya adili vya Biblia? (Mithali 5:18, 19; Waebrania 13:4)
Baada ya kufikiria sheria ya Biblia kwa kuitolea sababu namna hiyo, unaweza kuuliza hivi: ‘Wewe una maoni ya kwamba Yehova anataka sisi tupate faida zilizo bora zaidi? Je! unakubali kwamba sheria zake kwa kweli hazitunyimi wema wo wote?’
16. Kufikiri kwa njia hiyo huenda kukawa na matokeo gani juu ya mwanafunzi wako?
16 Mnapoendelea kujifunza, toa sababu za namna iyo hiyo juu ya sheria ya Mungu kuhusu ulevi, kulipa kodi, kuvuta sigara, suala la damu, na mambo kama hayo. Kwa njia hiyo mwanafunzi au mtoto wako anasaidiwa aone kwamba sheria zote za Mungu ni kwa faida yetu. Si kwamba nyakati zote mwanafunzi wako anapaswa kuwa na uhitaji wa kupewa sababu ili kumtii Mungu. Lakini mifano michache huenda ikasaidia kufikia moyo wake, imwongoze atake kupendeza Mungu. Hivyo, wakati “moto,” au jaribu, unapokuja, yeye atatii neno la Mungu kwa utayari zaidi.—1 Wakorintho 3:13.
Wasaidie Wamjue Mungu
17. Ni pendekezo gani zaidi linaloweza kukusaidia ufikie moyo wa mwanafunzi wako?
17 Pendekezo la nne ni hili: saidia mwanafunzi wako amjue Mungu. (Yohana 17:3) Zaidi ya kumsaidia mwanafunzi wako ajue tu kwamba Yehova yuko na ana jina, msaidie apate kumjua kindani. Hilo litagusa moyo wake kwa sababu kumjua Yehova ni kumpenda.
18. Wakati wa funzo, ungewezaje kuvuta fikira kwenye sifa za Yehova?
18 Unaweza kusaidiaje mwanafunzi wako amjue Yehova kindani? Kwanza, huwezi kupenda mtu usipojua sifa zake, njia zake. Kwa hiyo wakati wa funzo, kumbuka nyakati zote kuvuta fikira kwenye sifa za Yehova zisizolinganika na za mwingine. Mara nyingi hilo linaweza kufanywa hata kama ni habari gani inayozungumzwa. Kwa mfano, mnapozungumza ukombozi, ungeweza kutua mahali panapofaa na kuuliza: ‘Mpango wa ukombozi unatukuzaje kina cha upendo wa Yehova kwetu?’ Au mnapofikiria ruhusa ya Mungu juu ya uovu, ungeweza kuuliza hivi: ‘Yehova ameonyeshaje ustahimilivu mwingi ujapokuwako uovu wa mwanadamu?’ au, ‘Yehova alionyeshaje hekima isiyolinganika na ya mwingine kwa namna alivyoshughulika na uasi katika Edeni?’ Kufikiri kwa njia hiyo kutasaidia kujenga katika mwanafunzi wako maoni thabiti ya kujitoa kwa Yehova. Atakuja kumwona Yehova kuwa Mtu mwenye sifa za kupendeka, za kuvutia.
19, 20. (a) Ni nini zaidi linalohitajiwa ili kumjua Yehova kindani? (b) Jambo lililoonwa lililo katika fungu linaonyeshaje umaana wa kuweka mfano unaofaa kuhusu sala?
19 Zaidi ya hilo, huwezi kupata kujua mtu kweli kweli bila namna fulani ya kupashana habari. Vivyo hivyo, mwanafunzi wako hawezi kufurahia uhusiano wa kindani pamoja na Yehova bila kupashana habari naye. Kwa kuthamini hilo, fundisha mwanafunzi wako jinsi ya kusali. Msaidie aone mambo ya namna nyingi yanayoweza kutiwa katika sala. (1 Yohana 5:14) Jenga ndani yake uthamini kwa Yehova kuwa Ndiye anayesikia sala na kuzijibu pia. (Zaburi 65:2) Mtie moyo aeleze maoni yake ya ndani kabisa, ‘amwage moyo wake’ kwa Yehova.—Zaburi 62:8, NW.
20 Hapa tena, ni jambo la maana wewe mwenyewe uweke mfano. Je! sala zako zinaonyesha kina cha kujitoa kwako kwa Mungu? Jambo hilo linaweza kuwa na matokeo mazuri sana juu ya wale unaofundisha, kutia na watoto wako. Fikiria jambo hili lililoonwa.
Miaka kadha iliyopita, mume na mke Wakristo walikuwa wakifundisha kivulana wao wa miaka mitatu kusali. Usiku mmoja, baada ya kivulana huyo kusali Yehova abariki Mama na Baba, alimwomba Yehova abariki “Wali.” “Wali” alikuwa nani? Wazazi wake hawakujua, naye kivulana akaanza kusali kwa ukawaida sana kwa ajili ya “Wali”! Mwishowe, baada ya kukosa kujua kwa muda mrefu, wakatambua lililokuwa limetukia. Kivulana alikuwa akisali kwa ajili ya akina ndugu katika Malawi (waliokuwa wakipata mateso wakati huo), lakini yeye alitamka vibaya kwa kusema “Wali.” Jambo la maana ni kwamba, kivulana huyo alikuwa amesikia wazazi wake wakisali kwa njia hiyo, naye aliiga mfano mwema wao. Ebu wazia walivyojisikia wazazi hao!
Je! hiyo haionyeshi umaana wa kuweka mfano mwema katika kufundisha wengine jinsi ya kusali?
Thawabu
21. (a) Kulingana na 1 Wakorintho 3:14, 15, wewe mjenzi wa Kikristo unaweza kutazamia nini? (b) Je! ile “thawabu” ni zawadi ya uzima wa milele katika Utaratibu Mpya wa Mungu? Eleza.
21 Basi, ikiwa tutajenga katika wengine sifa zisizoweza kuchomwa na moto, kuwasaidia wakuze uhusiano mwema pamoja na Yehova, lazima tufikie mioyo yao. Huenda isiwe vyepesi kufanya hivyo, lakini inathawabisha. Paulo alionyesha hivyo aliposema: “Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea [kwa sababu alijenga vibaya, bila kutumia vitu visivyoweza kuchomwa na moto], atapata hasara [yaani, alichojenga kitakwenda hasara kwenye “moto”]; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto.” “Thawabu” ile ni nini? Ni wazi Paulo alikuwa akifikiria kitu tofauti na ile zawadi ya uzima wa milele katika Utaratibu Mpya wa Mungu, kwa maana angalia kwamba yule aliyejenga vibaya anaipoteza “thawabu,” ingawa huenda yeye mwenyewe akaokolewa kama akiweza kuupita “moto.”—1 Wakorintho 3:14, 15.
22, 23. (a) Ni thawabu gani aliyopokea mtume Paulo kuhusiana na ndugu zake Wakristo huko Thesalonike? (b) Tamaa ya moyo wako ni kupata “thawabu” gani, na unaweza kuipokeaje?
22 Basi, thawabu hiyo ni nini? Jambo fulani ambalo Paulo aliambia Wathesalonike linasaidia kufahamu. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo waliokuwa wakiteswa huko: “Tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari, ni nini? Je! si ninyi, mbele za Bwana wetu Yesu, wakati wa kuja kwake? Maana ninyi ndinyi utukufu wetu, na furaha yetu.” (1 Wathesalonike 2:19, 20) Paulo alikuwa amesaidia Wathesalonike hao wakaingia katika njia ya ukweli. Na ingawa tangu mwanzo wao walikuwa wamepatwa na mateso, walikuwa wakisimama imara. Thawabu ya Paulo ilikuwa furaha ya kuwaona wakivumilia ujapokuwako upinzani. Hilo lilithibitisha kwamba Paulo alikuwa amejenga vizuri.
23 Ndivyo ilivyo kwa habari yetu. Je! tamaa ya moyo wako si kusaidia wale unaofundisha wakuze sifa za kudumu za Kikristo zitakazowawezesha wasimame imara kujapokuwa na vishawishi na mikazo inayoweza kuwapata? Ndiyo, inathawabisha kama nini kuona wanafunzi wako wa Biblia na watoto wako wakisimama kwa kushinda majaribu hayo ya mfano wa moto! Hiyo inashuhudia kwamba umejenga vizuri. Hiyo na iwe thawabu yako unapojenga juu ya msingi unaofaa kwa vitu visivyoweza kuchomwa na moto unapotegemea Yehova abariki jitihada zako.—Kutoka w8/l/84.
Unaweza kukumbuka?
Ili kufikia moyo—
◻ Kwa sababu gani ni jambo la maana kuweka mfano unaofaa?
◻ Ni maulizo ya namna gani yanayosaidia, na kwa sababu gani?
◻ Kwa sababu gani mwanafunzi wako anahitaji kuona hekima ya kutii sheria za Mungu?
◻ Kwa sababu gani ni lazima mwanafunzi wako ajifunze jinsi ya kusali?
[Picha katika ukurasa wa 19]
Sala zako zinaonyesha kina cha kujitoa kwako kwa Mungu? Jambo hilo linaweza kugusa moyo wa mtoto wako
-