-
Vijana Mtafanya Nini na Maisha Zenu?Mnara wa Mlinzi—1987 | Agosti 15
-
-
Vijana Mtafanya Nini na Maisha Zenu?
“Ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.”—2 WAKORINTHO 5:15
1. Watu wamesema maneno gani ya shukrani, na kwa sababu gani?
1‘ASANTE! Ninakuwia uhai wangu!’ Watu ambao wanaokolewa kutoka nyumba inayoteketea au kufa maji wamewaambia hivyo wale waliowaokoa. Na vijana Wakristo wenye kuthamini wamewaambia wazazi wao maneno kama hayo. Hawakuwa wakielekeza tu kwenye maisha ya kimwili ambayo wamepokea kutoka kwa wazazi wao bali hasa utunzaji wenye upendo na agizo ambalo limewaweka vijana hao katika njia ya kupokea “ahadi aliyotuahidia, yaani uzima wa milele.”—1 Yohana 2:25.
2. Ni kwa ufahamu wa habari gani inawapasa kulifikiria ulizo hili, Mtafanya nini na maisha zenu?
2 Upendo ndio uliosukuma Yehova Mungu kufanya uzima wa milele, “uzima ulio kweli kweli,” upatikane kwa kila mmoja wetu. “Yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.” (1 Timotheo 6:19; 1 Yohana 4:10) Ebu fikiria, pia, upendo ambao Mwana wake Yesu alionyesha kwa kufa kifo chenye maumivu ili sisi tupate uzima wa milele! (Yohana 15:13) Kwa sababu ya mambo hayo yanayotangulia, Mtafanya nini na maisha zenu?
3. Ni kitu gani ambacho mara nyingi kinaamua yale ambayo watu watafanya na maisha zao?
3 Washauri wa wanafunzi shuleni au watu wanaopendezwa na wakati wao ujao, mara nyingi wanawauliza vijana ulizo hili, katika njia moja au nyingine. Ni nini kitakachoamua jibu lenu? Je! litaamuliwa tu na mambo mnayopendelea kibinafsi? Je! jambo litakaloamua litakuwa shauri la wale ambao wanawataka ninyi mpate cheo salama katika ulimwengu usio wa kidini? Au je! yale ambayo mtafanya na maisha zenu yataamuliwa na makusudio bora zaidi? Kikumbusho kilichoongozwa na roho kinasema: “Tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.” (2 Wakorintho 5:15) Ndiyo, jinsi lilivyo jambo zuri wakati njia tunayotumia maisha zetu inapoonyesha shukrani kwa yale ambayo Yesu Kristo na Baba yake wa kimbingu wametufanyia sisi!
Vielelezo Vinavyoigwa na Wengi
4. Ni nani walio vielelezo vinavyoigwa na walio wengi sana leo?
4 Hata hivyo, ni watu gani wanaopendwa na wengi zaidi sana leo, wale ambao kwa kawaida vijana wanachagua kama vielelezo vya kuiga? Je! si watu walio matajiri na mashuhuri katika ulimwengu, bila kujali viwango vyao vya adili? Unapotazama katika vyumba vya vijana wengi, ni picha za nani unazoona zikiwa zinaning’inia ukutani? Mara nyingi ni za wanamuziki, wachezaji sinema mashuhuri, na wanariadha. Kwa kawaida vijana wanaota ndoto za kupata siku moja mafanikio ya kilimwengu yanayofanana na hayo au labda kumwoa au kuolewa na mtu ambaye ana sifa za kimwili za watu hawa. Namna gani wewe? Unataka nini maishani?
5, 6. (a) Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba mafanikio ya kilimwengu yanashindwa kuleta uradhi wa kweli? (b) Chanzo cha uradhi wa kweli ni nini?
5 Ikiwa ungepata mafanikio ya kilimwengu ya watu mashuhuri wanaosifiwa, je! ungekuwa kweli na furaha na uradhi? Mmoja wa wanamke waigizaji michezo wenye mafanikio zaidi sana wa Hollywood alisema: ‘Nimepata mwonjo wangu wa mali na vitu vyote vya kimwili. Haimaanishi cho chote. Katika kila jamaa yenye utajiri wa kutosha kuwa na dimbwi la kuogelea kuna mikazo na matatizo ya akili, bila kutaja talaka na watoto wanaowachukia wazazi wao.’—Mhubiri 5:10; 1 Timotheo 6:10.
6 Mwanafunzi mmoja mwanariadha mwenye kutokeza, aliyekuwa mshindi wa mbio kubwa za wanawake za kilometa 10 katika New York katika 1981, alipata kukatishwa tumaini sana hivi kwamba alijaribu kujiua. “Nimejifunza kweli nyingi kuhusu maisha katika miezi michache iliyopita,” akaandika mwanamke huyo baadaye. ‘Ukweli mmoja ni kwamba uradhi wa kweli haupatikani katika njia ambazo watu wengi wanajitahidi kupata usitawi na ufaulu. Kwangu, uradhi haukutokana na kuwa mwanafunzi aliyepokea maksi za A, mkimbiaji shujaa wa mkoa au mwenye umbo la kuvutia.’ Ndiyo, watu wanahitaji kujifunza kwamba uradhi wa kweli unatokana tu na kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu, ambaye peke yake ndiye anaweza kutoa amani na furaha ya kweli.—Zaburi 23:1, 6; 16:11.
7. Kuhusu kupata uradhi wa kweli, elimu ya koleji na mafanikio ya kilimwengu ni ya muhimu kadiri gani?
7 Kwa wazi, basi, haikupasi utake kuwaiga wale ambao wanang’ang’ana ili wapate umashuhuri na mali tu. Hata waandikaji wa ulimwengu wanaona kwamba mafanikio ya kilimwengu yanashindwa kuleta uradhi wa kweli. Mchangiaji habari za safu za magazeti Bill Reel aliandika hivi: “Unahitimu kutoka kwenye koleji ukiwa na ndoto za wakati ujao. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, yaliyo mengi zaidi ya matazamio yako yatakosa kutimia. Sitaki kukuvunja moyo, lakini unaweza kuusikia ukweli pia: Unapopata mali unazotamani, ukizipata, unapopata mafanikio unayofuatia, ukiyapata, hayataridhisha. Badala yake, wakati ule ule unapotazamia kujifurahisha kwa ushindi wenye shangwe, unahisi ukiwa tupu badala ya kuwa umetimiza jambo, umeshuka moyo badala ya kutiwa moyo, umefadhaika badala ya kuwa na amani.”—New York Daily News, Mei 26, 1983.
8. Kuna sababu gani yenye nguvu ya kutokufuatia kazi ya maisha ya kilimwengu?
8 Lakini kwetu sisi ambao tu macho kuhusu maana ya matukio ya ulimwengu kwa msaada wa unabii wa Biblia, kuna sababu zenye nguvu sana za kutotanguliza maishani kazi ya maisha ya kilimwengu. (Mathayo 24:3-14) Tunaweza kujilinganisha sisi wenyewe na mtu anayeona jengo lenye ishara: “Kampuni Hii Inafilisika.” Je! tungetafuta kazi humo? Bila shaka la! Na ikiwa tungefanya kazi katika kampuni kama hiyo, kwa hekima tungetafuta kazi mahali pengine. Basi, ishara hiyo inaonekana wazi kila mahali katika taasisi za ulimwengu huu: “Zinafilisika —Mwisho Umekaribia!” Ndiyo, “Ulimwengu unapitilia mbali,” ndivyo Biblia inavyotuhakikishia. (1 Yohana 2:17, NW) Kwa hiyo, kwa hekima, hatutataka kuchagua wale ambao wanahusika sana nao kuwa vielelezo vya kuigwa.
Shauri la Kufuata
9. Wale ambao wanaonekana kuwa wanakutakia mema huenda wakatoa shauri gani la kilimwengu?
9 Maisha yako yanaongozwa si na wale ambao unaheshimu tu bali pia mara nyingi na watu wa ukoo na marafiki ambao, kama wanavyosema, ‘wanakutakia mema.’ ‘Lazima ujiruzuku,’ huenda wakasema. Kwa hiyo huenda wakakushauri kupata elimu ya koleji au ya chuo kikuu ili ujitayarishe mwenyewe kupata kazi ya ustadi. ‘Mwandikaji wa Biblia Luka alikuwa tabibu,’ huenda wakasema, ‘na mtume Paulo alifundishwa na mwalimu wa Torati Gamalieli,’ (Wakolosai 4:14; Matendo 5:34; 22:3) Hata hivyo, changanua kwa uangalifu sana shauri hilo.
10. Luka na Paulo walitoa shauri gani, na ni jambo gani linaloweza kusemwa kuhusu utendaji wao kabla ya kuwa Wakristo?
10 Tabibu Luka hakuwatia moyo kamwe Wakristo wafuate kiolezo cha kazi yake ya kwanza kwa kuwa daktari, bali Luka alionyesha maisha ya Yesu na mitume yaigwe. Kwa wazi Luka alipata kuwa tabibu kabla yeye hajajifunza juu ya Kristo lakini baadaye aliweka huduma ya Kikristo yake kwanza maishani. Ndivyo hali ilivyokuwa na Paulo. Badala ya kuwatia moyo wengine wamwige yeye kama vile yeye alivyokuwa amemwiga Gamalieli, Paulo aliandika hivi: “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo.” Paulo alithamini sana maarifa ya Kristo hivi kwamba kwa kulinganisha yeye alisema kwamba aliyafikiria mambo yake aliyofuatia kwanza “kuwa kama mavi.”—1 Wakorintho 11:1; Wafilipi 3:8.
11. (a) Petro alimwambia nini Yesu, na kwa sababu gani? (b) Yesu aliitikiaje?
11 Kumbuka, kusukumwa na hisia za moyoni kunaweza kuwafanya hata wale wanaokupenda watoe shauri baya. Kwa mfano, Yesu alipozungumuza juu ya yale yaliyomngojea yeye wakati wa huduma yake katika Yerusalemu, mtume Petro alijibu hivi: “Ujifadhili, Bwana; hutapatwa na jambo hili hata kidogo.” Petro alimpenda Yesu naye hakutaka Yesu ateseke. Hata hivyo Yesu alimkemea Petro kwa sababu Yeye alitambua kwamba kutimiza mapenzi ya Mungu kungetia ndani kuteseka na pia kuuawa na wapinzani,—Mathayo 16:21-23, NW.
12. Ni shauri gani ambalo watu wenye makusudio mazuri wanaweza kuwapa vijana, na kwa sababu gani?
12 Vivyo hivyo, wazazi fulani au marafiki huenda wakakuvunja moyo utoke kwenye mwendo wa kujidhabihu. Kwa sababu ya kusukumwa na hisia za moyoni zisizofaa, huenda wakasitasita kukutia moyo uchukue mgawo katika huduma ya painia wa wakati wote, kutumikia kama mmisionari, au kujitolea ufanye kazi katika afisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Huenda wakasema: ‘Badala yake, mbona, usioe au kuolewa kisha utulie karibu nasi.’ Au, ‘Unajua, kazi ni ngumu sana huko Betheli. Labda ni afadhali ukae nasi.’ Kwa maneno mengine, kama vile Petro alivyosema, “Ujifadhili.”
13. (a) Ni maoni gani yaliyorekebishwa ambayo Petro alisema? (b) Ni nini kinachohusika katika kuwa Mkristo wa kweli?
13 Hata watumishi wa Yehova wanahitaji kurekebisha kuwaza kwao nyakati nyingine. Petro alihitaji kufanya hivyo, na akiwa na maoni yaliyorekebishwa, yeye aliandika hivi: “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.” (1 Petro 2:21) Kuishi maisha ya Kikristo ya kweli kunahusu kujidhabihu, ndiyo, hata kuteseka. Siyo mwendo rahisi, lakini ndio tulioitiwa tukiwa Wakristo. Kuukubali kunahusu ‘kutokuwa hai tena kwa ajili ya nafsi zetu wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yetu.’ (2 Wakorintho 5:15) Kufikiria vielelezo vizuri kutatusaidia sisi tutumie maisha yetu katika njia hii ya kujidhabihu.
Vielelezo vya Kutazama
14. Yesu aliandaa mfano gani?
14 Kielelezo ambacho unahitaji kufikiria sana ni kile ambacho Yesu alitoa. Akiwa mtu mkamilifu, yeye angeweza kuwa mwanariadha, mwanamuziki, tabibu, au mwanasheria mkubwa zaidi sana ambaye ulimwengu umepata kujua. Lakini fikira zake zilikaziwa kupendeza Baba yake wa kimbingu, hata alipokuwa kijana. (Luka 2:42-49) Baadaye yeye alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” (Luka 4:43) Kiangazi kilichopita barua moja katika Ministry gazeti la kanisa ilieleza hivi: “Mwokozi wetu alipenda kujiondoa katika umati, kisha Yeye akaenda nyumba kwa nyumba —kuwinda nafsi. Furaha yake ilikuwa kusikilizwa na nafasi moja moja. Kisha Yeye angeweza kuumimina ukweli—upendo wa Mungu.”—Luka 10:1-16.
15. (a) Kwa sababu gani kuhubiri nyumba kwa nyumba ni mwito wa ushindani? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba huduma ya nyumba kwa nyumba ya vijana ni yenye matokeo mazuri?
15 Imekubaliwa kwamba, kuhubiri nyumba kwa nyumba si rahisi. Kunahitaji funzo la bidii ili kufahamu habari njema za Ufalme na kazi nyingi sana ili kutayarisha utoaji wenye maana. Pia, utumishi huu unahitaji ushujaa, kwa kuwa wenye nyumba walio wengi hawapendezwi, na hata wengine ni wenye uhasama. Hata hivyo, huduma ya nyumba kwa nyumba inayofanywa na ninyi vijana ina matokeo ya ajabu, kama ilivyosemwa katika gazeti la kimtaa wa kanisa la Kiitalia La Voce. Mwandikaji alisema hivi: “Mimi binafsi, nawapenda Mashahidi wa Yehova,” ambao, yeye alieleza, “wanakuja na kukutembelea wewe nyumbani.” Yeye alitoa maelezo hivi: “Wale ninaowajua wana tabia isiyolaumika, wenye kusema kwa njia nyororo; pia ni watu wazuri na sana sana vijana. Uzuri na ujana unapoonyeshwa, unakuwa wenye kushawishi sana.”
16. (a) Vijana wanastahili kusifiwa kwa ajili ya utendaji gani? (b) Tengenezo la Mashahidi wa Yehova linalinganaje na makanisa katika kufanya kazi iliyo ya maana zaidi duniani?
16 Hakika, ninyi vijana mnaokubali Kristo awe kielelezo chenu mnahitaji kusifiwa sana! Vijana zaidi ya 12,000 wenye umri wa 25 na chini wamo katika kazi ya painia katika United States, na bila shaka makumi ya maelfu zaidi wanapainia sehemu nyinginezo. (Zaburi 110:3) Mnahakikishiwa kwamba, hakuna kazi nyingine ambayo ninyi mngefanya ambayo ni ya muhimu zaidi! Hata mwandikaji wa gazeti la kanisa aliyetajwa juu alisema: “Mungu anasema kwamba kazi yenye maana kabisa ni kuzuru nyumba kwa nyumba—kuwinda nafsi,” hata hivyo anaendelea, “Unasema nini juu ya jambo hili? Ni ziara ngapi ambazo wewe na mimi tunafanya? Sijaona kazi ya aina hii ikitajwa sana katika “HUDUMA.” Je! hatuwezi kuwa wenye shukrani kwamba tunashirikiana pamoja na tengenezo linalokazia takwa la kuiga mfano wa Yesu wa kuhubiri?
17. Timotheo alitimiza nini akiwa pengine bado tineja, na ni jambo gani linaloonyesha kwamba huenda ikawa yeye alikuwa mchanga kadiri hiyo wakati huo?
17 Kwa kuwa yale utakayofanya na maisha yako yataongozwa sana na wale unaosifu mno, kuza sifa kubwa pia kwa kielelezo kinachotolewa na kijana Timotheo. Timotheo aliyezaliwa muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu, aliiacha jamaa yake akiwa kijana na akajiunga pamoja na mtume Paulo kwenye safari yake ya pili ya umisionari. Miezi michache baadaye watu wenye ghasia waliwalazimisha Paulo na Sila kutorokea Thesalonike, lakini si kabla wao hawajafanya wanafunzi fulani. (Matendo 16:1-3; 17:1-10, 13-15) Muda mfupi baadaye Paulo alimtuma Timotheo kwenye eneo hilo hatari ili awafariji wanafunzi hao katika majaribu yao. (1 Wathesalonike 3:1-3) Labda Timotheo alikuwa katika miaka yake ya kumalizia utineja wakati huo, kwa kuwa Paulo bado alizungumza juu ya “ujana” wake Timotheo miaka 12 hadi 14 baadaye. (1 Timotheo 4:12) Je! wewe husifu sana kijana kama huyo mwenye ushujaa, na mwenye kujidhabihu?
18. Kwa sababu gani Paulo alikuwa akitayarisha kumtuma Timotheo kwa Wakorintho?
18 Miaka mitano baada ya mgawo wa Timotheo wa kuwatia nguvu ndugu katika Thesalonike, Paulo aliwaandikia Wakorintho kutoka Efeso: “Mnifuate mimi. Kwa sababu hii nimemtuma Timotheo kwenu,. .. atakayewakumbusha njia zangu zilizo katika Kristo, kama vile nifundishavyo kila mahali.” (1 Wakorintho 4:16, 17) Tayari akiwa amefanya kazi pamoja na Paulo kwa miaka mitano, kijana Timotheo, alifahamiana vizuri sana na njia za Paulo za kufundisha. Yeye alijua jinsi Paulo alivyokuwa amewatolea Waefeso ujumbe, kutia na jinsi alivyokuwa amewafundisha “waziwazi, na nyumba kwa nyumba.” (Matendo 20:20, 21) Akiwa amezoezwa vizuri katika njia hizo za kuhubiri, Timotheo alikuwa msaada bora kama nini kwa makundi!
19. Paulo alisema nini juu ya Timotheo zaidi ya miaka kumi baada ya wao kuanza kutumikia pamoja?
19 Miaka mingine mitano au sita inapita, na Paulo yumo gerezani katika Roma. Timotheo ambaye amefunguliwa kutoka gerezani hivi majuzi, yu pamoja naye. (Waebrania 13:23) Ebu wazia tamasha hiyo: Labda akimtumia Timotheo kama mwandishi wake, Paulo anawaandikia Wafilipi barua. Akizungumza kwa makusudi, Paulo anaendelea hivi: “Natumani katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo afike kwenu karibu . . . maana sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli . . . mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili, kama mwana na baba yake.”—Wafilipi 1:1; 2:19-22.
20. Ni jambo gani linalomfanya Timotheo awe kielelezo cha cheo chenye kusifika sana kwa vijana?
20 Hakika, kijana Timotheo ni mfano wenye kusifika sana! Yeye alikuwa mwandamani wa Paulo mwenye kutegemeka, mwaminifu, akishikamana naye nyakati nzuri na mbaya, akimtegemeza katika kazi ya kuhubiri, na akiwa na nia ya kutumikia mahali po pote alipotumwa. Yeye alidhabihu yanayoitwa maisha ya kawaida ya nyumbani, hata hivyo, utumishi wa Mungu ulimletea uradhi na utosheki ulioje katika maisha yake! Hakika Timotheo hakuwa ‘hai tena kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, bali kwa ajili ya Kristo aliyekuwa amekufa kwa ajili yake.’ (2 Wakorintho 5:15) Je! wewe unasukumwa kuiga mfano wake?
Ishi kwa Ajili ya Ulimwengu Mpya wa Mungu
21. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Timotheo alikuwa mtu mwenye fikira za kiroho?
21 Kweli, Timotheo alikuwa akiishi kwa ajili ya ulimwengu mpya wa Mungu. Yeye hakuwa akifikiria tu mambo ya sasa hivi, bali alikuwa akifikiria kuyatumia maisha yake kutokeza manufaa yenye kudumu. (Mathayo 6:19-21) Kwa kuwa baba yake Timotheo alikuwa Mgiriki na ni wazi kwamba hakuwa mwamini, huenda alimsihi Timotheo afuatie elimu ya juu na kazi ya maisha ya kilimwengu. Lakini kama matokeo ya maagizo ya kimungu kutoka kwa mama na nyanya yake, maisha ya Timotheo yalikuwa yamefungamana pamoja na kundi la Kikristo. Yeye alifuatia mapendezi ya kiroho, yaelekea aliendelea kuwa mseja angaa kwa wakati fulani, na alistahili kutumikia pamoja na mtume Paulo.—2 Timotheo 1:5.
22. Broshua Shule inakaziaje mwendo wa maisha unaofanana na ule wa Timotheo kwa vijana leo?
22 Namna gani wewe? Je! wewe utatumia ujana wako katika njia aliyoutumia Timotheo? Broshua Shule na Mashahidi wa Yehova ilikuwa ikielekeza kwenye njia hiyo ya maisha ilipoeleza hivi kuhusu vijana Mashahidi: “Mradi wao mkubwa katika maisha ni kutumikia vya kufaa wakiwa wahudumu wa Mungu, na wanathamini masomo ya shule kuwa msaada wa kutimiza mradi huo. Basi, kwa ujumla wanachagua mitaala inayofaa ili wajipatie riziki katika ulimwengu wa sasa. Hivyo, huenda wengi wakajifunza mitaala ya kikazi au wakahudhuria shule zinazotoa mafundisho ya kazi. Wanapomaliza shule wanatamani kutafuta kazi itakayowaruhusu wakaze fikira zao juu ya kazi yao kuu, yaani, huduma ya Kikristo.”
23. Kwa sababu gani halipaswi kuwa jambo gumu kwa vijana Wakristo kujibu ulizo hili, Mimi nitafanya nini na maisha yangu?
23 Kwenu ninyi mnaothamini sana yale ambayo Yehova Mungu na Mwana wake wamewafanyia, halipasi kuwa jambo gumu kujibu ulizo hili: “Mimi nitafanya nini na maisha yangu? Badala ya kuishi kwa ajili yako mwenyewe na raha ya kibinafsi, utayatumia maisha yako kufanya mapenzi ya Mungu. Utaishi, kama alivyoishi Timotheo, akiwa mtu wa kiroho.
-
-
Vijana Je! Mnaendelea Kiroho?Mnara wa Mlinzi—1987 | Agosti 15
-
-
Vijana Je! Mnaendelea Kiroho?
“Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.”—1 TIMOTHEO 4:15.
1, 2. Kuendelea kiroho kunamaanisha nini, na hakumaanishi nini?
NI NINI maana ya kuendelea kiroho? Inamaanisha kuwa kama Yesu mchanga na Timotheo, ambao walitanguliza mapendezi ya kiroho maishani mwao. Ikiwa wewe unaendelea kiroho, utajua unalotaka kufanya na maisha yako. Wewe hutasema hivi: ‘Nitaanza kufikiria kwa uzito kuhusu kumtumikia Yehova nitakapokuwa mwenye umri mkubwa zaidi.’ La, wewe utamtumikia sasa!
2 Kwa upande mwingine, kuendelea kiroho hakumaanishi kuwa mtawa, kujifanya mtu wa dini, au hata kuwa mtu apendaye sana kusoma. Wala hakumaanishi kuwa mwenye kuhuzunika, mzito, na kutoshirikiana kirafiki na wengine kamwe. (Yohana 2:1-10) Yehova ni Mungu mwenye furaha, naye anawataka watoto wake wa kidunia wafurahi. Kwa hiyo Mungu anakubali ushirika wa kiasi katika michezo na utendaji mwingine wa tafrija.—1 Timotheo 1:11, NW; 4:8.
Ubatizo Ni Ushuhuda
3. Yaelekea sana Timotheo alibatizwa lini?
3 Kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo na kubatizwa ni ushuhuda wa kwamba kijana anaendelea kiroho. Ikiwa, kama ilivyodokezwa, Timotheo alikuwa angali tineja wakati alipokuwa mwandamani mmisionari wa mtume Paulo, labda Timotheo alibatizwa alipokuwa katika miaka ya katikati ya utineja au miaka ya mapema ya utineja. Yeye alifundishwa maandiko tangu utotoni, na mara alipofanywa kuwa tayari kwa maarifa ya kutosha na uthamini, yeye hakusitasita kubatizwa.—2 Timotheo 3:15.
4. Ni ulizo gani aliloulizwa Filipo, na ijapokuwa mwenye kuliuliza alikuwa ndipo tu amejifunza juu ya Kristo, kwa nini Filipo alimpa ombi lake?
4 Namna gani ninyi matineja ambao mmefundishwa katika Maandiko? Je! mmelifikiria ulizo hili: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Ulizo hilo liliulizwa na mwanamume mmoja katika karne ya kwanza ambaye alifahamiana vizuri sana na Maandiko lakini alikuwa tu ndipo amejifunza juu ya utu wa Kristo. Kweli, mtu huyo hakujua yote yaliyoko ili kujua makusudi ya Mungu, hata hivyo yeye alisukumwa na uthamini wenye kina kirefu kwa yale aliyojua! Hivyo, mwanafunzi Filipo hakuwa na sababu halali ya kutombatiza yeye.—Matendo 8:26-39.
5. Ni mambo gani yanayohitajiwa kwako ili ubatizwe?
5 Ni nini kinachokuzuia wewe usibatizwe? Bila shaka, ili ustahili, unahitaji kufahamu yanayohusika. Lazima kweli kweli uwe unataka kumtumikia Yehova kwa sababu unampenda yeye. Unahitaji pia kujitoa kwake kibinafsi katika sala. Kwa kuongezea, lazima uwe unashikamana na matakwa ya Mungu ya adili na uwe na maarifa ya kutosha katika kushiriki imani yako pamoja na wengine. Hivyo unapostahili, ni muhimu ufuatilie ubatizwe.—Mathayo 28:19, 20; Matendo 2:38.
6. Ubatizo unaweza kulinganishwa na nini, na ni lazima ufuatwe na nini?
6 Ingawa kubatizwa ni ushuhuda wa kwamba unaendelea kiroho, kumbuka kwamba ubatizo ni hatua ya kwanza tu. Kwa kujitoa wakfu kwa Yehova, wewe unakuwa mgeni katika ulimwengu huu unaotawalwa na Shetani. Hivyo kujitoa wakfu kunaweza kulinganishwa na kuomba uzima wa milele katika mfumo mpya wa Mungu, na sherehe ya kidesturi ya kubatizwa ni wonyesho mbele ya mashahidi ukithibitisha uhakika huo. (Yohana 12:31; Waebrania 11:13) Baada ya hapo lazima uishi kulingana na wakfu wako kwa uaminifu ili upokee zawadi ya Mungu ya uzima wa milele.—Warumi 6:23.
Kunashuhudiwa kwa Mwenendo
7. Mwelekeo wako kuhusu vitu vya ulimwengu unahusianaje na kuendelea kwako kiroho?
7 Ikiwa wewe unaendelea kiroho au la jambo hilo litashuhudiwa pia na nia yako kuelekea mambo ya ulimwengu. Mambo gani? Yanatia ndani mtindo wa maisha wa kufanya unavyotaka, dawa za kulevya, uhuru wa kufanya ngono, sinema zisizo za adili, muziki wenye kuingiza mawazo mabaya, mazungumzo machafu, kucheza dansi kunakoamsha nyege, majivunoa ya kikabila na kitaifa, na kadhalika. (1 Yohana 2:16; Waefeso 5:3-5) Vijana, hasa, wanahitaji kuwa macho. Kumbuka, jinsi unavyotenda kuhusu mambo haya kutafunua hali ya afya yako ya kiroho.—Mithali 20:11.
8. Kwa sababu gani vijana wengine wanasita-sita kubatizwa?
8 Shetani anahakikisha kwamba njia za ulimwengu zenye ukosefu wa adili zionekana kuwa zenye kuvutia sana. Kwa kweli, kijana mmoja mwenye miaka 15 alisema hivi: “Kadiri tunavyotazama ngono na dawa za kulevya kwenye TV, ndivyo zinavyozidi kuonekana kuwa za kawaida katika jamii.” Vijana wasioshiriki katika njia za ulimwengu wanafanywa wahisi kwamba wao si watu wa kawaida na kwamba wanakosa raha. Je! wewe huhisi hivyo nyakati fulani? Wengine ambao wanashirikiana na kundi wanahisi hivyo, nao wanasita-sita. Kijana mmoja alipoulizwa juu ya kubatizwa, yeye alisema hivi: ‘Sitaki kubatizwa sasa kwa sababu huenda nikafanya jambo fulani ambalo litafanya nitengwe na ushirika.’ Hata hivyo huwezi kuepuka kufanya uamuzi au kusita-sita kati ya maoni mawili tofauti. Wakati mmoja nabii wa Mungu alisema: “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana [Yehova, NW] akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni mungu, haya! mfuateni yeye.”—1 Wafalme 18:21.
9. Ni ulinzi gani unaopatikana kwa kuendelea kiroho?
9 Kwa kweli, kwa kuepuka njia za ulimwengu zenye ukosefu wa adili, unachokosa tu ni matata mengi. Mwanamke mmoja alikiri hivi: “Nilishindwa na hisia kubwa mno ya kuchukizwa na majuto kwa sababu ya maisha niliyokuwa nikiishi, nilikuwa nimeyavunjia heshima maisha yangu na kujidanganya mwenyewe pamoja na mtoto ambaye nilikuwa nimetungwa mimba.” Ndiyo, yanayoonekana kuwa uzuri na kimetimeti cha ulimwengu wa Ibilisi ni mazingaombwe tu, udanganyifu. Hauna kitu cho chote chenye thamani. Kufuata njia za ulimwengu kunaongoza kwenye kupata mimba nje ya ndoa, jamaa zilizovunjika, ugonjwa wenye kuambukizwa kwa njia ya ngono, na kuvurugika akili na huzuni isiyoelezeka. Kwa hiyo sikiliza shauri, endelea kiroho. ‘Acha mabaya, utende mema.’—1 Petro 3:11.
10. Kijana anayeendelea kiroho atatii onyo gani la upole na ni mifano ya nani atafuta?
10 Kijana anayeendelea kiroho atatii onyo la upole la mtume Paulo: “Katika uovu mgeuzwe watoto wachanga, bali katika akili zenu mkawe watu wazima.” (1 Wakorintho 14:20) Hakika kijana Timotheo alitumia shauri hili. Je! unaweza kuwazia yeye akitafuta kuandamana na vijana wa ulimwengu wa siku zake wenye ufisadi? Hasha! Waandamani wake walikuwa watumishi wenzake Mungu. (Mithali 13:20) Uige mfano wake. Ukikaribia kujiingiza katika utendaji wo wote unaotiliwa mashaka, jiulize mwenyewe: Je! Timotheo au Yesu angefanya hivi?
Kunashuhudwa kwa Funzo la Biblia
11. Vijana wa ulimwengu wanakosa njozi gani, nayo inapatikana na kudumishwaje?
11 Makala moja kutoka Italia iliyochapishwa katika World Press Review ilisema hivi: “Madanganyo na kukata tamaa kwa vijana kunapanda kila siku, na hakuna mtu anayeweza kuwatolea wakati ujao wenye kutia moyo.” Macho yaliyapofushwa ya wale walio katika ulimwengu wa Shetani hayaoni ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya na wakati ujao wenye utukufu unaowangojea wale wanaostahili uzima humo. (2 Wakorintho 4:4; Mithali 29:18; 2 Petro 3:13) Lakini vijana wanaoendelea kiroho wana njozi hiyo ambayo inawekwa ikiwa imeng’aa na wazi kupitia funzo la Biblia la kawaida.
12. (a) Ili kupata maarifa ya Mungu, lazima tuyafuatieje? (b) Kwa sababu gani maarifa hayo yanastahili jitihada?
12 Je! ulimwengu mpya wa Mungu ni halisi kwako? Unaweza kuwa halisi, lakini kuupata kunahitaji jitihada halisi kwa upande wako. Unahitaji kukuza hamu nyingi kwa ajili ya ufahamu wa Biblia ili ‘uutafute kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika.’ (Mithali 2:1-6) Ni kitu gani kinachomfanya mtu anayetafuta hazina aendelee kuitafuta na kuchimba, nyakati nyingine kwa miaka mingi? Anatamani kwa shauku utajiri ambao hazina hiyo itamletea. Hata hivyo maarifa ni yenye thamani sana zaidi ya hazina ya kimwili. “Na uzima wa milele ndio huu,” akasema Yesu, “wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Ikiwa kweli unayaamini yale aliyosema Yesu hapo, funzo la Biblia litafuatiwa kwa shauku nalo litakuthawabisha wewe kwa jambo ambalo ni lenye thamani zaidi kuliko vito vyenye thamani nyingi.—Mithali 3:13-18.
13. Vijana wanaoendelea kiroho watafuata vidokezi gani vya kujifunza?
13 Utapata kwamba unavyojifunza zaidi, ndivyo na hamu yako kwa chakula cha kiroho itakavyokuwa yenye nguvu zaidi. Jifunze njia nzuri za kujifunza. Usichore mistari kwa majibu tu, lakini fungua maandiko ya Biblia yanayotajwa, kisha tafuta maandiko yanayohusiana na hayo kupitia mitajo ya Biblia kwenye pambizo. Pia unaweza kufanya uchunguzi zaidi kwa kutumia fahirisi, kama ile Watch Tower Publications Index 1930-1985. Changanua jinsi habari hizo zinavyohusika na jinsi zinavyoweza kutumiwa. Zungumza na wengine kuhusu yale unayojifunza. Kufanya hivyo kutaingiza sana mambo akilini mwako nayo yatawatia moyo wengine wafanye uchunguzi pia. Kwa kujitia mwenyewe kweli kweli katika funzo, utakuwa ukitii shauri lililotolewa kwa kijana Timotheo: “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.”—1 Timotheo 4:15; 2 Timotheo 2:15.
Kunaonyeshwa Kwenye Mikutano na Katika Utumishi
14. Ni nini kinachosaidia kuifanya mikutano ya Kikristo kuwa yenye kufurahisha zaidi, na unaweza kuwatiaje wengine moyo unapohudhuria?
14 Unapofurahia funzo la Biblia na umetayarisha vizuri, mikutano ya Kikristo inafurahisha zaidi. (Zaburi 122:1; Waebrania 2:12) Unatazamia hata zaidi kushiriki katika sehemu zinazohitaji ushirika wa wasikilizaji na kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Lakini unapohudhuria mikutano, kuna njia nyingine za kutimiza agizo la ‘kutiana moyo’ na “kuchochea kupenda na kazi nzuri.” (Waebrania 10:24, 25, NW) Kwa mfano, je! wewe unachukua hatua ya kwanza ya kuongea na wengine? Salamu ya kirafiki, “Habari, nimefurahi kukuona!” au ulizo fulani la unyofu, “Unahisije?” linaweza kutia moyo, hasa linapotoka kwa kijana.
15. Unaweza kujifanyaje upatikane kufanya utumishi unaohitajiwa, na kwa nini ni vizuri kukumbuka mfano wa Kristo?
15 Kuna kazi nyingi sana inayohusika katika kuendesha kundi. Je! wewe unaweza kushiriki? Yaelekea, kijana Timotheo alimfanyia Paulo utumishi mwingi wenye msaada—alitumwa, alinunua vifaa, alipeleka ujumbe, na kadhalika. Ikiwa wewe hujafanya hivyo, mbona usiwatajie wazee nia yako ya kutaka kusaidia. Labda utaombwa upeane migawo ya mikutano, uliweke jumba katika hali safi, au ufanye utumishi mwingine wenye uhitaji. Kumbuka, Kristo aliosha miguu ya wanafunzi wake, kwa hiyo hakuna kazi yo yote ambayo inashusha cheo cha mtu anayeendelea kiroho.—Yohana 13:4, 5.
16. Ni utendaji gani ambao gazeti la pindi kwa pindi la Kikatoliki lilitambua kuwa daraka la Kikristo?
16 Tunapotazama dini nyingine, hakika tunaweza kuwa wenye shukrani kwa mazoezi tunayopokea katika mikutano yetu kwa ajili ya kazi ya muhimu sana ya kuhubiri. Akiandika katika U.S. Catholic Septemba uliopita, Kenneth Guentert alisema hivi: “Mimi nilikua katika siku ambazo Wakatoliki hawakupaswa kusoma Biblia kwa sababu wangepata maoni ya kigeni—kama kufikiri kwamba Wakristo wanapaswa kwenda huku na huku wakigonga milango wakijaribu kuongoa watu. Kisha ukaja [mkutano] Vatikani wa Pili, nami nikaanza kuisoma Biblia. Hakika; sasa nafikiri Wakristo wanapaswa kwenda huku na huku wakigonga milango na kujaribu kuongoa watu.” Yeye aliongezea hivi: “Si kwamba ninahisi nikiwa na raha sana kwa sababu ya oni hilo, ninyi mnaelewa; lakini ukisoma Agano Jipya, inakuwa vigumu kuepuka mkataa huu.”—Mathayo 10:11-13; Luka 10:1-6; Matendo 20:20, 21.
17. Huduma inaweza kukufurahishaje zaidi?
17 Ndiyo, Wakristo wa kwanza walikuwa watendaji katika kuhubiri nyumba kwa nyumba, na kwa wazi vijana kama Timotheo walikuwako kwenye huduma hiyo pamoja na wale wenye umri mkubwa zaidi. Hata hivyo, kwa kukubali wazi, kwa watu wengine leo hii si kazi yenye kufurahisha sana. Kwa sababu gani? Ufundi ni sehemu kubwa. Kwa mfano, unapofanya vizuri katika michezo, je! huifurahii zaidi? Ndivyo ilivyo na huduma. Unavyozidi kuwa stadi katika kutumia Biblia na kuzungumzia vichwa vya Biblia, huduma itakuwa chanzo cha furaha, hasa unapopata mtu ambaye unaweza kushiriki pamoja naye maarifa yenye kutoa uzima. Kwa hiyo endelea kiroho! Fanyia mazoezi utoaji wako wa nyumba kwa nyumba. Pata vidokezi kutoka kwa wengine. Mwombe Yehova msaada.—Luka 11:13.
Kwa Uhusiano Pamoja na Wale Wenye Umri Mkubwa Zaidi
18. Yesu na Timotheo walifurahia mahusiano ya namna gani pamoja na watu wenye umri mkubwa zaidi?
18 Wakati Yesu alipokuwa kijana mwenye umri wa miaka 12 tu, yeye alifurahia kutumia wakati pamoja na wale wenye umri mkubwa zaidi na kuzungumza mambo ya kiroho. Wakati mmoja wazazi wake walimpata “hekaluni, ameketi katikati ya waalimu akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” (Luka 2:46) Ndivyo ilivyokuwa na Timotheo. Mtume Paulo na waandamani wake walipotembelea Listra, kwa wazi Timotheo alifurahia ushirika wao na alisikiliza mafundisho yao. Yeye alikuwa na uhusiano uo huo pamoja na ndugu wa kundi lake ambao walimpendekeza sana.—Matendo 16:1-3.
19. Kwa sababu gani hasa Paulo alimchagua Timotheo awe mwandamani wa kusafiri, naye Timotheo alikuwaje msaada?
19 Ijapokuwa Timotheo aliwafanyia wengine utumishi wa kimwili kwa nia, Paulo alimchagua yeye kuwa mwandamani wake wa kusafiri hasa kwa sababu ya uwezo wake wa kuhudumia mahitaji ya kiroho ya watu. Kwa sababu hiyo, watu wenye ghasia walipomlazimisha Paulo kuondoka Thesalonike, yeye alimtuma kijana Timotheo awafariji na kuwatia nguvu wanafunzi wapya. Kwa hiyo Timotheo hakuwa na shauku ya kujifunza kutokana na watu wenye umri mkubwa zaidi tu na kufurahia ushirika wao, yeye pia alikuwa msaada halisi wa kiroho kwao.—Matendo 17:1-10; 1 Wathesalonike 3:1-3.
20. Wewe utakuwa mwenye hekima kufanya nini, nawe unaweza kuwatolea watu wenye umri mkubwa zaidi utumishi gani?
20 Utakuwa mwenye hekima ukiwaiga Yesu na Timotheo na kuwa na shauku ya kupata manufaa kutokana na maarifa na mambo ambayo watu wenye umri mkubwa zaidi wameona. Tafuta ushirika wao na uwaulize maulizo. Lakini pia onyesha maendeleo yako ya kiroho kwa kuwa mwenye msaada kwao. Je! kuna watu wazee-wazee au wagonjwa ambao wangethamini ikiwa wewe ungewanunulia vitu fulani au kuwafanyia utumishi mwingine unaohitajiwa? Labda unaweza kuwatembelea tu, uwasomea habari fulani, na kushiriki pamoja nao mambo ambayo umeona katika huduma.
Daraka la Wazazi na Wengine
21. Daraka la wazazi ni la umuhimu kadiri gani, na ni jambo gani lisiloweza kutiliwa mkazo kupita kiasi?
21 Kwa sehemu kubwa afya ya kiroho ya vijana inategemea maagizo na mfano unaotolewa na wazazi wao. (Mithali 22:6) Hakika Yesu alinufaika kutokana na mwongozo aliyopewa na wazazi wake wa kidunia wenye kumwogopa Mungu. (Luka 2:51, 52) Na hakuna shaka lo lote Timotheo asingekuwa kijana mwenye kuendelea kiroho kama alivyokuwa kama asingalipata mazoezi kutoka kwa mama yake na nyanya yake. (2 Timotheo 1:5; 3:15) Umuhimu wa maagizo ya Biblia ya kawaida hauwezi kukaziwa kupita kiasi! Mkiwa wazazi, je! ninyi mnautoa? Au je! unapuuzwa?
22. (a) Wazazi wanapoliona funzo la Biblia la jamaa kuwa la muhimu, watoto wanavutwaje? (b) Wazazi wanapaswa kuwapa watoto wao mwongozo gani?
22 Mwanamume kijana katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova anaeleza kwamba katika miaka ya kukua, sehemu isiyobadilika-badilika ya maisha yao ya jamaa ilikuwa funzo la Biblia la kila juma pamoja na watoto. “Nyakati nyingine baba angekuwa amechoka sana kwa sababu ya kazi hivi kwamba ilikuwa vigumu aepuke kuzinzia lakini hata hivyo funzo lilifanywa, na jambo hilo lilitusaidia sisi tuthamini uzito walo.” Wazazi, haielekei kwamba watoto wenu watathamini sana mambo ya kiroho ninyi msipoyathamini. Kwa hiyo wekeni mbele yao miradi ya upainia na umisionari na utumishi wa Betheli. Wasaidieni wathamini kwamba huduma ni kazi ya maisha iliyo na wakati ujao na kwamba hakuna wakati ujao wo wote katika kazi ya maisha ya kilimwengu.—Linganisha 1 Samweli 1:26-28.
23. Wengine kundini wanaweza kuwasaidiaje vijana waendelee kiroho?
23 Wengine pia, wanaweza kuwasaidia vijana waendelee kiroho. Unaweza kuweka mradi wa kuzungumza pamoja nao mikutanoni. Pia, jaribu kuwahusisha katika baadhi ya utendaji wako. Mzee, akiwa na ruhusa ya wazazi, huenda akapanga kumchukua kijana aende pamoja naye kwenye mgawo wa kutoa hotuba au kumhusisha katika matembezi. (Ayubu 31:16-18) Jambo ambalo huenda likaonekana kuwa dogo linaweza kumaanisha mengi. Mwangalizi mmoja asafiriye, alipoona kwamba kijana mmoja aliyekuwa akisikiliza hotuba yake hakuwa na Biblia, yeye alimpa zawadi ya Biblia baadaye. Kijana huyo alifurahi sana, si kwa sababu ya zawadi hiyo tu bali pia kwa sababu ya kupendezwa kulikoonyeshwa. Zaidi ya miaka 30 baadaye, kijana huyo, ambaye sasa yeye ni mzee, angali anakumbuka kwa upendo wonyesho wa upendo wa ndugu huyo.
24. Ni jambo gani ambalo ni lenye kusisimua kutambua, na azimio letu linapaswa kuwa nini?
24 Je! si jambo linalosisimua kutambua kwamba kuna mamia ya maelfu ya “wanaume vijana kama matone ya umande” wanaotangaza ujumbe wa Ufalme wenye kuburudisha na kwamba kuna angalau hesabu inayolingana na hiyo ya wanawake vijana wanaofanyiza ‘jeshi kubwa linalotangaza habari njema’? Wote na wajitie katika kuendelea kiroho, nasi sote na tuwasaidie wafanye hivyo.—Zaburi 110:3, NW; 68:11.
Maswali kwa Ajili ya Kurudia
◻ Ni nini kinachoweza kumsaidia kijana aamue wakati wa kubatizwa?
◻ Mwenendo wa kijana unakadiriaje maendeleo yake ya kiroho?
◻ Ni nini kinachoweza kuwasaidia vijana wafurahie mikutano na utumishi wa shambani?
◻ Vijana wanapasa wakuze uhusiano gani pamoja na watu wenye umri mkubwa zaidi?
◻ Wazazi na watu wenye umri mkubwa zaidi wanaweza kuwasaidiaje vijana?
-