-
Kwa Nini Lililo Baya Liripotiwe?Mnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
-
-
Kwa Nini Lililo Baya Liripotiwe?
WATU fulani katika Afrika Magharibi husema kwamba, “afunuaye jambo huwa adui ya watu.” Hivyo ndivyo ilivyotukia kwa Olu alipomshtaki ndugu yake mkubwa juu ya kufanya ngono ya maharimu na dada yake. “Wewe ni mwongo!” huyo ndugu yake akapiga yowe. Ndipo akampiga Olu vibaya, akamfukuza katika nyumba ya familia, na kuchoma nguo za Olu zote. Wanakijiji walimwunga mkono ndugu yake. Akiwa hatakikani tena kijijini, Olu alilazimika kuondoka. Ni baada tu ya huyo msichana kuonekana kuwa ana mimba ndipo watu walipong’amua kwamba Olu alikuwa amesema kweli. Huyo ndugu aliungama, na Olu akarudishwa kwenye upendeleo. Mambo yangaliweza kuwa tofauti sana na yalivyokuwa. Olu angaliweza kuuawa.
Kwa wazi, wale ambao hawampendi Yehova yamkini hawafurahii kufunuliwa makosa yao. Mwelekeo wenye dhambi wa kibinadamu ni kukinza karipio na kumwonea uchungu yeyote anayelitoa. (Linganisha Yohana 7:7.) Si ajabu kwamba watu wengi wako kimya kabisa inapohusu kufunua makosa ya wengine kwa wale ambao wana mamlaka ya kuyasahihisha.
Kuthamini Ubora wa Karipio
Hata hivyo, miongoni mwa watu wa Yehova, kuna mtazamo tofauti kuelekea karipio. Wanaume na wanawake wa kimungu huthamini sana mpango ambao Yehova amefanya wa kuwasaidia wenye kukosea ndani ya kutaniko la Kikristo. Wao huitambua nidhamu hiyo kuwa wonyesho wa fadhili-upendo zake.—Waebrania 12:6-11.
Hilo laweza kutolewa kielezi na tukio fulani katika maisha ya Mfalme Daudi. Ijapokuwa alikuwa mtu mwadilifu tangu ujana na kuendelea, kuna wakati ambapo alitumbukia katika kosa zito. Kwanza, alifanya uzinzi. Kisha, katika kujaribu kufunika kosa lake, akapanga mume wa huyo mwanamke auawe. Lakini Yehova alimfunulia nabii Nathani dhambi ya Daudi, ambaye alimkabili Daudi kwa moyo mkuu juu ya hilo jambo. Akitumia kielezi chenye nguvu, Nathani alimwuliza Daudi jambo ambalo apasa kufanyiwa mtu tajiri ambaye alikuwa na kondoo wengi lakini ili kumkaribisha rafikiye akachukua na kumchinja kondoo wa pekee, kipenzi, aliyethaminiwa sana, wa mtu maskini. Daudi, aliyekuwa mchungaji hapo zamani, aliwaka kwa ghadhabu na hasira. Akasema hivi: “Mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa.” Ndipo Nathani alipokitumia kielezi hicho kimhusu Daudi, akisema hivi: “Wewe ndiwe mtu huyo”!—2 Samweli 12:1-7.
Daudi hakumkasirikia Nathani; wala hakujaribu kujitetea mwenyewe wala hakuishia kutoa mashtaka. Badala ya hivyo, kemeo la Nathani liligusa sana dhamiri yake. Akiwa ameumia moyoni, Daudi aliungama hivi: “Nimemfanyia BWANA dhambi.”—2 Samweli 12:13.
Kufichuliwa kwa dhambi ya Daudi na Nathani, kukifuatwa na karipio la kimungu, kulileta matokeo mazuri. Ijapokuwa Daudi hakukingwa na matokeo ya kosa lake, alitubu na kupatanishwa na Yehova. Daudi alihisije juu ya karipio hilo? Aliandika hivi: “Mwenye haki na anipige, itakuwa fadhili; anikemee, itakuwa kama mafuta kichwani; kichwa changu kisikatae.”—Zaburi 141:5.
Katika siku yetu pia, watumishi wa Yehova waweza kujihusisha na kosa zito, hata wale ambao wamekuwa waaminifu kwa miaka mingi. Kwa kutambua kwamba wazee waweza kusaidia, watu walio wengi zaidi huchukua hatua ya kwanza kuwafikia kwa ajili ya msaada. (Yakobo 5:13-16) Lakini huenda nyakati nyingine mkosaji akajaribu kuficha dhambi yake, kama alivyofanya Mfalme Daudi. Twapaswa kufanya nini tukija kujua juu ya kosa zito katika kutaniko?
Ni Daraka la Nani?
Wazee wajuapo juu ya kosa zito, wao humfikia mtu anayehusika na kumtolea msaada na sahihisho lihitajiwalo. Ni daraka la wazee kuwahukumu watu hao ndani ya kutaniko la Kikristo. Kwa kuwa waangalifu juu ya hali ya kiroho ya kutaniko, wao husaidia na kuonya kwa upole yeyote anayechukua hatua isiyo ya hekima au yenye kosa.—1 Wakorintho 5:12, 13; 2 Timotheo 4:2; 1 Petro 5:1, 2.
Lakini vipi ikiwa wewe si mzee na unakuja kujua juu ya kosa zito la Mkristo mwingine? Miongozo inapatikana katika Sheria ambayo Yehova alilipa taifa la Israeli. Hiyo Sheria ilitaarifu kwamba ikiwa mtu alikuwa shahidi wa matendo ya uasi, uchochezi, kuua kimakusudi, au uhalifu mwingine mbaya, ilikuwa ni daraka lake kuuripoti na kushuhudia aliyojua. Andiko la Mambo ya Walawi 5:1 lataarifu hivi: “Na mtu awaye yote akifanya dhambi, kwa kuwa ameisikia sauti yenye kuapisha, naye akawa ni shahidi, kwamba aliona au kujua, asipolifunua neno lile, ndipo atakapouchukua uovu wake mwenyewe.”—Linganisha Kumbukumbu la Torati 13:6-8; Esta 6:2; Mithali 29:24.
Ijapokuwa hawako chini ya Sheria ya Kimusa, Wakristo leo wanaweza kuongozwa na kanuni zake za msingi. (Zaburi 19:7, 8) Kwa hiyo ukijua juu ya kosa zito la Mkristo mwenzako, wapaswa kufanya nini?
Kushughulikia Hilo Jambo
Kwanza kabisa, ni jambo la maana kuwe na sababu halali ya kuamini kwamba kosa zito kwa kweli limetokea. “Usimshuhudie [“usiwe shahidi dhidi ya,” NW] jirani yako pasipo sababu,” mtu mwenye hekima alitaarifu. “Wala usidanganye kwa midomo yako.”—Mithali 24:28.
Huenda ukaamua kuwaendea wazee moja kwa moja. Si kosa kufanya hivyo. Hata hivyo, kwa kawaida, mwendo wenye upendo zaidi ni kumfikia mhusika. Labda mambo ya hakika ni tofauti na vile yaonekanavyo kuwa. Au labda hiyo hali tayari inashughulikiwa na wazee. Zungumza kwa utulivu na huyo mtu juu ya jambo hilo. Ikiwa sababu yabaki ya kuamini kwamba kosa zito limefanywa, mtie moyo awafikie wazee kwa msaada, na umweleze hekima ya kufanya hivyo. Usizungumze na wengine juu ya jambo hilo, kwa maana hiyo ingekuwa porojo.
Ikiwa huyo mtu haripoti kwa wazee katika kipindi cha wakati ambacho chatosha, basi wapaswa kuripoti. Kisha mzee mmoja au wawili watazungumza juu ya jambo hilo pamoja na mshtakiwa. Hao wazee wahitaji ‘waulize na kutafuta, wakiuliza kwa bidii’ kuona ikiwa kosa limefanywa. Ikiwa limefanywa, watashughulikia kesi hiyo kulingana na miongozo ya Kimaandiko.—Kumbukumbu la Torati 13:12-14.
Angalau mashahidi wawili wanatakwa ili kuthibitisha shtaka la utendaji kosa. (Yohana 8:17; Waebrania 10:28) Mtu huyo akikana shtaka na kuwe hakuna ushuhuda mwingine isipokuwa huo wako, jambo hilo litaachwa mikononi mwa Yehova. (1 Timotheo 5:19, 24, 25) Hilo linafanywa kwa kujua kwamba vitu vyote “viko uchi” kwa Yehova na kwamba ikiwa huyo mtu ni mwenye hatia, dhambi zake ‘zitampata’ hatimaye.—Waebrania 4:13; Hesabu 32:23.
Lakini tuseme kwamba huyo mtu anakana hilo shtaka nawe ndiwe shahidi wa pekee dhidi yake. Je, wewe waweza sasa kustahili kushtakiwa na mshtakiwa kuwa mchongezi? La, isipokuwa uwe umepiga porojo na wale ambao hawahusiki katika jambo hilo. Si jambo la uchongezi kuripoti hali zinazoathiri kutaniko kwa wale walio na mamlaka na daraka la kusimamia na kusahihisha mambo. Kwa kweli, ni jambo ambalo lapatana na tamaa yetu kufanya lililo sahihi na lenye uaminifu-mshikamanifu sikuzote.—Linganisha Luka 1:74, 75.
Kudumisha Utakatifu Katika Kutaniko
Sababu moja ya kuripoti kosa ni kwamba jambo hilo huhifadhi usafi wa kutaniko. Yehova ni Mungu safi, Mungu mtakatifu. Yeye hutaka wale wote ambao humwabudu wawe safi kiroho na kiadili. Neno lake lililopuliziwa laonya kwa upole hivi: “Kama watoto watiifu, komeni kuwa mkifanyizwa kulingana na mtindo wa tamaa zenu mlizokuwa nazo hapo zamani katika kutokuwa kwenu na ujuzi, bali, kwa kupatana na Mtakatifu aliyewaita, nyinyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Lazima mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:14-16) Watu mmoja-mmoja wazoeao ukosefu wa usafi au utendaji makosa wanaweza kuliletea kutaniko zima unajisi na hali ya kutopendelewa na Yehova ikiwa hatua ya kuwasahihisha au kuwaondoa watu haitachukuliwa.—Linganisha Yoshua, sura ya 7.
Barua za mtume Paulo kwa kutaniko la Kikristo lililokuwa Korintho huonyesha jinsi ambavyo kuripoti kosa kulisaidia kutakaswa kwa watu wa Mungu huko. Katika barua yake ya kwanza, Paulo aliandika hivi: “Kwa kweli uasherati waripotiwa miongoni mwenu, tena uasherati wa namna ambayo haimo hata miongoni mwa mataifa, kwamba mtu fulani anaye mke wa baba yake.”—1 Wakorintho 5:1.
Biblia haituambii ni kutoka kwa nani huyo mtume alipata ripoti hiyo. Huenda ikawa Paulo alipata kujua juu ya hali ya mambo kutoka kwa Stefanasi, Fortunato, na Akaiko, waliokuwa wamesafiri kutoka Korintho hadi Efeso ambako Paulo alikuwa akikaa. Paulo pia alikuwa amepokea barua ya uchunguzi kutoka kutaniko la Kikristo la Korintho. Hata chanzo kiwe kilikuwa nini, mara hali ya mambo iliporipotiwa kwa Paulo na mashahidi wenye kutegemeka, ndipo alipokuwa na uwezo wa kutoa mwelekezo juu ya hilo jambo. “Ondoeni yule mtu mwovu miongoni mwenu wenyewe,” akaandika. Huyo mtu alifukuzwa katika kutaniko.—1 Wakorintho 5:13; 16:17, 18.
Je, maagizo ya Paulo yalileta matokeo mazuri? Kwa kweli yalileta! Kwa wazi, huyo mkosaji aling’amua ubaya wa matendo yake. Katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, Paulo alisihi sana kwamba kutaniko ‘limsamehe kwa fadhili na kumfariji’ huyo mtu mwenye toba. (2 Wakorintho 2:6-8) Hivyo kule kuripoti kosa kuliongoza kwenye tendo ambalo lilitokeza kutakaswa kwa kutaniko na kumrudisha kwenye upendeleo wa Mungu mtu aliyekuwa ameharibu uhusiano wake na Mungu.
Twapata kielelezo kingine katika barua ya kwanza ya Paulo kwa kutaniko la Kikristo la Korintho. Wakati huu mtume awataja mashahidi walioripoti hilo jambo. Aliandika hivi: “Kwa maana, ndugu zangu, wale wa nyumba ya Kloe walinifunulia juu yenu kwamba mitengano imo miongoni mwenu.” (1 Wakorintho 1:11) Paulo alijua kwamba mtengano huo, pamoja na kuwapa wanadamu heshima ambayo hawakustahili, kulikuwa kumetokeza mtazamo wa kifarakano uliotisha kuharibu muungano wa kutaniko. Kwa hiyo, kwa sababu ya kujali sana hali njema ya kiroho ya waamini wenzake huko, Paulo alitenda kwa haraka na kuliandikia hilo kutaniko shauri lenye kusahihisha.
Leo, ndugu na dada walio wengi katika makutaniko duniani pote hujitahidi kuhifadhi usafi wa kiroho wa kutaniko kwa mtu mmoja-mmoja kudumisha msimamo uliokubaliwa mbele ya Mungu. Ndugu fulani huteseka kwa kufanya hivyo; wengine hata wamekufa ili kutunza uaminifu-mshikaminifu. Hapana shaka kwamba kuruhusu au kufunika kosa kungeonyesha ukosefu wa uthamini kwa jitihada hizo.
Msaada kwa Wenye Kukosea
Kwa nini watu fulani ambao wametumbukia katika dhambi nzito husita kuwafikia wazee wa kutaniko? Mara nyingi ni kwa sababu hawajui faida za kuwaendea wazee. Wengine huamini kimakosa kwamba wakiungama, dhambi yao itafichuliwa kwa kutaniko zima. Wengine hujidanganya wenyewe kuhusu uzito wa mwendo wao. Na bado wengine hufikiri kwamba wanaweza kujirekebisha wenyewe upya bila msaada wa wazee.
Lakini wakosaji hao huhitaji msaada wenye upendo kutoka kwa wazee wa kutaniko. Yakobo aliandika hivi: “Je, kuna yeyote mgonjwa miongoni mwenu? Acheni awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, na acheni wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamfanya huyo asiyejisikia vizuri apone, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yakobo 5:14, 15.
Ni uandalizi wa ajabu kama nini wa kuwasaidia wenye kukosea kurudia hali yao ya kiroho! Kwa kutumia shauri lenye kutuliza kutoka Neno la Mungu na kwa kusali kwa niaba yao, wazee wanaweza kuwasaidia wenye kuugua kiroho wapate kupona njia zao zenye makosa. Hivyo, badala ya kuhisi kwamba wamehukumiwa, wenye toba mara nyingi hujihisi wameburudika na wametulia wakutanapo na wazee wenye upendo. Mwanamume mchanga kutoka Afrika Magharibi alikuwa amefanya uasherati na alikuwa amefunika dhambi yake kwa miezi kadhaa. Baada ya dhambi yake kudhihirika, aliwaambia wazee hivi: “Laiti mtu fulani angaliniuliza juu ya kuhusika kwangu na msichana huyo! Inatuliza sana kuungama dhambi yangu.”—Linganisha Zaburi 32:3-5.
Tendo la Upendo Wenye Kanuni
Watumishi wa Mungu waliobatizwa ‘wamevuka kutoka kifo hadi uhai.’ (1 Yohana 3:14) Lakini wakifanya dhambi nzito, wamegeukia tena njia ya kifo. Ikiwa hawatasaidiwa, huenda wakafanywa wagumu katika utendaji makosa, wakiwa hawataki kutubu na kuirudia ibada ya Mungu wa kweli.—Waebrania 10:26-29.
Kuripoti kosa ni tendo la kumhangaikia kihalisi mkosaji. Yakobo aliandika hivi: “Ndugu zangu, ikiwa yeyote miongoni mwenu aongozwa vibaya kutoka kwenye kweli na mwingine amrudisha, jueni kwamba yeye arudishaye mtenda-dhambi kutoka kwenye kosa la njia yake ataokoa nafsi yake kutoka kwenye kifo na atafunika wingi wa dhambi.”—Yakobo 5:19, 20.
Hivyo, basi, kwa nini lililo baya liripotiwe? Kwa sababu kufanya hivyo huleta matokeo mazuri. Kwa kweli, kuripoti kosa ni tendo la upendo wenye kanuni wa Kikristo kuelekea Mungu, kuelekea kutaniko, na kuelekea mkosaji. Kila mshiriki wa kutaniko ategemezapo viwango vya Mungu vyenye uadilifu kwa uaminifu-mshikaminifu, Yehova atalibariki sana kutaniko kwa ujumla. Mtume Paulo aliandika hivi: “Yeye [Yehova] atawafanya nyinyi imara hadi mwisho, ili msilaumike katika siku ya Bwana wetu Yesu Kristo.”—1 Wakorintho 1:8.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Ni jambo lionyeshalo upendo kumtia moyo Shahidi mwenye kukosea azungumze na wazee
[Picha katika ukurasa wa 28]
Wazee husaidia kuwarudisha wenye kukosea kwenye upendeleo wa Mungu
-
-
Maswali Kutoka kwa WasomajiMnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
-
-
Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je, Tetragramatoni (zile herufi nne za jina la Mungu kwa Kiebrania) ipatikanayo katika maandishi ya Kiebrania ya Mathayo ilinakiliwa na tabibu Myahudi Shem-Tob ben Isaac Ibn Shaprut wa karne ya 14?
La hasha. Hata hivyo, maandishi haya ya Mathayo hutumia hash·Shem’ (yakiwa yameandikwa kirefu au kifupi) mara 19, kama ilivyoonyeshwa katika ukurasa wa 13 wa Mnara wa Mlinzi wa Agosti 15, 1996.
Neno la Kiebrania hash·Shem’ humaanisha “lile Jina,” ambalo bila shaka hurejezea jina la Mungu. Mathalani, katika maandishi ya Shem-Tob, ufupizo wa hash·Shem’ waonekana katika Mathayo 3:3, kifungu ambacho katika hicho Mathayo alinukuu Isaya 40:3. Ni jambo la akili kukubali kwamba Mathayo aliponukuu mstari kutoka Maandiko ya Kiebrania ambamo Tetragramatoni ilipatikana, alitia ndani jina la Mungu katika Gospeli yake. Hivyo ingawa maandishi ya Kiebrania ambayo Shem-Tob alitumia hayatumii Tetragramatoni, matumizi yake ya “Lile Jina,” kama katika Mathayo 3:3, huunga mkono matumizi ya “Yehova” katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
Shem-Tob alinakili maandishi ya Kiebrania ya Mathayo katika kitabu chake chenye ubishi ʼEʹven boʹchan. Hata hivyo, chanzo cha maandishi yake ya Kiebrania kilikuwa nini? Profesa George Howard, ambaye amechunguza jambo hili sana, adokeza kwamba “maandishi ya Shem-Tob ya Mathayo katika Kiebrania yalikuwa ya wakati fulani kati ya karne nne za kwanza za kipindi cha Ukristo.”a Wengine waweza kukosa kukubaliana naye juu ya jambo hili.
Howard asema: “Mathayo katika Kiebrania iliyowekwa katika maandishi haya ya Shem-Tob yajulikana hasa kwa tofauti zake nyingi ilinganishwapo na maandiko yaliyokubaliwa rasmi ya Mathayo katika Kigiriki.” Mathalani, kulingana na maandishi ya Shem-Tob, Yesu alisema hivi kumhusu Yohana: “Kwa kweli, nawaambia, miongoni mwa wale waliozaliwa na wanawake hakujainuka mkubwa zaidi kuliko Yohana Mbatizaji.” Maandishi hayo huondoa maneno yafuatayo ya Yesu: “Lakini mtu ambaye ni mdogo zaidi katika ufalme wa mbingu ni mkubwa zaidi kuliko yeye.” (Mathayo 11:11) Katika njia zinazofanana na hiyo, kuna tofauti nyingi kati ya maandishi ya sasa ya Kiebrania ya Maandiko ya Kiebrania na maneno ya maandishi kama hayo ya fasiri ya Septuagint ya Kigiriki. Ingawa twatambua tofauti zake, maandishi kama haya ya kale bado yanafaa katika uchunguzi wa ulinganifu.
Kama ilivyotajwa, maandishi ya Shem-Tob ya Mathayo yatia ndani “lile Jina” ambapo kwa kweli kuna sababu nzuri kuamini kwamba Mathayo alitumia Tetragramatoni. Hivyo, tangu 1950, maandishi ya Shem-Tob yamekuwa yakitumiwa kuunga mkono kutumia jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na bado yanatajwa katika The New World Translation of the Holy Scriptures—With References.b
-