Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jina la Mungu na Watafsiri wa Biblia
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
    • Almeida, tafsiri ya awali (ya Kijeremani, iliyochapishwa mwaka wa 1871) iitwayo Elberfelder, na pia American Standard Version (ya Kiingereza, iliyochapishwa mwaka wa 1901). Tafsiri fulani, hasa inayojulikana sana kuwa The Jerusalem Bible, inatumia pia bila kigeugeu jina la Mungu lakini kwa maendelezo ya Yahweh.

      Sasa yasome maelezo ya watafsiri fulani waliolitia jina hilo katika tafsiri zao kisha ulinganishe sababu walizotoa na zile za wale walioacha kutumia jina hilo.

      Sababu Iliyofanya Wengine Walitie Jina Hilo Katika Tafsiri Zao

      Haya ndiyo maelezo ya watafsiri wa American Standard Version ya mwaka wa 1901: “[Watafsiri] walisadiki kwa umoja kwamba ushirikina wa Kiyahudi, ulioliona Jina la Kimungu kuwa takatifu mno lisiweze kutamkwa, haupasi tena utawale katika Kiingereza wala katika tafsiri nyingineyo ya Agano la Kale . . . Hilo Jina la Ukumbusho, linaloelezwa katika Kut. 3:14, 15, na kukaziwa kuwa hivyo mara nyingi katika maandishi ya awali ya Agano la Kale, linamtaja Mungu kuwa Mungu wa kibinafsi, kuwa Mungu wa agano, ndiye Mungu wa ufunuo, ndiye Mkombozi, aliye Rafiki ya watu wake . . . Jina hilo la kibinafsi, lenye mahusiano mengi matakatifu, sasa linarudishwa mahali linapopasa kuwa bila kupingwa katika maandishi matakatifu.”

      Hali moja na hiyo, katika dibaji ya tafsiri ya awali katika Kijeremani iitwayo Elberfelder Bibel tunasoma hivi: “Yehova. Sisi tumetunza jina hili la Mungu wa Agano wa Israeli kwa sababu msomaji amelizoea kwa miaka mingi.”

      Steven T. Byington, mtafsiri wa The Bible in Living English, anaeleza sababu gani yeye anatumia jina la Mungu: “Maendelezo na matamshi si ya maana sana. Kilicho cha maana sana ni kufanya iwe wazi kwamba hilo ni jina la kibinafsi. Kuna maandiko kadha ambayo hayawezi kufahamika vya kufaa ikiwa tunatafsiri jina hilo kwa kutumia neno la kutaja watu wengi kama ‘Bwana,’ au, lililo baya kuliko hilo, kwa kutumia neno la sifa [kwa mfano, Mwenyezi-Mungu] la namna ya mtajo.”

      Kisa cha tafsiri nyingine, ya J. B. Rotherham, ni chenye kupendeza. Yeye alitumia jina la Mungu katika tafsiri yake lakini akapendelea namna ya Yahweh. Ingawa hivyo, katika kitabu alichoandika baadaye, Studies in the Psalms, kikachapishwa mwaka wa 1911, alirudia matumizi ya namna ya Yehova. Kwa nini? Anaeleza hivi: “JEHOVAH.—Matumizi hayo ya namna ya Kiingereza ya jina la Ukumbusho (Kut. 3:18) katika tafsiri ya sasa ya Zaburi hayatokani na kuwa na shaka lo lote juu ya matamshi yaliyo sahihi zaidi, yakiwa Yahwéh; bali ni kutokana na ushahidi tu unaofaa uliochaguliwa kibinafsi kwa kutaka kuendeleza hali ya kupatana na jinsi watu wengi wanavyosikia na kuona kisa cha aina hii, ambacho katika hicho jambo kuu ni kutambuliwa vyepesi kulikokusudiwa kwa lile jina la Kimungu.”

      Katika Zaburi 34:3 waabudu wa Yehova wanatiwa moyo hivi: “Tumkuzeni Jehova, nyinywi na mimi, naswi tutukuze jina lakwe pamoja.” (OTSWMSA) Wasomaji wa tafsiri za Biblia zinazoacha kutumia jina la Mungu wanaweza kuitikiaje kikamili kitia-moyo hicho? Wakristo wanafurahi kwa vile angalau watafsiri fulani wamejipa moyo kiasi cha kulitia jina la Mungu katika tafsiri zao za Maandiko ya Kiebrania, na kwa njia hiyo wanahifadhi ambayo Smith na Goodspeed wanaiita “ladha ya maandishi ya awali.”

      Ingawa hivyo, tafsiri nyingi, hata zinapotia jina la Mungu katika Maandiko ya Kiebrania, zinaacha kulitumia katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, lile “Agano Jipya.” Sababu ya kufanya hivyo ni nini? Je! kuna sababu yo yote inayofanya jina la Mungu listahili kutiwa katika sehemu hiyo ya mwisho ya Biblia?

  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
    • Jina la Mungu na “Agano Jipya”

      CHEO cha jina la Mungu katika Maandiko ya Kiebrania, “Agano la Kale,” ni kile kisichotikisika. Ijapokuwa hatimaye Wayahudi waliacha kulitamka, imani zao za kidini ziliwazuia wasiliondoe jina hilo walipokuwa wakiandika nakala za hati za kale za Biblia. Kwa sababu hiyo, Maandiko ya Kiebrania yana jina la Mungu mara nyingi zaidi ya jina jinginelo lote.

      Hali hiyo ni tofauti kwa habari ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, “Agano Jipya.” Hati za kitabu cha Ufunuo (kile kitabu cha mwisho cha Biblia) zina jina la Mungu kwa namna ya kifupi hiki, “Yah,” (katika neno hili “Haleluya”). Lakini zaidi ya hiyo, hakuna hati ya Kigiriki ya kale-kale tuliyo nayo leo tangu Mathayo mpaka Ufunuo iliyo na jina la Mungu kwa ukamili. Je! maana yake ni kwamba jina hilo halipasi kuwa humo? Hilo lingekuwa jambo la kustaajabisha kwa sababu wafuasi wa Yesu waliukubali umaana wa jina la Mungu, na Yesu alitufundisha tusali jina la Mungu litakaswe. Basi ilikuwaje?

      Ili ufahamu hilo, kumbuka kwamba zile hati za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tulizo nazo leo si nakala zenyewe zile za awali. Vitabu vyenyewe vilivyoandikwa na Mathayo, Luka na waandikaji wengine wa Biblia vilitumiwa sana navyo vilichakaa upesi. Kwa sababu hiyo, nakala nyingine ziliandikwa, nazo zilipochakaa, nakala zaidi zikaandikwa kutokana na nakala hizo. Hivyo ndivyo tungetazamia, kwani kwa kawaida nakala hizo ziliandikwa zitumiwe, si zitunzwe.

      Kuna maelfu ya nakala za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zinazopatikana leo, lakini nyingi zazo ziliandikwa wakati wa karne ya nne ya Wakati wa Kawaida wetu au baada ya hapo. Hiyo inaonyesha kwamba yawezekana kuwe kulitokea jambo hili: Je! kuna kitu kilichoyapata maandishi ya awali ya Maandiko ya Kigiriki kabla ya karne ya nne kilichofanya jina la Mungu liachwe kutumiwa? Mambo ya hakika yanathibitisha kwamba kitu fulani kilifanya hivyo.

      Jina Hilo Lilikuwa Humo

      Tunaweza kuwa na hakika kwamba mtume Mathayo alitia jina la Mungu katika Injili yake. Kwa nini? Kwa sababu hapo awali aliandika katika Kiebrania. Katika karne ya nne, Jerome, aliyetafsiri Biblia ya Kilatini iitwayo Vulgate, alitoa ripoti hivi: “Mathayo, aliye pia Lawi, na ambaye kwenye kazi ya kutoza kodi akawa mtume, alitunga kwanza Injili ya Kristo katika Yudea katika lugha ya Kiebrania . . . Hakuna uhakika wa kutosha juu ya aliyeitafsiri katika Kigiriki baada ya hapo. Isitoshe, Kiebrania chenyewe hicho kimetunzwa mpaka leo hii katika maktaba katika Kaisaria.”

      Kwa kuwa Mathayo aliandika katika Kiebrania, haiwaziki kwamba yeye hakulitumia jina la Mungu, hasa alipokuwa akinakili maneno kutoka sehemu za “Agano la Kale” zilizokuwa na jina hilo. Ingawa hivyo, waandikaji wengine wa sehemu ya pili ya Biblia waliandikia wasikilizaji ulimwenguni pote katika lugha ya mataifa yote iliyokuwa ya wakati huo, yaani, Kigiriki. Kwa sababu hiyo, hawakunakili maneno kutoka maandishi ya awali ya Kiebrania bali kutoka tafsiri ya Kigiriki iitwayo Septuagint. Na hata Injili ya Mathayo ilitafsiriwa hatimaye katika Kigiriki. Je! jina la Mungu lingalionekana katika maandishi hayo ya Kigiriki?

      Visehemu fulani vya kale sana vya Septuagint Version vilivyokuwako hasa katika siku za Yesu vimesalimika mpaka wakati wetu, na ni jambo linalofaa kuangaliwa kwamba jina la kibinafsi la Mungu lilionekana humo. The New International Dictionary of New Testament Theology (Buku la 2, ukurasa wa 512) inasema hivi: “Mavumbuzi ya maandishi ya awali ya hivi majuzi yanatilia shaka wazo la kwamba watungaji wa LXX [Septuagint] waliitafsiri tetragramatoni YHWH kwa kutumia kyrios. [Hati] LXX MSS (visehemu) zilizo za kale sana zinazopatikana kwetu sasa zina tetragramatoni ikiwa imeandikwa kwa herufi za Kiebrania na kwa maandishi ya Kigiriki. Desturi hiyo ilitunzwa na watafsiri wa Kiyahudi waliokuja baadaye wa Agano la Kale katika karne zile za kwanza A.D.” Kwa hiyo, kwamba Yesu na wanafunzi wake waliyasoma Maandiko hayo katika Kiebrania ama katika Kigiriki, wangeliona jina la Mungu.

      Hivyo, Profesa George Howard, wa Chuo Kikuu cha Georgia, U.S.A., alieleza hivi: “Wakati Septuagint ambayo kanisa la Agano Jipya lilitumia na kunakili maneno yake ilipokuwa na namna ya Kiebrania ya jina la kimungu, bila shaka waandikaji wa Agano Jipya waliitia Tetragramatoni katika maneno yao waliyonakili.” (Biblical Archaeology Review, Machi 1978, ukurasa wa 14) Ni mamlaka gani ambayo wangalikuwa nayo wafanye tofauti na hivyo?

      Jina la Mungu liliendelea kuwa katika tafsiri ya Kigiriki ya “Agano la Kale” kwa muda zaidi kidogo. Katika sehemu ya kwanza ya karne ya pili W.K., Akila, mwongofu wa Kiyahudi alifanya tafsiri mpya ya Maandiko ya Kiebrania akiyaleta katika Kigiriki, na humo aliwakilisha jina la Mungu kwa Tetragramatoni katika herufi za kale za Kiebrania. Katika karne ya tatu, Origeni aliandika hivi: “Na katika hati zilizo sahihi zaidi sana LILE JINA linaonekana kwa herufi za Kiebrania, lakini si kwa [herufi za] Kiebrania cha leo, bali kwa zile zilizo za kale zaidi sana.”

      Hata katika karne ya nne, Jerome anaandika hivi katika utangulizi wa vitabu vya Samweli na Wafalme: “Na tunaliona jina la Mungu, ile Tetragramatoni [יהוה] katika mabuku fulani ya Kigiriki likionyeshwa hata leo hii katika herufi za kale.”

      Kuondolewa kwa Jina Hilo

      Ingawa hivyo, kufikia wakati huo uasi-imani uliotabiriwa na Yesu ulikuwa umetokea, na jina hilo, lijapoonekana katika hati, liliendelea kutumiwa mara chache sana. (Mathayo 13:24-30; Matendo 20:29, 30) Mwishowe, wasomaji wengi hata hawakulitambua na Jerome anaripoti kwamba katika wakati wake “kwa sababu ya kufanana kwa herufi, watu fulani wasiojua kitu walipokuta [ile Tetragramatoni] katika vitabu vya Kigiriki, walizoea kusoma ΠΙΠΙ.”

      Katika nakala zilizofuata za Septuagint, jina la Mungu liliondolewa na maneno kama “Mungu” (The·osʹ) na “Bwana” (Kyʹri·os) yakatumiwa badala yalo. Tunajua kwamba jambo hilo lilitukia kwa sababu tuna visehemu vya mapema vya Septuagint ambamo jina la Mungu lilitiwa ndani na nakala zilizofuata za sehemu izo hizo za Septuagint ambamo jina la Mungu limeondolewa.

      Jambo lile lile lilitukia katika “Agano Jipya,” au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Profesa George Howard anaendelea kusema: “Wakati namna ya Kiebrania ya jina la kimungu ilipoondolewa na maneno ya Kigiriki yakatumiwa badala yalo katika Septuagint, liliondolewa pia katika maneno yaliyonakiliwa ya Septuagint yakatiwa katika Agano Jipya. . . . Muda si muda lile jina la kimungu likapotea lisionekane kwa kanisa la Mataifa isipokuwa kama vile kufikia hapa lilivyoonyeshwa kwa vifupi vilivyotumiwa badala yalo au lilivyokumbukwa na wasomi.”

      Kwa sababu hiyo, ijapokuwa Wayahudi walikataa kutamka jina la Mungu, kanisa la Kikristo lenye kuasi imani lilifaulu kuliondoa kabisa katika hati za lugha ya Kigiriki za sehemu za Biblia, na pia katika tafsiri za lugha nyingine.

      Kuhitajiwa kwa Jina Hilo

      Mwishowe, kama tulivyotangulia kuona, lile jina lilirudishwa kwenye tafsiri

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki