Saburi—Kwa Nini Ni Nadra Sana?
EMILIO alikuwa katika umri wake wa miaka 60.a Alikuwa amekuja Oahu kwa shughuli ya kusikitisha—kumzika mwanaye aliyekuwa mtu mzima. Alipokuwa akitembea kando ya barabara tulivu vilimani huku akizungumza na marafiki fulani, Emilio alishtuliwa na gari lililokuwa likiendeshwa kasi kinyume-nyume kuelekea barabarani. Gari hilo karibu limgonge, na kwa hasira bila subira, Emilio akampazia sauti dereva na kuligonga gari hilo kwa mkono. Mabishano yakafuata. Inaonekana kwamba dereva huyo alimsukuma Emilio, aliyeanguka na kugonga kichwa chake pembeni mwa barabara palipokuwa pagumu. Baada ya siku chache, Emilio alikuwa amekufa kwa sababu ya jeraha la kichwa chake. Tokeo lenye huzuni kama nini!
Tunaishi katika ulimwengu ambao saburi ni sifa nadra. Madereva wengi zaidi na zaidi huendesha kwa kasi sana. Wengine hufuata kwa ukaribu sana magari yaendeshwayo kwa kasi. Na wengine hutangatanga kutoka sehemu moja ya barabara kwenda nyingine kwa sababu hawawezi kungoja wakiwa nyuma ya gari jingine. Nyumbani, washiriki wa familia huenda wakawa na hasira kali na kuwa wenye jeuri. Hata Wakristo fulani huenda wakawa na hasira kupita kiasi kwa sababu ya mapungukio au makosa ya ndugu zao wa kiroho.
Kwa nini saburi ni nadra sana? Je, imekuwa hivyo sikuzote? Kwa nini ni vigumu sana kuwa na saburi katika nyakati zetu?
Vielelezo vya Ukosefu wa Saburi
Biblia hueleza juu ya mwanamke mmoja ambaye hakusubiri aulize mumeye kabla ya kufanya uamuzi mzito. Jina lake lilikuwa Hawa. Bila kumsubiri, Adamu, labda kwa sababu ya kukosa saburi, yeye alikula tunda lililokatazwa. (Mwanzo 3:1-6) Vipi mumeye? Yeye pia huenda alionyesha ukosefu wa saburi kwa kumfuata Hawa katika dhambi bila kwanza kumwendea Baba yake wa kimbingu, Yehova, kwa msaada au mwelekezo. Pupa yao, yawezekana ikitia ndani ukosefu wa saburi uliotokeza dhambi, ilikuwa na matokeo mabaya sana kwetu sote. Kutoka kwao tumerithi mwelekeo wa kufanya dhambi, kutia ndani zile za kiburi na ukosefu wa saburi.—Warumi 5:12.
Karibu miaka 2,500 baada ya dhambi ya wazazi wetu wa kwanza, watu waliochaguliwa na Mungu, Waisraeli, walionyesha ukosefu mkubwa, wenye kuendelea wa imani, na vilevile ukosefu wa saburi. Ingawa Yehova alikuwa ametoka tu kuwaokoa kimuujiza kutoka utumwani Misri, kwa haraka “wakayasahau matendo yake” na “hawakulingojea shauri lake.” (Zaburi 106:7-14) Kwa kurudiarudia walifanya makosa mazito kwa sababu ya kukosa saburi. Walitengeneza ndama wa dhahabu na kumwabudu; waliteta juu ya uandalizi wa Yehova wa mana kwao; na wengi wao hata waliasi dhidi ya Musa, mwakilishi wa Yehova aliyewekwa kimungu. Kwa kweli, ukosefu wao wa saburi ulitokeza kwenye huzuni na uangamivu.
Sauli, mfalme wa kwanza wa kibinadamu wa Israeli, alipotezea wanawe fursa ya kumiliki ufalme baada yake. Kwa nini? Kwa sababu alikosa kungoja nabii Samweli, aliyepaswa kutoa dhabihu kwa Yehova. Woga wa mwanadamu ulimfanya Sauli kumtangulia Samweli kutoa dhabihu. Ebu wazia jinsi alivyohisi Samweli alipotokea mara tu baada ya Sauli kumaliza sherehe hiyo! Ikiwa tu angalisubiri dakika chache tu zaidi!—1 Samweli 13:6-14.
Ikiwa tu Hawa angelimsubiri Adamu badala ya kuchukua haraka tunda hilo! Ikiwa tu Waisraeli wangalikumbuka kusubiri shauri la Yehova! Ndiyo, huenda saburi ingaliwasaidia na kutusaidia sisi kutopatwa na huzuni na uchungu.
Visababishi vya Ukosefu wa Saburi
Biblia hutusaidia kuelewa kisababishi hasa cha ukosefu wa saburi leo. Andiko la Timotheo wa pili sura ya 3, (NW) hueleza kuwa kizazi chetu kinaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Linaeleza kwamba watu “watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema.” (Mistari 2, 3) Mtazamo kama huo wa pupa na kujipenda umo mioyoni na akilini mwa watu wengi, ikifanya iwe vigumu kwa wote, hata Wakristo wa kweli, kuonyesha saburi. Tunapoona watu wa ulimwengu wakiendesha magari kwa kasi sana au wakikatisha magari mengine au wakitutukana, saburi yetu yaweza kujaribiwa sana. Huenda tukashawishwa kuwaiga au kujilipizia kisasi dhidi yao, na hivyo kuonyesha kiburi kama chao.
Wakati mwingine ni maoni yetu yenye makosa ambayo hutufanya kukosa saburi. Ona jinsi Mfalme Sulemani mwenye hekima alivyoonyesha upatano kati ya uharaka, kusababu kwenye makosa na tabia isiyopendeza, yenye ukosefu wa saburi: “Heri . . . mvumilivu [“mwenye saburi,” NW] rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi. Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.” (Mhubiri 7:8, 9) Tukichukua wakati kupata picha kamili ya hali kabla ya kuchukua hatua yoyote, huenda tutakuwa wenye ufahamu zaidi, wenye huruma zaidi, wenye saburi zaidi kuelekea wengine. Kwa upande mwingine, roho yenye kiburi, yenye kujifikiria tu huenda ikatufanya kuwa na akili ndogo, kukosa saburi, na kuwa wenye uchungu, kama vile Waisraeli wanung’unikaji, wenye shingo ngumu waliomtesa Musa.—Hesabu 20:2-5, 10.
Sababu nyingine ya kuongezeka kwa ukosefu wa saburi wa ulimwengu huu ni hali yao ya kukosa tumaini, inayoletwa na tokeo la kutengwa na Yehova. Daudi alieleza hivi uhitaji wa mwanadamu wa kutumaini katika Yehova: “Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya, tumaini langu hutoka kwake.” (Zaburi 62:5) Watu wengi wasiomjua Yehova wana mtazamo mfupi usio na tumaini, hivyo wanajaribu kunyakua kila aina ya anasa na faida wanayoweza kupata kabla ya kufa. Kama vile baba yao wa kiroho, Shetani Ibilisi, mara nyingi hawajali jinsi matendo yao yaweza kuumiza wengine.—Yohana 8:44; 1 Yohana 5:19.
Hivyo haishangazi kwamba saburi ni nadra sana leo. Mfumo huu mwovu wenye ubinafsi, mungu wao Shetani, na mwelekeo wa mwili wetu wenye dhambi hufanya iwe vigumu kwa kila mmoja, hata wenye mioyo minyoofu, kuwa wenye saburi. Lakini, Biblia hutusihi ‘tutumie saburi,’ hasa kuhusu kutimizwa kwa makusudi ya Mungu. (Yakobo 5:8, NW) Kwa nini saburi ni ya maana sana? Inaweza kutuletea thawabu zipi?
Saburi—Kwa Nini Ni ya Maana Sana
“Hata wale hungoja kwa saburi hupata fursa za kutumika.” Maneno hayo yalisemwa na John Milton mwanashairi Mwingereza zaidi ya miaka mia tatu iliyopita katika shairi lake “Juu ya Upofu Wake.” Katika sehemu ya kwanza ya shairi hilo, alieleza kutojua la kufanya na masumbufu yake kuhusu hisia yake ya kutoweza kumtumikia Mungu kwa ukamili kwa sababu alikuwa amekuwa kipofu katika umri wake wa miaka 40. Lakini kama ionyeshwavyo na mstari wa mwisho wa shairi hilo lililonukuliwa hapo juu, alikuja kutambua kwamba mtu anaweza kumwabudu Mungu kwa kuvumilia dhiki kwa saburi na kwa utulivu kutafuta fursa za kutumika. Milton aliona ubora wa kutegemea Mungu kwa saburi.
Wengi wetu huenda tukawa na macho mazuri, lakini sisi sote tuna mapungukio yawezayo kutufanya kuwa na hasira au masumbufu. Tunawezaje kupata na kudhihirisha saburi?
Vielelezo Vyenye Kutia Moyo
Biblia hutuandalia vielelezo kadhaa vizuri vya saburi. Saburi ya Yehova hufanya uhai wa milele uwezekane kwa mamilioni mengi ya binadamu. (2 Petro 3:9, 15) Katika ukaribishaji wake wenye fadhili kwamba tuchukue nira yake na ‘kupata raha nafsini [mwetu],’ Yesu huonyesha kikamilifu saburi ya ajabu ya baba yake. (Mathayo 11:28-30) Kutafakari juu ya vielelezo vya Yehova na Yesu kunaweza kutusaidia kuwa wenye saburi zaidi.
Mtu mmoja aliyeonekana kuwa na sababu ya kutosha kuwa na hasira, uchungu, au kujilipizia kisasi alikuwa mwana wa Yakobo, Yusufu. Ndugu zake walikuwa wamemtenda kwa ukosefu wa haki kabisa, kwa kupanga kumuua na mwishowe kumuuza utumwani. Katika Misri, ujapokuwa utumishi wake wa ushikamanifu kwa Potifa, Yusufu aliwekelewa shtaka bandia na kufungwa gerezani. Kwa saburi alivumilia dhiki zake zote, labda akifahamu kwamba mitihani kama hiyo yaweza kutimiza makusudi ya Yehova. (Mwanzo 45:5) Kwa sababu alisitawisha imani na tumaini katika Yehova pamoja na unyenyekevu na utambuzi, Yusufu angeweza kudhihirisha saburi hata chini ya hali zenye majaribu mengi sana.
Msaada mwingine wa maana ni roho takatifu ya Yehova. Kwa kielelezo, ikiwa tunakasirika haraka na kuwa wenye maneno ya kuchoma, tunaweza kuomba msaada wa roho takatifu ili kwamba tuweze kusitawisha tunda layo. Kutafakari juu ya kila moja la matunda haya, kama vile uvumilivu na kiasi, kutatusaidia kuona jinsi yanavyopatana sana na saburi.—Wagalatia 5:22, 23.
Thawabu za Saburi
Kuwa wenye saburi kunaweza kutuletea faida nyingi. Hutia nguvu utu wetu na hutuzuia kufanya matendo ya haraka, ya upumbavu. Nani kati yetu hajawahi kufanya makosa yenye kuumiza kwa sababu ya kuwa kwetu wenye haraka mno kutenda dhidi ya tatizo au hali zenye mkazo? Huenda tulisema neno lisilo la fadhili au kujiendesha kwa njia ya kiburi. Huenda tuliruhusu tukio fulani dogo kuwa ugomvi mkubwa na mpendwa wetu. Baada ya hasira nyingi, kutojua la kufanya, na uchungu wa moyo, huenda kwa kusikitika tulifikiri hivi, ‘Kama tu ningalisubiri kidogo tu.’ Kudhihirisha saburi kunaweza kutulinda kutokana na huzuni ya aina zote. Uhakika huo pekee hupa maisha zetu amani, uthabiti, na uradhi mwingi hata zaidi.—Wafilipi 4:5-7.
Kuwa na saburi pia kunaweza kutusaidia kuwa na moyo mtulivu, wenye kutumainika. Hili laweza kutufanya tufurahie afya bora zaidi ya kimwili, kihisia-moyo, na kiroho. (Mithali 14:30) Isipozuiliwa, hasira kali yaweza kuleta ugonjwa mbaya wa kihisia-moyo na kimwili na kifo. Kwa upande mwingine, kwa kuwa wenye saburi tunaweza kuwa na mwelekeo chanya zaidi kuelekea wengine, hasa ndugu zetu wa kiroho na washiriki wa familia yetu. Kisha tutakuwa na mwelekeo zaidi wa kuwa wenye ufikirio na wenye kusaidia badala ya kuwa wenye kuudhika upesi na wachambuzi. Kisha, wengine wataona ikiwa rahisi na kupendeza kushirikiana na sisi.
Hasa wazee katika kutaniko la Kikristo wanahitaji kudhihirisha saburi. Mara nyingine, Wakristo wenzao huwaendea na matatizo mazito. Hawa wenye mioyo minyoofu huenda wamevurugika akili, wakakasirika, au kushuka moyo, wakati uleule wazee huenda wakawa wamechoka na kukengeushwa na matatizo yao wenyewe au ya familia. Lakini, ni jambo la maana jinsi gani wazee wadhihirishe saburi katika hali kama hizi zenye kujaribu! Kwa njia hii wanaweza kuwaagiza kwa ‘uanana’ na ‘kulihurumia kundi.’ (2 Timotheo 2:24, 25; Matendo 20:28, 29) Maisha zenye thamani zimo hatarini. Wazee wenye fadhili, upendo, na saburi ni baraka iliyoje kwa kutaniko!
Vichwa vya familia wanapaswa kutendea watu wa familia yao kwa saburi, uelewevu, na fadhili. Ni lazima pia watazamie na kutia moyo washiriki wote wa familia kudhihirisha sifa hizihizi. (Mathayo 7:12) Hili litachangia sana upendo na amani nyumbani.
Kudhihirisha saburi tunaposhiriki katika huduma ya shambani kutasaidia wahudumu Wakristo kufurahia huduma hii kwa ukamili zaidi. Wataweza hata zaidi kuvumilia ubaridi na upinzani wanaokabili. Badala ya kubishana na wenye nyumba wenye hasira, wahudumu wenye saburi wataweza kutoa jibu la upole au kwa utulivu waondoke, hivyo wakidumisha amani na furaha. (Mathayo 10:12, 13) Zaidi ya hayo, Wakristo watendeapo kila mmoja kwa saburi na fadhili, wenye mfano wa kondoo watavutwa na ujumbe wa Ufalme. Yehova amebariki jitihada zenye saburi ulimwenguni pote, huku mamia ya maelfu ya watafutaji kweli wanyenyekevu wamiminikiapo kutaniko la Yehova lenye upendo kila mwaka.
Kwa kweli, kudhihirisha saburi kutatuletea thawabu bora. Tutaepuka aksidenti nyingi na matatizo yanayofanyizwa na matendo ya haraka-haraka au kuwa wenye uharaka mno kwa ulimi wetu. Tutakuwa wenye furaha zaidi, wenye utulivu zaidi, na huenda hata wenye afya bora. Tutahisi shangwe na amani nyingi zaidi katika huduma yetu, kutanikoni, na nyumbani. Lakini la maana zaidi, tutafurahia uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Mungu. Hivyo mngojee Yehova. Dhihirisha saburi!
[Maelezo ya chinis]
a Jina limebadilishwa.
[Picha katika ukurasa w10]
Wewe ni mwenye saburi kadiri gani katika maisha ya kila siku?