Jinsi ya Kupata Shangwe Katika Kufanya Wanafunzi
MOJAWAPO shangwe kuu ambazo mtu aweza kupata ni ile ya kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu. Leo, kazi ya Mungu yatia ndani kuwakusanya watu wenye mwelekeo wa uadilifu katika kutaniko la Kikristo na kuwazoeza katika maisha wakiwa Wakristo sasa na vilevile kuokolewa katika ulimwengu mpya.—Mika 4:1-4; Mathayo 28:19, 20; 2 Petro 3:13.
Imekuwa chanzo cha shangwe kuu kwa Mashahidi wa Yehova katika Amerika ya Latini kuona watu milioni moja wakija kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo tangu 1980. Katika shamba hili lenye matokeo, ambamo wengi hustahi na kuamini Biblia, wahudumu wengine wa wakati wote wameweza kusaidia watu wengi kuweka maisha zao wakfu kwa Yehova. Wakiwa na uzoefu mwingi, labda wao waweza kutueleza jambo fulani kuhusu shangwe ya kufanya wanafunzi. Baadhi ya madokezo yao yaweza kukusaidia kupata shangwe katika kufanya wanafunzi unakoishi.
Kutambua Wale Waelekeao Kuwa “Kondoo”
“Na mji wo wote au kijiji cho chote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo aliye mtu mwaminifu [“anayestahili,” NW],” Yesu alisema hayo alipowatuma mitume wake kwenda kuhubiri. (Mathayo 10:11) Unapozuru watu, unaweza kutambuaje wale wanaoweza kusaidiwa kiroho? Edward, mhudumu wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 50, asema: “Wao huonyesha ishara kwa kuuliza maswali ya unyoofu na kuridhika wajibiwapo kutoka kwa Maandiko.” Carol aongezea: “Mtu akiniambia kisiri tatizo au hangaiko la kibinafsi, hilo hasa ni kilio cha kutaka msaada. Mimi hujaribu kupata habari yenye kusaidia katika vichapo vya Watch Tower Society. Upendezi huo kwa mtu mara nyingi huongoza kwenye funzo la Biblia.” Na bado si rahisi sikuzote kutambua wanyoofu. Luis aelezea: “Wengine walioonekana kuwa wenye kupendezwa sana kumbe hawakupendezwa kamwe, lakini wengine ambao mwanzoni walionekana kuwa wapinzani walibadilika waliposikia yale ambayo kwa kweli Biblia husema.” Kwa kuwa watu wengi wa Amerika ya Latini hustahi Biblia, yeye aongezea, “Mimi hutambua wale wawezao kusaidiwa kiroho wakubalipo mara moja yale Biblia hufundisha baada ya kuwaonyesha fundisho hilo.” Kusaidia hawa ‘wanaostahili’ kufanya maendeleo ya kiroho huleta shangwe ya kweli na uradhi. Unaweza kuwasaidiaje?
Kuanzisha Mafunzo ya Biblia
Kutumia visaidizi vya kujifunza Biblia vinavyotolewa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” mara nyingi ndiyo njia bora zaidi ya kusaidia watu kuelewa kweli ya Biblia. (Mathayo 24:45) Unaweza kujengaje uthamini kwa thamani ya visaidizi hivyo vya kujifunza Biblia? Edward asema: “Kwa kuwa hali, utu, na maoni ya watu hutofautiana sana, mimi hujaribu kubadilikana katika kuanzisha mafunzo.” Huwezi kutumia njia ileile kwa kila mtu.
Kwa wengine, mazungumzo kadhaa yasiyo rasmi juu ya Maandiko huenda yakahitajiwa kabla ya kutoa kitabu chenye mafundisho ya Biblia. Hata hivyo, wenzi fulani wa ndoa wamishonari waripoti hivi: “Sisi hutoa funzo katika ziara ya kwanza.” Vivyo hivyo, Shahidi ambaye amesaidia watu 55 kufikia hatua ya kujiweka wakfu asema hivi: “Njia yangu kuu ya kuanzisha mafunzo ya Biblia imekuwa ni kuingia moja kwa moja katika kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.” Ingawa wengine hawapendi wazo la kujifunza kitu chochote, wengine wanatamani kujifunza chochote wafikiricho kitawasaidia maishani. Toleo la mafunzo ya Biblia nyumbani bila malipo hupendeza sana watu kama hawa. Wamishonari fulani hueleza toleo hili kisha wao husema: “Ningependa kukuonyesha jinsi tunavyofanya. Ukipendezwa nayo, unaweza kuendelea. Usipopenda, chaguo ni lako.” Funzo likitolewa kwa njia hiyo, watu hawaogopi kukubali.
Shahidi mwingine, ambaye amesaidia wengi wasio na mali na elimu, asema hivi: “Nimepata kwamba trakti hasa zafaa sana katika kuanzisha mafunzo ya Biblia.” Hata watumie kichapo kipi, walimu wa wakati wote hujaribu kusisitiza Biblia. Carola asema: “Kwenye funzo la kwanza, mimi hutumia picha tu na karibu maandiko matano, ili mambo makuu yatokeze wazi na Biblia isionekane kuwa ngumu.”
Kudumisha Upendezi
Watu hufurahia kuwa na hisia za kufanya maendeleo, kwa hiyo Jennifer apendekeza hivi: “Fanya funzo liwe changamfu. Fanya funzo liwe lenye maendeleo.” Kuongoza funzo kwa ukawaida bila kukosa kwa majuma pia husaidia mafunzo kuhisi kwamba wanafanya maendeleo. Watu wengine wenye kupendezwa wapya huwa na maswali mengi sana hivi kwamba ni vigumu kwao kujenga ujuzi wao kwa njia yenye kuendelea kwa kukazia akili habari moja kwa wakati mmoja. Mishonari mmoja asema hivi: “Wewe hula milo mitatu kwa siku—kiamsha kinywa, chakula cha mchana na chakula cha jioni, lakini ukijaribu kula kiasi hicho cha chakula mara moja, utafura tumbo. Ukijaribu kuelewa mambo mengi sana ya Kimaandiko kwa wakati mmoja utafura tumbo kiroho, kwa hiyo fikiria mambo machache ambayo tumesema leo halafu juma lijalo tutaongezea mengine.” Hata watu wenye akili za kudadisi-dadisi ni lazima wajifunze kukazia akili jambo moja kwa wakati mmoja ikiwa watafanya maendeleo katika uelewevu. Yesu aliwaambia mitume wake: “Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa.”—Yohana 16:12.
Njia nyingine ya kudumisha upendezi ni kuwatia moyo wale unaowazuru kuendelea kufikiria juu ya Neno la Mungu baada ya wewe kwenda. Yolanda apendekeza: “Acha swali ambalo halijajibiwa bado. Uwape kazi fulani wafanye, kama vile kusoma sehemu ya Biblia au kuchunguza habari fulani inayowahusu.”
Kukuza Upendo kwa Yehova
Shangwe yako itaongezeka uwasaidiapo wanafunzi wako kuwa “watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu.” (Yakobo 1:22) Unaweza kufanyaje hivyo? Wakristo wa kweli huchochewa na upendo kwa Yehova. Pedro, anayetoka Mexico, aeleza: “Watu hawawezi kumpenda mtu wasiyemjua, hivyo tangu mwanzoni mwa funzo, mimi huwafundisha jina la Mungu kutoka kwa Biblia, nami hutafuta fursa za kukazia sifa za Yehova.” Katika mazungumzo, unaweza kujenga uthamini kwa Yehova kwa kuonyesha hisia zako kwake. Elizabeth asema: “Sikuzote mimi hujaribu kutaja wema wa Yehova. Wakati wa mafunzo yangu, nikiona maua maridadi, ndege mwenye kuvutia, au mtoto wa paka mwenye kupenda michezo, sikuzote mimi hutaja kwamba hiyo ni kazi ya Yehova.” “Sema juu ya ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa kama uujuavyo kuwa halisi,” adokeza Jennifer. “Waulize wangependa kufanya nini katika ulimwengu mpya.”
Mtu atafakaripo kwa uthamini juu ya yale anayojifunza kumhusu Yehova, hayo huingia moyoni mwake na kumchochea atende. Lakini yeye hawezi kutafakari mpaka awe anakumbuka. Pitio fupi la mambo makuu matatu au manne baada ya kila funzo ni msaada katika kukumbuka. Walimu wengi wa Biblia huwafanya wapya waandike maandiko makuu pamoja na habari fupi katika sehemu ya nyuma ya Biblia. Mishonari mmoja kutoka Uingereza aeleza faida nyingine ya mapitio: “Mimi huuliza jinsi habari hiyo imewafaidi. Jambo hilo huwafanya watafakari kwa uthamini juu ya njia na sheria za Yehova.”
Shahidi mmoja mwaminifu aliyehitimu kutoka darasa la tatu la Gileadi asema: “Ni lazima tuwe wenye shauku. Ni lazima wanafunzi wetu watambue kwamba twaamini yale tufundishayo.” Ile imani ambayo imekufanya uwe “mtendaji wa kazi” mwenye furaha ni yenye kuambukiza ukiionyesha.—Yakobo 1:25.
“Mimi hupata kwamba watu huhisi wakiwa karibu na Mungu nikiwasaidia kutambua majibu ya sala zao,” asema Shahidi mmoja ambaye amesaidia wengi wamwabudu Yehova. “Mimi huwatolea vielelezo kutoka kwa maisha yangu mwenyewe, kama hiki: Tulipofika kwenye mgawo wetu mpya na mwenzangu tukiwa mapainia, tulikuwa na mboga kidogo tu, pakiti ya siagi, bila pesa. Tulimaliza chakula cha jioni na kusema, ‘Sasa hatuna chochote kwa ajili ya kesho.’ Tulisali kuhusu jambo hilo, tukalala. Mapema asubuhi iliyofuata Shahidi mmoja wa huko alikuja na kujitambulisha, akisema, ‘Nilisali kwamba Yehova alete mapainia. Sasa naweza kuandamana nanyi kwa sehemu kubwa ya siku, lakini kwa kuwa naishi mbali mashambani, itanibidi nile chakula cha mchana pamoja nanyi, kwa hiyo nimeleta chakula hiki tule sisi sote.’ Chakula hicho kilikuwa nyama nyingi na mboga nyingi. Sikuzote mimi huwaambia wanafunzi wangu kwamba Yehova hatuachi kamwe tukitafuta kwanza Ufalme wake.”—Mathayo 6:33.
Toa Msaada Wenye Kutumika
Kuna mengi zaidi yanayohusika katika kufanya wanafunzi wa Kristo kuliko kuongoza tu funzo la Biblia. Mishonari mmoja aliyetumikia kwa miaka mingi akiwa mwangalizi asafiriye asema: “Wape wakati. Usiende mbio baada ya kumaliza funzo. Ikiwezekana, kaa mzungumze kidogo.” Elizabeth asema: “Mimi hupendezwa sana nao kwa sababu uhai wahusika. Mara nyingi mimi huwahangaikia kana kwamba wao ni watoto wangu.” Mashahidi wengine walitoa madokezo haya: “Wazuru wakiwa wagonjwa.” “Unapokuwa karibu na nyumbani kwao, kwa mfano katika huduma ya shambani, watembelee kifupi kuwajulisha Mashahidi wengine.” Eva asema: “Sikiliza kwa makini uelewe malezi na hali ya maishani ya mtu huyo. Hayo huathiri jinsi watu huitikia kweli nayo yaweza kuzuia maendeleo yao. Uwe rafiki yao, ili wawe na uhakika wa kusema matatizo yao.” Carol aongezea: “Upendezi wa kweli kwa mtu ni muhimu kwa kuwa mabadiliko ambayo kweli itamletea maishani mwake nyakati nyingine yaweza kumfanya apoteze familia na marafiki. Kwa kawaida, ni vizuri mwanafunzi ajue tunakoishi na awe na uhakika wa kuja wakati wowote ule.” Msaidie kuona kutaniko kuwa familia yake.—Mathayo 10:35; Marko 10:29, 30.
“Uwe chonjo kutoa msaada wenye kutumika. Keti nao mikutanoni, na kuwasaidia pamoja na watoto wao,” asema Yolanda. Kuonyesha wapya jinsi ya kuwazoeza watoto wao, kuboresha viwango vyao vya usafi, kutayarisha maelezo kwa ajili ya mikutano, na kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi zote ni sehemu za kazi ya kufanya wanafunzi. Dada mwingine aongezea: “Ni muhimu kuwazoeza wapya katika huduma. Sehemu hii ya mazoezi ikipuuzwa, wengine watabaki wakiwa wanahofu kazi ya kuhubiri, wapoteze shangwe yao ya kumtumikia Yehova, na kushindwa kuvumilia.” Basi andaa mazoezi yenye uangalifu katika kazi ya nyumba kwa nyumba, katika kufanya ziara za kurudia, na katika kuanzisha mafunzo ya Biblia. Shangwe yako itakuwa kubwa umwonapo mwanafunzi wako akifanya maendeleo kwa msaada na mwongozo wako.
Waimarishe Wavumilie
“Kuna mwelekeo fulani wa kupuuza funzo mara mwanafunzi abatizwapo,” aonya mfanya-wanafunzi mmoja mwenye uzoefu. Ni lazima wote wawili mwalimu na mwanafunzi wakumbuke kwamba Mkristo aliyetoka kubatizwa tu si mkomavu kiroho. Ana ukuzi mwingi sana wa kufanyia imani yake, uthamini wake kwa ajili ya sheria ya Mungu, na upendo wake kwa Yehova. Ni muhimu kumtia moyo kusitawisha zoea zuri la funzo la kibinafsi ili aweze kuendelea kufanya maendeleo.—1 Timotheo 4:15.
Huyo mpya huenda akahitaji msaada wa kufanya maendeleo na kuwa mshiriki mkaribishaji wa ushirika wa akina ndugu. Huenda akahitaji mwongozo katika kushughulikia kutokamilika kwa ndugu awakaribiapo zaidi. (Mathayo 18:15-35) Anaweza kuhitaji msaada awe mwalimu stadi, awezaye kufanya utafiti wake mwenyewe. Mishonari mmoja aeleza: “Baada ya ubatizo mwanafunzi mmoja alitaka kuboresha uwezo wake wa kufundisha, basi akaniambia, ‘Nina funzo la kuongoza juma lijalo, lakini nahitaji kujikumbusha sura za kwanza nilizojifunza. Tafadhali unaweza kupitia nami sura hizi tena, moja baada ya nyingine, ili niweze kuandika habari za maelezo ya maandiko na vielezi, kisha nizitumie nikienda kuongoza funzo langu?’ Amekuwa mwalimu bora, akapata kuwa na wanne kati ya wanafunzi wake wakibatizwa kwenye kusanyiko moja.”
Sababu Inayofanya Kufanya Wanafunzi Kustahili Jitihada
“Kufanya wanafunzi kwamaanisha kuwa na wasifaji wengi zaidi wa Yehova. Kwamaanisha uhai kwa wale wanaokubali kweli,” asema Pamela. “Mimi hupenda sana kufundisha wengine kweli—kwapendeza sana! Mtu huona wanafunzi wakikua hatua kwa hatua, wakifanya mabadiliko maishani mwao na kushinda vikwazo vionekanavyo kuwa havipitiki kama si kwa msaada wa roho ya Yehova. Wengi wa wale ambao wamekuja kumpenda Yehova wamekuwa marafiki niwapendao sana.”
“Nifikiripo juu ya wale ambao nimewasaidia kuwa wanafunzi,” aeleza mishonari mmoja kutoka Ujerumani, “Nimeona watu waliokuwa na haya sana ambao wamefanya maendeleo sana wakiwa wahudumu wa Mungu mpaka siamini. Naona watu wanaoshinda vikwazo vigumu sana, kwa wazi kwa msaada wa Yehova. Naona familia ambazo wakati mmoja zilivunjika na sasa zimeungana—watoto wenye furaha walio na wazazi wenye kuchukua madaraka. Naona watu wanaofurahia maisha zenye maana, wakimsifu Yehova. Hiyo ndiyo shangwe ya kufanya wanafunzi.”
Ndiyo, kuwa mfanyakazi mwenzi wa Yehova Mungu katika kazi ya kufanya wanafunzi ni chanzo cha shangwe isiyo na kifani. Hayo mambo yaliyoonwa ya wamishonari na mapainia yamethibitisha hilo. Unaweza kupata shangwe hiyo na uradhi huo ukitumia hayo madokezo na kufanya kazi kwa nafsi yote. Kwa baraka za Yehova, shangwe yako itakamilika.—Mithali 10:22; 1 Wakorintho 15:58.