Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wazazi, Kielelezo Chenu Chafundisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Julai 1
    • Wazazi, Kielelezo Chenu Chafundisha Nini?

      “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.”—WAEFESO 5:1, 2.

      1. Yehova alitoa mielekezo gani kwa wenzi wa kwanza wa kibinadamu?

      YEHOVA ndiye Mwanzilishi wa mpango wa familia. Kila familia hutokana naye kwa sababu yeye ndiye aliyeanzisha familia ya kwanza na kuwapa wenzi wa kibinadamu wa kwanza uwezo wa kuzaa. (Waefeso 3:14, 15) Aliwapa Adamu na Hawa maagizo ya msingi kuhusu madaraka yao na pia akawapa fursa ya kutosha ili wao wenyewe wachukue hatua ya kwanza kuyatimiza. (Mwanzo 1:28-30; 2:15-22) Baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, wanadamu walilazimika kukabili hali ngumu zaidi. Hata hivyo, kwa upendo Yehova aliwatolea mielekezo ambayo ingewasaidia watumishi wake washughulikie hali hizo.

      2. (a) Ni kwa njia zipi Yehova ametumia shauri lililoandikwa kuimarisha maagizo ya mdomo? (b) Wazazi wapaswa kujiuliza maswali gani?

      2 Akiwa Mfunzi wetu Mtukufu, Yehova amefanya mengi zaidi ya kutuandalia mielekezo iliyoandikwa kuhusu yale tupaswayo kufanya na yale tupaswayo kuepuka. Nyakati za kale aliambatanisha maagizo yaliyoandikwa na maagizo ya mdomo kupitia makuhani na manabii na kupitia vichwa vya familia. Yeye anatumia nani mwingine kutoa maagizo ya mdomo wakati wetu? Wazee Wakristo na wazazi. Ikiwa wewe ni mzazi, je, unatimiza sehemu yako ya kuagiza familia yako katika njia za Yehova?—Mithali 6:20-23.

      3. Vichwa vya familia wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kufundisha kwenye matokeo?

      3 Maagizo hayo yapasa kutolewaje katika familia? Yehova hutoa kiolezo. Yeye hutaarifu waziwazi yaliyo mema na yaliyo mabaya, naye hurudia mambo mara nyingi. (Kutoka 20:4, 5; Kumbukumbu la Torati 4:23, 24; 5:8, 9; 6:14, 15; Yoshua 24:19, 20) Yeye hutumia maswali yenye kuamsha fikira. (Ayubu 38:4, 8, 31) Huchochea hisia zetu na kuelekeza mioyo yetu kwa kutumia vielezi na mifano halisi. (Mwanzo 15:5; Danieli 3:1-29) Wazazi je, nyinyi hujaribu kuiga kiolezo hicho mnapowafundisha watoto wenu?

      4. Twajifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kutia nidhamu, na ni kwa nini nidhamu ni muhimu?

      4 Yehova ni imara kuhusu yaliyo sawa, lakini yeye huelewa matokeo ya kutokamilika. Kwa hiyo, kabla ya kutoa adhabu, yeye huwafundisha na kuwatolea maonyo na vikumbusha vingi wanadamu wasiokamilika. (Mwanzo 19:15, 16; Yeremia 7:23-26) Anapotia nidhamu, yeye hufanya hivyo kwa kiwango kifaacho, hapiti kiasi. (Zaburi 103:10, 11; Isaya 28:26-29) Ikiwa hivyo ndivyo sisi hushughulika na watoto wetu, jambo hilo latoa uthibitisho wa kwamba tunamjua Yehova, na itakuwa rahisi zaidi kwa watoto kupata kumjua pia.—Yeremia 22:16; 1 Yohana 4:8.

      5. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kusikiliza?

      5 Ni jambo la ajabu kwamba Yehova husikiliza kama Baba wa kimbingu mwenye upendo. Yeye hatoi maagizo tu. Yeye hututia moyo tumweleze hisia zetu zote. (Zaburi 62:8) Na ikiwa hisia hizo tunazomweleza hazifai kabisa, yeye hatukemei kwa sauti kubwa kutoka mbinguni. Yeye hutufundisha kwa subira. Hivyo, lafaa kama nini shauri hili la mtume Paulo: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa”! (Waefeso 4:31–5:1) Yehova anawatolea wazazi kielelezo kizuri kama nini wanapojaribu kuwaagiza watoto wao! Ni kielelezo kinachotugusa moyo na kufanya tutake kutembea katika njia yake ya maisha.

      Uvutano Unaotokezwa na Kielelezo

      6. Mtazamo na kielelezo cha wazazi kina uvutano gani kwa watoto wao?

      6 Kwa kuongezea maagizo ya mdomo, kielelezo pia kina uvutano mkubwa kwa wachanga. Wazazi wapende wasipende, watoto wao watawaiga. Huenda wazazi wakapendezwa—nyakati nyingine wakashtuka—kusikia watoto wao wakisema mambo ambayo wazazi wenyewe wameyasema. Mwenendo na mtazamo wa wazazi unapoonyesha kwamba wanathamini sana mambo ya kiroho, jambo hilo huwa na matokeo yafaayo kwa watoto.—Mithali 20:7.

      7. Yeftha alimwekea binti yake kielelezo akiwa mzazi wa aina gani, na matokeo yakawa nini?

      7 Biblia inatoa vielezi vizuri juu ya matokeo ya kielelezo cha wazazi. Yeftha, aliyetumiwa na Yehova kuongoza Waisraeli kuwashinda Waamoni, alikuwa baba pia. Rekodi ya jibu lake kwa mfalme wa Amoni yaonyesha kwamba ni lazima Yeftha awe alisoma mara nyingi historia ya jinsi Yehova alivyoshughulika na Israeli. Angeweza kunukuu historia hiyo bila tatizo, naye alionyesha imani yenye nguvu katika Yehova. Haikosi kielelezo chake kilimsaidia binti yake asitawishe imani na roho ya kujinyima aliyoionyesha kwa kuchukua daraka la kumtumikia akiwa mseja mwanamke aliyejitoa kwa Yehova.—Waamuzi 11:14-27, 34-40; linganisha Yoshua 1:8.

      8. (a) Wazazi wa Samweli walionyesha mtazamo gani mzuri? (b) Jambo hilo lilimnufaishaje Samweli?

      8 Katika maisha yake yote, Samweli alikuwa kielelezo chema akiwa mtoto na vilevile nabii mwaminifu kwa Mungu. Je, ungependa watoto wako wapate kuwa kama yeye? Ebu changanua kielelezo kilichowekwa na Elkana na Hana, wazazi wa Samweli. Ingawa hali katika familia yao haikuwa nzuri kabisa, walienda kuabudu huko Shilo kwa ukawaida, mahali ambapo tabenakulo takatifu lilikuwa. (1 Samweli 1:3-8, 21) Ona jinsi Hana alivyosali kwa hisia nyingi. (1 Samweli 1:9-13) Ona jinsi wote wawili walivyohisi kuhusu umuhimu wa kutimiza ahadi yoyote waliyomtolea Mungu. (1 Samweli 1:22-28) Haikosi kielelezo chao chema kilimsaidia Samweli asitawishe sifa zilizomsaidia afuatie mwenendo ufaao—hata wakati ambapo watu waliokuwa karibu naye, ambao walitarajiwa kumtumikia Yehova, walikosa kabisa kustahi njia za Mungu. Baada ya muda Yehova alimtwika Samweli daraka la kuwa nabii Wake.—1 Samweli 2:11, 12; 3:1-21.

      9. (a) Ni hali gani za nyumbani zilizokuwa na uvutano mzuri kwa Timotheo? (b) Timotheo alipata kuwa mtu wa aina gani?

      9 Je, ungetaka mwana wako awe kama Timotheo, ambaye akiwa kijana alipata kuwa mshiriki wa mtume Paulo? Baba ya Timotheo hakuwa mwamini, lakini mama na nyanya yake walimwekea kielelezo kizuri cha kuthamini mambo ya kiroho. Yaelekea jambo hilo lilisaidia kumwekea Timotheo msingi mzuri akiwa Mkristo. Tunaambiwa kwamba Eunike mama yake, na Loisi nyanya yake, walikuwa na “imani . . . isiyo na unafiki wowote.” Maisha yao wakiwa Wakristo hayakuwa yenye unafiki; kwa hakika waliishi kupatana na yale waliyodai kuamini, nao wakamfundisha kijana Timotheo kufanya vivyo hivyo. Timotheo alithibitisha kwamba alikuwa mwenye kutegemeka, na kwamba alijali kikweli hali njema ya wengine.—2 Timotheo 1:5; Wafilipi 2:20-22.

      10. (a) Ni vielelezo gani viwezavyo kuathiri watoto wetu nje ya nyumbani? (b) Tufanyeje uvutano huo ukijidhihirisha katika usemi na mtazamo wa watoto wetu?

      10 Si vielelezo vyote vinavyoathiri watoto ambavyo hupatikana nyumbani. Kuna watoto wanaosoma nao shuleni, walimu ambao kazi yao ni kufinyanga akili changa, watu ambao hushikilia kwa dhati kwamba kila mtu apaswa kufuata desturi za kikabila zilizo imara kabisa, wachezaji maarufu ambao mafanikio yao husifiwa na wengi, na maofisa wa umma ambao mwenendo wao hutajwa mara nyingi katika vyombo vya habari. Mamilioni ya watoto pia wameona ukatili wa vita. Je, tushangae uvutano huo ukijidhihirisha katika usemi na mtazamo wa watoto wetu? Tufanyeje inapokuwa hivyo? Je, kemeo au karipio kali linatatua tatizo hilo? Badala ya kuwajibu watoto wetu haraka-haraka, je, haingekuwa afadhali kujiuliza, ‘Je, kuna jambo lolote katika njia ambayo Yehova hushughulika nasi linaloweza kutusaidia kufahamu jinsi ya kushughulikia hali hii?’—Linganisha Waroma 2:4.

      11. Mtazamo wa watoto waweza kuathiriwaje wazazi wanapokosea?

      11 Bila shaka, si sikuzote wazazi wasiokamilika watashughulikia hali katika njia ifaayo kabisa. Watafanya makosa. Watoto wakitambua hivyo je, jambo hilo halitaharibu staha yao kwa wazazi wao? Linaweza, hasa wazazi wakijaribu kupunguza uzito wa makosa yao kwa kusisitiza mamlaka yao kwa ukali. Lakini matokeo yanaweza kuwa tofauti kabisa wazazi wakiwa wanyenyekevu na wanakubali makosa yao kwa hiari. Kwa kufanya hivyo wanaweza kuwawekea watoto wao, ambao pia wanahitaji kufanya vivyo hivyo, kielelezo chenye thamani.—Yakobo 4:6.

      Mambo Ambayo Kielelezo Chetu Chaweza Kufundisha

      12, 13. (a) Watoto wahitaji kujifunza nini kuhusu upendo, na jambo hilo laweza kufundishwaje kwa matokeo zaidi? (b) Kwa nini ni muhimu kwa watoto kujifunza kuhusu upendo?

      12 Kuna masomo mengi yenye thamani yawezayo kufundishwa kwa matokeo zaidi wakati maagizo ya mdomo yanapoambatanishwa na kielelezo kizuri. Fikiria machache.

      13 Kuonyesha upendo usio na ubinafsi: Mojawapo ya masomo muhimu ambayo huimarishwa kwa kielelezo ni maana ya upendo. “Twapenda, kwa sababu [Mungu] alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Yeye ndiye Chanzo na kielelezo bora kabisa cha upendo. Upendo huu wa kanuni, a·gaʹpe, umetajwa katika Biblia zaidi ya mara 100. Ni sifa ambayo hutambulisha Wakristo wa kweli. (Yohana 13:35) Upendo huo wapaswa uonyeshwe kwa Mungu na Yesu Kristo, na wanadamu pia wapaswa kuonyeshana upendo huo—hata kuuonyesha kwa wanadamu ambao huenda tusipendezwe nao sana. (Mathayo 5:44, 45; 1 Yohana 5:3) Ni lazima upendo huo uwe mioyoni mwetu na udhihirike maishani mwetu kabla ya kuweza kuufundisha watoto wetu kwa matokeo. Muungwana ni kitendo. Katika familia, watoto wanahitaji kuona na kuonyeshwa upendo na sifa nyinginezo zinazohusiana na upendo, kama vile shauku. Bila mambo hayo, ukuzi wa mtoto kimwili, kiakili, na kihisia-moyo unazuiwa. Watoto wanahitaji kuona namna ambavyo Wakristo wenzetu, ambao si wa familia yetu, huonyeshwa upendo na shauku ifaavyo.—Waroma 12:10; 1 Petro 3:8.

      14. (a) Watoto waweza kufundishwaje kufanya kazi nzuri inayoridhisha? (b) Hilo laweza kufanywaje katika familia yako?

      14 Kujifunza jinsi ya kufanya kazi: Kazi ni sehemu muhimu ya maisha. Mtu anahitaji kujifunza kufanya kazi vizuri ili apate kujistahi. (Mhubiri 2:24; 2 Wathesalonike 3:10) Mtoto akipewa kazi ambazo hajaonyeshwa vizuri jinsi ya kuzifanya, kisha akemewe kwa kutozifanya vizuri, haielekei atajifunza kufanya kazi nzuri. Lakini watoto wanapojifunza hasa kwa kufanya kazi pamoja na wazazi wao na kusifiwa ifaavyo, yaelekea zaidi watajifunza kufanya kazi inayoridhisha. Kielelezo cha wazazi kikiambatanishwa na maelezo, watoto wanaweza kujifunza jinsi ya kufanya kazi vizuri na pia jinsi ya kutatua matatizo, jinsi ya kuendelea kufanya kazi hadi inapoisha, na jinsi ya kusababu na kufanya maamuzi. Katika hali hiyo wanaweza kusaidiwa kufahamu kwamba Yehova pia hufanya kazi, kwamba yeye hufanya kazi nzuri, na kwamba Yesu humwiga Baba yake. (Mwanzo 1:31; Mithali 8:27-31; Yohana 5:17) Ikiwa familia inafanya kazi ya ukulima au biashara, baadhi ya washiriki wa familia hiyo wanaweza kufanya kazi pamoja. Au labda mama anaweza kumfundisha mwana wake au binti yake kupika na kusafisha vyombo baada ya mlo. Baba anayefanya kazi ya kuajiriwa mbali na nyumbani anaweza kupanga kuwa na kazi za kufanya nyumbani akiwa pamoja na watoto. Ni jambo lenye kunufaisha kama nini wazazi wanapokumbuka kwamba wanawaandaa watoto wao kwa muda wa maisha yao yote bali si wamalize tu kufanya kazi fulani ya wakati huo!

      15. Masomo katika imani yanaweza kufundishwa katika njia zipi? Toa kielezi.

      15 Kudumisha imani wakati wa janga: Imani pia ni sehemu muhimu ya maisha yetu. Imani inapozungumziwa katika funzo la familia, watoto wanaweza kujifunza kuifafanua. Wanaweza pia kufahamu uthibitisho unaofanya imani ianze kukua mioyoni mwao. Lakini wanapoona wazazi wao wakionyesha imani thabiti wanapopatwa na majaribu, jambo hilo laweza kuathiri maisha yao yote. Mwanafunzi mmoja wa Biblia wa Panama alitishwa na mumewe kufukuzwa nyumbani kwao asipoacha kumtumikia Yehova. Hata hivyo, yeye pamoja na watoto wake wanne, walitembea kwa ukawaida umbali wa kilometa 16, kisha wakasafiri kwa basi kilometa nyingine 30 ili kufika kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa karibu zaidi. Kwa kutiwa moyo na kielelezo chake, washiriki wapatao 20 wa familia yao walikubali njia ya ile kweli.

      Kuweka Kielelezo Katika Usomaji wa Biblia wa Kila Siku

      16. Kwa nini usomaji wa Biblia wa kila siku unapendekezwa?

      16 Mojawapo ya desturi zenye thamani zaidi ambazo familia yaweza kuanzisha—desturi itakayowanufaisha wazazi na kuwa kielelezo kwa watoto—ni usomaji wa Biblia wa kawaida. Ikiwezekana, someni Biblia kila siku. Kilicho muhimu zaidi si ukubwa wa sehemu inayosomwa bali ni ukawaida na namna usomaji huo unavyofanywa. Mbali na usomaji wa Biblia, watoto wanaweza pia kusikiliza kaseti za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, ikiwa zinapatikana katika lugha yenu. Kusoma Neno la Mungu kila siku hutusaidia kutanguliza mawazo ya Mungu. Na ikiwa usomaji huo unafanywa na familia, wala si mtu mmoja-mmoja, jambo hilo laweza kusaidia familia nzima itembee katika njia za Yehova. Familia zilitiwa moyo ziwe na desturi ya kufanya hivyo katika drama Familia—Fanyeni Usomaji wa Biblia Kila Siku Uwe Njia Yenu ya Maisha! kwenye Mikusanyiko ya hivi majuzi ya “Njia ya Mungu ya Maisha.”—Zaburi 1:1-3.

      17. Usomaji wa Biblia wa familia na kukariri maandiko muhimu husaidiaje kutumia shauri lililo kwenye Waefeso 6:4?

      17 Usomaji wa Biblia wa familia wapatana na yale mtume Paulo aliyopuliziwa kuandika katika barua yake kwa Wakristo wa Efeso, yaani: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Hilo lamaanisha nini? “Rekebisho la akilini” kihalisi humaanisha “kutia akili katika”; kwa hiyo, baba Wakristo wanahimizwa kutia akili ya Yehova Mungu katika watoto wao—kuwasaidia watoto wapate kujua mawazo ya Mungu. Kuwatia moyo watoto wakariri maandiko muhimu, kwaweza kusaidia kutimiza jambo hilo. Lengo ni kufanya mawazo ya Yehova yaongoze kufikiri kwa watoto ili hatua kwa hatua tamaa zao na mwenendo wao upate kudhihirisha viwango vya Mungu, iwe wazazi wako pamoja na watoto hao au la. Kufikiri kwa aina hiyo hutokana na Biblia.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

      18. Wakati wa kuisoma Biblia ni nini ambacho huenda kikahitajiwa ili (a) kuielewa vizuri? (b) kunufaishwa na shauri lake? (c) kuitikia yale ifunuayo kuhusu kusudi la Yehova? (d) kunufaishwa na yale isemayo kuhusu mitazamo na matendo ya watu?

      18 Bila shaka, ikiwa Biblia itaathiri maisha yetu, twahitaji kuelewa yale isemayo. Kwa wengi, hilo huenda likahitaji wasome sehemu mbalimbali mara kadhaa. Ili kuelewa vizuri semi fulani, huenda tukahitaji kuangalia maneno katika kamusi au katika Insight on the Scriptures. Ikiwa andiko linatoa shauri au amri, chukua wakati wa kuzungumzia hali za wakati wetu zinazofanya hilo lifae. Kisha unaweza kuuliza, ‘Twaweza kunufaikaje kwa kutumia shauri hili?’ (Isaya 48:17, 18) Ikiwa andiko hilo lasimulia sehemu fulani ya kusudi la Yehova, uliza, ‘Andiko hili laathirije maisha yetu?’ Labda unasoma simulizi linalotaja mitazamo na matendo ya watu. Ni mikazo gani ya maisha waliyokuwa wakivumilia? Walishughulikiaje mikazo hiyo? Twaweza kunufaishwaje na kielelezo chao? Ruhusu wakati sikuzote wa kuzungumzia maana ya simulizi hilo katika maisha yetu leo.—Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:11.

      19. Kwa kuwa waigaji wa Mungu, tutakuwa tukiwaandalia watoto wetu nini?

      19 Hiyo ni njia nzuri kama nini ya kukazia mawazo ya Mungu katika akili na mioyo yetu! Hivyo tutasaidiwa kwelikweli kuwa ‘waigaji wa Mungu, tukiwa watoto wapendwa.’ (Waefeso 5:1) Nasi tutatoa kielelezo ambacho kwa kweli chastahili kuigwa na watoto wetu.

      Je, Wakumbuka?

      ◻ Wazazi waweza kunufaishwaje na kielelezo cha Yehova?

      ◻ Kwa nini ni lazima kufundisha watoto kwa maneno kuambatanishwe na kielelezo kizuri cha wazazi?

      ◻ Ni baadhi ya masomo gani yawezayo kufundishwa vizuri zaidi kwa kielelezo cha wazazi?

      ◻ Twaweza kunufaikaje kikamili kutokana na usomaji wa Biblia?

  • Jifunzeni Neno la Mungu kwa Ukawaida Mkiwa Familia
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Julai 1
    • Jifunzeni Neno la Mungu kwa Ukawaida Mkiwa Familia

      “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.”—MATHAYO 4:4.

      1. Biblia husema nini kuhusu daraka la vichwa vya familia la kufundisha watoto wao njia za Yehova?

      YEHOVA MUNGU alikumbusha vichwa vya familia mara nyingi kuhusu daraka lao la kufundisha watoto wao. Maagizo hayo yangewaandaa watoto kwa ajili ya maisha ya sasa na pia yangeweza kuwatayarisha kwa ajili ya maisha ya baadaye. Malaika akimwakilisha Mungu alimkazia Abrahamu daraka lake la kufundisha jamaa yake ili iweze ‘kushika njia ya BWANA.’ (Mwanzo 18:19) Wazazi Waisraeli walitakiwa wawaeleze watoto wao jinsi Mungu alivyowaokoa Waisraeli kutoka Misri na jinsi alivyowatolea Sheria kwenye Mlima Sinai, huko Horebu. (Kutoka 13:8, 9; Kumbukumbu la Torati 4:9, 10; 11:18-21) Vichwa vya familia walio Wakristo wanashauriwa walee watoto wao “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Hata ikiwa ni mzazi mmoja tu anayemtumikia Yehova, yeye apaswa kujitahidi kuwafundisha watoto wake njia za Yehova.—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.

      2. Je, funzo la familia linahitajika ikiwa hakuna watoto nyumbani? Eleza.

      2 Hilo halimaanishi kwamba funzo la familia la Neno la Mungu ni kwa ajili ya jamaa zenye watoto tu. Mume na mke huonyesha uthamini mzuri wa mambo ya kiroho wanapokuwa na funzo la familia hata ikiwa hakuna watoto nyumbani.—Waefeso 5:25, 26.

      3. Kwa nini funzo la familia la kawaida ni muhimu?

      3 Ili yawe na matokeo mazuri zaidi, maagizo yapasa kutolewa kwa ukawaida, kupatana na somo ambalo Yehova aliwafundisha Waisraeli nyikani: “Mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 8:3) Kwa kutegemea hali za familia, huenda jamaa fulani zikapanga kujifunza kila juma; nyingine zikajifunza kwa vipindi vifupi-vifupi kila siku. Hata iwe mtachagua mpango gani, msikose kuratibu wakati kwa ajili ya funzo. ‘Nunueni wakati’ kwa ajili ya funzo. Kujidhabihu ili kupata wakati huo ni jambo linalonufaisha sana. Uhai wa washiriki wa familia yako umo hatarini.—Waefeso 5:15-17; Wafilipi 3:16.

      Malengo ya Kukumbukwa

      4, 5. (a) Ni nini ambacho Yehova aliwatolea wazazi kupitia Musa kiwe lengo muhimu katika kuwafundisha watoto wao? (b) Hilo lahusisha nini leo?

      4 Unapoongoza funzo la familia, litanufaisha zaidi ukikumbuka kuwa na malengo hususa. Chunguza malengo kadhaa.

      5 Kwenye kila funzo, jaribu kusitawisha upendo kwa Yehova Mungu. Waisraeli walipokusanyika kwenye uwanda wa Moabu, kabla ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa, Musa alikaza fikira zao kwenye ile ambayo baadaye Yesu Kristo angeitambulisha kuwa “amri kubwa zaidi sana katika ile Sheria.” Amri gani? “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:36, 37; Kumbukumbu la Torati 6:5) Musa aliwahimiza Waisraeli wakaze amri hiyo katika mioyo yao wenyewe na kuwafundisha watoto wao kuihusu. Jambo hilo lingehitaji kurudia-rudia, kuvuta fikira kwenye sababu za kumpenda Yehova, kushughulika na mitazamo na mwenendo uwezao kuzuia kuonyeshwa kwa upendo huo, na kuonyesha upendo wao kwa Yehova katika maisha yao wenyewe. Je, watoto wetu wanahitaji maagizo ya aina hiyo? Ndiyo! Nao pia wanahitaji msaada ili ‘kutahiri mioyo yao,’ yaani, kuondoa chochote ambacho kingewazuia wasimpende Mungu. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 16; Yeremia 4:4) Huenda baadhi ya vizuizi hivyo vikawa tamaa ya vitu vya ulimwengu na fursa za kujitia katika shughuli zake. (1 Yohana 2:15, 16) Upendo kwa Yehova wapaswa kuwa hai, dhahiri, ukitusukuma tufanye mambo yampendezayo Baba yetu wa kimbingu. (1 Yohana 5:3) Ili funzo la familia yako liwe na manufaa ya kudumu, kila kipindi chapasa kuongozwa katika njia inayoimarisha upendo huo.

      6. (a) Ni nini kihitajiwacho ili kutoa ujuzi sahihi? (b) Maandiko yanakaziaje umuhimu wa ujuzi sahihi?

      6 Toa ujuzi sahihi juu ya matakwa ya Mungu. Hilo lahusisha nini? Lahusisha mengi zaidi ya uwezo wa kusoma na kutoa majibu kutoka kwa gazeti au kitabu. Kwa kawaida lahitaji mazungumzo ili kuhakikisha kwamba maneno muhimu na mawazo makuu yanaeleweka vizuri. Ujuzi sahihi ni muhimu katika kuvaa utu mpya, katika kuzingatia mambo yaliyo ya maana hasa unaposhughulika na matatizo maishani, na vilevile, katika kufanya yale yampendezayo Mungu kikweli.—Wafilipi 1:9-11; Wakolosai 1:9, 10; 3:10.

      7. (a) Familia yaweza kusaidiwa kutumia maishani habari inayojifunza kwa kutumia maswali gani? (b) Maandiko yanakaziaje thamani ya kuwa na lengo kama hilo?

      7 Saidia washiriki wa familia watumie maishani mambo wanayojifunza. Ukiwa na lengo hilo akilini, uliza hivi wakati wa kila funzo la familia: ‘Habari hii inapaswa iathirije maisha yetu? Je, yahitaji tufanye mabadiliko yoyote katika maisha yetu ya sasa? Kwa nini tutake kufanya mabadiliko?’ (Mithali 2:10-15; 9:10; Isaya 48:17, 18) Kuwa waangalifu vya kutosha kutumia maishani mambo mnayojifunza kwaweza kuchangia ukuzi wa kiroho wa washiriki wa familia.

      Tumia Vifaa vya Kufundishia kwa Hekima

      8. Jamii ya mtumwa imeandaa vifaa gani vya kujifunzia Biblia?

      8 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametoa vifaa vingi vinavyoweza kutumiwa kujifunza. Gazeti la Mnara wa Mlinzi, la kutumia pamoja na Biblia, linapatikana katika lugha 131. Kuna vitabu vya kujifunzia Biblia katika lugha 153, broshua katika lugha 284, kaseti za kusikilizia Biblia katika lugha 61, kaseti za vidio katika lugha 41, hata programu ya kompyuta ya kufanya utafiti wa Biblia katika lugha 9!—Mathayo 24:45-47.

      9. Tunaweza kutumiaje mashauri katika maandiko yaliyoonyeshwa kwenye fungu hili tunapokuwa na funzo la familia la Mnara wa Mlinzi?

      9 Jamaa nyingi hutumia wakati wa funzo la familia ili kujitayarisha kwa ajili ya Funzo la kutaniko la Mnara wa Mlinzi. Kufanya hivyo kwaweza kusaidia kama nini! Gazeti la Mnara wa Mlinzi lina chakula muhimu cha kiroho ambacho huandaliwa ili kuimarisha watu wa Yehova ulimwenguni pote. Mnapojifunza Mnara wa Mlinzi mkiwa familia, fanyeni zaidi ya kusoma mafungu na kujibu maswali yaliyochapwa. Jitahidini sana kuelewa mambo. Chukueni wakati kusoma maandiko yaliyotajwa bila kunukuliwa. Waombe washiriki wa familia waeleze jinsi mambo hayo yanavyohusiana na yale yaliyotajwa katika fungu linalozungumziwa. Husisha moyo.—Mithali 4:7, 23; Matendo 17:11.

      10. Ni nini kiwezacho kufanywa ili kuhusisha watoto katika funzo na kulifanya liwafurahishe?

      10 Ikiwa kuna watoto katika jamaa yako, unaweza kufanya nini ili funzo lisiwe desturi tu ya familia, bali liwe lenye kujenga, lenye kupendeza, na lenye furaha? Jitahidi sana kushirikisha kila mmoja katika njia ifaayo ili fikira zikazwe kwenye habari inayozungumziwa. Inapowezekana, panga kila mtoto awe na Biblia yake mwenyewe na gazeti mnalojifunza. Kwa kuiga uchangamfu ulioonyeshwa na Yesu, huenda mzazi akataka mtoto mchanga aketi karibu sana naye, labda akimkumbatia mtoto huyo kwa mkono mmoja. (Linganisha Marko 10:13-16.) Huenda kichwa cha familia akataka kijana aeleze picha fulani katika habari wanayozungumzia. Mtoto mchanga aweza kupewa mgawo mapema wa kusoma andiko fulani. Mtoto mwingine mwenye umri mkubwa zaidi aweza kupewa mgawo wa kutaja fursa mbalimbali za kutumia habari wanayojifunza.

      11. Ni vifaa gani vingine vya kujifunzia ambavyo vimeandaliwa, navyo vyaweza kutumiwaje kwa manufaa kuhusiana na funzo la familia mahali vinapopatikana?

      11 Ingawa huenda ukawa unatumia Mnara wa Mlinzi kuwa msingi wa mazungumzo yako, usisahau vifaa vingine vya kujifunzia ambavyo vyapatikana katika lugha nyingi. Ikiwa habari au ufafanuzi wahitajiwa ili kuelewa usemi fulani wa Biblia, kichapo Insight on the Scriptures chaweza kuutoa. Maswali mengine yaweza kujibiwa kwa kurejezea Watch Tower Publications Index au kwa kutumia programu ya kompyuta ya kufanya utafiti ambayo imeandaliwa na Sosaiti. Kujifunza kutumia vifaa hivi, ikiwa vinapatikana katika lugha yako, kwaweza kuwa sehemu yenye manufaa ya funzo la familia. Ukiwa na lengo la kuchochea upendezi wa wachanga, pia huenda ukatenga sehemu ya wakati wako wa funzo ili kutazama sehemu fulani ya vidio za Sosaiti zenye maagizo au kusikiliza sehemu ya drama kwenye kaseti, kisha kuizungumzia. Kutumia ifaavyo vifaa hivi vya kujifunzia kutasaidia kufanya funzo la familia yako liwe lenye kupendeza na lenye kunufaisha familia nzima.

      Rekebisha Funzo Lifae Mahitaji ya Familia Yako

      12. Funzo la familia laweza kutimizaje fungu katika kushughulikia mahitaji muhimu ya famillia?

      12 Huenda ikawa kwa kawaida familia yako hujifunza somo la Mnara wa Mlinzi la kila juma. Lakini fahamu matatizo na maoni ya msingi ya familia. Ikiwa si lazima mama afanye kazi ya kuajiriwa, anaweza kutumia wakati pamoja na watoto kila siku wanapokuja nyumbani kutoka shuleni. Hali fulani zaweza kushughulikiwa wakati huo; huenda nyingine zikahitaji uangalifu zaidi. Kunapokuwa na mahitaji muhimu ya familia, usiyapuuze. (Mithali 27:12) Huenda hayo yakahusisha hali nyinginezo mbali na matatizo shuleni. Teua habari ifaayo, na uijulishe familia mapema kuhusu kile mtakachojifunza.

      13. Kwa nini mazungumzo ya familia kuhusu jinsi ya kukabiliana na umaskini yaweza kunufaisha?

      13 Kwa mfano, sehemu kubwa ya dunia imekumbwa na umaskini; hivyo katika mahali pengi, huenda ikahitajika kuzungumzia jinsi ya kukabiliana na hali hiyo. Je, jamaa yako ingenufaika na funzo la familia linalokazia hali halisi maishani na kanuni ya Biblia?— Mithali 21:5; Mhubiri 9:11; Waebrania 13:5, 6, 18.

      14. Ni hali gani zaweza kufanya mazungumzo ya familia juu ya maoni ya Yehova kuhusu jeuri, vita, na kutokuwamo kwa Kikristo yafae?

      14 Jeuri ni habari nyingine inayohitaji kuzungumziwa. Sote twahitaji kukazia kikiki maoni ya Yehova katika akili na mioyo yetu. (Mwanzo 6:13; Zaburi 11:5) Funzo la familia juu ya habari hiyo laweza kuandaa hali ya kuzungumzia jinsi ya kushughulika na wachokozi shuleni, kama watoto watajifunza mbinu za karate, na jinsi ya kuchagua tafrija ifaayo. Mapambano yenye jeuri yamekuwa mengi; karibu kila nchi imekumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe, ugomvi wa kisiasa au wa kikabila, au vita vya magenge. Tokeo likiwa kwamba, familia yako huenda ikahitaji kuzungumza juu ya kudumisha mwenendo wa Kikristo ingawa wamezungukwa na vikundi vyenye kupigana.—Isaya 2:2-4; Yohana 17:16.

      15. Maagizo juu ya ngono na ndoa yapasa yatoleweje kwa watoto?

      15 Watoto wanapokua, wanahitaji maagizo yanayofaa umri wao juu ya ngono na ndoa. Katika tamaduni fulani wazazi walio wengi hawazungumzii ngono kamwe pamoja na watoto wao. Watoto wasio na habari waweza kupata maoni yaliyopotoka kutoka kwa vijana wengine, na matokeo yaweza kuwa yenye msiba. Je, haingekuwa afadhali kumwiga Yehova, ambaye hutoa shauri moja kwa moja, lakini kwa busara kuhusu jambo hilo katika Biblia? Shauri la Mungu litawasaidia watoto wetu wadumishe hali ya kujistahi na kuwatendea kwa heshima wale wa jinsia tofauti. (Mithali 5:18-20; Wakolosai 3:5; 1 Wathesalonike 4:3-8) Hata ikiwa tayari umezungumzia mambo haya, usisite kufanya hivyo tena. Hali mpya zitokeapo, ni muhimu kurudia mambo hayo.

      16. (a) Funzo la familia hufanywa lini katika jamaa mbalimbali? (b) Umeshughulikiaje vizuizi ili kuwa na funzo la familia la kawaida?

      16 Funzo la familia laweza kufanywa wakati gani? Kwa kuiga familia za Betheli duniani pote, jamaa nyingi zimeratibu kufanya funzo la familia Jumatatu jioni. Nyingine zina ratiba tofauti. Huko Argentina familia yenye watu 11, kutia ndani watoto 9, iliamka kwa ukawaida saa 11 kila alfajiri ili kufanya funzo lao la familia. Kwa sababu ya ratiba za kazi zilizokuwa tofauti, hawangeweza kufanya funzo hilo wakati mwingine. Haikuwa rahisi, lakini kufanya hivyo kulikaza katika akili na mioyo ya watoto hao umuhimu wa funzo la familia. Nchini Filipino mzee mmoja alifanya funzo la familia la kawaida pamoja na mke wake na watoto wao watatu walipokuwa wakikua. Katikati ya juma wazazi pia walijifunza kibinafsi na kila mtoto ili kila mmoja wao afanye kweli kuwa mali yake mwenyewe. Huko Marekani, dada mmoja ambaye mume wake si Shahidi hutembea na watoto wake kila asubuhi hadi kwenye basi la shule. Wanapongojea basi hilo, wao hutumia takriban dakika kumi pamoja wakisoma na kuzungumzia habari ifaayo ya kujifunza itegemeayo Maandiko, kisha mama huyo hutoa sala fupi kabla ya watoto kupanda basi. Katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, mwanamke mmoja ambaye mume wake asiyeamini aliiacha familia hulazimika kujitahidi kujifunza kwa sababu hana elimu ya kutosha. Mwana wake aliye mtu mzima husaidia kwa kuitembelea familia hiyo kila juma ili kuongoza funzo linalotia ndani mama yake na ndugu zake wachanga. Mama huyo huweka kielelezo kizuri kwa kujitayarisha kwa bidii. Je, kuna hali inayofanya iwe vigumu kuwa na funzo la familia la kawaida katika jamaa yako? Usikate tamaa. Jitahidi sana kupata baraka ya Yehova juu ya jitihada zako za kuwa na funzo la Biblia la kawaida.—Marko 11:23, 24.

      Thawabu Zinazotokana na Kustahimili

      17. (a) Ni nini kinachohitajiwa ili kuwa na funzo la familia la kawaida? (b) Ni jambo gani lililoonwa ambalo latoa kielelezi juu ya umuhimu wa kuagiza familia kwa ukawaida kuhusu njia za Yehova?

      17 Kupanga kunahitajiwa. Kustahimili kunatakiwa pia. Lakini manufaa zinazotokana na funzo la familia la kawaida zinafanya funzo hilo listahili. (Mithali 22:6; 3 Yohana 4) Huko Ujerumani, Franz na Hilda walilea watoto 11 katika familia yao. Miaka kadhaa baadaye, binti yao Magdalena alisema hivi: “Ninachofikiria kuwa muhimu zaidi leo ni kwamba hakuna hata siku moja iliyopita bila sisi kupokea mafundisho fulani ya kiroho.” Wakati roho ya utukuzo wa taifa ilipochacha wakati wa Adolf Hitler, baba ya Magdalena alitumia Biblia kutayarisha familia yake kwa ajili ya majaribu ambayo aling’amua yalikuwa yanakuja. Baada ya muda, washiriki wa familia waliokuwa wachanga zaidi walikamatwa na kupelekwa kwenye shule ya kuadibisha; wengine katika familia wakakamatwa, wakatiwa katika gereza na kambi za mateso. Wengine wakauawa. Wote walidumisha imani thabiti—siyo tu wakati wa mnyanyaso huo mkali bali pia, kwa waokokaji, katika miaka iliyofuata.

      18. Jitihada za wazazi wasio na wenzi zimethawabishwaje?

      18 Wazazi wengi wasio na wenzi na pia wale ambao wenzi wao wana imani tofauti, hali kadhalika wamewatolea watoto wao maagizo ya Biblia kwa ukawaida. Mama mmoja, mjane huko India, alijitahidi sana kufundisha watoto wake wawili kumpenda Yehova. Hata hivyo, alivunjika moyo mwana wake alipojitenga na watu wa Yehova. Alimwomba Yehova amsamehe makosa yoyote aliyofanya alipokuwa akimzoeza mwana wake. Lakini mwana huyo hakuwa amesahau kabisa yale aliyokuwa amejifunza. Baada ya muda wa zaidi ya miaka kumi, alirudi, akafanya maendeleo ya kiroho, akawa mzee wa kutaniko. Sasa yeye na mke wake wanatumikia wakiwa wahudumu mapainia wa wakati wote. Wamekuwa wenye shukrani kama nini wazazi wale ambao wamezingatia moyoni shauri la Yehova na tengenezo lake kuhusu kutoa maagizo ya Biblia kwa ukawaida katika familia! Je, unatumia shauri hilo katika jamaa yako?

      Je, Waweza Kueleza?

      ◻ Kwa nini funzo la familia la kawaida ni muhimu?

      ◻ Malengo yetu yapasa kuwa nini wakati wa kila funzo la familia?

      ◻ Ni vifaa gani vya kufundishia ambavyo vimetolewa kwa ajili yetu?

      ◻ Funzo laweza kurekebishwaje lifae mahitaji ya familia?

      [Picha katika ukurasa wa 15]

      Malengo hususa yataboresha funzo la familia yako

  • Familia, Sifuni Mungu Mkiwa Sehemu ya Kutaniko Lake
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Julai 1
    • Familia, Sifuni Mungu Mkiwa Sehemu ya Kutaniko Lake

      “Katika makusanyiko nitamhimidi BWANA.”—ZABURI 26:12.

      1. Mbali na kujifunza na kutoa sala nyumbani, ni nini iliyo sehemu muhimu ya ibada ya kweli?

      KUMWABUDU Yehova hutia ndani sala na kujifunza Biblia nyumbani, na vilevile utendaji tukiwa sehemu ya kutaniko la Mungu. Waisraeli wa kale waliamriwa “wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto,” ili wajifunze sheria ya Mungu kusudi watembee katika njia yake. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Yoshua 8:35) Wazee na “vijana waume na wanawali” walitiwa moyo washiriki katika kulisifu jina la Yehova. (Zaburi 148:12, 13) Mipango sawa na hiyo hutumika katika kutaniko la Kikristo. Katika Majumba ya Ufalme kotekote duniani, wanaume, wanawake, na watoto hushiriki kwa hiari katika vipindi vinavyohusisha wasikilizaji, na wengi hufurahia kushiriki.—Waebrania 10:23-25.

      2. (a) Kwa nini kujitayarisha ni muhimu katika kusaidia wachanga wafurahie mikutano? (b) Ni kielelezo cha nani ambacho ni muhimu?

      2 Ni kweli kwamba huenda ikawa vigumu kuwasaidia wachanga wazoee kawaida yenye kujenga ya utendaji wa kutaniko. Huenda tatizo likawa nini ikiwa watoto fulani wanaohudhuria mikutano pamoja na wazazi wao hawaonekani kufurahia mikutano? Bila shaka, watoto wengi hukaza fikira zao kwa kipindi kifupi nao huchoshwa haraka. Kujitayarisha kwaweza kusaidia kutatua tatizo hilo. Bila kujitayarisha, watoto hawawezi kushiriki kwenye mikutano kwa njia yenye maana. (Mithali 15:23) Bila kujitayarisha, itakuwa vigumu kwao kufanya maendeleo ya kiroho yanayoridhisha. (1 Timotheo 4:12, 15) Ni nini kiwezacho kufanywa? Kwanza, wazazi wahitaji kujiuliza kama wao wenyewe hujitayarisha kwa ajili ya mikutano. Kielelezo chao ni uvutano wenye nguvu. (Luka 6:40) Kupanga kwa uangalifu kwa ajili ya funzo la familia kwaweza pia kuwa jambo muhimu.

      Kuimarisha Moyo

      3. Kwa nini jitihada ya pekee yapasa kufanywa wakati wa funzo la familia ili kuimarisha mioyo, na hilo lahitaji nini?

      3 Funzo la familia halipaswi kuwa wakati wa kujaza ujuzi akilini tu, bali lapaswa kuwa wakati wa kuimarisha mioyo. Hilo lahitaji kufahamu matatizo yanayokabili washiriki wa familia na pia kuhangaikia kwa upendo kila mmoja wao. Yehova “ni mchunguzi wa moyo.”—1 Mambo ya Nyakati 29:17, NW.

      4. (a) Inamaanisha nini ‘kupungukiwa na akili’? (b) Ni nini kinachohusika katika ‘kupata hekima’?

      4 Yehova huona nini anapochunguza mioyo ya watoto wetu? Wengi wao wangesema kwamba wanampenda Mungu, na jambo hilo lastahili pongezi. Hata hivyo, mtu mchanga au aliyeanza kujifunza karibuni juu ya Yehova, hana uzoefu mwingi kuhusu njia za Yehova. Kwa kuwa hana uzoefu, huenda akawa ‘amepungukiwa na akili,’ kama vile Biblia isemavyo. Labda si nia zake zote zilizo mbaya, lakini itachukua muda kuweka moyo wake katika hali itakayompendeza Mungu kikweli. Hilo latia ndani kupatanisha mawazo, tamaa, shauku, hisia, na miradi ya mtu maishani, na yale Mungu hukubali, kwa kadiri iwezekanavyo kwa wanadamu wasiokamilika. Mtu ‘anapata hekima’ anaporekebisha yule mtu wa ndani kwa njia ya kimungu.—Mithali 9:4; 19:8.

      5, 6. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao ‘wapate akili’?

      5 Je, wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao ‘wapate hekima’? Ni kweli kwamba hakuna binadamu awezaye kuweka hali nzuri ya moyoni ndani ya mtu mwingine. Kila mmoja wetu amepewa hiari, na mengi hutegemea yale ambayo sisi hujiruhusu tufikirie. Hata hivyo, kwa busara, wazazi wanaweza kufanya mtoto wao ajieleze na kujua yaliyo moyoni mwake, na msaada anaohitaji. Tumia maswali kama ‘Unahisije kuhusu hili?’ na ‘Nawe ungependa kufanya nini hasa?’ Kisha, usikilize kwa subira. Usitende kwa kupita kiasi. (Mithali 20:5) Hali yenye fadhili, uelewevu, na upendo ni muhimu ikiwa unataka kuufikia moyo.

      6 Ili kuimarisha mielekeo ijengayo, zungumzia mara nyingi matunda ya roho—kila sehemu yake—na kujitahidi mkiwa familia kuyasitawisha. (Wagalatia 5:22, 23) Imarisha upendo kwa Yehova na kwa Yesu Kristo, si kwa kusema tu kwamba twapaswa kuwapenda lakini kwa kuzungumzia sababu zinazofanya tuwapende na jinsi tunavyoweza kuonyesha upendo huo. (2 Wakorintho 5:14, 15) Imarisha tamaa ya kufanya yanayofaa kwa kusababu juu ya manufaa zitakazotokana na kufanya hivyo. Imarisha tamaa ya kuepuka kabisa mawazo mabaya, usemi, na mwenendo kwa kuzungumzia matokeo mabaya ya kufanya hivyo. (Amosi 5:15; 3 Yohana 11) Onyesha jinsi mawazo, usemi, na mwenendo—uwe mzuri au mbaya—uwezavyo kuathiri uhusiano wa mtu na Yehova.

      7. Ni nini kiwezacho kufanywa ili kuwasaidia watoto watatue matatizo na kufanya maamuzi katika njia itakayowaweka karibu na Yehova?

      7 Mtoto anapokuwa na tatizo au anapohitaji kufanya uamuzi muhimu, tungeweza kumwuliza hivi: ‘Wewe unafikiri Yehova anaonaje jambo hili? Ni nini ambalo unajua kumhusu Yehova linalokufanya useme hivyo? Je, umesali kwake kuhusu hilo?’ Kwa kuanza mapema iwezekanavyo, saidia watoto wako wasitawishe namna ya maisha ambayo jitihada nyingi hufanywa sikuzote ili kuhakikisha mapenzi ya Mungu ni nini, kisha kuyafanya. Wanapopata kuwa na uhusiano wa karibu na wa kibinafsi na Yehova, watafurahia kutembea katika njia zake. (Zaburi 119:34, 35) Jambo hilo litaimarisha ndani yao uthamini wa pendeleo la kushirikiana na kutaniko la Mungu wa kweli.

      Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano ya Kutaniko

      8. (a) Ni nini kiwezacho kutusaidia tutie ndani ya funzo letu la familia mambo yote yanayohitaji uangalifu? (b) Funzo hili ni muhimu jinsi gani?

      8 Kuna mambo mengi yanayohitaji uangalifu wakati wa funzo la familia. Unaweza kuyashughulikiaje yote? Haiwezekani kufanya mambo yote wakati uleule. Lakini huenda ukaona kwamba kuandika orodha kunasaidia. (Mithali 21:5) Mara kwa mara, pitia orodha hiyo na uchunguze kile kinachohitaji uangalifu wa pekee. Pendezwa kipekee na maendeleo ya kila mshiriki wa familia. Mpango huo wa funzo la familia ni sehemu muhimu ya elimu ya Kikristo, inayotuandaa kwa maisha ya sasa na kututayarisha kwa uhai udumuo milele utakaokuja.—1 Timotheo 4:8.

      9. Ni miradi gani kuhusiana na kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ambayo huenda tukashughulikia hatua kwa hatua wakati wa mafunzo yetu ya familia?

      9 Je, funzo la familia yako latia ndani kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya kutaniko? Kuna mambo kadhaa mnayoweza kushughulikia hatua kwa hatua mnapojifunza pamoja. Baadhi ya mambo hayo yaweza kuchukua muda wa majuma kadhaa, miezi kadhaa, au hata miaka kadhaa ili kuyatimiza. Fikiria miradi hii: (1) kila mmoja katika familia kuwa tayari kutoa maelezo kwenye mikutano ya kutaniko; (2) kila mmoja kujitahidi kutoa maelezo katika maneno yake mwenyewe; (3) kutia ndani maandiko katika maelezo; na (4) kuchanganua habari kwa lengo la kuitumia kibinafsi. Mambo hayo yote yanaweza kusaidia mtu aitumie kweli katika maisha yake mwenyewe.—Zaburi 25:4, 5.

      10. (a) Twaweza kutoaje uangalifu kwa kila mkutano wa kutaniko? (b) Kwa nini hilo lafaa?

      10 Hata ikiwa funzo lenu la familia kwa kawaida hutegemea somo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, usipuuze umuhimu wa kujitayarisha kibinafsi au mkiwa familia kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na Mkutano wa Utumishi. Hizo pia ni sehemu muhimu za programu ya kutufundisha kutembea katika njia ya Yehova. Huenda mara kwa mara mkaweza kujitayarisha kwa ajili ya mikutano yote mkiwa kikundi cha familia. Kwa kujifunza pamoja, ustadi wenu wa kujifunza utaboreka. Tokeo likiwa kwamba manufaa nyingi zaidi zitapatikana kutokana na mikutano yenyewe. Kati ya mambo mengine, zungumzieni manufaa za kujitayarisha kwa ukawaida kwa ajili ya mikutano hiyo na umuhimu wa kuwa na wakati hususa uliotengwa kwa ajili ya kufanya hivyo.—Waefeso 5:15-17.

      11, 12. Kutayarisha kwa ajili ya kuimba katika mikutano kwaweza kutunufaishaje, na jambo hilo laweza kufanywaje?

      11 Kwenye Mikusanyiko ya “Njia ya Mungu ya Maisha,” tulitiwa moyo tujitayarishe kwa ajili ya sehemu nyingine ya mikutano—kuimba. Je, umefanya hivyo? Kufanya hivyo kwaweza kukazia kweli za Biblia katika akili na mioyo yetu na wakati huohuo kufanya tufurahie zaidi mikutano ya kutaniko.

      12 Kujitayarisha ambako hutia ndani kusoma na kuzungumzia maana ya maneno katika nyimbo zilizoratibiwa kwaweza kutusaidia kuimba kutoka moyoni. Katika Israeli la kale, ala za muziki zilitumiwa sana katika ibada. (1 Mambo ya Nyakati 25:1; Zaburi 28:7) Je, kuna mmoja katika familia yenu ambaye hupiga ala fulani ya muziki? Kwa nini msitumie ala hiyo kujizoeza wimbo mmoja kati ya nyimbo zitakazoimbwa juma hilo, kisha mwimbe mkiwa familia. Mnaweza pia kutumia kaseti za nyimbo hizo. Katika nchi fulani ndugu zetu huimba vizuri bila ala za muziki. Wanapotembea barabarani au wanapohubiri shambani, mara nyingi hufurahia kuimba nyimbo ambazo zimeratibiwa kuimbwa kwenye mikutano ya kutaniko juma hilo.—Waefeso 5:19.

      Kujitayarisha kwa Ajili ya Utumishi wa Shambani Mkiwa Familia

      13, 14. Kwa nini mazungumzo yanayotayarisha mioyo yetu kwa ajili ya huduma ya shambani ni yenye thamani?

      13 Kutolea wengine ushahidi juu ya Yehova na kusudi lake ni sehemu muhimu ya maisha yetu. (Isaya 43:10-12; Mathayo 24:14) Tuwe vijana au wazee, tunafurahia kazi hii zaidi nasi hupata matokeo zaidi ikiwa tumejitayarisha. Tunaweza kufanyaje hivyo katika familia?

      14 Ni muhimu kutayarisha mioyo yetu, sawa na vile ilivyo na mambo yote yanayohusu ibada yetu. Twahitaji kuzungumzia kile tutakachofanya na pia sababu ya kukifanya. Katika siku za mfalme Yehoshafati, watu walifundishwa sheria ya Mungu, lakini Biblia hutuambia kwamba “hawakuwa wametayarisha mioyo yao.” Jambo hilo lilifanya iwe rahisi kwao kushawishiwa na mambo ambayo yangeweza kuwaondoa katika ibada ya kweli. (2 Mambo ya Nyakati 20:33; 21:11, NW) Mradi wetu si kuweza kuripoti tu saa nyingi tunazotumia katika utumishi wa shambani, wala si kuangusha tu fasihi. Huduma yetu yapaswa kuwa wonyesho wa upendo wetu kwa Yehova na kwa watu wanaohitaji fursa ya kuchagua uhai. (Waebrania 13:15) Ni utendaji ambao sisi ni “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Wakorintho 3:9) Ni pendeleo lililoje! Tunaposhiriki katika huduma, sisi hufanya hivyo kwa kushirikiana na malaika watakatifu. (Ufunuo 14:6, 7) Wakati wa mazungumzo ya familia ndio ufaao zaidi kuimarisha uthamini kwa kazi hiyo, iwe ni kwenye funzo letu la kila juma au iwe ni tunapozungumzia andiko kutoka katika Kuyachunguza Maandiko Kila Siku, linalohusiana na kazi hiyo!

      15. Ni wakati gani tunaweza kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani tukiwa familia?

      15 Je, wewe mara kwa mara hutumia wakati wa funzo la familia ili kusaidia washiriki wa jamaa yako wajitayarishe kwa ajili ya utumishi wa shambani? Kufanya hivyo kwaweza kuwa na manufaa makubwa. (2 Timotheo 2:15) Kwaweza kusaidia kufanya utumishi wao uwe wenye maana na wenye matokeo. Mara kwa mara, huenda ukatenga kipindi chote cha funzo kwa ajili ya kujitayarisha huko. Huenda ukashughulikia mara nyingi zaidi sehemu za huduma ya shambani katika mazungumzo mafupi-mafupi mwishoni mwa kila funzo la familia au wakati mwingineo katika juma.

      16. Zungumzia thamani ya kila hatua iliyoorodheshwa kwenye fungu hili.

      16 Huenda vipindi vya funzo la familia vikakazia mfululizo wa hatua, kama hizi zifuatazo: (1) Kutayarisha wonyesho uliofanyiwa mazoezi vizuri kutia ndani andiko linalosomwa kutoka katika Biblia ikiwa fursa yapatikana. (2) Kuhakikisha kwamba, ikiwezekana kila mmoja ana mfuko wake mwenyewe wa utumishi wa shambani, Biblia, daftari, kalamu, trakti, na fasihi nyinginezo katika hali nzuri. Si lazima mfuko wa utumishi uwe ghali bali ni lazima uwe nadhifu. (3) Kuzungumzia mahali na jinsi ya kutoa ushahidi wa vivi hivi. Fuatilia kila mojawapo ya hatua hizi za maagizo kwa pindi ambazo mnahubiri pamoja katika utumishi wa shambani. Toa madokezo yenye kusaidia, lakini usishauri juu ya mambo mengi kupita kiasi.

      17, 18. (a) Ni kujitayarisha kwa aina gani tukiwa familia kuwezako kufanya huduma yetu ya shambani iwe na matokeo zaidi? (b) Ni sehemu gani ya kujitayarisha huko iwezayo kufanywa kila juma?

      17 Kufanya wanafunzi ndiyo sehemu kubwa ya kazi ambayo Yesu Kristo aliwapa wafuasi wake. (Mathayo 28:19, 20) Kufanya wanafunzi huhusisha mengi zaidi ya kuhubiri. Kufundisha kwahitajiwa. Funzo la familia yako laweza kukusaidiaje uwe na matokeo katika kufanya hivyo?

      18 Mkiwa familia, zungumzieni watu ambao ingefaa mfanye ziara za kuwarudia. Huenda baadhi yao wakawa wamekubali fasihi; huenda wengine wakawa walisikiliza tu. Huenda ikawa mlikutana nao mlipokuwa mkihubiri nyumba hadi nyumba au mkitoa ushahidi wa kivivi hivi sokoni au shuleni. Acheni Neno la Mungu liwaongoze. (Zaburi 25:9; Ezekieli 9:4) Amueni ni nani kila mmoja wenu anataka kumrudia juma hilo. Ni nini kitakachozungumziwa? Mazungumzo ya familia yanaweza kusaidia kila mshiriki ajitayarishe. Andikeni maandiko hususa mtakayotumia pamoja na wenye kupendezwa na vilevile mambo yafaayo kutoka katika broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? au kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Usijaribu kuzungumzia mambo mengi mno kwenye ziara moja ya kurudia. Mwachie mwenye nyumba swali ambalo litajibiwa katika ziara itakayofuata. Kwa nini msifanye iwe sehemu ya kawaida ya familia ya kila juma ya kupanga ni ziara zipi za kurudia ambazo kila mmoja atafanya, wakati atakapozifanya, na kile atarajiacho kutimiza. Kufanya hivyo kwaweza kusaidia huduma ya shambani ya familia nzima iwe na matokeo zaidi.

      Endelea Kuwafundisha Njia ya Yehova

      19. Ikiwa washiriki wa familia wataendelea kutembea katika njia ya Yehova, ni lazima wapatwe na nini, na ni nini huchangia jambo hilo?

      19 Kuwa kichwa cha familia katika ulimwengu huu mwovu ni jambo gumu. Shetani na roho waovu wake hujitahidi sana kuharibu hali ya kiroho ya watumishi wa Yehova. (1 Petro 5:8) Isitoshe, leo nyinyi wazazi mna mkazo mwingi, hasa nyinyi wazazi msio na wenzi. Ni vigumu kupata wakati wa kufanya mambo yote ambayo mngependa kufanya. Lakini jitihada hiyo inafaa, hata ikiwa mnaweza kutumia dokezo moja kwa wakati mmoja, na kuboresha hatua kwa hatua programu yenu ya funzo la familia. Ni thawabu inayochangamsha kuona wale walio karibu zaidi nawe wakitembea katika njia ya Yehova. Ili kutembea kwa mafanikio katika njia ya Yehova, washiriki wa familia wanahitaji kufurahia kuwa kwenye mikutano ya kutaniko na kufurahia kushiriki katika huduma ya shambani. Ili jambo hilo litimizwe, kujitayarisha kwahitajiwa—kujitayarisha kunakoimarisha moyo na kuandaa kila mmoja wetu kushiriki kwa njia yenye maana.

      20. Ni nini kiwezacho kuwasaidia wazazi zaidi wawe na aina ya furaha inayoonyeshwa kwenye 3 Yohana 4?

      20 Mtume Yohana aliandika hivi kuhusu wale aliosaidia kiroho: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Mafunzo ya familia yanayofanywa kukiwa na malengo hususa akilini na vichwa vya familia wanaoshughulika na mahitaji ya kila mshiriki wa familia kwa njia ya fadhili na yenye kusaidia, waweza kufanya mengi kuwezesha familia ishiriki furaha hiyo. Kwa kusitawisha uthamini kwa njia ya Mungu ya maisha, wazazi wanasaidia familia ifurahie njia iliyo bora kabisa ya maisha.—Zaburi 19:7-11.

      Je, Waweza Kueleza?

      ◻ Kwa nini kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ni muhimu kwa watoto wetu?

      ◻ Wazazi waweza kuwasaidiaje watoto wao ‘wapate akili’?

      ◻ Funzo la familia laweza kusaidiaje katika kujitayarisha kwa ajili ya mikutano?

      ◻ Kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani tukiwa familia kwaweza kutusaidiaje tuwe wenye matokeo zaidi?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki