Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mungu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Je, hilo linapatana na akili? Akili zetu haziwezi kulifahamu kikamili. Lakini hiyo si sababu halali ya kulikataa. Fikiria mifano: (1) Wakati. Hakuna mtu anayeweza kusema wakati ulianza lini. Na ni kweli kwamba, hata ingawa maisha yetu hukoma, wakati haukomi. Sisi hatulikatai wazo la wakati kwa sababu kuna mambo fulani kuuhusu ambayo hatufahamu kikamili. Badala yake, sisi tunautegemea maishani mwetu. (2) Anga. Wataalamu wa nyota hawaoni mwanzo na mwisho wa anga. Kadiri wanavyoendelea kuuchunguza ulimwengu, ndivyo wanavyoona hauna mwisho. Hawapingi uthibitisho huo; wengi husema anga haina mwisho. Kanuni hiyohiyo inaweza kutumiwa kuhusu kuwako kwa Mungu.

      Mifano mingine: (1) Wataalamu wa nyota hutuambia kwamba joto la jua katika kiini chake ni digrii 15,000,000 Selsiasi. Je, tunapinga wazo hilo kwa sababu hatuwezi kufahamu kikamili joto jingi namna hiyo? (2) Wanatuambia kwamba galaksi yetu ya Kilimia ni kubwa sana hivi kwamba nuru inayosafiri mwendo wa zaidi ya kilometa 300,000 kwa sekunde moja ingechukua miaka 100,000 kuivuka. Je, akili zetu kweli zinaufahamu umbali huo? Hata hivyo tunakubali jambo hilo kwa sababu uthibitisho wa sayansi unaliunga mkono.

      Ni jambo gani linalopatana na akili zaidi—kwamba ulimwengu uliumbwa na Muumba aliye hai, mwenye akili? au kwamba ulitokea wenyewe tu kutokana na chanzo kisicho hai bila mwelekezo wenye akili? Watu fulani wanakubali maoni hayo ya mwisho kwa sababu kukubali vingine kungemaanisha kwamba wangelazimika kukubali kwamba kuna Muumba ambaye sifa zake hawawezi kuzifahamu kikamili. Lakini inajulikana sana kwamba wanasayansi hawafahamu kikamili utendaji wa chembe za urithi zilizo katika chembe hai na zinazoamua jinsi chembe hizo zitakavyokua. Wala hawajaelewa kikamili jinsi ubongo wa mwanadamu unavyofanya kazi. Hata hivyo, ni nani anayeweza kusema kwamba vitu hivyo haviko? Je, kwa kweli tutarajie kuelewa kila jambo kumhusu Mtu aliye mkuu sana hata akaweza kutokeza ulimwengu mzima, pamoja na ubuni wake wote ulio tata na wenye ukubwa wa kustaajabisha mno?

      Je, ni muhimu kulitumia jina la Mungu?

      Rom. 10:13: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”

      Eze. 39:6: “Watu watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”

      Yesu alimwambia Baba yake hivi: “Nimewajulisha [wafuasi wake wa kweli] jina lako nami nitalijulisha.”—Yoh. 17:26.

      Ona pia ukurasa wa 425, 426, chini ya “Yehova.”

      Maadamu tuna dini fulani, je, Mungu tunayemtumikia ni muhimu?

      1 Kor. 10:20: “Vitu ambavyo mataifa huvitoa dhabihu wao huvitoa dhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu.”

      2 Kor. 4:4: “Mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini, ili nuru ya habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, aliye mfano wa Mungu, isipenyeze mwangaza.” (Hapa Ibilisi anaitwa “mungu.” Ona 1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9.)

      Mt. 7:22, 23: “Wengi wataniambia [Yesu Kristo] siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mtu kudai kuwa Mkristo si uhakikisho wa kwamba anamtumikia Mungu wa kweli kwa njia inayokubalika.)

      Ona pia ukurasa wa 59, 60, chini ya kichwa “Dini.”

      Ikiwa Yehova ndiye “Mungu wa pekee wa kweli,” Yesu ni “Mungu” wa aina gani?

      Yesu mwenyewe alimwita Baba yake “Mungu wa pekee wa kweli.” (Yoh. 17:3) Yehova mwenyewe alisema: “Zaidi yangu hakuna Mungu.” (Isa. 44:7) Mtume Paulo aliandika kwamba, kwa Wakristo wa kweli, “kuna Mungu mmoja aliye Baba.” (1 Kor 8:5, 6) Kwa hiyo Yehova ni wa pekee; hakuna mwingine aliye na cheo kama chake. Yehova ni tofauti kabisa na vitu vyote ambavyo huabudiwa kama vile sanamu, wanadamu waliofanywa kuwa miungu, na Shetani. Wote hao ni miungu ya uwongo.

      Katika Maandiko Yesu anaitwa “mungu,” hata “Mungu Mwenye Nguvu.” (Yoh. 1:1; Isa. 9:6) Lakini haitwi popote kuwa Mweza-Yote, kama Yehova alivyo. (Mwa. 17:1) Yesu anasemwa kuwa ni “mng’ao wa utukufu wake [Mungu],” lakini Baba ndiye Chanzo cha utukufu huo. (Ebr. 1:3) Yesu hatafuti kwa vyovyote cheo cha Baba yake. Yeye alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Yeye yuko “katika umbo la Mungu,” na Baba ameamuru kwamba “katika jina la Yesu kila goti lipigwe,” lakini yote hayo yanafanywa “kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Flp. 2:5-11; ona pia ukurasa wa 430-434.

      Mtu Akisema—

      ‘Mimi siamini Mungu’

      Unaweza kujibu hivi: ‘Je, umekuwa na maoni hayo sikuzote? . . . Kabla ya kufikia uamuzi huo, je, ulichunguza uthibitisho fulani ambao ulikusadikisha?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Jambo hilo linanipendeza sana nami nimelifikiria sana. Haya ndiyo mambo yaliyonisaidia: . . . (Katika ukurasa wa 215, ona kichwa kidogo “Je, kuna sababu nzuri za kuamini kwamba kuna Mungu?” Pia ona ukurasa wa 390-392, chini ya “Uumbaji.”)’

      Au unaweza kusema: ‘Je, unamaanisha kwamba huamini kuna Muumba, au umeona unafiki mwingi katika makanisa hivi kwamba huamini yale wanayofundisha?’ Ikiwa ni kwa sababu ya unafiki, unaweza kuongezea: ‘Kuna tofauti kubwa kati ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo na Ukristo wa kweli. Ni kweli kwamba Jumuiya ya Wakristo imewakandamiza watu, lakini Ukristo haujawakandamiza watu. Jumuiya ya Wakristo imepigana vita, lakini Ukristo haujafanya hivyo. Jumuiya ya Wakristo imeshindwa kutoa mwongozo mzuri wa maadili, lakini Ukristo haujashindwa. Neno la Mungu, Biblia, haliungi mkono Jumuiya ya Wakristo. Kinyume chake, linailaumu Jumuiya ya Wakristo.’

      Pia unaweza kusema: ‘Nimekuwa na mazungumzo mazuri pamoja na wengine wenye maoni kama yako. Baadhi yao walisema kwamba hawawezi kuelewa kwa nini kuna Mungu na bado kuna kuteseka na uovu mwingi ulimwenguni. Je, hayo ndiyo maoni yako? (Ikiwa ndivyo, tumia habari katika ukurasa wa 216, 217, chini ya kichwa kidogo “Je, kuwako kwa uovu na kuteseka kunathibitisha kwamba hakuna Mungu?”)’

      ‘Mimi naamini tu kitu ninachoweza kuona, nami sijamwona Mungu kamwe’

      Unaweza kujibu hivi: ‘Siku hizi watu wengi huamini hivyo. Na kuna sababu ya maoni hayo. Tunaishi katika jamii inayofuatilia mali za kimwili. Lakini wewe ni mtu anayependa uhakika, sivyo.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Je, kuna vitu fulani ambavyo hatuwezi kuona kwa macho yetu lakini tunaamini kwamba viko kwa kuwa tuna sababu nzuri za kuamini hivyo? Namna gani hewa tunayopumua? Huenda tukaihisi kunapokuwa na upepo. Tunaweza kujua inapojaa katika mapafu yetu, hata ingawa hatuioni. Kwa sababu tunaona matokeo, kuna sababu nzuri ya kuamini kwamba ipo, sivyo?’ (2) ‘Na hatuwezi kuziona nguvu za uvutano. Lakini tunapoangusha kitu fulani tunaona uthibitisho kwamba nguvu za uvutano zinatenda kazi. Wala hatuoni harufu, lakini pua yetu inainusa. Hatuwezi kuona mawimbi ya sauti, lakini masikio yetu yanayasikia. Kwa hiyo tunaamini vitu tusivyoweza kuona—maadamu kuna sababu nzuri ya kufanya hivyo, sivyo?’ (3) ‘Je, kweli kuna uthibitisho kwamba Mungu asiyeonekana yuko? (Tumia habari iliyo katika ukurasa wa 215, 216, chini ya kichwa kidogo “Je, kuna sababu nzuri za kuamini kwamba kuna Mungu?”)’

      ‘Mimi nina maoni yangu mwenyewe kumhusu Mungu’

      Unaweza kujibu hivi: ‘Ninafurahi kusikia kwamba umelifikiria jambo hilo na kwamba unamwamini Mungu. Hebu nikuulize, Una maoni gani kumhusu Mungu?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Nina hakika unatambua kuwa ni muhimu kuhakikisha kwamba lolote tunaloamini linapatana na yale ambayo Mungu mwenyewe anasema. Je, nikuonyeshe wazo moja tu katika Biblia kuhusu jambo hilo? (Zab. 83:18)’

  • Nafsi
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Nafsi

      Maana: Katika Biblia, neno “nafsi” hutafsiriwa kutoka neno la Kiebrania neʹphesh na neno la Kigiriki psy·kheʹ. Matumizi ya Biblia huonyesha nafsi ni mtu au mnyama au uhai wa mtu au mnyama. Hata hivyo, kwa watu wengi, “nafsi” humaanisha sehemu isiyo na mwili au roho ya mwanadamu inayoendelea kuishi baada ya kufa kwa mwili. Wengine wanaielewa kuwa ndiyo msingi wa uhai. Lakini maoni hayo ya mwisho si mafundisho ya Biblia.

      Biblia inasema nini linalotusaidia kuelewa maana ya nafsi?

      Mwa. 2:7: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” (Ona kwamba andiko hilo halisemi kwamba mtu alipewa nafsi bali kwamba yeye akawa nafsi, mtu aliye hai.) (Sehemu ya neno la Kiebrania linalotafsiriwa hapa “nafsi” ni neʹphesh. UV na ZSB zinakubaliana na tafsiri hiyo. BHN na VB husema “kiumbe.”)

      1 Kor. 15:45: “Hata imeandikwa hivi: ‘Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi hai.’ Adamu wa mwisho akawa roho inayotoa uhai.” (Kwa hiyo Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanakubaliana na Maandiko ya Kiebrania kuhusu maana ya nafsi.) (Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “nafsi” ni psy·kheʹ. UV na ZSB pia husema “nafsi.” BHN, VB, na NAJ husema “kiumbe.”)

      1 Pet. 3:20: “Katika siku za Noa . . . watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “nafsi” ni psy·khaiʹ, ambalo ni wingi wa neno psy·kheʹ. UV, ZSB, BHN, na NAJ husema “watu.”)

      Mwa. 9:5: “Tena, damu ya nafsi [au, uhai; Kiebrania, kutokana na neʹphesh] zenu nitaitaka.” (Hapa nafsi inasemwa kuwa ina damu.)

      Yos. 11:11: “Wakaipiga kila nafsi [Kiebrania, neʹphesh] iliyokuwa ndani yake kwa makali ya upanga.” (Hapa nafsi inaonyeshwa kuwa kitu kinachoweza kupigwa kwa upanga, kwa hiyo nafsi hizo haziwezi kuwa roho.)

      Ni wapi ambapo Biblia inasema kwamba wanyama ni nafsi?

      Mwa. 1:20, 21, 24, 25: “Mungu akaendelea kusema: ‘Maji na yajawe na nafsi* hai . . . ’ Mungu akaanza kuumba wanyama wakubwa mno wa baharini na kila nafsi hai inayotembea, wakajaa majini kulingana na aina zake, na kila kiumbe kinachoruka chenye mabawa kulingana na aina yake. . . . Mungu akaendelea kusema: ‘Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake . . . ’ Mungu akafanya mnyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake na mnyama wa kufugwa kulingana na aina yake na kila mnyama anayetembea wa nchi kulingana na aina yake.” (*Katika Kiebrania neno hili ni neʹphesh. Tafsiri fulani zinatumia neno “kiumbe [viumbe].”)

      Law. 24:17, 18: “Ikiwa mtu ataipiga nafsi [Kiebrania, neʹphesh] yoyote ya mwanadamu kiasi cha kuiua, lazima atauawa. Naye mwenye kuipiga nafsi [Kiebrania, neʹphesh] ya mnyama wa kufugwa kiasi cha kuiua atalipa, nafsi kwa nafsi.” (Ona kwamba neno lilelile la Kiebrania kwa nafsi linatumiwa kuhusu wanadamu na wanyama pia.)

      Ufu. 16:3: “Nayo ikawa damu kama ya mwanadamu aliyekufa, na kila nafsi* iliyo hai ikafa, ndiyo, vitu vilivyo ndani ya bahari.” (Kwa hiyo, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia yanaonyesha wanyama ni nafsi.) (*Katika Kigiriki neno hili ni psy·kheʹ. Watafsiri fulani wanatumia neno “kiumbe” au “kitu.”)

      Je, wasomi wengine ambao si Mashahidi wa Yehova wanakubali kwamba Biblia inasema kwamba hiyo ndiyo maana ya nafsi?

      “Hakuna mgawanyo kati ya mwili na nafsi katika A[gano] la K[ale]. Mwisraeli aliona vitu kwa uhalisi, vikiwa jumla, na hivyo aliwaona wanadamu kuwa ni watu, wala si sehemu-sehemu. Neno hili nepeš [neʹphesh], ingawa linatafsiriwa na neno letu nafsi, halimaanishi kamwe nafsi iliyo tofauti na mwili au mtu mwenyewe. . . . Neno [psy·kheʹ] ndilo neno la A[gano] J[ipya] linalolingana na nepeš. Linaweza kumaanisha msingi wa uhai, uhai wenyewe, au yule aliye hai.”—New Catholic Encyclopedia (1967), Buku la 13, uku. 449, 450.

      “Neno la Kiebrania ‘nafsi’ (nefesh, kile kinachopumua) lilitumiwa na Musa . . . , kumaanisha ‘kitu kilicho hai’ na linahusu vivyo hivyo viumbe ambavyo si wanadamu. . . . Matumizi ya Agano Jipya ya psychē (‘nafsi’) yalilingana na nefesh.”—The New Encyclopædia Britannica (1976), Macropædia, Buku la 15, uku. 152.

      “Lile wazo kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya kufa kwa mwili si imani, bali ni makisio ya kifalsafa au ya kitheolojia, nalo halifundishwi waziwazi mahali popote katika Maandiko Matakatifu.”—The Jewish Encyclopedia (1910), Buku la 6, uku. 564.

      Je, nafsi ya mwanadamu inaweza kufa?

      Eze. 18:4: “Tazama! Nafsi zote—ni zangu. Kama ilivyo nafsi ya baba ndivyo ilivyo nafsi ya mwana—ni zangu. Nafsi* inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (*Neno la Kiebrania ni “neʹphesh.” ZSB hulitafsiri “nafsi.” Tafsiri fulani zinasema “roho,” “yeyote,” au “yule.”)

      Mt. 10:28: “Msiwaogope wale ambao wanaua mwili lakini hawawezi kuiua nafsi [au, “uhai”]; lakini badala ya hivyo mwogopeni yeye anayeweza kuangamiza vyote viwili nafsi* na mwili katika Gehena.” (*Neno la Kigiriki hapa ni psy·kheʹ. ZSB hulitafsiri “nafsi.”)

      Mdo. 3:23: “Kwa kweli, nafsi [Kigiriki, psy·kheʹ] yoyote isiyomsikiliza Nabii huyo itaangamizwa kutoka kati ya watu.”

      Je, nafsi za wanadamu (watu) zinaweza kuishi milele?

      Ona ukurasa wa 327-331, chini ya kichwa “Uhai.”

      Je, nafsi ni sawa na roho?

      Mhu. 12:7: “Kisha mavumbi huirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho [au, nguvu za uhai; Kiebrania, ruʹach] yenyewe humrudia Mungu wa kweli aliyeitoa.” (Ona kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa roho ni ruʹach; lakini neno linalotafsiriwa nafsi ni neʹphesh. Andiko hilo halimaanishi kwamba wakati wa kifo roho inasafiri moja kwa moja na kwenda katika makao ya Mungu; badala yake, tazamio lolote la mtu huyo kuishi tena linakaa kwa Mungu. Kwa mfano, tunaweza kusema kwamba, ikiwa mnunuzi wa shamba hafanyi malipo yanayohitajiwa, shamba hilo “humrudia” mwenyewe.) (UV, ZSB, BHN, na VB zote hapa zinatafsiri ruʹach kuwa “roho.”)

      Mhu. 3:19: “Kuna mwisho ambao huwafikia wana wa binadamu na mwisho ambao huwafikia wanyama, nao hufikiwa na mwisho uleule. Anavyokufa mmoja, ndivyo anavyokufa yule mwingine; nao wote wana roho [Kiebrania, ruʹach] moja.” (Kwa hiyo wanadamu na wanyama pia wanaonyeshwa kuwa wana ruʹach au roho ileile. Ili kupata maelezo kuhusu mstari wa 20 na 21, ona ukurasa wa 245.)

      Ebr. 4:12: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi [Kigiriki, psy·khesʹ; ] na roho [Kigiriki, pneuʹma·tos], na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ona kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “roho” si sawa na neno linalotafsiriwa “nafsi.”)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki