-
Muumba Wako—Jifunze Jinsi AlivyoMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 15
-
-
ya Lazaro, Maria, akiomboleza? Yesu “akapiga kite katika roho na kuwa mwenye kutaabika.” Yeye alijali na hakujitenga; “akatokwa na machozi.” (Yohana 11:33-35) Na hilo halikuwa wonyesho tu wa hisia. Yesu alisukumwa kuchukua hatua nzuri—akamfufua Lazaro. Unaweza kuwazia jinsi jambo hilo lilivyowasaidia mitume wafahamu hisia na matendo ya Muumba. Linapasa kutusaidia na kusaidia wengine pia kuelewa utu wa Muumba na njia zake.
18. Watu wanapaswa kuhisije juu ya kujifunza Biblia?
18 Hakuna sababu ya kuaibika kusoma Biblia na kujifunza zaidi kuhusu Muumba wetu. Biblia si kitabu kisichotumika. Yohana aliisoma akawa mshiriki wa karibu wa Yesu. Baadaye aliandika: “Twajua kwamba Mwana wa Mungu amekuja, na yeye ametupa sisi uwezo wa akili ili tupate ujuzi juu ya aliye wa kweli. Na sisi tumo katika muungano na aliye wa kweli, kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli na uhai udumuo milele.” (1 Yohana 5:20) Ona kwamba kutumia “uwezo wa akili” ili kupata ujuzi wa “aliye wa kweli,” Muumba, kwaweza kutuongoza kwenye “uhai udumuo milele.”
Unaweza Kuwasaidiaje Wengine Wajifunze Kumhusu?
19. Ni hatua zipi ambazo zimechukuliwa ili kuwasaidia watu wenye kutilia shaka?
19 Watu wengine wanahitaji kujua mengi zaidi ndipo waamini kwamba kuna Muumba mwenye huruma anayetujali ndipo watambue jinsi alivyo. Kuna mamilioni ya watu ambao bado wanatilia shaka kuhusu Muumba au ambao maoni yao juu yake hayapatani na yale yanayopatikana katika Biblia. Unaweza kuwasaidiaje? Kwenye mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa katika kipindi cha 1998/1999, chombo kipya chenye kufaa kilitolewa katika lugha nyingi—kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?
20, 21. (a) Kitabu cha Muumba kinaweza kutumiwaje kwa mafanikio? (b) Simulia mambo yaliyoonwa ya jinsi ambavyo kitabu Muumba tayari kimethibitika kuwa chenye matokeo.
20 Hicho ni kichapo ambacho kitaimarisha imani yako mwenyewe juu ya Muumba wetu na uthamini wako juu ya utu wake na njia zake. Kwa nini hili ni jambo la hakika? Kwa sababu kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kimetayarishwa hasa kwa malengo hayo. Jambo kuu linalokaziwa katika kitabu hicho chote ni “Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi?” Habari hii imeandaliwa kwa njia ya kwamba hata watu wenye elimu nyingi sana watapata ikiwa yenye kuvutia. Lakini, habari hiyo inagusia tamaa ambazo sisi sote tunazo. Kuna habari zenye kuvutia na zenye kushawishi wasomaji wanaotilia shaka kuwapo kwa Muumba. Kitabu hicho hakichukulii kwamba msomaji anaamini kuna Muumba. Wenye kutilia shaka kuhusu kuwapo kwa Muumba watavutiwa na uvumbuzi na hoja za kisayansi za karibuni. Mambo hayo yataimarisha pia imani ya wale wanaoamini Mungu.
21 Unapojifunza kitabu hiki kipya, itaonekana kwamba sehemu zake zinatoa pitio la historia ya Biblia kwa njia inayokazia sehemu mbalimbali za utu wa Mungu, kikisaidia wasomaji wamjue Mungu vizuri zaidi. Wengi ambao tayari wamekisoma wameeleza jinsi ambavyo wameona ukweli wa jambo hilo. (Ona makala ifuatayo, ukurasa wa 25-26.) Na iwe hivyo kwako pia unapokisoma kitabu hicho na kukitumia kuwasaidia wengine kupata kumjua Muumba wao vizuri zaidi.
-
-
‘Tamaa Inayochochea Moyo na Akili’Mnara wa Mlinzi—1999 | Juni 15
-
-
‘Tamaa Inayochochea Moyo na Akili’
“Hata sina maneno ya kuelezea shangwe na msisimuko ninaozidi kupata ninapoendelea kufurahia kusoma kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? Kinakuza tamaa ndani ya mtu—naam, uhitaji—wa kujua mengi zaidi. Asanteni kwa kuwasha tamaa inayochochea moyo wangu na akili yangu.”
HIVYO ndivyo mmoja wa Mashahidi wa Yehova wa North Carolina, Marekani, alivyohisi kuhusu kitabu kilichotolewa na Watch Tower Society kwenye Mikusanyiko ya Wilaya ya “Njia ya Mungu ya Maisha” katika kipindi cha 1998/1999. Hata kama huna kitabu hicho, tafadhali ona jinsi wengine wanavyoeleza.
Siku kadhaa baada ya kupokea kitabu hicho kwenye mkusanyiko wa San Diego, California, Marekani, mtu mmoja aliandika: “Naona kitabu hiki ni chenye kuimarisha imani sana. Kinafanya nithamini sana kazi za uumbaji za Yehova. Nimefikia ukurasa wa 98, na naogopa nisifikie mwisho! Kinaridhisha jinsi hiyo.”
Mwanamke mmoja wa nchi za Mashariki aliandika: “Msemaji wa mkusanyiko alitumia maneno ‘kitabu cha kipekee,’ na maneno hayo kwa kweli yanafafanua yaliyomo. Sehemu yenye kutokeza ni kwamba kitabu hiki hakimsukumi msomaji aamini kuna Mungu, bali kinataja tu mambo ya hakika.”
Mambo ya hakika yanatia ndani uvumbuzi wa kisayansi wenye kuvutia kuhusu ulimwengu wetu, uhai, na sisi. Jambo hilo lilivutia wengi. “Hata nashindwa kueleza jinsi ambavyo kitabu hiki kimenigusa moyo sana,” mwanamke mmoja wa California akaandika. “Nilishindwa kuacha kukisoma kwa kuwa kila ukurasa ulifafanua uvumbuzi zaidi kuhusu ulimwengu wetu na maisha yenyewe. Nilijifunza mengi sana! Nitathamini kitabu hiki kidogo na kukionyesha watu wengi kadiri iwezekanavyo.”
Sehemu iliyowafurahisha wengi ni jinsi kitabu hiki kinavyotoa muhtasari wa Biblia, kikikazia utu wa Muumba. “Muhtasari wa Biblia, ambao umetolewa katika sehemu ya mwisho-mwisho ya kitabu hicho, ni mmojawapo wa mihtasari bora ambayo nimepata kusoma,” ndivyo wengi waelezavyo. Punde tu baada ya mkusanyiko mmoja uliofanywa mapema jijini New York, Marekani, mwanamke mwingine aliandika hivi: “Ni lazima kitabu hiki kipya kiwe kichapo chenye kunasa akili zaidi ambacho mmepata kuchapa. Nilifurahia sana uthibitisho wa kisayansi kwamba kuna Muumba. Muhtasari mfupi wenyewe wa Biblia watosha kuelezea mambo yanayotajwa na kuchochea mtu aendelee kusoma.”
Sayansi Inayoeleweka
Habari za kisayansi zilizo katika sura za mwanzo huenda zikaonekana kuwa ngumu sana, lakini yafuatayo ni maelezo ya wengi.
Mtu mmoja wa Kanada aliandika: “Ni tofauti kama nini na vitabu vya kiufundi ambavyo watungaji wake hujaribu kutuvutia kwa kutumia maneno makubwa-makubwa. Uandishi wenu ni wenye kutokeza kwa kufanya tuweze kuelewa kwa urahisi habari za fizikia, kemia, DNA, kromosomu, na kadhalika. Laiti mngaliandika vitabu vya mafundisho vinavyotumiwa kwenye vyuo vikuu ambavyo nilitumia miaka mingi iliyopita!”
Profesa wa fizikia wa chuo kikuu aliandika: “Kinaeleza masuala yanayohusika kwa njia ya wazi bila kuingilia mno mambo madogo-madogo ya kiufundi. Kitabu hiki kinasababu pamoja na msomaji na kunukuu wanasayansi wengi mashuhuri. Hiki ni kitabu ambacho ‘ni lazima kisomwe’ na mtu yeyote ambaye anapenda kujua chanzo cha ulimwengu na uhai, awe mwanasayansi au mtu wa kawaida.”
Mwanamke mmoja mchanga ambaye anafanya mtaala wa uuguzi alisema hivi: “Sikuamini nilipofungua sura ya 4 na kusoma nukuu ya kitabu ambacho tunatumia darasani! Nilimpa profesa wetu kitabu hicho nikamwambia kwamba najua angefurahia habari zake. Nikamwonyesha ukurasa wa 54 kuhusu ubongo. Alisoma kimoyomoyo kisha akasema, ‘Kinapendeza! Nitakisoma.’”
Mbunge mmoja nchini Ubelgiji aliandika hivi: “Kilichonivutia na kunipendeza ni maelezo ya kisayansi ambayo yanakazia kwamba sayansi ya kisasa haipingi dokezo la Biblia la kwamba kuna Mungu mmoja, bali zinakubaliana. Huo ni mtazamo muhimu sana.”
Kumjua Muumba Vizuri Zaidi
Kitabu hicho kilisaidia watu katika nchi nyingi kumjua Mungu vizuri zaidi na kufanya wahisi kuwa karibu zaidi naye. Msomaji mmoja katika Fukuoka City, nchini Japani, alisema: “Ni kana kwamba kwa mara ya kwanza Yehova alifafanuliwa vizuri zaidi. Kitabu hiki kinasadikisha sana. Nilipata kumjua Yehova kwa njia ambayo sikuwa nimewazia kamwe.” Mtu mmoja wa El Salvador aliandika: “Mnaeleza wazi jinsi Mungu alivyo mwenye huruma, asiye mwepesi wa hasira, na mwingi wa rehema. Kwa kweli, hayo ndiyo mambo tunayohitaji hasa ili tuweze kuwa karibu zaidi na yeye na Mwana wake. Ndicho kitabu cha kwanza kinachofafanua hisia za Yehova na hisia za kibinadamu za Mwana wake, Yesu.” Na msomaji mmoja nchini Zambia alisema: “Nilianza kumwona Yehova kwa njia tofauti kabisa.”
Basi inaeleweka kwamba Mashahidi wa Yehova wamesisimuka kuhusu kuwaonyesha wengine kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? Mwanamke mmoja alisema: “Nilipokuwa nikimaliza kusoma sura ya 10 [“Ikiwa Muumba Anajali, Mbona Wanadamu Wanateseka Sana?”], nilishtuka nimesema kwa sauti, ‘Hiki ndicho kitabu hasa tunachohitaji Japani!’ Ningependa nifahamu vizuri habari iliyo kwenye sura hii na kuitumia zaidi na zaidi katika huduma ya shambani.” Mwanamke mwingine anajifunza Biblia na msichana mmoja aliyelelewa kwenye hekalu ambako babake alikuwa kuhani. “Imekuwa vigumu sana kwake kukubali wazo la kwamba kuna Muumba. Kitabu hiki hakisisitizi mambo, lakini kina mambo ya hakika, basi nafikiri kwamba hata Wabudha wanaweza kukisoma bila kusita. Kinatufanya tuhisi hata zaidi upendo wa Yehova.”
Uchanganuzi ufuatao ulitoka Uingereza: “Nimetoka tu kumaliza kusoma kitabu cha Muumba na ninataka kuanza kukisoma tena. Ni kitabu kizuri kama nini! Mtu yuampenda tu Yehova akikisoma. Nimempa jirani yangu kitabu kimoja, ambaye baada ya kusoma sura mbili tu alisema: ‘Siwezi kuacha kukisoma, kinasisimua sana.’ Nina hakika kitawasaidia watu wapate kumjua Muumba wetu Mtukufu na kumpenda.”
Mtu mmoja wa Maryland, Marekani, alisema: “Kwa kweli kimechochea hali yangu ya kiroho! Napangia kuwapa watu wote ninaoshughulika nao kikazi kitabu hiki. Nyakati nyingine mimi huona ugumu wa kuanza kutolea ushahidi watu kama hao wenye shughuli nyingi na wenye elimu. Nikiwa na kitabu hiki sasa nitapata njia nzuri na yenye kuvutia ya kuwafikia watu.”
Kwa wazi, kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kitagusa mioyo ya watu duniani pote.
-