Kueneza Kweli ya Biblia Katika Ureno
TOKA Caminha upande wa kaskazini hadi Vila Real de Santo Antônio upande wa kusini, maelfu ya mashua maridadi ya uvuvi yametawanyika-tawanyika katika Pwani ya Atlantiki ya Ureno yenye urefu wa kilometa 800. Wavuvi ‘wameshuka baharini katika merikebu’ kwa karne nyingi, wakifanya samaki kuwa chakula kikuu cha Wareno wengi.—Zaburi 107:23.
Kwa miaka 70 ambayo imepita, aina nyingine ya uvuvi imekuwa ikiendelea katika Ureno. Mashahidi wa Yehova wamekuwa na shughuli ya kupeleka habari njema kwa makumi ya maelfu ya samaki wa ufananisho. (Mathayo 4:19) Katika Mei 1995 kulikuwa na kilele kipya cha wahubiri wa Ufalme 44,650—uwiano wa 1 kati ya wakazi wapatao 210. Katika majiji fulani uwiano ni 1 kati ya kila wakazi 105.
Kukiwa na wahubiri wengi hivyo, maeneo ya kutoa ushahidi katika sehemu nyingi hufanywa karibu kila juma. Kwa hiyo Mashahidi Wareno ni wenye makini sana katika kutumia mifikio mbalimbali ili kushiriki tumaini lao la Biblia na wengine. Ndiyo, wao huthamini umaana wa kujulisha kweli ya Biblia katika kila njia iwezekanayo.—1 Wakorintho 9:20-23.
Kuwasaidia Wale Wenye Mwelekeo wa Kidini
Kulingana na hesabu ya watu iliyofanywa 1991, asilimia 70 ya wale wenye umri wa miaka 18 au zaidi katika Ureno hudai kuwa Wakatoliki wa Kiroma. Japo hali hiyo, ujuzi wa Biblia ni kidogo sana miongoni mwa watu. Gazeti la habari Jornal de Notícias lilisema: “Huu ni mojawapo misiba mikubwa zaidi ya ulimwengu wa Katoliki: Kutojua Biblia!” Kwa nini iwe hivyo? Gazeti la habari la Ureno Expresso latoa jibu. Likiripoti juu ya mkutano wa makasisi 500 katika Fátima, gazeti hilo lilisema: “Kulingana na askofu mkuu, ni lazima kasisi ajiondolee utendaji mwingi mno wa ziada ili aweze kuimarisha tena cheo chake kabisa akiwa ‘mtangazaji.’ . . . Kasisi akitoa nafsi yake yote katika utangazaji wa Gospeli, hatapata wakati wa kufuatia utendaji mwingine mbalimbali.”
Tofauti na hivyo, Mashahidi wa Yehova katika Ureno ni wenye shughuli wakifanya kweli ya Biblia ijulikane kwa kila njia iwezekanayo. Matokeo ni kwamba Wakatoliki wengi wanyoofu wanapata ujuzi wa Biblia.
Carlota alikuwa Mkatoliki mwenye kujitoa sana na pia mshiriki wa kikundi cha vijana katika jamii ya kidini. Yeye pia alikuwa mwalimu katika shule ya nasari ambako Antônio, aliye Shahidi, alifanya kazi. Akiwa painia wa kawaida, au mhudumu wa wakati wote, sikuzote Antônio alijitahidi kuzungumza na wafanyakazi wenzake juu ya Biblia wakati wa mapumziko ya mchana. Siku moja Carlota alimwuliza kuhusu itikadi yake juu ya moto wa helo na ibada ya Mariamu. Antônio alimwonyesha yale Biblia hufundisha juu ya habari hizo, na huo ukawa mwanzo wa mazungumzo mengi ya Biblia. Carlota alipohudhuria mkutano kwa mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme, alivutiwa sana. Hata hivyo, saa za mikutano ziligongana na zile za ile jamii ya kidini aliyokuwa mshiriki wayo. Akang’amua kwamba ni lazima afanye uamuzi. Angefanya nini?
Carlota alikikusanya kile kikundi chote cha vijana na kueleza kutoka kwenye Biblia sababu inayofanya ajiuzulu. Wote walishutumu uamuzi wake, ila msichana mmoja mchanga aitwaye Stela, aliyesikiliza kwa makini. Carlota alipozungumza naye baadaye, Stela aliuliza maswali mengi juu ya chanzo na kusudi la uhai. Carlota akampa kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?a na kuanza kujifunza Biblia pamoja naye.
Wakati uo huo, Carlota alifanya maendeleo mazuri ya kiroho, akabatizwa Juni 1991, akaanza kutumikia akiwa painia wa kawaida miezi sita baadaye. Katika Mei 1992, alifunga ndoa pamoja na Antônio, wakiendelea pamoja katika utumishi wa painia katika kutaniko la jirani lenye uhitaji mkubwa zaidi. Na vipi Stela? Alibatizwa katika Mei 1993 naye sasa anatumikia akiwa painia wa kawaida.
Francisco mchanga alikuwa mtu wa kidini sana. Kila Jumapili alihudhuria Misa asubuhi na alasiri alirudia-rudia sala za Rozari. Alitumikia akiwa msimamizi wa vyombo vitakatifu, akimsaidia kasisi wakati wa Misa. Hata alisali kwa Mungu kwamba siku moja afanywe “mtakatifu”!
Francisco alitaka sana kuwa na Biblia, na siku moja rafiki yake alimwazima moja. Alishangaa kupata kwamba Mungu ana jina, Yehova. (Kutoka 6:3; Zaburi 83:18) Aliposoma kwenye Kutoka 20:4, 5 kwamba Mungu hukataza matumizi ya sanamu katika ibada, alishangaa hata zaidi! Akiona kwamba kanisa lilijaa sanamu, alisali kwa bidii kwa Mungu amsaidie kuelewa mvurugo huo. Siku kadhaa baadaye alikutana na mwanashule mwenzake wa zamani akamwuliza ni kwa nini aliacha kuhudhuria shule ya usiku.
“Mimi huhudhuria shule bora ya usiku sasa,” rafiki yake akajibu.
“Ni shule gani hiyo, nanyi hujifunza nini?” Francisco akauliza. Hakutarajia hata kidogo jibu la rafiki yake.
“Ninajifunza Biblia kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova,” rafiki huyo akamwambia. “Je, ungependa kuja”?
Francisco hakuamini yale aliyoyaona kwenye mkutano wake wa kwanza—nyuso zenye furaha na zenye kutabasamu; watu wakizungumziana kwa uchangamfu na kwa urafiki; watoto wakiketi pamoja na wazazi wao na kutoa uangalifu kwa yale yasemwayo.
“Nilikuwa mgeni kabisa, na nilihisi nikiwa sehemu ya hiyo familia!” Francisco akasema kwa mshangao. Amekuwa akihudhuria mikutano kwa ukawaida tangu wakati huo. Sasa Francisco anatumikia akiwa mzee kutanikoni, na akiwa pamoja na mke wake na watoto wawili, yeye hushangilia ahadi tukufu za Ufalme zilizo katika Neno la Mungu.
Kushiriki Kweli na Watu wa Ukoo
Manuela, painia wa kawaida katika eneo la Lisbon, amevua samaki wengi wa kiroho kwa sababu ya uvumilivu wake katika kutoa ushuhuda kwa watu wote kwa fadhili, kutia ndani watu wa ukoo. Miongoni mwao mlikuwa ndugu yake wa kimwili, José Eduardo, aliyekuwa amejifunza karate na matumizi ya silaha. Alikuwa amevunja sheria mara nyingi sana hivi kwamba hatimaye alipelekwa hukumuni kwa mashtaka 22 na kuhukumiwa kifungo cha miaka 20 gerezani. Alikuwa mjeuri sana hivi kwamba hata wafungwa wenzake walimwogopa, naye alifungiwa katika korokoro yenye ulinzi wa hali ya juu sana.
Kwa miaka saba kwa subira Manuela alimzuru José Eduardo, na sikuzote alikataa ujumbe wake wa Biblia. Hatimaye, kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kilipotangazwa, alikichukua, na funzo la Biblia likaanzishwa. Upesi akafanya mabadiliko makubwa sana katika mwenendo wake. Juma moja baadaye yeye binafsi alitoa ushahidi kwa wafungwa 200, na juma lililofuata kwa wafungwa 600 zaidi. Hata alipewa ruhusa ya kuzuru wafungwa waliokuwa katika majengo mengine. Kwa sababu ya badiliko kubwa la mwenendo wake, hukumu yake ilipunguzwa kuwa miaka 15. Baada ya kutumikia miaka 10, alifunguliwa awe mfungwa wa nje. Tangu wakati huo, miaka mitano imepita, na José Eduardo sasa ni Shahidi wa Yehova aliyebatizwa, akitumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko la kwao. Kisa halisi cha ‘mbwa mwitu kukaa na mwana-kondoo’!—Isaya 11:6.
Kwa sababu ya jitihada zake zenye kuendelea za kutoa ushahidi kwa familia yake, Manuela amepata shangwe ya kusaidia mume wake na washiriki wengine wanne wa familia yake kuwa watendaji katika utumishi wa Yehova. Mume wake sasa ni mtumishi wa huduma.
“Nitawafukuza kwa Mateke na Mjeledi”
Maria do Carmo aliishi katika kiunga fulani cha Lisbon Mashahidi walipomtembelea. Alipenda yale aliyosikia akamwuliza mume wake, Antônio, ikiwa anaweza kuwa na funzo la Biblia nyumbani. “Usithubutu hata kufikiria jambo hilo!” akajibu. “Nikipata Mashahidi wa Yehova katika nyumba yetu, nitawafukuza kwa mateke na mjeledi.” Ikatukia kwamba Antônio alikuwa mfunzi wa karate mwenye kiwango cha tatu cha ukanda mweusi. Basi Maria do Carmo akaamua kuwa na funzo la Biblia mahali pengine.
Baadaye, Antônio alilazimika kwenda Uingereza kwa mtaala wa karate wa siku nane, na kwa uwerevu Maria do Carmo akaweka katika sanduku lake kichapo My Book of Bible Stories.b Kwa kuwa Antônio alikuwa na muda mwingi katika safari yake, alikisoma kitabu hicho. Akiwa anarudi, dhoruba ilitikisa ndege hiyo vibaya, ikapata matatizo wakati wa kutua. Kwa mara ya kwanza maishani mwake, Antônio alisali kwa Yehova.
Antônio aliporudi nyumbani, yule Shahidi aliyekuwa akijifunza pamoja na mke wake akamwalika mkutanoni. Alikubali, akapata kwamba kila mtu alikuwa mwenye urafiki sana. Mipango ilifanywa kwa ajili ya funzo la Biblia, na kwa muda mfupi, Antônio akajua kwamba ni lazima afanye maamuzi fulani. Matokeo yakawa kwamba aliacha kufundisha karate akaanza kufundisha wanafunzi wake jinsi ya kuishi kwa amani sasa na milele. Mmoja wao, pia mwenye ukanda mweusi, sasa ni Mkristo aliyebatizwa.
Antônio alibatizwa Aprili 1991. Siku iliyofuata ubatizo wake, alianza kutumikia akiwa painia msaidizi. Miezi sita baadaye alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida, na upesi alikuwa akiongoza mafunzo 12 ya Biblia nyumbani. Katika Julai 1993 aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma katika kutaniko.
Katika Maeneo Yanayohubiriwa kwa Ukawaida
Katika maeneo mengi ya hiyo nchi, eneo huhubiriwa karibu kila juma. Mashahidi huendelezaje utendaji wao wa “kuvua” kwa matokeo?
João hujaribu kupata kila mtu aishiye katika kila nyumba. Alipokuwa akizuru mwanamke mmoja, aliuliza ikiwa kuna wengine wanaoishi katika nyumba hiyo. Mwanamke huyo akajibu kwamba mume wake na wana wake wawili wanaishi hapo, lakini si rahisi kuwapata kwa sababu walikuwa wanafanya kazi na wangerudi nyumbani jioni tu. Basi João akaendelea kuzuru wengine katika eneo hilo. Karibu muda wa saa moja na nusu baadaye, mtu mmoja akamjia.
“Ulisema unataka kuongea nami,” mtu huyo akamwambia João. “Tafadhali niambie unataka nini.”
“Kunradhi, lakini sikujui,” João akajibu, akiwa na mshangao. “Wewe ni nani?”
“Mimi ni Antônio, naishi kwenye barabara hii. Ulimwambia mama yangu kwamba ulitaka kuzungumza na familia yote, basi nimekuja kujua ulitaka nini.”
João akamtolea Antônio ushahidi kwelikweli na funzo la Biblia lilianzishwa naye. Baada ya funzo la pili, Antônio aliomba ikiwezekana funzo hilo lifanywe mara mbili kwa juma. Kwa miezi minne tu, alijiunga na João akaanza kuhubiri habari njema kwenye barabara aishiyo mwenyewe. Miezi mitatu baadaye, alibatizwa. Majuzi mama yake pia alianza kujifunza Biblia. Ni muhimu kama nini kujaribu kuzungumza na washiriki wote wa nyumba katika huduma!
Mambo kama hayo yenye kusisimua yaliyoonwa yaonyesha kwamba kungali kuna uvuvi mwingi wa kiroho wa kufanywa katika maji ya Ureno. Yehova amebariki Mashahidi wenye kufanya kazi kwa bidii kwa maelfu ya mafunzo ya Biblia yenye maendeleo. Waendeleapo kutafuta njia nyingine zaidi na zaidi za kufanya kweli ya Biblia ijulikane kwa wote, maneno ya mtume Paulo kwa Wakristo katika Filipi kwa kweli yanatimizwa katika Ureno leo: “Kwa njia zote . . . Kristo anahubiriwa.”—Wafilipi 1:18.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Ramani katika ukurasa wa 23]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
HISPANIA
URENO
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Mashahidi katika Ureno hutumia kila fursa kujulisha kweli ya Biblia