-
NdotoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Ndoto
Maana: Mawazo au picha za kuwaziwa za mtu akiwa usingizini. Biblia hurejelea ndoto za kawaida, ndoto kutoka kwa Mungu, na ndoto zinazohusu uaguzi.—Ayu. 20:8; Hes. 12:6; Zek. 10:2.
Je, ndoto za wakati wetu zina maana ya pekee?
Wachunguzi wamegundua nini kuhusu ndoto?
“Kila mtu huota ndoto,” yasema The World Book Encyclopedia (1984, Buku la 5, uku. 279). “Watu wazima wengi huota kwa karibu dakika 100 wakati wa saa nane za usingizi.” Kwa hiyo ndoto ni jambo la kawaida kwa wanadamu.
Dakt. Allan Hobson, wa Shule ya Tiba ya Harvard alisema hivi: “[Ndoto] zinaweza kufasiriwa kwa njia mbalimbali, na mtaalamu huzifasiri kwa njia yoyote ile anayopenda. Lakini maana yake imo katika akili ya yule aonaye—si katika ndoto yenyewe.” Ikiripoti jambo hilo, safu ya “Science Times” ya The New York Times iliongeza hivi: “Katika vikundi vya wachunguzi wanaoamini sana ndoto, kuna njia nyingi za kupata ujumbe wa akilini wa ndoto, kila moja ikionyesha maoni tofauti-tofauti ya kinadharia. Mwanafunzi wa nadharia ya Freud atapata maana moja katika ndoto, naye mwanafunzi wa nadharia ya Jung atapata maana nyingine, na tabibu wa Gestalt bado atapata maana nyingine. . . . Lakini yale maoni ya kwamba ndoto zina maana inayohusu akili yamepingwa vikali na wanasayansi wa neva.”—Julai 10, 1984, uku. C12.
Je, ndoto zinazoonekana kuwapa watu ujuzi wa pekee zinaweza kutokana na chanzo kingine badala ya Mungu?
Yer. 29:8, 9: “Yehova wa majeshi . . . amesema hivi: ‘Msiache manabii wenu walio katikati yenu na waaguzi wenu wawadanganye, nanyi msisikilize ndoto zao ambazo wanaota. Kwa maana “wanawatolea ninyi unabii wa uwongo katika jina langu. Mimi sikuwatuma,” asema Yehova.’”
Harper’s Bible Dictionary inatuambia hivi: “Wababiloni waliamini ndoto sana hivi kwamba siku moja kabla ya kufanya maamuzi muhimu walilala katika mahekalu, wakitumaini kupata shauri. Wagiriki waliotaka maagizo kuhusu afya walilala katika madhabahu ya Aeskulapio [aliyewakilishwa na nyoka], nao Waroma walilala katika mahekalu ya Serapi [nyakati fulani alishirikishwa na nyoka aliyejipinda]. Wamisri waliandika vitabu vyenye mambo mengi kwa ajili ya kufasiri ndoto.”—(New York, 1961), Madeleine Miller na J. Lane Miller, uku. 141.
Zamani, Mungu alitumia ndoto ili kutoa maonyo, maagizo, na unabii, lakini je, yeye anaongoza watu wake kwa njia hiyo leo?
Baadhi ya ndoto zinazotoka kwa Mungu zinarejezewa katika Mathayo 2:13, 19, 20; 1 Wafalme 3:5; Mwanzo 40:1-8.
Ebr. 1:1, 2: “Mungu, ambaye zamani za kale alisema katika pindi nyingi na katika njia nyingi [kutia ndani ndoto] na mababu zetu kupitia manabii, mwishoni mwa siku hizi amesema nasi kupitia Mwana [Yesu Kristo, ambaye mafundisho yake yameandikwa katika Biblia].”
1 Kor. 13:8: “Kama kuna zawadi za kutoa unabii [na wakati mwingine Mungu aliwapa watumishi wake unabii kupitia ndoto], zitaondolewa mbali.”
2 Tim. 3:16, 17: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha . . . ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”
1 Tim. 4:1: “Hata hivyo, neno lililoongozwa na roho linasema kwa hakika kwamba katika vipindi vya nyakati za mwisho wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha [wakati mwingine kupitia ndoto] na mafundisho ya roho waovu.”
-
-
NgonoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Ngono
Maana: Tabia ya viumbe wa duniani ambayo ni njia ya kuzaana kutokana na wazazi wawili. Tofauti kati ya jinsia ya kiume na kike huleta mabadiliko mengi katika maisha ya wanadamu. Kwa kuwa Mungu mwenyewe ndiye Chanzo cha uhai na kwa kuwa wanadamu walikusudiwa waonyeshe sifa zake, uwezo wa kupitisha uhai kwa mahusiano ya ngono unapaswa uheshimiwe sana.
Je, Biblia inafundisha kwamba mahusiano ya ngono ni dhambi?
Mwa. 1:28: “Mungu akawabariki [Adamu na Hawa] na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.’” (Ili kutimiza amri hii ya Mungu, ingekuwa lazima wawe na mahusiano ya ngono, sivyo? Kufanya hivyo hakungekuwa dhambi bali kungepatana na kusudi la Mungu la kuijaza dunia watu. Watu fulani wamefikiri kwamba lile ‘tunda lililokatazwa’ katika Edeni lilimaanisha kwamba labda Mungu aliwazuia au hata kuwakataza Adamu na Hawa wasiwe na mahusiano ya ngono. Lakini hilo linapingana na amri ya Mungu iliyonukuliwa juu. Pia linapingana na uhakika wa kwamba, ingawa Adamu na Hawa walikula lile tunda lililokatazwa katika Edeni, mtajo wa kwanza wa kufanya kwao ngono ulikuwa baada ya kufukuzwa kutoka humo.—Mwa. 2:17; 3:17, 23; 4:1.)
Mwa. 9:1: “Mungu akambariki Noa na wanawe, akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.’” (Baraka hii ya ziada, pamoja na kurudiwa kwa amri ya Mungu ya kuzaa, ilitolewa baada ya ile Gharika duniani katika siku za Noa. Maoni ya Mungu kuhusu mahusiano halali ya ngono hayakuwa yamebadilika.)
1 Kor. 7:2-5: “Kwa sababu ya kuenea kwa uasherati, kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe. Mume na ampe mke wake haki yake; lakini mke pia na amfanyie vivyo hivyo mume wake. . . . Msiwe mkinyimana haki hiyo, ila kwa makubaliano kwa wakati uliowekwa, . . . ili Shetani asiendelee kuwajaribu kwa sababu ya ninyi kukosa kujizuia.” (Jambo ambalo linaonyeshwa kuwa ni kosa ni uasherati, lakini si mahusiano ya ngono halali kati ya mume na mke.)
Je, ni makosa kuwa na mahusiano ya ngono kabla ya ndoa?
1 The. 4:3-8: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu . . . kwamba mjiepushe na uasherati; kwamba kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono kama ile waliyo nayo pia mataifa wale wasiomjua Mungu; kwamba yeyote asifikie hatua ya kudhuru na kuziingilia haki za ndugu yake katika jambo hilo, kwa sababu Yehova ndiye anayelipiza adhabu kwa ajili ya mambo yote haya, kama vile tulivyowaambia ninyi kimbele na pia tukawapa ushahidi kamili. Kwa maana Mungu alituita sisi bila kuruhusu nafasi ya uchafu, bali kuhusiana na utakaso. Kwa hiyo, basi, mtu anayepuuza hampuuzi mwanadamu, bali Mungu, anayeitia roho yake takatifu ndani yenu.” (Neno la Kigiriki por·neiʹa, lililotafsiriwa “uasherati,” linamaanisha tendo la ngono kati ya watu ambao hawajaoana, pia mahusiano ya ngono nje ya ndoa kwa watu waliooana.)
Efe. 5:5: “Hakuna mwasherati au mtu asiye safi au mtu mwenye pupa—maana yake ni kuwa mwabudu-sanamu—aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.” (Hilo halimaanishi kwamba yeyote ambaye zamani alikuwa mwasherati hawezi kupata baraka za Ufalme wa Mungu, lakini ni lazima aache maisha hayo ili apate kibali cha Mungu. Ona 1 Wakorintho 6:9-11.)
Je, Biblia inakubali kuishi pamoja kama mume na mke bila kuoana kisheria?
Ona ukurasa wa 226-230, chini ya kichwa “Ndoa.”
Biblia inasema nini kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja?
Rom. 1:24-27: “Kwa kupatana na tamaa za mioyo yao, Mungu aliwaacha katika uchafu, ili miili yao ivunjiwe heshima kati yao . . . Mungu aliwaacha katika hamu za ngono yenye kufedhehesha, kwa maana wanawake wao walibadili matumizi yao wenyewe ya asili kuwa yale yaliyo kinyume cha asili; na vivyo hivyo pia hata wanaume waliacha matumizi ya asili ya mwanamke na kuwakiana tamaa kali katika uchu wao kuelekeana wao wenyewe, wanaume kwa wanaume, wakitenda mambo machafu na kupokea ndani yao wenyewe malipo kamili, yaliyostahili kosa lao.”
1 Tim. 1:9-11: “Sheria huwekwa, si kwa ajili ya mtu mwadilifu, bali kwa ajili ya watu wenye kuasi sheria na watundu, wasiomwogopa Mungu na watenda-dhambi, . . . waasherati, wanaume wanaolala na wanaume, . . . na jambo lingine lolote linalopinga fundisho lenye afya kulingana na habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha.” (Linganisha na Mambo ya Walawi 20:13.)
Yuda 7: “Sodoma na Gomora na majiji yaliyoyazunguka, baada ya hayo . . . kwenda kufuatilia mwili kwa ajili ya matumizi yasiyo ya asili, . . . yamewekwa mbele yetu kuwa kielelezo cha kuonya kwa kupatwa na adhabu ya hukumu ya moto wa milele.” (Jina Sodoma ndilo msingi wa neno la Kiingereza “sodomy,” ambalo kwa kawaida humaanisha tendo la ngono kati ya watu wa jinsia moja. Linganisha na Mwanzo 19:4, 5, 24, 25.)
Wakristo wa kweli wanawaonaje wale ambao wamekuwa na zoea la kufanya ngono na watu wa jinsia moja?
1 Kor. 6:9-11: “Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume . . . hawataurithi ufalme wa Mungu. Na bado wengine wenu mlikuwa hivyo. Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.” (Bila kujali matendo hayo ya zamani, ikiwa sasa watu wanayaacha matendo yao machafu ya zamani, wafuate viwango vya uadilifu vya Yehova, na kuwa na imani katika uandalizi wake wa msamaha wa dhambi kupitia Kristo, wanaweza kupata msimamo safi mbele za Mungu. Baada ya kujirekebisha, wanaweza kukaribishwa katika kutaniko la Kikristo.)
Wakristo wa kweli wanajua kwamba watu ambao kweli wanataka kumpendeza Yehova wanaweza kuzishinda hata tamaa mbaya zenye nguvu, kutia ndani zile ambazo huenda zikawa za kurithiwa au zile zinazohusisha visababishi vya kimwili au vya kimazingira. Watu fulani kwa asili wanakasirika upesi. Labda zamani walikuwa wepesi kukasirika; lakini kuyajua mapenzi ya Mungu, tamaa ya kutaka kumpendeza, na msaada wa roho yake huwawezesha kujizuia. Huenda mtu akawa mlevi, lakini, akiwa na kichocheo kinachofaa, anaweza kuacha kunywa na hivyo aepuke kuwa mlevi. Vivyo hivyo, huenda mtu akahisi kuvutiwa sana na watu wa jinsia yake, lakini akitii shauri la Neno la Mungu, anaweza kubaki safi bila kufanya ngono na watu wa jinsia yake. (Ona Waefeso 4:17-24.) Yehova haturuhusu tuendelee kufikiri kwamba mwenendo mbaya ni sawa tu; kwa fadhili lakini kwa uthabiti yeye hutuonya juu ya matokeo naye huwapa msaada mwingi wale wanaotaka ‘kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na kujivika utu mpya.’—Kol. 3:9, 10.
-