-
YehovaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
lakini waandikaji wa Maandiko ya Kikristo walioongozwa na roho ya Mungu hawakusita kutumia jina la Kigiriki, I·e·sousʹ. Katika lugha nyingine nyingi matamshi hutofautiana kidogo, lakini sisi hutumia jina la kawaida katika lugha yetu. Hivyo ndivyo ilivyo kuhusu majina mengine ya Biblia. Basi, tunaweza kumwonyeshaje heshima inayofaa Yule mwenye jina muhimu kuliko majina yote? Je, tungefanya hivyo kwa kutotaja kamwe wala kuandika jina lake kwa sababu hatujui vizuri jinsi lilivyokuwa likitamkwa hapo kwanza? Au, badala yake, je, hatungetumia matamshi na herufi za kawaida katika lugha yetu, huku tukisema mambo mazuri kumhusu Mwenye jina hilo na kujiendesha kwa njia inayomletea heshima tukiwa waabudu wake?
Kwa nini ni muhimu kujua na kutumia jina la Mungu?
Je, una uhusiano wa karibu na mtu yeyote ambaye hujui jina lake? Kwa watu wanaoona kwamba Mungu hana jina mara nyingi yeye ni nguvu tu zisizo na utu, si mtu halisi, si mtu wanayemjua na kumpenda na ambaye wanaweza kusema naye kutoka moyoni katika sala. Wanaposali, sala zao huwa desturi tu, kurudia-rudia kidesturi maneno yaliyokaririwa.
Yesu Kristo amewapa Wakristo wa kweli utume wa kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. Wanapowafundisha watu hao, wanawezaje kumtofautisha Mungu wa kweli na miungu ya uwongo ya mataifa? Ni kwa kutumia tu jina Lake, kama Biblia yenyewe inavyolitumia.—Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 8:5, 6.
Kut. 3:15: “Mungu akamwambia Musa . . . : ‘Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, “Yehova Mungu wa mababu zenu . . . amenituma kwenu.” Hilo ndilo jina langu mpaka wakati usio na kipimo, na huo ndio ukumbusho wangu kwa kizazi baada ya kizazi.’”
Isa. 12:4: “Mpeni Yehova shukrani! Liitieni jina lake. Tangazeni matendo yake kati ya vikundi vya watu. Semeni kwamba jina lake limeinuliwa juu.”
Eze. 38:17, 23: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amesema hivi, ‘ . . . Nami hakika nitajitukuza mwenyewe na kujitakasa mwenyewe na kujijulisha mwenyewe mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”
Mal. 3:16: “Wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana, kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.”
Yoh. 17:26: “[Yesu alimwomba Baba yake:] Nami nimewajulisha [wafuasi wake] jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”
Mdo. 15:14: “Simioni ameeleza kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.”
Je, Yehova katika “Agano la Kale” ndiye Yesu Kristo katika “Agano Jipya”?
Mt. 4:10: “Yesu akamwambia: ‘Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, “Yehova [“Bwana,” UV na nyinginezo] Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”’” (Ni wazi Yesu hakuwa akisema kwamba yeye mwenyewe alipaswa kuabudiwa.)
Yoh. 8:54: “Yesu akajibu [Wayahudi]: ‘Ikiwa mimi ninajitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu. Baba yangu ndiye ambaye hunitukuza, yule ambaye ninyi mnasema kwamba ni Mungu wenu.’” (Maandiko ya Kiebrania yanamtambulisha waziwazi Yehova kuwa Mungu ambaye Wayahudi walidai kuabudu. Yesu hakusema kwamba yeye mwenyewe ni Yehova, bali kwamba Yehova ni Baba yake. Hapa Yesu alionyesha wazi kabisa kwamba yeye na Baba yake walikuwa watu wawili tofauti.)
Zab. 110:1: “Neno la Yehova kwa Bwana wangu [Daudi] ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume Mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’” (Kwenye Mathayo 22:41-45, Yesu alieleza kwamba yeye mwenyewe ndiye “Bwana” wa Daudi, ambaye alitajwa katika Zaburi hiyo. Kwa hiyo, Yesu si Yehova bali ndiye aliyekuwa akiambiwa na Yehova maneno hayo.)
Flp. 2:9-11: “Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha [Yesu Kristo] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Ona kwamba Yesu Kristo hapa anatofautishwa na Mungu Baba na kwamba anamtii Yeye.)
Mtu anawezaje kumpenda Yehova ikiwa anapaswa kumwogopa pia?
Biblia hutuambia kwamba tunapaswa kumpenda Yehova (Luka 10:27) na pia kumwogopa. (1 Pet. 2:17; Met. 1:7; 2:1-5; 16:6) Kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa kutatufanya tuwe waangalifu sana tusimkasirishe. Kumpenda Yehova kutatusukuma tutake kufanya mambo yanayompendeza, kumshukuru kwa kutuonyesha upendo na fadhili zisizostahiliwa kwa njia nyingi.
Mfano: Mwana huogopa kumkasirisha baba yake, lakini kuthamini yote ambayo baba yake humfanyia kunapaswa pia kumsukuma mwana huyo kumpenda baba yake kikweli. Huenda mwogeleaji akasema kwamba yeye anaipenda bahari, lakini kuiogopa bahari humfanya afahamu kwamba kuna mambo anayopaswa kuepuka kufanya. Vivyo hivyo, kumpenda Mungu kunapaswa kuambatana na kuogopa kufanya lolote litakalomkasirisha.
-
-
Yesu KristoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Yesu Kristo
Maana: Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, Mwana pekee aliyefanyizwa na Yehova peke yake. Mwana huyo ndiye mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote. Vitu vingine vyote mbinguni na duniani viliumbwa kupitia kwake. Yeye ndiye mtu wa pili kwa ukuu ulimwenguni pote. Ndiye Mwana ambaye Yehova alimtuma duniani ili atoe uhai wake uwe fidia kwa ajili ya wanadamu, na kwa kufanya hivyo, alifungua njia ya uzima wa milele kwa ajili ya watoto wa Adamu ambao wangekuwa na imani. Mwana huyohuyo, aliyerudishwa kwenye utukufu wa mbinguni, sasa anatawala akiwa Mfalme, akiwa na mamlaka ya kuwaharibu waovu wote na kutimiza kusudi la kwanza la Baba yake kwa ajili ya dunia. Katika Kiebrania, jina Yesu humaanisha “Yehova Ni Wokovu”; jina Kristo linalingana na jina la Kiebrania Ma·shiʹach (Masihi), linalomaanisha “Mtiwa-Mafuta.”
-