-
DuniaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Yerusalemu Jipya la mbinguni, na kupitia hilo baraka zitawajia wanadamu watiifu.)
Met. 2:21, 22, UV: “Wanyofu watakaa katika nchi [“duniani,” NW], na wakamilifu [“waaminifu,” BHN] watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” (Kumbuka andiko hilo halisemi kwamba waaminifu watarudi duniani bali “watadumu ndani yake.”)
Je, kusudi la Mungu la kwanza kwa dunia limebadilika?
Mwa. 1:27, 28: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabariki na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.’” (Basi Mungu alionyesha kusudi lake la kutaka dunia ijawe na wazao wa Adamu na Hawa wakiwa watunzaji wa paradiso ya duniani pote. Baada ya Mungu kuiumba dunia hii vizuri ili iwe makao ya wanadamu, na kuifanya kuwa ya pekee kati ya sayari zote ambazo mwanadamu amechunguza kwa kutumia darubini na vyombo vya angani, je, Muumba alilitupilia mbali kusudi lake, na kuliacha milele bila kulitimiza kwa sababu ya dhambi ya Adamu?)
Isa. 45:18: “Kwa maana Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’” (Ona pia Isaya 55:10, 11.)
Ikiwa hakuna mtu atakayekufa katika Mfumo Mpya wa Mungu, je, watu wote watatoshea duniani?
Kumbuka kwamba Mungu alipoeleza kusudi lake kwa ajili ya dunia alisema: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” (Mwa. 1:28) Mungu alimpa mwanadamu uwezo wa kuzaa, na wakati kusudi Lake kuhusu jambo hilo litakapotimizwa Yeye anaweza kufanya uzazi ukome duniani.
Mungu atawapa watu wa aina gani uzima usio na mwisho duniani?
Sef. 2:3: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia, ambao mmetenda uamuzi Wake wa hukumu. Utafuteni uadilifu, utafuteni upole. Huenda mkafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.”
Zab. 37:9, 11: “Wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. . . . Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”
-
-
FalsafaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Falsafa
Maana: Neno falsafa linatokana na maneno ya Kigiriki yanayomaanisha “kupenda hekima.” Falsafa inayozungumziwa hapa haitokani na imani katika Mungu, bali inajaribu kuwapa watu wote maoni yanayopatana kuhusu ulimwengu na inajaribu kuwafanya wawe wachambuzi. Inatumia sana njia za kukisia-kisia badala ya kufanya uchunguzi ili kutafuta kweli.
Tunaweza kupataje ujuzi na hekima ya kweli?
Met. 1:7; Zab. 111:10: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa ujuzi . . . [na ] wa hekima.” (Ikiwa ulimwengu haukuumbwa na Muumba mwenye akili bali ulitokana na nguvu fulani tu zisizo na akili, basi je, kweli inawezekana kuwa na maoni yanayopatana kuhusu ulimwengu? Je, hekima inaweza kupatikana kwa kuchunguza kitu kisichopatana na akili? Wale wanaojaribu kuufahamu ulimwengu au uhai wenyewe, huku wakimkataa Mungu na kusudi lake, huambulia patupu. Wanaelewa kimakosa yale wanayojifunza na kutumia vibaya mambo wanayopata. Kutomwamini Mungu huharibu ufunguo unaoongoza kwenye ujuzi sahihi na hufanya isiwezekane kwa watu wote kuwa na maoni yanayopatana.)
Met. 2:4-7: “Ikiwa utaendelea kuutafuta kama fedha, na kuendelea kuutafuta kama hazina zilizofichika, ndipo utakapoelewa kumwogopa Yehova, nawe utapata kumjua Mungu. Kwa maana Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi. Naye atawawekea wanyoofu hazina ya hekima inayotumika.” (Yehova hutoa msaada unaohitajika kupitia Neno lake lililoandikwa na tengenezo lake linaloonekana. Ni lazima pia mtu awe na hamu na bidii na kutumia akili kwa njia inayofaa.)
Je, inawezekana kupata kweli kamili kutoka Chanzo hiki?
2 Tim. 3:16; Yoh. 17:17: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” “[Yesu alimwambia Baba yake wa mbinguni:] Neno lako ni kweli.” (Je, si jambo linalopatana na akili kwamba Muumba wa ulimwengu anauelewa kikamili? Katika Biblia yeye hajatuambia mambo yote kuhusu ulimwengu, lakini yale ambayo ameandika humo si makisio; hayo ni ya kweli. Yeye pia ameonyesha katika Biblia kusudi lake kwa dunia na kwa wanadamu na jinsi atakavyolitimiza. Nguvu zake zisizo na mwisho, hekima yake kuu zaidi, haki yake isiyo na kasoro, na upendo wake mkuu vinatoa uhakikisho kwamba kusudi hilo litatimizwa kikamili, na kwa njia bora zaidi. Kwa hiyo sifa zake zinatuhakikishia kwamba kusudi lake lililoandikwa hutegemeka kabisa; hilo ni kweli.)
Falsafa za wanadamu zilitoka wapi?
Zinatokana na watu walio na upungufu: Biblia inatuambia hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) Historia inathibitisha kwamba kujaribu kupuuza upungufu huo hakujatokeza mambo mema. Wakati mmoja, “Yehova a[li]anza kumjibu Ayubu kutoka katika dhoruba ya upepo, akasema: ‘Ni nani huyu anayefunika shauri kwa maneno yasiyo na ujuzi? Tafadhali jifunge viuno vyako, kama mwanamume, na acha mimi nikuulize maswali, nawe unijulishe. Ulikuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia? Niambie, ikiwa unaelewa.’” (Ayu. 38:1-4) (Kwa kawaida wanadamu wana upungufu. Isitoshe, maisha yao ni mafupi na kwa kawaida wanaishi katika utamaduni mmoja au mazingira ya aina moja tu. Kwa hiyo, ujuzi wao ni mchache, na mambo yote yanahusiana hivi kwamba sikuzote wanagundua mambo ambayo hawajapata kuyafikiria vya kutosha. Falsafa yoyote wanayoanzisha itakuwa na upungufu huo.)
Zinatokana na wanadamu ambao si wakamilifu: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rom. 3:23) “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Met. 14:12) (Kwa sababu ya kutokamilika huko, mara nyingi falsafa za wanadamu huonyesha ubinafsi ambao labda huleta raha ya muda lakini pia kukata tamaa na huzuni nyingi.)
-