-
Ni Nini Kinacholeta Umoja wa Kweli Miongoni mwa Wakristo?Huduma ya Ufalme—2003 | Desemba
-
-
Ni Nini Kinacholeta Umoja wa Kweli Miongoni mwa Wakristo?
1 Ni nini kinachoweza kuwaunganisha watu zaidi ya milioni sita katika nchi 234 wanaozungumza lugha zipatazo 380? Ni ibada ya Yehova Mungu tu inayoweza kufanya hivyo. (Mika 2:12; 4:1-3) Mashahidi wa Yehova wamejionea wenyewe kwamba kuna umoja wa kweli wa Kikristo leo. Tukiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” tumeazimia kuipinga kabisa roho ya ulimwengu inayoleta mgawanyiko.—Yoh. 10:16; Efe. 2:2.
2 Kusudi la Mungu lisiloweza kushindwa ni kwamba malaika na wanadamu wote waungane pamoja katika ibada ya kweli. (Ufu. 5:13) Yesu alijua umuhimu wa jambo hilo na ndiyo sababu alisali kwa bidii kwamba wafuasi wake wawe na umoja. (Yoh. 17:20, 21) Kila mmoja wetu anawezaje kudumisha umoja katika kutaniko la Kikristo?
3 Mambo Yanayoleta Umoja: Hakungekuwa na umoja wa Kikristo bila Neno la Mungu na roho yake. Tunapofuata yale ambayo tunasoma katika Biblia, tunaruhusu roho ya Mungu ituongoze maishani. Na hilo hutuwezesha ‘tuushike umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.’ (Efe. 4:3) Hutuchochea tuvumiliane kwa upendo. (Kol. 3:13, 14; 1 Pet. 4:8) Je, wewe hudumisha umoja kwa kutafakari Neno la Mungu kila siku?
4 Kazi yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi pia hufanya tuwe na umoja. Tunapohubiri na wengine katika huduma ya Kikristo, ‘tukikazana pamoja kwa ajili ya imani ya habari njema,’ tunakuwa “wafanyakazi wenzi katika kweli.” (Flp. 1:27; 3 Yoh. 8) Tunapofanya hivyo, vifungo vyenye kuunganisha vya upendo kutanikoni huimarishwa. Mbona usimwalike mtu ambaye hujahubiri naye hivi karibuni aambatane nawe kwenye huduma ya shambani juma hili?
5 Tumebarikiwa sana kuwa sehemu ya undugu wa pekee wa kweli wa kimataifa ulimwenguni leo! (1 Pet. 5:9) Hivi karibuni, maelfu ya watu walijionea wenyewe umoja huo wa ulimwenguni pote katika Makusanyiko ya Kimataifa ya “Mtukuzeni Mungu.” Sisi sote na tudumishe umoja huo wenye thamani kwa kusoma Neno la Mungu kila siku, kwa kutatua kwa upendo kutoelewana, na kwa kuhubiri habari njema “kwa umoja.”—Rom. 15:6.
-
-
Kuwatafuta Wale WanaostahiliHuduma ya Ufalme—2003 | Desemba
-
-
Kuwatafuta Wale Wanaostahili
1 Huenda isiwe rahisi kufuata maagizo ya Yesu kuhusu kazi ya kuhubiri. Aliagiza hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mtakapoingia, tafuteni ni nani humo anayestahili.” (Mt. 10:11) Kwa kuwa si rahisi kuwapata watu nyumbani siku hizi, tunawezaje kuwatafuta na kuwapata wale wanaostahili?
2 Chunguza Eneo Lenu: Kwanza chunguza eneo lenu. Kwa kawaida, watu hupatikana nyumbani wakati gani? Wanaweza kupatikana wapi mchana? Je, kuna siku fulani au wakati fulani ambapo huenda wakatukaribisha na kutusikiliza? Unaweza kupata matokeo zaidi ukibadili ratiba yako ya kuhubiri ili iwafae watu katika eneo lenu.—1 Kor. 9:23, 26.
3 Wahubiri wengi wamefanikiwa kuwapata watu nyumbani saa za jioni. Baadhi yao huwa wamestarehe zaidi na huwa tayari kutusikiliza wakati huo. Tunaweza pia kuwafikia watu kwa kuhubiri habari njema katika maeneo ya kibiashara na sehemu za umma.
4 Katika mwezi mmoja wa utendaji wa pekee, kutaniko fulani lilipanga kuhubiri Jumamosi na Jumapili jioni, na Jumatano na Ijumaa jioni. Kutaniko hilo lilipanga pia kuhubiri eneo la kibiashara. Wengi walifurahia kuhubiri wakati huo hivi kwamba kutaniko likaamua kuendelea na mpango huo.
5 Fanya Ziara za Kurudia kwa Bidii: Ikiwa ni vigumu kuwapata watu nyumbani unapofanya ziara za kurudia, kila wakati unapowatembelea jaribu kufanya mpango hususa wa kurudi. Kisha hakikisha umerudi kama ulivyoahidi. (Mt. 5:37) Inapofaa, unaweza kumwomba mwenye nyumba namba yake ya simu ili uweze kuwasiliana naye tena.
6 Bila shaka, Yehova atabariki jitihada zetu za kuwatafuta wanaostahili na kusitawisha upendezi wao.—Met. 21:5.
-