-
Kumpa Yehova Kilicho BoraHuduma ya Ufalme—2004 | Aprili
-
-
Kumpa Yehova Kilicho Bora
1 Sheria ya Yehova kwa Waisraeli iliagiza kwamba wanyama waliotolewa kuwa dhabihu ‘hawakupaswa kuwa na kasoro.’ Mnyama mwenye kasoro hakukubaliwa. (Law. 22:18-20; Mal. 1:6-9) Isitoshe, dhabihu ilipotolewa, Yehova alipewa mafuta yote, yaani, sehemu iliyo bora. (Law. 3:14-16) Akiwa Baba na Bwana-Mkuu wa Israeli, Yehova alistahili kupewa kilicho bora zaidi.
2 Kama ilivyokuwa nyakati za kale, Mungu anapendezwa sana na ubora wa dhabihu zetu leo. Utumishi wetu unapaswa kuonyesha heshima inayofaa kwa Yehova. Ni kweli kwamba hali za watu hutofautiana. Hata hivyo, tuna sababu nzuri za kujichunguza ili kuhakikisha kwamba tunampa Yehova kilicho bora.—Efe. 5:10.
3 Utumishi wa Moyo Wote: Ili huduma yetu imheshimu Yehova na kuchochea mioyo ya wasikilizaji wetu, haipaswi kuwa ya kidesturi. Yale tunayosema kumhusu Mungu wetu na makusudi yake matukufu yanapaswa kutoka katika mioyo iliyojaa shukrani. (Zab. 145:7) Hilo linakazia umuhimu wa kuwa na programu nzuri ya kusoma na kujifunza Biblia kibinafsi.—Met. 15:28.
4 Kumpa Yehova kilicho bora kunatia ndani kuiga upendo wake kwa watu. (Efe. 5:1, 2) Upendo wetu kwa watu utatuchochea kujaribu kuwajulisha wengi iwezekanavyo ujumbe wa kweli wenye kuokoa uhai. (Marko 6:34) Unatusukuma tupendezwe kibinafsi na wale tunaozungumza nao. Unatufanya tuendelee kuwafikiria baada ya kukutana nao mara ya kwanza na kutuchochea turudi tena. Unatuchochea kufanya yote tuwezayo kuwasaidia wafanye maendeleo ya kiroho.—Mdo. 20:24; 26:28, 29.
5 “Dhabihu ya Sifa”: Kuwa na bidii katika huduma ni njia nyingine ya kumpa Yehova kilicho bora. Tunaweza kutimiza mengi katika muda mfupi ikiwa tuna ratiba nzuri na tunakazia fikira kazi iliyo mbele yetu. (1 Tim. 4:10) Yaelekea watu wengi watatusikiliza ikiwa tutajitayarisha vizuri na kuzungumza kwa njia inayoeleweka na kwa usadikisho. (Met. 16:21) Tunapowahubiria wengine habari njema, yale tunayosema kutoka moyoni yanaweza kwa kufaa kuitwa “dhabihu ya sifa.”—Ebr. 13:15.
-
-
Vijana—Someni Neno la Mungu!Huduma ya Ufalme—2004 | Aprili
-
-
Vijana—Someni Neno la Mungu!
1 Ujana ni wakati wa matatizo na wa kufanya maamuzi mazito. Kila siku, ninyi vijana Wakristo hukabili mikazo ya kuvunja kanuni za Mungu za mwenendo. Kabla ya kufanya maamuzi kuhusu elimu, kazi, na ndoa, weka kwanza miradi ya kiroho. Kwa kufanya hivyo, utaweza kufanya maamuzi mengine yatakayokunufaisha maishani. Miradi hususa ya kiroho itakusaidia utende kwa hekima na kufanikiwa maishani. Kusoma na kutafakari Neno la Mungu kwa ukawaida kutakuchochea kufuata shauri lake liliongozwa na roho na hivyo jitihada zako zitafanikiwa.—Yos. 1:8; Zab. 1:2, 3.
2 Utanufaikaje? Ulimwengu wa Shetani umejaa vishawishi vingi vya kufanya mabaya. (1 Yoh. 2:15, 16) Huenda unajua wanashule wenzako au vijana wengine wa rika lako ambao wamepatwa na msiba kwa sababu ya kukubali kushawishiwa na marika zao. Kufuata shauri la Biblia kutakuimarisha kiadili na kiroho ili ukatae mwenendo wenye dhambi. Pia, shauri la Neno la Mungu litakusaidia kuepuka mitego isiyoonekana ya Shetani. (2 Kor. 2:11; Ebr. 5:14) Kutembea katika njia ya Mungu kutakuletea furaha ya kweli na utaridhika na maisha yako.—Zab. 119:1, 9, 11.
3 Kanuni za Neno la Mungu zisizobadilika zinapita hekima ya wanadamu. (Zab. 119:98-100) Kujua kanuni za Biblia na kutafakari makusudi ya Yehova yaliyofunuliwa, pamoja na kusali kutoka moyoni kunaweza kukusaidia kujenga uhusiano wa karibu na Yehova Mungu, Mtungaji wa Biblia aliye na hekima yote. Anaahidi hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”—Zab. 32:8.
4 Panga Wakati wa Kusoma Biblia: Kijana mmoja Mkristo aliweka mradi wa kusoma Biblia nzima, naye alifanya hivyo kwa mwaka mmoja. Alinufaikaje? Anasema: “Nilijifunza mambo mengi kumhusu Yehova. Mambo hayo yalinifanya nimkaribie na kutaka kumwogopa maisha yangu yote.” (Yak. 4:8) Je, umeisoma Biblia nzima? Ikiwa hujafanya hivyo, mbona usiweke mradi huo? Bila shaka Yehova atabariki jitihada zako, na utapata baraka nyingi.
-