-
Epuka Kufuatia “Mambo ya Upuzi”Huduma ya Ufalme—2002 | Septemba
-
-
Epuka Kufuatia “Mambo ya Upuzi”
1 Kuwasiliana kwa kutumia kompyuta, barua-pepe (E-mail), hupendwa sana leo. Ijapokuwa inafaa kupashana habari na kuwaeleza watu wa familia na marafiki mambo yaliyoonwa kwa kutumia barua-pepe, ni mambo gani ya upuzi yanayoweza kuhusianishwa na utumizi wa barua-pepe usio na mipaka?—Mit. 12:11.
2 Tahadhari Kuhusu Barua-Pepe: Watu fulani husema kwamba wanajihisi kuwa karibu na tengenezo la Yehova wanapopokea habari mpya kwa njia ya barua-pepe. Habari hizo zinaweza kuwa mambo yaliyoonwa, taarifa fupifupi kuhusu kile kinachoendelea huko Betheli, habari kuhusu misiba au mnyanyaso, na hata habari za siri zilizotangazwa kwenye Shule ya Huduma ya Ufalme. Wengine hupenda sana kutuma habari hizo, wakitaka kuwa wa kwanza kuwaeleza marafiki wao.
3 Habari mbalimbali na mambo yaliyoonwa yametiwa chumvi nyakati nyingine, au yamepotoshwa. Au huenda wengine waliosimulia habari fulani walitaka kumstaajabisha msomaji, na hivyo walifanya habari zisieleweke vizuri. Mara nyingi, watu walio na haraka ya kueneza habari kama hizo huwa hawajapata habari kamili. (Mit. 29:20) Hata hadithi zisizoaminika hata kidogo huenezwa kwa sababu tu zinavutia. Habari kama hizo ni “hadithi zisizo za kweli” zenye kupotosha, nazo haziendelezi ujitoaji-kimungu.—1 Tim. 4:6, 7.
4 Ukiwasilisha habari ambayo baadaye inajulikana kuwa ya uwongo, utalaumiwa kwa kadiri fulani kwa huzuni au mchafuko unaoweza kutokea. Daudi alipopata habari iliyotiwa chumvi kwamba wana wake wote walikuwa wameuawa, ‘alirarua nguo zake’ akiwa na uchungu mkubwa moyoni. Hata hivyo, mmoja tu wa wana wake ndiye aliyekuwa ameuawa. Jambo hilo lilimhuzunisha Daudi, lakini habari iliyotiwa chumvi ilimtia uchungu hata zaidi. (2 Sam. 13:30-33) Bila shaka hatutaki kuwadanganya au kuwavunja moyo ndugu zetu kwa njia yoyote.
5 Njia Ambayo Mungu Huwasiliana Nasi: Kumbuka kwamba Baba yetu wa mbinguni huwasiliana nasi kwa kutumia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye amemweka. “Mtumwa” huyo ana daraka la kuamua habari ambazo watu wenye imani wanahitaji na “wakati ufaao” wa kuzitoa. Chakula hicho cha kiroho chapatikana tu katika tengenezo la Mungu. Tunapaswa sikuzote kutegemea tengenezo la Mungu lililowekwa ili tupate habari za kweli, bali si watu mbalimbali wanaotumia Internet.—Mt. 24:45.
6 Vituo vya Internet: Tuna kituo cha Internet chenye anwani hii: www.watchtower.org. Kituo hicho kinatoa habari za kutosha kwa umma. Hakuna haja kwa mtu yeyote, halmashauri, au kutaniko kutengeneza kituo cha Internet kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Watu fulani wameweka vichapo vyetu kwenye Internet pamoja na maandiko na marejeo yote yanayotajwa katika vichapo hivyo, na hata wamejitolea kutuma hotuba za makusanyiko kwa watu wanaotoa michango ya hiari. Hata kama jambo hilo halikufanywa ili kupata faida ya kifedha, kufanya vichapo vya Mashahidi wa Yehova vipatikane kwenye Internet na kuvieneza kwa njia hiyo kunavunja sheria za haki ya kunukuu. Ijapokuwa wengine huenda wakaliona jambo hilo kuwa msaada kwa akina ndugu, halijaidhinishwa na linapaswa kukomeshwa.
7 Tukitumia busara na utimamu wa akili tunapowasiliana na wengine kwa kutumia kompyuta, akili zetu zitajaa “vitu vyote vya thamani na vya kupendeza.”—Mit. 24:4.
-
-
Mambo ya Kusema Kuhusu MagazetiHuduma ya Ufalme—2002 | Septemba
-
-
Mambo ya Kusema Kuhusu Magazeti
Mnara wa Mlinzi Ago. 15
“Wewe unaonaje? Tunapaswa kuwa waaminifu kwa nani hasa? [Ngoja jibu.] Makala hii inakazia uaminifu kwa Mungu wa kweli. [Onyesha ukurasa wa 5, na usome 2 Samweli 22:26.] Je, unajua kwamba uaminifu kwa Mungu unaweza kuwazuia watu wasiwatendee wengine bila upendo? Nina uhakika kwamba utafurahia kusoma juu ya jambo hilo.”
Amkeni! Ago. 22
“Je, umewahi kufikiri kwamba uchafuzi wa dunia umezidi kiasi cha kwamba hauwezi kukomeshwa? [Ngoja jibu.] Jambo moja linalosababisha uchafuzi ni kwamba watu huwa na zoea la kutupatupa vitu. Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasiharibu mali ovyoovyo. [Soma Yohana 6:12.] Gazeti hili linaonyesha jinsi kanuni za Biblia zinavyoweza kuwasaidia watu wasiwe na mwelekeo wa kutupa vitu ovyoovyo.”
Mnara wa Mlinzi Sept. 1
“Je, umetambua kwamba katika sehemu nyingi majirani hawajuani kama walivyojuana zamani? [Ngoja jibu.] Yesu alitaja kanuni moja inayoweza kumsaidia mtu kuwa jirani mzuri. [Soma Mathayo 7:12.] Gazeti hili linaonyesha jinsi tunavyoweza kuwa majirani bora na kuwatia wengine moyo kufanya vivyo hivyo.”
Amkeni! Sept. 8
“Siku hizi watu wengi wanahangaikia jinsi maisha yao yatakavyokuwa. [Soma Mhubiri 9:11.] Mwongozo unaofaa unapatikana wapi? [Ngoja jibu.] Watu fulani huamini kwamba namba fulani zinaweza kutabiri wakati ujao. Je, hiyo ndiyo njia ya kujua jinsi maisha yako yatakavyokuwa? Unaweza kupata wapi habari zenye kutegemeka kuhusu wakati ujao? Gazeti hili la Amkeni! linajibu maswali hayo.”
-