-
Kuhubiri Kuhusu Ufalme Ni Pendeleo la PekeeHuduma ya Ufalme—2005 | Agosti
-
-
Kuhubiri Kuhusu Ufalme Ni Pendeleo la Pekee
1 Kila siku, mabilioni ya watu duniani hunufaishwa na vitu vingi ambavyo Yehova huwaandalia ili waendelee kuwa hai. (Mt. 5:45) Hata hivyo, ni watu wachache sana walio na pendeleo la pekee la kumshukuru Muumba wao kwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Unalithamini kadiri gani pendeleo hilo la pekee?
2 Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme humletea Mungu heshima na huwapa tumaini na amani watu wanaosononeshwa na misukosuko ya leo. (Ebr. 13:15) Wale wanaoukubali ujumbe wa Ufalme watapata uzima wa milele. (Yoh. 17:3) Je, kuna kazi au taaluma yoyote katika ulimwengu inayoweza kutunufaisha jinsi hiyo? Mtume Paulo alitimiza huduma yake kwa njia iliyoonyesha kwamba aliithamini. Aliiona kuwa hazina.—Mdo. 20:20, 21, 24; 2 Kor. 4:1, 7.
3 Kulithamini Pendeleo Letu la Pekee: Njia moja ya kuonyesha kwamba tunalithamini pendeleo letu la kuhubiri ni kuzingatia ubora wa utumishi wetu. Je, tunajitahidi kutayarisha utangulizi ambao utagusa mioyo ya wasikilizaji wetu? Je, tunaweza kuboresha uwezo wetu wa kutumia Maandiko na wa kujadiliana na watu? Je, tunahubiri eneo letu kikamili? Je, tunaweza kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia? Kama Wakristo waaminifu, wa nyakati zilizopita na wa siku hizi, sisi pia tunachochewa na mtazamo unaofaa kuelekea kazi hii, nasi tunalithamini sana pendeleo letu.—Mt. 25:14-23.
4 Ikiwa tunasumbuliwa na matatizo ya uzeeni, afya mbaya, au matatizo mengine, inafariji kujua kwamba jitihada na bidii yetu katika huduma inathaminiwa sana. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova anathamini jitihada kama hizo za kumtumikia, kutia ndani jitihada ambazo huenda wengine wasizithamini.—Luka 21:1-4.
5 Kuhubiri kuhusu Ufalme huridhisha sana. Dada mwenye umri wa miaka 92 alisema hivi: “Ni pendeleo lililoje kufikiria miaka zaidi ya 80 ambayo nimekuwa nikimtumikia Mungu. Sina majuto yoyote! Ikiwa ningepewa nafasi nyingine, ningetumia maisha yangu kwa njia hiyohiyo kwa sababu, bila shaka, ‘fadhili zenye upendo za Mungu ni bora kuliko uzima.’” (Zab. 63:3) Sisi pia na tulithamini pendeleo hilo la pekee ambalo tumepewa na Mungu, yaani, pendeleo la kuhubiri kuhusu Ufalme.
-
-
Sehemu ya 12—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye MaendeleoHuduma ya Ufalme—2005 | Agosti
-
-
Sehemu ya 12—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuwasaidia Wanafunzi Kuanzisha na Kuongoza Mafunzo ya Biblia
1 Wanafunzi wetu wa Biblia wanapoanza kuhubiri huenda wakaogopa kuanzisha na kuongoza mafunzo yao ya Biblia. Tunaweza kuwasaidiaje wawe na maoni yanayofaa kuhusu sehemu hiyo muhimu ya huduma yetu?—Mt. 24:14; 28:19, 20.
2 Mwanafunzi wa Biblia anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, yaelekea tayari yeye ni mwanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mazoezi anayopata anapotayarisha na kutoa hotuba anazopewa katika shule yatamsaidia kusitawisha sifa anazohitaji ili awe ‘mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, akilitumia sawasawa neno la kweli.’—2 Tim. 2:15.
3 Fundisha kwa Kuweka Mfano: Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwapa maagizo yaliyo wazi na kwa kuwawekea mfano bora. Alisema: “Kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.” (Luka 6:40) Ni muhimu uige kielelezo cha Yesu kwa kuweka mfano mzuri katika huduma yako. Mwanafunzi anapoona mfano wako mzuri katika huduma, atatambua kwamba lengo la kufanya ziara za kurudia ni kuanzisha mafunzo ya Biblia.
4 Mweleze kwamba tunapomwalika mwenye nyumba ajifunze Biblia pamoja nasi, hatuhitaji kufafanua kwa undani jinsi funzo linavyoongozwa. Mara nyingi inafaa tu kumwonyesha jinsi funzo linavyofanywa kwa kujifunza naye fungu moja au mawili katika kichapo cha funzo. Mapendekezo yanayofaa ya kufanya hivyo yako kwenye ukurasa wa 8 wa nakala hii ya Huduma Yetu ya Ufalme na pia katika ukurasa wa 6 wa Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2002.
5 Inapofaa, mwalike mwanafunzi aandamane nawe, au aandamane na mhubiri mwingine mwenye ustadi kwenye mafunzo mengine ya Biblia. Anaweza kutoa maelezo kuhusu fungu au andiko fulani la msingi. Hivyo, kwa kukutazama, mwanafunzi atajifunza mambo mengi kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo. (Met. 27:17; 2 Tim. 2:2) Mpongeze na umweleze jinsi anavyoweza kufanya maendeleo.
6 Kuwazoeza wahubiri wapya wawe walimu wa Neno la Mungu kutawawezesha kuwa na vifaa kamili kwa ajili ya “kazi njema” ya kuanzisha na kuongoza mafunzo yao wenyewe. (2 Tim. 3:17) Ni furaha iliyoje kufanya kazi bega kwa bega pamoja nao katika kutoa mwaliko huu wa upendo: “Yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure!”—Ufu. 22:17.
-