-
‘Tunalishwa Maneno ya Imani’Huduma ya Ufalme—2005 | Januari
-
-
‘Tunalishwa Maneno ya Imani’
1 Kuishi maisha ya ujitoaji-kimungu hutaka jitihada nyingi. (1 Tim. 4:7-10) Hatuwezi kufanya hivyo kwa nguvu zetu wenyewe, kwa kuwa tutachoka upesi na kujikwaa. (Isa. 40:29-31) Njia moja tunayoweza kupata nguvu kutoka kwa Yehova ni kwa “kulishwa maneno ya imani.”—1 Tim. 4:6.
2 Chakula Kingi cha Kiroho: Kupitia Neno lake na pia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yehova huandaa chakula kingi cha kiroho. (Mt. 24:45) Je, sisi hujitahidi kunufaika na chakula hicho? Je, tunasoma Biblia kila siku? Je, tumetenga wakati wa kujifunza na kutafakari? (Zab. 1:2, 3) Chakula hicho cha kiroho chenye kujenga hututia nguvu na hutulinda na mambo yenye kudhoofisha imani yanayotokana na ulimwengu wa Shetani. (1 Yoh. 5:19) Yehova atakuwa nasi tukijaza akili zetu mambo yenye kujenga na kuyafuata maishani.—Flp. 4:8, 9.
3 Yehova pia hututia nguvu kupitia mikutano ya kutaniko. (Ebr. 10:24, 25) Mafundisho ya kiroho na ushirika wenye kujenga kwenye mikutano hiyo hutuimarisha ili kusimama imara wakati wa majaribu. (1 Pet. 5:9, 10) Kijana mmoja Mkristo alisema: “Ninakuwa shuleni mchana kutwa, na jambo hilo hunivunja moyo sana. Lakini mikutano ni kama sehemu yenye maji jangwani, ambako ninapata nguvu za kuvumilia shuleni siku inayofuata.” Tunabarikiwa sana tunapojitahidi kuhudhuria mikutano.
4 Kuhubiri Kweli: Kuwahubiria wengine kulikuwa kama chakula kwa Yesu. Kulimtia nguvu. (Yoh. 4:32-34) Vivyo hivyo, sisi hutiwa nguvu tunapozungumza na wengine kuhusu ahadi nzuri za Mungu. Pia, kuwa na mengi ya kufanya katika huduma hutusaidia kukazia akilini na moyoni mwetu Ufalme na baraka ambazo zitakuja hivi karibuni. Jambo hilo hutuburudisha kwelikweli.—Mt. 11:28-30.
5 Tuna pendeleo kubwa la kupata na kunufaika na chakula kingi cha kiroho ambacho Yehova anawaandalia watu wake leo. Na tuendelee kumsifu kwa vigelegele na shangwe.—Isa. 65:13, 14.
-
-
Sehemu ya 5: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye MaendeleoHuduma ya Ufalme—2005 | Januari
-
-
Sehemu ya 5: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuamua Kiasi cha Habari Mtakachozungumzia
1 Alipowafundisha wanafunzi wake, Yesu alitilia maanani uwezo wao, kwa hiyo alizungumza nao “kwa kadiri walivyoweza kusikiliza.” (Marko 4:33; Yoh. 16:12) Katika njia hiyohiyo, walimu wa Neno la Mungu leo wanahitaji kuamua kiasi cha habari wanachoweza kuzungumzia kwenye funzo la Biblia. Hiyo itategemea uwezo na hali ya mwalimu na mwanafunzi.
2 Jenga Imani Thabiti: Huenda ukahitaji kutumia vipindi viwili au vitatu kujifunza sehemu fulani ili kuwasaidia baadhi ya wanafunzi waelewe sehemu hiyo, hali utahitaji kutumia kipindi kimoja tu na mwanafunzi mwingine. Kilicho muhimu si kujifunza habari nyingi katika muda mfupi, bali ni kumsaidia mwanafunzi aelewe vizuri mambo anayojifunza. Kila mwanafunzi anahitaji msingi imara wa imani yake mpya katika Neno la Mungu.—Met. 4:7; Rom. 12:2.
3 Unapoongoza funzo kila juma, tumia muda unaohitajika ili kumsaidia mwanafunzi aelewe na kukubali yale anayojifunza katika Neno la Mungu. Epuka kupitia haraka-haraka habari mnazozungumzia hivi kwamba mwanafunzi anakosa kunufaika kikamili na kweli anazojifunza. Mwe na wakati wa kutosha wa kukazia mambo makuu na kuzungumzia maandiko muhimu ambayo ndiyo msingi wa yale mnayojifunza.—2 Tim. 3:16, 17.
4 Usikengeushwe: Mbali na kuepuka kupitia haraka-haraka habari tunazozungumzia wakati wa funzo, tunahitaji kuepuka kuzungumzia mambo mengine yasiyohusiana na habari zile. Ikiwa mwanafunzi anapenda kuzungumzia sana mambo yake ya kibinafsi, huenda tukahitaji kupanga kuzungumzia mambo hayo baada ya funzo.—Mhu. 3:1.
5 Kwa upande mwingine, shauku yetu kuhusiana na kweli inaweza kufanya tuzungumze kupita kiasi wakati wa funzo. (Zab. 145:6, 7) Mara kwa mara, kutaja jambo lililoonwa au jambo lingine ili kuongezea yale mnayozungumzia kunaweza kumsaidia mwanafunzi, lakini hatungependa mambo hayo yawe mengi au marefu sana hivi kwamba mwanafunzi anakosa kuelewa kwa usahihi mafundisho ya msingi ya Biblia.
6 Kwa kuzungumzia kiasi kinachofaa cha habari kwenye kila funzo, tunawasaidia wanafunzi wa Biblia ‘watembee katika nuru ya Yehova.’—Isa. 2:5.
-