Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Siku ya Yehova Iko Karibu
    Huduma ya Ufalme—2005 | Mei
    • Siku ya Yehova Iko Karibu

      1 Wakristo wanatamani sana kuja kwa siku ya Yehova, wakati ambapo Mungu ataharibu ulimwengu huu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Pet. 3:12, 13) Kwa kuwa hatujui siku hiyo itakuja lini, ni lazima tuendelee kukaa macho na kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo. (Eze. 33:7-9; Mt. 24:42-44) Kutafakari Neno la Mungu la kinabii kutaimarisha usadikisho wetu kwamba “ile siku kuu ya Yehova iko karibu.”—Sef. 1:14.

      2 Mfuatano wa Serikali Kuu za Ulimwengu: Katika Ufunuo 17:9-11 mtume Yohana anawataja “wafalme saba” ambao wanafananisha serikali kuu saba za ulimwengu. Yohana anamtaja pia “mfalme wa nane,” ambaye anafananisha Umoja wa Mataifa. Je, tutarajie serikali nyingine kuu za ulimwengu zitokee? La. Unabii unasema kwamba yule mfalme wa nane “anaenda zake kwenye uharibifu,” na baada yake hakuna wafalme wengine wa dunia wanaotajwa. Je, unabii huu unakusaidia kutambua tunaishi katika kipindi gani cha wakati?

      3 Andiko la Danieli 2:31-45 linatusaidia kuelewa kule kuja kwa siku ya Yehova. Katika unabii huo, sanamu kubwa ambayo Nebukadneza aliiona katika ndoto inafananisha mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu. Tayari kila moja ya serikali hizo imetokea. Ni serikali gani inayotawala leo? Ni ile inayofananishwa na nyayo za sanamu hiyo. Unabii huo unaonyesha waziwazi matukio yatakayofuata. Serikali za wanadamu zitaharibiwa kabisa ili “ufalme ambao hautaharibiwa kamwe” utawale. Je, unaona jinsi jambo hilo linavyoonyesha kwamba siku ya Yehova iko karibu?

      4 Uthibitisho Mwingine: Sisi huona mambo mengine ambayo yanathibitisha kwamba siku ya Yehova iko karibu. Tunaona utimizo wa yale ambayo mtume Paulo alitabiri kuhusu sifa za watu “katika siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1-5) Nasi tunashiriki kutoa ushahidi ulimwenguni pote, ushahidi unaopaswa kutolewa kabla ya ule mwisho. (Mt. 24:14) Kazi yetu ya kuhubiri na ionyeshe umuhimu wa ujumbe huu wa malaika: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.”—Ufu. 14:6, 7.

  • Sehemu ya 9—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
    Huduma ya Ufalme—2005 | Mei
    • Sehemu ya 9—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo

      Kuwazoeza Wanafunzi Kutoa Ushahidi Isivyo Rasmi

      1 Andrea na Filipo walipotambua kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa, hawakuweza kujizuia wasiwaambie wengine juu ya jambo hilo lenye kusisimua. (Yoh. 1:40-45) Vivyo hivyo leo, wanafunzi wa Biblia wanapoamini yale ambayo wanajifunza, wao husukumwa kusema kuyahusu. (2 Kor. 4:13) Tunawezaje kuwatia moyo watoe ushahidi isivyo rasmi na kuwazoeza kufanya hivyo kwa mafanikio?

      2 Unaweza kumuuliza mwanafunzi ikiwa ameongea na wengine juu ya mambo ambayo amejifunza katika Biblia. Huenda ana marafiki au watu wa familia ambao anaweza kuwaalika kwenye funzo. Muulize ikiwa kuna yeyote ameonyesha upendezi kati ya wafanyakazi wenzake, wanafunzi wenzake, au watu wengine ambao anafahamiana nao. Kwa njia hiyo, anaweza kuanza kutoa ushahidi. Msaidie aelewe kwamba anahitaji kuwa na busara na kuonyesha heshima na fadhili anapoongea na wengine kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake.—Kol. 4:6; 2 Tim. 2:24, 25.

      3 Kuwahubiria Wengine: Ni muhimu sana kuwazoeza wanafunzi wa Biblia kutumia Neno la Mungu kuhubiri. Mnapofikia sehemu fulani za pekee katika funzo, muulize mwanafunzi maswali kama haya: “Wewe ungetumiaje Biblia kuwaeleza watu wa familia yenu kweli hii?” au “Ungetumia andiko gani katika Biblia kumthibitishia rafiki yako jambo hili?” Sikiliza jibu lake, na umwonyeshe jinsi anavyoweza kutumia Maandiko anapofundisha. (2 Tim. 2:15) Kwa kufanya hivyo, utakuwa ukimzoeza mwanafunzi kutoa ushahidi isivyo rasmi, na baadaye kuhubiri pamoja na kutaniko atakapostahili.

      4 Ni jambo la hekima kuwasaidia wanafunzi wa Biblia kujua jinsi ya kushughulikia upinzani. (Mt. 10:36; Luka 8:13; 2 Tim. 3:12) Huenda wanafunzi wakapata fursa ya kutoa ushahidi wakati wengine wanapouliza maswali au wanapoongea kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini? inaweza kuwasaidia ili ‘wawe tayari kujitetea.’ (1 Pet. 3:15) Broshua hiyo ina habari sahihi ambazo wapya wanaweza kutumia kuwasaidia marafiki na watu wa familia wanaopinga wakiwa na nia nzuri waelewe imani yetu na utendaji wetu unaotegemea Biblia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki