Msiache Upendo Mliokuwa Nao Mwanzoni
1 Yesu aliyetukuzwa alishauri hivi kutaniko la Efeso la karne ya kwanza: “Nina jambo hili dhidi yako, kwamba umeacha upendo uliokuwa nao mwanzoni.” (Ufu. 2:4) Inaonekana kwamba wengi walikuwa wameacha upendo waliokuwa nao kwa Yehova hapo mwanzoni. Tulipokuwa tukijifunza kweli, tulisitawisha upendo wenye nguvu kwa Mungu na jirani. Upendo huo ulituchochea tutangaze kwa bidii tumaini letu jipya. Ni nini kitakachotusaidia tusipoteze upendo tuliokuwa nao mwanzoni na kupunguza bidii yetu katika huduma?
2 Funzo la Kibinafsi na Kuhudhuria Mikutano: Ni nini kilichofanya tusitawishe upendo kwa Mungu na jirani tulipojifunza kweli kwa mara ya kwanza? Je, si mambo yote ambayo tulijifunza kumhusu Yehova katika funzo letu la Biblia? (1 Yoh. 4:16, 19) Hivyo, ili upendo wetu “uwe mwingi hata zaidi na zaidi,” ni lazima tuendelee kutwaa ujuzi sahihi na tuchunguze kwa bidii “mambo mazito ya Mungu.”—Flp. 1:9-11; 1 Kor. 2:10.
3 Inaweza kuwa vigumu kuwa na ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi katika siku hizi za mwisho zilizojaa mahangaiko na vikengeusha fikira. (2 Tim. 3:1) Ni lazima tutenge wakati wa kujilisha kiroho. Ni muhimu pia kuhudhuria mikutano kwa ukawaida hasa ‘tunapoona siku ile kuwa inakaribia.’—Ebr. 10:24, 25.
4 Huduma: Kuhubiri kwa bidii hutusaidia kudumisha upendo tuliokuwa nao mwanzoni kwa Mungu. Tunapohubiri habari njema, sisi hujikumbusha kuhusu ahadi zenye upendo za Yehova, na hilo hutusaidia kudumisha tumaini letu likiwa jangavu na kuimarisha upendo wetu. Ili tuwafundishe wengine kweli za Biblia, tunahitaji kufanya utafiti ili tuzielewe vizuri zaidi. Kufanya hivyo huimarisha imani yetu.—1 Tim. 4:15, 16.
5 Yehova anastahili vitu vyote, kutia ndani upendo wetu. (Ufu. 4:11) Usiache upendo wako ufifie. Imarisha upendo uliokuwa nao mwanzoni kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na uwe na bidii ya kuwatangazia wengine jambo unalolipenda sana.—Rom. 10:10.