-
Kitabu cha Biblia Namba 64—3 Yohana“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
-
-
1. Yohana wa Tatu ilielekezwa kwa nani, na ni nini kijulikanacho juu yake?
BARUA hii ameandikiwa Gayo, Mkristo mwaminifu ambaye Yohana alimpenda kikweli. Jina Gayo lilikuwa la kawaida katika siku za kundi la mapema. Laonekana mara nne katika sehemu nyingine za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, likirejezea wanaume tofauti-tofauti angalau watatu na labda wanne. (Mdo. 19:29; 20:4; Rum. 16:23; 1 Kor. 1:14) Hakuna habari ambazo zingetambulisha wazi kabisa Gayo ambaye Yohana alimwandikia ni yeyote wa hawa wengine. Yote tujuayo juu ya Gayo ni kwamba alikuwa mshiriki wa kundi la Kikristo, kwamba alikuwa rafiki maalumu wa Yohana, na kwamba barua hii ilielekezwa kwake kibinafsi, na ndiyo sababu neno “-ako” (“nawe”) laonekana kila mara kwa idadi ya umoja.
2. Ni nini kitambulishacho mwandikaji, wakati, na mahali pa kuandikia Yohana wa Tatu?
2 Kwa kuwa namna ya salamu za kufungua na za kufunga ni kama ile ile ya Yohana wa Pili na mwandikaji ajitambulisha tena kuwa “mzee,” hakuwezi kuwa na shaka kwamba mtume Yohana ndiye aliyeandika barua hii pia. (2 Yn. 1) Ufanani wa yaliyomo na namna ya usemi uliotumiwa pia waonyesha kwamba iliandikwa katika au karibu na Efeso, kama ilivyokuwa kwa zile barua nyingine mbili, 98 W.K. hivi. Kwa sababu ya ufupi wayo, ilinukuliwa mara chache na waandikaji wa mapema, lakini ikiwa pamoja na Yohana wa Pili, yapatikana katika orodha za mapema za Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu.a
3. Yohana aeleza nini mwote mwote katika Yohana wa Tatu, na ni muono gani mfupi wa kupendeza ambao twapata juu ya udugu wa Wakristo wa mapema?
3 Katika barua yake Yohana aeleza uthamini kwa ukaribishaji-wageni ambao Gayo alionyesha kuelekea ndugu wenye kusafiri, naye ataja matata fulani pamoja na Diotrefe fulani mwenye kutaka makuu. Demetrio atajwaye aonekana kuwa ndiye aliyemletea Gayo barua hii, hivyo basi yawezekana alitumwa na Yohana naye alihitaji ukaribishaji-wageni wa Gayo katika safari yake, jambo ambalo lingewezeshwa na barua hii. Kama ilivyo katika kisa cha Gayo, sisi hatujui lolote juu ya Diotrefe na Demetrio zaidi ya yale tusomayo hapa. Hata hivyo, barua hii yatoa muono mfupi wa kupendeza juu ya udugu wa kimataifa wa Wakristo wa mapema. Miongoni mwa mambo mengine, huo ulihusisha ile desturi ya kuwakaribisha wageni waliosafiri “kwa ajili ya Jina hilo,” ingawa huenda hao wakawa hawakujulikana kibinafsi na wakaribishaji wao.—Mst. 7.
YALIYOMO KATIKA YOHANA WA TATU
4. Yohana ampongeza Gayo kwa jambo gani, ni mwenendo gani wa utukutu ambao ashutumu, na atoa ushauri gani timamu?
4 Mtume ashauri kuwa na hali ya kukaribisha wageni na kazi zilizo njema (mist. 1-14). Yohana ashangilia kusikia kwamba bado Gayo ‘aenda katika kweli.’ Ampongeza kwa kufanya kazi ya uaminifu, ile ya kuwatunza kwa upendo ndugu wanaotembelea. “Imetupasa sisi,” asema Yohana, “kuwakaribisha watu kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.” Yohana alitangulia kuliandikia kundi, lakini Diotrefe mwenye kujikweza hapokei chochote kutoka kwa Yohana au wengine wenye madaraka kwa staha. Yohana, ikiwa atakuja, atamtoza hesabu kwa ‘upuzi wake wa maneno maovu.’ Gayo mpendwa ashauriwa ‘asiuige ubaya, bali auige wema.’ Demetrio atajwa kuwa kielelezo kistahilicho sifa. Badala ya kuandika mengi, Yohana aeleza kwamba ana tumaini la kumwona Gayo uso kwa uso karibuni.—Mst. 4, 8, 10, 11.
KWA NINI NI CHENYE MAFAA
5. (a) Yohana alijionyeshaje kuwa mwangalizi aliye kielelezo chema, na lilikuwa jambo la maana kuhifadhi roho gani? (b) Kwa nini Yohana alisema wazi sana juu ya Diotrefe? (c) Sisi leo twapaswa kuwa na bidii kwa jambo gani, kupatana na kanuni gani iliyoelezwa na Yohana?
5 Mtume Yohana ajionyesha kuwa mwangalizi aliye kielelezo chema katika bidii yake ya kulilinda kundi na mavutano yenye kuchafua. Roho ya upendo na ukaribishaji-wageni iliyolienea kundi ilistahili pongezi, na kweli ulikuwa wajibu wao kuhifadhi hali hii yenye furaha, ili kwamba ndugu wa huko na “wageni” (watu mmoja mmoja wasiojulikana hapo kwanza na mkaribishaji wao Mkristo) waliokuja miongoni mwao waweze kutumikia pamoja wakiwa “watenda kazi pamoja na kweli.” (Mist. 5, 8) Hata hivyo, Diotrefe alikuwa na macho ya kujiinua juu sana, jambo la uchukivu kwa Yehova, naye alikosa staha kwa mamlaka ya kitheokrasi, hata kupayapaya kwa uovu juu ya mtume Yohana. (Mit. 6:16, 17) Yeye alikuwa akiweka pingamizi la kufunga njia ya ukaribishaji-wageni wa kundi la Kikristo. Si ajabu kwamba Yohana alisema wazi sana juu ya ovu hili na kupendelea upendo halisi wa Kikristo katika kundi. Sisi twapaswa kuwa wenye bidii jinsi hiyo hiyo kudumisha unyenyekevu, kutembea katika ile kweli, na kuzoea upendo na ukarimu wa kimungu, kupatana na kanuni iliyoelezwa na Yohana: “Yeye atendaye mema ni wa Mungu, bali yeye atendaye mabaya hakumwona Mungu.”—3 Yn. 11.
-
-
Kitabu cha Biblia Namba 65—Yuda“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
-
-
Kitabu cha Biblia Namba 65—Yuda
Mwandikaji: Yuda
Mahali Kilipoandikiwa: Palestina (?)
Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 65 W.K.
1. Ni kwa sababu ya hali zipi ndani ya kundi Yuda aliona ikihitajiwa kabisa kuandika barua yake thabiti kwa ajili ya ndugu zake?
NDUGU Wakristo wa Yuda walikuwa hatarini! Katika wakati uliokuwa umepita tangu kifo na ufufuo wa Kristo Yesu, watu wenye tabia ngeni walikuwa wamejongelea kwa siri wakaingia ndani ya kundi la Kikristo. Adui hao walikuwa wamepenya kwa kusudi la kuibomoa imani, kama vile mtume Paulo, karibu miaka 14 iliyotangulia, alivyokuwa ameonya. (2 The. 2:3) Akina ndugu wapaswa kuwekwaje macho na kufanywa wajihadhari na hatari? Barua ya Yuda, ambayo ni thabiti na yenye nguvu katika taarifa yayo ya kutoboa wazi, ilitoa jibu. Yuda mwenyewe alieleza msimamo wake waziwazi katika mistari 3 na 4: ‘Niliona imenilazimu kuwaandikia kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi.’ Misingi yenyewe ya fundisho timamu na maadili ilikuwa ikitishwa. Yuda alihisi akihitajika kupigania masilahi (faida) ya ndugu zake, ili kwamba wao, nao, waweze kufanya pigano kali kwa ajili ya imani.
2. (a) Yuda alikuwa nani? (b) Ni uhusiano gani pamoja na Yesu ambao Yuda aliuthamini zaidi ya mwingine wote?
2 Lakini Yuda alikuwa nani? Maneno ya kufungua yatuambia kwamba barua hiyo iliandikwa na “Yuda, mtumwa wa Yesu Kristo, ndugu yake Yakobo, kwa hao walioitwa.” Je! Yuda, au Yudasi, alikuwa mtume, kwa kuwa 2 wa mitume 12 wa awali wa Yesu waliitwa Yuda? (Luka 6:16) Yuda hajisemi kuwa mtume, bali awataja mitume kwa nafsi ya tatu “wa-” (“wao,” NW), ikiwa dhahiri kwamba yeye mwenyewe hajitii ndani. (Yuda 17, 18) Zaidi ya hilo, yeye ajiita “ndugu yake Yakobo,” kwa wazi akimaanisha yule mwandikaji wa barua ya Yakobo, aliyekuwa ndugu-nusu wa Yesu. (Mst. 1) Akiwa mmoja wa “nguzo” za kundi katika Yerusalemu, Yakobo huyu alijulikana sana, na kwa sababu hiyo Yuda ajitambulisha naye. Hiyo yafanya Yuda pia kuwa ndugu-nusu wa Yesu, naye ameorodheshwa kuwa hivyo. (Gal. 1:19; 2:9; Mt. 13:55; Mk. 6:3) Hata hivyo, Yuda hakujifaidi kibinafsi kwa kutumia uhusiano wake wa kimwili pamoja na Yesu, bali kwa unyenyekevu alitia mkazo juu ya uhusiano wake wa kiroho akiwa “mtumwa wa Yesu Kristo.”—1 Kor. 7:22; 2 Kor. 5:16; Mt. 20:27.
3. Ni nini kithibitishacho uasilia wa barua ya Yuda?
3 Uasilia wa kitabu hiki cha Biblia waungwa mkono na mtajo wacho katika Muratorian Fragment, cha karne ya pili W.K. Kwa kuongezea, Clement wa Aleksandria (karne ya pili W.K.) alikikubali. Origen alikirejezea kuwa kazi yenye “mistari michache, lakini iliyojawa na maneno yenye afya ya neema ya kimbingu.”a Tertullian pia alikiona kuwa asilia. Hakuna shaka kwamba chafaa kuwa pamoja na Maandiko yale mengine yaliyopuliziwa na Mungu.
-