-
Maswali Kutoka kwa WasomajiMnara wa Mlinzi—2004 | Julai 15
-
-
Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Ni nini kinachoonyeshwa kimbele na mpango kuhusu mwaka wa Yubile unaotajwa katika Mambo ya Walawi sura ya 25?
Sheria ya Musa ilisema kwamba “katika mwaka wa saba kutakuwa na sabato ya pumziko kamili kwa ajili ya nchi hiyo.” Kuhusu mwaka huo, Waisraeli waliagizwa hivi: “Shamba lako hutalipanda mbegu, nalo shamba lako la mizabibu hutalikata matawi. Mimea inayochipuka kutokana na mbegu zilizoanguka za mavuno yako hutavuna, na zabibu za mzabibu wako ambao haujakatwa matawi usikusanye. Kutakuwa na mwaka wa pumziko kamili kwa ajili ya nchi.” (Mambo ya Walawi 25:4, 5) Hivyo, kila mwaka wa saba ulipaswa kuwa mwaka wa Sabato kwa ajili ya nchi. Na kila mwaka wa 50, baada ya mwaka wa saba wa Sabato, ulipaswa kuwa Yubile. Ni nini ambacho kingetukia mwaka huo?
Yehova aliwaambia Waisraeli hivi kupitia Musa: “Mtautakasa mwaka wa 50 na kutangaza uhuru katika nchi kwa wakaaji wake wote. Itakuwa Yubile kwenu, nanyi mtarudi kila mmoja kwenye miliki yake nanyi mtarudi kila mmoja kwa familia yake. Mwaka wa 50 utakuwa Yubile kwenu. Hamtapanda mbegu wala kuvuna mimea ya nchi inayochipuka kutokana na mbegu zilizoanguka wala kukusanya zabibu kutoka katika mizabibu ambayo haijakatwa matawi.” (Mambo ya Walawi 25:10, 11) Yubile ilimaanisha kwamba nchi ingekuwa pia na sabato nyingine mwaka wa 49. Lakini Yubile ilileta uhuru kwa wakaaji wa nchi. Myahudi yeyote aliyekuwa ameuzwa utumwani alipaswa kuachiliwa huru. Urithi ambao mtu alilazimika kuuza ulipaswa kurudishiwa familia yake. Kwa Waisraeli wa kale, Yubile ilipaswa kuwa mwaka wa kurudishwa na kukombolewa. Hiyo inaonyesha jambo gani kimbele kuwahusu Wakristo?
Uasi wa mwanadamu wa kwanza, Adamu, uliwaweka wanadamu katika utumwa wa dhambi. Mungu ameandaa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ili kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi.a (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; 1 Yohana 2:1, 2) Wakristo huwekwa huru lini kutokana na sheria ya dhambi? Akizungumza na Wakristo waliotiwa mafuta, mtume Paulo alisema: “Ile roho ambayo hutokeza uzima katika muungano na Kristo Yesu imewaweka ninyi huru kutoka katika sheria ya dhambi na kifo.” (Waroma 8:2) Wale walio na tumaini la kuishi mbinguni hupata uhuru huo wanapotiwa mafuta kwa roho takatifu. Ingawa miili yao ni ya kibinadamu na isiyokamilika, Mungu huwatangaza kuwa waadilifu na kuwafanya kuwa wana wake wa roho. (Waroma 3:24; 8:16, 17) Kwa watiwa-mafuta, Yubile ya Kikristo ilianza Pentekoste mwaka wa 33 W.K.
Namna gani “kondoo wengine,” ambao wana tumaini la kuishi milele duniani? (Yohana 10:16) Kwa kondoo wengine, ule Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu utakuwa wakati wa kurudishwa na kukombolewa. Wakati wa Yubile hiyo ya Utawala wa Miaka Elfu, Yesu atatumia manufaa ya dhabihu yake ya fidia kwa wanadamu wanaoamini, naye atabatilisha matokeo ya dhambi. (Ufunuo 21:3, 4) Kufikia mwisho wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu, wanadamu watafikia ukamilifu nao watakuwa huru kabisa kutokana na dhambi na kifo walichorithi. (Waroma 8:21) Baada ya mambo hayo kutimizwa, Yubile ya Kikristo itakoma.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kweli, Yesu alitumwa “kutangaza uhuru kwa wale waliochukuliwa mateka.” (Isaya 61:1-7; Luka 4:16-21) Alitangaza uhuru wa kiroho.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Yubile ya Miaka Elfu itakuwa wakati wa kurudishwa na kukombolewa kwa “kondoo wengine”
-
-
“Kila Mtu Aliye Mwerevu Atatenda kwa Ujuzi”Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 15
-
-
“Kila Mtu Aliye Mwerevu Atatenda kwa Ujuzi”
MWONGOZO wa Neno la Mungu, Biblia, ‘ni wa kutamaniwa kuliko dhahabu, naam, kuliko dhahabu safi sana.’ (Zaburi 19:7-10) Kwa nini? Kwa sababu “Sheria ya mwenye hekima [Yehova] ni chemchemi ya uzima, ili kumwepusha mtu na mitego ya kifo.” (Methali 13:14) Linapotumiwa, shauri la Biblia huboresha maisha yetu na pia hutusaidia kuepuka mitego ambayo huyahatarisha. Hivyo, ni muhimu kama nini kutafuta ujuzi wa Biblia na kutenda kupatana nao!
Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alitoa shauri kwenye Methali 13:15-25, ambalo hutusaidia kutenda kwa ujuzi ili tuweze kufurahia maisha bora na marefu zaidi.a Akitumia methali fupi-fupi, anaonyesha jinsi Neno la Mungu linavyoweza kutusaidia kupata kibali cha wengine, kuendelea kuwa waaminifu katika huduma yetu, kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea nidhamu, na kuchagua marafiki wetu kwa hekima. Pia anazungumzia hekima ya kuwaachia watoto wetu urithi na pia kuwatia nidhamu kwa upendo.
Ufahamu Mzuri Huleta Kibali
“Ufahamu mzuri huleta kibali,” asema Sulemani, “lakini njia ya wale wanaotenda kwa hila ni ngumu.” (Methali 13:15) Neno la awali ambalo limetafsiriwa “ufahamu mzuri,” au uelewaji mzuri, “linafafanua uwezo wa kutumia busara, kufanya maamuzi mazuri, na kuwa na maoni ya hekima,” chasema kitabu kimoja cha marejeo. Si vigumu kwa mtu aliye na sifa hizo kupata kibali cha wengine.
-